Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • hp sura 11 kur. 103-111
  • Magonjwa na Kifo—Sababu Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Magonjwa na Kifo—Sababu Gani?
  • Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KISABABISHI CHA MAGONJWA NA KIFO
  • “UKOMBOZI” NI NINI?
  • NI KWA NJIA GANI TUNAWEZA KUSAMEHEWA DHAMBI ZETU?
  • WEWE UTAFANYA NINI?
  • Fidia​—Zawadi Bora Kutoka kwa Mungu
    Biblia Inatufundisha Nini?
  • Fidia—Zawadi Bora Zaidi Kutoka kwa Mungu
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Fidia ya Kristo Njia ya Mungu ya Wokovu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Kifo cha Yesu Chamaanisha Nini Kwako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Furaha​—Namna ya Kuipata
hp sura 11 kur. 103-111

Sura ya 11

Magonjwa na Kifo​—Sababu Gani?

HATA watu wafanye nini kutunza afya yao, bado wanazidi kuzeeka, wanakuwa wagonjwa na mwishowe wanakufa. Hakuna mtu anayeweza kuepuka mambo hayo. Hata watu waliojitolea sana utumishi wa Mungu walishindwa kuyaepuka. (1 Wafalme 1:1; 2:1, 10; 1 Timotheo 5:23) Sababu ni nini?

2 Chembe za miili yetu zinaonekana kuwa zenye uwezo wa kujitengeneza upya zichukue mahali pa zile zilizokwisha nguvu. Zinaweza kufanya hivyo kwa muda mrefu kuliko zinavyofanya sasa, na ubongo wetu una nafasi kubwa zaidi ya ile tunayoweza kutumia muda wa vipindi vingi sana vya maisha. Sababu gani iwe hivyo ikiwa hatukukusudiwa tutumie vitu hivyo kwa muda mrefu hivyo? Kusema kweli, wanasayansi hawawezi kueleza kwa nini tunazeeka, tunakuwa wagonjwa kisha tunakufa. Lakini Biblia inaeleza.

KISABABISHI CHA MAGONJWA NA KIFO

3 Mtume Paulo anatuelekeza upande unaofaa, akisema: “Katika Adamu wote wanakufa.” (1 Wakorintho 15:21, 22) Hapo Paulo anataja masimulizi ya Biblia juu ya Adamu na Hawa, na Yesu aliyathibitisha masimulizi hayo kuwa kweli. (Marko 10:6-8) Muumba alikuwa ameweka mwanamume na mwanamke wa kwanza katika makao ya kibustani, wakiwa na taraja lenye furaha la kuishi kupatana na mapenzi yake bila kufa. Walikuwa na chakula cha kutosha chenye kuwapa afya kutokana na miti mbalimbali na mimea mingine-mingine. Isitoshe, Adamu na Hawa walikuwa watu wakamilifu. Akili na milli yao haikuwa na kasoro, tena hakukuwa na sababu ya vitu hivyo kuharibika, kama inavyokuwa sasa kwa wanadamu.—Kumbukumbu la Torati 32: 4; Mwanzo 1:31.

4 Ni kizuizi kimoja tu walichowekewa hao watu wawili wa kwanza. Mungu alisema: “Walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:17) Kwa kufuata kizuizi hicho, wangeonyesha waliikubali mamlaka ya Mungu ya kuamulia wanadamu mema na mabaya. Baadaye, walijiwekea kanuni zao wenyewe za kuamulia mema na mabaya. (Mwanzo 3:6, 7) Wakatenda kile kinachoitwa na Biblia “dhambi,” kwa kutokuitii amri ya Mungu aliyoitaja waziwazi. Katika lugha zote mbili, Kiebrania na Kigiriki, “kutenda dhambi” maana yake ni “kukosa [shabaha unayolenga].” Adamu na Hawa waliikosa shabaha (lengo) au wakapungukiwa na utii mkamilifu. Sasa hawakuonyesha tena ukamilifu wa Yehova, basi wakajiletea hukumu ya Mungu yenye haki.—Luka 16:10.

5 Dhambi ya Adamu na Hawa iliwaumiza wao na sisi pia. Sababu gani sisi tuumie? Ni ya kwamba Mungu hakuwaua moja kwa moja. Yehova aliyafikiria mambo yote yaliyohusika, akawaruhusu hao watu wawili wa kwanza wazae watoto. Lakini sasa Adamu na Hawa hawakuwa wakamilifu tena; walipotenda dhambi walianza kuharibika miili na akili. Basi wasingeweza kuzaa watoto wakamilifu. (Ayubu 14:4) Hali hiyo inaweza kufananishwa leo na hali ya watu wawili waliooana ambao wanapitishia watoto wao kasoro za kimwili zinazohusiana na urithi. Sisi tuliirithi kasoro ya dhambi, kwa maana shina letu sote ni wale wazazi wawili wasiokuwa wakamilifu. Paulo anatoa maelezo haya: “Kwa njia ya mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia ulimwenguni, nayo ikasababisha kifo. Hivyo kifo kimeenea katika jumuiya yote ya binadamu, kwa maana wote wametenda dhambi.”—Waroma 5:12, Habari Njema kwa Watu Wote; Zaburi 51:5.

6 Je! hali yenyewe ilikosa tumaini kabisa? Mambo ambayo yametendeka katika historia, na hata Biblia, yanahakikisha kwamba kama wanadamu ndio wangaliachwa wajitengenezee mambo, kusingekuwa na tumaini hata kidogo. Sisi hatuwezi kujisafisha doa la dhambi lililotupata wala hatuwezi kujifungua katika laana iliyotoka kwa Mungu. Kama tulipaswa kufunguliwa tuwe huru, Mungu ndiye angetufungua. Sheria yake ndiyo iliyovunjwa, basi Yeye ndiye aliyepaswa kuamua namna haki iliyo kamilifu ingeweza kutimizwa kisha tufunguliwe. Yehova Mungu alionyesha fadhili zisizostahilika kwa kutoa msaada wa kufungua wazao wa Adamu na Hawa, kutia na sisi. Biblia inaueleza msaada huo na kuonyesha tunavyoweza kufaidika.

7 Vifungu vinavyofuata vinaweka msingi wa kulielewa jambo hilo:

“Mungu aliupenda ulimwengu [wanadamu], hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”— Yohana 3:16.

“Mwana wa Adamu [Yesu] naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.”—Marko 10:45.

“Wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu, na ni kama zawadi ya bure kwamba wao wanatangazwa kuwa waadilifu kwa fadhili zisizostahilika zake yeye kupitia kule kufunguliwa kwa njia ya ule ukombozi uliolipwa na Kristo Yesu. Mungu alimweka awe toleo [linatofunika] kupitia imani katika damu yake.”—Warumi 3:23-25, NW.

“UKOMBOZI” NI NINI?

8 Mawili kati ya maandiko hayo yametaja “ukombozi” (fidia). Ukombozi au fidia ni bei inayolipwa hasa kuweka huru mtu aliye mateka. (Isaya 43:3) Mara nyingi tunasikia neno hilo likitumiwa kuhusiana na fedha zinazotakwa ili kufungua mtu fulani aliyetekwa nyara na maharamia. Kwa habari yetu, mtekwa nyara atafananishwa na wanadamu wote kwa ujumla. Adamu alituuza kwa kutuingiza katika utumwa wa dhambi, kisha kukatokea magonjwa na kifo. (Warumi 7:14) Ni bei gani kubwa ingeweza kukomboa wanadamu na kutufungulia taraja la kupata uzima usio na madhara ya dhambi?

9 Kumbuka kwamba Biblia inasema Yesu ‘alitoa uhai wake uwe fidia’ (ukombozi). (Marko 10:45) Tunaweza kuona kutokana na hilo kwamba uhai wa kibinadamu ulihitajiwa. Kwa kutenda dhambi, Adamu alipoteza uhai mkamilifu wa kibinadamu. Ili kufungulia wanadamu njia ya kupata tena uzima wenye ukamilifu, uhai mwingine mkamilifu wa kibinadamu ulihitajiwa ili kununua tena alichopoteza Adamu. Jambo hilo linakazia sababu iliyofanya kusiwe na mzao wa Adamu aliye mkamilifu ambaye angeweza kuutoa ukombozi uliohitajiwa. Ni kama inavyosema Zaburi 49:7, 8: “Mwanadamu asingeweza kamwe kujikomboa mwenyewe wala kumlipa Mungu bei ya kujikomboa: ni gharama kubwa sana kukomboa uhai wake, ni jambo asiloweza yeye kufanya.”—Jerusalem Bible.

10 Mungu alimtuma Mwana wake wa kiroho aliye mkamilifu akatoka mbinguni azaliwe akiwa mwanadamu ili aitoe bei ya ukombozi iliyohitajiwa. Malaika alimweleza Mariamu bikira safi namna Mungu angehakikisha Yesu amezaliwa akiwa mkamilifu: “Uwezo wake Yeye Aliye Juu utakujia kama kivuli; kwa sababu hiyo, mtoto atakayezaliwa ataitwa Mtakatifu, na Mwana wa Mungu.” (Luka 1:35, HNWW; Wagalatia 4:4) Yesu hakuwa na dhambi ya kurithi kwa maana yeye hakuwa na baba asiye mkamilifu wa kibinadamu.—1 Petro 2:22; Waebrania 7:26.

11 Alipokwisha kuishi akiwa mwanadamu kupatana kabisa na mapenzi ya Mungu, Kristo aliyaacha maisha yake makamilifu ya kibinadamu. Yalikuwa maisha kama yale Adamu aliyokuwa nayo alipoumbwa, kwa hiyo Yesu akawa “ukombozi unaolingana kwa ajili ya wote.” (1 Timotheo 2:5, 6, NW; 1 Wakorintho 15:45) Ndiyo, yeye alilipa ile bei “kwa ajili ya wote” akanunua jamaa nzima ya kibinadamu. Kwa hiyo, Biblia inasema ‘tulinunuliwa kwa bei.’ (1 Wakorinto 6:20, HNWW) Basi kwa njia hiyo Mungu alitumia kifo cha Yesu kuweka msingi wa kuondoa dhambi, magonjwa na kifo ambavyo Adamu aliletea wanawe. Kweli hiyo inaweza kusaidia sana kutia maana na furaha katika maisha zetu.

NI KWA NJIA GANI TUNAWEZA KUSAMEHEWA DHAMBI ZETU?

12 Ni vema kujifunza katika Biblia kwamba Yesu alilipa bei ya ukombozi iliyohitajiwa. Lakini bado kuna kitu kinachoweza kutuzuia tusipate kibali na baraka ya Mungu. Kitu chenyewe ni kwamba sisi binafsi ni watenda dhambi. ‘Tunaikosa shabaha’ mara nyingi. Paulo aliandika hivi: “Wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Warumi 3:23, NW) Tunaweza kufanya nini na hilo? Tunawezaje kukubalika mbele za Mungu wetu, Yehova, mwenye uadilifu?

13 Pasipo shaka tusingemtazamia Mungu atukubali tukiendelea kufuata mwendo tunaojua ni kinyume cha mapenzi yake. Lazima tutubu kwa unyofu wa moyo kwa sababu ya tamaa zetu mbaya, usemi na mwenendo mbaya, kisha tujitahidi kufuata viwango vyake vilivyoonyeshwa wazi katika Biblia. (Matendo 17:30) Na bado dhambi zetu—za zamani na za sasa—zinahitaji kufunikwa. Hapo ndipo dhabihu ya ukombozi wa Yesu inapotusaidia. Paulo anaonyesha jambo hilo anapoandika kwamba ‘Mungu alimweka Yesu awe toleo linalofunika kupitia imani katika damu yake.’—Warumi 3:24, 25, NW.

14 Hapa mtume alikuwa akitaja jambo ambalo Mungu alipanga zamani sana, ambalo lingefananisha au kuelekeza mbele kwenye wakati wa kuja kwa Kristo. Katika Israeli ya kale dhabihu za wanyama za kulipia dhambi zilitolewa kwa ukawaida kwa ajili ya watu. Nao watu mmoja mmoja wangeweza kutoa matoleo yao wenyewe ya hatia kwa sababu ya visa vikubwa vya kutenda makosa. (Mambo ya Walawi 16:1-34; 5:1-6, 17-19) Mungu alikubali kwamba hizo dhabihu zenye damu zililipia au zikafuta dhambi za kibinadamu. Lakini hazikuleta ondoleo la daima, kwa sababu Biblia inasema “haiwezekani damu ya mafahali na mbuzi kuondoa dhambi.” (Waebrania 10:3, 4) Walakini, mambo hayo ya ibada yenye kuhusu makuhani, mahekalu, madhabahu na matoleo yalikuwa “mfano” au ‘kivuli cha yale mambo mema ambayo yangekuja’ kuhusiana na dhabihu ya Yesu.—Waebrania 9:6-9, 11, 12; 10:1.

15 Biblia inaonyesha namna jambo hilo linavyohitajiwa sana ili tuweze kupata msamaha, ikisema: “Kwa njia ya yeye tuna kule kufunguliwa kupitia ukombozi kwa ile damu ya huyo [Yesu], ndiyo, msamaha wa makosa yetu.” (Waefeso 1:7, NW; 1 Petro 2:24) Kwa hiyo zaidi ya kifo chake kutoa ukombozi, kinaweza pia kufunika dhambi zetu; tunaweza kusamehewa dhambi zetu. Lakini jambo fulani linatakwa kwetu. Kwa kuwa tumenunuliwa, ndiyo, ‘tukanunuliwa kwa bei’ ya ukombozi wa Kristo, lazima tuwe na nia ya kumkubali Yesu kuwa Bwana au Mwenyeji wetu na kumtii. (1 Wakorintho 6:11, 20; Waebrania 5:9) Kwa hiyo, tunahitaji tutubu dhambi zetu na kuiamini hiyo dhabihu ya Yesu Bwana wetu.

16 Tukifanya hivyo, si lazima tungoje kupata msamaha wakati ambao Mungu ataondolea wanadamu madhara yote ya dhambi, akomeshe magonjwa na kifo. Maandiko yanasema tunaweza kufurahia msamaha huo sasa hivi, kisha tuwe na dhamiri safi mbele za Mungu.—1 Yohana 2:12.

17 Basi, inampasa kila mmoja wetu athamini ubora ambao dhabihu ya Yesu inao kwake binafsi. Kupitia kwayo Mungu anaweza kutusamehe makosa tunayofanya. Mtume Yohana anaeleza hivi: “Nawaandikia haya ili kwamba msitende dhambi. Na kama mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki.” (1 Yohana 2:1; Luka 11:2-4) Hilo ni fundisho kubwa la Biblia na tunalihitaji kabisa ili tuweze kupata furaha ya kudumu.—1 Wakorintho 15:3.

WEWE UTAFANYA NINI?

18 Wewe unayaonaje mambo inayoyasema Biblia juu ya kisababishi cha magonjwa na kifo, ukombozi na mpango uliofanywa tusamehewe dhambi kupitia Yesu Kristo? Mtu anaweza kuingiza habari hizo akilini lakini zisiguse moyo na maisha yake kiasi cha kumbadili. Lakini kuna mambo mengine tunayotakwa tufanye.

19 Je! tunauthamini upendo wa Mungu wa kutufanyia mpango wa ukombozi? Mtume Yohana aliandika hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana sana hata yeye akatoa Mwana wake mzaliwa wa pekee.” (Yohana 3:16, NW) Kumbuka kwamba wanadamu waliohusika walikuwa watenda dhambi, wenye kuwekwa mbali na Mungu. (Warumi 5:10; Wakolosai 1:21) Je! wewe ungetoa kipenzi chako kwa ajili ya watu ikiwa wengi wao hawapendezwi sana na wewe, au hata hawapendezwi nawe hata kidogo? Ijapokuwa ni vigumu, Yehova aliagiza Mwanawe mwenye kutakata, aliye mwaminifu, Mzaliwa wa kwanza aliye mpendwa wake, aje duniani apatwe na madharau, aibu na kifo ili awape wanadamu ondoleo lenye kuwaweka huru. Jambo hilo lilimvuta Paulo kuandika hivi: “Mungu anapendekeza upendo wake mwenyewe kwetu sisi kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda dhambi Kristo alikufa kwa ajili yetu.”—Warumi 5:8, NW.

20 Mwana huyo alionyesha upendo wake pia. Wakati ulipowadia, alijishusha kwa moyo wa kupenda akawa mwanadamu. Alifanya kazi ya mtumwa kwa ajili ya wanadamu, akawafundisha na kuwaponesha magonjwa. Na ajapokuwa bila hatia, alivumilia dhihaka, kuteswa-teswa kisha akafa kwa njia yenye aibu mikononi mwa adui za ile kweli. Kukusaidia uthamini jambo hilo, tafuta wakati usome masimulizi ya kusalitiwa kwa Yesu, kujaribiwa kwake, kutukanwa, kutendwa mabaya ya kimwili na kuuawa kwake katika Luka 22:47 mpaka 23:47.

21 Wewe utachukua hatua gani ukiisha kufahamu hayo yote? Kwa uhakika mtu hapaswi kutumia ukubali wake wa ukombozi huo wa upendo uwe kisababu cha kuwa na mwenendo mbaya. Kufanya hivyo kungekuwa ni kulikosa kusudi la ukombozi huo, na hata kunaweza kutendesha mtu dhambi isiyosameheka. (Waebrania 10:26, 29; Hesabu 15:30) Badala ya hivyo, inatupasa tujitahidi tuishi kwa njia itakayoheshimu Muumba wetu. Tena kuamini mpango mkubwa alioufanya kupitia Mwanawe kunapasa kutuongoze tuwaeleze wengine juu ya mpango huo, tuwasaidie wafahamu namna wao pia wanavyoweza kufaidika.—Matendo 4:12; Warumi 10:9, 10; Yakobo 2:26; 2 Wakorintho 5:14, 15.

22 Yesu Kristo alipokuwapo duniani alisema angeweza kutolea watu msamaha wa Mungu kwa dhambi zao. Adui wengine walimlaumu kwa kusema hivyo. Basi Yesu akathibitisha jambo hilo kwa kuponesha mwanamume aliyepooza. (Luka 5:17-26) Kwa hiyo, sawasawa na vile dhambi ilivyoletea wanadamu madhara ya kimwili, ndivyo msamaha wa dhambi unavyoweza kuwaletea faida nyingi. Ni jambo la maana kujua hivyo. Matendo ya Yesu duniani yanaonyesha kwamba Mungu anaweza kukomesha magonjwa na kifo. Hilo linapatana na maneno ya Yesu Kristo mwenyewe, ya kwamba Yehova Mungu alitoa Mwanawe ili watu wenye imani waweze kuwa na “uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Lakini wawe nao namna gani? Wakati gani? Namna gani juu ya wapendwa wetu waliokufa?

[Mambo ya Kuzungumziwa]

Sababu gani watu wanashindwa kujua kinachosababisha magonjwa na kifo? (1, 2)

Magonjwa na kifo yalianzaje kutupata? (3-5)

Sababu gani Mungu ndiye mwenye uwezo wa kumaliza magonjwa na kifo? (6, 7)

Ukombozi umetolewa kwa njia gani? (8-11)

Kuna msingi gani wa kusamehewa dhambi zetu? (12-17)

Wewe unayaonaje mambo ambayo Mungu na Yesu wamefanya? (1 Yohana 4:9-11) (18-21)

Msamaha wa dhambi zetu unaweza kuhusu taraja gani? (22)

[Sanduku katika ukurasa wa 103]

Isaac Asimov, mwandikaji wa mambo ya kisayansi, alieleza kwamba chembe-molekyuli za kunakili tabia (RNA) zilizo katika ubongo wa kibinadamu ni “mfumo wenye kutunza maarifa unaoweza kutunza kwa ukamilifu furushi lo lote la masomo na mambo ya kukumbukwa yanayoweza kuingizwa humo na mwanadamu—na mfumo huo unaweza kufanya hivyo mara bilioni moja zaidi ya kiasi hicho.”—Gazeti New York “Times.”

[Picha katika ukurasa wa 108]

Dhabihu zilizotolewa katika Israeli zilielekeza mbele kwenye dhabihu ya ukombozi iliyotolewa na Yesu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki