Ni Nini Kinachohitajiwa ili Kuwa na Ndoa Yenye Mafanikio?
Je, ungeamua kupiga mbizi mtoni bila kujifunza kuogelea kwanza? Tendo hilo la kijinga lingeweza kuleta madhara—hata kusababisha kifo. Ingawa hivyo, fikiria jinsi ambavyo watu wengi hukimbilia ndoa bila kujua jinsi ya kuchukua madaraka yanayohusika.
YESU alisema: “Ni nani kati yenu atakaye kujenga mnara asiyeketi kwanza na kupiga hesabu ya gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha?” (Luka 14:28) Kama ilivyo katika kujenga mnara ndivyo ilivyo na kujenga ndoa. Wale wanaotaka kuoa wanapaswa kupiga hesabu kwa uangalifu juu ya gharama ya ndoa ili wahakikishe kwamba wanaweza kutimiza matakwa.
Kuichunguza Ndoa
Kuwa na mwenzi wa kushiriki shangwe na huzuni za ndoa kwa kweli ni baraka. Ndoa yaweza kujazia utupu usababishwao na upweke au kukata tumaini. Yaweza kutosheleza tamaa yetu tuliyozaliwa nayo ya kutaka upendo, uandamani, na ukaribu. Baada ya kumwumba Adamu, Mungu alikuwa na sababu nzuri ya kusema hivi: “Si vema huyo mtu awe peke yake, nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye.”—Mwanzo 2:18; 24:67; 1 Wakorintho 7:9.
Naam, kuoa au kuolewa kwaweza kutatua matatizo fulani. Lakini kutaleta mengine mapya pia. Kwa nini? Kwa sababu ndoa yaunganisha nyutu mbili zilizo tofauti ambazo labda zapatana lakini hazifanani kabisa. Kwa sababu hiyo, hata wenzi wa ndoa wanaopatana vizuri watahitilafiana mara kwa mara. Mtume Mkristo Paulo aliandika kwamba wale wanaofunga ndoa watakuwa na “dhiki katika mwili wao”—au kama vile The New English Bible inavyotafsiri, “maumivu na huzuni katika maisha haya ya kimwili.”—1 Wakorintho 7:28.
Je, Paulo alikuwa na maoni yasiyofaa? Sivyo hata kidogo! Alikuwa tu akiwasihi wale waliokuwa wakifikiria ndoa waone mambo kihalisi. Hisia ya furaha ya kuvutiwa na mtu mwingine si kipimio sahihi cha jinsi maisha ya ndoa yatakavyokuwa katika miezi na miaka inayofuata siku ya arusi. Kila ndoa ina magumu na matatizo yake yenyewe ya pekee. Suala si kwamba yatatokea bali namna ya kuyakabili yanapotokea.
Matatizo humpa mume na mke fursa ya kuonyeshana ukweli wa upendo wao. Ili kutoa kielezi: Meli yaweza kuonekana ikiwa nzuri ajabu inapoelea tu, ikiwa imetia nanga gatini. Hata hivyo, uzuri wake baharini, huthibitishwa baharini—labda hata katikati ya mawimbi makali ya dhoruba. Vivyo hivyo, nguvu ya kifungo cha ndoa haithibitishwi tu nyakati za amani za utulivu wa kimahaba. Nyakati nyingine, yathibitishwa katika hali zenye kujaribu ambamo wenzi wa ndoa huvumilia taabu nyingi.
Ili kufanya hivyo, wenzi wa ndoa wanahitaji kuwajibika, kwa kuwa Mungu alikusudia kwamba mwanamume ‘aambatane na mkewe’ na kwamba wote wawili wawe “mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Lile wazo la uwajibikaji huogopesha watu wengi leo. Lakini, ni jambo la kiakili tu kwamba watu wawili wanaopendana kikweli watataka kutoa ahadi rasmi ya kuishi pamoja. Uwajibikaji huipa ndoa adhama. Huandaa msingi wa uhakika ambao, hata kutokee nini, mume na mke watategemezana.a Ikiwa hauko tayari kwa uwajibikaji huo, kwa kweli hauko tayari kufunga ndoa. (Linganisha Mhubiri 5:4, 5.) Hata wale ambao tayari wameoana wanahitaji kuboresha uthamini wao wa jinsi uwajibikaji ulivyo muhimu kwa ndoa yenye kudumu.
Kujichunguza Mwenyewe
Bila shaka waweza kuorodhesha sifa utakazotaka kutoka kwa mwenzi. Hata hivyo, ni vigumu sana kujichunguza mwenyewe na kuamua jinsi unavyoweza kuchangia katika ndoa. Kujichunguza mwenyewe ni jambo muhimu, kabla na baada ya kuweka nadhiri za kifungo cha ndoa. Kwa kielelezo, jiulize mwenyewe maswali yafuatayo.
• Je, niko tayari kuwajibika kwa mwenzi wangu kwa muda wa maisha yangu yote?—Mathayo 19:6.
Katika siku za Malaki nabii wa Biblia, waume wengi waliwaacha wenzi wao, labda ili waoe wanawake wachanga. Yehova alisema kwamba madhabahu yake ilifunikwa kwa machozi ya wake walioachwa, naye aliwahukumia adhabu wanaume ambao ‘waliwatenda [wenzi wao] mambo ya hiyana.’—Malaki 2:13-16.
• Ikiwa nafikiria kuoa au kuolewa, je, nimepita umri wa ujanani ambao hisia za ngono huwa zenye nguvu zaidi na zaweza kupotosha uamuzi mzuri?—1 Wakorintho 7:36.
“Kuna hatari kubwa kuolewa ukiwa mchanga sana,” asema Nikki, aliyeolewa akiwa na umri wa miaka 22. Yeye aonya hivi: “Hisia zako, miradi yako, na mapendezi yako yataendelea kubadilika kuanzia unapokuwa katika umri wa mwisho-mwisho wa utineja hadi unapokuwa na umri wa katikati hadi mwisho-mwisho wa miaka ya 20.” Bila shaka, kuwa tayari kufunga ndoa hakuwezi kupimwa na umri peke yake. Hata hivyo, kuoa wakati mtu hajapita hali ya ujanani wakati hisia za ngono zinapoanza kutokea na hasa zinapokuwa zenye nguvu kwaweza kupotosha kufikiri kwa mtu na kumfanya asione uwezekano wa kuwa na matatizo.
• Nina tabia zipi ambazo zitanisaidia kuchangia ndoa yenye mafanikio?—Wagalatia 5:22, 23.
Mtume Paulo aliandikia Wakolosai hivi: “Jivikeni wenyewe shauku nyororo za huruma, fadhili, hali ya akili ya kujishusha chini, upole, na ustahimilivu.” (Wakolosai 3:12) Shauri hilo lafaa kwa wale wanaofikiria ndoa na pia wale ambao tayari wameoana.
• Je, nina ukomavu unaohitajiwa ili kumtegemeza mwenzi katika nyakati zilizo ngumu?—Wagalatia 6:2.
“Matatizo yatokeapo,” asema daktari mmoja, “huwa kuna mwelekeo wa kumlaumu mwenzi. Jambo la maana zaidi si ni nani wa kulaumiwa. Badala yake, ni jinsi mume na mke wanavyoweza kushirikiana kuboresha uhusiano wa ndoa.” Maneno ya Mfalme Solomoni mwenye hekima yanatumika kwa wenzi wa ndoa. “Afadhali kuwa wawili kuliko mmoja,” akaandika, “kwa maana wakianguka, mmoja wao atamwinua mwenzake; lakini ole wake aliye peke yake aangukapo, wala hana mwingine wa kumwinua!”—Mhubiri 4:9, 10.
• Je, kwa kawaida mimi ni mchangamfu na mwenye maoni yanayofaa, au mimi huwa mwenye huzuni na mwenye maoni yasiyofaa?—Mithali 15:15.
Mtu mwenye maoni yasiyofaa huiona kila siku kuwa mbaya. Ndoa haibadilishi mtazamo huo kimuujiza! Mseja—mwanamume au mwanamke—ambaye ni mchambuzi sana au asiye na maoni yafaayo atakuwa mtu aliyefunga ndoa ambaye ni mchambuzi au asiye na maoni yafaayo. Mtazamo huo usiofaa waweza kuletea ndoa mkazo mkubwa.—Linganisha Mithali 21:9.
• Je, mimi huwa mtulivu ninapokuwa chini ya mkazo, au mimi hujiingiza katika usemi usiodhibitiwa wa hasira kali?—Wagalatia 5:19, 20.
Wakristo wanaamriwa kuwa “wa polepole juu ya hasira ya kisasi.” (Yakobo 1:19) Kabla ya ndoa na baada ya ndoa, mwanamume na mwanamke apaswa kusitawisha uwezo wa kuishi kupatana na shauri hili: “Iweni na hasira ya kisasi, na bado msifanye dhambi; msiache jua litue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.”—Waefeso 4:26.
Kumchunguza Atakayekuwa Mwenzi Wako
“Mwenye busara huangalia sana aendavyo,” yasema mithali ya Biblia. (Mithali 14:15) Kwa hakika hiyo ni kweli unapochagua mwenzi wa ndoa. Kuchagua mwenzi wa ndoa ni mojawapo ya maamuzi ya maana zaidi ambayo mwanamume na mwanamke atapata kufanya. Hata hivyo, imeonwa kwamba watu wengi hutumia wakati mwingi zaidi wakiamua ni gari jipi watakalonunua au ni shule gani watakayoenda kuliko aina ya mtu watakayefunga ndoa naye.
Katika kutaniko la Kikristo, wale waliopewa madaraka ‘wanajaribiwa juu ya kufaa kwanza.’ (1 Timotheo 3:10) Ikiwa wafikiria kuoa au kuolewa utataka kuhakikisha “kufaa” kwa mtu yule mwingine. Kwa mfano, chunguza maswali yafuatayo. Ijapokuwa yametolewa kulingana na maoni ya mwanamke, kanuni zilizo nyingi zatumika kwa mwanamume pia. Na hata wale ambao wameoana wanaweza kunufaika kwa kuchunguza mambo haya.
• Yeye ana sifa ya aina gani?—Wafilipi 2:19-22.
Mithali 31:23 humfafanua mume ambaye “hujulikana malangoni; aketipo pamoja na wazee wa nchi.” Wazee wa jiji waliketi kwenye malango ya jiji ili watoe hukumu. Kwa hiyo, ni dhahiri kwamba alikuwa na cheo cha kuamaniwa katika umma. Jinsi mwanamume anavyoonwa na wengine huonyesha jambo fulani kuhusu sifa yake. Ikifaa, chunguza pia jinsi anavyoonwa na wale walio chini ya mamlaka yake. Hiyo yaweza kuonyesha jinsi wewe, ukiwa mwenzi wake, utakavyomwona baada ya muda.—Linganisha 1 Samweli 25:3, 23-25.
• Ana adili za aina gani?
Hekima ya kimungu “kwanza kabisa ni safi kiadili.” (Yakobo 3:17) Je, yule atakayekuwa mwenzi wako anapendezwa zaidi na kujitosheleza kingono kuliko msimamo wake na wako mbele za Mungu? Ikiwa hajitahidi kuishi kupatana na viwango vya adili vya Mungu sasa, kuna msingi gani wa kuamini kwamba atafanya hivyo baada ya ndoa?—Mwanzo 39:7-12.
• Yeye hunitendeaje?—Waefeso 5:28, 29.
Kitabu cha Biblia cha Mithali husema juu ya mume ambaye “humwamini” mke wake. Zaidi ya hayo, “humsifu.” (Mithali 31:11, 28) Yeye si mwenye wivu kupita kiasi, wala si mwenye kukosa kukubali sababu katika matazamio yake. Yakobo aliandika kwamba hekima kutoka juu ni “yenye kufanya amani, yenye kukubali sababu, . . . yenye kujaa rehema na matunda mema.”—Yakobo 3:17.
• Yeye huwatendeaje washiriki wa familia yake?—Kutoka 20:12.
Kustahi wazazi si takwa kwa watoto tu. Biblia husema: “Msikilize baba yako aliyekuzaa, wala usimdharau mama yako akiwa mzee.” (Mithali 23:22) Kwa kupendeza, Dakt. W. Hugh Missildine aliandika hivi: “Magumu mengi ya ndoa na kutopatana huenda yakaepukwa—au angalau kuonekana mapema—ikiwa wanaotazamiwa kuwa bwana na bibi-arusi wangetembeleana nyumbani bila kupanga mapema na kuchunguza uhusiano kati ya ‘mchumba’ wako na wazazi wake. Jinsi anavyowaona wazazi wake ndivyo atakavyomwona mwenzi wake. Huenda mtu akauliza: ‘Je, nataka kutendewa kama awatendeavyo wazazi wake?’ Na jinsi wazazi wake wanavyomtendea itaonyesha vizuri jinsi atakavyojitendea na jinsi atakavyotazamia wewe umtendee—baada ya fungate.”
• Je, yeye ni mwenye kukasirika haraka au mwenye usemi wenye kuudhi?
Biblia hushauri hivi: “Acheni uchungu wote wenye nia ya kudhuru na hasira na hasira ya kisasi na kupiga kelele na usemi wenye kuudhi viondolewe mbali kutoka kwenu.” (Waefeso 4:31) Paulo alimwonya Timotheo juu ya baadhi ya Wakristo ambao wangekuwa ‘wenye maradhi ya kiakili juu ya maswali-maswali na mashindano juu ya maneno’ na ambao wangekuwa na “husuda, zogo, semi zenye kuudhi, shuku zenye uovu, mabishano makali sana juu ya mambo madogo-madogo.”—1 Timotheo 6:4, 5.
Kwa kuongezea, Paulo aliandika kwamba yule anayestahili kupata mapendeleo ya pekee katika kutaniko hapaswi kuwa “mpiga-watu”—kulingana na Kigiriki cha awali, “si mwenye kushughulika na kupiga.” (1 Timotheo 3:3, kielezi-chini NW) Hawezi kuwa mtu apendaye kupiga watu kimwili au kuwadhulumu kwa maneno. Mtu aelekeaye kuwa mwenye jeuri anapokasirika si mtu afaaye kuwa mwenzi wa ndoa.
• Ana miradi gani?
Wengine hufuatia utajiri na kuvuna matokeo yasiyoepukika. (1 Timotheo 6:9, 10) Wengine huishi bila kusudi maishani bila miradi ya kufikia. (Mithali 6:6-11) Hata hivyo, mtu wa kimungu, ataonyesha azimio lilelile aliloonyesha Yoshua, aliyesema: “Mimi na nyumba yangu tutamtumikia BWANA.”—Yoshua 24:15.
Thawabu na Madaraka
Ndoa ni kifungo cha kimungu. Iliidhinishwa na kuanzishwa na Yehova Mungu. (Mwanzo 2:22-24) Alianzisha mpango wa ndoa ili kufanyiza kifungo cha daima kati ya mwanamume na mwanamke ili waweze kusaidiana. Kanuni za Biblia zinapofuatwa, mume na mke wanaweza kutarajia shangwe katika maisha yao.—Mhubiri 9:7-9.
Ingawa hivyo, yapasa kutambuliwa kwamba tunaishi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Biblia ilitabiri kwamba katika kipindi hiki cha wakati, watu wangekuwa “wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, wenye kujitanguliza, wenye kiburi, . . . wasio waaminifu-washikamanifu, wasio na shauku ya kiasili, wasiotaka upatano wowote, . . . wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kututumuka kwa kiburi.” (2 Timotheo 3:1-4) Tabia hizi zaweza kuwa na athari yenye nguvu sana katika ndoa ya mtu. Hivyo, wale wanaofikiria ndoa wanapaswa kuhesabu gharama kwa makini. Na wale ambao sasa wameoana wapaswa kuendelea kuboresha muungano wao kwa kujifunza na kutumia mwongozo wa kimungu unaopatikana katika Biblia.
Naam, wale wanaofikiria ndoa itafaa wafikirie zaidi baada ya siku ya arusi. Na wote wanapaswa kufikiria si tu tendo la kufunga ndoa bali pia maisha ya ndoa. Mtegemee Yehova akupe mwongozo ili ufikirie mambo kihalisi badala ya kimahaba tu. Kwa kufanya hivyo, yaelekea utafurahia zaidi ndoa yenye mafanikio.
[Maelezo ya Chini]
a Biblia huruhusu sababu moja tu ya talaka kukiwa na uwezekano wa kuoa tena, nayo ni “uasherati”—mahusiano ya ngono nje ya ndoa.—Mathayo 19:9.
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
“Ufafanuzi Bora Zaidi wa Upendo Ambao Nimepata Kusoma”
“Wajuaje kwa kweli ikiwa unampenda mtu?” aandika Dakt. Kevin Leman. “Kuna kitabu cha kale kilicho na ufafanuzi wa upendo. Kitabu chenyewe kina miaka ipatayo elfu mbili hivi, lakini bado ndicho chenye ufafanuzi bora zaidi wa upendo ambao nimepata kusoma.”
Dakt. Leman alikuwa akirejezea maneno ya mtume Mkristo Paulo yapatikanayo katika Biblia kwenye 1 Wakorintho 13:4-8:
“Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujitutumui, haujiendeshi bila adabu, hautafuti masilahi yao wenyewe, haupati kuwa wenye kuchokozeka. Hauweki hesabu ya ubaya. Haushangilii ukosefu wa uadilifu, bali hushangilia pamoja na kweli. Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.”
[Sanduku katika ukurasa wa 8]
Hisia-Moyo Zaweza Kudanganya
Ni dhahiri kwamba msichana Mshulami wa nyakati za Biblia alijua kuhusu nguvu yenye kudanganya ya hisia za kimahaba. Alipobembelezwa na Mfalme Solomoni mwenye mamlaka, aliwaambia waandamani wenzake wa kike ‘wasiyachochee mapenzi [yake], wala kuyaamsha hata yatakapoona vema yenyewe.’ (Wimbo Ulio Bora 2:7) Mwanamke huyo mchanga mwenye hekima hakutaka rafiki zake wamsonge aongozwe na hisia-moyo zake. Pia jambo hilo lafaa, kwa wale wanaofikiria ndoa leo. Dhibiti hisia zako. Ukifunga ndoa, yapasa iwe kwa sababu wampenda mtu huyo, si kwa sababu tu ya lile wazo la kuoa au kuolewa.
[Picha katika ukurasa wa 6]
Hata wale waliooana kwa muda mrefu wanaweza kuimarisha vifungo vyao vya ndoa
[Picha katika ukurasa wa 7]
Yeye hutendeaje wazazi wake?