Sura ya 5
Unaweza Kushindana na Matatizo ya Maisha
“MAISHA yamejawa na matatizo,” watu wanasema. Labda utakubaliana nao.
2 Matatizo (magumu) ya kifedha yamewakaba sana watu wengi—deni, infuleshoni, wasiwasi wa kufutwa kazi, au shida ya kupata nyumba nzuri. Ni jambo la kawaida sana kuona watu wakiwa na matatizo makubwa ya ndoa na jamaa. Ngono, pombe au dawa za kulevya ni matatizo ya vijana wengi. Nayo afya mbaya inatatiza sana walio wazee-wazee. Mambo yote hayo yanaongezea watu wasiwasi mwingi na mikazo.
3 Ni kwa kadiri gani wewe unashindana na matatizo ya maisha? Habari zinazotangazwa juu ya halI ya kushuka moyo na visa vya watu kujiua wenyewe zinaonyesha kwamba watu wengi wanashindwa kabisa kutatua matatizo yao. Lakini kuna mamilioni wengine wasiokosa usawaziko wa akili wanapokabiliwa na misiba. Kwa nini?
4 Hao wa pili wamejifunza kutegemea maoni ya Muumba wa wanadamu yaliyo katika Biblia. Hakuna msaikolojia ye yote (mwenye kuchunguza fikira za watu), hakuna mshauri wa mambo ya ndoa, wala mwandishi mwenye kushauri watu magazetini anayejua mambo mengi ya maisha kuliko Mungu. Yeye ndiye aliyewaumba watu wale wa kwanza, kwa hiyo ana maarifa mengi kabisa juu ya namna sisi tulivyo katika mwili, akili na mioyo yetu. (Zaburi 100:3; Mwanzo 1:27) Yehova anajua mambo yanayotendeka ndani yetu na sababu tunafanya hivi na vile, kuliko mwanadamu ye yote mwenye maisha mafupi.—1 Samweli 16:7.
5 Tena, yeye anayafahamu matatizo yanayotupata katika ulimwengu huu zaidi ya ye yote kati yetu. Tangu wakati wa yule mtu wa kwanza, wala si kwa muda wa miaka michache tu, Yehova amekuwa akiyachunguza matatizo yote ya wanadamu. Biblia inatuambia: “Toka mbinguni [Yehova] huchungulia, huwatazama wanadamu wote pia. . . . Huwaangalia wote wakaao duniani. . . . Huzifikiri kazi zao zote.” (Zaburi 33:13-15) Ndiyo kusema yeye anajua ni njia gani ya kushindana na matatizo yetu iliyo na matokeo mazuri au mabaya.
6 Yeye anatuwezesha kwa ukarimu mwingi tufaidike na maarifa na ujuzi wake wa maisha. Biblia ina mashauri yake, nayo yamepangwa kwa njia yenye kuyafaa mahitaji yetu hata tuwe tuna hali gani maishani na tunaishi wapi. Ni kama inavyosema Zaburi 19:7-11: “Sheria ya [Yehova] ni kamilifu, huiburudisha nafsi. Ushuhuda wa [Yehova] ni amini, humtia mjinga hekima.”
7 Acha tuangalie kwa ufupi ni namna gani shuhuda hizo zinaweza kusaidia mtu ashindane na matatizo ya kibinafsi, yaani, mkazo mkali sana na upweke. Tukiisha kuangalia msaada wenye mafaa unaotolewa na Biblia kuhusiana na mambo hayo, tutachunguza matatizo mengine yanayopata watu wengi—kuhusu fedha, ndoa na dawa za kulevya.
UNAWEZA KUSHINDANAJE NA MIKAZO?
8 Ni watu wachache ambao, wakiulizwa, watasema hawapatwi kamwe na mikazo mikali. Kadiri matatizo ya kila mmoja wetu yanavyozidi kuongezeka—kuhusu fedha, jamaa, ngono, uhalifu—ndivyo mikazo inavyozidi kuwa mikali. Habari za hivi majuzi za gazeti zilieleza kwamba kinachoonyesha nyakati hizi zetu ni za namna gani, si namna watu wanavyotenda wala namna wanavyovaa mavazi. Bali ni “yale maoni ya kuwa na wasiwasi mwingi sana.”
9 Je! wewe ulijua kwamba mikazo inaweza hata kufupiza maisha yako? Angalia:
“Mikazo inatokana sana-sana na mambo ambayo akili zinafikiria sana katika maisha ya sasa, nayo imebandikwa jina la kuitwa ‘Mwuaji wa Karne ya Ishirini.’ Kwa wakati huu magonjwa ya kimwili yanayoongezwa na mikazo hiyo yanafanya watu wengi wapelekwe hospitali na wengi wafe kila mwaka—watu wasiopungua makumi ya mamilioni.”—Gazeti la Kiafrika la habari, To the Point.
“Mikazo mikali au ile yenye kuchukua muda mrefu inaweza kudhoofisha mwili hata kuufanya uwe rahisi kupatwa na maradhi mengi, ya vipele-vipele na mafua hata ugonjwa wa moyo na kansa.”—The Wall Street Journal, U.S.A.
Hata vitoto ambavyo havijazaliwa vinapatwa na magonjwa. Mikazo inayopata wanawake wenye mimba, kama ile inayoletwa na magombano katika ndoa au wasiwasi wa kukosa kazi ya kuajiriwa, inaweza kuharibu vitoto mwilini, akilini na katika maoni ya moyoni vikiwa katika tumbo la uzazi.
10 Mikazo inaleta uharibifu pia kwa sababu inatokeza matatizo mengine. Inafanya watu wengi wapoteze wakati wa kufanya kazi, na hapo matatizo yao ya kifedha yanaongezeka. Mikazo inatokeza jeuri, hata katika ndoa. Mume mmoja aliandika hivi:
“Kila siku mimi ninapatwa zaidi na mkazo na kuwa na wasiwasi mwingi. Najisikia nikitaka kumrushia kila mtu maneno naye mke wangu ndiye hukiona cha-mtema-kuni mara nyingi. Najisikia nikitaka kulewa, lakini hakunifai kitu.”
11 Mikazo mingine ni kawaida tu ya maisha, wala si mibaya nyakati zote. Kuamka kitandani asubuhi kunaleta mkazo, kama vile kutazama mchezo mzuri wa mpira. Mkazo unaoharibu mwili wa mtu ni ule unaomwuma sana, ule wa muda mrefu (au, dhiki). Bila shaka, huenda mingi ya mikazo yetu ikaelekea kuwa isiyoepukika, kwa kuwa inahusu watu wengine au hali katika maisha yetu wenyewe. Hata hivyo, je! kuna jambo tunaloweza kufanya tuepuke mkazo wenye kuumiza mwili? Tukiweza kushindana na mikazo vizuri zaidi, huenda matatizo mengine yakapungua, kama yale yanayoharibu afya yetu.
12 Njia ya kushindana na mikazo ilionyeshwa na mwanamume mmoja anayetambuliwa ulimwenguni pote kuwa mmoja wa walimu wakubwa zaidi waliopata kuishi, yaani, Yesu Kristo. Alipoulizwa ni amri ipi iliyo ya maana zaidi kati ya amri zote za Mungu, Yesu alijibu, ‘Lazima umpende Yehova kwa moyo wako wote, nafsi yote na akili zote. Na lazima umpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’ (Mathayo 22:37-39, NW) Fanya kama alivyosema, nawe utapata msaada wa kushindana na mikazo.
13 Kwa mfano, ukitendea mwenzi wako wa ndoa au watu wa ukoo kwa upendo, inaelekea sana amani itaongezeka. Hali ya kuoneana uchangamfu na kufurahiana itasitawi. Wasiwasi utapungua. Ndiyo, shauri hilo la Kimaandiko likifuatwa mikazo inaweza kuwa michache.
14 Lakini jambo hilo halihusu jamaa tu. Bali unapotumia maoni ya Biblia juu ya kuonyesha upendo—pamoja na ile kanuni bora ya kutendea wengine kama vile ungependa wao wakutendee—watu watazidi kukupenda. (Luka 6:31) Ndivyo imekuwa kazini, shuleni, mtaani. Ndi-yo-o, huenda matata madogo ya kugombana yakawako, lakini ni machache zaidi. Ni wazi kwamba ukifanya hivyo mikazo yako itapungua.
15 Hata wanasayansi wanazidi kuthamini kwamba mapendekezo ya Biblia yanasaidia watu wapunguze mikazo na kushindana nayo. Profesa Hans Selye (wa Chuo Kikuu cha Montreal), aliye mmoja wa wataalamu wenye kujua zaidi mambo yanayoletwa na mikazo, alishauri hivi:
“Badala ya kutegemea dawa za kulevya au njia nyinginezo, mimi nadhani kuna njia nyingine bora ya kushughulika na mikazo, nayo ni kuyafikiria kwa njia tofauti matukio mbalimbali ya maishani mwetu.”
Yeye alikazia uhitaji wa kutafuta “namna ya tabia ambazo watu wanaweza kufuata maishani mwao,” na ikitukia hivyo ‘jamii ya wanadamu kwa ujumla ingefaidika zaidi ya vile ingefaidika kukiwa na uvumbuzi wa kitu kingine cho chote.’ Tabia gani? Baada ya kutumia miaka 40 akichunguza mambo yanayoleta mkazo, yeye alisema utatuzi wa tatizo hilo ulionekana kuwa—upendo.
16 Kwa nini kuonyesha upendo kama Biblia inavyopendekeza, hata katika maisha ya kila siku, kunaleta mafaa mengi sana? Kwa nini matokeo ni mazuri? Dakt. Selye alisema:
“Maoni mawili ya moyoni yanayoondoa au yanayoleta mikazo ni upendo na chuki. Biblia inalitaja-taja jambo hilo mara nyingi. Maana ni kwamba tusiporekebisha kwa njia fulani uchoyo tunaozaliwa nao, tunachochea woga na uhasama katika watu wale wengine. . . . Tutakavyozidi kuwasadikisha watu watupende badala ya kutuchukia, ndivyo tutakavyopata usalama zaidi, na mikazo yetu kupungua zaidi.”
17 Hasira ni kisababishi kingine cha mikazo. Nyakati fulani-fulani sisi sote tunakasirika, na Biblia inataja wazi hivyo. Hata hivyo inashauri hivi: “Asiye mwepesi wa hasira ni mwema kuliko shujaa; na mtu aitawalaye roho yake kuliko mtu atekaye mji.” (Mithali 16:32; Waefeso 4:26) Kwa hiyo tukikasirika, tukumbuke Mungu anatuonya tusihamaki wala kufoka kwa hasira. Mara nyingi watu wanaoyapuza maoni hayo wanaropoka-ropoka maneno machafu au kujitia katika mapigano yenye jeuri nyingi. Basi nyakati nyingine wanaumizwa au wanawekea watu undani (kinyongo), na hivyo mikazo inawauma muda mrefu. Kwa hiyo, kadiri uwezavyo kuyafuata maoni ya Biblia yenye hekima na mafaa kuhusu hasira, utasaidika ushindane na mikazo.
18 Biblia inatusaidia tupunguze mikazo kwa kututia moyo pia tutende mambo ya namna nyingi na kuwa na usawaziko maishani. Watu wengine wakishika kazi haiwaondoki mikononi, na wengine wanafanya kazi mara chache sana. Watu wengine hawacheki. Wengine ni mswaki kucheka. Lo lote kati ya mambo hayo linapita kiasi kinachofaa, na linaelekea kutokeza matatizo mengi na mikazo. Walakini, yasome maelezo ya Mhubiri 3:1-8, mahali anaposema Mungu kuna wakati wa kila utendaji. Kumbe, Biblia ina maoni yenye kiasi kinachofaa na pia yenye usawaziko zaidi kuhusu maisha. Afadhali kazi kuliko uvivu. Biblia inahimiza watu pia wajistareheshe kiasi na kufurahia matunda ya kazi yao. (Mhubiri 3:12, 13; 10:18; Mithali 6:9-11) Tutapata faida tukitumia wakati fulani kufikiria kwa uzito kusudi la maisha na namna ya kuishi. Lakini kuna ubora wa kujistarehesha pia pamoja na jamaa na rafiki. Tukiweza kufuata sana mashauri ya Biblia juu ya usawaziko, hatutakuwa na mikazo mingi.
KUSHINDANA NA MAUMIVU MAKALI YA UPWEKE
19 “Upweke ni jambo la ulimwenguni pote,” ndivyo alivyosema Henry Regehr anayeshughulika na matatizo yanayopata jamii za watu mitaani. “Wewe simamisha mtu ye yote tu barabarani kisha umwambie ‘nieleze habari za upweke wako,’ nawe utasimuliwa hadithi isiyofikia kikomo.” Katika uchunguzi wa maoni ya watu wengi uliofanywa kwa kuzungumza na watu 52,000, zaidi ya asilimia (%) 40 walisema ‘mara nyingi wanajisikia wapweke.’ Kujisikia hivyo ndiko kuliwaletea masumbufu ya daima na kuwaharibia furaha. Upweke haubagui watu. Unapata wazee kwa vijana, wanaume kwa wanawake. Ingawa huenda tukadhani kwamba mtu asiye na mwenzi wa ndoa, kama mjane, ndiye mwenye upweke hasa, kati ya watu wengi zaidi walio na upweke mwingi leo ni wale waliooana lakini wasiweze kupashana habari.
20 Watu wengi wanajaribu kuzuia upweke kwa kufanya ngono za haramu, kulewa au kula kupindukia. Lakini visababishi vya upweke wao bado vinabaki. Jambo moja linalouleta ni kuongezeka kwa watu katika majiji, ambako unaweza kuwa na majirani wengi na bado ujisikie mpweke kabisa. Kuvunjika-vunjika kwa ndoa nyingi kumeliongeza tatizo hilo. Hata televisheni inaelekea kuongeza upweke kwa sababu inamalizia watu wakati wa mazungumzo.
21 Ni jambo gani linaloweza kufanywa lisaidie kushindana na upweke? Ingawa hatutaki kulifanya tatizo lenyewe lionekane kuwa jepesi mno, inaweza kusemwa kwamba Biblia inaweza kusaidia mtu ye yote ashindane vizuri zaidi na upweke. Kwa nini? Kwanza, mara nyingi upweke unafanya mtu ashuke moyo na kuacha kujiheshimu. Mtu huyo anaweza kuburudika moyoni akisitawisha uhusiano mwema na Muumba wake. Anaweza kusitawisha hali kubwa zaidi ya kujiona anafaa akifahamu kwamba Mungu anapendezwa naye, kisha anaweza kuanza kutazamia mema maishani. (Mathayo 18:10) Zaidi ya hilo, Biblia inawaonyesha Wakristo njia ya maisha inayoweza kuwasaidia kuondoa upweke.
22 Mara nyingi watu wenye upweke wanaambiwa ‘wajishughulishe.’ Kufanya hivyo kuna ubora fulani. Lakini Biblia inatoa maoni yenye mafaa zaidi. Inawahimiza Wakristo wawe watendaji katika kufanya mema kwa ajili ya wengine, na hilo pia linaleta furaha. (Matendo 20:35) Dorkasi alifanya hivyo, akatumia wakati wake akitengenezea Wakristo wenzake vitu fulani, wengi wao wakiwa ni wanawake wajane. Jitihada zake ziliwasaidia kimwili, na inaelekea pia ziliwasaidia kushinda upweke. Kwa upande mwingine Dorkasi mwenyewe hakuwa mpweke bali alipendwa. Unaweza kufurahia kusoma habari zake katika Matendo 9:36-42.
23 Utendaji ambao umefaidi sana Wakristo wengi ni kusaidia watu wengine wamjue Mungu na Biblia. Kwa kweli, mtume Paulo alisema kwamba kuwa na uhuru mwingi wa kufanya hivyo kungefaidi waseja, na bila shaka wangesaidika washindane na upweke pia. (1 Wakorintho 7:32-35) Paulo mwenyewe ni mfano wa waseja hao. Soma katika Matendo 17:1-14 uone namna Paulo alivyozidi kuwa na kazi nyingi akisaidia watu wengi katika mji wa Thesalonike, ajapopatwa na upinzani mkubwa ajabu. Halafu sasa angalia urafiki mwingi sana uliotokea kati yao, kama unavyotajwa katika 1 Wathesalonike 2:8. Mamia ya maelfu ya Mashahidi wa Yehova leo wanaweza kuthibitisha kwamba kujishughulisha kufundisha wengine Biblia kuna faida nyingi sana.
24 Pia, Mashahidi wa Yehova wanakutana kwa ukawaida wakiwa vikundi-vikundi wajifunze Maandiko. Wanapojifunza, wanafurahia ushirika mchangamfu wa Kikristo. Ndiyo, kuwa karibu tu na watu wengine hakuondoi upweke, na watu wengi mijini wanajua hivyo. Lakini wale wanaohudhuria mikutano hiyo ni Wakristo wanaojitahidi kufuata kwa moyo kipa-moyo cha Biblia cha kwamba wapendezwe na wenzao kikweli. (Wafilipi 2:4) Mikutano hiyo ni yenye kuchangamsha na kufurahisha. Wahudhuriaji wanajiunga pamoja katika kumtolea Mungu sala fupi, na watu wengi wamesaidiwa na hilo kujua hawako peke yao. (Yohana 16:32) Tunakutia moyo uhudhurie mkutano wo wote wa Mashahidi wa Yehova. Utaweza kuona namna kufuata maoni ya Biblia kunavyosaidia watu wengi washindane na upweke na matatizo mengine, ka-ma yale yanayohusu fedha au jamaa.
[Mambo ya Kuzungumziwa]
Tuna sababu gani za kutazamia kwamba matatizo ya maisha yanaweza kutatuliwa? Mungu anahusikaje? (1-7)
Tatizo la mikazo ni kubwa kadiri gani? (8-11)
Mashauri ya Biblia yanaweza kutusaidiaje tushindane na mikazo? (12-14)
Ni jambo gani ambalo wanasayansi wamejua juu ya mashauri ya Biblia yanayohusu upendo? (15, 16)
Ni kwa njia gani nyingine mashauri ya Biblia yanavyoweza kutusaidia tushindane na mikazo? (17, 18)
Upweke ni tatizo lenye ukubwa gani? (19, 20)
Ni shauri gani la Biblia linaloweza kusaidia mtu ashindane na upweke? Kwa njia gani? (21-23)
Ushirika wa Kikristo una ubora gani? (Mhubiri 4:9, 10) (24)
[Sanduku katika ukurasa wa 45]
HALI ZA MAISHA ‘ZINAZOJAA MIKAZO ZAIDI’
NAMBA TUKIO LA MAISHA
1 Kifo cha mwenzi wa ndoa
2 Talaka
3 Mtengano wa ndoa
4 Kifungo gerezani
5 Kifo cha mwanajamaa
6 Kuumia mwilini au kuwa mgonjwa
7 Ndoa
8 Kufutwa kazi
9 Kufanya upya mapatano ya ndoa
10 Kustaafu
11 Badiliko la afya ya mwanajamaa
12 Mimba
13 Matatizo ya ngono
14 Kuzaliwa kwa mtoto mwingine
15 Marekebisho mapya ya kikazi
Habari hizi zinategemea uchunguzi uliofanywa na Madakt. T. Holmes na R. H. Rahne—“Modern Maturity.”
[Sanduku katika ukurasa wa 50]
“Katika maisha yao wenyewe ya kikundi Mashahidi ni jamii ya watu wenye kutumainiana na kukubaliana kikweli. . . . Mashahidi wa Yehova wanaonyesha [mtu] maarifa mapya ya maisha yanayowapa wafuasi njia ya kutambuliwa na wenzao na kujiheshimu wenyewe, kukubaliwa na wale wengine, na kupata tumaini la waati ujao.”—“Religious Movements in Contemporary America.”
[Picha katika ukurasa wa 41]
INFULESHONI
MAGONJWA
WASIWASI WA KUFUTWA KAZI
MATATIZO YA KIJAMAA
UKOSEFU WA NYUMBA
[Picha katika ukurasa wa 49]
Kutumikia wengine, kama Dorkasi, kunasaidia kuzuia upweke