Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 11/1 kur. 11-16
  • Ninyi Waume, Onyesheni Upendo wa Kujinyima

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ninyi Waume, Onyesheni Upendo wa Kujinyima
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Pendeni Kama Kristo Alivyopenda Kundi
  • Wa Hali ya Chini Katika Moyo
  • Kionyeshe Heshima Kile “Chombo Kisicho na Nguvu”
  • “Haki” ya Mke
  • Kujinyima Kunaugusa Moyo
  • Msaada Kutoka Juu
  • Mume Anayejipatia Heshima Nyingi
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Kutimiza Fungu Letu la Kuendeleza Maisha Yenye Furaha ya Jamaa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Funguo Mbili za Kuwa na Ndoa Yenye Kudumu
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Mwongozo Wenye Hekima kwa Wenzi wa Ndoa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 11/1 kur. 11-16

Ninyi Waume, Onyesheni Upendo wa Kujinyima

“Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda kanisa, akajitoa kwa ajili yake.”​—WAEFESO 5:25.

1. Kwa sababu gani ukichwa wa Kikristo unadai mtu mambo mengi na kuthawabisha?

“NDOA! Hakuna jambo linalomdai mwanamume mambo mengi kama ndoa!” Ndivyo alivyoandika Ibsen mtunga mashairi wa Norway. Huenda ukakubaliana kabisa na maneno hayo kwa sababu ya ile kanuni ya Biblia ya ukichwa. Hata hivyo, wakati ukichwa wa Kikristo unapotumiwa inavyofaa unaweza pia kuleta maisha ya kinyumbani ya kupendana na kuheshimiana nyakati zote, hata moyo wako upate starehe. Lakini, cheo ulichowekewa na Mungu cha kuwa kichwa kinafuatana na daraka kubwa la kumtolea Mungu jibu kwa mambo unayotenda.​—Luka 12:48.

2. Je! ni Juu ya mume peke yake kufanya jitihada za kuleta furaha katika Jamaa?

2 Je! hiyo maana yake ni kwamba wewe mume ndiwe peke yako uliye na daraka la kuleta furaha katika nyumba yako? Hapana, nyote wawili, wewe na mkeo, ni lazima mjaribu kuiletea maendeleo hali iliyoko. (Mithali 14:1) Kwa sababu mengi ya mambo yatakayosemwa sasa yanahusu mume, hiyo haimaanishi kwamba wake wamewazidi waume kidogo kwa ukamilifu. Lakini mambo yenyewe yamekusudiwa yasaidie waume watimize mambo wanayodaiwa na ukichwa wa Kikristo. Ukichwa huo unapasa kutumiwaje hasa? Hilo ni jambo linalohitaji kufahamiwa na Wakristo wote, hata wale ambao hawajaoa au kuolewa.

Pendeni Kama Kristo Alivyopenda Kundi

3. Andiko la Waefeso 5:25 linauelezaje ukichwa unaofaa, na hiyo ina maana gani?

3 “Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake,” ndivyo alivyoandika mtume Paulo. (Waefeso 5:25) Kwa kuwa waume wana haki ya Kimaandiko ya kufanya maamuzi ya mwisho katika jamaa, ni jambo jepesi kwako wewe kuruhusu uchoyo uingie. Ni jambo la wazi kwamba mengi ya maamuzi ya kijamaa yanafanywa hasa kulingana na mapendezi ya mtu binafsi. Je! mapendezi yako mwenyewe ndiyo yanayotawala ikiwa hakuna kanuni ya Biblia inayohusika katika jambo? Angalia kwamba ni lazima mume aige upendo wa Yesu wa kujinyima. Yeye alijitoa mwenyewe kwa ajili ya wanafunzi wake. ‘Kristo hakujipendeza mwenyewe.’ (Warumi 15:3) Kujinyima maana yake ni kuacha jambo fulani la raha au kupita katika matatizo au hali isiyofaa kwa faida ya mtu mwingine.

4. Yesu alionyeshaje hangaiko lake kwa wanafunzi wake?

4 Upendezi uliokuwa ukiwaka ndani ya Yesu ulikuwa kusaidia wanafunzi wake kiroho. Ingawa yeye alitetea uadilifu kwa imara, hakuwa kamwe mkali-mkali wakati wanafunzi wake walipoonyesha maoni mabaya, au walipokuwa na kiburi, waliposhtukia kufanya mambo bila kufikiri au walipokuwa waoga-waoga. (Mathayo 18:1-3; Luka 22:24-26, 47-51, 59-62) ‘Kupitia Neno la Mungu,’ na kwa mfano wake, yeye alisaidia wanafunzi wake wakashinda udhaifu mzito wa namna mbalimbali ili wao, kwa ujumla, wawe ‘watakatifu na bila mawaa.’​—Waefeso 5:26, 27.

5, 6. Mume anaweza kuuigaje upendo wa Yesu wa kujinyima, na ni wakati gani hasa Jambo hilo linapokuwa gumu?

5 Je! wewe unaonyesha upendo huo wa kujinyima? Wanaume wengine wana maoni ya kwamba wakiwapa wake zao vitu vya kimwili, hiyo imetosha. Ni kweli kwamba kazi ya kutafuta vitu hivyo ni ngumu na inapasa kuthaminiwa sana sana. Hata hivyo jambo kuu katika mfano aliouweka Yesu ni jitihada yake ya kutokuchoka aache kutunza mahitaji ya kiroho na ya kimoyoni ya wanafunzi wake, si mahitaji yao ya kimwili tu. Ni jambo lenye kueleweka vizuri kwamba wanaume wengi hawawezi kutaka wasumbuliwe akili nyumbani baada ya kupatwa na mahangaikio mengi ya ulimwengu wakitafutia jamaa zao vitu vya kimwili. Ingawa nia hiyo inaonyeshwa sana katika jamaa zisizojaribu kuifuata Biblia, ni jambo la kusikitisha kwa sababu hata mke mmoja Mkristo alitoa wazi maoni yake ya moyoni: “Mume wangu hakunipa mwelekezo wo wote. Ziko nyakati nilipommwagia mambo yangu yote ya moyoni ili nipate mwongozo juu ya mambo fulani, lakini akili zake zilikuwa zikijishughulisha na mambo tofauti.”

6 Upendo wa kujinyima ndilo jawabu. Ikiwa mkeo ana tatizo lenye kumvuruga akili, upendo huo utakusukuma uzungumze naye kwa subira ukimtolea sababu za kumfanya afikirie mambo vizuri badala ya kumwambia aende zake kwa maneno au uso mbaya. Wewe utahangaikia sana hali ya kiroho yake, kujifunza Biblia na kushiriki pamoja naye katika utumishi mtakatifu. Utaepuka kumwacha ajifanyie maamuzi mazito ambayo kwa haki Wewe ndiwe unayepaswa kuyafanya. Pia utahakikisha kwamba anapata nafasi ya kustarehe na kupumzika kidogo. (Marko 6:31) Kuchukua hatua kwa njia hiyo bila ya kuambiwa-ambiwa kunafanya mke ajiheshimu na kujisikia ana usalama wa kweli.

Wa Hali ya Chini Katika Moyo

7. Ili kutumia ukichwa wenye usawaziko, ni sifa gani inayohitajiwa?

7 Mara nyingi, wanaume wanatatizwa kupata usawaziko katika kutumia ukichwa. Nyakati nyingine wengine wao wanajisikia kwamba mke anataka kuchukua cheo chao hata ikiwa yeye ametoa maoni ya kufanya jambo fulani tu au ikiwa ametoa lawama kidogo. Yesu, yule mfano bora kwa vichwa vya Kikristo, alisema: “Mimi ni mpole wa hasira na wa hali ya chini katika moyo.” (Mathayo 11:29, NW) Unyenyekevu wake haukuonyeshwa kijuujuu tu, kisha ukapotelea mbali wakati maoni ya mwingine yalipotofautiana na yake.

8, 9. (a) Sara alimlaumia Abrahamu jambo gani, na kwa sababu gani? (b) Kwa sababu gani Abrahamu hakudharau Sara wala kumjibu akiwa mkali-mkali?

8 Abrahamu pia alikuwa mfano mwema wa unyenyekevu. Sara, mke wake, alitendwa madharau na Hajiri msichana wake mtumwa. Ama Abrahamu hakuliona tendo hilo la kiburi ama hakuchukua hatua ya haraka. “Ubaya ulionipata na uwe juu yako,” akasema Sara. “Nimekupa mjakazi wangu kifuani mwako, naye alipoona kwamba amepata mimba, mimi nimekuwa duni machoni pake. [Yehova] na ahukumu kati ya mimi na wewe.”​—Mwanzo 16:5.

9 He! yalikuwa maneno ya kuumiza moyo kama nini! Hiyo ni kwa sababu Abrahamu alimpenda sana Sara naye hangetaka Sara audhike moyoni. Ingawa labda Sara alikuwa na sababu ya kumlaumu Abrahamu kwa udhia uliompata, huenda ikawa yeye alipita kiasi katika tendo lake, kwa maana hata aliomba msaada wa Mungu kama kwamba Abrahamu hangetenda lililo haki. Sasa, je! Abrahamu alimfyatukia kwa maneno ya kutetea ukichwa wake? Je! alimfikiria Sara kuwa mwanamke asiye mtiifu? Yeye alijua kwamba Sara alikuwa ameacha makao yenye starehe katika Uru na kwa muda unaozidi miaka 10 alikuwa amekaa katika mahema akiuitikia mwongozo wa Mungu. Huo ulikuwa utii! Sara alipata kupendwa sana na Abrahamu kwa sababu alikuwa akimwunga mkono kwa utiifu na bila uchoyo. (1 Petro 3:5, 6) Abrahamu alitoa jibu la upole akasema, “Tazama, mjakazi wako yu mkononi mwako, mtendee lililo jema machoni pako.” (Mwanzo 16:6) Abrahamu alikuwa na moyo wa kujishusha. Mwanamume kweli kweli!

10. (a) Mume anaweza kuigaje Abrahamu? (b) Je! utafanikiwa sikuzote?

10 Mke wako akikulaumu wewe kwa tatizo fulani, jaribu kutenda kama Abrahamu. Si vyepesi kutenda hivyo nyakati zote. Kuna nyakati ambazo utapungukiwa. Lakini sikiliza, jaribu kuelewa na kukadiri ubora wa maneno anayokuambia mkeo. Nyakati nyingine huenda mke akashindwa kusema maneno yale yanayofaa kwa sababu ya kutupa hasira yake nje bila kufikiri. Huenda akatenda kwa njia ya kupita kiasi kama Sara. Wewe jaribu kuona ni njia gani inaweza kutumiwa mkamilishe jambo hilo.

11. Kwa sababu gani haipasi mume amwone mke wake kuwa mtu ovyo tu?

11 Ni kweli kwamba mume anaweza kuwekea watu wa nyumba yake sheria mbalimbali. (Warumi 7:2) Lakini mke wako si mtoto wala si mtu ovyo tu. Yehova alisema, “Nitamfanyia [mwanamume] msaidizi, awe kikamilisho chake [kwa uhalisi, “mwenye kuwa kama yeye”] (Mwanzo 2:18, NW) Hawa angekuwa na akili zinazolingana na za Adamu. Angefanana naye, aweze kweli kweli kumsaidia kutimiza mgawo aliopewa na Mungu.

12. (a) Ni jambo gani lililotimizwa wakati mume mmoja alipokuza unyenyekevu wa moyoni? (b) Unyenyekevu unasaidiaje kuleta furaha katika ndoa?

12 Yule mke hodari ambaye habari zake zimeelezwa katika Mithali 31 alitumainiwa na mume wake. Yeye alinunua shamba; hata akapanda mizabibu “kwa mapato ya mikono yake”​—hiyo si kazi nyepesi! Je! mume wake aliona uchungu, akawa na maoni ya kwamba anataka kunyang’anywa ukichwa wake? Hapana, bali alimsifu mke wake! (Mistari 10, 11, 16, 28) Kuwa na nia kama hiyo kunaweza kukusaidia wewe uepuke mabishano mengi ya bure. Kwa mfano, mume mmoja na mke wake walikuwa kazi yao ni kushinda wakibishana tu. Mume alikubali kwamba ukichwa wake ulikuwa wa kutumia ‘ubwanamkubwa.’ Alipojichunguza kwa sala alimeza kiburi hicho kisichofaa. Akaanza kukadiri ubora wa mapendekezo ya mke wake. Mwishowe hata alimruhusu atunze mengine ya mambo yanayohusu pesa. Sasa mume huyo anasema: “Mke wangu anafanya mambo vizuri sana!” Naye mke anaongezea hivi: “Nililotaka ni kutumainiwa tu. Mtu anajisikia vizuri moyoni akijua kwamba mume wake anamwamini.” Hivyo Mithali 13:10 inatuonya hivi: “Kwa kujitanguliza mtu anasababisha mng’ang’ano tu, lakini kwa wale wanaoshauriana mambo pamoja kuna hekima.” (NW) Mume mwenye unyenyekevu katika cheo chake, anayejua anapungukiwa katika mambo fulani, anafurahia ujuzi mbalimbali wa mke wake. Kwa njia hiyo anajionyesha kuwa ni mnyenyekevu moyoni.​—Mithali 11:2.

Kionyeshe Heshima Kile “Chombo Kisicho na Nguvu”

13. (a) Barua ya Kwanza ya Petro, sura ya 3, mstari wa 7, inaonyesha ni lazima mume afanye nini? (b) Ni uhitaji gani wa moyoni unaofanya mke awe “chombo kisicho na nguvu”?

13 Mtume Petro aliandika akasema, “Ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu.” (1 Petro 3:7) Ni lazima ujue maumbile ya maoni ya moyoni ya mke wako, kwa sababu hayo ndiyo hasa yanayofanya aonwe kuwa chombo kisicho na nguvu. Ni lazima mke ajisikie kwamba yeye anapendwa na kuthaminiwa sana na mume wake. Bila ya kuchukua hatua hiyo moja mke atajisikia hafai sana, hata awe ana vitu vingapi vya kimwili. Ni lazima asadikishwe kwamba mume wake ana maoni kama yale ya mume wa kale aliyemwambia mke wake hivi: “Binti za watu wengi wamefanya mema, lakini wewe umewapita wote.”​—Mithali 31:28, 29.

14. Ni nini kinachofanya mwanamke ajisikie moyoni kwamba ana usalama?

14 Huenda wanaume fulani wakawa na wazo la kusema, ‘Inampasa mke wangu awe anajua kwamba nampenda. Kwani si mimi niliyemwoa?’ Lakini, wanawake wanafurahi zaidi wanapopata shauku ya upendo wenye kuonyeshwa kwa maneno. Isaka yule mwanamume mwaminifu aliujua sana uhitaji huo. Baada ya kukaa miaka 35 akiwa ameoa, bado alikuwa akimwonyesha mke wake shauku ya upendo (Mwanzo 26:8) Hata wewe fanya hivyo. Kwa kuelekeza fikira zako kwake, acha ajue kwamba moyo wako uko pamoja naye kwamba kulingana na maoni yako ‘yeye amewapita wanawake wote.’

15. Ili waume waelekeze fikira zao kwa wake zao, ni lazima wajihadhari na nini, na kwa sababu gani hilo ni jambo la maana sana?

15 Ili kuweka fikira zako juu ya mke kwa njia hiyo, unahitaji wakati na fikira. Waume wengine wanaona ni vyepesi zaidi kuelekeza fikira zao kwa mtu fulani ambaye hawajazoeana sana na anayeelekea kuwa mwenye kusisimua. Jambo hilo lilitukia katika Israeli wakati wa Malaki. Yehova aliwaambia hivi wanaume hao waliokuwa wakifikiria kujifaidi wenyewe tu kwa kuwatenda wake zao hila: “Jihadharini roho zenu.” (Malaki 2:13-16) Ndiyo, walihitajiwa kujihadhari na vile walivyokuwa wakijisikia kwa ndani. Hata sisi ni lazima tujihadhari, kwa sababu labda tunafanya kazi pamoja na wanawake wengine au tunaishi karibu nao. Unahitajiwa ufanye jitihada na kujitia adabu ili kuzuia majivuno, hali ya kuchoshwa na mambo yenu au utafiti usigeuze roho yako, maoni yako ya ndani, kuelekea mke wako.​—Mathayo 5:27-30.

“Haki” ya Mke

16. Ni eneo gani la ndoa lililo na matatizo mengi, na kutokuwa na uchoyo kumeonyeshwaje kwenye 1 Wakorintho 7:3, 4?

16 Kujinyima kwako kunahitajiwa sana hasa kuhusiana na ile “haki” ya ndoa. “Mume na ampe mkewe haki yake, na vivyo hivyo mke na ampe mumewe haki yake. Mke hana amri juu ya mwili wake, bali mumewe; vivyo hivyo mume hana amri juu ya mwili wake, bali mkewe.” (1 Wakorintho 7:3, 4) Kuna matatizo chungu zima katika uhusiano huu wenye mambo. Uchunguzi fulani-fulani wa matukio umeonyesha kwamba nusu moja ya watu wote waliooana wanapatwa na tatizo zito la ngono wakati fulani wa ndoa yao.

17. (a) Ni nini kinachopasa kutiwa ndani ya kumlipa mke haki yake ya mambo ya ndoa? (b) Mchunguzi mmoja alielezaje mahitaji ya mke?

17 Waume wengi wanafikiri mara nyingi Kwamba mahitaji ya wake zao au ‘‘haki” ya ngono ya wake zao iko sawa na ile yao wenyewe. Lakini Paulo alionyesha kwamba si “haki” zote zinazofanana alipokuwa akitaja jambo lililo tofauti kabisa na hilo. Kwenye Warumi 13:7 inaonyeshwa kwamba maafisa fulani wa serikali wana haki ya kulipwa kodi, wengine ushuru, na hata wengine heshima. Haki inayotakwa inategemea uhitaji wa waziwazi uliopo au jambo ambalo mtu mwenyewe anaomba. Kwa habari ya haki ya mambo ya ndoa ya mke wako, kinachohitajiwa si mwungano wa kimwili tu. Katika Kitabu The Family, Society, and the Individual (Jamaa, Jamii ya Watu, na Mtu Mwenyewe), mchunguzi William M. Kephart anasema hivi: “Jambo lililo la maana zaidi katika kutosheleza tamaa ya mke ya ngono linawezwa kusemwa kwa njia bora kuwa ni kumwonyesha upendo na shauku. . . . Wakati ngono inapoendelea, inaweza kuwa kwamba kinachotakwa zaidi na karibu kila mwanamke ni kufanyiwa mambo kwa njia ya mapenzi​—kushikwa, kupapaswa-papaswa, kupigwa busu . . . inaonekana kuwa asili ya wanawake kuichukua ngono kuwa jambo la kutendewa mambo kwa upole mwororo na kwa mapenzi, badala ya ngono kuwa ni uhusiano wa kimwili peke yake.”

18. Ni nini kinachoweza kufanya mtu awe akifikiria mambo yake tu?

18 Maumbile ya kimoyoni ya mke wako aliye “chombo kisicho na nguvu” yanakutaka wewe uwe mwenye kujinyima wala usiwe mtu wa kuhangaikia kujitosheleza mwenyewe tu. Zaidi ya hilo, kujifurahisha kwa kuangalia au kusoma mambo yanayoonyesha ngono kunaweza kutokeza “hamu ya ngono” isiyofaa na kufanya mtu afikirie mambo yake tu, na kufanya kitu kinachopasa kuwa chenye upendezi kiwe ovyo-ovyo tu. Epuka kuangalia mambo hayo kama vile unavyoepuka ugonjwa wa tauni! (Wakolosai 3:5) Lakini tumia subira umpe mke wako haki yake kamili kwa kumtendea mawonyesho ya upendo mwororo.​—1 Wakorintho 10:24.

Kujinyima Kunaugusa Moyo

19. Ikiwa mume ni mwenye kujinyima, je! mke Mkristo anapaswa kutumia nafasi hiyo ajiinue?

19 Kwa sababu ya mkazo kutiwa sana hivyo juu ya kujinyima kwa mume, huenda wewe ukawa na maoni ya kuuliza, ‘Je! wanawake walioolewa hawatajiinua​—sikuzote wawe wakishikilia kauli yao wenyewe?’ Haipasi kuwa hivyo! Wake Wakristo wanapaswa waitikie kama vile kundi lilivyoitikia lilipoonyeshwa na Yesu upendo wa kujinyima. Paulo anaandika hivi: “Mapendo ya Kristo yanatutazimisha sisi . . . alikufa kwa ajili ya wote hata walio hai wasiwe hai tena kwa ajili yao wenyewe.” (2 Wakorintho 5:14, 15, ZSB) Vivyo hivyo, mke wako anapaswa aitikie bila uchoyo. Ni kama vile mke wa Kikristo mwenye furaha alivyosema: “Mimi nakubaliana upesi na uamuzi wa mume wangu ili tuweze kuendelea kutumikia katika mgawo wa kitheokrasi ulio mgumu sana, kwa sababu najua ananijali.”

20. (a) Kufikiria Mwanzo 3:16 kunaonyeshaje kwamba waume na hata wake wanaweza kukosa usawaziko? (b) Kwa sababu gani wake wasiwe na haraka ya kuelekeza kidole kwenye makosa ya waume wao?

20 Ndiyo, ninyi wake, hakuna haja ya kuwa na uchoyo upande wenu. Sawa na vile mwanamume anavyoweza kutumia vibaya ukichwa wake kwa kumtawala mke wake kwa uchoyo, ndivyo mke anavyoweza kuwa na tamaa ya kupita kiasi ya kutaka mume wake aelekeze fikira kwake. (Mwanzo 3:16) Kuwa na usawaziko si jambo jepesi. Kwa sababu kuna mambo mengi yanayomdai mume wako ayatimize, kutia ndani wajibu mzito-mzito wa kundi, bila shaka kuna nyakati ambazo huenda asitosheleze mahitaji yako yote ya moyoni. Mtunga zaburi alikiri ya kwamba “[Yehova], kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” Hakuna hata mmoja wetu angesimama! (Zaburi 130:3) Kama vile itakavyompasa mume wako kumtolea Yehova jibu kwa matendo yake, hata wewe itakupasa kufanya hivyo. Lakini kwa wakati uu huu uliopo maneno yako ya kumshukuru kwa mema anayofanya pamoja na kumrehemu yatafanya akupende kwa kukuelekezea moyo wake, si fikira zake tu.

Msaada Kutoka Juu

21. Mungu anasaidiaje? Toa mfano.

21 Bila shaka, huenda madaraka yote hayo yakaelekea kuwa yenye kulemea mtu. Lakini Mungu atakusaidia ‘ufanywe hodari katika mwanamume [au, mwanamke] uliye kwa ndani kwa uwezo wa kupitia roho yake.’ Nguvu hizo za ndani ndizo zinazoweza kukufanya uweze kuchukua furushi lo lote, kwa maana Yehova anaweza kutumia uwezo wake ili ‘afanye zaidi ya wingi upitao ule wa kawaida wa kuyazidi mambo yote tunayoomba au kuwazia.’ (Waefeso 3:16, 20, NW) Wakristo wawili waliooana walitengana kwa sababu ya matatizo. Baada ya muda fulani waliketi pamoja wazungumze kama wanaweza kuwa na upatano. Wakaanza tena kupigiana makelele. Halafu mume akapendekeza wasali pamoja. Walituliza makelele yao. Mume alisema wazi kwamba, “Sababu halisi ya tatizo katika ndoa yetu ilionekana kuwa ni ukosefu huo wa kusali.” “Sikuzote tulijaribu kutatua matatizo yetu kwa kujitegemea sisi wenyewe badala ya kumwingiza Yehova ndani ya matatizo hayo. Hatukupata matokeo mazuri tulipokuwa tukifanya hivyo.” Baada ya kukaa wakiwa wameungana tena kwa muda unaozidi miaka mitano, mke alisema: “Mambo yanazidi tu kuwa mazuri. Tunavyozidi kuifuata ile kweli ya Biblia, ndivyo tunavyozidi kuwa wenye furaha. Sasa sisi tunajaribu kumtia Yehova katika kila upande wa ndoa yetu. Tunafurahia sana kufanya pamoja kazi ya kuhubiri.”

22, 23. (a) Ndoa ya Kikristo inapasa kutegemea nini katika pande zote? (b) Kwa sababu gani wake wengi wanapasa kusifiwa sana?

22 Ndiyo, ndoa ya Mkristo inapasa kutegemea katika pande zote uhusiano wake na Mungu, si kutegemea kupendeza mwenzi wake tu. Ni kama vile Paulo alivyoandika: “Wale walio na wake na wawe kama hawana.” (1 Wakorintho 7:29) Bila shaka, Paulo hakuwa akiambia waume wapuze wake zao. Inafaa kabisa mwanamume aliyeoa awe na bidii ya kutaka ‘apate ukubali wa mke wake.’ (1 Wakorintho 7; 33 NW) Lakini mwanamume anapozidi kufanya maendeleo ya kiroho na kuonyesha sifa za mume mwema, inaelekea kuwa atawekwa kwenye mapendeleo ya utumishi kundini. Utumishi huo utaondoa kiasi fulani cha wakati aliokuwa akitumia akiwa na mke wake, lakini hapaswi kukosa usawaziko. Hata hivyo, bado huenda ikampasa mke akose kuelekezewa fikira kamili na mume wake mara kwa mara.

23 Wengi wa ninyi wake mmekaa kwa subira nyakati mbalimbali mkingojea waume wenu walipopaswa kushughulikia wajibu mbalimbali wa kundi unaohitajiwa kabisa. Hakika ninyi mnastahili sifa! Hatua yenu ya kuliunga mkono jambo hilo inathaminiwa sana sana na waume wenu, hata na Yehova. Ninyi kwa uhakika ni kitu kile kile kinachotajwa na Biblia.​—“taji” kwa waume wenu, inayoleta “nia njema kutoka kwa Yehova”!—Mithali 12:4, UV; 18:22, NW.

24. Kila mmoja kati ya mume na mke anapaswa ajaribu kufanya nini?

24 Kwa hiyo, ninyi waume, endeleeni kuonyesha upendo wa kujinyima. Ninyi wake, endeleeni kuitikia kwa kuwaunga mkono waume wenu bila uchoyo. Jengeni ndoa yenu itegemee katika pande zote uhusiano wenu pamoja na Mungu. Naye Baba yetu mwenye upole mwororo azibariki sana jitihada zenu!—Kutoka w6/1./83.

Wewe Unakumbuka?

□ Mume ‘anapendaje mke wake kama Kristo alivyolipenda kundi’?

□ Mume anaweza kuigaje hali ya kujishusha ya moyo wa Abrahamu?

□ Mume anaheshimuje mke wake kuwa chombo kisicho na nguvu?

□ Inawapasa wake wawe na itikio gani kwa tendo hilo la kujinyima?

[Picha katika ukurasa wa 13]

MUME ANAPASWA KUTOA UONGOZI

Katika huduma ya shambani

Katika starehe

Katika kushughulikia mambo ya kijamaa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki