Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • kl sura 12 kur. 108-117
  • Kinza Majeshi ya Roho Waovu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kinza Majeshi ya Roho Waovu
  • Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ROHO WAOVU—MWANZO WAO NA SHABAHA YAO
  • JINSI ROHO WAOVU HUJARIBU KUKUONGOZA VIBAYA
  • SABABU KWA NINI BIBLIA HUPINGA UWASILIANI-ROHO
  • KUTOKA KUVUTIA HADI KUSHAMBULIA
  • JINSI YA KUKINZA ROHO WAOVU
  • ENDELEA NA PIGANO LAKO DHIDI YA ROHO WAOVU
  • Jinsi Viumbe wa Roho Wanavyohusika Maishani Mwetu
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Kubali Msaada wa Yehova wa Kuwapinga Roho Waovu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
  • Roho Waovu Ni Wenye Nguvu
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Sababu Uepuke Uwasiliani-roho
    Amkeni!—2000
Pata Habari Zaidi
Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
kl sura 12 kur. 108-117

Sura 12

Kinza Majeshi ya Roho Waovu

1. Yesu alitendaje alipokabili roho waovu?

MARA tu baada ya ubatizo wake, Yesu Kristo aliingia jangwani mwa Yudea ili kusali na kutafakari. Akiwa huko Shetani Ibilisi alijaribu kumfanya avunje sheria ya Mungu. Hata hivyo, Yesu alikataa katakata chambo cha Ibilisi naye hakunaswa na mtego wake. Yesu alikabili roho waovu wengine wakati wa huduma yake duniani. Hata hivyo, mara kwa mara, yeye aliwakaripia na kuwakinza.—Luka 4:1-13; 8:26-34; 9:37-43.

2. Tutazungumzia maswali gani?

2 Masimulizi ya Biblia yanayofafanua makabiliano hayo yanapaswa yatusadikishe kwamba kuna majeshi ya roho waovu. Wao hujaribu kuwaongoza watu vibaya. Hata hivyo, tunaweza kuwakinza roho hawa waovu. Lakini roho waovu wanatoka wapi? Sababu gani wao hujaribu kuwadanganya wanadamu? Na ni njia zipi wanazotumia ili kutimiza makusudi yao? Kupata majibu kwa maswali kama haya kutakusaidia ukinze majeshi ya roho waovu.

ROHO WAOVU—MWANZO WAO NA SHABAHA YAO

3. Shetani Ibilisi alitokeaje?

3 Yehova Mungu alifanya viumbe wengi wa roho muda mrefu kabla ya kuumba wanadamu. (Ayubu 38:4, 7) Kama vile ilivyoelezwa katika Sura ya 6, mmoja wa malaika hao alikuza tamaa ya kuabudiwa na wanadamu badala ya wao kumwabudu Yehova. Akifuatia kusudi hilo, malaika huyo mwovu alimkinza na kumchongea Muumba, hata akidokeza kwa yule mwanamke wa kwanza kwamba Mungu alikuwa mwongo. Kwa kufaa basi, kiumbe huyu wa roho aliyekuwa mwasi alikuja kuitwa Shetani (mkinzani) Ibilisi (mchongezi).—Mwanzo 3:1-5; Ayubu 1:6.

4. Malaika fulani walitendaje dhambi katika siku ya Noa?

4 Baadaye, malaika wengine walimuunga mkono Shetani Ibilisi. Katika siku za yule mtu mwadilifu Noa, baadhi yao waliacha utumishi wao mbinguni na kujivika miili yenye nyama ili kuridhisha uchu wao wa kufanya ngono na wanawake wa kidunia. Bila shaka Shetani aliwavuta malaika hao wafuate mwendo huo wa kutokutii. Tokeo likawa kwamba wakawa baba za watoto walio nusu-binadamu na nusu-malaika ambao waliitwa Wanefili, waliokuja kuwa wachokozi-wajeuri. Yehova aliposababisha ile Gharika kubwa, iliharibu wanadamu waliofisidiwa na uzao usio wa asili wa wale malaika wasiotii. Hao malaika waasi walitoroka uharibifu kwa kuvua miili yao ya nyama na kurudi kwenye makao ya roho. Lakini Mungu aliwazuia roho hawa waovu kwa kuwatendea kuwa waliotupwa katika giza la kiroho. (Mwanzo 6:1-7, 17; Yuda 6) Hata hivyo, Shetani, “mtawala wa roho waovu,” na malaika wake waovu wameendelea na uasi wao. (Luka 11:15, NW) Mradi wao ni nini?

5. Shetani na roho wake waovu wana kusudi gani, nao hutumia nini kunasa watu?

5 Kusudi ovu la Shetani na roho wake waovu ni kugeuza watu dhidi ya Yehova Mungu. Kwa hiyo, waovu hao wamekuwa wakiongoza watu vibaya, kuwaogopesha, na kuwashambulia muda wote wa historia. (Ufunuo 12:9) Vielelezo vya siku ya kisasa vinathibitisha kwamba ujeuri wa roho waovu ni mbaya zaidi sasa kuliko vile imekuwa wakati mwingine wowote. Ili kunasa watu, mara nyingi roho waovu hutumia uwasiliani-roho katika namna zao zote. Hao roho waovu hutumiaje chambo hiki, nawe unaweza kujikingaje?

JINSI ROHO WAOVU HUJARIBU KUKUONGOZA VIBAYA

6. Uwasiliani-roho ni nini, na ni nini baadhi ya namna za huo?

6 Uwasiliani-roho ni nini? Ni kuhusika na roho waovu, moja kwa moja au kupitia mwasiliani-roho wa kibinadamu. Uwasiliani-roho husaidia roho waovu kama vile chambo husaidia wawindaji: Huvutia windo. Na kama vile mwindaji hutumia namna mbalimbali za vyambo ili kuvuta wanyama ndani ya mtego wake, ndivyo roho waovu hutia moyo namna mbalimbali za uwasiliani-roho ili kuwaleta wanadamu chini ya udhibiti wao. (Linganisha Zaburi 119:110.) Baadhi ya namna hizo ni uaguzi, mizungu, kutafuta ndege, uchawi, ulozi, kuwaendea wawasiliani-roho, na kuwasiliana na wafu.

7. Uwasiliani-roho umeenea kadiri gani, na sababu gani unasitawi hata katika mabara yaitwayo eti ya Kikristo?

7 Hivyo vyambo huwa na mafanikio, kwani uwasiliani-roho huvutia watu ulimwenguni pote. Wale wanaoishi katika vijiji vya msituni huendea waganga, na wale wafanyao kazi ofisini mjini huendea wanajimu (wataalamu wa nyota). Uwasiliani-roho unasitawi hata katika mabara yaitwayo eti ya Kikristo. Utafiti huonyesha kwamba katika Marekani pekee, magazeti yapatayo 30 yenye jumla ya nakala 10,000,000 zinazogawanywa, hushughulika hasa na namna mbalimbali za uwasiliani-roho. Kila mwaka Wabrazili hutumia dola zaidi ya milioni 500 kwa vitu vinavyohusiana na uwasiliani-roho. Hata hivyo, asilimia 80 ya wale wanaoenda kwa kawaida kwenye vitovu vya ibada inayohusiana na uwasiliani-roho katika nchi hiyo ni Wakatoliki waliobatizwa ambao huhudhuria Misa pia. Kwa kuwa makasisi wengine huzoea uwasiliani-roho, watu wengi wa kidini hufikiri kwamba kufuata zoea hilo kunakubalika kwa Mungu. Lakini je, ni hivyo?

SABABU KWA NINI BIBLIA HUPINGA UWASILIANI-ROHO

8. Ni nini maoni ya Kimaandiko juu ya uwasiliani-roho?

8 Ikiwa umefundishwa kwamba namna fulani za uwasiliani-roho ni njia za kuwasiliana na roho wazuri, huenda ukashangaa kujua yale ambayo Biblia husema juu ya uwasiliani-roho. Watu wa Yehova walionywa hivi: ‘Msiwaendee wenye pepo [“wawasiliani-roho,” NW] wala wachawi; msiwatafute; ili kutiwa unajisi na wao.’ (Mambo ya Walawi 19:31; 20:6, 27) Kitabu cha Biblia cha Ufunuo hutoa onyo kwamba mwisho wa “wale wanaozoea uwasiliani-roho” utakuwa katika “ziwa ambalo huwaka moto na salfa. Hii humaanisha kifo cha pili [cha milele].” (Ufunuo 21:8, NW; 22:15, NW) Namna zote za uwasiliani-roho hazikubaliki kwa Yehova Mungu. (Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Sababu gani ni hivyo?

9. Sababu gani tunaweza kukata maneno kwamba ujumbe mbalimbali wa siku hii unaotoka kwenye ulimwengu wa roho hautokani na Yehova?

9 Yehova alituma roho wazuri, au malaika waadilifu, wawasiliane na wanadamu fulani kabla ya Biblia kukamilishwa. Tangu kukamilishwa kwalo, Neno la Mungu limeandaa mwongozo ambao wanadamu wanahitaji ili kumtumikia Yehova kwa njia ya kukubalika. (2 Timotheo 3:16, 17; Waebrania 1:1, 2) Yeye hatoi ujumbe kupitia wawasiliani-roho badala ya kupitia Neno lake takatifu. Ujumbe huo wote wa siku hii unaotoka kwenye ulimwengu wa roho hutokana na roho waovu. Zoea la uwasiliani-roho laweza kuongoza kwenye hali ya kusumbuliwa na roho waovu au hata kupagawa na roho waovu. Kwa hiyo, Mungu hutuonya kwa upendo tusijihusishe na mazoea ya uwasiliani-roho. (Kumbukumbu la Torati 18:14; Wagalatia 5:19-21) Zaidi ya hayo, ikiwa tungeendelea kuzoea uwasiliani-roho baada ya kujua maoni ya Yehova juu ya huo, tungekuwa tukiwaunga mkono wale roho waovu wenye kuasi na tungekuwa adui za Mungu.—1 Samweli 15:23; 1 Mambo ya Nyakati 10:13, 14; Zaburi 5:4.

10. Uaguzi ni nini, na sababu gani tuuepuke?

10 Namna moja ya uwasiliani-roho inayopendwa na wengi ni uaguzi—kujaribu kujua habari za wakati ujao au juu ya jambo fulani lisilojulikana, kwa msaada wa roho. Baadhi ya namna za uaguzi ni unajimu, kutazama ndani ya matufe ya kifuwele, kufafanua ndoto, kusoma kiganja cha mkono, na kutabiri matukio kwa kutumia karata za kutabiri jaha. Wengi huona uaguzi kuwa tafrija isiyo na madhara, lakini Biblia huonyesha kwamba wenye kutabiri matukio na roho waovu wanahusiana sana. Kwa kielelezo, Matendo 16:16-19 hutaja “pepo wa uaguzi” aliyemwezesha msichana fulani azoee “[“ustadi wa,” NW] kuagua.” Hata hivyo, uwezo wake wa kutabiri juu ya wakati ujao ulipotea wakati huyo roho mwovu alipoondoshwa. Kwa wazi, uaguzi ni chambo kinachotumiwa na roho waovu ili kuvuta watu waingie ndani ya mtego wao.

11. Majaribio ya kuwasiliana na wafu huongozaje kwenye mtego?

11 Ikiwa unahuzunika kwa sababu ya kifo cha mshiriki wa familia mpendwa au rafiki wa karibu, ungeweza kwa urahisi kushawishwa na chambo kingine. Mwasiliani-roho angeweza kukupa habari ya pekee au angeweza kusema kwa sauti inayoonekana kuwa ya yule mtu aliyekufa. Jihadhari! Majaribio ya kuwasiliana na wafu huongoza kwenye mtego. Sababu gani? Kwa sababu wafu hawawezi kusema. Kama vile unavyokumbuka bila shaka, Neno la Mungu husema waziwazi kwamba wakati wa kifo mtu “huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.” Wafu “hawajui neno lo lote.” (Zaburi 146:4; Mhubiri 9:5, 10) Zaidi ya hayo, kwa kweli ni roho waovu ambao wamejulikana kuiga sauti ya aliyekufa na kumpa mwasiliani-roho habari za yule ambaye amekufa. (1 Samweli 28:3-19) Kwa hiyo “mtu [yeyote] awaombaye wafu” amenaswa na roho waovu na anatenda kinyume cha mapenzi ya Yehova Mungu.—Kumbukumbu la Torati 18:11, 12; Isaya 8:19.

KUTOKA KUVUTIA HADI KUSHAMBULIA

12, 13. Kuna uthibitisho gani kwamba roho waovu huendelea kushawishi na kusumbua watu?

12 Unapotii shauri la Neno la Mungu kuhusiana na uwasiliani-roho, unakatalia mbali chambo cha roho waovu. (Linganisha Zaburi 141:9, 10; Warumi 12:9.) Je, hilo lamaanisha kwamba roho waovu wataacha kujaribu kukunasa? La hasha! Baada ya kujaribu kumshawishi Yesu mara tatu, Shetani “akaondoka kwake mpaka wakati mwingine unaofaa.” (Luka 4:13, NW) Vivyo hivyo, roho wakaidi hawavutii watu tu bali pia huwashambulia.

13 Kumbuka mazungumzo yetu ya mapema juu ya shambulio la Shetani dhidi ya mtumishi wa Mungu Ayubu. Ibilisi alisababisha mifugo yake ipotee na pia kifo cha watumishi wake walio wengi. Shetani hata aliwaua watoto wa Ayubu. Kisha, Ibilisi akampiga Ayubu mwenyewe kwa ugonjwa wenye maumivu. Lakini Ayubu alishika uaminifu-maadili wake kwa Mungu naye akabarikiwa sana. (Ayubu 1:7-19; 2:7, 8; 42:12) Tangu wakati huo, roho waovu wamefanya watu fulani wasiweze kusema au wawe vipofu nao wameendelea kujifurahisha wanadamu watesekapo. (Mathayo 9:32, 33; 12:22; Marko 5:2-5) Leo, ripoti zinaonyesha kwamba roho waovu husumbua watu fulani kingono na husababisha wengine warukwe akili. Wao huchochea wengine bado waue kimakusudi na kujiua, ambazo ni dhambi dhidi ya Mungu. (Kumbukumbu la Torati 5:17; 1 Yohana 3:15) Hata hivyo, maelfu ya watu ambao wakati mmoja walinaswa na roho hawa waovu wameweza kujiweka huru. Hilo limewezekanaje kwao? Wamefanya hilo kwa kuchukua hatua ya muhimu.

JINSI YA KUKINZA ROHO WAOVU

14. Kwa kupatana na kielelezo cha Wakristo wa Efeso wa karne ya kwanza, unaweza kukinzaje roho waovu?

14 Ni nini njia moja ambayo unaweza kukinza roho waovu na kujilinda mwenyewe na familia yako dhidi ya mitego yao? Wakristo wa karne ya kwanza katika Efeso waliokuwa wamezoea uwasiliani-roho kabla ya kuwa waamini walichukua hatua chanya. Sisi twasoma kwamba “watu wengi katika wale waliotumia mambo ya uganga wakakusanya vitabu vyao, wakavichoma moto mbele ya watu wote.” (Matendo 19:19) Hata ikiwa wewe hujazoea uwasiliani-roho, tupilia mbali kitu chochote chenye matumizi au madokezo ya uwasiliani-roho. Hivyo vinatia ndani vitabu, magazeti, vidio, picha kubwa za kubandikwa ukutani, mirekodi ya muziki, na vitu vinavyotumiwa kwa makusudi yanayohusiana na uwasiliani-roho. Vinavyotiwa ndani pia ni sanamu, hirizi na vitu vingine vinavyovaliwa kwa ajili ya ulinzi, na zawadi zinazopokewa kutoka kwa wale wanaozoea uwasiliani-roho. (Kumbukumbu la Torati 7:25, 26; 1 Wakorintho 10:21) Kutoa kielezi: Mume na mke fulani katika Thailand walikuwa wamesumbuliwa na roho waovu. Kisha wakatupilia mbali vitu vilivyohusika na uwasiliani-roho. Tokeo lilikuwa nini? Kushambuliwa na roho waovu kuliondolewa kwao na baada ya hapo wakafanya maendeleo halisi ya kiroho.

15. Katika kukinza majeshi ya roho waovu, ni hatua gani nyingine inayohitajiwa?

15 Ili kukinza roho waovu, hatua nyingine inayohitajiwa ni kutumia shauri la mtume Paulo la kujivika suti kamili ya silaha za kiroho zinazopewa na Mungu. (Waefeso 6:11-17) Ni lazima Wakristo watie nguvu ulinzi wao dhidi ya roho waovu. Hatua hii inatia ndani nini? “Zaidi ya yote,” akasema Paulo, “mkiitwaa ngao ya imani, ambayo kwa hiyo mtaweza kuizima mishale yote yenye moto ya yule mwovu.” Kwa kweli, kadiri imani yako ilivyo yenye nguvu zaidi, ndivyo uwezo wako wa kukinza majeshi ya roho waovu utakavyokuwa mkubwa zaidi.—Mathayo 17:14-20.

16. Unaweza kutiaje imani yako nguvu?

16 Unaweza kutiaje imani yako nguvu? Kwa kuendelea kujifunza Biblia na kutumia shauri layo maishani mwako. Nguvu ya imani ya mtu yategemea hasa uthabiti wa msingi wayo—ujuzi juu ya Mungu. Je, hukubali kwamba ujuzi sahihi ambao umepata na kuzingatia kadiri ambavyo umejifunza Biblia, umejenga imani yako? (Warumi 10:10, 17) Kwa hiyo, uendelezapo funzo hili na kufanya desturi yako iwe kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova, bila shaka imani yako itatiwa nguvu hata zaidi. (Warumi 1:11, 12; Wakolosai 2:6, 7) Itakuwa ngome yenye uweza dhidi ya mashambulio ya roho waovu.—1 Yohana 5:5.

17. Ni hatua zipi za ziada ambazo huenda zikahitajiwa katika kukinza majeshi ya roho waovu?

17 Ni hatua zipi nyingine zinazoweza kuchukuliwa na mtu ambaye ameazimia kukinza majeshi ya roho waovu? Wakristo Waefeso walihitaji ulinzi kwa sababu wao waliishi katika jiji lililojaa ibada ya roho waovu. Kwa hiyo, Paulo aliwaambia hivi: “Mkisali kila wakati katika [r]oho.” (Waefeso 6:18) Kwa kuwa twaishi katika ulimwengu uliojaa roho waovu, kusali mara nyingi tukimwomba Mungu ulinzi wake ni kwa muhimu katika kukinza roho waovu. (Mathayo 6:13) Jambo linalosaidia katika habari hii ni msaada wa kiroho na sala za wazee waliowekwa rasmi katika kutaniko la Kikristo.—Yakobo 5:13-15.

ENDELEA NA PIGANO LAKO DHIDI YA ROHO WAOVU

18, 19. Ni nini kinachoweza kufanywa ikiwa roho waovu wanamsumbua mtu tena?

18 Hata baada ya kuchukua hatua hizi za msingi, bado wengine wamesumbuliwa na roho waovu. Kwa mfano, mtu mmoja katika Côte d’Ivoire alijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova akaharibu hirizi zake zote. Baada ya hapo, alifanya maendeleo mazuri, akaweka wakfu maisha yake kwa Yehova, naye akabatizwa. Lakini juma moja baada ya ubatizo wake, roho waovu walianza kumsumbua tena, na sauti zilimwambia aache imani yake aliyopata. Ikiwa hilo lingekupata, je, lingemaanisha kwamba ulikuwa umepoteza ulinzi wa Yehova? Sivyo hasa.

19 Ingawa mtu mkamilifu Yesu Kristo alikuwa na ulinzi wa kimungu, yeye alisikia sauti ya yule kiumbe aliye roho mwovu, Shetani Ibilisi. Yesu alionyesha la kufanywa katika kisa cha jinsi hiyo. Yeye alimwambia Ibilisi: “Nenda zako, Shetani.” (Mathayo 4:3-10) Vivyo hivyo, wewe unapaswa kukataa kusikiliza sauti zinazotoka ulimwengu wa roho. Kinza roho waovu kwa kumwomba Yehova akusaidie. Ndiyo, sali kwa sauti kubwa ukitumia jina la Mungu. Mithali 18:10 yasema: “Jina la BWANA [“Yehova,” NW] ni ngome imara; mwenye haki huikimbilia, akawa salama.” Huyo mwanamume Mkristo katika Côte d’Ivoire alifanya hivyo, na roho waovu wakaacha kumsumbua.—Zaburi 124:8; 145:18.

20. Kwa muhtasari, unaweza kufanya nini ili kukinza roho waovu?

20 Yehova ameruhusu roho waovu waendelee kuwako, lakini yeye huonyesha nguvu yake, hasa kwa niaba ya watu wake, na jina lake linatangazwa duniani pote. (Kutoka 9:16) Ukikaa karibu na Mungu, wewe huhitaji kuhofu roho waovu. (Hesabu 23:21, 23; Yakobo 4:7, 8; 2 Petro 2:9) Nguvu yao ina mipaka. Wao waliadhibiwa katika siku ya Noa, wakatupwa kutoka mbinguni katika nyakati za majuzi, na sasa wanangojea hukumu ya mwisho. (Yuda 6; Ufunuo 12:9; 20:1-3, 7-10, 14) Kwa kweli, wanauogopa uharibifu wao unaokuja. (Yakobo 2:19) Kwa hiyo iwe roho waovu wanajaribu kukuvuta na namna fulani ya chambo au kukushambulia kwa njia yoyote ile, wewe waweza kuwakinza. (2 Wakorintho 2:11) Epuka kila namna ya uwasiliani-roho, tumia shauri la Neno la Mungu, na utafute kibali cha Yehova. Fanya hivyo bila kukawia, kwa maana uhai wako wategemea kukinza kwako majeshi ya roho waovu!

TAHINI UJUZI WAKO

Roho waovu hujaribuje kuongoza watu vibaya?

Sababu gani Biblia hupinga uwasiliani-roho?

Mtu anaweza kujiwekaje huru na majeshi ya roho waovu?

Sababu gani uendelee kukinza roho waovu?

[Picha katika ukurasa wa 110]

Wewe huonaje uwasiliani-roho katika namna zao nyingi?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki