Nafasi Kubwa Zaidi kwa Vijana
“[Utawa] hufaa kwa mambo yote; yaani, unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye. Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa.”—1 Timotheo 4:8, 9
1, 2. (a) Vijana wengi wanaona nini kuwa ndizo nafasi za maana, na ni maswali gani yanayotokezwa? (b) Ni kwa sababu gani kuna mikazo ya pekee juu ya vijana wa leo?
NI NAFASI gani kubwa zaidi unayotolewa na maisha? Uchunguzi mbalimbali wa karibuni wa kisehemu cha vijana unaonyesha kwamba walio wengi wanafikiria “kuwa na kazi ninayofurahia” na “kuwa na pesa nyingi” ndiyo miradi yao ya maana zaidi. Hesabu zenye kuongezeka za vijana wanafikiria kufuatia kazi fulani maishani, na katika sehemu fulani wanaingia katika vyuo vikuu kwa hesabu kubwa zisizopata kufikiwa tena wakiwa wanatafuta kazi zenye kulipa mshahara mnono. Wengi wanatazamia nafasi hizo za kimwili ili wapate usalama, nguvu, na kufanikiwa maishani. Ikiwa wewe ni kijana, je, ndivyo unavyohisi? Na ninyi ambao ni watu wazima, hasa wazazi, mnawezaje kweli kweli kuziona nafasi hizo? Je! hizo ndizo njia za kuwa na “maisha bora”?
2 Ikiwa kuna wakati vijana wanapohitaji nguvu na kufanikiwa, ni sasa wakati wa hizi “siku za mwisho” ambapo nyakati ni “ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1-5, NW) Vijana wa leo wamekua wakiwa chini ya mikazo ambayo ilikuwa haiwaziki kizazi kimoja kilichopita. Mabadiliko ya upesi sana katika jamii, kama vile kuvunjika kwa maisha na adili za jamaa, yamesababisha mvurugo mkubwa wa maono ya ndani.
Uhitaji wa Nguvu na Kufanikiwa
3, 4. Ni ushuhuda gani unaoonyesha kwamba vijana wengi hawana nguvu za kindani, na ni kwa sababu gani faida za kimwili hazitoi jambo hilo?
3 Vijana wengi zaidi na zaidi wanakuta kwamba hawana nguvu za ndani za kukabiliana na mikazo ya maisha. (Linganisha Waefeso 3:16.) Ripoti ya karibuni ya Taasisi ya Kitaifa ya Afya ya Akili inamalizia kwa kusema kwamba mmoja kati ya vijana watano anashuka moyo vibaya sana.a Tangu 1961 hadi 1975, hesabu ya vijana wanaojiua katika United States imeongezeka zaidi ya mara mbili! Katika nchi hiyo moja karibu vijana 8,000 wanajiua kila mwaka, hata hivyo mara 50 ya hesabu hiyo wanajaribu kujiua. Wataalamu fulani wanalitaja tatizo hilo kuwa pigo. Pia ripoti zinaonyesha kwamba hesabu ya kushangaza ya vijana wanaolazwa katika hospitali za magonjwa ya akili.b
4 Bila shaka, si vijana wote wanaoishi chini ya hali zinazotoa nafasi za kuwa na mali. Hata hivyo, unapofikiria kwamba ripoti zilizotangulia kutajwa zinahusu nchi kubwa ambako nafasi za kuwa na mali ni tele, ni wazi kwamba mali hizo peke yake hazisaidii vijana ‘waondoe majonzi moyoni wao na ubaya mwilini mwao.’(Mhubiri 11:9,10) Faida za kimwili zinaleta nguvu chache kwa mtu ambaye moyo wake unasumbuliwa na mashaka ya kibinafsi yenye huvunja moyo, ukosefu wa usalama, au hatia Biblia inasema hivi: Ukizimia [ukivunjika moyo] siku ya taabu, nguvu zako [zitakuwa] ni chache.”—Mithali 24:10.
5, 6 Je? kuwa na vitu vya kimwili kutaleta “maisha Wakati ujao? Onyesha mfano.
5 Lakini je, kuwa na mali hatimaye kutaleta uradhi, “maisha bora”? Mfalme Sulemani aliyekuwa tajiri alikubali hivi: Nikaziangalia kazi zote zilizofanywa kwa mikono yangu, na taabu yote niliyotaabika katika kuzitenda; na tazama, yote ni ubatili na kujilisha upepo.” (Mhubiri 2:3-11) Ingawa mambo aliyotimiza yalimletea raha fulani, bado aliona utupu fulani, ubatili.
6 Wengi leo wanatangaza elimu ya juu kuwa moja ya njia za kuelekeza kwenye “maisha bora” ya wakati ujao. Mmoja aliyekuwa gavana wa jimbo la United States hata alisema elimu hiyo ni ya “lazima ili kuwa na nguvu, kufanikiwa na kuishi.” Je! ndivyo ilivyo kweli? Watu 846 waliohitimu katika chuo kikuu chenye sifa walikusanya “ripoti ya darasa” juu ya jinsi hali yao ilivyokuwa miaka kumi baada ya kuhitimu. “Ingawa uchangamshi wa kupendeza unasambaa katika ripoti hiyo,” akasema mshiriki mmoja wa darasa, “chini yake kuna msingi wa matazamio mabaya, uchungu na hata kukata tamaa.” Baada ya miaka 25, mmoja aliyehitimu alikuwa amefikia “miradi fulani ya kifedha,” lakini alikubali hivi: “Mambo niliyoshindwa katika maisha yangu ya kibinafsi yanayazidi mambo niliyotimiza hivi kwamba yote hayo yatapotelea mbali yasiripotiwe hata.” Je! hayo ndiyo mambo bora zaidi ambayo maisha yanatoa?
Nafasi Kubwa Zaidi
7. Timotheo angaliweza kujizoeza kwa ajili ya kazi gani za maishani, lakini Paulo alipendekeza nini?
7 Katika barua zake zilizoongozwa kwa roho alizoandikia mwanafunzi Mkristo Timotheo, mtume Paulo alielekeza kwenye jambo bora zaidi. Mwanamume huyo kijana alikuwa amepewa mgawo atumikie katika Efeso, kimoja cha vituo vikuu zaidi vya kibiashara katika nyakati za kale. Lo! bila shaka aliona kazi ambazo angaliweza kufuatia maishani! Yeye mwenyewe angaliweza kujitahidi kuwa mfanyi-biashara mwenye kufanikiwa au kutafuta sifa ya kujulikana ama kwenye shule ya Tirano au kwenye jumba la michezo la mahali hapo. (1 Timotheo 1:3; Matendo 19:1, 9, 29) Bila shaka Timotheo angaliweza kujizoeza kwa ajili ya kazi fulani ambayo ingempatia mapesa mengi, lakini Paulo aliandika hivi: “Nawe ujizoeze kupata [utawa]. Kwa maana kujizoeza kupata nguvu za mwili kwafaa kidogo, lakini [utawa] hufaa kwa mambo yote; yaani, unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.” Ndiyo, utawa “hufaa kwa mambo yote.” Hiyo haikuwa dhana tu, kwa maana Paulo aliongeza hivi: “Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa.” Kwa alivyojionea, Paulo alijua jambo ambalo lingetokeza njia bora zaidi ya maisha.—1 Timotheo 4:7-9; 2 Wakorintho 6:10.
8, 9. (a) Utawa ni nini? (b) Nafasi yako kubwa zaidi ni nini, na ni kwa sababu gani jitihada inahitajiwa ili uitumie kwa faida nzuri?
8 Utawa ni nini? Ni mtu kujishikamanisha na Mungu kwa kusukumwa na moyo unaoongozwa na kuthamini sana sifa zake zinazovutia. Ingawa “kicho” (Waebrania 12:28) kwa msingi maana yake ni hofu ya kimungu ya kutofanya kisichompendeza Mungu, “utawa” ni itikio la moyo litakalokusukuma uishi katika njia inayompendeza Mungu kwa sababu unampenda.c Sifa hiyo ya moyo inaongoza kwenye “ukaribu na Mungu,” uhusiano wa kibinafsi ambao katika huo unahisi kibali na msaada wake. (Ayubu 29:4, NW) Nafasi ya kuwa na urafiki huo wa kibinafsi pamoja na Mungu ni yenye thamani zaidi ya kinginecho chote ambacho huenda kikatolewa kwako.—Linganisha Yeremia 9:23, 24.
9 Je! kuwa na wazazi wenye utawa au kubatizwa kuwa Mkristo kunaufanya uhusiano huo na Mungu ujilete wenyewe? Hapana, kwa sababu m0oyo mweupe ni lazima usitawishwe, pamoja na sifa nyingine za wema wa Kikristo. (2 Petro 1:5-8) Ni lazima uwe mtu ‘ambaye moyo wake unamhimiza’ kufanya matendo ya ‘utawa.’ (Linganisha Kutoka 36:2, UV; 2 Petro 3:11, NW; Kolosai 3:22.) Ingawa alilelewa tangu utoto katika njia ya ukweli, Timotheo kusitawisha utawa. Leo, pia, jitihada bidii nyingi ni ya lazima. Hata hivyo, utawa huo utathibitika kuwa “faida kubwa. (1 Timotheo 6:6) Jinsi gani?
Njia ya Maisha ya Juu
10, 11. Utawa uliwekaje juu maisha ya Timotheo?
10 Katika Efeso, Timotheo alifuatia utawa miongoni mwa watu waliokuwa ‘wakienenda katika ubatili wa [akili] zao.’ (Waefeso 4:17) Yaliyojaa akili zao hayakuwa na faida yo yote bali yalikuwa ni ubatili. “Inastaajabisha!” asema mwanafunzi wa Biblia R. C. H. Lenski juu ya Waefeso 4:17. “Watu wenye kufikiri, wenye akili zenye kutaka, viumbe wenye akili timamu, wakitembea na wakiendelea kutembea maishani mwote, wakifuata amri za akili inayowaongoza kwenye kila hatua na mwishowe kuwaongoza kwenye hakuna kitu, kwenye kushindwa vibaya sana kunakoleta msiba!”
11 Timotheo aliweza kuona kwamba mwendo wa maisha wa Waefeso ulikuwa ni ubatili na wenye kushusha tabia njema. Wengi waliabudu mungu wa kike Artemi, lakini ibada yao isiyotegemezwa juu ya kufikiri kuzuri ilielekezwa kwenye sanamu isiyo na uhai. Ilitia ndani karamu zenye utovu mkubwa wa adabu na sherehe ya kufanya umalaya. (Matendo 19:23-34) Njia ya Maisha ya Timotheo, hata hivyo, ilikuwa juu ya ile ya mataifa, waliokuwa “wamefarikishwa na uzima wa Mungu . . . [na] kufa ganzi.” (Waefeso 2:6; 4:18, 19) Mwendo wake wa kimungu katika kuishi “uzima wa Mungu” ulikuwa umemfanya awe na Rafiki mkubwa zaidi katika ulimwengu wote! Nafasi ya kusitawisha uhusiano huo pamoja na Mungu aliye hai kupitia utawa ni yenye thamani zaidi! Je! unaweza kuifikia?
12. Kijana mmoja Mkristo alisema nini juu ya faida kubwa” ya utawa? Wewe una maoni gani juu ya hilo?
12 Wengi leo wanaabudu ngono, anasa, utajiri, na elimu ya juu kwa bidii ile ile ambayo Waefeso wa kale walimwabudu Artemi. (Mathayo 6:24; Waefeso 5:3-5; Wafilipi 3:19) Lakini, wale wanaofuatia utawa wanafurahia uzima ulio wa hali bora zaidi. “Nawatazama vijana niliokuwa nikishirikiana nao kabla sijaanza kujifunza Biblia,’ anaripoti Mkristo mmoja mwenye miaka 24. “Nusu yao wako gerezani. Wengi wanatumia dawa za kulevya, na wengi wa wasichana wana watoto haramu. Maisha zao zimevurugika. Wengine wao hata wamekufa. Nashukuru sana kuweza kuyatazama maisha yangu na kujivunia ninayoona.” Vijana wengine Wakristo wanakubaliana na hayo kwa moyo wote!
13. Ni kwa sababu gani kufuata amri katika 2 Timotheo 4:5 kunaongeza maana kwenye maisha?
13 Wale wanaoishi kwa utawa wana hazina ya huduma. (2 Wakorintho 4:1, 7; 2 Timotheo 4:5) Jambo hilo linatoa kusudi halisi na mwito wa kushindana. Badala ya msisimuko wa uwongo wa wonyesho Fulani wa kubuni tu wa televisheni au sinema, Wakristo wanaohusika katika huduma wanatembelea nyumba za watu halisi ili wawasaidie. Wanashughulika pia na matatizo halisi. Ni furaha isiyoelezeka iliyoje kuona watu ambao wameishi maisha yasiyo ya adili, ya jeuri, au yasiyo na tumaini wakikubali maagizo ya Biblia na kuondolea mbali tabia mbaya za zamani, na kusitawisha hali ya kujiheshimu, na kumtumikia Yehova. Hakuna kazi nyingine ya kufuatiwa maishani iliyo na maana kama hiyo au yenye kuleta faida ya kudumu!
Uradhi na Dhamiri Safi
14, 15. Uradhi wa utawa juu ya pesa unafanyaje maisha kuwa bora?
14 “[Utawa] pamoja na kuridhika ni faida kubwa. . . . Ila tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo. Lakini hao watakao kuwa na mali . . . [wamejichoma] kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:6-10) Mwaka 1981 uchunguzi mmoja uliofanywa na kichapo Psychology Today ulifunua kwamba vijana wanafikiria “zaidi sana” juu ya pesa kuliko watu wengine wa umri wo wote. Hata hivyo, nusu ya kikundi cha waliojibu waliohangaikia zaidi pesa (kutia walio matajiri na maskini) walilalamika juu ya “wasiwasi na hangaiko la daima.”
15 Kijana mmoja katika Japani alifaulu kushinda ‘umaskini akawa tajiri,’ lakini katika kufanya hivyo aliharibu afya yake. Baadaye, kwa msaada wa funzo la Biblia, alisitawisha utawa. “Ninapofikiria wakati ambao mradi wangu mkuu maishani ulikuwa ni utajiri, haiwezekani kulinganisha jinsi nilivyo mwenye furaha zaidi tangu nilipobadili mradi wangu,” ndivyo anavyomalizia. “Kweli kweli hakuna lo lote linaloweza kulingana na uradhi na kutosheka kunakoletwa na kutumia maisha ya mtu katika utumishi wa Muumba Mkuu.”d—Mithali 10:22; Mhubiri 5:10-12.
16. Matokeo ni nini kwa wale wanaoshindwa ‘kuwa na dhamiri njema’?
16 Paulo alimsihi Timotheo ‘awe na dhamiri njema.’ Jinsi gani? Njia moja ilikuwa kwake kutendea wanawake “katika usafi wote.” (1 Timotheo 1:19; 5:2) Hata hivyo, usafi unakosekana kwa vijana wengi kwa kuwa dhamiri zao zimechomwa moto zikafa ganzi. (1 Timotheo 4:2) Lakini ukosefu wa adili hauleti amani ya ndani na uradhi. Uchunguzi mmoja ulifikiria nia na mwenendo wa ngono wa wabalehe mia kadha. Kuhusu wale waliokuwa wenye kufanya ngono ovyoovyo zaidi, ripoti hiyo ilisema: “Wanasadiki wanatenda wakiwa na kusudi na uradhi mdogo.” Karibu nusu ya hao walikuwa na maoni haya: “Kwa jinsi ninavyoishi sasa, mwingi wa uwezo wangu utapotea.”
17. Ni kwa sababu gani ‘upendo unaotokezwa na dhamiri njema’ unatusaidia kupata faida bora zaidi maishani?
17 Ikiwa, baada ya wakati, wenzi wanafuatia ndoa yenye heshima, watafaidika kwa kuonyesha “upendo utokao katika moyo safi na dhamiri njema.” (1 Timotheo 1:5) Mwaka 1984 kichapo Journal of Marriage and the Family kiliripoti kwamba uchunguzi wa wenzi wa ndoa 309 wa hivi karibuni ulionyesha kwamba ngono kabla ya ndoa ilishirikishwa na “upungufu wa kutosheka kwa wenzi wote wawili wa ndoa.” Lakini ni tofauti kama nini na wale walio safi! “Ni hisia ya kupendeza kuangalia nyuma na kujua mimi ni safi,” asema mke kijana mmoja Mkristo ambaye sasa amekuwa aliyeolewa kwa miaka saba. Ndiyo, dhamiri njema ni thawabu kubwa kwa vijana wanaokuwa “kielelezo . . . katika . . . usafi.”—1 Timotheo 4:12.
Nguvu za Ndani
18, 19. (a) Timotheo alilazimika kukabiliana na mikazo gani? (b) Mungu alimsaidiaje?
18 Bila shaka Timotheo alikabili mikazo mingi katika Efeso. Vishawishi vya mji wenye kufanikiwa na usio na adili wenye kukazia ‘raha na michezo’ vingaliweza kuleta mkazo wa kutoka nje. Bila shaka inaelekea haya ya Timotheo na pia ‘magonjwa yaliyompata mara kwa mara’ yalitokeza mikazo ndani yake. (1 Timotheo 5:23) Lakini Paulo alimkumbusha hivi: “Mungu alitupa si roho ya woga, bali ile ya nguvu na ya upendo na ya utimamu wa akili.”—2 Timotheo 1:7, NW.
19 Hakika, jinsi walivyo wengi wa rika lako wanaotamani nguvu hizo! Mwanamke mmoja kijana alishinda kabisa maisha ya umalaya na ya kutumia dawa za kulevya. “Ilikuwa kwa msaada wa Yehova tu,” akasema. “Kuna nyakati ambazo hisia hizo za zamani zinanirudia, lakini naanza kusali tu—mara hiyo. Uweza wa kushinda matatizo hayo unasisimua zaidi ya jambo lo lote ambalo nimepata kutimiza maishani mwangu.” Hakuna shaka, Mungu anaweza ‘kutia nguvu’ ndani yako na kukupa nguvu za ndani ukabiliane na mkazo wo wote na kufanya maamuzi yaliyo timamu.—2 Timotheo 4:17.
20, 21. (a) Simulia nyingine za faida za utawa. (b) Ni jambo gani litakalozungumzwa katika Makala inayofuata?
20 Kwa hiyo utawa unakuletea faida nyingi. “Mwendo wa maisha” yako unakuwa na kusudi linalopita sana miradi ya wale wanafuatia nafasi za mali tu. (2 Timotheo 3:10, NW) Ni kama alivyosema kijana mmoja. Mkristo aliyekataa kudhaminiwa chuoni akawa mwevanjeli wa wakati wote: “Nina kazi ya maishani iliyo bora zaidi ambayo ingetamaniwa na kila mtu, kuwa mwalimu wa habari njema na kuwasaidia wengine wajifunze juu ya Baba yetu mwenye upendo! Na ‘faida ya ziada’—utu wangu mwenyewe ukawa bora zaidi—inafaa zaidi ya cho chote ambacho mtu ye yote anaweza kutoa. Ongezea hayo thawabu ya kuishi katika paradiso milele bila huzuni tena. Sasa jiulize: Ni maisha gani bora zaidi ambayo ye yote angetaka?”
21 Unaweza kusema, ‘Naweza kusitawishaje utawa?’ Ili kupata jibu, soma makala inayofuata.
[Maelezo ya Chini]
a “Hesabu fulani ya wataalamu wa ukuzi na tabia ya wabalehe wanaona kushuka moyo huko kuwa sababu kuu inayotokeza matatizo mazito ya vijana kama vile kutoroka na kuleta matata shuleni, kutumia vibaya dawa za kulevya na kileo, kufanya ngono, kupata mimba, kutoroka nyumbani na kujiua,” ndivyo anavyoripoti mbuni wa kitabu, Kathleen McCoy, katika kitabu Coping with Teenage Depression.
b Ingawa katika United States hesabu ya wagonjwa wa vikundi vyote vya umri wanaolazwa katika hospitali imepungua wakati wa kipindi cha miaka 13, kikundi cha wenye umri wa miaka 15-24 kimeongezeka kwa asilimia 19, na kikundi cha walio chini ya miaka 15 kimeongezeka kwa asilimia 158!
c “Hisia ya moyo inayojitokea yenyewe [kumwelekea Mungu],” ndivyo Lexicon ya Edward Robinson inavyofafanua neno la awali la Kigiriki eu·seʹbei·a. J. A. H. Tittmann, katika kitabu chake Remarks on the Synonyms of the New Testament, anaongeza hivi: “[Utawa] ni kumwogopa Mungu kunakojionyesha kwa matendo, . . . lakini [kicho] kinaonyesha maelekeo yale, yanayohofu na kuepuka kufanya cho chote kilicho kinyume cha yanayofaa, . . . [utawa] ni nguvu za kumcha Mungu maishani.”
d Soma hadithi ya maisha ya Shozo Mima, “Finding Something Better Than Wealth,” katika Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) wa Machi 1, 1978.
Je! Unakumbuka?
◻ Ni kwa sababu gani nafasi za kuwa na mali ni zenye thamani ndogo tu?
◻ Nafasi yako kubwa zaidi ni nini?
◻ Utawa unatoa nini kinachokusaidia upate faida bora zaidi maishani?
[Picha katika ukurasa wa 11]
Ni nini kitakachokufanya uwe na furaha ya kweli?
[Picha katika ukurasa wa 13]
Timotheo alijizoeza utawa ukiwa lengo lake. Kufanya hivyo kuliinua maisha yake juu ya yale ya Waefeso wasiokuwa na adili