Sura ya 3
Baada ya Siku ya Harusi
1. Ushirikiano unaoelezwa katika Mhubiri 4:9, 10 ungewezaje kumpa mwenzi wa ndoa faida?
SASA arusi yako imekwisha, wewe na mwenzi wako wa ndoa mnaanza kutulia kama msingi mpya wa jamaa. Je! furaha yako imetimilika? Sasa hauko peke yako bali una mwenzi wa kutumaini, kushiriki naye furaha zako na magurnu yako. Je! sasa unaona maneno ya Mhubiri 4:9, 10 yakikuhusu wewe? —“Afadhali kuwa wawili kuliko mmoja; maana wapata ijara njema kwa kazi yao. Kwa maana wakiangua, mmoja wao atamwinua mwenzake; lakini ole wake aliye peke yake aangukapo, wala hana mwingine wa kumwinua!” Je! ndoa yako inasitawi ikiwa na ushirikiano wa namna hiyo? Ili mwungano huo wa watu wawili uwe wenye furaha, kwa kawaida inachukua wakati na kufanya bidii. Lakini inasikitisha kusema ndoa nyingi haziko hivyo hata kidogo.
2, 3. (a) Ni matatizo gani ya maisha yanayopaswa kuondolewa baada ya siku ya harusi? (b) Sababu gani ni jambo la busara kutazamia kwamba mabadiliko yatapaswa yafanywe mtu akiisha kuoa au kuolewa?
2 Katika hadithi za mambo ya mahaba ya kuwazia tu, mara nyingi kunakuwa taabu kuunganisha watu wawili wanaopendana. Lakini baadaye wanaishi kwa furaha. Katika maisha ya kweli na yasiyo ya kuwazia tu, kinacholeta taabu ni kuishi kwa furaha kila siku baadaye. Zikiisha furaha za siku ya arusi kunatokea kawaida ya kila siku ya maisha: kuamka mapema, kwenda kufanya kazi, kununua vitu, kupika vyakula, kusafisha sahani na sufuria, kusafisha nyumba, na mengineyo.
3 Uhusiano wa ndoa unataka mabadiliko. Ninyi wawili mliingia katika uhusiano huo mkiwa na matazamio fulani na kufikiria mambo fulani yaliyokuwa bado kutokea. Huenda ukakata tamaa baada ya juma chache za kwanza yasipotimizwa hayo. Lakini kumbuka kwamba umefanya badiliko kuu katika maisha yako. Sasa huishi peke yako tena wala kuishi pamoja na jamaa ambayo umekuwa nayo maisha yako yote. Sasa uko pamoja na mtu mwingine, mtu ambaye huenda ukaanza kupata habari kwamba humjui kama ulivyokuwa umedhani. Orodha yako ni mpya, labda kazi yako vilevile ni mpya, mpango wa matumizi ya fedha ni tofauti, tena wako rafiki wapya na wakwe wa kuzoeana nao. Kufanikiwa kwa ndoa yako na furaha yako yategemea utayari wako wa kubadilika.
JE! UNAWEZA KUBADILIKA ILI UPATANE NA HALI?
4. Ni kanuni gani za Maandiko ambazo zingeweza kumsaidia mtu aliyeoa au kuolewa afanye mabadiliko? (1 Wakorintho 10:24; Wafilipi 4:5)
4 Wengine wanaona ni vigumu kubadilika kwa sababu ni wenye kiburi. Lakini, kama Biblia inavyosema, “kiburi hutangulia uangamivu; na roho yenye kutakabari hutangulia maanguko.” Kuendelea kuwa mwenye kichwa kikubwa kunaweza kuleta msiba. (Mithali 16: 18) Yesu alipendekeza mtu awe na nia na wepesi wa kukubali kubadilika wakati aliposema kwamba ikiwa mtu ye yote angetaka “kuitwaa kanzu yako, mwachie na joho pia,” na ikiwa mtu fulani angetaka uende “mwendo wa maili moja, nenda naye mbili.” Badala ya kubishana na mtu aliye karibu sana nawe, mtume Paulo aliuliza hivi: “Maana si afadhali kudhulumiwa?” (Mathayo 5:40, 41; 1 Wakorinthe 6:7) Ikiwa Wakristo wanaweza kufikia kiasi hicho ili wapatane na wengine, bila shaka, watu wawili waliooana wamepaswa wawe na uwezo wa kubadilika ili wafanikishe uhusiano wao mpya.
5. Mtu anaweza kumfikiriaje mwenzi wa ndoa kwa njia inayofaa au isiyofaa?
5 Ziko nafasi kila mahali za kumfanya mtu ama awe na furaha ama akose furaha. Utaangalia nafasi gani? Je! utakaza fikira juu ya kuwa na furaha au juu ya kukosa furaha? Huenda mke mpya akafikiri hivi: ‘Kwa vile sasa tumeoana, yuko wapi mwanamume yule mwenye mahaba aliyekuwa akinipeleka kwenye mahali pa kupendeza na kutumia wakati wake akiwa name? Sasa amefuata kawaida ile ile bila kubadilika. Sasa ananiona vivi hivi tu. Bila shaka si mwanamume yule niliyetangulia kujua! Au je! mke anafahamu na kuthamini kwamba sasa mume anafanya kazi kwa bidii ili awe mtoaji mwema wa riziki ya jamaa yake? Je! mume mpya huyo anafahamu kwamba mke wake anafanya kazi kwa bidii ili apike vyakula na kusafisha nyumba, na nyakati nyingine anachoka sana na kuwa hana wakati mwingi wa kutumia ajaribu kuwa na sura yenye kupendeza? Au anajisemea mwenyewe hivi: ‘Hee! yule mwanamke aliyekuwa msichana mrembo niliyeoa amekuwaje sasa? Sasa ameaeha kuwa mrembo kwa vile ana mume’?
6. Wakati mume na mke wanapojaribu sana kufanikisha ndoa yao, jambo hilo linapasaje uhusiano wao kwa wao?
6 Imewapasa wote wawili wawe watu waliokomaa na kufahamu kwamba hakuna mmoja wao aliye na wakati wala nguvu za kufanya mambo yote yaliyokuwa yakifanywa kabla ya kufunga ndoa. Sasa ndio wakati wa kuonyesha hali ya kubadilikana na kukubali daraka lenye kufurahisha sana la kufanikisha ndoa. Mtu mmoja anaweza kuharibu ndoa, lakini watu wawili wanatakiwa ili kuifanya ifanikiwe. Kufanikisha ndoa ni tendo. Tendo maana yake ni kutimiza jambo fulani yajapokuwa matatizo. Wakati ninyi wawili mnapoingia katika jambo hilo, sehemu ya kila mmoja wenu inashiriki kufanyiza tendo hilo. Bidii hiyo ya pamoja yenye mradi wenu nyote, inawaunganisha pamoja; inawafungamanisha pamoja; inawafanya ninyi wawili kuwa mmoja. Halafu hilo linafanyiza kifungo cha upendo unaopita jambo lo lote linaloonwa wakati wa kutazamia ndoa, na inafurahisha katika furaha hiyo inayounganisha kubadili tofauti zako ili zilingane na tofauti za mwenzako.
7. Ikiwa ni lazima kufanya maamuzi, inafaa kukubali yanayompendeza mwenzako wakati gani?
7 Kiburi kinakwisha wakati upendo unapoongezeka, tena kuna furaha, si katika kutoa tu, bali vilevile katika kuacha yanayokupendeza ili kukubali yanayompendeza mwenzako ikiwa hakuna kanuni inayovunjwa kwa kufanya hivyo. Huenda ikawa ni kununuliwa kwa kitu fulani cha nyumbani, au namna ya kutumia wakati wa kupumzika (likizo). Wakati kufikiria furaha ya mmoja na mwenzake kunapoonyeshwa, mume na mke wanaanza kupatana na maneno haya ya mtume Paulo: “Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, Bali kila mtu aangalie mambo ya wengine.”—Wafilipi 2:4.
MAONI YALIYOSAWAZIKA JUU YA NGONO
8, 9. Ni maoni gani ya Maandiko juu ya ngono?
8 Biblia haina haya ya kusema habari za ngono. Inaonyesha kwa kutumia usemi wa mashairi furaha ambayo ngono imepaswa kuletea mume na mke; inatia mkazo vilevile kwamba ngono imepaswa ifanywe na mume na mke waliooana tu. Maneno hayo yanapatikana katika Mithali 5:15-21:
“Unywe maji ya birika lako mwenyewe, na maji, yenye kububujika katika kisima chako. Je! chemchemi zako zitawanyike mbali, na mito ya maji katika, njia kuu? Yawe yako mwenyewe peke yako, wala si ya wageni pamoja nawe. Chemehemi yako ibarikiwe; nawe umfurahie mke wa ujana wako. Ni ayala apendaye na paa apendezaye; maziwa yake yakutoshe sikuzote; na kwa upendo wake ushangilie daima. Mwanangu! mbona unashangilia malaya, na kukikumbatia kifua cha mgeni? Kwa maana njia za mwanadamu zi mbele za macho ya [Yehova!].”
9 Lakini, lingekuwa kosa kutia mkazo mkubwa mno juu ya ngono hata ionekane kwamba kufanikiwa kwa ndoa kunategemea mume na mke wafanye ngono, au kwamba ingeweza kulipia makosa mazito yaliyo katika sehemu nyingine za uhusiano huo. Habari nyingi mno juu ya ngono zinazotolewa katika vitabu, sinema na television na watu wa biashara, zinatolewa kwa kusudi la kuamsha nyege na kufanya ngono ionekane kuwa ya maana sana. Walakini, Neno la Mungu halikubaliani na hayo, linapendekeza kujiweza katika mambo yote ya maisha. Hata katika ndoa, kukosa kujizuia kunaweza kuongoza kwenye mazoea yanayopunguza heshima ya uhusiano wa ndoa.—Wagalatia 5: 22, 23; Waebrania 13:4.
10. Ni mambo gani ya kufikiria ambayo yangeweza kusaidia mume na mke wasawazishe ngono zao?
10 Si vyepesi mara nyingi kuwa na kiasi katika kufanya ngono, na huenda ikachukua muda baada ya arusi ili mtu awe na kiasi. Inakuwa hivyo kwa kawaida kwa sababu ya kutojua na kukosa kufahamu mahitaji ya mwenzako. Labda kuzungumza mapema na rafiki aliyeoa au kuolewa kunaweza kusaidia. Mwanamume na mwanamke hawakuumbwa kwa njia tofauti tu, bali vilevile wana maoni yaliyo tofauti. Ni jambo la maana kufikiria uhitaji wa kumhurumia mwanamke. Lakini kusiwe maoni mabaya ya kuwa na haya mno au maoni ya kwamba ngono ni jambo la aibu. Wala isiwe nafasi ya mume kumshinda mke, kama walivyo wanaume wengine. “Mume na ampe mkewe haki yake,” Biblia inasema, “na vivyo hivyo mke ampe mumewe haki yake.” Na kanuni hii ya Biblia inafaa katika kufanya hivyo: “Mtu asitafute faida yake mwenyewe, bali ya mwenzake.” Ukiwako upendo huo pande zote mbili na kutaka kumpendeza mwingine, mabadiliko mema yatafanywa.—1 Wakorintho 7:3; 10:24.
MKOSANE B1LA KUGOMBANA
11-13. Kunapokuwa na kutopatana, imetupasa tukumbuke nini ili tofauti hizo zisiendelee kukua ziwe ugomvi mkubwa?
11 Duniani hakuna watu wawili wanaofanana kabisa. Kila mmoja ni mtu aliye tofauti kabisa na mwenzake. Maana ya jambo hilo ni kwamba watu wawili hawawezi kupatana katika kila jambo. Ugomvi mwingi hauwi mkubwa sana, lakini mwingine unakuwa mkubwa sana. Kuna nyumba ambamo ugomvi unatokeza upesi makelele, kusukumana-sukumana, mmoja akimpiga mwenzake na kutupiana vitu au huenda mwingine akaondoka nyumbani kwa muda wa siku au juma fulani, au labda wanaweza kuacha kusemezana. Inawezekana sana kukosana bila ugomvi wa namna hiyo kutokea. Namna gani? Kwa kufuata wazo fulani la msingi ambalo ni kweli.
12 Sisi sote ni watu wasiokamilika, sote tuna makosa, nayo makosa yanatokea hata tukiwa na makusudi mazuri sana. Mtume Paulo alijiona hivyo: “Lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo.” (Warumi 7: 19 ) Tumerithi dhambi kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza. Ukamilifu uko mbali nasi. Kwa hiyo, “nani awezaye kusema, Nimesafisha moyo wangu; nimetakasika dhambi yangu!”—Mithali 20:9; Zaburi 51:5; Warumi 5:12.
13 Tunakubali makosa yetu na kutoa sababu za kuyaachilia. Je! hatuwezi kukubali na kuachilia makosa ya mwenzi wetu wa ndoa? Bila shaka tunakubali vyepesi kwamba sisi ni watenda dhambi, lakini je! tunajitetea na kukataa kukubali dhambi tunayoambiwa kwamba tumefanya? Je! tunafahamu kwamba watu wengine wanakataa kukubali kuwa wamefanya kosa, kutia na mwenzi wetu wa ndoa? Je! tunakumbuka kwamba hilo laweza kutokea? “Akili ya mutu inamuzuiza kukasirika mbio; na ni utukufu wake kusamehe kosa,” mithali iliyoongozwa na Mungu inasema hivyo. Bila shaka wewe unataka uwatendee wengine kama vile unavyotaka wakutendee. Katika Mahubiri yake ya Mlimani yenye kujulikana sana, Yesu alisema hivi: “Yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.” Watu wengi wanasema hivyo kwa maneno tu; wachache ndio wanaofuata maneno hayo. Kama yangefuatwa kwa unyofu, yangeondoa magumu ya uhusiano wa wanadamu, kutia na yale ya ndoa.—Mezali 19:11, ZSB; Mathayo 7:12.
14, 15. (a) Kwaweza kutokea nini ikiwa mtu anamlinganisha mwenzi wake wa ndoa isivyofaa na mtu mwingine? (b) Nyakati nyingine ulinganisho huo unafanywa juu ya mambo gani yasiyofaa?
14 Kila mmoja wetu anataka kufikiriwa na kutendewa kama mtu aliye tofauti. Mtu anapotulinganisha na mwingine isivyofaa, labda akidharau sifa zetu au uwezo wetu, tunaonaje? Kwa kawaida tunaudhika au kuona uchungu. Kwa kweli tunasema hivi, ‘Lakini mimi si mtu huyo. Mimi ni MIMI.’ Kwa kawaida ulinganifu huo hautii moyo, kwa sababu sisi tunataka tutendewe katika njia ya ufahamu.
15 Kwa mfano: Wewe mume, je! unatoa shukrani kwa vyakula ambavyo mke wako anapika au unanung’unika ukisema kwamba hawezi kupika kama mama yako? Wajuaje mama yako alivyoweza kupika vizuri alipokuwa ameolewa karibuni hivi? Labda mke wako anapika vizuri kuliko mama yako alivyopika. Mpe mke wako nafasi ya kuzoelea kazi zake mpya apate kujua sana kuzifanya. Na wewe mke, je! unanung’unika kwamba mume wako mpya haleti mshahara wa kutosha kama ule ambao baba yako alikuwa akileta? Baba yako alikuwa akipata mshahara gani alipokuwa ameoa karibuni hivi? Hata hilo si jambo la maana. Jambo la maana ni ule msaada unaompa mume wako Je! unaamka mapema na kumtayarishia kiamshakinywa (chakula cha asubuhi) kabla hajaenda kazini, ili apate kuona kwamba unamwunga mkono na kuthamini bidii zake? Je! ye yote kati yenu anagombana na mwenzake kwa sababu ya wakwe, au kukosana juu ya nani wanaopaswa kuwa rafiki zenu au tafrija ya kushiriki? Huenda ukatokea ugomvi huo au mwingine. Utaumaliza namna gani?
16. Ni kosa gani la kuwaza kwamba magombano makali yanasaidia kumaliza matata?
16 Wachunguzi wengine wa siku hizi wa magonjwa ya akili wanapinga wakisema kwamba ugomvi unafaa ili kumaliza matatizo. Wanawaza kwamba vipingamizi vinaongezeka, vikifanyiza mkazo na mwishowe vinatokea ghafula kuwa ugomvi wenye jeuri. Wanawaza kwamba wakati wa kutupiana maneno makali namna hiyo, ule uchungu ambao umezuiliwa ndani muda mrefu unaondolewa moyoni na kutupwa. Isipokuwa inakuwa hivyo, vipingamizi hivyo vinazuiliwa ndani ya moyo na kuanza kujazana sana na mwisho kutokeza hasira kali. Lakini kuna hatari kubwa kiasi cha kwamba kupandwa hasira hivyo kwaweza kukufanya useme maneno usiyotaka kusema, na mambo mabaya yaweza kufanywa isiwezekane hata kuyaondoa. Huenda ukamkosea sana mwenzako hata kutokee kizuizi usichoweza kuondoa baadaye. Kama Mithali 18: 19 inavyoonya: “Ndugu aliyechukizwa ni mgumu kuliko mji wa nguvu; na mashindano ni kama mapingo ya ngome.” Shauri jema linalopatikana katika Biblia ni: “Acheni mabishano mbele ya kugeuka kuwa ugomvi.”—Mezali 17:14, ZSB.
PASHANENI HABARI:
17. Ni nini linaloweza kufanywa ili kuzuia mambo yanayoleta ugomvi yasijazame ndani ya mtu na kugeuka kuwa ugomvi mkubwa?
17 Afadhali kuzungumza mambo yanayoleta ugomvi wakati yanapotokea, kuliko kuyaacha yaongezeke ndani ya moyo hata yageuke kuwa ugomvi mkubwa. Kuendelea kufikiria kosa lile lile kila wakati, kunalifanya lionekane kuwa baya sana kuliko lilivyo. Lizungumzeni sasa au mlisahau. Je! ni neno la muda tu? Liachilieni mbali. Je! ni lazima lizungumzwe? Je! mwenzako amefanya jambo linalokuudhi? Usilaumu jambo hilo bila kutumia busara; jaribu kulitaja kwa njia ya kuuliza ulizo, au kutoa wazo litakaloweka mwanzo wa kulizungumza. Kwa mfano, unaweza kusema: ‘Mpenzi wangu, kuna neno ambalo mimi sifahamu. Ungeweza kunisaidia?’ Kisha sikiliza. Jaribu kufahamu maoni ya mwenzako. Fuata onyo la Mithali 18:13: “Yeye ajibuye kabla hajasikia, ni upumbavu na aibu kwake.” Hakuna mtu ye yote kati yetu anayependa wakati mwingine anapotudhania mambo mabaya bila kujua habari zote. Kwa hiyo, kabla ya kujibu upesi, jaribu kufahamu kusudi au nia iliyoleta tendo hilo. Fanya kama Mithali 20:5 inavyoshauri: “Mashauri ya moyoni ni kama kilindi; lakini mtu mwenye ufahamu atayateka.”
18. Ni nini linaloweza kutusaidia tuondoe moyo mzito?
18 Je! wewe ni mtu mwenye moyo mzito? Si vyepesi kuishi na mtu aliye na moyo mzito. Wengine wanapinga wakisema kwamba hatuwezi kuzuia hali ya kuwa na moyo mzito (kutochangamka), maana hali hizo zinaongozwa na mageuzo yanayofanyika katika ubongo. Kwamba ni hivyo au sivyo, maoni yanaenea kwa watu wengi. Huenda ama tukachangamshwa ama tukashushwa (tukavunjwa) moyo na wale walio karibu yetu. Muziki unaweza kutia hali mbalimbali ndani ya mioyo yetu. Vilevile hadithi zaweza kufanya hivyo. Mawazo tunayoendelea kuweka katika akili zetu yanaongoza maoni yetu. Ukizidi kufikiria mambo yasiyofaa utashushwa moyo; kwa kutumia nia yako unaweza kuzilazimisha akili zifikirie mawazo yaliyo hakika na yenye matumaini mema. Yafikirie. (Wafilipi 4:8) Ukiona hilo kuwa jambo gumu, jaribu kufanya mazoezi sana ya kutumia viungo vya mwili—fanya kazi ya nguvu, hata ikiwa ni kupalilia magugu shambani au kusafisha nyumba chini; toka nje na kutembea polepole msituni, au, tafuta jambo la kufaa kumfanyia mtu mwingine—lo lote la kugeuza fikira na nguvu kwingine. Afadhali kusitawisha moyo mchangamfu kuliko moyo mzito. Tena unakuletea furaha nyingi sana, na zaidi mwenzi wako!
19. Mtu anawezaje kumtendea mwenzi wake wa ndoa aliye na moyo mzito kwa ufahamu?
19 Lakini, kuna nyakati matukio yanapokuhuzunisha sana, au unaposumbuliwa sana na ugonjwa na maumivu. Au, ikiwa ni mke wako, vile vipindi vya kuingia mwezini na wakati wa kuwa na mimba vinatofautiana sana katika utoaji wa umajimaji wenye nguvu ulio katika damu unaochochea viungo vingine vya mwili. Na huo unageuza hali ya mishipa na maono ya moyoni. Huenda mwanamke akapatwa na wasiwasi unaotangulia kipindi cha kuingia mwezini pasipo yeye kufahamu. Hilo ni jambo kubwa linalompasa mume kukumbuka ili aweze kuonyesha busara badala ya kukasirika. Katika hali hizo za pekee mume na mke wamepaswa kufahamu kinachogeuza tabia wapate kuitikia katika njia yenye kujenga. “Moyo wa mwenye hekima unafanya kinywa chake kionyeshe busara, nao unaongeza ushawishi kwenye midomo yake.” Naye “mwenzi wa kweli anapenda wakati wote, naye ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya wakati ambapo kuna taabu.”—Mithali 16:23; 17:17, NW.
20-22. (a) Sababu gani wivu usiofaa wapaswa uepukwe? (b) Ni nini linaloweza kufanywa ili mwenzi wa ndoa ajisikie salama?
20 Je! mwenzi wako wa ndoa ni mwenye wivu? Inafaa mtu aonee sifa yake wivu, na ndoa yake vilevile. Kama vile umajimaji unaotolewa na viungo vya mwili unavyoamsha moyo ukaanza kupigapiga tena, ndivyo na wivu unavyoiamsha nafsi ipate kulinda kitu kinachopendwa sana. Kinyume cha wivu ni ubaridi, nasi haitupasi tuonyeshe ndoa yetu. ubaridi.
21 Lakini kuna wivu wa namna nyingine, ule unaoletwa na ukosefu wa usalama na kusitawishwa kwa kuwazia tu mambo yasiyo kweli. Wivu huo usio wa busara na wenye kutaka mambo mno au kupendwa mno unageuza ndoa kuwa gereza lisilopendeza ambapo tumaini na upendo wa kweli hauwezi kuendelea. “Upendo hauna wivu” katika njia hiyo, nao wivu wenye kuendelea kusumbua sana akili “ni ubovu wa mifupa.”—1 Wakorintho 13:4, NW; Mithali 14:30.
22 Ikiwa mwenzi wako ana sababu inayofaa ya kujiona kukosa usalama kwa sababu ya wivu, ondoa sababu hiyo bila kukawia. Ikiwa hakuna sababu ya kweli, fanya kadiri uwezavyo umsaidie mwenye wivu apate kuwa na uhakika, kwa maneno na hata zaidi kwa matendo yako. Ufikie moyo wake!
23. Ni jambo gani linaloweza kufikiriwa kwa kufaa wakati mtu anapokuwa na maelekeo ya kuomba watu wa nje msaada wa kumaliza matatizo ya ndoa?
23 Je! watu wa nje wanaweza kusaidia kumaliza ugomvi kati ya watu waliooana? Labda, lakini hawapaswi kuitwa isipokuwa mume na mke wote wawili wanakubali hivyo. Kwanza, “sema neno lako pamoja na jirani yako, wala usifunue siri ya mutu mwingine.” (Mezali 25:9, ZSB) Kuna hatari sana katika kuomba wakwe wapate kupatanisha watu wanaogombana. Inaelekea kwamba watapendelea mtu mmoja. Bibila inasema hivi kwa hekima: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe.” (Mwanzo 2:24) Jambo lilo hilo linahusu mke kwa habari ya wazazi wake na mume wake. Badala ya kuomba wazazi au wakwe wapatanishe watu wanaogombana, wapendelee mwenzi mmoja kuliko mwingine, mume na mke wamepaswa waambatane pamoja, wakifahamu kwamba wote wawili wanashiriki matatizo yao yanayohitaji kumalizwa wakiwa pamoja. Mtu mmoja akiomba watu wa nje wawapatanishe bila mwenzake kukubali, kunawaaibisha wote wawili machoni pa wengine. Ikiwa mtapashana habari waziwazi, kwa unyofu na kwa upendo, hakuna sababu inayoweza kuzuia msiweze ninyi wenyewe kumaliza matatizo yenu. Watu wengine waliokomaa wanaweza kuombwa shauri, lakini ni juu yako na mwenzi wako kutoa uamuzi wa mwisho juu ya kumaliza kukosana.
24, 25. Mtu anaweza kufanya nlni ikiwa kiburi kinamzuia kumaliza matatizo ya ndoa?
24 “Usiwe mwenye kichwa kikubwa wala kujivuna mno,” anashauri mtume Paulo. (Warumi 12:3, New English Bible) Kisha anaongeza maneno haya: “Katika kuonyeshana heshima, wekeni mfano.” (Warumi 12:10, NW) Mara nyingine kiburi chetu kinapoumizwa inatusaidia tuone kwamba sisi si watu wakubwa sana. Bila shaka sisi si wakubwa tukilinganishwa na dunia, na dunia nayo ni ndogo ikilinganishwa na jua na kundi la sayari zinazozunguka jua, nalo kundi hilo linaonekana kuwa dogo sana likilinganishwa na ulimwengu wote. Machoni pa Yehova “mataifa yote huwa kama si kitu ... huhesabiwa kwake kuwa duni ya si kitu, na ubatili.” (Isaya 40:17) Mawazo hayo yanasaidia kuona mambo vizuri kulingana na yanavyohusiana, ili tufahamu kwamba huenda magombano yasitie ndani mambo hayo makubwa.
25 Ucheshi (kuchekesha ) vilevile unaweza kutusaidia nyakati nyingine tusijione kuwa watu wenye maana sana kuliko wengine. Kuweza kujicheka mwenyewe kunaonyesha hali ya kukomaa, nako kunaondoa matata mengi maishani.
“TUPA CHAKULA CHAKO USONI PA MAJI”
26, 27. Ni kanuni gani za Biblia zinazopaswa kutumiwa wakati mwenzi wa ndoa hakubali bidii za kutaka kumaliza tofauti kwa amani, na kwa sababu gani?
26 Namna gani ikiwa mwenzi wako anakataa kukubali bidii zako za kutaka kumaliza ugomvi kwa amani? Fuata shauri hili la Biblia: “Msimlipe mtu ovu kwa ovu.” Yesu ndiye mfano wetu wa kufuata: Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano.” Kawaida ya watu ni kurudisha tendo lile lile. Lakini ukifuata mwendo huo unaruhusu wengine wakugeuze uwe kama ulivyo sasa. Kwa kweli, wanakufanya uwe kama wao walivyo. Ukiruhusu jambo hilo litokee ni kujikana mwenyewe, ni kukana unalotetea, ni kukana kanuni unazopenda sana. Badala yake, fuata mfano wa Yesu, asiyejikana, asiyegeuzwa na makosa ya wale walio karibu yake: “Kama sisi hatuamini, yeye hudumu wa kuaminiwa. Kwa maana hawezi kujikana mwenyewe.”—Warumi 12:17; 1 Petro 2:23; 2 Timotheo 2:13.
27 Ikiwa una uwezo wa kuzuia mabaya kwa mema, unaweza kuanzisha mema. “Jibu la upole linageuza hasira.” (Mezali 15:1, ZSB) Jibu la upole halitokani na udhaifu bali latokana na nguvu, na mwenzi wako atajua hivyo. Kwa kuwa watu wengi wanalipa mabaya kwa mabaya, unaweza kugeuza mabaya yawe mema kwa kutumia wema. Maandiko fulani yanaonyesha hivyo. “Anyweshaye atanyweshwa mwenyewe.” “Kwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa.” “Tupa chakula chako usoni pa maji; maana utakiona baada ya siku nyingi.” (Mithali 11:25; Luka 6:38; Mhubiri 11:1) Huenda ikachukua muda mrefu ili wema wako utokeze mema kwa mwenzi wako. Hupandi mbegu siku moja na kesho yake ukavuna. Hata hivyo, “cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna .. . Tena tusichoke katika kutenda mema, maana tutavuna wakati wake, tusipozimia roho.”—Wagalatia 6:7-9.
28. Ni baadhi ya kanuni gani bora zinazopatikana katika kitabu cha Biblia cha Mithali, zinazoweza kusaidia kuendeleza maisha ya ndoa yenye furaha, na kwa njia gani?
28 Haya ni maandiko na maulizo yanayopaswa kufikiriwa na waume na wake waliooana:
Mithali 14:29: “Asiye mwepesi wa hasira ana fahamu nyingi; bali mwenye roho ya hamaki hutukuza upumbavu.” Ukitafuta nafasi ya kufikiri, je huoni mara nyingi kwamba hakuna sababu inayofaa kukasirika?
Mithali 17:27: “Azuiaye maneno yake ni mwenye maarifa; na mwenye roho ya utulivu ana busara.” Je! unatuliza roho yako, na kuzuia maneno ambayo yangechochea roho ya mwenzi wako?
Mithali 25:11: “Neno linenwalo wakati wa kufaa ni kama machungwa, katika vyano vya fedha.” Huenda neno linalofaa wakati mmoja lisifae wakati mwingine. Je! wafahamu lililo neno linalofaa wakati wa kufaa?
Mithali 12:18: “Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga; bali ulimi wa mwenye haki ni afya.” Kabla hujasema, je! unafikiri kidogo namna maneno yako yanavyoweza kuwa na matokeo juu ya mwenzi wako?
Mithali 10:19: “Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa, na maovu; bali yeye azuiaye midomo yake hufanya akili.” Mara nyingine tukikasirika, tunasema maneno mengi kuliko tunavyotaka kusema, na baadaye tunasikitika. Je! unajiangalia na hilo?
Mithali 20:3: “Mtu kujitenga na ugomvi ni heshima kwake; bali kila mpumbavu ataka kugombana.” Ugomvi unataka watu wawili. Je! umekomaa vya kutosha kuweza kuuzuia?
Mithali 10:12, “New World Translation”: “Chuki ndiyo inayochochea ugomvi, lakini upendo unafunika hata makosa yote.” Je! unaendelea kuvumbua ugomvi wa kale, au unampenda sana mwenzi wako kiasi cha kuweza kuusahau?
Mithali 14:9, “New English Bible”: “Kwa sababu ya kuwa mwenye kiburi mno, mpumbavu hawezi kusawazisha makosa; wanyofu wanajua maana ya upatanisho.” Je! wewe una kiburi mno hata huwezi kukubali makosa na kutafuta amani katika ndoa yako?
Mithali 26:20: “Moto hufa kwa kukosa kuni.” Unaweza kuacha ugomvi, au ni lazima useme neno lako la mwisho?
Waefeso 4:26 : “Jua lisichwe na uchungu wenu bado haujawatoka.” Je ! unaendelea katika hali ya kukosana na mwenzako, na kwa njia hiyo unajifanyia hali yako na ile ya mwenzi wako izidi kuwa mbaya?
29. Ni mambo gani ya msingi yanayofaa kukumbukwa wakati wa kutafuta kuendeleza ndoa yenye furaha?
29 Shauri la hekima linaleta faida linapofuatwa tu. Jaribu kulitumia. Vilevile, jaribu kutumia wazo analotoa mwenzi wako. Jaribu uone kama litafaa. Jambo fulani likiwa baya, nani atalaumiwa? Hilo si jambo la maana. Jambo la maana ni namna ya kutengeneza mambo. Uwe mwepesi wa kubadilika, eleza tofauti, zizungumze pamoja na mwenzi wako, na usijione kuwa mtu mkubwa sana. Pashaneni habari! Iwapo ‘wampenda mwenzi wako kama unavyojipenda,’ haitakuwa vigumu sana kubadili hali yako ipatane na ile ya ndoa na kuifanya iwe yenye furaha.—Mathayo 19:19.