Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • sj kur. 12-16
  • Sikukuu na Maadhimisho

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sikukuu na Maadhimisho
  • Shule na Mashahidi wa Yehova
  • Habari Zinazolingana
  • “Wokovu Una Bwana”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Kanuni za Adili Zinazostahili Staha
    Mashahidi wa Yehova na Elimu
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Kusalimu Bendera, Kupiga Kura, na Utumishi wa Kiraia
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
Pata Habari Zaidi
Shule na Mashahidi wa Yehova
sj kur. 12-16

Sikukuu na Maadhimisho

Inaweza kutatiza mwalimu kidogo kuona kwamba Mashahidi wa Yehova hawashiriki maadhimisho mengi ya sikukuu. Tunatumaini habari ifuatayo itakusaidia ufahamu kwa nini jambo hilo tunalichukua kwa uzito sana.

Labda kwa kadiri kubwa zaidi ya vile unavyojua, sikukuu na desturi nyingi zinazohusiana nazo zinatokana na chanzo cha kidini kisicho cha Kikristo. Hiyo ndiyo sababu Mashahidi wa Yehova wanakataa kuzishiriki. Sisi tunajaribu kufuata kanuni iliyosemwa na Paulo, mtume Mkristo:

“Pana urafiki gani kati ya haki na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari [mungu wa uwongo]? Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini? . . . Kwa hiyo, tokeni kati yao, mkatengwe nao, asema [Yehova].”—2 Wakorintho 6:14-17.

Kwa hiyo ikiwa kwa njia fulani sikukuu au mwadhimisho unahusiana na miungu fulani ya kiume au ya kike, au ikiwa kuiadhimisha ni kinyume cha ufahamu wetu wa kanuni za Biblia, hatushiriki.

Sikukuu za Ukumbusho wa Kuzaliwa: Hakika si vibaya kufurahia karamu na kuwapa wapendwa vitu kwa ukarimu. (Luka 15:22-25; Matendo 20:35) Mashahidi wa Yehova wanafurahia kuwapa watu zawadi na kuwa na nyakati za kustarehe mwaka wote. Lakini, maadhimisho mawili tu ya ukumbusho wa kuzaliwa yanayotajwa katika Biblia ni yale yaliyohusu watu wasio waamini wa kweli. Watu hao ni Farao wa Misri na Herode Antipa, mtawala Mroma. Kila sikukuu ya ukumbusho wa kuzaliwa kwa watu hao ilikuwa na matokeo ya kuuawa kwa mtu. (Mwanzo 40:18-22; Marko 6:21-28) Hivyo si ajabu kuona mitajo hii ya kihistoria kuhusu mwelekeo wa Wakristo wa kwanza kwenye maadhimisho ya sikukuu za ukumbusho wa kuzaliwa:

“Wazo la sikukuu ya ukumbusho wa kuzaliwa halikutokana kabisa na mawazo ya Wakristo wa kipindi hiki kwa ujumla.”—The History of the Christian Religion and the Church, During the Three First Centuries (New York, 1848), cha Augustus Neander (kilichotafsiriwa na Henry John Rose), ukurasa wa 190.

“Kati ya watu watakatifu wanaotajwa katika Maandiko, hakuna mmoja aliyeandikwa kuwa alifanya sikukuu wala akafanya karamu kuu katika siku yake ya ukumbusho wa kuzaliwa. Ni wafanya dhambi tu (kama Farao na Herode) ndio wanaofanya sherehe kubwa za kushangilia siku waliyozaliwa katika ulimwengu huo wa chini.”—The Catholic Encyclopedia (New York, 1911, Buku la 10, ukurasa wa 709 (kikimnakili Origen Adamantio wa karne ya tatu).

Tena, maadhimisho ya siku za ukumbusho wa kuzaliwa yanaelekea kutukuza sana mtu. Bila shaka hiyo ni sababu moja kwa nini Wakristo wa kwanza waliyaepuka. (Mhubiri 7:1) Hivyo utaona kwamba Mashahidi wa Yehova hawashiriki sherehe za ukumbusho wa kuzaliwa (karamu, kuimba, kupeana zawadi na kadhalika).

Krismasi: Kama inavyoelekea kuwa unajua, Desemba 25 haikuwa siku ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo. Labda unahisi kwamba si kitu—kwamba tukio ndilo jambo la maana. Lakini jinsi sikukuu ya Krismasi ilivyositawishwa inaonyesha kwamba kuna zaidi ya hilo. Ensaiklopedia zifuatazo zinaeleza:

“Mwadhimisho wa Krismasi si agizo la kimungu, wala hautokani na Agano Jipya. Siku ya kuzaliwa kwa Kristo haiwezi kujulikana kutoka Agano Jipya, wala, kwa kweli, kutoka chanzo kinginecho chote. Mababa wa karne tatu za kwanza hawataji mwadhimisho wa pekee wo wote wa kuzaliwa huko.”—Cyclopedia of Biblical, Theological, and Ecclesiastical Literature (Grand Rapids, Michigan, chapa mpya ya 1981), cha John McClintock na James Strong, Buku la 2, ukurasa wa 276.

“Nyingi za desturi za Krismasi zilizoenea sasa katika Ulaya, au zilizoandikwa tangu nyakati za zamani, si desturi za Kikristo za kweli, bali ni desturi za kipagani ambazo zimechukuliwa au zikakubaliwa na Kanisa. . . . Ile Sikukuu ya Saturn katika Roma ilitolea mfano desturi nyingi za shangwe za wakati wa Krismasi.”—Encyclopædia of Religion and Ethics (Edinburgh, 1911), kilichohaririwa na James Hastings, Buku la 3, kurasa 608, 609.

Inajulikana na watu wengi kwamba hapo mwanzo Krismasi haikuwa mwadhimisho wa kuzaliwa kwa Kristo. Gazeti U.S. Catholic la Desemba 1981, linasema hivi katika ukurasa wa 32: “Haiwezekani kutenganisha Krismasi na mianzo yayo ya kipagani.” Gazeti hilo laeleza:

“Sikukuu yenye kupendwa sana na Waroma ilikuwa Sikukuu ya Saturn, iliyoanza Desemba 17 na kumalizika na ‘sikukuu ya ukumbusho wa kuzaliwa kwa jua lisiloshindwa’ (Natalis solis invicti) Desemba 25. Mahali fulani katika robo ya pili ya karne ya nne, maofisa werevu wa kanisa la Roma waliamua kwamba Desemba 25 ingekuwa siku bora sana ya kuadhimisha siku ya kuzaliwa kwa ‘jua la uadilifu.’ Krismasi ikazaliwa.”

Watu fulani wamegeuzwa namna gani wakati wa kujua mambo ya hakika hayo juu ya Krismasi? The World Book Encyclopedia (cha 1982) kinaeleza hivi chini ya “Krismasi”: “Wakati wa miaka ya kuanzia 1600 na kuendelea . . . Krismasi ilipigwa marufuku katika Uingereza na katika sehemu za makoloni ya Uingereza katika Marekani.” Kwa kuwa zamani watu walikataa kuadhimisha Krismasi kwa sababu ina mianzo ya kipagani, ni lazima ijulikane wazi kwamba hiyo ndiyo sababu Mashahidi wa Yehova leo hawaiadhimishi. Sisi hatushiriki karamu za Krismasi, michezo ya kuigiza yake, nyimbo zake, kupeana zawadi za Krismasi, wala shughuli yo yote kama hizo inayohusiana na Krismasi.

Mashahidi wa Yehova wanachukua msimamo ule ule wa kutoshiriki kabisa katika sikukuu nyingine za kidini au zilizo kama za kidini zinazotokea wakati wa mwaka wa shule. Sababu ni kwamba sikukuu hizo, pia, zinakamatana na ibada isiyo ya Kikristo. Kwa kweli, mara nyingi mambo fulani ya ibada hiyo ndiyo yanayoongoza maadhimisho hayo. Ebu ifikirie mifano ifuatayo:

Ista: Ijapokuwa kusudi la sikukuu hii ni kuadhimisha ufufuo wa Kristo, ebu angalia waandikaji wa kilimwengu wanayosema juu yayo:

“Ista. Awali ilikuwa sikukuu ya masika ya kuheshimu mungu-mke wa nuru na masika wa Waingereza wa kale iliyojulikana kwa Waingereza wa kale kuwa Ista. Mapema karne ya 8 jina hilo lilihamishwa na Waingereza wa kale likapelekwa kwenye sikukuu iliyokusudiwa kuadhimisha ufufuo wa Kristo.”—The Westminster Dictionary of the Bible (Philadelphia, 1944), ya John D. Davis, ukurasa wa 145.

“Kila mahali wanatafuta-tafuta mayai ya Ista yenye rangi nyingi, yanayoletwa na sungura wa Ista. Huu si mchezo tu wa watoto, bali ndilo baki la sherehe ya uwezo wa kuzaa, mayai na sungura pia vikifananisha uwezo wa kuzaa.”—Standard Dictionary of Folklore Mythology and Legend ya Funk na Wagnall (New York, 1949), Buku la 1, ukurasa wa 335.

Sikukuu ya Mwaka Mpya: “Katika Roma ya kale, ile siku ya kwanza ya mwaka ilitumiwa ili kuheshimu Jano, mungu wa milango mikubwa na midogo na wa mianzo na miisho. . . . Sikukuu ya Mwaka Mpya ikawa siku takatifu katika kanisa la Kikristo mwaka wa 487 A.D.”—The World Book Encyclopedia (1982), Buku la 14, ukurasa wa 237.

Siku ya Mama: “Sikukuu iliyochukuliwa kutokana na desturi ya ibada ya mama katika Ugiriki wa kale. Ibada rasmi ya mama, pamoja na kusherehekea Sibele, au Rea, Mama Mkuu wa Miungu, zilifanywa katika Ides ya Machi katika Esia Ndogo yote.”—Encyclopædia Britannica (1959), Buku la 15, ukurasa wa 849.

Hiyo ni mifano michache ya sikukuu zinazoadhimishwa na watu wengi, na ambazo mara nyingi watoto wa shule wanatazamiwa kushiriki kwa kufanya shughuli fulani fulani. Lakini, kwa sababu za kidhamiri Mashahidi wa Yehova hawashiriki hata kidogo shughuli hizo za sikukuu—kuwe ni kuimba nyimbo, kupiga muziki, kuwa katika michezo ya kuigiza, kuandamana katika magwaride, kuchora picha, kuhudhuria karamu, kula na kunywa, na kadhalika. Hata hivyo, wakati uo huo, sisi hatukatazi wengine wasiadhimishe sikukuu hizo wala hatujaribu kuwazuia. Tunathamini sana sana wakati walimu kwa hisani yao wanawapa watoto wetu ruhusa ya kutoshiriki shughuli zote ambazo kwa njia yo yote zinaadhimisha sikukuu hizo.

[Blabu katika ukurasa wa 12]

Wakristo wa kwanza hawakuadhimisha sikukuu za ukumbusho wa kuzaliwa

[Blabu katika ukurasa wa 15]

Kwa sababu za kidhamiri, Mashahidi wa Yehova hawashiriki shughuli za sikukuu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki