Sura ya 22
Je! Unyofu Una Faida?
1-4. Umeona udanganylfu gani kati ya vijana? Sababu gani si jambo la ajabu sana kuona vijana wakifanya mambo hayo? (Isaya 9:16)
WATU wengi leo hawadhani kuna faida ya kusema kweli wakati wote. Umepata kuona hivyo ? Watu wengi wa biashara wanadai kwamba biashara yao haingesitawi bila kudanganya. Kila siku tunaona matangazo ya biashara yenye kutiwa chumvi au kupotoa kweli. Ijapokuwa viongozi wa siasa wanatakiwa kuangalia hali njema ya raia, watu wengi wanawaona kuwa wasioaminika.
2 Wakiona udanganyifu mwingi sana katika watu wazima, mara nyingi vijana wanafuata mwendo uo huo. Wengi wanadanganya wakati wa mitihani shuleni au kuruka masomo (madarasa) mengine kwa masingizio yasiyo ya kweli. Huenda wakajisifu wanaposema na rafiki zao, wakieleza namna walivyo au waliyofanya na hali ni uongo mtupu. Huenda wakawadanganya wazazi wao nyumbani —wakijibu maulizo ya mwenendo wao kwa kusema mambo ambayo si ya kweli kabisa, wakificha mambo yenyewe ya hakika kwa kutoa majibu ya ujanja tu ili wadanganye. Wazazi wao au watu wengine wakijaribu kuchunguza maoni yao juu ya ufisadi, dawa za kulevya au mambo kama hayo, labda hawatawaambia maoni yao waziwazi. Labda watamdanganya mzazi kwa maneno ya kujipendekeza ili wapate fedha au ruhusa ya kufanya jambo fulani.
3 Lakini hilo ni jambo geni kweli? Ukweli ni kwamba, vijana wengi wanaona wana haki ya kufanya hivyo. Kwa sababu gani? Basi, ni kweli kwamba labda wazazi wao wanawafundisha kwamba ni vibaya kusema uongo. Lakini huenda wakawaona wazazi wao wakidanganya ili wasipate taabu au waepuke malipo fulani, deni au kodi. Umepata kuona kwamba wazazi wengine hata wanatumia watoto wao ili wawatolee sababu zisizo za kweli?
4 Zikiwako hali kama hizo, kuna maneno gani ya kutia vijana au sisi moyo wa kujaribu sana kuwa wanyofu katika mambo yote? Kufuata kweli kwakufaa nini wewe katika ulimwengu wenye kujaa uongo, udanganyifu na wivi? Je! kweli kutakuletea faida kubwa kuliko kudanganya, na ikiwa hivyo, ni faida gani?
KUCHAGUA FAIDA ZA MUDA MFUPI AU FAIDA ZA MUDA MREFU
5-7. Sababu gani faida zo zote za udanganyifu ni za muda tu?
5 Jiulize mwenyewe: Mimi nataka nini—faida za haraka au faida zisizo na mwisho? Ukifikiri, je! si kweli kwamba faida zo zote zinazoonekana kutokana na kusema uongo na kudanganya ni za muda mfupi? Ndiyo, Neno la Mungu linasema kweli hivi: “Mdomo wa kweli utathibitishwa milele; bali ulimi wa uongo ni wa kitambo tu.”—Mithali 12:19.
6 Kwa mfano, mfikirie mfanya biashara anayetangaza kitu cha kuuza akisema ni kizuri kumbe sivyo. Labda akiuza, mwishowe anaweza kukosa mtu wa kununua kwake sikuzote, akijua kwamba alidanganywa. Au tuseme ikiwa ungetaka kudanganya shuleni wakati wa mtihani. Ikiwa hungekamatwa, labda ungepata hesabu za juu zaidi. Lakini ikiwa ungeacha shule ukiwa na maarifa kidogo sana, labda hata usiweze kusoma na kujumlisha hesabu vizuri, kungekuwa kwa faida gani kupita mtihani vizuri sana au kuandikiwa “A” penye karatasi yako?
7 Basi, mwishowe mtu anayedanganya anajidanganya zaidi ya wote. Ebu linganisha mtu mnyofu na yule anayedanganya. Yafikirie mambo ambayo mdanganyifu anakosa nawe utakubali bila shaka kwamba ye yote anayedhani kudanganya kunasaidia kufanya maisha yawe bora au yenye furaha zaidi, ni mpumbavu kweli kweli.
8-10. Unyofu una faida namna gani (a) katika kazi ya kimwili? (b) katika ushirika wa jamaa? (c) katika ushirika na rafiki?
8 Ikiwa unajulikana kuwa msema kweli na mnyofu katika matendo yako, wengine watakuheshimu na kukutumaini. Rafiki zako wataelekea sana kuwa rafiki za kweli kwa sababu wanakuona kuwa mtu wa kweli nao wanathamini hilo. Ijapokuwa mara nyingi watu wa biashara ni wadanganyifu, kwa kawaida matajiri wana akili sana za kuona wafanya kazi walio bora na wanyofu. Basi, sifa ya kuwa mnyofu yaweza kukupatia kazi inapokuwa vigumu sana kuona kazi, au inaweza kukusaidia uendelee na kazi uliyo nayo wakati wengine wanapopoteza kazi zao.
9 Nyumbani, unyofu unaleta hali ya kustarehe na yenye kupendeza, ukiondoa mashaka kati ya watu waliooana na kati ya wazazi na watoto. Watoto wanapotumainiwa sana na wazazi wao kwa unyofu wao, vilevile wazazi nao wana nia ya kuendelea kuwapa watoto wao uhuru zaidi. Kusema kweli juu ya kosa fulani au tendo baya kunaweza kuleta adhabu. Lakini adhabu hiyo yaweza kuwa nyepesi kwa sababu ulisema kweli. Kisha wakati ujao, utakapokataa kikweli kuwa hukufanya kosa, inaelekea maelezo yako yataaminiwa.
10 Tofautisha hayo na mtu anayedanganya ili asipate adhabu au ili apate faida fulani. Anaweza kupoteza faida zote hizo. Kwa sababu kushirikiana matendo na mdanganyifu ni kama kupanda motokaa yenye usukani mbaya—hujui hata kidogo analoweza kufanya. Basi fahamu kwamba unapomwambia mtu uongo au kumdanganya, yale mashaka aliyo nayo juu yako yatachukua miaka mingi kufutika. Ikiwa unadanganya wazazi au rafiki, litakuwa jambo litakalochukua muda mrefu kusahaulika. Ukizoea kudanganya, utakuja wakati utakapotaka sana wengine wakuamini na kukutumaini wasiweze. Je! yafaa upate hasara hiyo kwa kudanganya?
11-13. (a) Mazoea ya kusema uongo yanaanzaje mara nyingi? (b) Sababu gani kusema uongo ni woga, si uhodari?
11 Kwa kweli, kusema uongo ni kama kutembea katika mchanga unaotopeza. Mara nyingi uongo unataka uongo mwingine wa kuutegemeza, na mtu akimwambia mwenzake uongo naye anaambiwa uongo ule ule. Je! hatuwezi kuona hekima ya shauri hili nyofu la Biblia: “Msiambiane uongo”?—Wakolosai 3:9.
12 Mara nyingi wale wanaosema uongo wanasema mambo yanayoelekea kidogo kuwa ya kweli na ule unaoitwa “uongo mdogo,” halafu kidogo-kidogo wanaendelea kwenye uongo ulio mbaya zaidi. Kwa njia hiyo kusema uongo kunaanza kama vile kucheza kamari. Mtu anayecheza kamari anaanza kwa kutumia fedha kidogokidogo, lakini—kwa kawaida ili alipe hasara ambazo amepata—anavutwa kidogokidogo kutia fedha nyingi zaidi katika mchezo wa kamari.
13 Kwanza, kusema uongo bila haya kwaweza kuonwa kuwa uhodari. Labda hata unawajua watu wanaojizoeza kumkazia mwingine macho wakati wa kusema uongo. Je! huo si uhodari? Hapana, kusema uongo ni woga hakika, si uhodari. Kusema kweli ndiko kunakotaka uhodari na kupatwa na yo yote yanayotokana na kusema kweli. Pahali pa kuwa nguvu, uongo hauna nguvu, hauwezi kujitegemea wenyewe, unahitaji uongo mwingine wa kuutegemeza, hauna nia ya kukutana na kweli uso kwa uso. Basi, sababu gani uwe kama mtu ambaye maisha yake yote anadanganya, anajificha, hasemi kweli na anatoa visababu tu? Sababu gani uwe kama Yuda Iskariote, ambaye akawa mdanganyifu, na mwisho akashindwa na kujinyonga? Sababu gani usiwe mwanamume au mwanamke wa kuweza kuwa mnyofu? Hiyo ndiyo njia peke yake ya kuendelea kujiheshimu na kuwa na dhamiri njema.
KUTIMIZA AHADI ZAKO
14-16. Sababu gani ni jambo la maana kutimiza ahadi zako?
14 Vilevile kutimiza ahadi zako kunatiwa ndani ya jambo hili la unyofu. Labda ungeudhika sana ikiwa wazazi wako wangekuahidi kitu fulani kisha wasitimize ahadi yao. Lakini unaona vibaya sana vilevile juu ya kushindwa kutimizia wazazi wako ahadi zako? Uko namna gani katika jambo hilo? Ukimwambia mtu kwamba utamsaidia kufanya jambo fulani au utajitolea kusaidia kazi fulani, je! unajaribu sikuzote kutimiza ahadi zako? Ukipatana na mtu mkutane wakati fulani, je! unafika bila kuchelewa? Ahadi zako zinafaa kadiri gani?
15 Ujana ndio wakati unaofaa kuanza kusitawisha mazoea ya kuwa mtu anayetimiza ahadi zake. Kutimiza au kutokutimiza ahadi zako kunaonyesha namna ulivyo kwa ndani sasa; vilevile kunageuza akili na moyo wako. Unaongeza nia, maoni ya mambo yawezayo kufanyiza tabia za muda mrefu.
16 Ikiwa sasa wewe ni mtu anayetegemeka, labda utakuwa hivyo miaka itakayofuata. Vivyo hivyo ukiwa mtu asiyetegemeka sasa, miaka itakayofuata utakuwa hivyo. Kwa mfano, ikiwa hutimizi ahadi zako sasa, huenda miaka ijayo ukafanya mapatano imara ya kufanya kazi au mgawo fulani —kisha upesi utake kuyavunja. Watu wengi wanafanya hivyo, lakini hawaheshimiwi na wengine.
17-19. (a) Ni kwa sababu gani watu wanavunja ahadi zao? (b) Ni nini linaloweza kukusaidia uepuke hali ambazo katika hizo unaelekea kuvunja ahadi zako?
17 Ni kwa sababu gani watu wanavunja ahadi zao? Basi, kwanza kutimiza ahadi kunawekea mtu vizuizi na kumpa wajibu wa kuitimiza. Wakati wa kutimiza mapatano unapofika, huenda jambo jingine likaonekana kuwa lenye kuvutia zaidi. Halafu, tena, huenda mara nyingine mtu akaona kwamba kutimiza ahadi zake ni kazi ngumu kupita alivyodhani ingekuwa.
18 Ikitukia hivyo utafanya nini? Je! utatimiza ahadi yako ijapokuwa itakuwa vigumu au hasara kwako? Labda mtu atasema, “Lakini sikujua jambo nililokuwa nikiahidi kufanya!” Ulizo ni hili: Lilikuwa kosa la nani? Je! mtu yule mwingine ndiye aliyekudanganya? Ikiwa sivyo, ukivumilia taabu yo yote ya kutimiza ahadi zako, unajifunza jambo la maana sana. Yaani: Fikiri kabla ya kusema, kabla ya kutoa ahadi. Kisha, ukisema, timiza unayosema.
19 Kusema “Ndiyo” kwa sababu tu unadhani itamfurahisha mtu—lakini bila kufikiria kwanza yatakayotokea—kwaweza kukutia katika matata. Lakini, ikiwa wewe ni mwangalifu kabla ya kutoa ahadi, ikiwa unafikiria sana mambo na kuona yatakavyogeuza maisha yako ya wakati ujao, hapo itakuwa vyepesi zaidi kutimiza ahadi zako ukiisha kuahidi. Utakuwa umekwisha kuweka moyo na akili zako tayari utimize ahadi zako. “Maneno yenu yawe Ndiyo, ndiyo,” akasema Yesu.—Mathayo 5:37.
SABABU KUBWA INAYOONYESHA KWAMBA UNYOFU UNA FAIDA
20-22. (a) Ni sababu gani iliyo kubwa inayoonyesha kwamba ni jambo la maana kuwa mnyofu nyakati zote? (Zaburi 15:1-4) (b) Ni mfano gani bora ambao Mungu anaweka katika kutimiza ahadi zake? Ni nini linaloweza kutusaidia tufuate mfano wake?
20 Sababu kubwa inayoonyesha kwamba kuna faida ya kuwa mnyofu na msema kweli ni kwamba watu wa namna hiyo ndio peke yao ambao Yehova Mungu anahesabu kuwa rafiki zake. Kwa sababu gani? Kwa sababu yeye mwenyewe anatimiza ahadi zake nyakati zote. Ndiyo sababu Yoshua aliweza kuliambia taifa la Israeli hivi: “Mnajua mioyoni mwenu, na [nafsini] mwenu, ya kuwa halikuwapungukia ninyi hata neno moja katika mambo hayo mema yote aliyoyanena [Yehova], Mungu wenu, katika habari zenu; yote yametimia kwenu, hapana neno lo lote mlilopungukiwa.” (Yoshua 23:14) Maandishi mengi ya Biblia ni ahadi ambazo Yehova ametimiza. Uaminifu wake ambao ameonyesha zamani unatupa uhakika huo wa kwamba atatimiza ahadi zake juu ya baraka za wakati ujao.
21 Je! wataka kibali ya Mungu? Basi kumbuka kwamba anawapa wale tu wanaomwabudu “katika roho na kweli.” (Yohana 4:23) Kumbuka kwamba yeye anachukia sana uongo wa namna zote—kudanganya, kujisifu, kuchongea—kwa sababu unatokana na choyo, pupa na kutofikiria watu wengine. Yeye anajua kwamba taabu zote na mateso ya wanadamu yalitokana kwanza na uongo uliosemwa na “baba wa huo,” Shetani, adui mkuu wa Mungu.—Yohana 8:44.
22 Je! kweli wewe wataka kufuata sana mwendo wa unyofu? Basi imekupasa ufahamu kwamba kumpenda Muumba wako na jirani yako kweli kweli ndiko kunakoweza peke yake kukuongoza ufanye hivyo. Ni lazima uipende kweli kwa moyo wote kwa sababu ya faida zake, vilevile kuuchukia sana uongo kwa sababu ya hasara zake. Inakupasa utafute kibali ya Mungu kuliko faida yo yote kutoka kwa mtu mwingine. Kumbuka, tunaweza kuwa na tumaini imara la wakati ujao, linalotegemea ahadi zake zisizoshindwa na kutegemeka kwa Neno lake, kwa sababu yeye mwenyewe anaipenda kweli na kuuchukia uongo. Basi jaribu sana kuwa kama yeye. Kumbuka kwamba “mdomo wa kweli utathibitishwa milele; bali ulimi wa uongo ni wa kitambo tu.”—Mithali 12:19.
[Picha katika ukurasa wa 174]
Je! kweli unapata faida ukiiba?