SURA YA PILI
Kutayarisha Kwa Ajili Ya Ndoa Yenye Mafanikio
1, 2. (a) Yesu alikaziaje umaana wa kupanga? (b) Kupanga ni muhimu katika sehemu gani hasa?
KUJENGA nyumba kwataka utayarishaji wenye uangalifu. Kabla ya msingi kuwekwa, ni lazima uwanja upatikane na ramani zichorwe. Hata hivyo, jambo jingine ni muhimu. Yesu alisema hivi: “Ni nani kati yenu atakaye kujenga mnara asiyeketi kwanza na kupiga hesabu ya gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha?”—Luka 14:28.
2 Kama ilivyo kwa habari ya kujenga nyumba ndivyo ilivyo pia kwa habari ya kujenga ndoa yenye mafanikio. Wengi husema: “Ninataka kufunga ndoa.” Lakini ni wangapi hutua ili wahesabu gharama? Ingawa Biblia husema mema juu ya ndoa, pia huvuta uangalifu kwenye magumu ambayo ndoa hutokeza. (Mithali 18:22; 1 Wakorintho 7:28) Kwa hiyo, wale wanaofikiria ndoa wanahitaji kuwa na maoni halisi juu ya baraka na pia gharama za kuwa watu ambao wamefunga ndoa.
3. Kwa nini Biblia ni msaada wenye thamani kwa wale wanaopanga kwa ajili ya ndoa, na ni maswali gani matatu ambayo itatusaidia kujibu?
3 Biblia yaweza kusaidia. Shauri layo limepuliziwa na Mwanzilishi wa ndoa, Yehova Mungu. (Waefeso 3:14, 15; 2 Timotheo 3:16) Kwa kutumia kanuni zinazopatikana katika kitabu hiki chenye mwongozo kilicho cha kale na bado chenye kufaa hali ya kisasa, acheni tuone (1) Mtu anaweza kujuaje kama yeye yu tayari kwa ajili ya ndoa? (2) Ni nini kitafutwe katika mwenzi? na (3) Utafutaji wa uchumba waweza kudumishwaje ukiwa wenye kuheshimika?
JE, UKO TAYARI KWA AJILI YA NDOA?
4. Ni jambo gani lililo muhimu katika kudumisha ndoa yenye mafanikio, na kwa nini?
4 Huenda kujenga nyumba kukagharimu pesa nyingi, lakini kuidumisha kwa muda mrefu kunagharimu pesa nyingi pia. Ndivyo ilivyo na ndoa. Kufunga ndoa huonekana kuwa jambo gumu vya kutosha; hata hivyo, kudumisha uhusiano wa kindoa mwaka baada ya mwaka lazima kufikiriwe pia. Kudumisha uhusiano wa jinsi hiyo huhusisha nini? Jambo muhimu ni uwajibikaji wa moyo wote. Hivi ndivyo Biblia hufafanua uhusiano wa ndoa: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Yesu Kristo alitoa msingi pekee wa Kimaandiko wa kutaliki kukiwa na uwezekano wa kufunga ndoa tena—“uasherati,” yaani, kufanya ngono haramu nje ya ndoa. (Mathayo 19:9) Ikiwa unafikiria ndoa, kumbuka viwango hivi vya Kimaandiko. Ikiwa wewe si tayari kwa uwajibikaji huu mzito, basi wewe si tayari kwa ajili ya ndoa.—Kumbukumbu la Torati 23:21; Mhubiri 5:4, 5.
5. Ingawa uwajibikaji mzito wa ndoa huogopesha watu fulani, kwa nini badala ya hivyo, wapaswa kuthaminiwa sana na wale wanaokusudia kufunga ndoa?
5 Wazo la uwajibikaji mzito huogopesha wengi. “Kujua kwamba sisi wawili tulikuwa tumeshikamanishwa pamoja kwa muda wote wa maisha kulinifanya nihisi nimezuiliwa, nimefungiwa, nimewekewa mipaka kabisa,” akaungama mwanamume mmoja kijana. Lakini ikiwa kwa kweli unampenda yule mtu unayekusudia kufunga ndoa naye, uwajibikaji hautaonekana kuwa mzigo wenye kulemea. Badala ya hivyo, utaonwa kuwa chanzo cha usalama. Hisia ya uwajibikaji inayohusika katika ndoa itafanya mume na mke watake kukaa pamoja kupitia nyakati nzuri na mbaya na kutegemezana hata iwe ni nini kinachotendeka. Mtume Mkristo Paulo aliandika kwamba upendo wa kweli “huhimili mambo yote” na “huvumilia mambo yote.” (1 Wakorintho 13:4, 7) “Uwajibikaji wa ndoa hunifanya nihisi nikiwa salama zaidi,” asema mwanamke mmoja. “Napenda ile hali ya faraja ya kuwa tumekiri kwetu wenyewe na kwa ulimwengu kwamba twakusudia kushikamana pamoja.”—Mhubiri 4:9-12.
6. Kwa nini ni jambo bora zaidi kutofanya haraka kufunga ndoa ukiwa na umri mchanga?
6 Kuishi kulingana na uwajibikaji wa jinsi hiyo kwataka ukomavu. Hivyo, Paulo ashauri kwamba Wakristo hufanya vema zaidi kutofunga ndoa mpaka wawe wamepita “mchanuko wa ujana,” kipindi ambacho hisia za kingono ni zenye nguvu na zaweza kupotosha uamuzi wa mtu. (1 Wakorintho 7:36) Vijana hubadilika upesi sana wanapokua kimwili. Wengi wanaofunga ndoa wakiwa wachanga sana hupata kwamba baada ya miaka michache tu mahitaji na tamaa zao, na pia zile za mwenzi wao, zimebadilika. Takwimu huonyesha kwamba matineja wanaofunga ndoa huelekea zaidi kukosa furaha na kutafuta talaka kuliko wale wanaongoja muda mrefu zaidi. Hivyo usifanye haraka kufunga ndoa. Kutumia miaka kadhaa ukiwa mtu mzima kijana, aliye mseja, kwaweza kukupa uzoefu wenye thamani sana utakaokufanya uwe mkomavu zaidi na mwenye kustahili zaidi kuwa mwenzi afaaye. Kuahirisha ndoa kwaweza pia kukusaidia ujielewe mwenyewe vizuri zaidi—jambo ambalo ni la lazima ikiwa utasitawisha uhusiano wenye mafanikio katika ndoa yako.
JIJUE MWENYEWE KWANZA
7. Kwa nini wale wanaopanga kufunga ndoa wajichunguze wenyewe kwanza?
7 Je, wewe huliona kuwa jambo rahisi kuorodhesha sifa unazotaka katika mwenzi? Walio wengi huona hivyo. Hata hivyo, namna gani sifa zako mwenyewe? Una vitabia gani vitakavyokusaidia uchangie ndoa yenye mafanikio? Utakuwa mume au mke wa aina gani? Kwa kielelezo, je, wewe hukiri makosa yako kwa hiari na kukubali shauri, au sikuzote unajitetea unaposahihishwa? Je, wewe ni mchangamfu na mwenye kutazamia mazuri kwa kawaida, au unaelekea kuwa mwenye huzuni, ukilalamika mara nyingi? (Mithali 8:33; 15:15) Kumbuka, ndoa haitabadili utu wako. Ikiwa wewe ukiwa mseja ni mwenye kiburi, mwenye kugusika hisia kupita kiasi, au mwenye kutazamia mabaya kupita kiasi, utakuwa vivyo hivyo unapofunga ndoa. Kwa kuwa ni vigumu kujiona wenyewe jinsi wengine hutuona, kwa nini usimuulize mzazi au rafiki anayetumainiwa akueleze mambo waziwazi na akupe madokezo? Ukipata kuyajua mabadiliko ambayo yanaweza kufanywa, yatengeneze hayo kabla ya kuchukua hatua za kufunga ndoa.
Unapokuwa ungali mseja, kuza sifa, tabia, na uwezo mbalimbali utakaokutumikia vizuri katika ndoa
8-10. Biblia hutoa shauri gani ambalo litamsaidia mtu atayarishe kwa ajili ya ndoa?
8 Biblia hututia moyo turuhusu roho takatifu ya Mungu ifanye kazi ndani yetu, ikitokeza sifa kama vile “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti.” Hiyo hutuambia pia ‘tufanywe upya katika kani inayotendesha akili zetu’ na ‘tuvae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.’ (Wagalatia 5:22, 23; Waefeso 4:23, 24) Kutumia shauri hili ukiwa ungali mseja kutakuwa kama vile kuweka fedha katika benki—jambo ambalo litathibitika kuwa lenye thamani sana wakati ujao, unapofunga ndoa.
9 Kwa kielelezo, ikiwa wewe ni mwanamke, jifunze kuelekeza uangalifu zaidi kwenye “mtu wa siri wa moyo” kuliko kwenye sura yako ya kimwili. (1 Petro 3:3, 4) Kiasi na utimamu wa akili utakusaidia uwe na hekima, ‘taji ya uzuri’ ya kweli. (Mithali 4:9; 31:10, 30; 1 Timotheo 2:9, 10) Ikiwa wewe ni mwanamume, jifunze kutendea wanawake kwa njia ya fadhili na yenye staha. (1 Timotheo 5:1, 2) Huku ukijifunza kufanya maamuzi na kuchukua madaraka, jifunze pia kuwa mwenye kiasi na mnyenyekevu. Mtazamo wa kutawala utaongoza kwenye matata katika ndoa.—Mithali 29:23; Mika 6:8; Waefeso 5:28, 29.
10 Ingawa kufanya upya akili katika mambo haya si jambo rahisi, ni jambo ambalo Wakristo wote wapaswa watengeneze. Na litakusaidia uwe mwenzi wa ndoa aliye bora.
MAMBO YA KUTAFUTA KATIKA MWENZI
11, 12. Watu wawili waweza kujuaje kama wao wanafaana au la?
11 Je, ni desturi mahali unapoishi mtu kujichagulia mwenzi wake mwenyewe wa ndoa? Ikiwa ndivyo, basi, uchukue hatua gani ikiwa wampata mtu fulani wa jinsia tofauti kuwa mwenye kuvutia? Kwanza, jiulize mwenyewe, ‘Je, kweli kusudi langu ni kufunga ndoa?’ Ni jambo la kikatili kuchezea hisiamoyo za mtu mwingine kwa kutokeza matazamio yasiyo ya kweli. (Mithali 13:12) Kisha, jiulize, ‘Je, niko tayari kufunga ndoa?’ Ikiwa jibu kwa maswali hayo mawili ni ndiyo, hatua zifuatazo utakazochukua zitakuwa tofauti kwa kutegemea desturi za kwenu. Katika nchi fulani, baada ya kumchunguza mtu huyo kwa muda fulani, waweza kumwendea na kueleza kutaka kwako kufahamiana naye vizuri zaidi. Ikiwa jibu ni la, usisisitize kufikia hatua ya kuwa mwenye kuchukiza. Kumbuka, yule mtu mwingine ana haki pia ya kufanya uamuzi katika jambo hili. Hata hivyo, ikiwa jibu ni ndiyo, huenda mkapanga kutumia wakati pamoja katika utendaji ufaao. Hilo litakupa fursa ya kuona kama kufunga ndoa na mtu huyu kungekuwa jambo lenye hekima.a Wapaswa kutafuta nini kwenye hatua hii?
12 Ili kujibu swali hilo, wazia ala mbili za muziki, labda marimba (piano) na gambusi (gita). Zikirekebishwa sauti kwa usahihi, yoyote moja kati yazo yaweza kutokeza muziki mtamu ikiwa moja tu. Hata hivyo, inakuwaje ikiwa ala hizi zinapigwa pamoja? Sasa ni lazima sauti zao zipatanishwe. Ndivyo ilivyo na wewe na yule atazamiwaye kuwa mwenzi. Huenda kila mmoja wenu akawa amejitahidi ‘kurekebisha’ vitabia vya utu wake akiwa mtu binafsi. Lakini sasa swali ni: Je, nyinyi mwapatana? Yaani, je, mwafaana?
13. Kwa nini ni jambo linalokosa hekima sana kutafuta uchumba na mtu ambaye hashiriki imani yako?
13 Ni jambo la maana kwamba nyote wawili mwe na itikadi na kanuni zilezile. Mtume Paulo aliandika hivi: “Msiwe wenye kufungwa nira isiyosawazika pamoja na wasio waamini.” (2 Wakorintho 6:14; 1 Wakorintho 7:39) Ndoa pamoja na mtu ambaye hashiriki imani yako katika Mungu hufanya iwe yamkini zaidi kwamba kutakuwa na hali mbaya ya kutopatana. Kwa upande ule mwingine, ujitoaji wa wote wawili kwa Yehova Mungu ndio msingi ulio imara zaidi sana wa kuwa na muungano. Yehova akutaka uwe na furaha na ufurahie kifungo cha karibu zaidi iwezekanavyo pamoja na mtu ambaye unafunga ndoa naye. Yeye ataka mfunganishwe kwake Yeye na kwa nyinyi kwa nyinyi kwa kifungo cha upendo chenye nyuzi tatu.—Mhubiri 4:12.
14, 15. Je, kuwa na imani ileile ndiyo sehemu pekee ya muungano katika ndoa? Eleza.
14 Ingawa kumwabudu Mungu pamoja ndiyo sehemu ya maana zaidi ya zote ya muungano, mengi zaidi yahusika. Ili kupatana, wewe na yule atazamiwaye kuwa mwenzi wako mwapaswa mwe na miradi ileile. Miradi yenu ni nini? Kwa kielelezo, nyote wawili mwahisije juu ya kuwa na watoto? Ni mambo gani hutangulizwa maishani mwenu?b (Mathayo 6:33) Katika ndoa yenye mafanikio kwelikweli, mume na mke ni marafiki wema nao hufurahia ushirika wa mmoja na mwenzake. (Mithali 17:17) Ili kuwa na hali hiyo, ni lazima wapendezwe na mambo yaleyale. Isipokuwa hivyo, ni vigumu kudumisha urafiki wa karibu—na ni vigumu hata zaidi kudumisha ndoa. Bado, ikiwa yule atazamiwaye kuwa mwenzi wako hufurahia utendaji fulani, kama vile kutalii nchi kwa miguu, nawe hupendi, je, hilo lamaanisha kwamba nyinyi wawili hampaswi kufunga ndoa? Sivyo hasa. Labda mnashiriki mambo mengine yenye kupendeza, yaliyo ya maana zaidi. Zaidi ya hayo, huenda ukamfurahisha yule atazamiwaye kuwa mwenzi wako kwa kushiriki utendaji mbalimbali ufaao kwa sababu yule mtu mwingine huufurahia.—Matendo 20:35.
15 Kwa kweli, kwa kadiri kubwa, kufaana kunaamuliwa na jinsi nyinyi wawili mlivyo wenye kubadilikana na hali badala ya jinsi mnavyoshabihiana. Badala ya kuuliza, “Je, sisi hukubaliana juu ya kila jambo?” baadhi ya maswali yaliyo bora huenda yakawa: “Inakuwaje wakati hatukubaliani? Je, tunaweza kuzungumza juu ya mambo kwa utulivu, tukionyeshana staha na adhama? Au mazungumzo mara nyingi huzorota yakawa majibizano makali?” (Waefeso 4:29, 31) Ikiwa unataka kufunga ndoa, uwe mwangalifu juu ya mtu yeyote aliye mwenye kiburi na ashikaye maoni yake sana, asiye tayari kamwe kuridhiana, au ambaye sikuzote hudai na kutunga hila ili njia yake mwenyewe ifuatwe.
PATA KUJUA KIMBELE
16, 17. Huenda mwanamume au mwanamke akatafuta nini anapofikiria yule atazamiwaye kuwa mwenzi wa ndoa?
16 Katika kutaniko la Kikristo, wale wanaokabidhiwa madaraka wanapaswa “wajaribiwe juu ya kufaa kwanza.” (1 Timotheo 3:10) Wewe pia waweza kutumia kanuni hii. Kwa kielelezo, mwanamke huenda akauliza, “Mwanamume huyu ana sifa ya aina gani? Marafiki wake ni nani? Je, yeye huonyesha sifa ya kujidhibiti? Yeye huwatendeaje watu wazee-wazee? Yeye atoka katika familia ya aina gani? Yeye hupatanaje nayo? Mtazamo wake ni nini kuelekea fedha? Je, yeye hutumia vibaya vinywaji vya alkoholi? Je, yeye ni mwepesi wa kukasirika, hata ni mjeuri? Yeye ana madaraka gani ya kutaniko, naye huyashughulikiaje? Je, ningeweza kumstahi kwa kina kirefu?”—Mambo ya Walawi 19:32; Mithali 22:29; 31:23; Waefeso 5:3-5, 33; 1 Timotheo 5:8; 6:10; Tito 2:6, 7.
17 Mwanamume mseja huenda akauliza, “Je, mwanamke huyu huonyesha upendo na staha kumwelekea Mungu? Je, anaweza kutunza nyumba? Familia yake itatazamia nini kwetu? Je, yeye ni mwenye hekima, mwenye bidii ya kazi, mwenye kiasi katika kutumia fedha? Yeye huongea juu ya mambo gani? Je, yeye hufikiria kwa kweli hali njema ya wengine, au ni mwenye kufikiria mambo yake mwenyewe, mjishughulishaji katika mambo ya watu wengine? Je, ni mwenye kustahili kuaminiwa? Je, yuko tayari kujinyenyekeza chini ya ukichwa, au ni mshupavu, hata labda ni mwasi?”—Mithali 31:10-31; Luka 6:45; Waefeso 5:22, 23; 1 Timotheo 5:13; 1 Petro 4:15.
18. Ikiwa udhaifu mbalimbali mdogo unatambuliwa wakati wa utafutaji wa uchumba, ni nini kipaswacho kufikiriwa?
18 Usisahau kwamba unashughulika na mzao wa Adamu asiyekamilika, si na shujaa mkamilifu kutoka katika riwaya ya kimahaba. Kila mtu ana makosa, na baadhi yayo yatapaswa kupuuzwa—yako na yale ya yule atazamiwaye kuwa mwenzi wako. (Waroma 3:23; Yakobo 3:2) Zaidi, udhaifu unaotambuliwa unaweza kutokeza fursa ya kukua. Kwa kielelezo, tuseme wakati wa utafutaji wenu wa uchumba mnagombana. Fikiria hili: Hata watu wanaopendana na kustahiana hukosa kukubaliana nyakati nyingine. (Linganisha Mwanzo 30:2; Matendo 15:39.) Je, ingeweza kuwa kwamba nyinyi wawili mwahitaji tu ‘kutawala roho zenu’ zaidi kidogo na kujifunza kusuluhisha mambo kwa amani zaidi? (Mithali 25:28) Je, yule atazamiwaye kuwa mwenzi wako huonyesha kwamba ataka kufanya maendeleo? Je, wewe wataka? Je, ungeweza kujifunza kutokuwa mwenye kugusika hisia upesi sana, mwenye kuathiriwa haraka sana? (Mhubiri 7:9) Kujifunza kusuluhisha matatizo kunaweza kuweka kiolezo cha uwasiliano wa haki ambao ni muhimu ikiwa nyinyi wawili mtafunga ndoa.—Wakolosai 3:13.
19. Mwendo wa kutenda wenye hekima ungekuwa upi ikiwa matatizo mazito yatokea wakati wa utafutaji wa uchumba?
19 Lakini, namna gani ikiwa unaona mambo yanayokusumbua sana? Shaka hizo zapaswa kufikiriwa kwa uangalifu. Hata iwe unahisi kimahaba jinsi gani au hata iwe una wasiwasi jinsi gani juu ya kufunga ndoa, usipuuze makosa mazito. (Mithali 22:3; Mhubiri 2:14) Ikiwa una uhusiano pamoja na mtu ambaye una shaka nzito juu yake, ni jambo la hekima kukatiza uhusiano huo na kuepuka uwajibikaji wenye kudumu pamoja na mtu huyo.
DUMISHA UTAFUTAJI WENU WA UCHUMBA UKIWA WENYE KUHESHIMIKA
20. Watu wawili wanaotafuta uchumba wanaweza kudumishaje mwenendo wao wa kiadili ukiwa bila suto?
20 Mnaweza kudumishaje utafutaji wenu wa uchumba ukiwa wenye kuheshimika? Kwanza, hakikisheni kwamba mwenendo wenu wa kiadili hauna suto lolote. Je, mahali mnapoishi, kushikana mikono, kubusu, au kukumbatiana huonwa kuwa mwenendo unaofaa kwa watu wawili wasiooana? Hata ikiwa maonyesho hayo ya shauku hayachukizi, yanapaswa kuruhusiwa tu wakati ambapo uhusiano umefikia hatua ambayo ndoa imepangwa kwa hakika. Iweni waangalifu kwamba maonyesho ya shauku hayazidi kufikia hatua ya kuwa mwenendo mchafu au hata uasherati. (Waefeso 4:18, 19; linganisha Wimbo Ulio Bora 1:2; 2:6; 8:5, 9, 10.) Kwa sababu moyo ni mdanganyifu, nyote wawili mngekuwa wenye hekima kuepuka kuwa peke yenu ndani ya nyumba, chumba, gari lililoegeshwa, au pengine popote ambapo pangetolea fursa mwenendo mbaya. (Yeremia 17:9) Kudumisha utafutaji wenu wa uchumba ukiwa safi kiadili hutoa uthibitisho wa wazi kwamba una sifa ya kujidhibiti na kwamba unatanguliza ufikirio usio na ubinafsi wa hali njema ya yule mtu mwingine mbele ya tamaa zako mwenyewe. La maana zaidi, utafutaji wa uchumba ulio safi utampendeza Yehova Mungu, anayewaamuru watumishi wake wajiepushe na ukosefu wa usafi na uasherati.—Wagalatia 5:19-21.
21. Ni uwasiliano gani wa wazi huenda ukahitajiwa ili kudumisha utafutaji wa uchumba ukiwa wenye kuheshimika?
21 Pili, utafutaji wa uchumba wenye kuheshimika hutia ndani pia uwasiliano wa haki. Utafutaji wenu wa uchumba uendeleapo kuelekea ndoa, mambo fulani yatahitaji kuzungumzwa waziwazi. Mtaishi wapi? Je, nyote wawili mtafanya kazi ya kimwili? Je, mwataka kuwa na watoto? Pia, ni jambo la haki tu kufunua mambo, labda yaliyotokea katika wakati uliopita wa mtu, ambayo yanaweza kuathiri ndoa. Huenda haya yatie ndani madeni au wajibu mbalimbali ulio mkubwa au mambo yanayohusu afya, kama vile ugonjwa au hali yoyote mbaya ambayo huenda ukawa nayo. Kwa kuwa watu wengi walioambukizwa HIV (virusi inayosababisha UKIMWI) hawaonyeshi dalili zozote mara moja, halingekuwa jambo baya kwa mtu au kwa wazazi wanaojali kuomba kwamba, mtu ambaye wakati uliopita ameshiriki katika ngono za ovyoovyo au alikuwa mwenye kutumia dawa za kulevya kupitia mishipani, achunguzwe damu kuona kama ina UKIMWI. Ikiwa uchunguzi huo waonyesha kuna ugonjwa, mtu mwenye ambukizo hapaswi kumsonga yule akusudiwaye kuwa mwenzi kuendelea na uhusiano huo ikiwa huyo ataka sasa kuukomesha. Kwa kweli, yeyote yule ambaye ameshiriki katika mtindo-maisha wenye hatari kubwa ya kuambukiza angefanya vema ajitolee mwenyewe kuchunguzwa damu kuona ikiwa ana UKIMWI kabla ya kuanza utafutaji wa uchumba.
KUTAZAMA MBELE BAADA YA ARUSI
22, 23. (a) Usawaziko ungeweza kupotezwaje wakati wa kutayarishia arusi? (b) Ni maoni gani yenye usawaziko yapasayo kudumishwa wakati wa kufikiria arusi na ndoa?
22 Katika miezi ya mwisho-mwisho kabla ya ndoa, ni yamkini kwamba nyote wawili mtakuwa wenye shughuli sana mkipangia arusi. Mnaweza kupunguza mkazo mwingi kwa kuwa wenye kiasi. Arusi yenye madoido mengi huenda ikapendeza watu wa ukoo na jumuiya, lakini yaweza kuwaacha wale wenye kufunga ndoa karibuni na familia zao wakiwa wamechoka kimwili na wameishiwa kifedha. Kushikamana kidogo na desturi za kwenu kwafaa, lakini kushikamana nazo kwa njia ya kimtumwa na labda ya kushindana na wengine kwaweza kupunguza umaana wa pindi hiyo na huenda kukakunyang’anya ile shangwe unayopaswa kuwa nayo. Ingawa ni lazima hisia za wengine zifikiriwe, bwana-arusi ndiye mwenye daraka hasa la kuamua kile kitakachotendeka kwenye karamu ya arusi.—Yohana 2:9.
23 Kumbuka kwamba arusi yako yadumu siku moja tu, lakini ndoa yako yadumu muda wote wa maisha. Epuka kukazia fikira sana lile tendo la kufunga ndoa. Badala ya hivyo, mwendee Yehova Mungu ili kupata mwongozo, na upangie kimbele maisha ya kuwa mtu ambaye amefunga ndoa. Hapo ndipo utakuwa umetayarisha vizuri kwa ajili ya ndoa yenye mafanikio.
a Hili lingehusu nchi ambako kufanya urafiki na mtu wa jinsia tofauti huonwa kuwa jambo linalofaa kwa Wakristo.
b Hata katika kutaniko la Kikristo, huenda kukawa na watu fulani ambao si wenye kujitoa sana. Badala ya kuwa watumishi wa Mungu wenye moyo wote, huenda wakavutwa na mitazamo na mwenendo wa ulimwengu.—Yohana 17:16; Yakobo 4:4.