Songa Mbele Kuuelekea Mradi!
Mambo Makuu Kutokana na Wafilipi
MTUME Paulo alitaka Wakristo katika Filipi wasonge mbele kuelekea mradi wa zawadi ya uhai wa milele. Kwa sababu hiyo, yeye aliwaandikia katika 60 au 61 W.K. hivi, wakati wa kifungo-gereza chake cha kwanza katika Roma. Barua yake ilipelekwa kwenye kundi moja alilokuwa ameanzisha yapata miaka kumi mapema katika Filipi, jiji lililowekewa misingi na Filipo wa Makedoni (baba ya Aleksanda Mkubwa). Kufikia karne ya kwanza W.K., lilikuwa limekuwa “mji wa Makedonia, mji ulio mkuu katika jimbo lile,” ambalo sasa ni sehemu ya Ugiriki kaskazini na Yugoslavia kusini.—Matendo 16:11, 12.
Waamini Wafilipi walikuwa maskini lakini wakarimu. Zaidi ya mara moja, walikuwa wamepeleka kitu fulani kutimiza mahitaji ya Paulo. (Wafilipi 4:14-17) Lakini barua yake ilikuwa zaidi ya maandishi mafupi ya asante. Iliwapa kitia-moyo pia, ilionyesha upendo, na iliandaa shauri.
Sifa za Kikristo Zaonekana Wazi
Barua ya Paulo ilifunguka kwa ushuhuda wa upendo wake kwa waamini Wafilipi. (1:1-30, NW) Yeye alimshukuru Yehova kwa mchango wao wa kusogeza mbele habari njema na akasali kwamba upendo wao uongezeke. Paulo aliterema kwamba kifungo-gereza chake kiliwasababisha waonyeshe ‘moyo mkuu zaidi wa kusema neno la Mungu pasipo hofu.’ Alitamani kuwa pamoja na Kristo lakini akahisi angeweza bado kuwahudumia. Paulo alitaka pia waendelee ‘kujitahidi upande kwa upande kwa ajili ya ile imani ya habari njema.’
Ndipo likaja shauri juu ya mtazamo na mwenendo. (2:1-30, NW) Wafilipi walitiwa moyo waonyeshe upendezi wa kibinafsi katika wengine na kuonyesha unyenyekevu kama ule wa Kristo. Walikuwa ‘waking’aa kama wamulikaji katika ulimwengu’ na walihimizwa wadumishe “mshiko imara juu ya neno la uhai.” Paulo alitumainia kuwapelekea Timotheo na alikuwa na uhakika kwamba yeye mwenyewe angekuja karibuni. Ili kuwahakikishia upya juu ya Epafrodito, aliyekuwa amekuwa mgonjwa sana, Paulo alikuwa akiwapelekea huyu mtumishi mwaminifu-mshikamanifu.
Endeleeni Kusonga Mbele Kuuelekea Mradi
Ndipo mtume awaonyesha Wafilipi mahali pa kuweka uhakika wao wasongapo mbele kuuelekea mradi. (3:1-21) Wapasa kuwekwa katika Yesu Kristo, si katika mnofu wala katika tohara kama watu fulani walivyokuwa wakifanya. Paulo alifikiria sifa za ustahili wake wa kimnofu kuwa takataka kwa sababu ya “uzuri [thamani, NW] usio na kiasi wa kumjua Kristo.” Mtume alikuwa ‘akikaza mwendo, aifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu’ na akawatia moyo Wafilipi wawe na mtazamo ule ule wa akilini.
Kutumia shauri la Paulo la kumalizia kungesaidia Wafilipi waendelee kukaza macho kwenye mradi na zawadi. (4:1-23) Aliwahimiza wamkabidhi Mungu mambo ya wasiwasi wao katika sala na kujaza akili zao fikira zifaazo. Paulo aliwapongeza tena kwa ukarimu wao na akamalizia kwa salamu na kutaka kwamba fadhili zisizostahiliwa za Bwana Yesu Kristo ziwe pamoja na roho waliyoonyesha.
Barua ya Paulo kwa Wafilipi yaendeleza ukarimu, upendo, na unyenyekevu. Yatia moyo kuwa na uhakika katika Kristo na sala yenye kuhisiwa moyoni kwa Mungu. Na maneno ya Paulo kwa uhakika yasaidia Mashahidi wa Yehova kuendelea kusonga mbele kuelekea mradi wa zawadi ya uhai wa milele.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 25]
Kuuelekea Mradi: “Nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele,” akaandika Paulo, “nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu.” (Wafilipi 3:13, 14) Mtume alikuwa akijitahidi sana kama mtu aliye katika mbio. Hakupoteza wakati na jitihada akitazama nyuma bali alisonga mbele kuelekea mradi wake—kama mkimbiaji mwenye kujikaza avuke mstari wa kumalizia. Kwa Paulo na Wakristo wengine wapakwa-mafuta, zawadi ilikuwa uhai wa kimbingu kwa kufufuliwa baada ya kumaliza mwendo wa kidunia wa uaminifu kwa Mungu. Matumaini yetu yawe ni ya kimbingu au ya kidunia, acheni tushike uaminifu wa kimaadili kwa Yehova na tusonge mbele kuuelekea mradi tukiwa Mashahidi wake.—2 Timotheo 4:7.