Sura ya 4
Kujifunza Juu ya Usichoweza Kuona
HATUWEZI kuona vingi vya vitu vilivyo vya kupendeza zaidi. Kwa mfano, picha za kwanza zenye kuonyesha kitoto kikikua ndani ya tumbo la uzazi zilikuwa ajabu kubwa kwa sababu huo ulikuwa “mwujiza” usiopata kuonekana kabla ya hapo.
2 Kuna vitu vingine vya maana tusivyoweza kuona, kama kani za sumaku na za uvutano. Lakini hizo ni nguvu zilizopo kweli kweli. Tunaweza kujua mengi juu yazo kwa kutazama matokeo yazo. Ndivyo ilivyo kuhusu Mungu. Walakini, ikiwa tunataka kujua habari za Muumba wetu—na inatupasa tutake kufanya hivyo—lazima tujitahidi sana.—Linganisha Yohana 3:12.
3 Hasa, ziko njia mbili za kujifunza habari za Mungu, yeye tusiyeweza kumwona. Paulo, mtume wa Yesu Kristo, alitaja njia moja kwa kuandika hivi: “uwezo wake wa milele na uungu wake, ingawa havionekani kwa macho, vinafahamika wazi. Watu wanaweza kuyajua mambo hayo kutokana na vitu hivyo Mungu alivyoviumba.” (Warumi 1:20, Habari Njema kwa Watu Wote) Ndiyo, uumbaji unatoa ushuhuda wa kwamba kuna Mtu Mkubwa Kupita Wote. Tena, unazionyesha sifa zake, kuonyesha namna alivyo. Njia ile ya pili ndiyo ya maana zaidi, kwa kuwa inawapa watu habari kamili juu ya Mungu. Njia hiyo ndio ufunuo ulioandikwa katika Biblia.
YEYE YUKO NAMNA GANI?
4 Kama ilivyoandikwa katika Biblia, Yesu alisema “Mungu ni Roho.” (Yohana 4:24) Maana yake ni kwamba Muumba hana mwili wenye nyama kama sisi, Hilo halipasi liwe jambo gumu kukubaliwa na watu wanaofahamu habari za vitu vya kweli kama kani (nguvu) za uvutano, kani za sumaku na mawimbi ya redio. Walakini, tofauti kubwa sana kuhusu Mungu ni kwamba yeye ni Mtu aliye hai, mwenye akili na sifa tunazoweza kufahamu. Nyingine za hizo ni sifa gani?
5 Je! umepata kuyatazama mawimbi makubwa sana ya bahari yakipiga kwa kishindo pwani yenye miamba-miamba? Au je! umepata kuziona kani nyingi ajabu za volkeno (mzima wenye kulipua moto)? Hivyo ni vionyesho vidogo tu vya uwezo ambao Muumba anao pasina shaka, kwa maana ndiye aliyeiumba dunia na nguvu zayo zote.
6 Kwa kutumia njia ya Einstein inayojulikana sana ya kuhesabu nishati, wanasayansi wanaeleza kwamba kitu chote ambacho ni tungamo (asili ya vitu vinavyoonekana) ni nishati zilizofungiwa katika atomi zile za msingi tu. Wanadamu wameonyesha ukweli wa jambo hilo kwa kulipua makombora yao ya atomi. Lakini je! wewe ulijua kwamba milipuko mikubwa ya namna hiyo inatokeza nishati za atomi zinazopungua asilimia moja (1%)? Ebu basi wazia Muumba aliyeziweka atomi zote katika ulimwengu mzima. Yeye ana uwezo wa kuogopesha kama nini! Maelfu ya miaka kabla Einstein hajazaliwa, Maandiko yalijulisha kwamba Mtu Aliye Mkubwa Kupita Wote ndiye chanzo cha nishati zilizo nyingi ajabu. (Isaya 40:29, NW) Basi Maandiko yana sababu nzuri ya kumwita “Mungu Mweza Yote.”—Mwanzo 17:1, NW; Ufunuo 11:17.
7 Mungu ametumia uwezo wake mara nyingi kwa njia ambazo zimewagusa wanadamu moja kwa moja. Mfano mmoja ni ule wakati wa Kutoka, Mungu alipomkomboa Musa na Waisraeli kutoka Misri. Ingefaa usome kwa sauti kubwa yale masimulizi mafupi yaliyo katika Kutoka 13:21-14:31. Ebu jione mwenyewe ukiwa kati ya wale wanaolindwa na nguzo ya wingu lenye kuogopesha sana wakati wa mchana na kulindwa na nguzo yenye kuwaka moto wakati wa usiku. Wewe ungalijisikiaje ilipoelekea kuwa jeshi lenye wafuatia lingewanasa kwa sababu mbele yenu kuna Bahari Nyekundu? Lakini, sasa ebu wazia, uone Mungu akitumia uwezo wake kuyafanya maji yawe kuta ndefu sana kila upande uweze kuokoka. Salaala! Mungu Mweza!—Kutoka 15:1, 2, 11; Danieli 4:35.
8 Wakati huo wa Kutoka ulionyesha pia uwezo Mungu wa kutimiza mambo akiwa mbali. Ili kufanya hivyo, yeye anatumia kani ya utendaji wake isiyoonekana, roho yake, au roho takatifu. Ingawa hiyo kani ya utendaji haina utu, inaweza kutokeza nguvu nyingi mfano wa mpulizo wa hewa wenye nguvu. Mungu alitumia roho yake kuumba ulimwengu mzima unaoonekana. (Zaburi 33:6; Mwanzo 1:2) Lakini anaweza pia kuitumia awatie watu nguvu na kuwasaidia —Waamuzi 14:5, 6; Zaburi 143:10.
9 Pasina shaka mtu anayebuni mwundo wa mashine kisha anaifanyiza ana maarifa ya kujua umbo mashine hiyo na kazi zayo. Kwa hiyo, je! vitu tunavyoviona duniani na mbinguni havituhakikishii kwamba Mungu ana maarifa mengi sana sana? Wanakemia wanatumia maisha yao yote wakijaribu kufahamu namna vitu vya asili vimefanyizwa. Basi Yeye aliyevifanyiza ana maarifa mengi kama nini! Pia, wana sayansi wanaichunguza chembe ya uhai na namna ndogo sana za uhai. Basi unaona! Ilikuwa lazima kwanza Muumba ayajue sana mambo hayo kutokeza uhai!
10 Maarifa ya Mungu yanaizidi mipaka yote ya ulimwengu mzima. Yeye anaweza kuyaita kwa majina mabilioni yote ya nyota alizoumba. (Isaya 40:26) Sehemu ndogo tu ya maarifa mengi mno ya Mungu ilipokwisha kutajwa-tajwa, mwanamume mmoja jina lake Ayubu aliungama hivi: “Sasa nimepata kujua kwamba wewe unaweza kufanya mambo yote, na hakuna wazo lisiloweza kuwazwa nawe.” (Ayubu 42:2 ,NW) Je! nasi hatuna sababu inayotosha kutufanya tujisikie ivyo hivyo?
11 Mungu pia ndiye mwenye kujaa hekima, kwa sa babu yeye anatumia maarifa yake kwa njia yenye matokeo mazuri. Kwa mfano, aliumba mimea kwa namna ya kwamba mimea hiyo inaweza kuunganisha maji na kaboni dayoksaidi kutoka kwenye hewa ili vitengeneze sukari za namna-namna na wanga wa namna-namna, hivyo vikiwa ni vitu ambavyo wanadamu na wanyama wanakula. Mimea inaweza pia kutengeneza mafuta ya namna nyingi sana protini za namna namna na vitamin tunazotumia kudumisha afya yetu. Chakula chote tuna chokula kinategemea kawaida ya kustaajabisha inayohusu jua, mvua, umeme wa mvua na bakteria (viini) zilizo katika udongo. (Yeremi 10:12; Isaya 40:12-15) Mtu anapoendelea kuyajua matendo ya Mungu, anakuja kuthamini moyoni sababu iliyofanya mwandikaji mmoja wa Biblia apaze sauti akisema: “Loo! zina kina kirefu kama nini, mali nyingi na hekima na maarifa ya Mungu!” (Warurr 11:33, NW) Je! hivyo sivyo ungetaka kujisikia juu ya Mungu unayeabudu?
MTU WA KUPENDEZA SANA
12 Ni jambo jepesi kuona kwamba Muumba ni mpaji mwenye kufikiria shida za watu ambaye anawapa vitu tele. Tumekwisha kutaja mambo kadha juu ya namna alivyopanga chakula kiwepo. Lakini mwandikaji mmoja wa zaburi za Biblia alisema hivi:
“Wewe uliziweka chemchemi zikichururika-chururika katika magenge, zikitiririka kati ya milima, zikitolea wanyama-mwitu maji, . . . Wewe wafanya nyasi mbichi-mbichi zikue kwa ajili ya mifugo na ile mimea inayotumiwa na wanadamu, wao wapate chakula udongoni: divai kuwafanya wachangamke, mafuta kuwafanya wafurahi na mkate kuwafanya wawe na nguvu.”—Zaburi 104:10-15, Jerusalem Bible.
Mungu aliitayarisha dunia kuweze kuwako chakula cha kuwatosha kabisa wanadamu wote. Ukosefu mwingi wa chakula unaoleta maafa mengi kwa kawaida unatokana na pupa ya wanadamu au usimamizi mbaya.
13 Muumba wetu hatutolei tu vitu tele tunavyohitaji ili tuendelee kuwa na uhai. Yeye anafanya uhai huo ufurahishe pia. Kama Mungu angalitaka, angaliweza kutupa sisi chakula chenye kujenga mwili kisicho na ladha yo yote. Lakini, tumepewa namna nyingi mno za ladha na harufu za kupendeza sana katika vyakula vyenye kuleta afya. Pia, tusisahau kwamba Mungu alitufanya tuweze kufurahia upendezi wa rangi mbali-mbali, kama za maua na matunda. Kisha alitupa uwezo wa kufurahia mpigo wa muziki. Mambo hayo yote yanakufanya wewe uwe na maoni gani juu ya Mungu?
14 Kwa kufikiria hayo, watu wengi wameguswa moyoni wakakata kauli kwamba pasina shaka Mungu ni mwenye upendo mwingi sana. Wanasadiki ndivyo alivyo. Biblia nayo inakubali, kwa maana mtume Yohana aliandika hivi: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Muumba ndiye kifano halisi cha upendo; hiyo ndiyo sifa yake iliyo kuu. Kama mtu fulani angekuomba umweleze Mungu yuko namna gani, inaelekea kwamba ungeitaja sifa hiyo kabla ya nyinginezo. Yeye anaonyesha wanadamu shauku yenye upendo. Mungu ni mtu halisi mwenye kuwakaribia wanadamu. Ni mtu mwenye huruma nyingi ambaye tunaweza kuhusiana naye kwa upendo. Yesu alisema wafuasi wake wangeweza kupelekea Mungu sala akiwa ndiye Baba yao, mtu mwenye kuwapenda sana na kupendezwa nao.—Mathayo 6:9.
15 Kama unapenda mtu fulani kweli kweli, unamtakia mema. Ndivyo Mungu anavyojisikia juu ya wanadamu. Kwa sababu ya kutupenda anatuonya tusishike vitu vinavyoweza kutuumiza. Maonyo anayotutolea yanatulinda. Pia, yanatusaidia tufahamu viwango vya Mungu na kutujulisha namna atakavyotenda au atakavyojisikia tukifanya hivi au vile. Kwa mfano, Biblia inatuambia anachukia kusema uongo. (Mithali 6:16-19; 8:13; Zekaria 8:17) Jambo hilo linatuhakikishia kwamba Mungu mwenyewe hawezi kusema uongo; tunaweza kuamini kila jambo analosema. (Tito 1:2; Waebrania 6:18) Kwa hiyo tunaposoma maneno fulani ya Biblia ambayo huenda mtu akaona yana sheria zinazomzuia kufanya anayotaka, inatupasa tutambue yanaonyesha Mungu ana utu wenye upendo na uadilifu na anapendezwa nasi.
16 Ikiendelea kutusaidia tumwone Mungu kuwa mtu tunayeweza kuhusiana naye, Biblia inaonyesha kwamba ana maoni ya moyoni, wala si upendo tu. Kwa mfano, ‘aliona maumivu’ wakati mwanadamu alipoasi njia zake za uadilifu. (Zaburi 78:8-12, 32, 41, NW) Yeye ‘anafurahi wanadamu wanaposhika sana yaliyo haki. (Mithali 27:11; Luka 15:10) Tunapofanya makosa, ni mwenye huruma na rehema na anafahamu kwa nini makosa yanaweza kutokea. Utatiwa moyo ukisoma hivyo kwenye Zaburi 103:8-14. Tena Muumba hana upendeleo, bali anawapa watu wote jua na mvua, na anakubali jamii zote tu za watu au mataifa yote tu wamwabudu yeye.—Matendo 14:16, 17; 10:34, 35.
17 Wengi wetu wanataka furaha. Basi inafaa tumjue Aliye Juu Zaidi. Biblia inamtaja kuwa “Mungu wa furaha” na kuonyesha kwamba anataka sisi tufurahi. (1 Timotheo 1:11, NW; Kumbukumbu la Torati 12:7) Daima yeye anawapa thawabu wale wanaomwamini. (Waebrania 11:6; 13:5) Naye Mungu ametayarishia wanadamu njia ya kuwa wenye afya na furaha bila mwisho, kama tutakavyozungumza katika sura za baadaye.
“YULE” MUNGU
18 Jambo jingine la maana ambalo Biblia inafunua juu ya Muumba ni kwamba ana jina la kibinafsi. Katika Kiebrania jina hilo liliandikwa kwa konsonanti (herufi bubu) nne, kama hivi: Lugha nyingi za ki-si-ku-hizi zinalitafsiri jina hilo la pekee kwa njia zinazolingana. Katika Kiswahili ni Yehova. Zaburi 83:18 inatuambia kwamba watu wanapaswa ‘kujua ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako Yehova, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.’ (Linganisha Yohana 17:6.) Angalia kwamba hapo panasema yeye peke yake ndiye Aliye Juu Zaidi. Kuna mmoja tu aliye Mtu Mkubwa Kupita Wote. Mara nyingi Waisraeli wa kale walilitaja jambo hilo hivi: “Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja. Na wewe lazima upende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na nafsi yako yote na kani zote za uhai ulizo nazo.”—Kumbukumbu la Torati 6:4, 5 NW; linganisha Yohana 17:3.
19 Yehova, Mungu wetu, hawekewi mipaka na wakati, nasi tukitumia akili zetu tunaona hilo wazi. Wanasayansi wanasema ulimwengu mzima ulitokea maelfu ya mamilioni ya miaka iliyopita. Kwa hiyo ni wazi kwamba Muumba wa ulimwengu huo alikuwako kabla haujatokea. Jambo hilo linapatana na vile Biblia inavyomtaja, yaani, “Mfalme wa umilele,” asiye na mwanzo wala mwisho. (1 Timotheo 1:17, NW; Ufunuo 4:11; 10:6) Maelfu machache ya miaka ambayo mwanadamu amekuwapo duniani ni kidakika (kitambo kidogo) tu kinapolinganishwa na umilele-umilele wa Yehova.—Zaburi 90:2, 4.
WATU WENGINE TUSIOWEZA KUONA
20 Biblia inafunua kwamba kuna watu wengine pia walioumbwa wakiwa roho. Mweza Yote alipomaliza muda mrefu wa kuwa pekee, alichagua kuumba watu wengine wa kiroho. Kwanza kabisa, alimtokeza aliye “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote” na “mwanzo wa kuumba kwa Mungu.” (Wakolosai 1:15; Ufunuo 3:14) Mzaliwa wa kwanza huyo alikuwa pamoja na Mungu Mweza Yote katika mwanzo wa uumbaji. Baadaye Yehova angemtumia awe mneni, au Neno, katika kupasha wengine habari. (Yohana 1:1-3; Wakolosai 1:16, 17) Hatimaye, Mwana huyu mzaliwa wa kwanza alitumwa duniani akawe mwanadamu. Anaitwa Yesu Kristo.—Wagalatia 4:4; Luka 1:30-35.
21 Akifanya kazi kwa kumtumia Mwana huyu aliyekuwa wa kwanza kuumbwa, Mungu alifanyiza viumbe wengine wa kiroho, ambao kwa ujumla wanajulikana kuwa malaika. Wanamtumikia Mungu wakiwa wajumbe wake wa kupeleka habari na kufanya kazi mbalimbali katika ulimwengu mzima, kutia na utumishi mbalimbali kwa ajili ya wanadamu.—2 Petro 2:11; Waebrania 2:6, 7; Zaburi 34:7; 103:20.
22 Kufikiri kuzuri na hata Biblia vinaonyesha kwamba Mwana mzaliwa wa kwanza aliyeumbwa na kutumwa na Mungu duniani asingekuwa sawa na Baba yake katika cheo. Watu fulani wanaosema wanaamini Biblia wanafundisha kwamba Yesu na Baba yake ni sehemu zinazolingana cheo za uungu ulioungana pamoja. Hilo si wazo jipya, kwa maana dini nyingi za kale ziliabudu vikundi-vikundi vya miungu. Lakini kinyume cha hilo, Biblia inasema waziwazi kwamba Yesu, akiwa mtu aliye kando, alipokea mamlaka kutoka kwa Baba yake mweza yote. Inatuhakikishia kwamba Mweza Yote alijua mambo asiyoyajua Yesu, na kwamba Yesu Kristo hajapata kuwa na cheo kinacholingana na cha Baba yake, alipokuwa duniani wala baada ya hapo.—Yohana 5:30; 8:28; 14:10, 28; Marko 13:32.
23 Mwana aliendelea kuwa na uhusiano wa karibu na Mungu Mweza Yote kwa maelfu ya miaka huko mbinguni, na hivyo aliweza kujifunza mambo kwa Mungu na kuiga njia zake. Ndiyo sababu mwanafunzi mmoja aliposema, “utuonyeshe Baba,” Yesu alimjibu hivi: “Aliyeniona mimi amemwona Baba.” (Yohana 14:8, 9; 1:18) Tukijifunza masimulizi ya Biblia juu ya maisha ya Yesu ya kidunia tunaweza kujua mambo mengi juu ya Baba, kama sababu inayofanya Mungu atende shughuli fulani na namna anavyotutazamia tuwe. Wakati mmoja Yesu alisema: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima.” (Yohana 14:6) Ni jambo la maana kabisa tupate kumjua yeye vizuri zaidi, na hivyo tupate kumjua Baba pia. Kuisoma Injili ya Yohana ni msaada bora kabisa. Unapoisoma, usikaze fikira zako juu ya matukio tu bila kujali yanakusaidiaje, bali jaribu kuingiwa sana na nia ambayo Kristo anaonyeshwa alikuwa nayo. Yeye alikuja kuwa ndiye mwanadamu wa maana zaidi unayeweza kujifunza habari zake.
TUNAMHITAJI MUNGU
24 Tunapojifunza juu ya Mweza Yote kwa kuutazama sana uumbaji na kuisoma Biblia, inakuwa wazi kwamba wanadamu hawakuumbwa wakae bila kumtegemea yeye. Tuliumbwa tuwe na uhusiano pamoja na Mungu. Ndiye ametupa sisi uhai na misaada ya kila siku inayoendeleza maisha zetu. Kujaribu kuacha kumtegemea yeye na Neno lake, Biblia, kunaweza kulinganishwa na mtu anayetafuta njia atakayopitia katika jangwa asilolijua, bila ramani nzuri ya kumwongoza. Baada ya muda fulani huenda akapotea kabisa na kufa kwa kukosa mahitaji ya kuendelezea uhai wake. Ndivyo inavyokuwa wakati wanadamu wanapomsukuma mbali Mungu na uongozi wake kutoka maishani mwao. Biblia na historia vinatuhakikishia kwamba si chakula tu, si mavazi wala makao tu tunayohitaji ili kupata furaha bora kabisa maishani. Ili tufurahi kweli kweli, tunahitaji uongozi na msaada wa Mfanyi wetu.—Mathayo 4:4; Yohana 4:34.
25 Watu wengine wengi wanajua machache tu juu ya Muumba. Unapoonana nao na kupata nafasi, jaribu kuwaeleza mengine ya mambo mazuri ambayo tumezungumza humu. Inakuwa vizuri watu wanapokuwa na nia ya kuzungumza na wenzao kweli za maana ambazo wamejua juu ya Yehova, Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo.—Zaburi 40:5.
[Mambo ya Kuzungumizwa]
Inawezekanaje kujua habari za Mungu asiyeonekana? (1-3)
Sababu gani unaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu ana uwezo wa kuogopesha sana na kwamba anaweza kuutumia? (4-8)
Inatupasa tujue nini juu ya maarifa ya Mungu? Nanma gani hekima yake? (9-11)
Wewe unafaidikaje na maonyesho ya utu wa Mungu? (12-14)
Ni kwa njia gani Mungu anaonyesha anapendezwa nawe kwa upendo? Basi wewe unajisikiaje? (Zaburi 30:4, 5) (15-17)
Tunaweza kujua nini juu ya jina la Mungu na urefu wa maisha yake? (18, 19)
Kwa sababu gani Mungu hayuko peke yake mbinguni? (20, 21)
Kuna uhusiano gani kati ya Baba na Mwana? (22, 23)
Sababu gani Mungu awe wa maana katika maisha yako? (24, 25)
[Picha katika ukurasa wa 33]
Uwezo wa Mungu uliyatenganisha maji ya Bahari Nyekundu
[Picha katika ukurasa wa 36]
Jua, mvua na udongo wenye mazao vinaonyesha nini juu ya Mungu?
Je! si kweli kwamba yeye ni Mpaji wa vitu tele, mwenye upendo?