Sura ya 5
Mke Anayependwa Sana
1-4. Ni manung’uniko gani ambayo mara nyingine wanawake wanatoa juu ya kupendwa na waume zao?
MWANAMKE mmoja alimwambia mwenzake kwa kunung’unika hivi, ‘Mimi najua mume wangu anipenda, lakini hajasema hivyo. Eeh, anasema pindi fulani nikimwuliza, lakini bila hivyo, anaona vigumu kusema.’
2 Yule mwanamke mwenzake alijibu hivi, ‘Najua. Hivyo ndivyo walivyo wanaume. Wakati mmoja nilimwuliza mume wangu kama anipenda, naye akasema, “Mimi nilikuoa wewe, sivyo? Ninakulisha na kukuvika, ninaishi pamoja nawe; singefanya hivyo ikiwa singekuwa nakupenda.”’
3 Alinyamaza kidogo, kisha akaendelea kusema: ‘Lakini, jioni ya jana kulitukia jambo lenye kuvuta sana mawazo. Mchana nilikuwa nikisafisha katika chumba chake cha kusomea, na ndani ya mmojawapo watoto wa meza (masanduku ya meza) yake niliona picha moja. Ni ile niliyokuwa nimemwonyesha katika kitabu changu cha zamani cha kuwekea picha za jamaa. Ilikuwa picha yangu nikiwa nimevaa mavazi ya kuogea wakati nilipokuwa mwenye umri wa miaka saba. Alikuwa ameiondoa katika kitabu cha kuwekea picha na kuitia katika kitoto cha meza (sanduku la meza) yake.’
4 Alipokumbuka hayo, mwanamke huyo alitabasamu (alichekelea), kisha akamtazama rafikiye. ‘Wakati mume wangu aliporudi nyumbani jioni hiyo kutoka kazini, nilimwonyesha picha hiyo. Aliichukua mkononi mwake, akatabasamu (akachekelea), akasema, “Nampenda sana msichana mdogo huyu.” Kisha akaiweka chini na kunishika uso wangu mikono yake miwili na kusema, “Napenda vilevile alivyogeuka kuwa.” Kisha akanibusu kwa upendo sana. Jambo hilo lilinitosha machozi.’
5. Ili apendwe sana na mume wake, inampasa mke ajiendeshe namna gani?
5 Mke anayejua kwamba anapendwa sana na mumewe anajiona kuchangamka na salama ndani yake. Neno la Mungu linawashauri waume wawapende hivyo wake zao: “Imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama milii yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. Maana hakuwa mtu anayeuchukia nawili wake po pote; bali huulisha na kuutunza, . . . hao wawili watakuwa mwili mmoja.” (Waefeso 5:28, 29, 31) Kama tulivyokwisha kuzungumza, inampasa mke amheshimu sana mume wake, lakini inampasa mume awe na mwenendo utakaomfanya ajipatie heshima hiyo. Hali iyo hiyo wakati mume wako anaposhauriwa akupende na kukutunza: Jiendeshe kwa njia itakayomfanya naye atende hivyo kwa moyo.
JE! UNAMWUNGA MKONO?
6, 7. (a) Katika Mwanzo 2:18, Yehova alisema kwamba alimfanya mwanamke atimize daraka gani? (b) Ili mke awe msaidizi kweli kweli wa mume wake, anatakiwa kufanya nini?
6 Ili mke naye apendwe kweli kweli, kuna mambo mengi yanayotakiwa kuliko kunyenyekea tu ukichwa wa mume wake. Kwani, ikiwa ni shauri la kunyenyekea tu, angeweza kuwa na farasi au mbwa aliyefundishwa vizuri amnyenyekee. Adamu alikuwa pamoja na wanyama katika bustani ya Edeni, nao walimnyenyekea. Hata hivyo alikuwa bado peke yake, kwa vile hakuwa na mwenzi wa aina yake. Alikuwa anahitaji mwanadamu mwenzake aliye na akili, ambaye angekuwa kikamilisho na msaidizi wa kufanya kazi naye: “Si vizuri mwanamume aendelee kuwa peke yake,” Yehova Mungu akasema. “Nitamfanyia msaidizi, awe kikamilisho chake.”—Mwanzo 2:18, NW.
7 Anachohitaji mume ni mke anayempenda, kumheshimu, na vilevile msaidizi wake kweli kweli, anayemwunga mkono katika maamuzi yake. Ikiwa wote wawili wanazungumza pamoja kisha kufanya maamuzi, hilo si jambo gumu. Lakini huenda lisiwe jepesi ikiwa hukuombwa shauri wala ikiwa hukubali maamuzi. Kwa hiyo, je! ungeweza kumwunga mkono mume wako kwa ushikamanifu—ukijitahidi kutimiza uamuzi wake, mradi uwe utendaji mzuri au unaopatana na maandiko? Au ungeelekea kukataa kwa ukaidi kumwunga mkono, ukitazamia ashindwe ili uweze kusema, ‘Unaona, si nilikuambia’? Akikuona unafanya kazi kwa bidii ili mpango huo ufanikiwe, ijapokuwa mashaka yako, je! wewe huoni kwamba atazidi kukupenda sana kwa sababu unamwunga mkono kwa ushikamanifu?
8. Mke anaweza kumtiaje moyo mume wake atumie ukichwa unaofaa?
8 Zaidi ya yote, usijaribu kunyakua ukichwa wake! Ukifanya hivyo, huwezi kumpenda; naye hawezi kukupenda wala kujipenda mwenyewe. Labda inaweza kuwa kwamba haongozi mambo kama inavyompasa aongoze. Unaweza kumtia moyo afanye hivyo? Je! unashukuru kwa bidii yake yo yote ya kuongoza? Je! unashirikiana naye na kumtia moyo anapoonyesha nia fulani ya kuongoza, au unamwambia kwamba amekosa, kwamba mpango wake haufai kitu? Mara nyingine mke anashiriki lawama ikiwa mume wake haongozi. Kwa mfano, ikiwa anadharau mawazo ya mume au kupinga jitihada zake, au mpango usipokamilika na kusema, Si nilikuambia haufai kitu? Mwishowe, jambo hilo linaweza kumfanya mume wako awe mwenye mashaka na mwenye kusitasita. Kwa upande mwingine, ushikamanifu wako na kumwunga mkono, kumtumaini na kuwa na hakika naye, kutamtia nguvu na kumsaidia afanikiwe.
“MKE MWEMA”
9. Mithali 31:10 inasema nini juu ya mke mwema?
9 Ili uwe mke anayependwa sana, inakupasa vilevile utimize vizuri madaraka yako ya nyumbani. Biblia inasema habari za mwanamke wa namna hiyo hivi: “Kima [bei] chake chapita kima cha marijani.” (Mithali 31:10) Je! wewe ni mke wa namna hiyo? Je! wataka kuwa hivyo?
10, 11. Mke anaweza kuonyeshaje kwamba anafaa kutajwa kama Mithali 31:15 inavyoeleza?
10 Kinapozungumza kazi za “mke mwema,” kitabu cha Mithali kinaarifu hivi: “Anaamka [wakati]ungali usiku, na kuwapa watu wa nyumba yake chakula.” (Mezali 31:15, ZSB) Wanawake wengi vijana wanaanza maisha ya ndoa wakiwa na kizuizi fulani kwa sababu mama zao hawakuwafundisha kupika; lakini wanaweza kujifunza. Naye mwanamke mwenye hekima atajifunza kupika vizuri! Kupika ni ufundi. Chakula kinapopikwa vizuri, hakishibishi tumbo tu, bali kinaufurahisha moyo vilevile.
11 Kuna mambo mengi ya kujifunza juu ya kupika chakula. Inafaa ujulishwe kanuni za chakula kinachofaa mwili ili uweze kulinda afya ya jamaa yako. Lakini kumpikia tu mume wako chakula chenye kufaa mwili hakutakupatia sifa yake. Biblia inatuambia kwamba Rebeka, mke wa Isaka, alijua kupika chakula “kitamu,” kwa namna aliyopenda mume wake. (Mwanzo 27:14) Wake wengi wangeweza kupata faida kutokana na mfano wake.
12. Ni mambo gani mengine ambayo mwanamke anaweza kufanya zaidi ya yale yanayotajwa katika Mithali 31:14?
12 Katika sehemu fulani za ulimwengu wanawake wanakwenda sokoni kila asubuhi wakanunue vitu wanavyohitaji siku hiyo. Mahali pengine, wananunua vitu labda mara moja kila juma na kuviweka vyakula vinavyoweza kuharibika katika mashine ya barafu (frigo au friji). Kwa vyo vyote, inampasa mume amshukuru mke anayetumia kwa uangalifu fedha za jamaa, na anayefuata mpango wa jamaa wa matumizi ya fedha. Akijifunza kujua namna ya chakula na mavazi ya aina bora, na kujua faida yake, nyakati zote atakuwa akichunguza kwanza kabla ya kununua kitu. Kama Mithali 31: 14 inavyosema: “Afanana na merikebu za biashara; huleta chakula chake kutoka mbali.”
13. Kulingana na Mithali 31:27, mke mwema anaweza kutazamiwa kufanya nini kwa habari ya utunzaji wa nyumba?
13 Vilevile, kama vile anavyopendezwa na kazi yake, ndivyo anavyopaswa apendezwe na hali ya nyumba yake. Katika kueleza zaidi kinachotambulisha mke kuwa mwema, Mithali 31:27 inasema hivi: “Huangalia sana njia za watu wa nyumbani mwake; wala hali chakula cha.uvivu.” Yeye hana mazoea ya kuchelewa kulala, akipoteza wakati mwingi mno katika kupiga porojo (kusema-sema) tu pamoja na jirani zake. Ijapokuwa huenda nyakati nyingine ugonjwa au hali zisizotazamiwa zikamchelewesha kufanya kazi yake ya nyumbani, kwa kawaida nyumba yake itakuwa yenye utaratibu mzuri na safi. Mume wake anaweza kuwa na hakika kwamba hataaibishwa (hatapata haya) na sura ya nyumba yao, ikiwa rafiki zao wanawatembelea.
14, 15. Biblia inawashauri wanawake nini juu ya mavazi na mapambo?
14 Wanawake wengi hawahitaji kuambiwa kwamba ni jambo la maana vilevile kuangalia sura yao, lakini wengine wanahitaji kukumbushwa. Si vyepesi kumpenda mke ambaye sura yake inaonyesha kwamba hajifikirii sana. Biblia inapendekeza kwamba wanawake “wajipambe kwa mavazi ya kujisitiri [yaliyotengenezwa vizuri] , pamoja na adabu nzuri, na moyo wa kiasi.” Lakini inashauri vilevile ikipinga kuhangaikia mno kusuka nywele, vitu vya dhahabu na mavazi ya bei kubwa yanayovuta macho ya watu juu ya mwenye kuyavaa kwa njia isiyofaa.—1 Timotheo 2:9.
15 Iliyo bora sana kuliko mavazi hayo ni nia ya mtu aliye nayo. Mtume Petro anawaambia wake Wakristo kwamba “roho ya upole na utulivu, [ni] ya thamani kuu mbele za Mungu.” (1 Petro 3:3, 4) Nayo Mithali, inapozitaja tabia za mke mwema, inaongeza kwamba “huwakunjulia maskini mikono yake” na kwamba “sheria ya wema i katika ulimi wake.” Si mwenye choyo wala mkorofi (mwenye kudhulumu), bali ni mkarimu na mwenye fadhili. (Mithali 31:20, 26) “Upendeleo hudanganya,” masimulizi yanaendelea, “na uzuri ni ubatili; bali mwanamke amchaye [Yehova], ndiye atakayesifiwa.”—Mithali 31:30.
16. Mume anayethamini atamwonaje mke huyo?
16 Ndiyo, mwanamke huyo atapendwa sana na mume ye yote anayeshiriki maoni ya Muumba. Atamwona mke wake kama mwandikaji wa Mithali alivyosema: “Binti za watu wengi wamefanya mema, lakini wewe umewapita wote.” (Mithali 31:28, 29) Yeye mwenyewe atamjulisha mke wake maoni hayo, bila kuulizwa na mtu.
MAONI YAKO JUU YA NGONO YANATOFAUTISHA
17, 18. Maoni ya mke juu ya ngono yanaweza kumfanya mume awe na maoni gani juu ya mke wake?
17 Mojawapo ya sababu zinazoleta magumu mengi katika ndoa ni ngono zisizofurahisha. Mara nyingine hayo yanatokea kwa sababu mume hafikirii na kufahamu mahitaji ya mwili na ya moyoni ya mke wake, na nyakati nyingine ni kwa vile mke hataki kushiriki ngono pamoja na mume wake wala kumfurahisha. Ikiwa mume na mke wanashiriki ngono pamoja kwa kupenda na kwa furaha, bila shaka tendo hilo litakuwa wonyeshano wa upendo wa kila mtu na mwenzake.
18 Huenda ubaridi wa mke unatokea kwa sababu ya kutofikiriwa na mume wake. Lakini ubaridi wa mke vilevile unamwumiza mume wake, na huenda kutopenda kwa mke kufanya ngono kukaharibu uwezo wa mume wake au hata kumfanya aanze kupendezwa na mwanamke mwingine. Mke akikubali vivi hivi tu, akiwa na maoni ya kutojali, huenda mume akadhani kwamba hilo linaonyesha kwamba mke wake hamjali. Maono ya moyoni yanaongoza wepesi wa kutaka au kutotaka kufanya ngono, na mke akiwa na ubaridi huo labda itampasa achunguze tena maoni yake mwenyewe juu ya ngono.
19. (a) Biblia inaonyeshaje kwamba lingekuwa kosa kumnyima mwenzi wa ndoa ngono kwa muda mrefu? (b) Sababu gani haingekuwa lazima kuuliza watu wasio wenzi wa ndoa, watoe amri juu ya kufaa au kutofaa kwa mwenendo wa mume na mke katika mambo ya ngono?
19 Biblia inashauri mume na mke wasiwe ‘wakinyimana.’ Neno la Mungu haliruhusu kutumia ngono kuwa njia ya kumwadhibia mwenzi wa ndoa au kuwa njia ya kuonyeshea chuki, kama vile mke kumnyima mumewe ngono muda wa juma nyingi au hata miezi mingi. Kama vile mume anavyopaswa “ampe mkewe haki yake, na vivyo hivyo mke na ampe mumewe haki yake.” (1 Wakorintho 7:3-5) Hiyo haina maana kwamba imempasa mke atazamiwe kukubalia tendo fulani lisilo la kawaida ambalo anaona kuwa lenye kuchukiza sana na si jema. Na mume anayempenda na kumheshimu mke wake hangemtaka afanye hivyo. “Upendo ... haukosi kuwa na adabu.” (1 Wakorintho 13:4, 5) Haingekuwa lazima kumwomba mtu asiye mwenzi wa ndoa atoe amri juu ya kufaa au kutofaa kwa mwenendo wa mume na mke. Katika 1 Wakorintho 6:9-11, Biblia inataja mazoea moja moja ambayo waabudu. wa Yehova Mungu wanakatazwa kufuata: uasherati, uzinzi, tendo la wanaume kulalana wao kwa wao na wanawake kwa wanawake. (Linganisha vilevile Mambo ya Walawi 18:1-23.) Watu wengine wa kisasa wanaotetea haki za kibinafsi na wenye kufuata “adili mpya”—uasherati hakika—wanadai kwamba inafaa uasherati mwingine kati ya huo ukubaliwe, lakini wengine wasiotaka mageuzi ya tabia wangependa kuongezea makatazo hayo. Biblia inatoa maoni yaliyosawazika. Kwa jumla, ikiwa uhusiano mwingine wote katika ndoa ni mzuri, ikiwa kuna upendo, heshima, kupashana habari vizuri na kufahamiana, ngono haitakuwa jambo gumu mara nyingi.
20. Ikiwa mke anatumia ngono kwa makusudi ya kubadilishana vitu, matokeo yanakuwa nini?
20 Mke anayependwa sana hatumii ngono kwa makusudi ya kubadilishana kitu kingine. Bila shaka si wake wote wanaobadilishana vitu kwa ngono, lakini wengine wanafanya hivyo. Wanatumia ngono katika njia ambazo huenda zikawa za werevu ili wapate ruhusa za waume zao wafanye mambo fulani. Matokeo ni nini? Basi, je! unamwonea shauku mtu anayekuuzia vazi? Wala mume hamwonei shauku mke anayebadilishana ngono na mume wake ili aruhusiwe kufanya mambo fulani. Labda mwanamke anayefanya hivyo anaweza kupata faida za kimwili, lakini anakosa upendo na mambo ya kiroho.
WALIAJI, WENYE CHOKOCHOKO (KUSUMBUA-SUMBUA)
21-23. Kama inavyoonyeshwa na habari ya Samsoni, kulia na uchokochoko (kusumbua) kunaweza kuharibuje furaha?
21 Samsoni alikuwa mwanamume mwenye nguvu, lakini hakuweza kuvumilia mkazo wa wanawake waliozoea kulia au kwa kusumbua sana ili wapate walichokuwa wakitaka. Pindi moja alisumbuliwa na mwanamke ambaye alitazamia awe mke wake, ambaye aliendelea kulia-lia bila mwisho. Kama ilivyoandikwa katika Waamuzi 14:16, 17, mwanamke huyo “akalia mbele yake, akasema, Wewe wanichukia tu, wala hunipendi; wewe umewategea kitendawili hao wana wa watu wangu, nawe hukuniambia mimi. Naye akamwambia, Angalia, sikumwambla baba yangu wala mama yangu, nami nikuamble wewe?” Sababu nzuri za Samsoni hazikufaa kitu. Hazifai kitu mara nyingi wakati moyo unapohangaika sana. “Naye akalia mbele yake hizo siku saba, wakati ulioendelea karamu yao; basi ikawa siku ya saba akamwambia, kwa sababu alikuwa akimsisitiza sana; naye akawaambia wale wana wa watu wake hicho kitendawili.”
22 Usidhani kwamba mume wako hakupendi kwa sababu tu hakupi nyakati zote ruhusa ya kufuata njia yako mwenyewe. Yule aliyetazamiwa kuwa mke wa Samsoni alimlaumu kuwa hampendi, lakini kwa kweli yeye ndiye aliyekuwa hampendi Samsoni. Alimkaza sana hata ikawa hawezi kuvumilia tena. Wakati Samsoni alipomwambia kitendawili hicho, upesi mwanamke huyo hakuficha siri yake, bali alikimbia kwenda kuwaambia adui za Samsoni siri yake. Mwishowe, akawa mke wa mwanamume mwingine.
23 Wakati uliofuata, Samsoni akampenda mwanamke mwingine, jina lake Delila. Labda alikuwa mwenye umbo (sura) lenye kuvutia, lakini je! alionekana kuwa mwanamke ambaye Samsoni angeweza kupenda sana? Ili apate kwa njia ya ubembelezi habari ambayo angeweza kutumia kwa faida ya kichoyo, Delila alitumia njia ya uchokochoko (kusumbua-sumbua). Habari inasema hivi: “Ikawa, kwa vile alivyomsumbua kwa maneno yake kila siku, na kumwudhi, roho yake ikadhikika hata kula.” Matokeo ya mwisho yalikuwa mabaya sana.—Waamuzi 16:16.
24-27. (a) Kitabu cha Mithali kinasema nini juu ya matokeo ya chokochoko ya mke? (b) Sababu gani kinashauri wanawake peke yao hivyo? (c) Ni jambo gani linaloelekea kuwa laweza kumwongoza mume atake kumtendea mke wake mambo mazuri?
24 Kulia-lia na chokochoko (kusumbua-sumbua) hakufai. Kunaharibu ndoa. Kunatenga mume. Biblia inaonya juu ya mazoea hayo, kama vile katika maandiko yanayofuata, yanayotokana na The New English Bible ya Kiingereza: “Mwenye kurudia-rudia neno lile lile anavunja urafiki.” “Mke mwenye chokochoko anafanana na maji yanayochururika bila mwisho.” “Bora kuishi peke yako jangwani kuliko na mke mwenye chokochoko na mkorofi.” “Kuchururika kusiko na mwisho siku ya mvua—ndivyo alivyo mke mwenye choko-choko. Kumzuia huyo ni kama kujaribu kuuzuia upepo! Ni kama mtu anayejaribu kuokota mafuta katika vidole vyake!”—Mithali 17:9; 19:13; 21:19; 27:15, 16.
25 Sababu gani Maandiko yanamshauri hivyo mke peke yake? Labda ni kwa sababu kwa kawaida wanawake ni wepesi na wenye kuelekea zaidi kuvutwa na maono ya moyoni, sana sana wanapoudhika juu ya jambo fulani. Huenda vilevile wakaona kwamba hiyo ndiyo silaha peke yake wanayoweza kutumia. Huenda mume kama kichwa cha nyumba akaamua mambo kwa njia yake mwenyewe bila sababu nzuri, hivyo labda mke anaweza kuona kwamba inampasa atumie njia ya kuhangaisha moyo. Haikupasi wewe mke utumie njia hizo, naye mume wako hapaswi akufanye ulazimike kutenda hivyo.
26 Ni kweli kwamba huenda zikawako nyakati ambapo hujisikii vizuri, labda unajiona unaanza kulia, hata usipotaka. Lakini hiyo ni tofauti sana na kufanya matata na kukasirika ili upate ruhusa ya kufanya kama unavyotaka.
27 Ikiwa wanawapenda sana wake zao, waume wengi watataka wawapendeze kuliko kujipendeza wenyewe, wakati kunapokuwa na mambo ambayo mtu binafsi anapendelea kuliko mengine. Mpendeze mume wako, naye bila shaka atatafuta nafasi za kukupendeza wewe.
“WAKATI WA KUNYAMAZA, NA WAKATI WA KUNENA”
28-35. (a) Ebu eleza mazoea ya kuongea yanayofanya iwe vigumu kwa mume kuongea na mke wake. (b) Ni Jambo gani linaloweza kufanywa ili maongezi kati ya mume na mke yawe bora?
28 Wake wengi wananung’unika wakisema, ‘Mume wangu haongei nami hata kidogo.’ Labda yeye ndiye mwenye lawama. Lakini, mara nyingi mume anataka kuongea na mke wake, lakini mke anafanya iwe vigumu mume aongee naye. Kwa njia gani? Wanawake wote hawafanani. Lakini jiulize mwenyewe uone kama unafanana na mmojawapo wa wanawake hawa:
29 Mwanamke wa kwanza hana taabu hata kidogo ya kuongea na wanawake wenzake mtaani. Lakini yeye anaongea namna gani? Mwanamke mwenzake anapotua (anaposimama) kidogo ili avute pumzi, anamkata kauli (anamkatiza maneno). Huenda akauliza maulizo mawili matatu hivi, au akaacha na kuanza kuzungumza jambo ambalo ni tofauti kabisa. Upesi yule aliyekatizwa anajiingiza na kuendelea na mazungumzo yake kwa muda fulani. Hakuna mmojawapo anayeonekana kuwa anajali mashindano hayo ya maneno.
30 Sasa mume wake anarudi nyumbani, naye ana habari za kumwambia mkewe. Anapoingia mlangoni, anaanza kwa kusema, ‘Lo! unajua yaliyotendeka kazini . . . .’ Haendelei kuzidi hapo. Mke anamkatiza, akiuliza hivi, ‘Ulipata wapi doa hilo katika koti (vazi) lako? Angalia sawa sawa mahali unapotembea. Sasa hivi nimesafisha sakafu.’ Huenda mume akasita kuendelea na habari yake tena.
31 Au, labda wanaongea na rafiki zao naye mume anaeleza yaliyotokea, lakini anaacha mambo fulani au hayaelezi yote sawasawa. Mke wake anamkatiza, amwonye makosa kwanza, kisha anasawazisha habari hiyo. Muda si muda mume anatweta (anavuta pumzi) na kusema, ‘Sababu gani usisimulie yote?’
32 Mwanamke mwingine ni yule anayemtia moyo mume wake kuongea. Akijaribu kuwa kama anafanya tu mchezo, lakini kwa utafiti (kwa uchunguzi), anauliza hivi: ‘Ulikuwa wapi?’ ‘Nani aliyekuwako?’ ‘Kulikuwa nini?’ Yeye hapendezwi na mambo ya kawaida ya maisha, bali na yale yanayoonekana kuwa yenye siri zaidi. Anaunganisha pamoja visehemu vya habari ambavyo anaweza kukusanya-kusanya, kisha anawazia jambo fulani. Labda sehemu ya habari hiyo ni ile ambayo mume wake hangalitaka ifunuliwe. Labda mambo mengine yangalifaa yazungumzwe pamoja na mke wake, lakini yalisemwa kwa siri. Ikiwa, sasa mke huyo anazungumza habari hiyo kwa wengine, siri hiyo imefunuliwa. “Usifunue siri ya mtu mwingine,” Mithali 25:9 inaonya. Lakini ikiwa angefanya hivyo, labda ingeleta matata. Mume wake ataonaje uhuru wa kuzungumza naye wakati ujao?
33 Hata hivyo mwanamke wa namna ya tatu si msemaji sana. Yeye anajua kufanya kazi inayotakiwa nyumbani, lakini hasemi sana. Ye yote anayejaribu kuongea naye atakuwa wakati wote akizungumza peke yake. Labda huyo ni mke mwenye haya, au labda hakuwa na nafasi nyingi ya kupata elimu alipokuwa mtoto. Hata iwe sababbu gani, ni kazi bure kujaribu kuongea naye.
34 Lakini mageuzo yanaweza kufanywa. Mtu anaweza kujifunza kuwa mwenye kujua sana kuongea. Ikiwa mwanamke anasoma vilevile mambo yanayofaa na kuwafanyia watu wengine matendo ya fadhili zaidi ya kazi yake ya nyumbani, atakuwa na mambo yenye kujenga ashiriki pamoja na mume wake. Nayo maongezi yenye faida yanataka mtu ayashiriki pamoja na mwenzake. Vilevile yanataka heshima—heshima ya kutosha kumruhusu mume amalize anayosema, kumruhusu ayaseme katika njia yake mwenyewe, na kujua wakati kunapokuwa na siri ya kuficha. Kama Mhubiri 3:7 asemavyo, kuna “wakati wa kunyamaza, na wakati wa kunena.”
35 Kwa hiyo, mahali pa kunung’unika kwamba mume wako hasemi sana nawe, sababu gani usijaribu kumfanyia iwe vyepesi kusema nawe? Pendezwa na vitu anavyofanya. Msikilize sana anaposema. Acha kuitika kwako kuonyeshe kwamba unampenda kwa uchangamfu na kumheshimu sana. Hakikisha kwamba mambo unayosema sana ni yenye kufaa na yenye kujenga. Labda upesi utaona kwamba maongezi yanawafurahisha ninyi wawili.
‘WAVUTWE PASIPO NENO’
36-38. Ni njia gani chache zinazoweza kutumiwa ili kuufikia moyo wa mwenzi wa ndoa asiyeamini?
36 Mara nyingine, matendo yana nguvu kuliko maneno, sana sana kwa habari ya waume ambao si waamini wenzetu wa Neno la Mungu. Mtume Petro alisema kwa habari yao hivi: “Wavutwe kwa mwenendo wa wake zao, pasipo lile Neno; wakitazama mwenendo wenu safi, na wa [heshima nyingi].” (1 Petro 3:1, 2) Waume wengi wasioamini wamelalamika wakisema kwamba wake zao ‘wanawahubiri’ nyakati zote, nao wanachukia sana hilo. Tofauti na hayo, wengine wameamini kwa kuona namna kweli ya Neno la Mungu imewageuza wake zao. Mara nyingi watu wanavutwa sana kwa kuona matendo kuliko kusikia maneno matupu ya mtu.
37 Unaposema na mwenzi wako asiyeamini, ‘maneno yako na yawe na neema sikuzote,’ yawe yenye kupendeza, au “yakikolea munyu” (chumvi), kama andiko linavyosema. Kuna wakati wa kusema. “Neno linenwalo wakati wa kufaa, ni kama machungwa katika vyano vya fedha,” Biblia inasema. Je! mume wako amevunjika moyo kwa sababbu ya jambo fulani? Labda mambo hayakuwa mazuri kazini kwake. Wakati huo ndipo maneno machache ya ufahamu yangeonwa kuwa ya maana sana. “Maneno yapendezayo . . . ni tamu nafsini na afya mifupani.” (Wakolosai 4:6; Mithali 25:11; 16: 24) Au, ikitegemea hali ilivyo, kumshika tu mkono wake kwaweza kuwa na maana kama unamwambia hivi: Nimefahamu, niko upande wako, nitasaidia nikiweza.
38 Hata ajapokuwa si pamoja na wewe katika imani yako, Neno la Mungu linaonyesha kwamba bado inakupasa umtii. Huenda mwishowe mwenendo wako ukamvuta ashiriki imani yako. Lo! hiyo ingekuwa siku yenye furaha kama nini! Na wakati huo utakapofika, atajua kwamba anazo sababu nyingi za kukupenda wewe kuliko alivyojua hapo zamani. Kwa sababu kujitoa kwako pamoja na imara yako kwa ajili ya kile unachojua kuwa ni sawa, kutakuwa kumemsaidia aushike “uzima ulio kweli kweli.”—1 Wakorinto 7:13-16; 1 Timotheo 6:19.
39, 40. Ni sifa gani zinazotajwa katika Tito 2:4, 5, zinazomfanya mke kuwa mwenye thamani, si kwa mume wake tu, bali kwa Yehova vilevile?
39 Kwamba waume wao ni watu walioamini ama wasioamini, Maandiko yanawatia moyo wake Wakristo “wawapende waume zao, na kuwapenda watoto wao; na kuwa wenye kiasi, kuwa safi, kufanya kazi nyumbani mwao, kuwa wema, kuwatii waume zao wenyewe; ili neno la Mungu lisitukanwe.”—Tito 2:4, 5.
40 Ikiwa wewe, mke, unafanya hivyo kwa kadiri ya uwezo wako, utapendwa sana, si na mume wako tu, bali na Yehova Mungu vilevile.
[Picha katika ukurasa wa 57]
“Mke mwema . . . kima chake chapita cha marijani.”—Mithali 31:10.
[Picha katika ukurasa wa 64]
Wanawake wakati wa maisha ya Samsoni