Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • hp sura 13 kur. 121-130
  • Kuwasiliana na Ulimwengu wa Roho

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuwasiliana na Ulimwengu wa Roho
  • Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUSEMA NA MUUMBA
  • MAJIBU YANAYOTOKA KWENYE ULIMWENGU WA ROHO
  • JE! KUNA WATU WAOVU KATIKA ULIMWENGU WA ROHO?
  • UVUTANO MBOVU KUTOKA ULIMWENGU WA ROHO
  • KUEPUKA UHUSIANO NA ROHO WAOVU
  • Jinsi Viumbe wa Roho Wanavyohusika Maishani Mwetu
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Tunaweza Kuwapinga Roho Waovu Jinsi Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Ni Nani Hasa Anayeutawala Ulimwengu?
    Ni Nani Hasa Anayeutawala Ulimwengu?
  • Roho Waovu Ni Nani?
    Amkeni!—2010
Pata Habari Zaidi
Furaha​—Namna ya Kuipata
hp sura 13 kur. 121-130

Sura ya 13

Kuwasiliana na Ulimwengu wa Roho

“TAMAA inayolazimisha mtu atake kuwasiliana na wengine ni kubwa sana moyoni.” Huo ndio uliokuwa utangulizi wa sura moja ya kitabu Machines ikieleza mambo yanayohusiana na redio. Kwa kutumia redio tunaweza kuwasiliana (kupashana habari) na watu walioko kote duniani au hata kusikia maneno ya wanaanga katika anga za juu.

2 Sasa mawasiliano ya redio yamekuwa kawaida ya maisha. Lakini watu wengi wanapuza au wanakuwa na maoni yasiyofaa juu ya namna ya mawasiliano iliyo ya maana zaidi—kuwasiliana na ulimwengu wa roho.

KUSEMA NA MUUMBA

3 Karne nyingi kabla ya redio kuvumbuliwa, Mfalme Daudi aliandika hivi:

“Ee [Yehova], uyasikilize maneno yangu . . . Uisikie sauti ya kilo changu, Ee Mfalme wangu na Mungu wangu, kwa maana Wewe ndiwe nikuombaye.”—Zaburi 5:1, 2.

Je! si jambo la akili kusema kwamba mtu aliye na hekima nyingi kuliko wote katika ulimwengu mzima anaweza ‘kusikiliza’ tunayosema katika sala, akitaka? Na je! si jambo la akili tutafute msaada wa Mungu, anayeweza kutupa mwongozo bora zaidi tunaohitaji?—Zaburi 65:2.

4 Transimita na risiva (kisafirisha-habari na kipokea habari) ni vyombo vinavyohitajiwa kabisa ili iwezekane kuwasiliana kwa njia ya redio. Lakini sisi tunahitaji nini ili tumfikie Yehova katika sala? Takwa la kwanza ni imani. “Mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao [kwa bidii].” (Waebrania 11:6) Pia, lazima mtu awe anafuata viwango na njia za Mungu alizoweka kuhusu adili. Ama sivyo Mungu hatamsikiliza yeye. Ni kama vile mtu mwenye njia nyofu asivyoweza kusikiliza kipindi cha redio anachokiona kuwa chenye mawazo na misemo michafu.—1 Yohana 3:22; Isaya 1:15.

5 Yehova hakuchagua njia fulani ya kuomba na kusisitiza kwamba hiyo ndiyo njia pekee ya kutolea sala zinazokubalika. Kama unasali kwa sauti kubwa au kwa kimya, yeye bado anaweza ‘kusikia.’ Unaweza kusali ukiwa umesimama, umeketi, umepiga magoti au ukiwa umelala kitandani. (1 Samweli 1:12, 13; 1 Wafalme 8:54) Huhitajiwi useme maneno ya namna ya pekee wala utumie usemi fulani wa kidini. Jambo la maana zaidi ni unyofu wa moyo na roho ya unyenyekevu. Angalia mfano alioutoa Yesu kwenye Luka 18:10-14 kuhusu jambo hilo.

6 Tunaweza kumfikia Yehova katika sala tukiwa watu mmoja mmoja, wakati wo wote tu. Walakini, yeye anafurahia pia sala za umoja, kama zile zinazotolewa na kundi la Wakristo. Kwa kuzisikiliza sala zinazotolewa kwenye mikutano ya kundi, watu wengine ambao hawakuwa wamesali hata siku moja wamejifunza kutumia njia hiyo ya mawasiliano iliyo ya maana kabisa. Hata jamaa zinaweza na zinapaswa kusali pamoja. Nafasi moja ya kufanya hivyo ni nyakati za chakula, kwa kufuata mfano wa Yesu wa kupigia Mungu asante ya chakula alichofanya kiweze kupatikana.—Marko 8:6.

7 Labda wewe unajua watu fulani ambao wamesali lakini wakawa wanalalamika wakisema hawakujibiwa. Kwa nini hawakujibiwa? Kristo aliwaambia wafuasi wake: “Mkimwomba Baba neno lo lote atawapa kwa jina langu.” Yesu Kristo ndiye njia ya kumfikia Mungu, wala si mtu mwingine ye yote. Je! inaweza kuwa kwamba mtu amekosa kujibiwa kwa sababu hakuthamini jambo hilo? (Yohana 16:23; 14:6) Pia, Yesu alikuwa na maana gani kwa kusema “lo lote”? Mtume Yohana anaonyesha ni “lo lote” ambalo liko ‘sawasawa na mapenzi ya Yehova.’ Hatuwezi kumtazamia Mungu mwenye uadilifu akubali sala zinazomwomba ruhusa ya kutenda mabaya, kufanya mambo machafu au kula pupa. (1 Yohana 5:14) Hata hivyo watu wengi wanaomba utajiri wa mara hiyo au mamlaka ya kutawala wengine. Basi, si ajabu kwamba Mungu haitikii sala za namna hiyo. Imetupasa tuombe mahitaji ya kibinafsi yanayofaa baada ya kutaja mambo mengine, kwa mfano kusema mapenzi ya Mungu yatendeke duniani.—Mathayo 6:9-11.

8 Sala inatutolea nafasi nyingi za kuongea na Mungu kama vile mtu anavyoweza kuongea na baba mwenye upendo. Inatutolea nafasi za kumwonyesha furaha zetu, taabu na mahitaji yetu. Ikiwa umekuwa hufanyi hivyo kwa ukawaida, usiendelee kukawia. Ukipata uhusiano wa kutumainiana na Mungu na kuweza kuwasiliana naye wakati wo wote, utapata amani nyingi ya akilini kisha furaha. Unaweza kujitushia mzigo unaokulemea, ukiwa na uhakika wa kwamba yeye anapendezwa nawe.—Zaburi 86:1-6; Wafilipi 4:6, 7.

MAJIBU YANAYOTOKA KWENYE ULIMWENGU WA ROHO

9 Moja ya habari kubwa-kubwa zinazofaa kuwa katika sala ni uhitaji wetu wa kupata hekima na mwongozo kwa Mungu. (Zaburi 27:11; 119:34-36; Yakobo 1:5) Mungu atajibu kwa njia gani? Nyakati za kale, mara kwa mara alitoa ujumbe mwingi kwa mdomo, akatumia malaika au manabii wa kibinadamu waseme. Lakini mtume Paulo anasema kwamba sasa Mungu “amesema na sisi katika Mwana,” na mafundisho hata kielelezo cha maisha ya huyo yameonyeshwa wazi katika Biblia. (Waebrania 1:1, 2; 2:1-3; Yohana 20:31) Kwa hiyo, badala ya kumtazamia Mungu mwenyewe aseme nasi, inatupasa tutafute msaada kwa kutumia njia ambayo ameichagua, yaani, Biblia. Kwa kukumbuka jambo hilo, inatupasa tutende kulingana na sala zetu za kuomba uongozi kwa kujibidiisha tujifunze Neno lake. (Mithali 2:1-5) Msaada zaidi unapatikana kwa Wakristo wenye bidii ya utumishi ambao wanakutana kwa ukawaida kujifunza Biblia na kuizungumza.—2 Timotheo 2:1, 2.

10 Mungu anaweza kutusaidia sisi binafsi kwa kutumia roho yake pia anapojibu sala zetu. Kwa roho hiyo anasaidia Wakristo walielewe Neno lake na kulifuata. (Yohana 16:7-13) Daudi alisali akasema: “Unifundishe kutenda mapenzi yako . . . Roho yako ni njema; na iniongoze mimi katika ile nchi ya unyofu.”—Zaburi 143:10, NW.

JE! KUNA WATU WAOVU KATIKA ULIMWENGU WA ROHO?

11 Biblia inatuhakikishia kwamba Yehova, Mwanawe na malaika wako katika ulimwengu wa roho, na kwamba tuna ruhusa ya kuwasiliana na Mungu kwa njia ya sala. Vivyo hivyo, Maandiko yanaonyesha kwa njia yenye kuaminika kwamba kuna watu wa kiroho wenye akili ambao sasa ni waovu sana, yaani, Shetani na mashetani zake.

12 Watu wengine wana maoni ya kwamba “Ibilisi” hayuko, na kwamba watu walipata wazo la kwamba yuko kutokana na ushirikina (woga wa kupatwa na misiba) au hadithi fulani ya uongo ya zamani zilizopita. Wengine wanafikiri kwamba wakati Biblia inapotaja “Shetani” ina maana ya kanuni fulani tu ya uovu.

13 Walakini, Mathayo 4:1-11 inatueleza habari za wakati ambao Shetani alimtolea Yesu vishawishi vitatu vya wazi sana. Pasipo shaka, Shetani anayetajwa hapo hakuwa kanuni ya uovu iliyokuwa ndani ya Yesu, kwa maana Mwana wa Mungu hana uovu wala dhambi. (Waebrania 7:26; 1:8, 9) Hapana, Shetani ni mtu ambaye kwa kweli yuko. Jambo hilo linaonyeshwa wazi pia na masimulizi yaliyo katika Ayubu 1:6-12, yanayoeleza kwamba Shetani alikwenda mbele za Yehova.

14 Lakini Shetani alianzaje? Tunajua kwamba Yehova ndiye Muumba wa vitu vyote na “kazi yake ni kamilifu.” (Kumbukumbu la Torati 32:4; Ufunuo 4:11) Kwa hiyo, je! si wazi kwamba pasipo shaka Shetani alikuwa mtu mnyofu wa kiroho aliyeumbwa na Yehova pamoja na malaika wale wengine? Basi aliharibikaje? Yakobo 1:14, 15 inatudokezea kwa kutuambia:

“Mtu hujaribiwa anapovutwa na kunaswa na tamaa zake mbaya. Tamaa ikiiva huzaa dhambi.” (HNWW)

15 Kwa kuyafikiria mambo ambayo yametukia kati ya wanadamu, tunajua kwamba hata mtu mwenye cheo cha kutumainiwa huenda akaona njia ya kutumia vibaya hali fulani ili ajipatie mamlaka zaidi. Inaonekana ndivyo ilivyokuwa kwa mmoja wa malaika za Mungu. Kiumbe huyo wa kiroho alichagua mwendo mbaya kwa sababu alikuwa ameumbwa akiwa na uhuru wa kuchagua matakwa yake, labda akidhani angeweza kuwa kama Mungu, kisha wanadamu wamfuate yeye. Lililotukia linalinganika na yaliyompata mfalme mmoja wa Tiro, kama yanavyosimuliwa kwenye Ezekieli 28:1-19. Mwanamume huyo alikuwa katika cheo chenye upendeleo kuhusiana na Israeli wa kale, lakini akajitutumua kwa kiburi, akaanguka. Hivyo ndivyo kiburi kilivyomharibu yule aliyejifanya mwenyewe kuwa Shetani, mpingaji wa Mungu.

16 Kufahamu kwamba Shetani yuko kunasaidia kuyajua vizuri matukio yaliyotendeka katika bustani ya Edeni mpaka sisi tukaja kuwa watu wasio wakamilifu, watenda dhambi, watu wenye maelekeo ya kuwa wagonjwa-wagonjwa na wenye kufa. Shetani alitumia akili zake zinazopita za mwanadamu akapeleka nyoka fulani awasiliane na Hawa juu ya habari ya uongo, yenye kuleta msiba, ili Hawa afuate shauri lake. (Mwanzo 3:1-5) Kwa hiyo, Ufunuo 12:9 unamwita Shetani “yule nyoka wa kale.” (HNWW) Naye Yesu alisema huyu ‘hakusimama imara katika ile kweli,’ bali akawa “yule baba wa ule uongo” na “mwua-watu.”—Yohana 8:44, NW.

17 Shetani siye kiumbe wa pekee aliyeasi. Historia iliyo katika Mwanzo 6:1-3 inaeleza kwamba siku za Noa malaika fulani walivaa miili ya kibinadamu ili wajifurahishe ngono na wanawake. Labda walichochewa na uasi wa Shetani. Tendo hilo halikuwa la asili. Lilikuwa chafu. (Yuda 6, 7) Wakati Mungu alipoufagilia mbali uovu utoke duniani kwa kuleta gharika ya dunia nzima, malaika hao wasiotii walirudia ulimwengu wa roho, ila sasa wakawa upande wa Shetani, wakiwa mashetani. (2 Petro 2:4, 5) Kuna hadithi za mapokeo, za Kigiriki na za Kirumi, zinazosimulia habari za miungu iliyokuja-kuja duniani na kurudi-rudi mbinguni. Labda hadithi hizo zinayaeleza mambo yale ya kweli juu ya wale malaika wasiotii wanaotajwa katika Biblia, lakini zikiwa na maelezo yaliyopotoshwa.

UVUTANO MBOVU KUTOKA ULIMWENGU WA ROHO

18 Roho waovu hawataki kuona tukiwa na hali njema bali wamekaza nia wadanganye wanadamu na kuwapoteza, kuwaondoa upande wa Mungu. Mtume Paulo alimwita Shetani “mungu wa hii taratibu ya mambo” ambaye “amepofusha akili za wasioamini” ili wasiweze kujifunza zile “habari njema” zinazohusu Kristo. (2 Wakorintho 4:4, NW) Amefaulu sana kufanya hivyo.

19 Ujanja mmoja ambao ametumia ni kutia watu moyo wawe na maoni ya kwamba hakuna mtu aishiye anayeitwa Ibilisi au Shetani. Yeye ni kama mhalifu (mkora) anayeeneza wazo la kwamba hakuna genge la wahalifu (wakora), na hivyo anapumbaza watu wajisikie kuwa salama na kumbe sivyo. Ujanja mwingine anaotumia unaonekana katika ukatili mkubwa sana uliotendwa na washupavu wa kidini, yaani, vita vya kidini, baraza za kuhukumu waasi wa dini na kubariki vita. Mambo hayo yamefanya watu wengi wenye kuchukizwa vyepesi wamwachilie mbali Yehova Mungu, wakidhani ati makanisa yanamwakilisha yeye.

20 Kumbuka, pia, kwamba mtume Paulo alisema Shetani ndiye “mungu wa hii taratibu ya mambo.” Watu wengine wanafanya mzaha juu ya wazo la kwamba Shetani ndiye anayeongoza mataifa kwa hila. Lakini wakati Shetani alipotaka kumpa Kristo mamlaka ya kutawala mataifa, Yesu hakukana akisema Ibilisi siye mwenye mamlaka juu ya falme za kisiasa. (Luka 4:5-8) Na je! haielekei kuwa kuna kani (nguvu) fulani ya uovu inayochochea mambo ya ulimwengu leo? Unapofikiria jambo hilo, soma maneno ya Ufunuo 12:9, 12 juu ya jitihada za Shetani.

KUEPUKA UHUSIANO NA ROHO WAOVU

21 Wanasayansi wamechunguza kile kinachoitwa ESP (kuwa na fahamu zinazoupita uwezo wa kibinadamu wa kujua mambo). Hiyo ni pamoja na maajabu kama kujua mawazo yaliyo katika akili za wengine, kueleza habari za matukio au vitu ambavyo mtu asingaliweza kuviona au kuvijua kama asingalikuwa na uwezo huo wa ziada, na kutabiri mambo yatakayotukia kwa kutegemea ‘ndege mbaya’ na mambo mengine kama hayo. Wenye kuchunguza mambo yanayofanyika katika akili za watu wamejaribu kuepa uwezekano wa kwamba mambo hayo yanatokea kwa sababu ya ujanja fulani unaotumiwa. Lakini bado wanashindwa kueleza maajabu hayo yasiyo kawaida ya mwanadamu yanatoka wapi. Je! haielekei kuwa kwamba maelezo ya Maandiko ndiyo yanayokilenga chanzo chenyewe?

22 Shetani na mashetani wake wanaweza kuwaongoza moja kwa moja wanadamu na mambo yao. Kwa mfano, msichana mmoja katika mji wa kale wa Filipi, katika Ugiriki, alikuwa na uwezo wa kutabiri mambo. Namna gani? Maandishi ya kweli yanasema kwamba “roho fulani, shetani fulani wa uaguzi,” ndiye aliyekuwa akiongoza maneno ya msichana huyo. Mtume Paulo alimsaidia kutoka katika kifungo cha shetani huyo.—Matendo 16:16-18, NW.

23 Neno la Mungu linatuonya mara nyingi ttisihusike na mashetani kwa sababu ni watu waliopo, wenye nguvu nyingi. Linakataza kuloga watu kwa uchawi, kuendea wachawi au kujaribu kuongea na wafu upate habari fulani. (Kumbukumbu la Torati 18:10-12; Mambo ya Walawi 20:6, 27; Wagalatia 5:19-21) Maonyo hayo yangali ni yenye mafaa. Labda wewe umeona kwamba watu wengi sana wanataka kujua matabiri ya kiuchawi na siri za mambo yasiyoweza kujulikana kwa akili za kibinadamu. Sinema nyingi na vitabu vya hadithi za kubuni vimeonyesha mambo ya ‘roho’ (mashetani) au jitihada za mwanadamu za kujaribu kupunga pepo, au kufukuza mashetani wawatoke watu. Wanapiga sana bao, kutumia vibuyu vya uganga au hata unajimu ili wapate uongozi.

24 Ni hatari kuwasiliana (kupashana habari) na roho waovu. Habari zinaonyesha kwamba mashetani wakiisha kumtawala mtu, wanaweza kumwumiza sana—mwilini, akilini na katika maoni ya moyoni. (Linganisha Mathayo 8:28-33.) Wamenyanyasa (wamesumbua) watu kweli kweli, wakapiga makelele ya namna nyingi usiku, wakarusha-rusha vitu huku na huku, wakapapasa-papasa viungo vya uzazi vya watu ili kuamsha nyege. Tena wameleta magonjwa makubwa. “Sauti” zao hata zimefanya watu waende uwazimu, waue wengine au wajinyonge.

25 Bila shaka, huenda matukio fulani ‘ya kigeni’ yakatokana na matatizo ya kimwili, kama vile utendaji usiofaa wa kemikali za mwili ambao unaweza kuleta madhara akilini na kwenye neva (mishipa ya fahamu). Lakini ungekuwa upumbavu kufikiri ni upuzi tu inaposemwa kwamba Shetani na mashetani wapo. Usilichezee onyo la Biblia linalosema wapo.

26 Ikiwa mtu ananyanyaswa-nyanyaswa na mashetani, je! kuna njia ya kupata faraja? Kwa sasa Mungu hatumii wanadamu kuponesha wagonjwa, kufukuza mashetani wawatoke watu wala kufufua wafu, kama alivyowatumia mitume. Lakini atasaidia mtu atoke katika kifungo cha “nguvu za Shetani.” (Matendo 26:18; Waefeso 6:12) Mtu anahitaji kabisa amwendee Yehova katika sala, atumie jina lake na kumwomba msaada kwa bidii nyingi. (Mithali 18:10) Pia, lazima ayapinge sana mashauri ya kishetani, kama Yesu alivyofanya, aache mazoea ya kupashana habari na roho waovu na kuacha ushirika usio wa lazima wa watu wanaofuata mambo ya mashetani.—Mathayo 4:1-11; 2 Wakorintho 6:14-17.

27 Tena, habari za mambo yaliyotukia zinaonyesha kwamba mara nyingi mashetani wanahusiana na mwanadamu kwa kutumia chombo fulani, kwa hiyo ni jambo la maana kuharibu vitu vilivyokuwa vikitumiwa katika kupashana habari na roho waovu (hirizi, talasimu, mafingo, makago, na vinginevyo). Biblia inatuambia kwamba wengine waliokuwa wamezoea ufundi wa kufanya mambo ya kiuchawi katika mji wa kale wa Efeso waliharibu vitu vyao.—Matendo 19:18-20.

28 Hata hivyo hakuna uhitaji wa kuogopa-ogopa roho waovu saa zote. Bali, Biblia inatuhimiza tujivike silaha za kiroho:

“Simameni imara, basi, vikiwa viuno vyenu vimefungwa mshipi wa KWELI, na mkiwa mmevaa bamba la chuma la kifuani la UADILIFU, na zikiwa nyayo zenu zimevishwa vile vifaa vya zile HABARI NJEMA ZA AMANI. Juu ya mambo yote, chukueni ile ngao ya IMANI, ambayo kwayo mtaweza ninyi kuyazima yaie makombora yote yanayowaka moto ya yule mwovu. Pia, mwipokee ile kofia ya chuma ya kukinga kichwa ya WOKOVU, na ule upanga wa tie roho, yaani, NENO LA MUNGU, huku . . . ninyi mkiendelea na SALA katika kila pindi.”—Waefeso 6:14-18, NW.

Kama linavyoonyesha Neno la Mungu hapa, ulinzi bora kabisa wa kujikinga juu ya kuwasiliana kubaya na roho waovu ni kuwasiliana na Yehova kwa ukawaida kupitia sala. Kwa kufaa Biblia inasema: “Basi, jiwekeni chini ya Mungu; mpingeni Shetani naye atawakimbieni.”—Yakobo 4:7, HNWW.

[Mambo ya Kuzungumziwa]

Kwa sababu gani inatupasa tupendezwe na kuwasiliana na Muumba? (1-3)

Ni nini kinachohitajiwa ili sala zikubalike? (1 Petro 3:12) (4, 5)

Tunaweza kujifunza nini kutokana na Biblia juu ya hali ya sala zetu? (6-8)

Tunaweza kupata habari kutoka kwa Mungu kwa njia gani? (9, 10)

Tunaweza kujuaje kwamba Shetani yuko? Na chanzo chake ni nini? (11-15)

Tunapata msaada gani kwa kujua habari za Shetani na mashetani wake? (16, 17)

Roho waovu wameongoza wanadamu kwa njia gani? (2 Wakorintho 11:13-15) (18-20)

Ni mazoea gani yanayoweza kuhusianisha mtu na roho waovu? (21-23)

Wewe unaweza kujilindaje juu ya kuwasiliana na ulimwengu wa roho? (24-28)

[Picha katika ukurasa wa 123]

Kila siku tunaweza kuwasiliana na Mungu kupitia sala

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki