Tieni Ujitoaji Kimungu Katika Uvumilivu Wenu
“Katika imani yenu tieni . . . saburi [uvumilivu, NW], na katika saburi yenu utauwa [ujitoaji kimungu, NW].”—2 PETRO 1:5, 6.
1, 2. (a) Kuanzia miaka ya 1930, ni nini kilichowapata Mashahidi wa Yehova katika mabara yaliyokuwa chini ya utawala wa Nazi, na kwa nini? (b) Watu wa Yehova walikabilianaje waliponyanyaswa kwa ukatili?
KILIKUWA kipindi chenye giza katika historia ya karne ya 20. Kuanzia miaka ya 1930, maelfu ya Mashahidi wa Yehova katika mabara yaliyokuwa chini ya utawala wa Nazi walikamatwa isivyo haki na kufungwa katika kambi za mateso. Kwa nini? Kwa sababu walithubutu kuendelea kutokuwamo na kukataa kusema heil Hitler. Walitendwaje? “Hakuna kikundi kingine cha wafungwa . . . kilichopatwa na ukatili wa askari wa SS wa njia ile ambayo Wanafunzi wa Biblia [Mashahidi wa Yehova] walipatwa nao. Ulikuwa ukatili wenye mfululizo wa mateso mengi ya kimwili na kiakili, ambao hakuna lugha ulimwenguni inayoweza kueleza.”—Karl Wittig, aliyekuwa ofisa wa serikali ya Ujerumani.
2 Mashahidi walikabilianaje? Katika kitabu chake The Nazi State and the New Religions: Five Case Studies in Non-Conformity, Dakt. Christine E. King alisema hivi: “Serikali ilikosa kufanikiwa dhidi ya Mashahidi tu [tofauti na vikundi vingine vya kidini].” Naam, Mashahidi wa Yehova kwa ujumla walisimama imara, hata ingawa kwa mamia yao, hilo lilimaanisha kuvumilia hadi kifo.
3. Ni nini kimewawezesha Mashahidi wa Yehova wavumilie majaribu makali?
3 Ni nini kimewawezesha Mashahidi wa Yehova wavumilie majaribu hayo si katika Ujerumani wa Nazi tu bali ulimwenguni pote? Baba yao wa kimbingu amewasaidia wavumilie kwa sababu ya ujitoaji kimungu wao. “Bwana [Yehova, NW] ajua kuwaokoa watauwa [watu wenye ujitoaji kimungu, NW] na majaribu,” mtume Petro aeleza. (2 Petro 2:9) Mapema zaidi katika barua iyo hiyo, Petro alikuwa amewashauri Wakristo hivi: “Katika imani yenu tieni . . . saburi [uvumilivu, NW], na katika saburi yenu utauwa [ujitoaji kimungu, NW].” (2 Petro 1:5, 6) Kwa hiyo uvumilivu unahusiana kwa ukaribu na ujitoaji kimungu. Kwa kweli, ili kuvumilia hadi mwisho, ni lazima ‘tufuatie ujitoaji kimungu’ na kuudhihirisha. (1 Timotheo 6:11, NW) Lakini ujitoaji kimungu ni nini hasa?
Maana ya Ujitoaji Kimungu
4, 5. Ujitoaji kimungu ni nini?
4 Nomino ya Kigiriki kwa neno “ujitoaji kimungu” (eu·seʹbei·a) yaweza kutafsiriwa kihalisi kuwa “kustahi kunakofaa.”a (2 Petro 1:6, Kingdom Interlinear) Hilo huonyesha hisia changamfu ya moyoni kumwelekea Mungu. Kulingana na W. E. Vine, kivumishi eu·se·besʹ, kinachomaanisha kihalisi “-enye staha inayofaa,” humaanisha “ile nishati ambayo, ikielekezwa na kicho kitakatifu kwa Mungu, huonekana katika utendaji wa kujitoa.”—2 Petro 2:9, Int.
5 Kwa hiyo usemi “ujitoaji kimungu” unarejezea staha au ujitoaji kwa Yehova ambao hutusukuma kufanya yale yanayompendeza. Hayo yanafanywa hata tunapokabili majaribu magumu kwa sababu tunampenda Mungu kutoka moyoni. Ni ushikamano wa kibinafsi kwa Yehova, wenye uaminifu-mshikamanifu ambao huonekana katika njia tunayoishi maisha zetu. Wakristo wa kweli wanahimizwa kusali kwamba waweze kuongoza “maisha ya utulivu na amani katika utauwa [ujitoaji kimungu, NW] wote.” (1 Timotheo 2:1, 2) Kulingana na watunga-kamusi J. P. Louw na E. A. Nida, “katika lugha kadhaa [eu·seʹbei·a] katika 1 Tm 2.2 laweza kutafsiriwa kwa kufaa kuwa ‘kuishi kama vile Mungu angetaka tuishi’ au ‘kuishi kama vile Mungu ametuambia twapaswa kuishi.’”
6. Kuna uhusiano gani kati ya uvumilivu na ujitoaji kimungu?
6 Sasa tunaweza kufahamu vizuri zaidi uhusiano kati ya uvumilivu na ujitoaji kimungu. Kwa sababu tunaishi kama vile Mungu angetaka tuishi—kwa ujitoaji kimungu—tunapatwa na chuki ya ulimwengu, ambayo sikuzote huleta majaribu ya imani. (2 Timotheo 3:12) Lakini hakuna njia yoyote tungechochewa kuvumilia majaribu hayo ikiwa isingekuwa kwa sababu ya ushikamano wetu wa kibinafsi kwa Baba yetu wa kimbingu. Zaidi ya hayo, Yehova huitikia ujitoaji huo wa kuhisiwa moyoni. Ebu wazia jinsi ambavyo ni lazima iwe anahisi anapoangalia chini kutoka mbinguni na kuona wale ambao, kwa sababu ya ujitoaji wao kwake, wanajitahidi kumpendeza kujapokuwa upinzani wa kila aina. Haishangazi kwamba ana nia ya “kuwaokoa watauwa [watu wenye ujitoaji kimungu, NW] na majaribu”!
7. Kwa nini ni lazima ujitoaji kimungu ukuzwe?
7 Hata hivyo, hatuzaliwi tukiwa na ujitoaji kimungu, wala hatuupati moja kwa moja kutoka kwa wazazi wanaomwogopa Mungu. (Mwanzo 8:21) Badala ya hivyo, ni lazima ukuzwe. (1 Timotheo 4:7, 10) Ni lazima tujitahidi kutia ujitoaji kimungu katika uvumilivu wetu na imani yetu. Petro asema hilo huhitaji ‘kujitahidi sana.’ (2 Petro 1:5) Basi, tunaweza kupataje ujitoaji kimungu?
Tunapataje Ujitoaji Kimungu?
8. Kulingana na mtume Petro, ni nini ufunguo wa kupata ujitoaji kimungu?
8 Mtume Petro alieleza ufunguo wa kupata ujitoaji kimungu. Alisema hivi: “Neema na iwe kwenu na amani iongezwe katika kumjua Mungu na Yesu Bwana wetu. Kwa kuwa uweza wake wa Uungu umetukirimia vitu vyote vipasavyo uzima na utauwa [ujitoaji kimungu, NW], kwa kumjua [ujuzi sahihi juu ya, NW] yeye aliyetuita kwa utukufu wake na wema wake mwenyewe.” (2 Petro 1:2, 3) Kwa hiyo ili kutia ujitoaji kimungu katika imani yetu na uvumilivu wetu, ni lazima tukue katika ujuzi sahihi, yaani, ujuzi wote au kamili, juu ya Yehova Mungu na Yesu Kristo.
9. Ni kielezi gani kinachoweza kuonyesha kwamba kuwa na ujuzi sahihi juu ya Mungu na Kristo kwahusisha zaidi ya kujua tu wao ni nani?
9 Ni nini maana ya kuwa na ujuzi sahihi juu ya Mungu na Kristo? Kwa wazi, kunatia ndani zaidi ya kujua wao ni nani. Kwa kutoa kielezi: Huenda ikawa unajua jirani yako ni nani na huenda hata ukamsalimu kwa jina. Lakini, je, ungemkopesha kiasi kikubwa cha fedha? Sivyo, isipokuwa tu kama ungemjua yeye ni mtu wa aina gani. (Linganisha Mithali 11:15.) Vivyo hivyo, kumjua Yehova na Yesu kwa usahihi, au kikamili, hakumaanishi kuamini tu kwamba wako na kujua majina yao. Ili kuwa na nia ya kuvumilia majaribu kwa ajili yao hata hadi kifo, ni lazima tuwajue kikweli kwa ukaribu sana. (Yohana 17:3) Hilo lahusisha nini?
10. Kuwa na ujuzi sahihi juu ya Yehova na Yesu kwahusisha mambo gani mawili, na kwa nini?
10 Kuwa na ujuzi sahihi, au kamili, juu ya Yehova na Yesu huhusisha mambo mawili: (1) kupata kuwajua wakiwa watu—sifa zao, hisia zao, na njia zao—na (2) kuiga kielelezo chao. Ujitoaji kimungu huhusisha ushikamano wa kibinafsi kwa Yehova, wenye kuhisiwa moyoni, na unadhihirishwa kwa njia tunayoishi maisha zetu. Kwa hiyo, ili kuupata ni lazima tumjue Yehova binafsi na kufahamu kikamili mapenzi yake na njia zake kadiri hilo liwezekanavyo kibinadamu. Ili kumjua Yehova kikweli, ambaye tumeumbwa kwa mfano wake, ni lazima tutumie ujuzi huo na kujitahidi kuwa kama yeye. (Mwanzo 1:26-28; Wakolosai 3:10) Na kwa kuwa Yesu alimwiga Yehova kikamilifu katika yale aliyosema na kufanya, kumjua Yesu kwa usahihi ni msaada wenye thamani katika kukuza ujitoaji kimungu.—Waebrania 1:3.
11. (a) Tunaweza kupataje ujuzi sahihi juu ya Mungu na Kristo? (b) Kwa nini ni jambo la maana kutafakari juu ya yale tunayosoma?
11 Lakini, tunaweza kupataje ujuzi huo sahihi juu ya Mungu na Kristo? Kwa kujifunza Biblia na vichapo vyenye msingi wa Biblia kwa bidii-nyendelevu.b Hata hivyo, ikiwa funzo letu la Biblia la kibinafsi litatokeza kupata kwetu ujitoaji kimungu, ni muhimu kwetu kuchukua wakati wa kutafakari, yaani, kufikiria, au kutia maanani, yale tunayosoma. (Linganisha Yoshua 1:8.) Kwa nini hilo ni la maana? Kumbuka kwamba ujitoaji kimungu ni hisia changamfu, yenye kuhisiwa moyoni kuelekea Mungu. Katika Maandiko, kutafakari hushirikishwa tena na tena na moyo wa kitamathali—mtu wa ndani. (Zaburi 19:14; 49:3; Mithali 15:28) Tunapofikiria kwa uthamini yale tunayosoma, yanachujwa hadi kwenye mtu wa ndani, hivyo yakichochea hisia zetu, yakigusa hisiamoyo zetu, na kuvuta fikira zetu. Ndipo tu kujifunza kunapoweza kuimarisha ushikamano wetu wa kibinafsi kwa Yehova na kutusukuma kuishi katika njia inayompendeza Mungu hata tunapokabili hali ngumu au majaribu makali.
Kuzoea Ujitoaji Kimungu Nyumbani
12. (a) Kulingana na Paulo, Mkristo anaweza kuzoeaje ujitoaji kimungu nyumbani? (b) Kwa nini Wakristo wa kweli huwajali wazazi waliozeeka?
12 Ujitoaji kimungu unapaswa kuzoewa nyumbani kwanza. Mtume Paulo asema hivi: “Lakini mjane akiwa ana watoto au wajukuu, na wajifunze kwanza kuyatenda yaliyo wajibu wao [ujitoaji kimungu, NW] kwa jamaa zao wenyewe, na kuwalipa wazazi wao. Kwa kuwa hili lakubalika mbele za Mungu.” (1 Timotheo 5:4) Kama vile Paulo anavyosema, kuwatunza wazazi waliozeeka, ni wonyesho wa ujitoaji kimungu. Wakristo wa kweli huandaa msaada huo si kwa sababu tu ya kuhisi wajibu bali kwa sababu ya kuwapenda wazazi wao. Lakini, zaidi ya hayo, wanatambua umaana ambao Yehova huweka juu ya mtu kuitunza familia yake. Wanafahamu sana kwamba kukataa kuwasaidia wazazi wao wanapokuwa na uhitaji kungekuwa sawasawa na ‘kuikana imani ya Kikristo.’—1 Timotheo 5:8.
13. Kwa nini kuzoea ujitoaji kimungu nyumbani kwaweza kuwa jambo gumu, lakini ni uradhi gani unaotokana na mtu kuwatunza wazazi wake?
13 Kwa kweli, si rahisi sikuzote kuzoea ujitoaji kimungu nyumbani. Huenda ikawa washiriki wa familia wako mbalimbali sana. Huenda ikawa watoto ambao wamekuwa watu wazima wanalea familia zao wenyewe na huenda ikawa wanang’ang’ana kiuchumi. Asili au kadiri ya utunzaji unaohitajiwa na mzazi yaweza kuathiri afya ya kimwili, kiakili, na kihisiamoyo ya wale wanaoandaa msaada huo. Hata hivyo, mtu aweza kuwa na uradhi wa kweli akijua kwamba kuwatunza wazazi wake si “kuwalipa” tu bali pia kwampendeza Yule “aliye asili ya jamaa zote [kila familia, NW] duniani na mbinguni.”—Waefeso 3:14, 15, HNWW.
14, 15. Simulia kielelezo cha utunzaji wa kuonyesha kumwogopa Mungu kwa upande wa watoto kwa mzazi fulani.
14 Fikiria kielelezo kimoja chenye kugusa moyo kwelikweli. Ellis na ndugu na dada zake watano wana kazi ngumu ya kumtunza baba yao nyumbani. “Katika 1986 baba yangu alipatwa na ugonjwa wa ghafula, uliompooza kabisa,” aeleza Ellis. Hao watoto sita hushiriki katika kutunza mahitaji ya baba yao, kuanzia kumwogesha hadi kuhakikisha kwamba anageuzwa kwa ukawaida ili asipatwe na vidonda vinavyosababishwa na kulala kwa upande mmoja tu kitandani. “Sisi humsomea vitabu, huongea naye, humchezea muziki. Hatujui kwa hakika kama anafahamu yale yanayoendelea karibu na yeye, lakini sisi humtendea kama kwamba anafahamu kila kitu kikamili.”
15 Kwa nini watoto hao humtunza baba yao hivyo? Ellis aendelea hivi: “Baada ya kifo cha mama yetu katika 1964, Baba alitulea akiwa peke yake. Wakati huo, tulikuwa na miaka kuanzia 5 hadi 14. Wakati huo alitusaidia sisi; sasa tunamsaidia.” Kwa wazi, si rahisi kuandaa msaada huo, na watoto hao huvunjika moyo nyakati nyingine. “Lakini tunatambua kwamba hali ya baba yetu ni tatizo la muda tu,” asema Ellis. “Tunatazamia wakati baba yetu anaporudishwa kwenye afya njema na tunapoweza kuungana tena na mama yetu.” (Isaya 33:24; Yohana 5:28, 29) Kwa hakika, ni lazima iwe utunzaji huo wa kujitoa kwa mzazi huchangamsha moyo wa Yule ambaye huwaamuru watoto kuwaheshimu wazazi wao!c—Waefeso 6:1, 2.
Ujitoaji Kimungu na Huduma
16. Ni nini inayopaswa kuwa sababu kuu ya yale tunayofanya katika huduma?
16 Tunapokubali mwaliko wa Yesu wa ‘kumfuata daima,’ tunapata utume wa kimungu wa kuhubiri habari njema za Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mathayo 16:24, NW; 24:14; 28:19, 20) Kwa wazi, kushiriki katika huduma ni wajibu wa Kikristo katika “siku [hizi] za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Hata hivyo, ni lazima kusudi letu la kuhubiri na kufundisha liwe zaidi ya kutimiza kazi fulani au wajibu tu. Lazima kumpenda Yehova kuwe sababu kuu ya yale tunayofanya na kadiri ya yale tunayofanya katika huduma. “Kinywa cha mtu huyanena yaujazayo moyo wake,” akasema Yesu. (Mathayo 12:34) Naam, mioyo yetu inapofurika kwa kumpenda Yehova, tunahisi kusukumwa kuwatolea wengine ushahidi juu yake. Kumpenda Mungu kunapokuwa kichocheo chetu, huduma yetu ni wonyesho wenye maana wa ujitoaji kimungu wetu.
17. Tunaweza kusitawishaje kichocheo kifaacho kwa ajili ya huduma?
17 Tunaweza kusitawishaje kichocheo kifaacho kwa ajili ya huduma? Fikiria kwa uthamini sababu tatu ambazo Yehova ametupa sisi za kumpenda. (1) Twampenda Yehova kwa sababu ya yale ambayo ametufanyia tayari. Asingaliweza kuonyesha upendo mwingi zaidi ya kuandaa fidia. (Mathayo 20:28; Yohana 15:13) (2) Twampenda Yehova kwa sababu ya yale anayotufanyia sasa. Tuna uhuru wa kusema pamoja na Yehova, anayejibu sala zetu. (Zaburi 65:2; Waebrania 4:14-16) Tunapotanguliza masilahi ya Ufalme, tunapata mahitaji ya uhai. (Mathayo 6:25-33) Tunapokea ugavi wa kawaida wa chakula cha kiroho ambao hutusaidia kukabiliana na matatizo tunayopata. (Mathayo 24:45) Na tuna baraka ya kuwa sehemu ya udugu wa Kikristo wa ulimwenguni pote ambao kwa kweli hututenga kando na ile sehemu nyingine yote ya ulimwengu. (1 Petro 2:17) (3) Pia sisi twampenda Yehova kwa sababu ya yale atakayotufanyia bado. Kwa sababu ya upendo wake, ‘tunashika imara uhai ulio kwelikweli’—uhai wa milele katika wakati ujao. (1 Timotheo 6:12, 19, NW) Tunapofikiria upendo wa Yehova kwa ajili yetu, kwa hakika mioyo yetu itatusukuma kushiriki kwa kujitoa katika kuwaambia wengine juu yake na makusudi yake yenye thamani kubwa! Wengine hawatalazimika kutuambia jambo la kufanya au kadiri ya kufanya katika huduma. Mioyo yetu itatusukuma kufanya yale tuwezavyo.
18, 19. Dada mmoja alishinda kizuizi kipi ili kushiriki katika huduma?
18 Hata tunapokabili hali ngumu, moyo uliochochewa na ujitoaji kimungu utasukumwa kusema. (Linganisha Yeremia 20:9.) Hilo laonyeshwa katika hali ya Stella, ambaye ni mwanamke Mkristo mwenye haya sana. Alipoanza kujifunza Biblia kwa mara ya kwanza, alifikiri, ‘Singeweza kamwe kwenda nyumba kwa nyumba!’ Yeye aeleza hivi: “Nilikuwa mnyamavu sana sikuzote. Sikuweza kamwe kuwakaribia wengine ili kuanza mazungumzo.” Alipoendelea kujifunza, kumpenda kwake Yehova kulikua, akasitawisha tamaa yenye bidii ya kusema na wengine juu yake. “Nakumbuka nikimwambia mwalimu wangu wa Biblia, ‘Nataka sana kuongea, lakini siwezi hata kidogo, na hilo hunisumbua kwelikweli.’ Sitasahau kamwe lile aliloniambia: ‘Stella, uwe na shukrani kwamba wataka kuongea.’”
19 Upesi, Stella alijipata akimtolea jirani yake ushahidi. Halafu akachukua hatua iliyokuwa kubwa sana kwake—alishiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba kwa mara ya kwanza. (Matendo 20:20, 21) Yeye akumbuka hivi: “Nilikuwa nimeandika utoaji wangu. Lakini niliogopa sana hivi kwamba ingawa ulikuwa mbele yangu, nilikuwa mwoga mno kutazama maandishi yangu!” Sasa, baada ya miaka 35 na zaidi, Stella angali mwenye haya sana kiasili. Lakini, aipenda huduma ya shambani na aendelea kuwa na ushiriki wenye maana katika huduma hiyo.
20. Ni kielelezo kipi kinachoonyesha kwamba wala mnyanyaso wala kufungwa gerezani hakuwezi kufunga vinywa vya Mashahidi wa Yehova wenye kujitoa?
20 Wala mnyanyaso wala kufungwa gerezani hakuwezi kufunga vinywa vya Mashahidi wa Yehova wenye kujitoa. Fikiria kielelezo cha Ernst na Hildegard Seliger wa Ujerumani. Kwa sababu ya imani yao, kati yao walitumia zaidi ya miaka 40 katika kambi za mateso za Nazi na magereza ya Kikomunisti. Hata wakiwa gerezani, waliendelea kutolea ushahidi wafungwa wengine. Hildegard alikumbuka hivi: “Maofisa wa gereza waliniona mimi kuwa hatari sana, kwa sababu, kama vile mlinzi mmoja mwanamke alivyosema, nilisema juu ya Biblia siku nzima. Kwa hiyo niliwekwa katika seli ya chini ya ardhi.” Baada ya wao kupewa uhuru wao hatimaye, Ndugu na Dada Seliger walitoa wakati wao wote kwenye huduma ya Kikristo. Wote wawili walitumikia kwa uaminifu hadi vifo vyao, Ndugu Seliger katika 1985 na mke wake katika 1992.
21. Ni lazima tufanye nini ili kutia ujitoaji kimungu katika uvumilivu wetu?
21 Kwa kujifunza Neno la Mungu kwa bidii-nyendelevu na kuchukua wakati wa kutafakari kwa uthamini juu ya yale tunayojifunza, tutakua katika ujuzi sahihi juu ya Yehova Mungu na Yesu Kristo. Kisha, hilo litatufanya tupate kiwango kikamilifu zaidi cha ile sifa yenye thamani kubwa—ujitoaji kimungu. Bila ujitoaji kimungu hakuna njia ya kuvumilia majaribu mbalimbali tunayopatwa nayo tukiwa Wakristo. Kwa hiyo acheni tufuate shauri la mtume Petro, tukiendelea ‘kutia katika imani yetu uvumilivu na katika uvumilivu wetu ujitoaji kimungu.’—2 Petro 1:5, 6, NW.
[Maelezo ya Chini]
a Kuhusu eu·seʹbei·a, William Barclay asema hivi: “Ni sehemu ya seb- [mzizi] ya neno ambalo humaanisha staha au ibada. Eu ni neno la Kigiriki kwa neno faa; kwa hiyo, eusebeia ni ibada, staha inayotolewa ifaavyo na kwa haki.”—New Testament Words.
b Ili kupata mazungumzo juu ya njia ya kujifunza ili kuongeza ujuzi wetu juu ya Neno la Mungu, ona Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 1993, kurasa 12-17.
c Ili kupata mazungumzo kamili juu ya njia ya kuzoea ujitoaji kimungu kuelekea wazazi wazee-wazee, ona Mnara wa Mlinzi la Juni 1, 1987, kurasa 13-18.
Jibu Lako Ni Nini?
◻ Ujitoaji kimungu ni nini?
◻ Kuna uhusiano gani kati ya uvumilivu na ujitoaji kimungu?
◻ Ni nini ufunguo wa kupata ujitoaji kimungu?
◻ Mkristo aweza kuzoeaje ujitoaji kimungu nyumbani?
◻ Sababu kuu yapaswa iwe nini kwa yale tunayofanya katika huduma?
[Picha katika ukurasa wa 18]
Uvumilivu na ujitoaji kimungu vilionyeshwa na Mashahidi wa Yehova waliotiwa gerezani katika kambi moja ya mateso ya Nazi huko Ravensbrück