Nyongeza ya Sura ya 14
Wanahistoria wanashikilia kwamba Babuloni uliangushwa na jeshi la Koreshi katika Oktoba 539 K.W.K. Wakati huo Nabonido alikuwa mfalme, lakini Belshaza mwanaye alikuwa mtawala mwenzake wa Babuloni. Wanachuo fulani wamepanga orodha ya wafalme wa Babuloni-mamboleo na urefu wa tawala zao tangu ule mwaka wa mwisho wa Nabonido na kurudi nyuma mpaka kwa Nabopolasa, baba ya Nebukadreza.
Kulingana na orodha hiyo ya tarehe za Babuloni-mamboleo, Nebukadreza mwana-mtawala aliwashinda Wamisri katika lile pigano Ia Karkemishi mwaka wa 605 K.W.K. (Yeremia 46:1, 2) Baada ya Nabopolasa kufa, Nebukadreza alirudi Babuloni ili aketi tena penye kiti cha enzi. Mwaka wake wa kwanza wa kutawala ulianza masika yaliyofuata (mwaka wa 604 K.W.K.).
Biblia inaripoti kwamba Wababuloni chini ya Nebukadreza waliharibu Yerusalemu katika mwaka wa 18 wa kutawala kwake (mwaka wa kupanda kwenye kiti cha enzi ukitiwa ndani, inakuwa mwaka wa 19). (Yeremia 52:5, 12, 13, 29) Kwa hiyo ikiwa mtu angekubali orodha hiyo iliyotangulia kutajwa ya Babuloni-mamboleo, ukiwa wa Yerusalemu ungalikuwa katika ule mwaka wa 587/6 K.W.K. Lakini orodha hiyo ya tarehe za kilimwengu inategemea nini na inalinganaje na ile orodha ya tarehe za Biblia? Hati fulani kubwa za ushuhuda wa orodha hiyo ya tarehe za kilimwengu ni hizi:
Kanuni ya Ptolemi: Klaudio Ptolemi alikuwa mtaalamu wa nyota Mgiriki aliyeishi katika karne ya pili W.K. Kanuni yake, au orodha yake ya wafalme, ilihusiana na kitabu chenye habari za nyota alichotunga. Wanahistoria wengi wa kisasa wanakubali habari ya Ptolemi juu ya wafalme wa Babuloni-mamboleo na ule urefu wa tawala zao (ijapokuwa Ptolemi hataji utawala wa Labashi-Marduki). Kwa wazi Ptolemi alitegemeza habari yake ya kihistoria juu ya vyanzo vya tangu tarehe ya kipindi cha Seleuko, kilichoanza miaka zaidi ya 250 baada ya Koreshi kuteka Babuloni. Kwa hiyo haishangazi kwamba tarakimu za Ptolemi zinapatana na zile za Berossusi, kuhani Mbabuloni wa kipindi cha Seleuko.
Bamba la Nabonido Harran (NABON H 1, B): Bamba hilo la wakati ule ule, au nguzo yenye mchoro, lilipatikana mwaka wa 1956. Linataja tawala za wafalme wa Babuloni-mamboleo, Nebukadreza, Evil-Merodaki, Neriglisa. Tarakimu wanazotolewa wafalme hao watatu zinapatana na zile za kutoka Kanuni ya Ptolemi.
NYUNGU 4956: Hili ni bamba la maandishi ya michoro ya chunifomu linalotoa habari za utaalamu wa nyota zinazoweza kutajwa kuwa za mwaka wa 568 K.W.K. Linasema kwamba habari hizo za maoni zilikuwa za tangu mwaka wa 37 wa Nebukadreza. Hiyo ingelingana na orodha ya tarehe inayoweka mwaka wake wa kutawala wa 18 katika mwaka wa 587/6 K.W.K. Walakini, kwa wazi bamba hilo ni nakala iliyofanyizwa katika karne ya tatu K.W.K. Kwa hiyo inawezekana kwamba habari yalo ya kihistoria ni ile tu iliyokubaliwa katika kipindi cha Seleuko.
Mabamba ya Kibiashara: Maelfu ya mabamba ya wakati ule ule ya Babuloni-mamboleo, ya michoro ya chunifomu, yamepatikana yakiwa na habari za shughuli nyepesi za kibiashara. Yanaeleza ule mwaka wa mfalme wa Babuloni wakati shughuli ya kibiashara ilipotukia. Mabamba ya namna hiyo yamepatikana kwa miaka yote ya utawala wa wafalme wenye kujulikana wa Babuloni-mamboleo katika orodha iliyokubaliwa ya tarehe za kipindi hicho.
Kwa maoni ya kilimwengu, hati hizo za ushuhuda huenda zikaonekana kuwa zinathibitisha ile orodha ya tarehe za Babuloni-mamboleo inayoonyesha mwaka wa 18 wa Nebukadreza (na uharibifu wa Yerusalemu) kuwa katika mwaka wa 587/6 K.W.K. Walakini, hakuna mwanahistoria anayeweza kukana ule uwezekano wa kwamba hali ya sasa ya historia ya Kibabuloni huenda ikawa yenye kupoteza au yenye makosa. Kwa mfano, imejulikana kwamba mara nyingine makuhani na wafalme wa kale walibadili maandishi ili yapatane na makusudi yao wenyewe. Au, hata ikiwa ule ushuhuda uliopatikana ni sahihi, huenda ukafasiriwa vibaya na wanachuo wa kisasa au ukawa usio kamili hivi kwamba habari isiyovumbuliwa bado ingeweza kuibadili kabisa orodha ya tarehe za kipindi hicho.
Kwa wazi akifahamu mambo hayo ya hakika, Profesa Edward F. Campbell Mdogo, alitoa chati, iliyokuwa pia na orodha ya tarehe za Babuloni-mamboleo, kwa onyo hili: “Ni wazi kwamba orodha hizo ni za muda tu. Kadiri mtu anavyozidi kuchunguza magumu ya matatizo ya orodha ya tarehe katika eneo la kale la Mashariki ya Karibu, ndivyo anavyoelekea kuzidi kutoifikiria habari yo yote kuwa ni kamili. Kwa sababu hiyo, usemi huu circa [karibu na] ungeweza kutumiwa hata zaidi sana kuliko ulivyo.”—The Bible and the Ancient Near East (chapa ya mwaka wa 1965), uku. 281.
Wakristo wanaoiamini Biblia wameona mara nyingi kwamba maneno yayo yameshinda lile jaribu la uchambuzi mwingi na yamethibitishwa kuwa sahihi na yenye kutegemeka. Wanafahamu kwamba kwa kuwa hiyo ni Neno Ia Mungu lililoongozwa kwa roho yake inaweza kutumiwa kuwa ufito wa kupimia ubora wa historia na maoni ya kilimwengu. (2 Timotheo 3:16, 17) Kwa mfano, ijapokuwa Biblia ilisema juu ya Belshaza kuwa mtawala wa Babuloni, kwa karne nyingi wanachuo walitatizwa juu yake kwa sababu hakuna maandishi ya kilimwengu yaliyopatikana kueleza kuwako kwake, alikuwa mtu wa aina gani au alikuwa na cheo gani. Walakini, mwishowe wachimbuzi wa mambo ya kale walipata maandishi ya kilimwengu yaliyothibitisha Biblia. Ndiyo, ule upatano wa ndani wa Biblia na ule uangalifu uliotumiwa na waandikaji wayo, hata katika mambo ya orodha ya tarehe, unaipendekeza kwa Mkristo kwa nguvu sana hivi kwamba anaiona mamlaka yayo kuwa ya maana kuliko mamlaka ya maoni yanayobadilika-badilika ya wanahistoria wa kilimwengu.
Lakini Biblia inatusaidiaje kujua wakati Yerusalemu ulipoharibiwa, na wakati huo unalinganaje na orodha ya tarehe za kilimwengu?
Yule nabii Yeremia alitabiri Wababuloni wangeharibu Yerusalemu na kuufanya mji na nchi kuwa ukiwa. (Yeremia 25:8, 9) Aliongeza kusema: “Na nchi hii yote pia itakuwa ukiwa, na kitu cha kushangaza; nayo mataifa haya watamtumikia mfalme wa Babeli miaka sabini.” (Yeremia 25:11) Miaka hiyo 70 ilimalizika wakati Koreshi Mkuu alipowafungua Wayahudi katika mwaka wake wa kwanza, nao wakarudia nchi ya kwao. (2 Mambo ya Nyakati 36:17-23) Sisi tunaamini kwamba maelezo yaliyo ya moja kwa moja zaidi sana ya Yeremia 25:11 na maandiko mengine ni ya kwamba ile miaka 70 ingeanza kuhesabiwa wakati Wababuloni walipoharibu Yerusalemu na kuiacha nchi ya Yuda ukiwa.—Yere-mia 52:12-15, 24-27; 36:29-31.
Hata hivyo wale wanaotegemea hasa habari ya kilimwengu ili wapate orodha ya tarehe ya kipindi hicho wanafahamu kwamba ikiwa Yerusalemu uliharibiwa mwaka wa 587/6 K.W.K kwa hakika miaka 70 ilipita ndipo Babuloni ukaja kushindwa, naye Koreshi akaruhusu Wayahudi warudie nchi ya kwao. Ili wajaribu kupatanisha mambo, wanadai kwamba unabii wa Yeremia ulianza kutimizwa mwaka wa 605 K.W.K. Waandikaji wa baadaye wanamtaja Berossusi kuwa akisema kwamba baada ya lile pigano la Karkemishi Nebukadreza alipanua uvutano wa Kibabuloni mpaka katika Siria (Shamu) na Palestina yote na, alipokuwa akirudia Babuloni (katika mwaka wake wa kupanda kiti cha enzi, 605 K.W.K.), alichukua mateka ya Kiyahudi katika uhamisho. Kwa njia hiyo wanakadiri ile miaka 70 ambayo ni kipindi cha utumwa Babuloni kuwa ilianza mwaka wa 605 K.W.K. Hiyo ingekuwa na maana kwamba kipindi hicho cha miaka 70 kingemalizika mwaka wa 535 K.W.K
Lakini kuna matatizo kadha kuhusiana na fasiri hiyo:
Ijapokuwa Berossusi anadai kwamba Nebukadreza alichukua mateka ya Kiyahudi katika mwaka wake wa kupanda kiti cha enzi, hakuna maandishi ya michoro ya chunifomu yanayounga mkono dai hilo. Kwa maana zaidi, andiko la Yeremia 52:28-30 linaripoti kwa uangalifu kwamba Nebukadreza alichukua mateka ya Kiyahudi katika mwaka wake wa saba, mwaka wake wa 18 na mwaka wake wa 23, si mwaka wake wa kupanda kiti cha enzi. Pia, Yosefo, mwandikaji wa historia Myahudi, anaeleza kwamba katika mwaka huo wa pigano la Karkemishi Nebukadreza alishinda Siria na Palestina yote “isipokuwa Yudea,” kwa njia hiyo akipinganisha maneno ya Berossusi na kupingana na lile dai la kwamba miaka 70 ya utumwa wa Wayahudi ilianza katika mwaka wa Nebukadreza wa kupanda kiti cha enzi.—Antiquities of the Jews X, vi, 1.
Isitoshe, mahali pengine Yosefo anaeieza ule uharibifu wa Yerusalemu ukifanyizwa na Wababuloni kisha anasema kwamba “Yudea yote na Yerusalemu, na hekalu, iliendelea kuwa jangwa kwa miaka sabini.” (Antiquities of the Jews X, ix, 7) Yeye anaeieza wazi kwamba “mji wetu uliachwa ukiwa wakati wa kipindi cha miaka sabini, mpaka zile siku za Koreshi.” (Against Apion 1, 19) Hilo linapatana na 2 Mambo ya Nyakati 36:21 na Daniell 9:2 kwamba Ile miaka 70 iliyotabiriwa ilikuwa miaka 70 ya ukiwa kamili wa nchi hiyo. Pia Theofilo wa Antiokia, mwandikaji wa karne ya pili (W.K.), anaonyesha kwamba miaka hiyo 70 ilianza na ule uharibifu wa hekalu baada ya Sedekia kutawala miaka 11.—Ona pia 2 Wafalme 24:18-25:21.
Lakini Biblia yenyewe inatoa ushuhuda wenye nguvu hata zaidi kupinga lile dai la kwamba miaka 70 ilianza mwaka wa 605 K.W.K. na la kwamba Yerusalemu uliharibiwa mwaka wa 587/6 K.W.K. Kama tulivyokwisha kutaja, kama tungehesabu kutoka mwaka wa 605 K.W.K., ile miaka 70 ingefika kwenye mwaka wa 535 K.W.K. Walakini, Ezra, yule mwandikaji wa Biblia aliyeongozwa na Mungu, alitaarifu kwamba ile miaka 70 iliendelea mpaka “mwaka wa kwanza wa Koreshi, mfalme wa Uajemi,” aliyetoa amri ya kuwaruhusu Wayahudi warudie nchi ya kwao. (Ezra 1:1-4; 2 Mambo ya Nyakati 36:21-23) Wanahistoria wanakubali kwamba Koreshi alishinda Babuloni katika Oktoba 539 K.W.K. na kwamba mwaka wa kwanza wa kutawala kwa Koreshi ulianza katika masika ya mwaka wa 538 K.W.K. Ikiwa amri ya Koreshi ilitokea baadaye katika mwaka wake wa kwanza wa kutawala, wale Wayahudi wangeweza vyepesi kuwa wamerudia nchi ya kwao mnamo mwezi wa saba (Tishri) kama andiko la Ezra 3:1 linavyosema; hiyo ingekuwa Oktoba 537 K.W.K.
Walakini, hakuna sababu nzuri ya kupanua mwaka wa kwanza wa Koreshi kutoka mwaka 538 mpaka 535 K.W.K. Wengine ambao wamejaribu kueleza sababu ya tatizo hili wamejilazimisha kudai isivyo haki kwamba Ezra na Danieli walipoutaja “mwaka wa kwanza wa Koreshi,” walikuwa wakitumia maoni fulani ya Kiyahudi yasiyo ya kawaida ambayo yalitofautiana na hesabu rasmi ya utawala wa Koreshi. Lakini hilo haliwezi kukubaliwa, maana gavana asiye Myahudi na pia maandishi kutoka nyaraka za kale za Kiajemi yanakubaliana yakisema kwamba ile amri ilitukia katika mwaka wa kwanza wa Koreshi, kama vile waandikaji wa Biblia walivyoripoti kwa uangalifu na kwa njia ya wazi.—Ezra 5:6, 13; 6:1-3; Danieli 1:21; 9:1-3.
‘Neno jema’ la Yehova limefungamana na kile kipindi cha miaka 70 kilichotabiriwa, kwa kuwa Mungu alisema:
“Maana [Yehova] asema hivi, Babeli utakapotimiziwa miaka sabini, nitawajilia ninyi, na kulitimiza neno langu jema kwenu, kwa kuwarudisha mahali hapa.” (Yeremia 29:10)
Danieli alitegemea neno hilo, akaamini kwamba ile miaka 70 haikuwa ‘tarakimu inayokaribia tu hesabu kamili,’ bali ni hesabu kamili ambayo ingeweza kutegemewa. (Danieli 9:1, 2) Na ndivyo ilivyokuwa.
Hali kadhalika, sisi tunataka kuongozwa hasa na Neno la Mungu badala ya kuongozwa na orodha ya tarehe inayotegemea sana ushuhuda wa kilimwengu au isiyokubaiiana na Maandiko. Inaonekana kwamba ufahamu ulio rahisi na wa wazi zaidi sana wa misemo mbalimbali ya Kibiblia ni kwamba ile miaka 70 ilianza wakati wa ukiwa wa Yuda baada ya Yerusalemu kuharibiwa. (Yeremia 25:8-11; 2 Mambo ya Nyakati 36:20-23; Danieli 9:2) Kwa sababu hiyo, tukihesabu miaka 70 kurudi nyuma tangu Wayahudi waliporudia nchi ya kwao mwaka wa 537 K.W.K., tunafikia mwaka wa 607 K.W.K. kuwa ndiyo tarehe ambayo Nebukadreza, katika mwaka wake wa 18 wa kutawala, aliharibu Yerusalemu, akamwondoa Sedekia katika kiti cha enzi na kukomesha ile nasaba ya Kiyudea ya kukaa kwa wafalme katika kiti cha enzi katika mji wa kidunia wa Yerusalemu.—Ezekieli 21:19-27.