Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • T-22 kur. 2-6
  • Ni Nani Hasa Anayeutawala Ulimwengu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni Nani Hasa Anayeutawala Ulimwengu?
  • Ni Nani Hasa Anayeutawala Ulimwengu?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Dalili Katika Hali za Ulimwengu
  • Watawala wa Ulimwengu Watambuliwa
  • Kinza Roho Waovu
  • Adui wa Uzima wa Milele
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Je! Viko Viumbe Vibaya vya Kiroho?
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Watawala Katika Makao ya Roho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Kinza Majeshi ya Roho Waovu
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
Pata Habari Zaidi
Ni Nani Hasa Anayeutawala Ulimwengu?
T-22 kur. 2-6

Ni Nani Hasa Anayeutawala Ulimwengu?

Watu wengi wangejibu swali lililo juu kwa neno moja—Mungu. Lakini kwa kutokeza, hakuna mahali popote ambapo Biblia inasema kwamba ama Yesu Kristo ama Baba yake ndio hasa watawala wa ulimwengu huu. Kinyume cha hilo, Yesu alisema: “Mtawala wa ulimwengu huu atatupwa nje.” Na akaongeza: “Mtawala wa ulimwengu anakuja. Na yeye hana lolote juu yangu mimi.”—Yohana 12:31; 14:30; 16:11, New World Translation.

Kwa hiyo mtawala wa ulimwengu huu anampinga Yesu. Huyo anaweza kuwa nani?

Dalili Katika Hali za Ulimwengu

Kujapokuwa na jitihada za wanadamu wenye makusudi mazuri, ulimwengu umeteseka sana katika historia yote. Jambo hilo hufanya watu wenye kufikiri, kama vile David Lawrence mhariri aliyekufa, wajiulize hivi: “‘Amani duniani’—karibu kila mtu anaitaka. ‘Nia njema kuelekea watu’—karibu watu wote ulimwenguni huhisi nia njema kuelekea mmoja na mwenzake. Basi, shida iko wapi? Kwa nini kuna tisho la vita kujapokuwa tamaa ya watu ya kiasili?”

Yaonekana kuwa kinyume, sivyo? Kwamba ingawa tamaa ya watu ya kiasili ni kuishi kwa amani, wao huchukiana na kuuana—tena kwa ukatili mwingi sana. Fikiria ukatili wa kinyama wa umwagaji damu mwingi usio na huruma. Wanadamu wametumia vyumba vya gesi, kambi za mateso, silaha zenye kutupa moto, mabomu ya petroli inayowaka moto, na njia nyinginezo zinazochukiza ili kutesana na kuchinjana bila huruma.

Je! wewe waamini kwamba ni wanadamu wenye kutamani sana amani na furaha, ndio kwa uwezo wao wenyewe hutendea wengine maovu hayo mabaya sana? Ni kani gani zinazowasukuma watu kutenda maovu yenye kuchukiza au kuwaongoza katika hali ambazo wanahisi ni lazima wafanye mambo ya ukatili? Je! umepata kujiuliza ikiwa uwezo fulani mwovu, usioonekana unawaongoza watu kufanya matendo hayo ya jeuri?

Watawala wa Ulimwengu Watambuliwa

Hakuna haja ya kukisia jambo hilo, kwani Biblia huonyesha wazi kwamba mtu fulani asiyeonekana mwenye weledi, amekuwa akidhibiti watu na mataifa pia. Hiyo husema: “Dunia yote pia hukaa katika yule mwovu.” Na Biblia humtambulisha, ikisema: ‘Yule aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote.’—1 Yohana 5:19; Ufunuo 12:9.

Katika pindi moja ambapo Yesu ‘alijaribiwa na Ibilisi,’ Yesu hakubisha juu ya jukumu la Shetani akiwa mtawala wa ulimwengu huu. Biblia hueleza yale yaliyotokea: “Ibilisi akamchukua mpaka mlima mrefu mno, akamwonyesha milki zote za ulimwengu, na fahari yake, akamwambia, Haya yote nitakupa, ukianguka kunisujudia. Ndipo Yesu alipomwambia, Nenda zako, Shetani.”—Mathayo 4:1, 8-10.

Ebu fikiria hilo. Shetani alimjaribu Yesu kwa kumtolea “milki zote za ulimwengu.” Lakini, je! toleo la Shetani lingalikuwa jaribu halisi ikiwa Shetani hakuwa hasa mtawala wa milki hizo? La, halingalikuwa. Na angalia, Yesu hakukana kwamba serikali hizo zote za kilimwengu hazikuwa za Shetani, jambo ambalo angalifanya ikiwa Shetani hangalikuwa na uwezo juu yazo. Kwa hiyo basi, Shetani Ibilisi ndiye hasa mtawala asiyeonekana wa ulimwengu! Kwa kweli, Biblia humwita “mungu wa dunia hii.” (2 Wakorintho 4:4) Hata hivyo, mtu mwovu jinsi hiyo alikuja kupataje cheo hicho chenye uwezo?

Yule aliyekuja kuwa Shetani alikuwa malaika aliyeumbwa na Mungu, lakini alionea wivu cheo cha Mungu. Yeye alipinga utawala wa Mungu wa haki. Ili afanye hivyo alitumia nyoka kuwa msemaji ili kumdanganya mwanamke wa kwanza, Hawa, na hivyo alifaulu kumfanya yeye na mumewe Adamu, wamtii yeye badala ya kumtii Mungu. (Mwanzo 3:1-6; 2 Wakorintho 11:3) Yeye alidai pia kwamba angeweza kuwageuza wazao wote wa Adamu na Hawa ambao bado hawakuwa wamezaliwa, wawe mbali na Mungu. Kwa hiyo Mungu aliruhusu kuwe na wakati ili Shetani ajaribu kuthibitisha dai lake, lakini Shetani hajafanikiwa.—Ayubu 1:6-12; 2:1-10.

Kwa kiwango fulani, Shetani hayuko peke yake katika utawala wake wa ulimwengu. Yeye alifanikiwa kusadikisha baadhi ya malaika wengineo waungane naye katika kumwasi Mungu. Hao wakaja kuwa mashetani, waandamani wake wa roho. Biblia husema juu yao inapohimiza Wakristo hivi: “Simameni imara mweze kuzipinga hila za Shetani; kwa maana tunako kushindana mweleka, si juu ya damu na nyama, bali . . . juu ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.”—Waefeso 6:11, 12, NW.

Kinza Roho Waovu

Watawala hao wa ulimwengu wasioonekana wana nia ya kupotosha ainabinadamu yote, wakiigeuza mbali na ibada ya Mungu. Njia moja ambayo roho waovu hufanya hivyo ni kwa kuendeleza wazo la kuishi baada ya kifo, hata ingawa Neno la Mungu huonyesha wazi kwamba wafu hawajui lolote. (Mwanzo 2:17; 3:19; Ezekieli 18:4; Zaburi 146:3, 4; Mhubiri 9:5, 10) Hivyo, roho mwovu, akiiga sauti ya mtu aliyekufa, anaweza kuzungumza na watu wa ukoo walio hai wa mtu aliyekufa au marafiki wake, ama kupitia mtu anayewasiliana na roho ama kwa “sauti” kutoka makao yasiyoonekana. “Sauti” hiyo husingizia kuwa yule mtu aliyekufa, lakini hiyo hasa ni roho mwovu!

Kwa hiyo ukisikia “sauti” kama hiyo wakati wowote, usidanganyike. Kataa chochote isemacho, na urudie maneno ya Yesu kwa kusema hivi: “Nenda zako, Shetani”! (Mathayo 4:10; Yakobo 4:7) Usiruhusu udadisi kuhusu makao ya roho ukufanye ushirikiane na roho waovu. Ushirikiano kama huo huitwa uwasiliani-roho, na Mungu huwaonya waabudu wake dhidi ya uwasiliani-roho wa aina yoyote ile. Biblia hushutumu “mtu ambaye hutumia uaguzi . . . au yeyote ambaye hutafuta shauri kwa mtu anayewasiliana na roho au mtabiri kikazi wa matukio au yeyote ambaye huulizia habari za wafu.”—Kumbukumbu la Torati 18:10-12, NW; Wagalatia 5:19-21; Ufunuo 21:8.

Kwa kuwa uwasiliani-roho hufanya mtu awe chini ya uvutano wa mashetani, kinza mazoea yao yote hata yawe yenye kufurahisha au kusisimua jinsi gani. Mazoea hayo yanatia ndani kutazama tufe la fuwele, kupiga bao, uwezo wa kubashiri matukio bila kutumia hisia za asili (ESP, extrasensory perception), kuchunguza mistari ya kiganja, na unajimu. Mashetani pia wamefanya kelele na vituko vingine halisi katika nyumba wanamofanya makao yao.

Isitoshe, roho waovu hutumia kwa faida yao mwelekeo wa wanadamu wenye dhambi kwa kuendeleza fasihi, sinema, na vipindi vya televisheni vinavyoonyesha tabia ya kukosa adili na ya ngono zisizo za asili. Mashetani wanajua kwamba ikiwa fikira mbovu haziondolewi akilini, zitakuwa na matokeo yasiyoweza kuondolewa kisha yaongoze wanadamu watende kwa njia isiyo ya adili—kama vile mashetani wenyewe.—Mwanzo 6:1, 2; 1 Wathesalonike 4:3-8; Yuda 6.

Ni kweli, huenda wengi wakapuuza wazo la kwamba ulimwengu huu unatawalwa na roho waovu. Lakini kutosadiki kwao hakushangazi, kwa kuwa Biblia husema hivi: “Shetani mwenyewe hujigeuza awe mfano wa malaika wa nuru.” (2 Wakorintho 11:14) Udanganyifu wake mkubwa zaidi umekuwa ni kuwapofusha wengi wasitambue uhakika wa kwamba yeye na mashetani wake wanaishi hasa. Lakini wewe usidanganywe! Ibilisi na mashetani wake ni halisi, na unahitaji kuendelea kuwakinza.—1 Petro 5:8, 9.

Kwa furaha, wakati sasa u karibu ambapo Shetani na majeshi yake hawatakuwapo tena! “Ulimwengu [kutia ndani watawala wao wa roho waovu] unapitilia mbali,” Biblia inatoa uhakikishio, “lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hubaki milele.” (1 Yohana 2:17, NW) Kutakuwa kitulizo kilichoje baada ya uvutano huo mwovu kuondolewa! Basi, na tuwe miongoni mwa wale wanaofanya mapenzi ya Mungu na kufurahia milele maisha katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu.—Zaburi 37:9-11, 29; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4.

Isipokuwa iwe imeonyeshwa vingine, manukuu yote ya Biblia yametolewa katika Union Version ya Kiswahili.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Je! Shetani angaliweza kumtolea Yesu serikali hizi zote za ulimwengu ikiwa hazingalikuwa zake?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki