Sura ya 2
Kuwekea Nyumba Yako Msingi Mzuri
1-3. KuIingana na Mathayo 7:24-27, fanikio la kweli katika maisha linategemea nini?
NYUMBA, maisha au ndoa inakuwa nzuri ikiwa msingi wake ni mzuri tu. Katika mmojawapo wa mifano yake, Yesu alisema habari ya watu wawili —mtu mwenye akili aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba mgumu, na mtu mpumbavu aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga. Upepo mkubwa ulipotokea, mafuriko (maji) na pepo zikapiga nyumba hizo mbili. Ile iliyojengwa juu ya mwamba mgumu ilibaki ikisimama, lakini ile iliyojengwa juu ya mchanga ilianguka kwa anguko kubwa.
2 Yesu hakuwa akifundisha watu namna ya kujenga nyumba. Alikuwa akikazia uhitaji (lazima) wa kuweka maisha juu ya msingi mzuri. Akiwa mjumbe wa Mungu, alisema hivi: “Kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya,” anafanana na mtu anayejenga juu ya mwamba. Lakini “kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye,” anafanana na yule anayejenga juu ya mchanga.—Mathayo 7:24-27.
3 Fahamu kwamba katika, mifano yote hiyo miwili Yesu anaonyesha kwamba si kusikia tu shauri la hekima na kujua tu jambo la kufanya. Kinachotofautisha kufanikiwa na kushindwa ni kufanya shauri la hekima linavyosema. “Mkiyajua hayo, [wenye furaha ni] ninyi mkiyatenda.”—Yohana 13:17.
4. Ni mambo gani tunayoweza kujifunza kutokana na ndoa ya watu wawili wa kwanza? (Mwanzo 2:22-3:19)
4 Hivyo ndivyo ndoa ilivyo. Tukiweka, ndoa yetu juu ya msingi ulio kama mwamba, itashinda mikazo ya maisha. Lakini msingi huo ulio mzuri unatoka wapi? Kwa Muumba wa ndoa, Yehova Mungu. Yeye alianza ndoa, alipounganisha watu wawili wa kwanza wawe mune na mke. Kisha akawapa maagizo ya hekima ili wapate faida. Jambo ambalo lingeamua kama wangeishi milele ama sivyo, lingetegemea kufuata maagizo hayo. Wote wawili waliyajua maagizo ya Mungu, lakini jambo la kusikitisha ni kwamba waliruhusu choyo kiwazuie wasitii maongozi hayo. Walichagua kutokufuata shauri hilo na, kwa sababu hiyo, ndoa na maisha yao yaliharibika kama nyumba iliyojengwa juu ya mchanga.
5, 6. Mungu anawapa msaada gani watu waliooana na wale wanaofikiria kuoana?
5 Yehova Mungu aliunganisha watu wawili wa kwanza katika ndoa, lakini yeye mwenyewe hawafanyii watu waliooana mipango ya ndoa leo. Walakini, shauri lake juu ya ndoa lingali linapatikana. Ni juu ya kila mtu leo anayefikiria kuoa au kuolewa aamue kama atafuata shauri hilo au hatalifuata. Vilevile Neno la Mungu linaonyesha kwamba tunaweza kumwomba atusaidie tuamue kwa hekima juu ya mtu tunayetazamia kuoana naye.—Yakobo 1:5, 6.
6 Walakini, hali zinatofautiana sana katika sehemu mbalimbali za dunia. Leo katika sehemu nyingi za dunia, wanaume na wanawake wanajichagulia wenyewe mtu wa kuoana naye. Lakini katika sehemu kubwa ya watu wanaoishi duniani, wazazi ndio wanaofanya mipango ya ndoa, mara nyingi kupitia kwa mjumbe anayefanyia wengine mipango ya ndoa. Katika sehemu nyingine za dunia mwanamume anapata mke akiisha kuwalipa wazazi wa msichana “mahari,” na huenda kiasi ambacho mwanamume anaombwa kulipa kama mahari (mali ya ndoa) kikawa kikubwa hata akashindwa kuoa. Lakini, hata hali ziwe namna gani, Biblia inatoa shauri linaloweza kusaidia ndoa ifanikiwe kwa muda mrefu.
UJIJUE MWENYEWE KWANZA
7-10. (a) Yampasa mtu ajue nini juu yake mwenyewe anapofikiria ndoa? Anawezaje kujua? (b) Biblia inasema, nini juu ya sababu za maana za kutaka kuoa au kuolewa?
7 Wataka nini katika ndoa? Mambo ya kimwili, ya moyoni na ya kiroho unayotaka ni nini? Ni mambo gani unayoona kuwa ya maana sana? Una miradi na njia gani za kuyatimizia? Ili ujibu maulizo hayo inakupasa ujijue mwenyewe. Jambo hilo si jepesi kama mtu anavyoweza kudhani. Linataka maoni yaliyokomaa ili tujichunguze, na hata hivyo haiwezekani kujijua wenyewe kabisa katika kila jambo. Paulo mtume Mkristo alionyesha jambo hilo alipoandika maneno haya katika 1 Wakorintho 4:4: “Maana sijui sababu ya kujishitaki nafsi yangu, lakini sihesabiwi haki kwa akili hiyo; ila anihukumuye mimi ni [Yehova].”
8 Wakati fulani Muumba alitaka mwanadamu Ayubu ajue mambo fulani aliyokuvva akikosa kuyafahamu, naye Mungu akamwambia hivi: “Nitakuuliza neno, nawe niambie.” (Ayubu 38:3) Maulizo yanaweza kutusaidia tujijue wenyewe na kupata kujua habari ya makusudi yetu. Basi jiulize mwenyewe upate kujua namna unavyopendezwa na ndoa.
9 Je! wataka kuoa an kuolewa ili utimize mambo ya kimwili yanayotakiwa—chakula, mavazi, nyumba? Hayo ni mambo ya kwanza kwetu sote, kama Biblia inavyosema: “Tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo.” Na uhitaji (lazima) wa ngono? Vilevile hilo ni jambo la kawaida linalotakiwa. “Ni afadhali kuoa kuliko kuwaka tamaa.” (1 Timotheo 6:8;1 Wakorintho 7:9) Je! kusudi la ndoa ni kuwa na mwenzi? Hiyo ilikuwa sababu kubwa iliyomfanya Mungu aanzishe mpango wa ndoa. Sababu nyingine ilikuwa ya kwamba watu wawili washirikiane wafanye kazi pamoja. (Mwanzo 2:18; 1:26-28) Kutimiza kazi njema kunafurahisha na kunapaswa kuwe na thawabu yake: “Imempasa kila mtu ale na kunywa, aone mema kwa kazi yake yote ngumu. Hiyo ni zawadi kutoka kwa Mungu.”—Mhubiri 3:13, NW.
10 Watu wanaopendana wameuona moyo kwa muda mrefu kuwa mfano wa maoni yao. Lakini, Biblia inauliza ulizo lenye kusumbua juu ya moyo: “Nani awezaye kuujua?” (Yeremia 17:9) Je! unajua yaliyo katika moyo wako hakika?
11. Ni mambo gani ya kwanza ya moyoni yanayotakiwa, ambayo yamepaswa kutimizwa atika ndoa?
11 Mara nyingi, uzuri wa nje unatuzuia tusijue mambo mengine ya moyoni tunayotaka. Unapotafuta mtu wa kuoana naye, je! unataka sana kufahamika, kuonyeshwa fadhili na kuhurumiwa? Mambo ya kwanza ambayo sote tunataka ni haya: mtu wa kuwa karibu nasi, wa kutumainia, wa kufunulia mambo yetu pasipo kuogopa kwamba atakasirika, mtu ambaye ‘hatatuzuilia huruma zake.’ (1 Yohana 3:17) Je! unaweza kumpa mwenzi wako yote hayo, je! naye atakurudishia yayo hayo?
12. Sababu gani kutimizwa kwa mahitaji ya kimwili na ya moyoni hakutoshi kuifanya ndoa iwe yenye furaha?
12 Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaoona uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3, NW) Uhitaji wako wa kiroho ni nini? Je! unahusiana (unakamatana) na kutafuta kazi ya maisha? Utajiri? Mali za kimwili? Basi, je! mambo hayo yanaleta amani na furaha ya moyoni? Kwa kawaida hayaleti. Kwa hiyo inatupasa tufahamu ya kwamba kunabaki njaa ya roho ndani ya watu wote, hata yakiisha kutimizwa mahitaji yote ya kimwili. Roho yetu yatamani sana kujua sisi ni nani, tuko namna gani, sababu ya kuwapo hapa, na tunakoelekea. Je! wewe unaona uhitaji (lazima) wa mambo hayo ya kiroho, na namna ya kuyatimiza?
KUFAANA
13. Ili ndoa iwe yenye furaha, inakupasa ufahamu nini zaidi ya mambo unayotaka mwenyewe?
13 Ukifahamu mambo yote hayo yanayotakiwa na mwili, akili na roho, je! unajua kama mtu unayetazamia kuoana naye anayafahamu vilevile? Haikupasi ujue tu mambo ambayo wewe peke yako unataka ili uwe na furaha katika ndoa, bali yakupasa vilevile ufahamu na yale ya mwenzako. Bila shaka wataka mwenzako awe na furaha vilevile. Huzuni ya mmoja itakuwa huzuni ya nyote wawili.
14. Sababu gani waume na wake katika ndoa nyingi wanaona kwamba hawafaani?
14 Ndoa nyingi zinakuwa na mwisho wenye huzuni au talaka kwa sababu za kukosa kufaana (kutopatana). Kutofaana ni neno kubwa, lakini linakuwa kubwa hata zaidi katika ndoa. Ikiwa watu wawili hawafaani kukaa pamoja, maisha yanaweza kuwa yenye matata. Hali hiyo inakumbusha mpango wa sheria ya Musa ambayo kwa sababu ya rehema ilikataza kufunga pamoja wanyama wawili wenye mwili nguvu tofauti katika nira moja, kwa sababu kufanya hivyo kungefanyiza matata. (Kumbukumbu la Torati 22:10) Ndivyo walivyo mwanamume na mwanamke wasiofaana lakini wanaofungwa katika ndoa. Ikiwa waume na wake wanakuwa na mapendezi tofauti, rafiki tofauti na tafrija tofauti, na kushiriki pamoja mambo machache, vifungo vya ndoa vinapata matata makubwa.
15, 16. Ni mambo gani machache yanayopaswa kuzungumzwa pamoja na yule unayetazarnia kuoana naye, na kwa namna gani?
15 “Pasipo mazungunazo ya siri, mipango inavunjika,” ndivyo Biblia inavyotuambia. (Mithali15:22,NW) Je! mambo yanayofaa yamezungumzwa wakati wa kufikiria ndoa? Kazi ya mwanamume itapatanaje na ndoa? Itaamua mahali mtakakoishi na kiasi cha fedha zitakazokuwa zikipatikana ili mtimize mambo yanayofaa mnayotaka. Ni nani atakayekuwa akifanya mipango ya matumizi ya fedha? Je! kuna lazima ya mke kufanya kazi, na je! inafaa? Uhusiano (hali) pamoja na wakwe utakuwaje, sana sana wazazi wa mume na wale wa mke? Kila mmoja anaonaje ngono, watoto na kulea watoto? Je! mmoja anataka kumtawala mwenzake, au huruma ndiyo itakayoongoza uhusiano huo?
16 Je! maulizo hayo yote na mengine vilevile, yaweza kuzungumzwa kwa utuliva na kwa busara, na kumalizwa kwa njia ambayo nyote wawili mwaweza kuishi kwa raha? Je! mwaweza kupata magumu na kuyamaliza pamoja, na kuendelea kupashana habari sikuzote? Hiyo ndiyo njia ya maisha ya ndoa inayofanikiwa.
17-19. Sababu gani hali za ukoo (zinahusu) zinapasa kufaana katika ndoa?
17 Kwa kawaida kufaana zaidi kunakuwako kati ya watu wawili wanaopatana hali za maisha. Kitabu Aid to Bible Understanding, ukurasa 1114, kinaeleza hivi juu ya ndoa katika nyakati za Biblia: “Inaonekana kwamba desturi ya watu wote ilikuwa ile ya mwanamume kuoa katika watu wa ukoo au katika kabila lake mwenyewe. Kanuni hiyo inaonyeshwa na maneno ya Labani aliyomwambia Yakobo: ‘Afadhali nikupe wewe [binti yangu] kuliko kumpa mtu mwingine.’ (Mwa. 29:19) Sana sana desturi hiyo ilifuatwa na waabudu wa Yehova, kama Ibrahimu alivyoonyesha. Alipeleka mjumbe aende kwa watu wa ukoo wake katika nchi yake mwenyewe akamtafutie Isaka mwanawe mke badala ya kuchukua mmojawapo wa binti za Wakanaani ambao alikuwa akikaa kati yao. (Mwa. 24:3, 4)”
18 Lakini, hiyo haina maana ya kwamba yamfaa mtu leo aoe an aolewe na mtu wa ukoo wake wa karibu sana, kwa maana hiyo ingeweza kuleta magumu na kufanya watoto wazaliwe wakiwa na kasoro fulani. Lakini hali za jamaa moja zinahusu (zinapasa) sana kanuni za watu. Wakati wa utoto na ujana, mwenendo wa mtu na maoni yake yanaongozwa na hali ya jamaa. Watu wawili wanapokuwa wa hali moja ya maisha, wanaona kuwa vyepesi zaidi kupatana. Lakini, watu wasio wa hali moja za maisha na ukoo mmoja wanaweza vilevile kufanya mageuzo mema katika ndoa, sana sana wote wawili wakiwa wamekomaa moyoni.
19 Kwa wazi, inafaa sana ikiwa unaweza kujua habari za jamaa ya mtu unayetazamia kuoana naye. Chunguza vilevile ujue uhusiano wake na jamaa hiyo —na wazazi na ndugu na dada zake. Anatendeaje wazee, au anapatanaje na watoto wadogo?
20, 21. Ni maoni gani yanayokufaa uwe nayo juu ya makosa ya mtu mmoja mmoja katika kuchagua mwenzi wa kuoana naye?
20 Ijapokuwa unakuwa mwangalifu katika mambo yote, yakupasa bado ukumbuke hili: Watu wawili hawawezi kufaana kabisa kabisa hata. Wote wawili watakuwa na makosa fulani. Labda wanaweza kujua machache kabla ya kuoana; na mengine watayajua baadaye. Halafu?
21 Si makosa yenyewe yanayofanya ndoa zisifanikiwe, bali ni namna hao wawili wanavyoyaona. Unaweza kuona kwamba mema yanashinda mabaya, au unakaza fikira juu ya mabaya na kuyarudia-rudia? Je! uko tayari kukubali na kukumbuka kwamba mwenzako anaweza kufanya makosa, kama vile wewe unavyotaka utendewe? Mtume Petro alisema, “Upendo unafunika wingi wa dhambi.” (1 Petro 4:8, NW) Je! unampenda namna hiyo mtu yule unayefikiria kuoana naye? Ikiwa sivyo, afadhali usioane na mtu huyo?
‘NAWEZA KUMGEUZA’
22-24. Sababu gani si hekima kuoana na mtu kwa vile ameahidi kugeuza njia yake au kwa kutaka kujaribu kumgeuza mtu huyo?
22 Je! unasema, ‘Naweza kumgeuza,’ hata iwe hivyo? Lakini unampenda nani? Unampenda mtu huyo kama alivyo sasa, au kama atakavyokuwa ukiisha kujitahidi kumgeuza? Ikiwa ni vigumu kwetu kujigeuza wenyewe, ni vigumu zaidi kugeuza wengine. Lakini, kweli zenye nguvu kutoka Neno la Mungu zaweza kumfanya mtu ajigeuze mwenyewe. Mtu anaweza ‘kuvua utu wa zamani,’ afanywe mpya katika nguvu inayotendesha akili. (Waefeso 4:22, 23) Lakini usiamini ikiwa mtu unayetazamia kuoana naye anakuahidi kwamba atageuka mara hiyo kwa sababu yako! Ijapokuwa tabia mbaya zaweza kuondolewa au kugeuzwa, hiyo inaweza kuchukua muda mrefu, hata miaka. Wala hatuwezi kuachilia mbali uhakika wa kwamba tabia tulizorithi na hali za makao yetu, zimetupa mwenendo fulani, na kutufanya tutende katika njia fulani na kuwa watu mmoja mmoja walio tofauti. Upendo wa kweli unaweza kutuongoza tusaidiane tuweze kufanya maendeleo na kushinda makosa, lakini hautatuongoza tujaribu kumlazimisha mwenzi wetu wa ndoa afuate mfano mpya ambao hakuzaliwa nao na unaopingana na utu wake.
23 Watu wengine wanawazia mtu fulani ambaye ni bora sana, nao wanajaribu kufanya kila wazo la upumbavu na la muda lipatane na mtu huyo. Bila shaka, hakuna anayeweza kupatana na mtu huyo asiyeweza kupatikana, lakini mwenye kupumbazika hivyo anafuata sana wazo hilo na kujaribu kulazimisha mwingine awe kama huyo ambaye anawazia. Isipokuwa hivyo, anakata tamaa kisha anaanza kutafuta mwingine aliye bora wa kuwazia tu. Lakini watu kama hao hawamwoni mtu aliye bora hata kidogo. Wanatafuta mtu wa kuwazia tu ambaye hawawezi kuona. Watu wanaofikiri hivyo hawafai ndoa.
24 Labda umepata kuwa na mawazo kama hayo. Nyakati fulani maishani mwetu, wengi wetu tumewaza hivyo; vijana wengi wanawaza hivyo. Lakini tunapozidi kuwa na maoni yaliyokomaa, tunafahamu kwamba mawazo hayo yanapaswa yaachwe kwa vile yasivyowezekana. Jambo la manna katika ndoa ni lile la kweli, si lile la kuwazia tu.
25. Ni tofauti gani kati ya upendo wa kweli na upendo wa kupumbaza tu akili?
25 Upendo wa kweli si wa upumbavu kama wengi wanavyodhani. Unafunika makosa mengi, lakini upendo wa kweli hauyasahau. Upendo wa kijinga, usioona magumu yanayotangulia kuonwa na wengine ndio upendo wa kupumbazika akili. Upendo wa kweli hauko hivyo. Upendo wa kijinga hata unaficha mashaka yake wenyewe yenye kusumbua; lakini uwe na hakika kwamba baadaye yatafunuka. Ukifumba (ukifunga) macho usione mambo yasiyofaa wakati wa uchumba, utayaona bila shaka baada ya arusi. Maelekeo yetu ya asili ni kujaribu kujifanya kuwa mtu bora kwa yule tunayetazamia kupendeza au kuvuta, lakini wakati ujao tutajulikana kabisa namna tulivyo. Jiruhusu wakati mwingi upate kujua sana namna mwenzako alivyo, nawe ujionyeshe bila kuficha namna ulivyo. Maneno yenye kutia moyo ya mtume katika 1 Wakorintho 14:20 yanaweza kupasa vilevile kutafuta mtu wa kuoana naye: “Msiwe watoto . . . katika akili zenu mkawe watu wazima.”
WAJIBU UNAOPASWA KUTIMIZWA KATIKA NDOA
26. Kulingana na Maandiko, kifungo cha ndoa ni cha muda gani? (Warumi 7:2, 3)
26 Imempasa mtu afikirie kwa makini wajibu unaopaswa kutimizwa katika ndoa. Ikiwa mmoja kati ya hao wawili hatimizi wajibu wake, ndoa itakuwa juu ya msingi wenye kutikisika. Katika sehemu nyingi za ulimwengu leo, ndoa zinafungwa kisha zinavunjika upesi. Inakuwa hivyo mara nyingi kwa sababu watu wanaooana hawakuuona wajibu wao kuwa wa lazima sana, badala yake, walikuwa na maoni ya kwamba ‘ikiwa haifanikiwi, nitaivunja.’ Maoni hayo yakiwapo, karibu ndoa inakuwa imevunjika tangu mwanzo, nayo inaleta huzuni badala ya kuleta furaha. Tofauti na hayo, Biblia inaonyesha kwamba ndoa imepaswa iwe uhusiano wa maisha. Kwa habari ya watu wawili wa kwanza, Mungu alisema kwamba hao wawili “watakuwa mwili mmoja.” (Mwanzo 2:18, 23, 24) Mwanamume kuwangekuwa na mwanamke mwingine, naye mwanamke hangekuwa na mwanamume mwingine. Mwana wa Mungu alihakikisha jambo hilo, akisema: “Hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe.” Uasherati peke yake ndio ungekuwa msingi wa kuvunja kifungo cha ndoa.—Mathayo 19:3-9.
27-29. (a) Inamfaa mwanamke atafute kuona nini katika Yule ambaye anatazamia kuwa mwenzi wake wa ndoa? (b) Mwanamume anaweza kutafuta kwa hekima kuona nini katika yule ambaye anatazamia kuwa mwenzi wake wa ndoa?
27 Kwa sababu ndoa ni jambo zito, mwanamke anayetaka afanikiwe itamfaa aolewe na mwanamume ambaye anaweza kuheshimu tu—mwanamume aliye imara na mwenye kusawazika, mwenye kuamua kwa busara, anayeweza kutimiza daraka na amekomaa vya kutosha kukubali lawama la kumpa msaada. Jiulize hivi: Je! atakuwa mtoaji mwema wa riziki, baba mwema wa watoto wo wote wanaoweza kuwa baraka ya ndoa? Je! ana mwenendo bora hivi kwamba nyote wawawili mwaweza kukaza nia mkifanye kitanda cha ndoa kiheshimike na kuwa bila kuchafuliwa? Je! anaonyesha unyenyekevu na kiasi au ni mwenye kiburi na kichwa kikubwa, anayetaka kujionyesha ukichwa wake, ambaye nyakati zote anadhani hakosi na hataki kufikiria mambo? Mambo hayo yaweza kujulikana kwa kushirikiana na mwanamume huyo kwa muda wa kutosha kabla ya kuoana, sana sana kanuni za Biblia zikitumiwa kuwa kanuni za uamuzi.
28 Vilevile, mwanamume anayetaka sana ndoa yake ifanikiwe, atatafuta mke ambaye anaweza kupenda kama mwili wake mwenyewe. Mke huyo amepaswa awe kikamilisho chake, akiwa mwenzi katika kuanzisha nyumba. (Mwanzo 2:18) Kusimamia nyumba vizuri ni kazi ngumu yenye madaraka mbalimbali. Inataka kuonyesha uwezo wa kuwa mpishi, mpambaji wa nyumba, anayejua sana kutumia vizuri fedha za jamaa, mama watoto, mwalimu, na mengine zaidi ya hayo. Daraka lake laweza kuwa lenye kutaka uwezo wa kubuni vitu tena laweza kuwa gumu, likimpa nafasi nyingi za ukuzi wake na kutimiza mambo. Mke mwema ni mfanya kazi kama mume anayefaa: “Huangalia sana njia za watu wa nyumbani mwake; wala hali chakula cha uvivu.”—Mithali 31:27.
29 Ndiyo, inawafaa wote wawili wafikirie mambo ambayo wanaona—ushuhuda unaoonyesha kama mtu anajitunza kuwa safi na kuwa mtaratibu ama hakuna; ushuhuda unaoonyesha kuwa ana bidii au, badala yake, unaoonyesha uvivu; kiasi na huruma ambayo ni tofauti ya kuwa mwenye kichwa kikubwa na kujipenda; ushuhuda unaoonyesha uangalifu wa kutumia vizuri fedha na mali nyingine au unaoonyesha hali ya kutumia vibaya fedha na mali nyingine; unaoonyesha uwezo wa kufikiri unaofanya mazungumzo yapendeze na kuongeza hali kubwa ya kiroho tofauti na uvivu wa akili unaofanya maisha kuwa kawaida ile ile tu ya kutimiza mahitaji ya kimwili ya kila siku na mengine machache.
30, 31. Sababu gani uasherati unaofariywa wakati wa uchumba unaweza kumzuia mtu asifurahie ndoa nzuri?
30 Kuheshimiana kwa moyo mnyofu ni sehemu ya maana ya kufanikisha ndoa. Jambo hilo linahusu vile-vile maonyesho ya mapenzi wakati wa uchumba. Kuzoeana kusikofaa au nyege zisizozuilika zaweza kuufanya uhusiano ukose maana kabla ya kuanza ndoa. Uasherati si msingi mzuri wa kuanza kuweka ndoa juu yake. Unaonyesha kutokufikiria furaha ya mwenzako ya wakati ujao. Ule mwasho mkubwa wa nyege ambao kwa muda unaelekea kufanyiza kifungo kisichovunjika waweza kupoa mara na, huenda kwa muda wa juma chache au hata siku chache, ndoa ikavunjika. —Linganisha habari inayoonyesha namna Amnoni alivyowashwa na nyege juu ya Tamari kama inavyosimuliwa katika 2 Samweli 13: 1-19.
31 Kuonyesha nyege wakati wa uchumba kunaweza kutia mashaka moyoni, yanayoweza kutokeza baadaye hali ya kutokuwa na hakika kama ndoa ina kusudi la kweli. Je! kusudi lake lilikuwa kutuliza tu nyege, au lilikuwa kuishi pamoja na mtu anayethaminiwa na kupendwa kweli kweli? Mara nyingi kukosa kujiweza kabla ya ndoa kunaonyesha kutokujiweza hata baadaye, kukitokeza ukosefu wa uaminifu na furaha. (Wagalatia 5:22, 23) Kukumbuka mabaya yaliyoachwa na uasherati uliofanywa kabla ya kufunga ndoa kunaweza kuzuia usiwe na maoni mazuri juu ya ndoa tokea mwanzo wake.
32. Uasherati unaofanywa wakati wa uchumba tunawezaje kuharibu uhusiano wa mtu na Mungu?
32 Jambo ambalo ni zito hata zaidi ni kwamba uasherati huo unamharibia mtu uhusiano (ukamatano) wake na Muumba wetu, ambaye tunahitaji sana msaada wake. “Maana haya ndiyo mapenzi ya Mungu, kutakaswa kwenu, mwepukane na uasherati; . . mtu asimpunje ndugu {au, dada} yake wala kumkosa katika jambo hili . . . Basi yeye anayekataa, hakatai mwanadamu bali Mungu, anayewapa ninyi [roho yake takatifu].”—1 Wathesalonike 4: 3-8.
MSINGI ULIO KAMA MWAMBA
33, 34. Wakati wa kuchagua mwenzi wa ndoa, ni sifa gani ambazo Maandiko yanaonyesha kuwa za maana sana sana kufikiriwa kuliko sura ya nje?
33 Je! nyumba yako, jamaa yako, itakuwa juu ya msingi ulio kama mwamba au kama mchanga? Inategemea kadiri ya hekima inayotumiwa wakati wa kuchagua mwenzi wa ndoa. Uzuri na ngono hautoshi. Mambo hayo hayaondoi tofauti za akili na za kiroho. Shauri lililo katika Neno la Mungu ndilo linalotoa msingi ulio imara katika ndoa.
34 Biblia inaonyesha kwamba mtu wa ndani ni bora kuliko sura ya nje. “Upendeleo hudanganya, na uzuri ni ubatili,” yasema mithali iliyoongozwa na Mungu, “bali mwanamke amchaye [Yehova] , ndiye atakayesifiwa.” (Mithali 31: 30) Mtume Petro, mwanamume aliyeoa, anasema habari ya “mutu wa moyo, asiyeonekana” na “roho ya upole na utulivu” kuwa “ya damani [thamani] kubwa mbele ya Mungu.” (1 Petro 3:4, ZSB) Mungu ‘haitazami sura ya nje ya mwanadamu,’ nasi twaweza kupata faida kutokana na mfano wake kwa kuangalia tusije tukavutwa bure na sura ya nje tu ya mtu tunayemtazamia kuwa mwenzi wa ndoa. —1 Samweli 16:7.
35, 36. (a) Sababu gani ni jambo la maana kuoana na mtu anayemwamini Mungu na kuliamini Neno lake? (b) Ungetazamia yule atakayekuwa mwenzi wako wa ndoa aonyeshe imani hiyo kwa kadiri gani?
35 Mfalme Sulemani mwenye hekima aliyafikiria maisha, akaamua hivi: ‘Ogopa Mungu, na shika amri zake; maana maneno haya ni yote inayofaa mutu kufanya.” (Muhubiri 12:13, ZSB) Waisraeli waliokuwa katika agano la kutii sheria ya Mungu, waliamriwa waziwazi wasifunge ndoa pamoja na watu ambao hawakushiriki ibada yao, wasije wakavutwa mbali na Mungu wa kweli. “Usioane nao; binti yako usimpe mwanawe mume, wala usimtwalie mwanao mume binti yake. Kwa kuwa atamkengeusha mwanao mume asinifuate, ili wapate kuabudu miungu mingine.”—Kumbukumbu la Toarti 7:2-4.
36 Wale walio katika “agano jipya,” katika kundi la Kikristo, walishauriwa kwa upole kwa sababu kama hizo waoe an waolewe “katika Bwana tu.” (Yeremia 31:31-33; 1 Wakorintho 7:39) Badala ya kushikilia sana mambo bila akili, hilo linaongozwa na hekima na upendo. Hakuna linaloweza kuvitia nguvu nyingi vifungo vya ndoa kuliko kushiriki pamoja kumwabudu Muumba. Ukioana na mtu anayemwamini Mungu na kuliamini Neno lake, na anayelifahamu kama unavyolifahamu, hapo nyote wawili mtakuwa na mamlaka moja ya kupewa shauri. Labda utaona hilo kuwa lisilo na maana, lakini “msipotezwe. Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.” (1 Wakorintho 15:33, NW) Lakini, hata katika kundi la Kikristo yamfaa mtu ahakikishe kwamba yule ambaye anatazamia awe mwenzi wake wa ndoa ni mtumishi wa Mungu aliye na bidii kweli kweli, si mtu anayejaribu tu kuwa Mkristo na huku akitegemea sana maoni na mazoea ya ulimwengu. Huwezi kutembea na Mungu na wakati uo huo ushirikiane na ulimwengu.—Yakobo 4:4.
37, 38. (a) Sababu gani imempasa intu aepuke kufanya ama uchumba ama kufunga ndoa haraka haraka? (b) Inawafaa wale wanaorikiria kuoana wasikihze shauri la nani?
37 “Ni nani katika ninyi, kama akitaka kujenga gharama mnara,” akauliza Yesu, “asiyeketi kwanza na kuhesabu kwamba anavyo vya kuumalizia? Asije akashindwa kuumaliza baada ya kuupiga msingi.” (Luka 14:28, 29) Kanuni iyo hiyo inapasa ndoa. Kwa kuwa Mungu anaiona ndoa kuwa kifungo cha maisha, usichague mwenzi wa ndoa haraka haraka. Tena uhakikishe kwamba wewe mwenyewe uko tayari kumaliza ulichokwisha anza kufanya. Hata uchumba si jambo la kuchukuliwa kwa mchezo. Kufanya mapenzi na mwenzako bila kuwa na kusudi la kuoana naye ni mchezo mbaya wa kutaka kumtesa, na matokeo yake yenye kuudhi na kusikitisha yanaweza kuendelea muda mrefu.—Mithali 10:23; 13:12.
38 Itawafaa vijana walio na akili, wanaofikiria kufunga ndoa wasikilize shauri la wazee (watu wazima), sana sana wale ambao wameonyesha kwamba wanapendezwa sana na faida zako. Andiko la Ayubu 12:12 linatukumbusha ubora wa kufanya hivyo kwa kusema: “Wazee ndio walio na hekima, na katika kuishi siku nyingi iko fahamu.” Zisikilize sauti hizo zenye ujuzi. Zaidi ya yote, “mtumaini [Yehova] kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.”—Mithali 3:5, 6.
39. Biblia inawezaje kuwa msaada kwa watu waliokwisha kuoana?
39 Labda wengi mnaosoma maneno haya tayari mmekwisha funga ndoa. Ijapokuwa msingi wenu umekwisha wekwa kwa kadiri fulani, Biblia yaweza kuwasaidieni mfanye mageuzo fulani yanayotakiwa, mpate matokeo yenye faida. Hata ikiwa ndoa yenu iko katika hali gani, inaweza kuongezewa ubora kwa kufikiria zaidi shauri la Muumba juu ya furaha ya jamaa.
[Picha katika ukurasa wa 12]
Je, ndoa yako yaweza kuvumilia nyakati za taabu?