Kwa Sababu Gani Uwe Mwaminifu?
Mambo ya hakika ambayo vijana wanataka kujua
“KATIKA ulimwengu huu, mmoja kati ya watu elfu kumi ndiye mwaminifu.” Ndivyo alivyoandika William Shakespeare zaidi ya miaka 300 iliyopita. Tangu wakati huo watu hawaoni maana ya kuwa waaminifu. Kama ujuavyo, ndivyo ilivyo na kati ya vijana. Kwa sababu gani uaminifu unadharauliwa?
Watu walio wengi leo hawadhani kuna maana ya kusema kweli wakati wote. Wafanya biashara wengi wanadai hawawezi kufanikiwa bila ya kudanganya kidogo. Kila siku, twaona matangazo yanayotia chumvi au kusingizia. Ijapokuwa viongozi wa kisiasa wana daraka kubwa la kuangalia hali njema ya watu, watu wengi wanaziona ahadi zao kama zisizotumainika mara nyingi.
Wakiona udanganyifu mwingi sana kati ya watu wazima, mara nyingi vijana wanafuata mwendo ule ule. Shuleni, wengi wanapunja katika mitihani au kukosa kuhudhuria masomo fulani kwa kusingizia. Wakiwa pamoja na rafiki, huenda wakajivuna, kujigamba na kujionyesha kwa uongo namna walivyo au ambavyo wamefanya. Wakiwa nyumbani, huenda hata wakawadanganya wazazi wao—wakijibu maulizo juu ya mwenendo wao kwa kuchanganya-changanya ukweli na uongo, wakificha mambo ya hakika kwa kutoa jibu lenye maana iliyo tofauti sana na jibu la kweli. Wazazi wao, au watu wengine wakihangaikia hali yao kwa kufaa, wakijaribu kujua maoni yao juu ya ufisadi au dawa za kulevya au mambo kama hayo, huenda wakawapumbaza, wakisema vile wao wanavyodhani wenye kuwahoji wanataka kusikia, si maoni yao yalivyo hasa. Ili kupata pesa au ruhusa kufanya jambo fulani, huenda wakarairai wazazi wakisema wanawapenda.—Linganisha Zaburi 55:21.
Ni ajabu sana kwamba vijana wengi leo wanasisitiza kwamba wanataka watu wawaambie mambo yalivyo hasa, hali wao wenyewe wanatumia wakati mwingi sana wakisema uongo. Na hali wengi wanaona wana haki ya kufanya hivi. Kwa sababu gani? Ni kweli kwamba huenda wazazi wao wakawafundisha kwamba ni vibaya kusema uongo. Lakini huenda wakawaona wazazi wao wenyewe wakisema uongo wapate kuepuka hali fulani isiyofaa au kuepuka kulipa deni au kodi. Wazazi wengine hata wanatumia watoto wao kudanganya kwa kutoa udhuru.
Hali za namna hii zikiwapo, vijana wanatiwaje moyo—au ye yote kati yetu—ajitahidi kuwa mwaminifu katika mambo yote? Katika ulimwengu ambamo kusema uongo na kupunja kunaonekana sana, inafaa nini na kuna faida gani kwako kushikamana na yaliyo kweli? Je! kutakuletea faida kuu zaidi kuliko ambavyo udanganyifu ungeweza kukuletea, na, ikiwa ndivyo, ni faida ya namna gani?
FAIDA ZA KITAMBO NA FAIDA ZA DAIMA
Jiulize mwenyewe: Mimi nataka nini—faida ya kitambo kidogo tu, inayoelekea kuwa faida, au faida zinazodumu? Zo zote zinazoelekea kuwa faida kutokana na kusema uongo na kupunja ni za kitambo tu. Kwa mfano, chukua mfanya biashara anayetoa kifaa fulani kisichofaa. Ni kweli, huenda akakiuza lakini baadaye huenda akampoteza mnunuzi mtu huyo akigundua alipunjwa. Au, tuseme unapunja shuleni. Usipokamatwa, huenda ukapata viwango bora. Lakini kupita mitihani na “A zinazofuatana” kungekuwa na faida gani ukimaliza masomo ukiwa na maarifa haba? Sababu gani upoteze bure miaka hiyo shuleni hali ungeweza kuitumia kujifunza mambo yanayoweza kuwa ya manufaa katika maisha ya baadaye?
Kwa hiyo, mwishowe mtu anayepunja kwa kweli anajipunja mwenyewe zaidi kuliko wote. (Linganisha Mithali 20:17.) Yaangalie mambo fulani anayoelekea kuyapoteza mtu mdanganyifu nawe utaona sababu kwa nini ye yote anayedhani udanganyifu unasaidia kuleta maisha bora au yenye furaha zaidi ni mpumbavu hasa.
Ikiwa unajulikana kama mtu mnyofu na mwaminifu katika matendo, unaheshimiwa na kutumainiwa na watu. Rafiki utakaokuwa nao wataelekea kuwa wa kweli kwa sababu wanakuona wewe kuwa wa kweli na wanalithamini hili. Ijapokuwa ni kweli kwamba ulimwengu wa kisasa wa biashara ni mdanganyifu kwa kawaida, ni kweli pia kwamba matajiri kwa ujumla wana akili ya kutosha kuwathamini wafanya kazi walio waaminifu. Wana nia zaidi kuwakabidhi madaraka makubwa zaidi. Kwa hiyo, sifa njema ya uaminifu yaweza kukuletea kazi ambapo kazi ni haba au yaweza kukusaidia kudumisha kazi hali wengine wakipoteza zao. Nyumbani, uaminifu unasaidia kuleta hali ya starehe na ya furaha, ukiondoa mashaka au shuku kati ya wenzi wa ndoa na kati ya wazazi na watoto. (Zab. 34:13, 14) Wakati watoto wanapoweza kutumainiwa na wazazi wao kabisa kwa sababu ya uaminifu huu, kwa kawaida wazazi ni wenye nia kuwapa uhuru fulani wakiuongeza kidogo kidogo. Ni kweli, kusema kweli juu ya kosa fulani kwaweza kuleta adhabu. Lakini adhabu hiyo huenda ikawa nyepesi kwa sababu ulikuwa mwaminifu. Na ikiwa, wakati ujao, unakana kwa kweli hukufanya kosa, maelezo yako yataelekea sana kuaminiwa.
Tofautisha hili na mtu anayedanganya asije akaadhibiwa. Anaelekea kupoteza faida zote hizi. Kwa kuwa kushughulika na mtu mdanganyifu ni kama kuendesha gari lenye kasoro ya usukani—huna hakika linaweza kufanya nini. Kwa hiyo ujue kwamba unapomwambia mtu fulani uongo au kumpunja, kutokuaminiwa unakotokeza kwaweza kuchukua miaka mingi kabla hakujaondolewa. Ikiwa mzazi au rafiki anahusika, jeraha lililotiwa laweza kuponywa lakini huenda likaacha kumbukumbu baya lililo kama kovu la daima. Ukizoea kudanganya, huenda wakati ukafika unapotaka hasa wengine wakuamini na kukutumaini lakini wao watajisikia hawawezi. (Linganisha Mithali 10:9; 17:20.) Je! faida yo yote ya kitambo inayoletwa na udanganyifu inastahili kukuweka katika hali hiyo?
NI NINI KINACHOLETA UHURU MWINGI NA FURAHA ZAIDI?
Je! udanganyifu unaleta uhuru mwingi zaidi? Wengine wanadhani hivyo kwa sababu wanaiona kama njia nyepesi ya kuepukia hali au vizuizi visivyofaa. Lakini, kwa kweli, kusema uongo ni kama kutopea-topea mchangani. Kila uongo unahitaji mwingine wauunge mkono, na karibuni mtu anajikuta akisema-sema uongo kila mara. (Mit. 12:13) Kusema uongo mara nyingi kunaanza kama vile kucheza kamari. Mcheza kamari anatumia senti chache kwanza, lakini—kwa kawaida ili arudishe kiasi alichohasirika—anavutwa kidogo kidogo kutumia senti nyingi zaidi na zaidi. Wasema uongo mara nyingi wanaanza kwa kuchanganya-changanya ukweli na “uongo mdogo mdogo,” halafu polepole wanaendelea na mbaya hata zaidi.
Ukiwaambia wengine uongo, kwa kawaida unakuja kujiambia mwenyewe uongo. Huenda ukaanza kujidhania kwamba uko hivi na vile na kwamba maisha yako ni bora zaidi na yenye furaha zaidi kumbe sivyo ilivyo. Huenda ukajidhania u mjanja na mwenye hekima nyingi, hali u mpumbavu. Kuwaza kubaya kunakutetea ukimlaghai mtu kwa kudhani kwamba, ingawaje, unapata yaliyo haki yako. Walakini, baadaye mtu anayefanya hivi anakutana na hali zinazomlazimisha ayaone mambo kama yalivyo. Ndipo anapoweza kushtuka akijiona mwenyewe kama alivyo hasa, akigundua namna ambavyo maisha yake yamekuwa yasiyofaa kitu—kama vile jengo lenye msingi wa mchanga unaotelezesha.—Linganisha Mathayo 7:26, 27; Zaburi 36:2.
Kusema uongo kwa kujikaza huenda kukaonekana kuwa ujasiri, uhodari, na wengine wanajizoeza kumtazama mtu machoni hali wakisema uongo. Lakini kwa kweli kusema uongo ni woga wala si ushujaa. Ushujaa ni kusema kweli na kupambana na matokeo yake. Badala ya kuonyesha nguvu, uongo ni kama kiwete kisichojiweza, kisichoweza kujisimamisha, kikihitaji uongo mwingine ukitegemeze, kisitake kamwe kuuona ukweli kama ulivyo. Kwa hiyo, sababu gani uwe kama mtu anayetumia maisha yake akijisingizia, akijificha, akikwepa-kwepa na kutoa udhuru? Sababu gani uwe kama Yuda Iskariote, aliyekuwa mdanganyifu, akajaribu kuishi maisha ya uongo na kushindwa kufanikiwa akajiua? (Yohana 12:4-6; Mt. 27:3-5) Sababu gani usiwe mwanamume shujaa au mwanamke shujaa kutosha kuweza kuwa mwaminifu? Ndiyo njia ya pekee kuendelea kujiheshimu na kudumisha dhamiri njema.
Hii yaonyesha jambo la maana kuliko yote: nia njema ya Mungu na kibali. Yehova Mungu anawakubali wale tu wanaomwabudu yeye “katika roho na kweli,” naye Mwanawe alisema kwamba uhuru wa kweli unafuatana na kweli tu. (Yohana 4:23, 24; 8:31, 32) Yehova anachukia namna zote za uongo—udanganyifu, majivuno, uchongezi, kupunja—kwa maana zinatokana na choyo, pupa na kutopendezwa na faida za wengine. (Mit. 6:16, 17; 11:1; Zab. 5:5, 6; 15:1-3) Anajua kwamba taabu zote za wanadamu asili yake ni kusema uongo—kwa upande wa ‘baba wa uongo,’ Shetani, adui mkuu wa Mungu. (Mwa. 3:1-5; Yohana 8:44) Kwa haki Neno la Mungu linashirikisha uongo na wizi, uzinzi na makosa mengine mazito—ama kwa njia ya wazi au kwa njia isiyo wazi—karibu kila namna ya kosa inaanzia na namna fulani ya udanganyifu. Hos. 4:1, 2; Rum. 1:24-32; Ufu. 21:8.
Je! unataka kufuata mwendo wa uaminifu? Basi ujue kwamba huwezi kupinga vishawishi vya kudanganya kwa kuukubali uaminifu akilini tu kama “shauri bora.” Mengi zaidi yahitajiwa. Ni upendo wa kweli tu kwa Muumba wako na kwa jirani yako uwezao kukupa kichocheo unachokihitaji. Lazima uwepo upendo wa moyoni wa kweli kwa sababu ya faida zake na kuchukia uongo sana kwa sababu ya madhara yake. (Mit. 4:23, 24) Kibali ya Mungu, pia, lazima ithaminiwe zaidi kuliko ile ya mtu mwingine ye yote. Kumbuka, ni kwa sababu tu Yeye mwenyewe anaipenda kweli na kuchukia uongo sisi twaweza kuwa na tumaini thabiti la wakati ujao, lenye msingi wa ahadi Zake zisizoshindwa na kutegemeka kwa Neno Lake.—Linganisha Yoshua 23:14; Waebrania 6:18, 19.
Hakikisha, pia, kwamba rafiki zako ni wapenda kweli. “Rafiki” wanaosema uongo na kudanganya wengine wanaweza kukufanyia wewe vivyo hivyo wakiona inafaa. Uyasome maneno ya Mfalme Daudi kama yalivyoandikwa katika Zaburi 101:5-7 na kuzifuata kanuni zake za urafiki. Ndiyo, kumbuka kwamba “mdomo wa kweli utathibitishwa milele; bali ulimi wa uongo ni wa kitambo tu.”—Mit. 12:19.