Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • hp sura 2 kur. 10-20
  • Je! Kuna faida ya Kumwamini Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Kuna faida ya Kumwamini Mungu?
  • Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UHAI WAKO—JE! ULIJITOKEZA WENYEWE?
  • CHEMBE ZA MWILI WAKO—UBONGO WAKO—WEWE
  • “MSABABISHI WA KWANZA” WA HUU ULIMWENGU MZIMA
  • Je, Kweli Kuna Aina Yoyote ya Uhai Inayoweza Kuitwa Duni?
    Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai
  • Tuliumbwa Tuishi Milele
    Amkeni!—1995
  • Kuchunguza Chembe kwa Hadubini
    Amkeni!—1999
  • Jinsi Tunavyoweza Kujua Kwamba Kuna Mungu
    Je, Kweli Mungu Anatujali?
Pata Habari Zaidi
Furaha​—Namna ya Kuipata
hp sura 2 kur. 10-20

Sura ya 2

Je! Kuna faida ya Kumwamini Mungu?

MOJA kati ya maulizo yaliyo ya maana zaidi utakalokutana nalo nyakati zote ni, ‘Je! Mungu yuko?’ Kauli utakayokata inaweza kuwa na matokeo tofauti juu ya namna utakavyoiona jamaa yako, kazi yako, fedha zako, adili na hata maisha yenyewe.

2 Watu wengi wakiulizwa, ‘Je! Mungu yuko?’ watajibu kwa kurudia kutaja mambo waliyosoma au wakasikia kwa wengine. Walakini, inakupasa wewe binafsi ulifikirie ulizo hilo. Katika kitabu chake Man, God and Magic, Dakt. Ivar Lissner anasema kwamba “tofauti kubwa kati ya mwanadamu na mnyama” ni kwamba “mwanadamu hatosheki na kulala tu, kula na kujipasha moto tu.” Mwanadamu ana “tamaa ya ajabu ya kurithi, inayomsukuma,” inayoweza kuitwa “hali ya kiroho.” Dakt. Lissner anaongeza kusema kwamba ‘sehemu zote za ustaarabu wa wanadamu zimeimarishwa katika kutafuta Mungu.’ Kwa hiyo unapokumbana na lile ulizo, ‘Je! Mungu yuko?’ ni kuonyesha kwamba wewe hukuachilia ovyo sifa fulani ya maana, yaani, hali ya kiroho yako.

3 Utajuaje kama kuna ‘mfanyi na mtawala wa huu ulimwengu mzima, Mtu Mkubwa Kupita Wote,’ kama kamusi moja inavyotoa maana ya “Mungu”? Kufikiri kuzuri kunaonyesha kwamba ikiwa kuna ‘mfanyi wa huu ulimwengu mzima,’ kunapasa kuwe vionyesho vya kujulisha namna ulimwengu huo ulivyotokea, na pia namna ulivyobuniwa na kufanywa kwa utaratibu mzuri. Unapojarihu kuchunguza kama kuna vionyesho vya namna hiyo, tunakuomba ufikirie mavumbuzi ya wachunguzi wa vitu vilivyo hai juu ya maisha (yaani, wabayolojia) na ufikirie mavumbuzi yanayohusu ulimwengu mzima wetu yaliyofanywa na wachunguzi wa nguvu za adili (yaani, wanafizikia) na wachunguza-nyota wenye kutumia darubini na vyombo vya kukusanyia habari kutoka sayari zile nyingine.

UHAI WAKO—JE! ULIJITOKEZA WENYEWE?

4 Kwa nini usijichunguze mwenyewe kwanza? Maisha yako yalitoka wapi? Ni kweli kwamba ulipitishiwa maisha hayo na wazazi wako. Lakini maisha duniani yalianzia wapi?

5 Kwa kujaribu kujianzishia uhai katika maabara (vyumba vya uchunguzi wa kisayansi) na hivyo waeleze mahali ulikoanzia, wanakemia wametokeza cheche za moto kwa kuchanganya sehemu fulani za pekee za gesi (hewa) za pekee. Kitu kimoja ambacho wametokeza kwa kufanya hivyo ni asidi amino (chembe ndogo sana zinazosaidia ulishaji, ukuzi na ujenzi wa sehemu zilizoharibika katika miili ya vitu vilivyo hai). Hata hivyo, asidi amino hizo walizotengeneza hazikuwa na uhai. Tena, hazikujitokea zenyewe; zilifanyizwa na wanasayansi wenye elimu katika mazingira yenye kusimamiwa vizuri ya maabara za kisasa.

6 Kuna asidi amino zaidi ya 200 zisizo za kufanyizwa na wanadamu, lakini ni 20 tu za namna ya pekee zinazopatikana katika protini za vitu vilivyo hai. Hata ikiwa asidi amino fulani zinaweza kutokana na umeme wa mvua, ni nani aliyezichagua zile 20 tu zinazofaa zenye kupatikana katika vitu vilivyo hai? Nazo ziliongozwaje zifuatishe utaratibu mzuri kabisa unaohitajiwa kabisa ili kufanyiza protini? Mchanganuaji Dakt. J. F. Coppedge alikadiri kwamba ‘uwezekano wa chembe moja tu ya protini-molekyuli kutokea kwa kujipanga kwa asidi amino zenyewe ni mdogo sana, sana, sana, sana.’ Tena, yeye anaonyesha kwamba si protini-molekyuli moja inayohitajiwa, bali ni ‘protini-molekyuli zisizopungua 239 zinazohitajiwa ili kutengeneza namna iliyo ndogo zaidi ya uhai unaofikiriwa kufanyizwa.’ Je! wewe unafikiri kwamba ushuhuda huo unaonyesha uhai ulijitokeza wenyewe tu, au ulitokezwa na mtu mwenye akili nyingi za kubuni?

7 Fikiria pia namna nyingine ya majaribio yaliyofanywa katika maabara (vyumba vya uchunguzi wa kisayansi) ambayo imetangazwa katika magazeti kuwa ni “kuumba uhai.” Kwa kutumia vifaa vilivyofanyizwa kwa ufundi mwingi wanasayansi wamechukua kiini cha ugonjwa (virasi) kinachotokezwa na kiumbe kilicho hai kisha wakazitenganisha sehemu mbalimbali za kiini hicho cha ugonjwa. Baadaye wamechukua sehemu hizo wakaziunganisha tena zikawa kiini cha ugonjwa. Walakini, Rene Dubos mbayolojia (mchunguzi wa vitu vilivyo hai) anaeleza katika kitabu Encyclopcedia Britannica kwamba kuuita ufundi huo “kuumba uhai” ni kosa sana. Wala wanasayansi hao wala wengineo hawakuweza kufanyiza uhai mpya kutokana na kitu kisicho na uhai. Badala ya kuonyesha kwamba uhai unajitokeza wenyewe tu, majaribio hayo yalionyesha kwamba ilikuwa lazima “vifaa vyote vyenye kufanyiza uhai vitokane na uhai uliotangulia kuwako kabla yavyo.”

8 Hata kama wanasayansi wangeweza kutokeza protini yenye uhai kutokana na vitu visivyo na uhai, hiyo ingesaidia tu kuhakikisha kwamba mtu fulani aliye hai na mwenye akili angehitajiwa atangulie kuishi ndipo awe nguvu yenye kufanyiza uhai mwingine. Ni wazi kwamba wanadamu hawakutangulia kuwapo ndipo waweze kuanzisha uhai duniani. Hata hivyo uhai uliumbwa, kutia na uhai wa kibinadamu. Ni nani aliyeuumba? Zamani za kale waandikaji wa Biblia walikata kauli inayofaa kufikiriwa kwa uzito. Mmoja wao alisema: “Pumuzi ya Mwenyezi ilinipa uzima.” Mwingine akaongezea: “[Mungu] mwenyewe ndiye mpaji wa uzima wa ulimwengu mzima.”a

9 Ukijichunguza sana mwili wako utasaidiwa ufikirie vizuri zaidi jambo hilo.

CHEMBE ZA MWILI WAKO—UBONGO WAKO—WEWE

10 Uhai unapiga-piga katika mwili wako ambao umefanyizwa kwa chembe ndogo sana kama 100,000,000,000,000. Chembe ya mwili ndicho kisehemu cha msingi kilicho katika kila kiumbe hai duniani. Inavyozidi kuchunguzwa kwa uangalifu, ndivyo inavyozidi kuonekana kwamba ni ngumu kufahamika.

11 Kila moja ya chembe za mwili wako inaweza kufananishwa na jiji lenye kuta linaloweza kuonekana kwa kutumia darubini ya kulikuza. Chembe ya mwili ina sehemu zilizo kama mashine za umeme zinazotokeza nishati. “Viwanda” vilivyo katika chembe ya mwili vinatengeneza protini na vilevile homoni (namna fulani za umajimaji unaochochea viungo mwilini) ili zisafirishwe kwenye sehemu nyingine za mwili. Kuna mfumo wenye mifereji mingi ya kusafirisha kemikali za mwili ziingie na kutoka ndani ya chembe ya mwili. Kuna “askari-walinzi” wanaosimama milangoni kuzuia vitu vibaya visiingie chembeni na kupigana na vishambuliaji vyo vyote vinavyokuja. Kitu ambacho kinaongoza utendaji wote huo ni ile sehemu ya kati, “nyumba kuu ya jiji” la chembe. Sehemu hii ya kati inaendesha utendaji wote wa chembe na ndiyo yenye chapa zinazorithiwa na watoto wakati wa uzazi. Nyingine za sehemu za chembe ya mwili ni ndogo sana sana hivi kwamba visehemu vilivyomo haviwezi kuonekana vizuri sana hata mtu akitumia darubini ya elektroni yenye nguvu za kukuza vitu mara 200,000. (Kama sisimizi au siafu angekuzwa kiasi hicho angekuwa na urefu unaozidi kilometa 0.8 au nusu-maili.) Ni nini kinachoweza kueleza mahali ulikotoka mfumo huo wa ajabu na utaratibu mzuri ulio katika kila moja ya chembe ndogo sana za mwili wako ambazo jumla yake ni 100,000,000,000,000?

12 Siku moja wewe ulikuwa chembe moja tu iliyotungwa mimba katika tumbo la uzazi la mama yako. Chembe hiyo iligawanyika ikawa chembe mbili, kisha nne, na kuendelea ivyo hivyo. Baadaye, nyingine za chembe hizo zikawa minofu. Nyingine zikawa macho yako, zikawa mifupa na moyo wako. Ilikuwaje hata chembe hizo zikafanyiza kila kiungo cha mwili wako kwa wakati unaofaa na katika mahali panapofaa? Kwa mfano, sababu gani chembe zikawa masikio na kujiweka mahali palipofaa, badala ya kujiweka kwenye goti lako au mkono wako?

13 Fungua macho uangalie vizuri zaidi. Katika kila chembe wewe una makumi ya maelfu ya vipokeza-urithi (genes) na vichukua-tabia (DNA), vinavyoiambia chembe namna itakavyofanya kazi na kuzidisha hesabu ya chembe. Inasemwa kwamba kichukua-tabia (DNA) katika kila chembe kina habari zinazotosha kujaza ensaiklopedia (kitabu kikubwa) moja yenye vitabu 1,000 ndani yake. Kichukua-tabia hicho ndicho kilichoamua utakuwa na nywele za rangi gani, kikaamua mwendo wa ukuzi wako, upana wa tabasamu (kicheko) yako na mambo mengine yasiyohesabika yanayokuhusu wewe. Yote hayo ‘yaliandikwa’ katika kichukua-tabia (DNA) cha chembe moja katika tumbo la uzazi la mama yako.

14 Kulingana na hata machache hayo tuliyosema juu ya chembe, tunauliza hivi: Kwa kuwa wazazi wetu sio waliokusudia ziweko zile chapa za kushangaza sana zinazorithiwa wakati wa uzazi, wala sio waliotayarisha chembe iwe namna ilivyo, aliyefanya hivyo ni nani? Je! jibu linaweza kutolewa kwa njia ya akili nzuri bila ya kumtaja Mbuni mwenye akili sana?

15 Kati ya viungo vyote vya mwili wako, labda kilicho cha kustaajabisha zaidi ni kile ambacho wewe hutakiona hata siku moja, yaani, ubongo wako. Ubongo umefanyizwa kwa chembe za neva (mishipa ya fahamu) kama 10,000,000,000, na hiyo ni hesabu iliyo mara mbili za idadi ya watu walio katika uso wa dunia. Halafu huenda kila moja ya chembe hizo ikawa na maelfu ya viunganishi vya chembe nyingine za neva. Jumla ya viunganishi haiwaziki hata kidogo!

16 Wewe umeweka katika ubongo wako mamia ya mamilioni ya habari na taswira (picha) mbalimbali, lakini ubongo si ghala tu ya kuwekea habari ulizojifunza. Kwa kuutumia unaweza kujifunza kufunga kifundo kwenye kamba, kusema lugha mpya, kuoka mkate au kupiga mluzi (ubinja). Unaweza kuwaza—likizo lako litakuwaje au tunda lenye maji mengi litakuwa na ladha gani. Unaweza kuchanganua mambo na kubuni vitu. Pia unaweza kupanga mambo ya huko mbele, unaweza kuthamini vitu, kupenda na kuhusianisha mawazo yako na zamani zilizopita, na wakati wa sasa na ule ujao. Ni wazi kwamba Yeye aliyebuni ubongo ana hekima inayopita hekima ya mwanadamu ye yote, kwa sababu wanasayansi wanaungama hivi:

“Hatujui hata kidogo jinsi kazi hizi zinavyotimizwa na chombo hiki kilichojawa na maajabu, ambacho kilitengenezwa kwa ufundi mwingi sana, kwa utaratibu na kwa njia ya kustaajabisha sana. . . . huenda wanadamu wasiweze hata siku moja kutatua mambo mbalimbali yenye kuwatatanisha yanayohusiana na ubongo.”—Scientific American.

17 Unapofikiri uone kama kuna Muumba aliye Mtu Mkubwa Kupita Wote, usiisahau sehemu ile iliyobaki ya mwili wako. Macho yako—yenye kunasa picha kwa uzuri mwingi sana na kujirekebisha yaone maumbo mbalimbali vizuri kuliko kamera yo yote (chombo cha kupigia picha). Masikio yako—yanayoweza kutega namna za sauti mbalimbali na kukuelekeza upande unaofaa, hata kukupa msimamo uliosawazika vizuri wa mwili. Moyo wako—bomba la kushangaza sana linaloweza kufanya maajabu ambayo hata wahandisi (ingenieurs) walio wastadi zaidi wameshindwa kufuatisha. Kuna vitu vingi ambavyo vingeweza kutajwa, lakini tutaongeza kutaja ulimi, halafu mfumo wa kuyeyushia chakula kisha mikono, halafu tuachie hapo. Mhandisi mmoja aliyeajiriwa abuni na kujenga kompyuta kubwa aliwaza hivi:

“Ikiwa kompyuta yangu ilihitaji mtu wa kuibuni, ile mashine ya kifizikia, ya kikemia na kibayolojia ambayo ndiyo mwili wangu wa kibinadamu—ambao nao ni sehemu iliyo ndogo sa-a-na ya ulimwengu mzima unaoelekea kutokuwa na mipaka—itakosaje kuwa na mtu aliyeibuni?”

“MSABABISHI WA KWANZA” WA HUU ULIMWENGU MZIMA

18 Zamani za kale, yapata miaka 3,000 iliyopita, mwanamume mmoja wa Mashariki ya Kati jina lake Elihu alisema: “Tazama juu kwenye anga kisha ufikiri.”b

19 Je! wewe umepata kufanya hivyo wakati wa usiku wenye anga lilibo wazi, lisilo na mawingu? Kila mtu amepaswa afanye hivyo. Ni nyota kama 5,000 tu zinazoweza kuonwa kwa macho bila kutumia darubini. Walakini, galaksi (kundi la nyota) yetu inayoitwa Njia ya Kimaziwa ina nyota zaidi ya 100,000,000,000. Nazo galaksi ni ngapi? Wachunguzi wa nyota wanasema kwamba kuna maelfu ya mamilioni—si ya nyota, bali ya galaksi, na kila moja ina mabilioni ya nyota! Salaala! Kumbe wanadamu ni vitu vidogo sana wakilinganishwa na zote hizo? Basi vyote hivyo vilitoka wapi?

20 Wanasayansi wamevumbua kwamba galaksi za nyota zinaonekana kama zinaruka zikiacha mahali fulani pa kati na kwenda mbali. Wachunguzi wengi wa nyota wanakisia kwamba maelfu ya mamilioni ya miaka iliyopita, mlipuko mkubwa sana, “mshindo mkubwa,” ndio uliotokeza nishati na tungamo (asili ya vitu vinavyoonekana) kisha vitu hivyo viwili vikaenea na kuufanyiza ulimwengu mzima tunaoujua. Kisio lao halielezi ni kitu gani kilichosababisha tukio hilo. Lakini kisio hilo lina habari zinazofaa kuangaliwa, yaani, kwamba kulikuwa na mwanzo fulani, dakika fulani wakati ulimwengu mzima ulipozaliwa.

“Leo mtu anaweza kuhisi wanasayansi wanatetema kwa kuogopeshwa na ushuhuda unaozidi kuongezeka sana kuonyesha kwamba kulikuwako mwanzo wenye ‘mshindo mkubwa’ wa huu ulimwengu mzima. Jambo hilo linatokeza ulizo juu ya kile kilichotangulia kutokea, na imani iliyo tegemeo kubwa zaidi la wanasayansi inatikiswa wanapojikuta wakiwa hawawezi kabisa kuyajibu maulizo yote.”—The Wall Street Journal.

21 Ndiyo, kwa watu wasioamini Mungu yuko, kuna maulizo yenye kuwatatanisha: Ni kitu gani au mtu gani aliyeiingiza tungamo (asili ya vitu vinavyoonekana) katika ulimwengu mzima? Je! ulimwengu mzima uliumbwa kutokana na patupu? Kwa kuwa tungamo inaonwa kuwa namna fulani ya nishati, chanzo cha nishati hizo ni nini?

22 Dakt. Robert Jastrow, mkurugenzi wa Taasisi ya Godard ya Uchunguzi wa Anga za Juu ya NASA, alisema hivi: “Kwa sababu ya ushuhuda huo uliopo, bila wazo la kusema kwamba kuna Mungu aliyeuumba ulimwengu mzima lina ukweli wa kisayansi sawa na mawazo mengine mengi.”

23 Watu wenye maarifa mazuri katika kila kizazi wamekata kauli kwamba pasina shaka kuna Msababishi wa Kwanza Mwenye Akili, muumba aliye Mtu Mkubwa Kupita Wote. Biblia inaeleza namna watu hao walivyojisikia, inaposema hivi: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake.”c

24 Uwe au usiwe umekata kauli kwamba Mungu yuko, mambo ambayo tumezungumza juu ya uhai, juu ya sisi binafsi, na juu ya ulimwengu mzima yanapasa yasaidie kueleza kwa nini watu wengi wanaotumia akili wanasadiki kuna Mungu. Hiyo inatuelekeza kwenye jambo jingine linalohusiana nalo: Ikiwa Muumba yuko, je! si jambo la akili nzuri kutazamia kwamba yeye angepashana habari na viumbe vyake, na kujibu maulizo yetu haya: Kwa nini sisi tupo hapa? Kwa nini uovu ni mwingi sana? Wakati ujao kutakuwako mambo gani? Tunaweza kupata furaha namna gani?

[Maelezo ya Chini]

a Ayubu 33:4, ZSB: Matendo 17:25, New English Bible.

b Ayubu 35:5, New English Bible.

c Zaburi 19:1.

[Mambo ya Kuzungumziwa]

Sababu gani inatupasa tulifikirie ulizo, ‘Je! Mungu yuko?’ (1-3)

Uhai ulio duniani unaonyesha nini? (4-9)

Tunaweza kujifunza mambo gani juu ya chembe za mwili wetu yanayotusaidia tunapofikiria kuwako kwa Mungu? (10-14)

Ubongo wa kibinadamu unatoaje ushuhuda wa kwamba kuna mtu aliyeubuni? (15-17)

Ni nini kinachoongoza watu wengi wakate kauli kwamba ulimwengu mzima uliumbwa na Mungu? (18-24)

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

“Leo asilimia (%) isiyopungua 80 ya wanasayansi wanaoshughulika na masomo ya bayolojia labda wataungama kwamba bayolojia na uhai ni mambo yanayoendeshwa na mamlaka fulani yenye cheo cha juu zaidi.

“Utaratibu mzuri ajabu na uongozi unaoonekana katika namna mbalimbali za uhai na katika utendaji mbali-mbali wa asili, wa chembe na molekyuli za mwili, unaithibitisha sana imani ya kwamba kuna mamlaka fulani yenye cheo cha juu zaidi.”—“Journal of the American Medical Association.”

[Sanduku katika ukurasa wa 19]

UTARATIBU ULITOKA WAPI?

Dakt. Paul Davies, mhadhiri (mtoa-hotuba) wa somo la hesabu za ufundi kwenye Chuo Kikuu cha King, London, anaandika hivi katika “New Scientist”:

“Kila mahali tunapopatazama katika Ulimwengu Mzima, tangu galaksi za nyota zilizotapakaa sana mpaka kwenye visehemu vidogo sana sana vya atomi, tunaona utaratibu. . . . Ikiwa nyakati zote maarifa na utaratibu yana maelekeo ya asili ya kutaka kupotea, basi maarifa yote yanayoufanya ulimwengu upendeze sana yalianzia wapi?”

Sir Bernard Lovell, wa Jengo la Uchunguzi la Benki ya Jodrell linalojulikana sana, anaandika akisema kwamba maoni yake yanafanana na yale ya Albert Einstein:

“Ni ajabu kubwa inayohusu upatani mzuri sana wa sheria ya maumbile, inayoonyesha kuna mtu fulani mwenye akili kubwa sana inayofanya mawazo na matendo yote ya wanadamu yenye utaratibu mzuri yawe bure kabisa yakilinganishwa nayo.”—“Centre of Immensities.”

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

CHEMBE ZA MWILI WAKO

MITOKONDRIA zinatokeza kemikali ili kufanyiza nishati

KIINICHEMBE kinaongoza utendaji wote wa chembe

RIBOSOMU zinafanyiza protini na homoni za kusafirishwa kwenye sehemu nyinginezo za mwili

MFUMO wa MIFEREJI unasafirisha kemikali kuziingiza na kuzitoa ndani ya chembe ya mwili

UTANDO na PROTINI zinazuia vitu vibaya visiingizwe ndani ya chembe na kupigana na vishambuliaji

[Picha katika ukurasa wa 15]

UBONGO WAKE unamwezesha

Kusawazisha baisikeli

Kusikia motokaa zinazokaribia

Kunusa harufu ya maua

Kuhisi upepo mzuri ukivuma

Kutazama asimkanyage mbwa

Kukumbuka njia ya kurudi nyumbani

[Picha katika ukurasa wa 17]

NI NANI ALIYEUBUNI MWILI WA MWANADAMU?

UBONGO:

Unaishinda sana kompyuta, nao una nafasi ya kuingiza ndani maarifa kadiri ya mara kama bilioni moja kuliko yale yanayotumiwa katika muda wa sasa wa maisha ya kibinadamu.

JICHO:

Ni kamera inayojiendesha na kujirekebisha yenyewe. Picha zinazopigwa na jicho ni safi kabisa. Hata linapiga picha zenye mwendo, kama za sinema.

MOYO:

Bomba linalofanya kazi vizuri zaidi ya mashine yo yote iliyobuniwa na mwanadamu. Moyo unapiga na kusukuma galani 1,500 (litre 5,700) au zaidi kila siku.

INI:

Maabara ya kemikali yenye kazi zaidi ya 500. Ini linatengeneza enzaimu zaidi ya 1,000. (Hizo ni protini imara zinazobadili utendaji wa visehemu vya chembe ya mwili bila ya hizo zenyewe kubadilishwa.)

MIFUPA:

Fremu ya mwundo wenye uzito wa ratili 20 (kilogramu 9) tu, lakini yenye nguvu kama maboriti ya chuma.

MFUMO WA NEVA:

Mfumo wa kupasha habari unaopokea na/au kuitikia misisimko ya mwili 100,000,000 kila nukta.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki