Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 2/15 kur. 3-7
  • Kutimiza Fungu Letu la Kuendeleza Maisha Yenye Furaha ya Jamaa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutimiza Fungu Letu la Kuendeleza Maisha Yenye Furaha ya Jamaa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UKICHWA
  • UTII WA MKE
  • Mume Anayejipatia Heshima Nyingi
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Kufanikisha Maisha ya Jamaa
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Ninyi Waume, Onyesheni Upendo wa Kujinyima
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Ujitiisho Katika Ndoa Humaanisha Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 2/15 kur. 3-7

Kutimiza Fungu Letu la Kuendeleza Maisha Yenye Furaha ya Jamaa

”Kila mtu ampende mke wake kama nafsi yake mwenyewe; wala mke asikose kumstahi mumewe”​—Efe. 5:33

1, 2. Ni jambo gani la kutamanika, na ni mambo gani ya kuepukwa katika ndoa, nao watu wengi wanatafuta msaada wapi?

NDOA yenye furaha! Ni mwanadamu gani anayeingia katika mpango huo uliofanywa na Mungu asiyetaka kuwa na furaha? Hata katika ulimwengu huu uliojawa na huzuni, wako watu ambao wameweza kupata furaha ya kweli katika maisha ya ndoa. Wameweza kuepuka migawanyiko na matatizo mazito yanayopatikana kwa wingi sana ulimwenguni leo. Lakini wamewezaje? Je! wamefuata mashauri ya umati wa washauri wa mambo ya ndoa ambao maoni yao yenye kutofautiana sana yamepigwa chapa kila mahali leo?

2 Karne nyingi zilizopita mwenye hekima aliandika hivi: “Hakuna mwisho wo wote wa kutunga vitabu vingi,” na kwa kweli inaonekana hakuna mwisho wa kutunga vitabu vinavyohusu ndoa na mambo kama hayo. (Mhu. 12:12) Wachunguzi na madaktari wa akili na matabibu wengineo wanatoa maoni juu ya mambo yanayopasa kufanywa au yasiyopasa kufanywa ili watu wawe na ndoa yenye furaha. Kwa kawaida magazeti yanakuwa na mashauri kwa watu walioachwa na wapenzi wao. Hata hivyo, magumu yanaongezeka, tena hesabu zinazohusu ndoa na talaka zinaonyesha kwamba watu wengi wanatengana au kutalikiana kwa sababu hawakupata furaha. Lakini wale walio na matatizo wanaweza kujipa moyo. Mwanzishi wa ndoa anatueleza jinsi inavyowezekana kupata furaha ya kiasi katika mpango huo wa kimungu, katika ulimwengu wenye migawanyiko.

3. Ni maulizo gani yanayoulizwa juu ya ndoa, na ni kitu gani tunachoshauriwa kwamba kinaweza kusaidia?

3 Je! ndoa yako ni yenye furaha? Je! wewe na mwenzi wako wa maisha mmepata furaha mliyoitazamia? Enyi mliooana miaka mingi, je! mngali ‘mnafurahia mke wa ujana wenu’? (Mit. 5:18) Kwa upande mwingine, je! mna matatizo? Ikiwa mnayo, bila shaka ungependa kukijua kitu kinachoweza kuwapa mashauri mazuri. Ni hakika kwamba kitu hicho hakiwezi kuondoa magumu yote yanayoweza kuwapata katika ulimwengu huu usiokamilika, lakini kinaweza kuwasaidia mtatue matatizo na kukuonyesha jinsi wewe bi nafsi unavyoweza kufanya maendeleo katika ndoa yako. Kitu hicho ndilo Neno la Mungu, Biblia Takatifu. Kurasa zake zina mashauri yatakayosaidia wenye nia ya kuishi kupatana na maagizo yake. Sasa angalia baadhi ya matatizo yaliyo katika ndoa za kisasa, kisha uone jinsi Neno la Mungu linavyoweza kusaidia mtu ayatatue ili kuifaidi jamaa.​—Zab. 19:7, 8.

UKICHWA

4. (a) Wanawake wengi wana maoni gani juu ya ukichwa katika mpango wa ndoa? (b) Biblia ina maoni gani juu ya madaraka ya ukichwa wa mwanamume?

4 Jambo moja linalotia wanawake wengi uchungu leo ni ukubwa ambao mwanamume amepewa katika ndoa. Wanawake fulani wanasema kwamba mwanamume anajivuna mno kwa sababu ya cheo cha ukichwa alicho nacho juu ya mwanamke. Inafaa tuseme hapa mwanzo mwanzo kwamba majivuno ambayo huenda mume akaonyesha katika jamaa kwa sababu ya ukubwa wake hayapatani na mafundisho ya Maandiko Matakatifu. Ingawa Mwanzo 3:16 inatuambia kwamba mwanamke angemtamani mumewe na kwamba mumewe ndiye angemtawala, Biblia inaonyesha wazi kwamba Mungu hakukusudia mwanamke awe mtumwa wa mwanamume. Bali, mwanamume alipaswa kuwa katika cheo cha ukichwa, akiwa ndiye amekabidhiwa daraka la kuangalia mkewe na jamaa ambayo wangezaa. Siku za Waebrania wa kale, ambao habari zao zinaelezwa sana na Biblia, wanawake wenye kumcha Mungu waliokuwa na bidii na uwezo walipewa ruhusa na uhuru mwingi wa kufanya mambo ingawa walitii waume wao, tena walifurahia cheo chao na kupata baraka ya kutumiwa na Yehova Mungu wamfanyie utumishi wa pekee. Sara, Rebeka, Ruthu, Hana, Esta, Elisabeti, na Mariamu mama ya Yesu ni mifano ya wake wengi waaminifu wanaotajwa na Biblia.

5, 6. (a) Hatua za ukichwa zinafuatanaje, kulingana na 1 Wakorintho 11:3? (b) Mitume Paulo na Petro wanasema mume atumieje ukichwa wake?

5 Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yaliyo katika Biblia Takatifu yanatoa maelezo mengi juu ya daraka ambalo mwanamume analo katika ndoa. Kwanza na tusome habari hizo kisha tupate ufahamu mzuri juu ya kuzitumia tuyatatue matatizo ya ndoa yaliyoko leo.

6 Tukifungua kitabu cha Wakorintho wa Kwanza, sura ya 11, mstari wa 3, tunaona kwamba mtume Paulo aliliandikia kundi la Korintho maneno haya: “Nataka mjue ya kuwa kichwa cha kila mwanamume ni Kristo, na kichwa cha mwanamke ni mwanamume, na kichwa cha Kristo ni Mungu.” Hapa anaonyesha hatua za mamlaka katika kundi la Kikristo, kuanzia kwa Yehova kuja kwa Kristo, kwa mwanamume halafu kwa mwanamke. Sasa basi, ukichwa huo wa mwanamume utatumiwaje? Tukifungua Waefeso 5:28, 29, tunasoma hivi: “Imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza.” Naye mtume Petro anaongeza kwa kusema: “Ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu.”​—1 Pet. 3:7.

7. Nyakati nyingine wake fulani wanakuwa na maoni gani juu ya waume wao naye mume anaweza Kujiuliza ulizo gani juu ya ukichwa wake? ,

7 Basi, hivyo ndivyo roho takatifu inavyoshauri waume washughulike na wake wao. Shauri hilo linasikika kama jambo jepesi sana. Tatizo kubwa ni kwamba, ingawa mume anataka kuwa kichwa cha jamaa, nyakati nyingine anashindwa kumwonyesha mkewe, kile chombo dhaifu, upendo na huruma iliyo ya lazima kwa sababu ya kutokamilika na choyo ambayo watu wanazaliwa wakiwa nayo. Mara nyingi huenda mke akasema kwamba yeye haoni kama mumewe anampenda, kwamba anajitafutia raha na kujitosheleza mwenyewe tu. Basi, katika kundi la Kikristo lazima mume ajichunguze na kukubali makosa akiona kwamba mkewe anasema kweli. Jiulize hivi, Je! mimi nampenda mke wangu kama nafsi yangu? Je! namheshimu kama chombo dhaifu? Au nimekuwa mtu wa kutaka kujitosheleza mwenyewe na kupata nitakacho tu? Je! nafikiria mahitaji na matakwa yake? Wakati wa kufanya maamuzi, je! namsikiliza, au mimi ndimi ninayefanya maamuzi yote, bila kufikiria mambo anayoweza kuwa akitaka?

8, 9. Ni pande zipi ambazo mume anaweza kufikiria aone jinsi anavyotumia ukichwa wake?

8 Na tuangalie baadhi ya matatizo yanayoondoa furaha katika ndoa kwa sababu ya kutokuwa na ukichwa unaofaa. Pengine mume na mkewe wana tumaini moja la Kikristo, tena ni watumishi wa Mungu Aliye Juu Zaidi, Yehova, waliojiweka wakf na kubatizwa. Ewe mume, unaona ubora wa kutumia wakati mkiwa pamoja na watu wa ukoo wa mkeo, si wale wa upande wako tu? Au unamhuzunisha mkeo wakati watu wa ukoo wake wanapokuwa wakija kuwatembelea, au wakati ninyi mnapowatembelea? Je! unaunga mkono upande wa jamaa za mkeo kama vile unavyotaka aunge mkono upande wa jamaa yenu, kwa kadiri hali zako zinavyokuwezesha?

9 Namna gani nyakati za kustarehe pamoja? Je! sikuzote jamaa inafanya mambo ambayo wewe peke yako unataka yafanywe? Je! unamwambia mkeo atoe maoni juu ya mambo ambayo angependa kufanya, badala ya kumfanyia maamuzi kwa lazima. Ingekuwa vizuri sana mume na mkewe waketi pamoja na kupanga mahali wanakotaka kwenda likizoni siku kadha, badala ya mume kutumia mamlaka yake na kufanya uamuzi bila kumwomba mkewe maoni.

10. Inampasa mume Mkristo akumbuke nini juu ya kulea watoto?

10 Fikiria, pia, jinsi ukichwa unavyohusu kulea watoto katika jamaa. Ewe mume, unamwachia mkeo kazi yote ya kutia watoto adabu? Wakati watoto wanapofanya mambo mema, hapo ndipo wanapokuwa watoto wako, lakini wanapofanya mabaya wanakuwa watoto wake? Jamaa inazidi kuwa na furaha ya kweli wakati wazazi wote wawili wanaposhirikiana kulea watoto. Mtume Paulo aliandikia Waefeso akawaambia: “Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika Bwana, maana hii ndiyo haki.” (Efe. 6:1) Angalia kwamba amri hiyo inasema wazazi watiiwe, si mzazi mmoja tu. Baada ya hapo Waefeso walishauriwa hivi: “Nanyi, akina baba, msiwachokoze watoto wenu; bali waleeni katika adabu na maonyo ya Bwana.” Tafsiri inayoitwa New Testament in Modern English inasema hivi katika mstari huo: “Akina baba, msisahihishe watoto wenu kupita kiasi wala msiwafanyie iwe vigumu kuitii amri hiyo. Waleeni kwa fundisho la Kikristo katika adabu za Kikristo.”​—Efe. 6:4.

11. Waume wengine wanashindwaje kutimiza ukichwa wao, nao wake wao wanalalamika wakisema nini?

11 Jambo jingine linalopasa kufikiriwa na mume bila mchezo katika jamaa ya Kikristo ni kuukubali ukichwa ambao Mungu amempa. Nyakati nyingi wake wanalalamika kwamba waume wao wanakataa kufanya maamuzi na kuwaacha wajiamulie mambo yote. Bila shaka, nyakati nyingine hilo ndilo linalokuwa jambo jepesi zaidi kufanya. Lakini, enyi waume Wakristo, kufanya hivyo ni kuepa daraka mlilopewa na Yehova! Mume Mkristo anatakiwa na Mungu pamoja na Neno lake aongoze jamaa maana ndiye amewekwa kufanya hivyo katika mpango wa kitheokrasi.

12. (a) Kwa sababu gani mke anapojichukulia madaraka ya ukichwa katika jamaa hapati furaha? (b) Je! hiyo inashusha cheo cha mke, kumfanya awe si wa maana sana akilinganishwa na mumewe?

12 Kunakuwa na huzuni wakati mume anapoachilia mambo yote yaamuliwe na mkewe. Kwanza, ingawa wanawake wengine wanaongoza jamaa wanapoachwa na waume wao, uwezo alio nao mwanamke ni wa kusaidia mumewe wala si wa kuongoza jamaa. Hivyo ndivyo Mungu alivyomfanya. Hapo mwanzo aliumbwa awe kitu cha kumkamilisha mwanamume, awe mwenzi wake, na hilo ndilo daraka linaloweza kumfurahisha zaidi. Unakumbuka maneno ambayo Yehova alisema wakati mwanamume alipokosa mwenzi kati ya viumbe vingine vyote vya dunia? Maandishi yanasema: “[Yehova] Mungu akasema, Si vema huyo mtu awe peke yake, nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye.” (Mwa. 2:18) Kwa hiyo mwanamke alipaswa kuwa msaidizi wa mwanamume. Hicho ni cheo kikubwa. Kitabu cha Mithali kinataja habari za Yesu kabla hajawa mwanadamu na kumwita hekima, kisha kinasema kwamba alikuwa kando ya Yehova akiwa “stadi wa kazi.” (Mit. 8:30) Kwa hiyo, waume fanyeni kazi pamoja na wake wenu na kuwaona kama wasaidizi wenye maana sana, mshauriane nao, mpate maoni yao, kisha mwongoze jamaa katika maamuzi makubwa. Mkifanya hivyo ndoa inaweza kuwa na furaha ya kweli. Hiyo si kusema kwamba wewe mume utajifanyia mambo yote, lakini kumbuka kwamba jamaa yako inatafuta uongozi ikitaka kujua mambo yanayopaswa kufanywa na anayepaswa kuyafanya. Ushirikiano utafanya mume afurahie ukichwa wake na mke afurahie kutii.

UTII WA MKE

13. Je! mke anakuwa mtumwa mnyonge kwa sababu ya kumtii mumewe kupatana na Biblia? Toa sababu za jibu lako.

13 Tunapoingia sasa katika habari inayoelekea kukasirisha watu upesi, yaani, utii wa mke kwa mumewe, na tuangalie kwanza maneno ambayo Paulo aliandikia kundi la Efeso. Paulo alisema: “Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu.” Naye mtume Petro aliandika hivi: “Kadhalika ninyi wake, watiini waume zenu.” (Efe. 5:22; 1 Pet. 3:1) Katika ulimwengu wa leo ambamo wanawake wanapigania kuwa sawa na wanaume, wengi wao watasema kwamba hayo ni maneno yenye kutokeza ubishi. Lakini si lazima yatokeze. Ikiwa mume anatimiza sifa za mume Mkristo, kama zile tulizotaja katika makala hii (ingawa hatukuzungumza pande zote za sifa hizo) mke anaweza kufurahia kumtii ikiwa anampenda mumewe kikweli. Anapomtii hawi mtumwa mnyonge. Bali, anatimiza daraka alilopewa na Mungu, kisha anapata furaha. Lakini ni mambo gani hasa ambayo mke Mkristo anaweza kufanya alete furaha katika ndoa?

14. (a) Kwa sababu gani huenda wake wengine wakatatizwa kuonyesha waume wao utii unaopatana na Biblia? (b) Kwa sababu gani shauri la Petro katika 1 Petro 3:2 linahusu hata wanawake ambao waume wao wanaamini?

14 Huenda ikampasa kubadili utu wake kama vile impasavyo mumewe. Ikiwa mwanamke ana maelekeo ya kujitegemea, kujisikia anaweza sana. kujitunza mwenyewe, huenda akaona si vyepesi kutii mumewe. Huenda ikampasa kubadili mawazo yake, tena ayabadili sana nyakati nyingine, ili atimize fungu lake la kufanya ndoa iwe yenye furaha. Ikiwa mpaka sasa mumewe hajamfikiria sana anavyopaswa, hapo mke anapata nafasi ya kufanya maendeleo. Mtume Petro alisema kwamba wanawake wanaweza kusaidia waume wao wasioamini wakiwaonyesha utii wa Kikristo kwa kuwa na mwenendo safi na heshima nyingi. (1 Pet. 3:2) Basi, iwapo mke anaweza kusaidia mume asiyeamini kwa njia hiyo, mambo yatakuwa mepesi zaidi ikiwa mume ni Mkristo aliyejiweka wakf na kubatizwa, ikiwa anashirikiana na mkewe katika utumishi wa Yehova.

15. Mke anawezaje kupata upendeleo wa mumewe katika kazi yake ya kupamba nyumba?

15 Kuna njia nyingi ambazo wake wanaweza kutumia wavute waume wao. Wanaweza kuwavuta kwa jinsi wanavyotunza nyumba. Ikiwekwa katika hali safi na ya kutengenea, mume anaweza kutiwa sana moyo atimize daraka lake sawasawa. Ewe mke, unafurahia daraka lako la kupamba nyumba? Wakati rafiki za mumeo wanapowatembelea, mume wako anaona fahari juu ya nyumba anamowakaribisha? Hilo ni jambo la kufikiria. Nyumba ikiwa chafu-chafu, vyombo vilivyotumiwa kwa chakula cha jana vikiwa havijasafishwa bado, na ikiwa viti na vimeza vimejaa mavumbi matupu, kisha wageni wafikapo wanaona hali ya uzembe, mambo hayo yanaweza kupunguza furaha katika ndoa. Ni wazi kabisa kwamba nyakati nyingine waume wanaweza kusaidia kwa kuweka vitu katika hali safi. Lakini sasa hivi hatusemi habari yao, bali tunaeleza njia za kumsaidia mumeo ili akuonee fahari kwamba u mke mwenye upendo na bidii.

16. Mke akiruhusiwa kutumia pesa za jamaa, anapaswa kufanya nini?

16 Fikiria pia mipango ya matumizi ya pesa katika jamaa. Je! wewe unajiangalia usinunue vitu msivyo na uwezo wa kununua? Ikiwa mumeo amekupa pesa za matumizi ya nyumbani, za kununulia vyakula na kulipia gharama za nyumba, je! wewe unajitahidi usiruke mpaka katika matumizi mliyopanga, bila kutazamia kuponda pesa kwa sababu anaweza kukuletea pesa zaidi ukizihitaji? Tunasema tena kwamba, ni wazi kabisa kwamba inampasa mume ajaribu kutafutia jamaa pesa za kutosha matumizi yao. Lakini ikiwa pesa zinapasa zitumiwe kwa uwekevu, wote wawili wanapaswa kushirikiana ili kuifaidi jamaa.​—Mit. 31:10-31.

17. Ni kwa njia gani mke anavyoweza kuonyesha anapendezwa na madaraka ya mumewe (bila kupeleleza mambo ambayo inampasa mumewe atunze kama siri) na kuweka wazi njia za kupashana habari?

17 Ni jambo la maana wewe mke uendelee kupashana habari na mumeo. Lakini tena, si mke peke yake anayepaswa kufanya hivyo, bali inawapasa wote wajitahidi. Hata hivyo, mke anaweza kusaidia kwa kuepuka kumwuliza-mwuliza mumewe mambo ya watu bi nafsi ikiwa mumewe ana madaraka katika kundi. Mke anaweza kujitahidi kuzungumza na mumewe habari za kushinda kazini, labda juu ya matatizo anayoweza kumsaidia, na kumweleza jinsi yeye mwenyewe alivyoshinda nyumbani akiwa na watoto, au vile alivyowapa watu ushuhuda wa Ufalme. Kila mmoja anapopendezwa na maisha ya mwenzake kwa njia hiyo, jamaa inapata baraka na furaha.​—Mit. 16:24.

18. Taja matatizo mengine yanayozuia jamaa isiwe na umoja yatakayoendelea kuzungumzwa.

18 Mpaka hapo tumezungumza pande mbili kubwa za kuendelezea umoja wa jamaa, yaani, ukichwa wa mume katika mpango wa Mungu, na utii ambao mke ameagizwa katika Biblia. Lakini ziko pande nyingine nyingi tunazohitaji kuzungumza kuhusu maisha ya jamaa. Kwa mfano, kuna matatizo kama ya mwenzi mwenye kunung’unika-nung’unika, ya kutia watoto adabu, na vilevile uhusiano katika ndoa, unaotajwa na mtume Paulo kama kupeana haki anazostahili kila mwenzi katika maisha yao ya ndani ndani. (1 Kor. 7:3-5) Itafaa tuzungumze mambo hayo, kwa hiyo makala inayofuata itaeleza mambo hayo kwa urefu ili kutusaidia.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki