‘Kufuatia Mradi’
“Nikisahau mambo yaliyo nyuma na kujinyoosha kufikia mambo yaliyo mbele, ninafuatia mradi.”—WAFILIPI 3:13, 14, New World Translation.
1, 2. (a) Sauli wa Tarso alipokeaje mgawo katika huduma, na mgawo huo ulikuwa nini? (b) Aliuitikiaje mgawo huo?
WAKATI Sauli wa Tarso alipokuwa njiani kwenda Dameski akiwa ameazimia kutesa Wakristo, nuru kutoka mbinguni iling’aa kumzunguka, naye akasikia sauti ikisema: “Sauli, Sauli, mbona waniudhi? Akasema, U nani wewe, Bwana? Naye akasema, Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe. Lakini simama, uingie mjini, nawe utaambiwa yakupasayo kutenda.”—Matendo 9:3-6.
2 Ni kwa sababu gani Yesu alimpa Sauli wa Tarso kisa hicho? Yesu alieleza sababu kwa mwanafunzi Anania: “Huyu [Sauli] ni chombo, kiteule kwangu, alichukue Jina langu mbele ya Mataifa, na wafalme, na wana wa Israeli.” Kwa kutii Anania alienda, akamwekelea Sauli mikono na kusema: “Bwama amenituma, Yesu, yeye aliyekutokea katika njia uliyoijia, upate kuona tena, ukajazwe [roho takatifu].” (Matendo 9:15-17) Mara uwezo wa kuona ulipomrudia alibatizwa, akaanza kushirikiana na kundi la Kikristo katika Dameski. Sasa, akiwa mhudumu Mkristo aliyebatizwa, upesi akaanza kujishughulisha kuhubiri kwa bidii habari njema juu ya Yesu, Mwana wa Mungu, kati ya Wayahudi.—Matendo 9:20-22.
3, 4. (a) Paulo aliionaje huduma yake? (b) Ni kwa njia gani maoni ya Paulo yalitofautiana na yale yaliyoonyeshwa na kundi katika Efeso?.
3 Mhudumu huyo mwenye bidii anajulikana vizuri zaidi kama mtume Paulo. Sikuzote yeye alisema kwa kujivunia huduma yake na fadhili zisizostahilika alizoonyeshwa: “Ninamshukuru Kristo Yesu Bwana yetu, ambaye alinipa uwezo, kwa sababu alinichukua kuwa mwaminifu kwa kunigawia huduma, ingawa hapo kwanza nilikuwa mwenye kukufuru na mtesaji na mkaidi. Hata hivyo, nilionyeshwa rehema, kwa sababu nilikuwa asiyejua na nilitenda kwa kukosa imani.” (1 Timotheo 1:12-14, NW) Ndiyo, yeye aliheshimu sana huduma hiyo.—Warumi 11:13; 2 Wakorintho 4:7.
4 Semi hizo za Paulo zinaonyesha jinsi alivyoiona huduma katika mwendo wote wa kazi yake ya maisha. Yeye hakuingia katika hali ambayo ilikuwako wakati mmoja kwenye kundi katika Efeso, ambalo juu yake Yesu alisema: “Nina neno juu yako, ya kwamba umeuacha upendo wako wa kwanza.” (Ufunuo 2:4) Badala yake, Paulo aliendelea kuweka mradi wake mbele yake akaendelea na bidii na shauku ile ile kwa ajili ya huduma aliyokuwa nayo siku za mapema katika Dameski.
5. Baada ya kumtumikia Yehova kwa miaka mingi, tunaweza kutiaje moyo wengine?
5 Baada ya kuwa mhudumu mwaminifu Mkristo kwa makumi mengi ya miaka, Paulo alitumia hali aliyokuwa nayo hapo mbele ya maisha na mambo aliyojionea ili kutia moyo wahudumu wenzake katika kundi la Filipi kusudi wasikate tamaa. Je! hujaona kwamba kwa kawaida ni jambo lenye kupendeza sana kusikia jinsi mtu alivyojifunza ukweli akawa mhudumu? Basi, je, wewe unawatia wengine moyo kwa msingi wa historia yako ya kibinafsi na miaka ya utumishi wa uaminifu ukiwa mhudumu Mkristo aliye wakfu?
6. Hali ya maisha ya Paulo ilikuwa nini akiwa Myahudi?
6 Paulo katika barua aliyowaandikia Wafilipi, angeweza kutaja juu ya maisha yake akiwa Myahudi mwenyewe hasa. Alisema: “Mtu ye yote akijiona kuwa anayo sababu ya kuutumainia mwili, mimi zaidi. Nilitahiriwa siku ya nane, ni mtu wa taifa la Israeli, wa kabila la Benyamini, Mwebrania wa Waebrania, kwa habari ya kuishika torati, ni Farisayo, kwa habari ya juhudi, mwenye kuliudhi [kundi], kwa habari ya haki ipatikanayo kwa sheria sikuwa na hatia.”—Wafilipi 3:4-6.
7. Ni kwa sababu gani Paulo aliacha mambo hayo nyuma, na alipata faida ya nini kwa kufanya hivyo?
7 Akiwa alikuwa na hali ya maisha ya namna hiyo Paulo angaliweza kuwa na faida nyingi za kimwili kwa kukamatana na Wayahudi. Lakini, aliendelea kusema: “Mambo yale yaliyokuwa faida kwangu, naliyahesabu kuwa hasara kwa ajili ya Kristo. Naam, zaidi ya hayo, nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu; ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi . . . ili nimjue yeye, na uweza wa kufufuka kwake, na ushirika wa mateso yake, nikifananishwa na kufa kwake; ili nipate kwa njia yo yote [kuufikia ufufuo wa] wafu.” (Wafilipi 3:7-11) Hayo ni maneno yanayoonyesha imani kamili katika Kristo Yesu na maandalizi yaliyofanywa na Yehova Mungu. Je! wewe ni kama Paulo kwa kutoruhusu tamaa ya umashuhuri au faida ya kimwili iongoze maisha yako?
Maoni ya Akili Yanayofaa
8. (a) Baada ya kutumikia kwa muda mrefu katika huduma, Paulo alisema nini juu ya mradi wake? (b) Maneno ya Paulo katika 1 Wakorintho 9:24-27 yanaweza kuwaje ya kweli katika habari yetu?
8 Baada ya Paulo kumtumikia Mungu kwa makumi mengi ya miaka, je, angeacha kufuatia mradi wake? Aliwaandikia Wafilipi hivi: “Akina ndugu, ningali sijidhanii kuwa nimeishika; lakini kuna jambo moja juu ya hilo: Nikisahau mambo yaliyo nyuma na kujinyoosha kufikia mambo yaliyo mbele, ninafuatia kuelekea mradi wa zawadi ya mwito wa juu wa Mungu kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 3:13, 14, NW) Alikuwa tayari amefanya kumbukumbu zuri katika huduma ya Kikristo na alivumilia mambo mengi, na ni wakati alipokuwa angali gerezani Roma akaandika maneno hayo kwa Wafilipi, na bado huduma yake haikuwa imefikia mwisho. Ikiwa angepewa zawadi ya kupewa wale waliotumikia katika kundi la Kikristo la karne ya kwanza, yaani “mwito wa juu wa Mungu kwa njia ya Kristo Yesu,” basi alipaswa aendelee kufuatia mradi. Hayo ndiyo maoni yanayofaa waliyo nayo Wakristo wote waliokomaa, wawe tumaini lao la uzima wa wakati ujao ni katika mbingu au duniani. Kila mmoja wetu anafanya vema kuchunguza msimamo wake mwenyewe na njia yetu ya kufikiri ili kuona kama tunathamini kweli kweli huduma tuliyopewa chini ya mpango wa Mungu.
9. Tunaweza kuwa na maoni ya akili gani ya ukomavu?
9 Paulo anatambulisha maoni ya Kikristo yaliyokomaa, kwa kusema: “Acheni, basi, kwa kadiri wengi wetu walivyokomaa, na tuwe wenye hayo maoni ya akili; na ikiwa mna maelekeo ya akili tofauti kwa njia yo yote, Mungu atawafunulia maoni hayo yaliyo juu.” (Wafilipi 3:15, NW) Maoni ya Kikristo yaliyokomaa yanaongoza kwenye kufanikiwa. Hiyo inatia kufuata hatua za Kristo Yesu, ambaye kwa kufanikiwa alimaliza huduma yake ya kidunia aliyogawiwa. Yesu aliweza kusali hivi kwa Babaye: “Mimi nimekutukuza duniani, hali nimeimaliza kazi ile uliyonipa niifanye. Na sasa, Baba, unitukuze mimi pamoja nawe, kwa utukufu ule niliokuwa nao pamoja nawe kabla ya ulimwengu kuwako.”—Yohana 17:4, 5.
10. Ni nini zaidi yanayoweza kusemwa juu ya maoni ya akili yaliyo mfano mwema ya Kristo kuelekea utumishi wa Yehova?
10 Ikiwa tutampendeza Yehova Mungu, na kwa njia hiyo tupokee zawadi ya uzima wa milele, ni lazima tuwe na maoni ya akili yale yale ambayo Kristo Yesu alionyesha. Akiwa anajua hilo, Paulo alisihi hivi: “Endeleeni kuwa na maoni ya akili hayo ndani yenu ambayo yalikuwamo ndani ya Kristo Yesu pia, ambaye, ingawa alikuwako katika mfano wa Mungu, hakufikiria kunyakua, yaani, kwamba alingane na Mungu. La, lakini alijimwaga mwenyewe na kuchukua mfano wa mtumwa akaja kuwa mfanano wa watu. Zaidi ya hilo, alipojikuta kwa mtindo wa mtu, alijinyenyekeza mwenyewe na kuwa mtiifu hata kufa, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso. Kwa sababu hiyo hiyo pia Mungu alimpandisha kwenye cheo kikuu na kwa fadhili akampa jina lililo juu ya kila jina jinginelo.” (Wafilipi 2:5-9, NW) Yesu alikuwa na maoni mazuri ajabu kama nini! Je! tunaweza kufuata mfano wake? Kutafuta kufanya mapenzi ya Mungu kwa unyenyekevu sikuzote kunaongoza kwenye baraka. Mgawo unapotimizwa, matokeo yake yanakuwa ni mazuri.
11. Walio na nguvu na ukomavu wa kiroho wanapaswa kufanya nini?
11 Kwa sababu ya yale aliyoandika Paulo, wengine katika kundi la Filipi kwa wazi wangali walipaswa kujitahidi wafikie maoni ya Kikristo yaliyokomaa. Paulo alichukua hatua ya kwanza awatie moyo na kuwasaidia. Katika makundi yaliyo mengi leo, kuna wale wenye nguvu zaidi katika imani na wale wenye udhaifu fulani fulani. Wenye nguvu zaidi, kama Paulo, wanapaswa kutia moyo wale wengine. Kristo Yesu alijitahidi sana kutia nguvu wale waliokuwa na mahitaji ya kiroho, akawekea Wakristo mfano wa kufuata. “Hata hivyo, sisi, tulio na nguvu tunapaswa kubeba udhaifu wa wale wasio na nguvu, wala tusiwe tukijipendeza wenyewe. Acheni kila mmoja wetu ampendeze jirani yake katika yaliyo mema kwa ajili ya kumjenga. Sasa Mungu anayetoa uvumilivu na faraja na awajalie mwe miongoni mwenu na maoni ya akili yale yale aliyokuwa nayo Kristo Yesu, ili kwa kupatana pamoja kwa kinywa kimoja mweze kumtukuza Mungu na Baba ya Bwana yetu Yesu Kristo.”—Warumi 15:1, 2, 5, 6, NW.
12. Tunapaswa kuwa na maoni gani juu ya zawadi ambayo Mungu atatoa?
12 Paulo, katika kutia nguvu imani ya Waroma, alitaja kwamba “zawadi anayotoa Mungu ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana yetu.” (Warumi 6:23, NW) Wakati wa huduma yake Yesu, pia, alikuwa na mengi ya kusema juu ya uzima wa milele. Hiyo ni zawadi nzuri ajabu ambayo Mungu anawapa watumishi wake. Mungu anataka watumishi wake waweke macho yao kwenye zawadi, kwa maana kufanya hivyo kunawasukuma wawe waaminifu. Tunapofanya hivyo tunaonyesha imani yenye nguvu katika ahadi zake. Kwenye mikutano yetu ya Kikristo tuna nafasi za kuzungumza mara nyingi juu ya zawadi ambayo Yehova anawapa waaminifu.
Huduma Yetu Yajapokuwa Magumu
13. Maandiko yanatimiza sehemu gani katika kuwa kwetu na maoni ya akili yanayofaa?
13 Kuendelea kwetu kuwa na nia, au maoni ya akili yanayofaa, kutathibitika kuwa kwenye faida sana tunapotekeleza huduma yetu katika hizi siku za mwisho. Ingawa huenda wengine wakapoteza upendo waliokuwa nao kwanza, sisi na tuazimie kwamba jambo hilo lisitupate. Maandiko yenyewe ni msaada wa kuwezesha jambo hilo. (Warumi 15:4) Kupitia kujifunza kwetu hayo tunapata tumaini. Je! wewe unamshukuru Yehova sana sana kwa ajili ya Maandiko, yenye mambo mengi yaliyoandikwa ndani yayo juu ya watumishi waaminifu wa Yehova kama vile mtume Paulo?
14. Paulo aliendeleaje kuwa na maoni yanayofaa akikabiliana na visa vya matatizo?
14 Sisi tungefanyaje kama tungekuwa na visa vya kibinafsi ambavyo Paulo anataja katika 2 Wakorintho 11:23-28? Ni kwa sababu gani Paulo hakukata tamaa? Kwa sababu alikuwa na mradi wake akilini. Huenda tukapatwa na mambo kama hayo. Lakini ni lazima tuendelee kufuatia mradi wetu kwa ajili ya zawadi anayotutolea Mungu. Wakati Paulo alipowaandikia Wafilipi, alionyesha mawazo yake mazuri kwa kutaja kwamba alikuwa na vifungo vya gereza kwa ajili ya kutetea habari njema. (Wafilipi 1:7, 16) Yeye alifahamu ni kwa sababu gani alikuwa huko. Hilo ni jambo la maana tunapokuja chini ya jaribu kama hilo. Zaidi ya hayo, tunajua kwamba Yehova anaweza kututumia sisi kutoa ushuhuda iwe kwa sifa yake.
15. (a) Ni kwa sababu gani kundi la Filipi lilihitaji kitia moyo, na Paulo aliwaambia nini ili awajenge? (b) Kundi katika Roma lilikuwa limetendaje kijapokuwa kifungo cha Paulo?
15 Wafilipi walikuwa wanapata majaribu yanayofanana na yale aliyokuwa akipata Paulo katika Roma. Yeye aliandika hivi: “[Mna] mashindano yale yale mliyoyaona kwangu, na kusikia kwamba ninayo hata sasa.” (Wafilipi 1:30) Katika hali hizo Paulo angeweza kuwaandikia kwa njia yenye kutia moyo. Yeye alisema kwamba habari njema zilikuwa zimejulikana kwa Walinzi wa Praetoria. Kwa wazi ujumbe wa Kikristo ulikuwa umeingia kwenye nyumba yenyewe ya mfalme, wengine wa nyumba hiyo wakawa Wakristo walio wakfu. Kundi katika Roma lilikuwa likishughulikia hali hiyo vizuri, wala halikushuka moyo, kuvunjika moyo au kuogopa kwa ajili ya uhakika wa kwamba Paulo alikuwa amezuiwa gerezani. Badala yake walikuwa wakijishughulisha sana na kazi ambayo Yehova alitaka ifanywe, wakionyesha uhodari hata zaidi katika kusema neno la Mungu bila woga.—Wafilipi 1:12-14; 4:22.
16. Ni nini hasa tunachohitaji kufanya upinzani unapotokea?
16 Upinzani unapotokea, kuna faida kubwa za kudumisha umoja wa kundi la Kikristo. Paulo alikazia muungano na umoja. (Wafilipi 1:27–2:4) Nyakati hizo tunahitaji kusema maneno ya imani kwa mtu na mwenzake, ili tusiache kufuatia mradi. Ni wakati wa kuendelea kuwa na maoni ya upendo na unyenyekevu na kufanyiana mema, kutafuta faida za mtu na mwenzake.—Linganisha Wafilipi 2:19-21.
Kushinda Vizuizi
17. Ni kwa sababu gani hatupaswi kuacha kufuatia mradi wetu wakati matatizo ya afya yanapotokea?
17 Mshiriki wa karibu wa Paulo alikuwa ni Epafrodito. Kwa ajili ya kazi ya Bwana alikaribia kifo sana, lakini hakuna ushuhuda wo wote kwamba tatizo lake la afya lilimfanya aache kuona mradi uliokuwa mbele yake. (Wafilipi 2:25-30) Kwenye 2 Wakorintho 12:7, Paulo alitaja kisa chake mwenyewe cha “mwiba katika mwili,” yawezekana kuwa anasema juu ya tatizo fulani la macho yake. Alisali kwamba tatizo hilo litoke kwake, lakini ombi lake halikutimizwa. Hata hivyo, kuwa na mradi wake akilini kulimsaidia Paulo aendelee kuufuatia yajapokuwa maradhi yo yote ya kimwili. Ingawa alikuwa na udhaifu mbalimbali, alipata njia kwa msaada wa Kristo Yesu.—2 Wakorintho 12:9.
18. Paulo alionyeshaje usawaziko mzuri kuhusiana na vitu vya kimwili?
18 Barua aliyowaandikia Wafilipi (4:11-13) pia ilitaja mambo ya lazima maishani. Kupatwa na upungufu wa vitu kwaweza kuwa jaribu kwa Mkristo juu kama ataacha kufuatia mradi wake. Au je, atakuwa na maoni ya ukomavu kwa kushughulika na tatizo hilo na bado ashiriki katika huduma? (Linganisha Matendo 18:1-4.) Paulo awe alikuwa amepungukiwa na vitu au awe alikuwa navyo tele, huduma yake ilikuja kwanza. Alipokuwa navyo tele hakutumia pindi hiyo kupoteza wakati mwingi akitafuta anasa, bali aliendelea kufuatia mradi wa zawadi.
19. Andiko la Wafilipi 4:6, 7 linatushauri tufanye nini tunapohitaji msaada? Matokeo yanakuwa nini?
19 Paulo hakutaja kila aina ya kisa ambacho Mkristo anaweza kupatwa nacho maishani. Hata hivyo mambo yanapokuja ambayo yanaweza kuingiliana na huduma, tukiwa Wakristo waliokomaa tunapaswa kumgeukia Yehova katika sala, na huu ndio mwendo unaopendekezwa katika Wafilipi 4:6, 7. Halafu Yehova atatupa amani ya akili, atusaidie tufikiri kwa njia inayofaa na kutusaidia tushinde matatizo tunapoendelea kuwa wahudumu wake waaminifu. Sala inatusaidia tudumishe imani yetu na kuendelea kufuatia mradi wetu.
20. (a) Mifano ya waaminifu wenye umri mkubwa zaidi katika ukweli inatutiaje moyo? (b) Sisi tunapaswa kufanya nini? Kwa sababu gani?
20 Kuna wengi wanaoshirikiana na makundi leo ambao wamemtumikia Yehova kwa makumi mengi ya miaka. Wote wamepitia majaribu huku wakiendelea na huduma yao. Lakini Yehova amewasaidia, kwa hiyo wanaendelea kufuatia mradi wa zawadi. Tunamshukuru Yehova kwamba, kama walivyokuwako katika karne ya kwanza, katika nyakati za kisasa kuna ndugu na dada ambao ni mifano ya uvumilivu, waaminifu katika utumishi wao wa Ufalme na wenye kuendelea kuweka macho kwenye zawadi. Wale ambao ni wachanga au wapya zaidi katika “Njia hii” wanafaidika kwa kuchunguza maandishi ya mtume Paulo au watumishi waaminifu katika kundi la kisasa, wakiangalia jinsi hawa wameshughulikia matatizo yao. (Matendo 9:2; Waebrania 13:7) Kila mmoja wetu na atumie kila pindi kutia mwenzake moyo ili tuweze kuvumilia kwa uaminifu katika utumishi tuliouchukua na kwa umoja kuendelea kufuatia mradi ambao Yehova ameweka mbele yetu. Kwa kufanya hivyo, tuna taraja la kumtumikia Yehova Mungu milele katika ushirika wa furaha na walio waaminifu.—Wafilipi 3:13-16.
Mambo Makuu ya Kuweka Akilini
◻ Hali ya kwanza ya maisha ya kibinafsi ya Paulo ilikuwa nini, na aliitumiaje kutia moyo akina ndugu?
◻ Mifano ya Kristo Yesu na Paulo inatuonyeshaje ni nini maoni ya Kikristo ya ukomavu?
◻ Tunaweza kuonyeshaje umoja wetu upinzani unapotokea?
◻Ni kwa sababu gani tunapaswa kuendelea kufuatia mradi wetu?
[Picha katika ukurasa wa 12]
Kristo Yesu alijitahidi sana kutia nguvu wale waliokuwa na mahitaji ya kiroho