Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 7/15 kur. 4-7
  • Watawala Katika Makao ya Roho

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Watawala Katika Makao ya Roho
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kiumbe Halisi cha Roho Kinachompinga Mungu
  • Kwa Nini Shetani Ameruhusiwa Kutawala
  • Wakati wa Shetani Ni Mfupi!
  • Kushangilia Chini ya Utawala wa Ufalme
  • Adui wa Uzima wa Milele
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Shetani Ibilisi
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Shetani
    Amkeni!—2013
  • Uwe Macho​—Shetani Anataka Kukumeza!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 7/15 kur. 4-7

Watawala Katika Makao ya Roho

NANI anayeutawala ulimwengu? Je, kuna usimamizi wa aina fulani unaozidi uwezo wa kibinadamu? Au Mungu amewaacha binadamu wajishughulikie na kujiandalia wenyewe? Tutafutapo majibu ya maswali haya, acheni kwanza tufikirie tukio fulani lililotukia wakati wa huduma ya kidunia ya Yesu Kristo.

Muda mfupi baada ya ubatizo wake, Yesu alijaribiwa na kiumbe cha roho kisichoonekana kiitwacho Shetani Ibilisi. Ikieleza moja la majaribu hayo, Biblia husema: “Ibilisi akamchukua [Yesu] mpaka mlima mrefu mno, akamwonyesha (“falme zote za ulimwengu,” New World Translation) milki zote za ulimwengu, na fahari yake.” (Mathayo 4:8) Kisha Shetani akamwambia Yesu hivi: “Nitakupa mamlaka yote hii na utukufu wazo, kwa sababu nimekabidhiwa, na yeyote nimtakaye mimi humpa hiyo. Kwa hiyo, wewe ukifanya tendo la ibada mbele yangu, yote itakuwa yako.”—Luka 4:6, 7, NW.

Shetani alidai kuwa na mamlaka juu ya falme zote, au serikali, za ulimwengu huu. Je, Yesu alikataa dai hili? La. Kwa kweli, alilithibitisha kwenye tukio jingine kwa kurejezea Shetani kuwa “mkuu (“mtawala,” NW) wa ulimwengu.”—Yohana 14:30.

Kulingana na Biblia, Shetani ni malaika mwovu aliye na uwezo mkubwa. Mtume Mkristo Paulo anamhusianisha Shetani na “majeshi ya roho waovu” naye anazungumza juu yao kuwa “watawala wa ulimwengu wa giza hili.” (Waefeso 6:11, 12, NW) Zaidi ya hayo, mtume Yohana alisema kwamba “dunia yote pia hukaa katika yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Kitabu cha Biblia cha Ufunuo husema kwamba Shetani ‘huudanganya ulimwengu wote.’ (Ufunuo 12:9) Kwa maneno ya ufananisho, Ufunuo pia humfafanua Shetani kuwa joka ambalo linaupa mfumo wa kisiasa wa ulimwengu “nguvu zake na kiti chake cha enzi na uwezo mwingi.”—Ufunuo 13:2.

Matukio ya ulimwengu pia hushuhudia kwamba kuna uwezo mwovu unaotenda kazi, unaochochea binadamu wajiumize. Ni kwa sababu gani nyingine ambayo serikali za binadamu hushindwa kuendeleza amani? Nini kingine kingeweza kufanya watu wachukiane na kuchinjana? Akifadhaishwa na machinjo na kifo katika vita vya wenyewe kwa wenyewe, shahidi mmoja aliyejionea kwa macho alisema: “Mimi sijui jinsi haya yangeweza kutokea. Ni zaidi ya chuki. Ni roho mwovu ambaye anatumia binadamu hawa kumalizana.”

Kiumbe Halisi cha Roho Kinachompinga Mungu

Leo, wengi hawaamini kuna Shetani Ibilisi. Hata hivyo, yeye si uovu tu miongoni mwa binadamu, kama wengine wanavyoamini. Biblia na matukio ya ulimwengu vilevile yanaonyesha kwamba yeye ni mtu halisi. Zaidi ya hayo, Shetani humpinga Yehova Mungu kabisa. Bila shaka, Shetani si sawa na Mungu. Kwa kuwa Yehova ndiye Muumba mwenye uwezo wote, yeye ndiye Mtawala anayestahili juu ya uumbaji wote.—Ufunuo 4:11.

Mungu hakumuumba kiumbe mwovu mpinzani wake. Bali, mmoja wa “wana wa Mungu” wa kimalaika alikuza tamaa ya ubinafsi ajipatie ibada anayostahili Yehova. (Ayubu 38:7; Yakobo 1:14, 15) Tamaa hii ilimwongoza kuingia katika mwendo wa uasi dhidi ya Mungu. Kwa kuasi, kiumbe hiki cha roho kilijifanya Shetani (maana yake “mpingaji”) na Ibilisi (maana yake “mchongezi”). Ukifikiria yote haya, huenda ukashangaa kwa nini Shetani ameruhusiwa kutawala ulimwengu.

Kwa Nini Shetani Ameruhusiwa Kutawala

Je, unakumbuka yale Shetani alimwambia Yesu kuhusu utawala juu ya dunia? “Nitakupa mamlaka yote hii . . . kwa sababu nimekabidhiwa,” Shetani akasema. (Luka 4:6, NW) Taarifa hiyo inaonyesha kwamba Shetani Ibilisi yuna mamlaka kwa ruhusa ya Mungu tu. Lakini kwa nini Mungu amvumilie Shetani?

Jibu la swali hilo linahusiana na matukio katika bustani ya Edeni, ambapo Shetani alianza kazi yake akiwa mtawala wa ulimwengu. Hapo Shetani alidokeza kwamba Mungu alikuwa akitawala kwa njia mbaya kwa kuwanyima kitu kizuri mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa. Kulingana na Shetani, ikiwa wangekula tunda walilokatazwa na Mungu, wangewekwa huru. Adamu na Hawa wangekuwa huru na wenye kujitawala bila Yehova. Wangekuwa kama Mungu mwenyewe!—Mwanzo 2:16, 17; 3:1-5.

Kwa kusema uwongo kwa njia hii na kushawishi Hawa na kupitia kwake kumshurutisha Adamu kuvunja sheria ya Mungu, Shetani aliwaingiza wanadamu wawili wa kwanza chini ya uongozi na utawala wake. Hivyo Ibilisi akawa mungu wao, mpinzani wa Yehova. Hata hivyo, badala ya kuwekwa huru, Adamu na Hawa wakawa watumwa wa Shetani, wa dhambi, na kifo.—Warumi 6:16; Waebrania 2:14, 15.

Kwa kupatana na haki yake kamilifu, Yehova angaliwaua Shetani na wafuasi wake wapya wawili mara moja. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Lakini, kulikuwa na suala la maadili lililotokezwa. Shetani alikuwa ametilia shaka haki ya njia ya Yehova ya kutawala. Kwa hekima yake, Mungu aliruhusu wakati upite ili kwamba ingeweza kuthibitishwa kwamba kujitegemea bila yeye huleta hasara. Yehova aliruhusu waasi hao waendelee kuishi kwa wakati fulani, akiwaruhusu Adamu na Hawa kupata watoto.—Mwanzo 3:14-19.

Ingawa wengi wa watoto wa Adamu hawajajitiisha chini ya utawala wa Yehova, kushughulika kwa Mungu na waabudu Wake kumeonyesha ubora wa utawala huo. Kutambua kwa njia inayofaa mamlaka ya Yehova huleta furaha na usalama wa kweli. Kwa upande mwingine, taabu na ukosefu wa usalama umekuwa tokeo la utawala wa kibinadamu chini ya mwongozo wa Shetani. Ndiyo, “mwanadamu ametawala mwanadamu kwa umizo lake.” (Mhubiri 8:9, NW) Binadamu hawajapata usalama wa kweli na furaha yenye kudumu chini ya utawala wa binadamu katika ulimwengu huu ulio chini ya uwezo wa Shetani. Hata hivyo, kuna sababu inayofaa ya kuwa na mwelekeo chanya.

Wakati wa Shetani Ni Mfupi!

Uvutano wa Shetani duniani ni wa muda tu. Yehova hatavumilia utawala wa kishetani kwa muda mrefu zaidi! Karibuni Ibilisi atanyang’anywa uwezo wa kutenda. Mtawala mpya ataongoza dunia, mfalme mwenye haki aliyechaguliwa na Mungu mwenyewe. Mfalme huyo ni Yesu Kristo. Kuhusu kutawazwa kwake mbinguni, Ufunuo husema: “Ufalme wa dunia umekwisha kuwa ufalme wa Bwana [Yehova] wetu na wa Kristo wake.” (Ufunuo 11:15) Orodha ya matukio ya Biblia, pamoja na kutimizwa kwa unabii wa Kimaandiko, huthibitisha kwamba tukio hili lilitukia katika mwaka wa 1914.—Mathayo 24:3, 6, 7.

Biblia pia inasimulia yaliyotokea muda mfupi baada ya Yesu kutawazwa. Inasema hivi: “Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli [Yesu Kristo] na malaika zake wakapigana na yule joka [Shetani Ibilisi], yule joka naye akapigana nao pamoja na malaika zake; nao hawakushinda, wala mahali pao hapakuonekana tena mbinguni. Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye.”—Ufunuo 12:7-9.

Matokeo ya kufukuzwa kwa Shetani kutoka mbinguni yangekuwa nini? Wale walioko mbinguni wangeshangilia, lakini vipi juu ya wakazi wa dunia? “Ole wa nchi na bahari!” Ufunuo 12:12 lasema, “kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” Kwa kweli, kutupwa kwa Shetani nje ya mbingu kumeletea dunia ole. The Columbia History of the World chasema hivi: “Msiba mkuu wa ile Miaka Minne ya Vita ya 1914–1918 . . . ulionyesha ulimwengu wa Magharibi kuwa haungeweza kulinda maendeleo kutokana na upumbavu au msukumo wao wa uovu. Uhodari wa ulimwengu wa Magharibi daima haujaimarika kutokana na angamizo hilo.”

Ole mwingi wa kizazi hiki umetiwa alama na mengi zaidi ya uhodari uliodhoofika. Yesu alitabiri hivi: “Taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; kutakuwa na njaa, na matetemeko ya nchi mahali mahali.” Pia alitabiri magonjwa. (Mathayo 24:7, 8; Luka 21:11) Zaidi ya hayo, Biblia husema kwamba katika “siku za mwisho” za mfumo wa mambo wa Shetani, wengi wangekuwa “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, . . . wasiotii wazazi wao, . . . wasiotaka kufanya suluhu.” Watu wangekuwa “wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu.”—2 Timotheo 3:1-5.

Vita, magonjwa, upungufu wa chakula, matetemeko ya dunia, na kuharibika kwa maadili—mambo yote kama hayo yamefanyika kwa hali ya juu sana tangu 1914, kama tu vile Biblia ilivyotabiri. Yanaonyesha kwamba adui mwenye ghadhabu wa Mungu na mwanadamu—Shetani Ibilisi—ametupwa kutoka mbinguni na sasa analazimika kuelekeza ghadhabu yake kwenye makao ya dunia pekee. Lakini Biblia pia huonyesha kwamba Shetani hataruhusiwa kutenda kwa muda mrefu zaidi. Ana “wakati mchache tu” uliobaki Mungu atakapoharibu mfumo wa ulimwengu ambao Shetani hutawala kwenye Har–Magedoni.

Ni nini kitakachompata Shetani wakati huo? Mtume Yohana aliandika hivi: “Nikaona malaika akishuka kutoka mbinguni, mwenye ufunguo wa kuzimu, na mnyororo mkubwa mkononi mwake. Akamshika yule joka, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani, akamfunga miaka elfu; akamtupa katika kuzimu, akamfunga, akatia muhuri juu yake.” (Ufunuo 20:1-3) Litakuwa pumziko jinsi gani kwa wanadamu wanaoteseka!

Kushangilia Chini ya Utawala wa Ufalme

Shetani akiwa hayupo, Ufalme wa Mungu chini ya Yesu Kristo utachukua mamlaka yote ya mambo ya wanadamu. Badala ya kuwa na serikali nyingi duniani, serikali moja tu ya kimbingu itabaki itawale juu ya sayari nzima. Vita haitakuwapo tena, nayo amani itaenea kila mahali. Chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, wote watakaa pamoja katika udugu wenye upendo.—Zaburi 72:7, 8; 133:1; Danieli 2:44.

Yesu atakuwa mtawala wa namna gani? Alipokuwa duniani, alionyesha watu upendo wenye kina. Kwa huruma, Yesu aliwapa wenye njaa chakula. Aliwaponya wagonjwa na kurudishia vipofu uwezo wa kuona, bubu uwezo wa kusema, na viwete akaponya ulemavu wao. Yesu hata aliwafufua wafu! (Mathayo 15:30-38; Marko 1:34; Luka 7:11-17) Miujiza hiyo ilikuwa mimweko ya mambo ya ajabu atakayofanya akiwa Mfalme. Itakuwa ajabu jinsi gani kuwa na mtawala mkarimu kama huyo!

Baraka zisizokuwa na mwisho zitafurahiwa na wale wanaojitiisha chini ya enzi kuu ya Yehova. Maandiko huahidi hivi: “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.” (Isaya 35:5, 6) Akitangulia kuonyesha siku hiyo yenye furaha, mtume Yohana aliandika hivi: “Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha enzi ikisema, Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:3, 4.

Mambo ya kupendeza yatakayotolewa na utawala wa Yehova kupitia Mwanaye, Yesu Kristo, yatalipia mateseko yoyote ambayo huenda yalitupata katika mfumo wa mambo uliopo unaotawalwa na Shetani Ibilisi. Katika ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa, watu hawatashindwa kujua, ‘Nani hasa anayetawala?’ (2 Petro 3:13) Wanadamu watiifu watakuwa na furaha na salama katika makao ya kidunia ya Watawala wenye upendo katika makao ya roho, Yehova na Kristo. Kwa nini usikubali tumaini la kuwa miongoni mwa watakaotawaliwa nao?

[Picha katika ukurasa wa7]

Wanadamu watakuwa salama katika makao ya kidunia ya Ufalme wa Mungu

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]

Picha ya NASA

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki