Sura 10
Roho Waovu Ni Wenye Nguvu
1. Sababu gani watu wengi wanaamini kwamba wanaweza kusema na wafu?
MARA NYINGI watu wanasema kwamba wamezungumza na wafu. James A. Pike, askofu mashuhuri wa Episkopali ambaye sasa ni mfu, alisema kwamba alizungumza na mwanawe aliyekufa, Jim. Kulingana na Pike, mwanawe alimwambia hivi: “Ninao watu chungu nzima wanaonizunguka, na inakuwa kana kwamba mikono inaniinua . . . nilipoweza kupata njia ya kukupasha habari, hapo tu ndipo nilipoweza kujiondolea huzuni nyingi niliyokuwa nayo.”
2. (a) Sababu gani hakuna mtu anayeweza kusema na wafu? (b) Basi ni maulizo gani yanayotokezwa?
2 Kwa kuwa vituko hivyo ni vya kawaida sana, ni wazi kwamba watu wengi wamesema na mtu fulani wa ulimwengu wa roho. Lakini kwa kufanya hivyo hawakuwa wakizungumza na wafu. Biblia inasema waziwazi hivi: “Lakini wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Basi ikiwa si wafu wanaosema kutoka ulimwengu wa roho, ni nani wanaosema? Ni nani wanaojifanya kuwa watu waliokufa?
3. (a) Ni nani wanaojifanya kuwa watu waliokufa, na kwa sababu gani? (b) Mara nyingi roho waovu wanawapa nani habari hizo?
3 Ni roho waovu. Roho hao, au mashetani, ni malaika waliojiunga na Shetani katika kumwasi Mungu. Sababu gani wanajifanya kuwa watu waliokufa? Ni kwa kusudi la kuendeleza lile wazo la kwamba wafu wangali wanaishi. Roho waovu wameongoza watu wengine waamini vilevile uongo wa kwamba kifo ni badiliko tu la kwenda kwenye uzima wa namna nyingine. Ili kueneza uongo huo, roho waovu wanatolea watu njia za kupashana habari nao, njia hizo zikiwa ni wapiga ramli na wachawi (au, walogi) walio na maarifa ya pekee yanayoonekana kama kwamba yanatoka kwa watu waliokufa.
KUJIFANYA KWA UONGO KUWA SAMWELI ALIYEKUFA
4. (a) Sababu gani Mfalme Sauli alitafuta sana msaada? (b) Ni sheria gani ya Mungu iliyopinga wachawi na wapiga ramli?
4 Kuna mfano mmoja katika Biblia wa roho mwovu aliyejifanya aonekane kama nabii wa Mungu aliyekufa, yaani, Samweli. Ilikuwa katika mwaka wa 40 wa utawala wa Mfalme Sauli. Jeshi lenye nguvu la Wafilisti lilikuja kupigana na jeshi la Kiisraeli la Sauli, naye akaogopa sana. Sauli alijua sheria hii ya Mungu: “Msiwaendee wenye pepo, wala wachawi; msiwatafute; ili kutiwa unajisi na wao.” (Mambo ya Walawi 19:31) Walakini, baadaye Sauli alimwacha Yehova. Kwa hiyo Samweli, aliyekuwa hai wakati huo, akakataa kabisa kumwona Sauli. (1 Samweli 15:35) Na sasa, katika wakati huu wa taabu, Mfalme Sauli alihitaji msaada wa haraka sana kwa sababu Yehova hakusikiliza maombi yake.
5. (a) Sauli alikwenda wapi akapate msaada? (b) Yule mchawi aliweza kufanya nini?
5 Sauli alitaka sana kujua mambo ambayo yangetukia hata akamwendea mchawi katika Endori. Mchawi huyo wa kike aliweza kutokeza umbo la mtu aliloweza kuliona yeye mwenyewe. Alipoeleza umbo hilo lilivyokuwa, Sauli akamtambua kuwa “Samweli.” Ndipo mtu huyo wa kiroho, akijifanya kuwa Samweli, akasema hivi: “Mbona umenitaabisha mimi, hata kunipandisha juu?” Sauli akajibu: “Mimi nimetaabika sana; kwa kuwa hao Wafilisti wananifanyia vita.” Yule mtu wa kiroho akajibu hivi: “Kwa nini kuniuliza mimi, akiwa [Yehova] amekuacha, naye amekuwa adui yako?” Kisha mtu mwovu huyo wa kiroho, aliyekuwa akijifanya kuwa Samweli aliyekufa, akaendelea kumwambia Sauli kwamba angeuawa wakati wa kupigana na Wafilisti.—1 Samweli 28:3-19.
6. Kwa sababu gani haiwezi kuwa ni Samweli aliyesema na Sauli?
6 Kwa wazi, si Samweli ambaye mchawi huyo alikuwa amepashana habari naye. Samweli alikuwa amekufa, na wakati mtu anapokufa “huurudia udongo wa-ke, siku hiyo mawazo yake yapotea.” (Zaburi 146:4) Kufikiria kidogo jambo hilo kunaonyesha zaidi kwamba sauti hiyo haikuwa kamwe ile ya Samweli aliyekufa. Samweli alikuwa nabii wa Mungu. Basi alikuwa amepinga wachawi. Na, kama tulivyokwisha kuona, alipokuwa hai alikuwa amekataa kusema tena na Sauli asiyetii. Hivyo basi, ikiwa Samweli angekuwa bado hai, je! angeruhusu mchawi amfanyie mpango wa kuonana na Sauli? Fikiri vilevile: Yehova alikuwa amekataa kumpa Sauli habari yo yote. Je! mchawi angeweza kumlazimisha Yehova ampe Sauli ujumbe kupitia Samweli aliyekufa? Na ikiwa kwa hakika walio hai wangeweza kuzungumza na wapendwa waliokufa, bila shaka Mungu wa upendo hangesema kwamba walikuwa wamekuwa na “unajisi” kwa sababu ya kuendea mchawi.
7. Ni onyo gani ambalo Mungu alitoa ili kulinda watu wake juu ya roho waovu?
7 Uhakika ni kwamba roho waovu wanakusudia kuumiza wanadamu, na hivyo Yehova anatoa maonyo ili kulinda watumishi wake. Ebu soma onyo hili ambalo taifa la Israeli lilipewa. Linakujulisha kidogo njia ambazo mashetani wanatumia ili kupoteza watu. Biblia inasema hivi: “Asionekane kwako . . . mtu atazamaye bao, wala mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri, wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi, wala mtu awaombaye wafu. Kwa maana mtu atendaye hayo ni chukizo kwa [Yehova].” (Kumbukumbu la Torati 18:1-12) Imetupasa tutake kuchunguza wanayofanya roho waovu ili waumize watu leo na namna tunavyoweza kujilinda tusiumizwe nao. Lakini kabla ya kujifunza hayo, ebu tuzungumze ni wakati gani na namna gani roho hao walianza kuwa waovu.
MALAIKA WALIOGEUKA KUWA ROHO WAOVU
8. (a) Ni nani vilevile ambao Shetani alishawishi wamwasi Mungu? (b) Baada ya kuacha kazi yao mbinguni, walikwenda wapi?
8 Kwa kumwambia Hawa uongo katika bustani ya Edeni, kiumbe fulani wa kimalaika alijifanya kuwa yule roho mwovu Shetani Ibilisi. Baada ya hapo alianza kujaribu kushawishi malaika wengine vilevile wampinge Mungu. Baadaye alifaulu. Malaika fulani waliacha kazi ambayo Mungu alikuwa amewapa wafanye huko mbinguni, wakashuka duniani wakajifanyia wenyewe miili nyama kama ile ya wanadamu. Mwanafunzi Mkristo Yuda aliandika juu yao alipotaja “malaika wale ambao hawakutunza cheo chao cha kwanza bali wakaacha makao yao wenyewe yanayofaa.” (Yuda 6, NW) Sababu gani walikuja duniani? Ni tamaa gani mbaya ambayo Shetani alitia katika moyo wao ili waache vyeo bora walivyokuwa navyo mbinguni?
9. (a) Sababu gani malaika hao walikuja duniani? (b) Biblia inaonyeshaje kwamba walilofanya lilikuwa kosa?
9 Biblia inatujulisha inaposema hivi: “Wana wa Mungu waliwaona hao binti za wanadamu ya kuwa ni wazuri; wakajitwalia wake wo wote waliowachagua.” (Mwanzo 6:2) Ndiyo, malaika hao walijivika miili yenye nyama. Kisha wakaja du-niani wafanye ngono pamoja na wanawake warembo. Lakini mahaba hayo hayakuwafaa malaika. Hilo lilikuwa tendo la kutokutii. Biblia inaonyesha kwamba walilofanya lilikuwa kosa kubwa kama matendo ya watu wa Sodoma na Gomora ya ngono za wanaume kwa wanaume. (Yuda 6, 7) Kulitokea nini?
10, 11. (a) Malaika hao walizaa watoto wa aina gani? (b) Jambo gani liliwapata majitu hao Gharika ilipokuja? (c) Jambo gani liliwapata malaika wakati wa Gharika hiyo?
10 Wake wa malaika hao waliwazalia vitoto. Lakini vitoto hivyo vilikuwa tofauti. Vilizidi kuwa vikubwa zaidi na zaidi mpaka vikawa majitu, ndiyo, majitu yenye uovu. Biblia inawaita “watu hodari zamani, watu wenye sifa.” Majitu hayo yalijaribu kulazimisha kila mtu awe mbaya kama wao. Basi, Biblia inasema kwamba ‘maovu ya mwanadamu yalikuwa makubwa duniani na kila kusudi alilowaza moyoni mwake likawa ni baya tu sikuzote.’ (Mwanzo 6:4, 5) Basi Yehova akaileta Gharika. Majitu hayo, au “Wanefili,” na watu wote waovu walikufa maji. Lakini namna gani malaika waliokuwa wamekuja duniani?
11 Hawakufa maji. Waliivua miili yao yenye nyama wakarudi mbinguni wakiwa watu wa kiroho. Lakini hawakuruhusiwa wawe tena sehemu ya tengenezo la Mungu la malaika watakatifu. Badala yake, Biblia inasema kwamba “Mungu hakukosa kuadhibu malaika waliofanya dhambi, bali, kwa kuwatupa katika Tartaro, aliwapeleka kwenye mashimo yenye giza zito mno wawekwe akiba kwa hukumu.”—2 Petro. 2:4, NW.
12. (a) Kulitukia nini malaika hao waovu waliporudi mbinguni? (b) Sababu gani hawa-wezi kuvaa tena miili ya kibinadamu? (c) Hivyo sasa wanafanya nini?
12 Malaika hao waovu hawakutupwa katika mahali halisi panapoitwa Tartaro. Badala yake, Tartaro, neno ambalo limetafsiriwa vibaya kuwa “helo” katika Biblia fulani, linamaanisha hali ya kushushwa au ya kuanguka kwa hao malaika. Walikatiliwa mbali na nuru ya kiroho ya tengenezo la Mungu, nao wanangojea uharibifu wa milele tu. (Yakobo 2:19; Yuda 6) Tangu wakati wa Gharika, Mungu hajaruhusu malaika hao mashetani wajivike miili yenye nyama, hivyo hawawezi kutosheleza moja kwa moja nyege zao zisizo za asili. Hata hivyo bado wanaweza kutumia uwezo wao wenye hatari kuongoza wanaume na wanawake. Kwa kweli, kwa msaada wa mashetani hao Shetani ‘anapoteza dunia nzima inayokaliwa na watu.’ (Ufunuo 12:9, NW) Ongezeko kubwa la uasherati, jeuri na makosa mengine lililopo leo linaonyesha tunahitaji kujilinda tusipotezwe nao.
NAMNA ROHO WAOVU WANAVYOPOTEZA WATU
13. (a) Roho waovu wanapotezaje watu? (b) Maana yake nini kupashana habari na roho waovu, nayo Biblia inasema nini juu yake?
13 Tulijifunza hapo mapema kwamba Shetani, akiwa ndiye “mungu wa hii taratibu ya mambo,” anatumia serikali za ulimwengu na dini ya uongo ili apofushe watu wasizione kweli za Biblia. (2 Wakorintho 4:4, NW) Njia nyingine kubwa ambayo roho waovu wanatumia ili kupoteza wanaume na wanawake ni kupashana habari na hao wenyewe. Kupashana habari na roho waovu ni nini? Ni kuzungumza na mashetani, moja kwa moja au kwa kutumia mwanadamu fulani. Kupashana habari nao kunaleta mtu chini ya uvutano wa mashetani. Biblia inatuonya tujitenge na kila zoea la kupashana habari na roho waovu.—Wagala-tia 5:19-21; Ufunuo 21:8.
14. (a) Uaguzi ni nini? (b) Biblia inasema nini juu yake?
14 Uaguzi ni namna iliyo ya kawaida sana ya kupashana habari na roho waovu. Ni zoea la kujaribu kujua habari za wakati ujao, au juu ya jambo fulani lisilojulikana, kwa msaada wa roho wasioonekana. Hilo linaonyeshwa na maneno ambayo Luka mwanafunzi Mkristo aliandika: “Kijakazi kimoja aliyekuwa na pepo wa uaguzi akatukuta, aliyewapatia bwana zake faida nyingi kwa kuagua.” Mtume Paulo aliweza kumwokoa kijakazi huyo katika uwezo wa roho huyo mwovu, asiweze tena kutabiri mambo ya wakati ujao. —Matendo 16:16-19.
15. (a) Ni baadhi ya mambo gani yanayohusiana na kupashana habari na roho waovu? (b) Sababu gani kushiriki mambo hayo ni hatari?
15 Watu wengi wanapenda kupashana habari na roho waovu kwa sababu ni jambo la kushangaza au ni ajabu kubwa. Kunawavutia. Hivyo wanajishughulisha na uchawi, ulozi, kutia wengine katika hali kama ya usingizi, uchawi wa kufanya miujiza, maajabu na hata kuzungumza na wafu, unajimu, kupiga bao au jambo jinginelo linalohusu kupashana habari na roho waovu. Huenda wakasoma vitabu juu ya mambo hayo, au kwenda kwenye sinema, au kutazama vipindi vya televisheni vinavyoonyesha mambo hayo. Huenda hata wakahudhuria mkutano ambapo mchawi anataka kuzungumza na ulimwengu wa roho. Lakini yote hayo si yenye hekima kwa mtu anayetaka kumtumikia Mungu wa kweli. Vilevile ni yenye hatari. Yanaweza kuongoza kwenye taabu kubwa sasa. Vilevile, Mungu atahukumu na kuwatu-pa wote wanaozoea kupashana habari na roho waovu.—Ufunuo 22:15.
16. Biblia inaonyeshaje kwamba Wakristo wana vita juu ya roho waovu?
16 Hata mtu anapofanya yote kadiri awezavyo ili aache kupashana habari na roho waovu, huenda bado akashambuliwa na roho waovu. Kumbuka kwamba sauti ya Ibilisi mwenyewe ilisikiwa na Yesu Kristo, akimshawishi avunje sheria ya Mungu. (Mathayo 4:8;9) Watumishi wengine wa Mungu wamepata mashambulio ya namna hiyo. Mtume Paulo alisema hivi: “Tunako kushindana mweleka . . . juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” Maana yake ni kwamba lazima kila mtumishi wa Mungu avae “silaha kamili kutoka kwa Mungu [ili apate] kuweza kupinga.”—Waefeso 6:11, 12, NW.
KUPINGA MASHAMBULIO YA ROHO WAOVU
17. Imekupasa ufanye nini “sauti” kutoka ulimwengu wa roho ikisema na wewe?
17 Imekupasa ufanye nini “sauti” kutoka ulimwengu wa roho ikisema na wewe? Namna gani “sauti” hiyo ikijifanya isikike kama ya mtu wa ukoo aliyekufa au roho mzuri? Yesu alifanya nini wakati “mtawala wa mashetani” aliposema naye? (Mathayo 9: 34, NW) Alisema hivi: “Nenda zako, Shetani.” (Mathayo 4:10) Wewe vilevile unaweza kufanya hivyo. Vilevile, unaweza kumwomba Yehova msaada. Sali kwa sauti kubwa na kutumia jina la Mungu. Kumbuka kwamba yeye ana nguvu nyingi kuliko roho waovu. Fuata mwendo huo wa hekima. Usisikilize sauti hizo zinazotoka kwenye ulimwengu wa roho. (Mithali 18:10; Yakobo 4:7) Haimaanishi kwamba kila mtu anayesikia “sauti” anaambiwa mambo na mashetani. Nyakati nyingine kusikia sauti kunaweza kusababishwa na magonjwa fulani ya mwili au ya akili.
18. Ni mfano gani wa Wakristo wa kwanza katika Efeso ambao ni mzuri kufuata ikiwa mtu anataka kuacha kupashana habari na roho waovu?
18 Labda wakati fulani ulishiriki mazoea fulani ya kupashana habari na roho waovu na sasa unataka kuyaacha. Unaweza kufanya nini? Basi, uchunguze mfano wa Wakristo wa kwanza katika Efeso. Walipokwisha kulipokea “neno la [Yehova]” likihubiriwa na mtume Paulo, Biblia inasema hivi: “Na watu wengi katika wale waliotumia mambo ya uganga wakakusanya vitabu vyao, wakavichoma moto mbele ya watu wote.” Na vitabu hivyo vilikuwa na thamani ya vipande vya fedha 50,000! (Matendo 19:19, 20) Kama una vitu vinavyohusu moja kwa moja kupashana habari na roho waovu, mwendo ulio wa hekima ni kuviharibu hata ikiwa ni vya fedha nyingi. Kwa kufanya hivyo unaiga wale waliogeuka wakawa wafuasi wa Kristo katika Efeso.
19. (a) Ni nini wasichojua watu walio wengi wanaopashana habari na roho waovu? (b) Ikiwa tunataka kuishi milele kwa furaha duniani, lazima tufanye nini?
19 Kwa kuwa leo watu wengi wanapendezwa sana na maajabu na mambo ya mafumbo, watu zaidi na zaidi wanapashana habari na roho waovu. Walakini, wengi kati ya watu hao hawajui kwamba wanajishughulisha kwa hakika na roho waovu. Huo ni mchezo wenye hatari. Roho waovu wana uwezo wa kuumiza watu. Ni waovu sana. Na, kabla Kristo hajawafunga milele katika uharibifu, wanafanya yote wawezayo ili watie wanadamu chini ya uwezo wao mwovu. (Mathayo 8:28, 29) Basi ikiwa unataka kuishi milele kwa furaha duniani baada ya uovu wote kuondolewa, ni lazima ujiepushe na uwezo wa mashetani kwa kujitenga na kila namna ya kupashana habari na roho hao waovu.
[Picha katika ukurasa wa 91]
Yule mwanamke mchawi wa Endori alipashana habari na nani?
[Picha katika ukurasa wa 92, 93]
Wana wa Mungu wa kimalaika wakawachunguli hao binti za wanadamu
[Picha katika ukurasa wa 94]
Hao malaika waliojivika miiii ya nyama hawakufa maji. Waliivua wakarudi mbinguni
[Picha katika ukurasa wa 97]
Biblia inaonya hivi: ‘Jitengeni na namna zote za kupashana habari na roho waovu’
[Picha katika ukurasa wa 98]
Wale waliogeuka wakawa Wakristo katika Efeso walichoma vitabu vyao vya mambo ya kupashana habari na roho waovu, na huo ni mfano bora kwetu leo