Sura 8
Waokokaji Kutoka Mataifa Yote
1. Ni ahadi gani aliyopewa Abrahamu inayoonyesha kwamba inawezekana “jamaa zote” za wanadamu zipate kibali ya Mungu?
YEHOVA anajali kwa upendo watu wa mataifa na makabila yote. Ameandaa ili jamaa zote za duniani ziweze kufurahia kibali na baraka yake. Yehova alimwambia hivi, Abramu (Abrahamu), mzao wa Shemu mwana wa Noa: “Nenda zako utoke katika nchi yako na katika watu wako wa ukoo na katika nyumba ya baba yako uende kwenye nchi ambayo nitakuonyesha; nami nitafanya taifa kubwa kutoka katika wewe na nitakubariki wewe nami nitafanya jina lako kuwa kubwa; na wewe jithibitishe mwenyewe kuwa baraka. Nami nitabariki wale wanaokubariki wewe, na yeye anayeita ovu lishuke juu yako mimi nitalaani, na jamaa zote za ardhi hakika zitajibariki zenyewe kupitia wewe.” (Mwanzo 12:1-3, New World Translation; Matendo 7:2-4) “Jamaa zote za ardhi”—ni pamoja na sisi leo, bila kujali taifa tulimozaliwa au lugha tunayosema.—Zaburi 65:2.
2. (a) Kama Abrahamu, sisi tunahitaji sifa gani? (b) Kama inavyoonyeshwa katika Waebrania 11:8-10, Abrahamu alitoaje ushahidi wa sifa hiyo?
2 Mtu ambaye Yehova alieleza ahadi hiyo alikuwa mwanamume wa imani, kama ilivyo lazima kwetu sisi kuwa na imani ikiwa tungeishiriki baraka hiyo inayoahidiwa hapa kutoka kwa Mungu. (Yakobo 2:23; Waebrania 11:6) Imani ya Abrahamu haikuwa kuamini bila kufanya lo lote, bali ilifuatana na tendo. Ilimfanya ahame kutoka Mesopotamia aingie katika nchi ya mbali ambayo hakuwa amepata kuiona kabla ya hapo. “Kwa imani alikaa ugenini katika ile nchi ya ahadi, kama katika nchi isiyo yake,” asijishikamanishe mwenyewe huko na wo wote wa falme za miji. “Maana alikuwa akiutazamia mji [Ufalme wa Mungu] wenye misingi, ambao mwenye kuubuni na kuujenga ni Mungu.”—Waebrania 11:8-10.
3. Abrahamu alipata jaribu gani la imani lenye kuchunguza moyo kuhusiana na Isaka?
3 Abrahamu alipofikia umri wa miaka 100 na Sara mke wake, miaka 90, Yehova aliwabariki kimuujiza kwa kuwapa mwana, Isaka. Kuhusiana na mwana huyo, Abrahamu alijaribiwa imani na utii wake kuelekea Mungu. Yehova alimwelekeza Abrahamu achukue Isaka, wakati huo akiwa kijana, aende kwenye nchi ya Moria akamtoe huko awe toleo la kuteketezwa. Abrahamu alitii, akiwa na imani katika uwezo wa Mungu wa kumrudishia mwanaye uhai kupitia ufufuo. (Waebrania 11:17-19) Isaka, kwa kumnyenyekea babaye, alikuwa amekwisha kufungwa kwenye madhabahu, na katika mkono wake Abrahamu alikuwa na kisu cha kumuulia hapo ndipo malaika wa Yehova alipomzuia. Jaribu hilo lilikuwa limefika mbali sana kuthibitisha kwamba Abrahamu hangemnyima Mungu cho chote. Kwa hiyo Mungu alifanya agano lake pamoja na Abrahamu liwe thabiti, kama hivi Biblia inavyosema:
4. Pindi hiyo, ni ahadi gani zaidi yenye maana ambayo Mungu alifanya juu ya watu wa mataifa yote?
4 “‘Naapa kwangu mwenyewe,’ ni usemi wa Yehova, ‘kwamba kwa sababu ya uhakika wa kwamba wewe umefanya jambo hili na hukuninyima mwana wako, mwanako pekee, bila shaka mimi nitakubariki wewe na bila shaka nitazidisha mbegu yako kama nyota za mbingu na kama chembe za mchanga zilizo katika ufuo wa bahari; na mbegu yako itachukua miliki ya lango la adui zake. Na kupitia mbegu yako mataifa yote ya dunia hakika yatajibariki yenyewe kwa sababu ya uhakika wa kwamba umesikiliza sauti yangu.’”—Mwanzo 22:15-18, New World Translation.
5. (a) Jaribio la Abrahamu la kumtoa Isaka lilikuwa mfano wa nini? (b) Kwa utimizo wa Mwanzo 12:3, watu ‘wanaitaje ovu lishuke’ juu ya Abrahamu Mkubwa Zaidi, na matokeo ni nini? (c) Sisi tunawezaje ‘kumbariki’ yeye?
5 Tunapofahamu kwamba aliye Abrahamu Mkubwa Zaidi ni Yehova na kwamba Isaka alikuwa mfano wa Yesu Kristo, tunaweza kuanza kuthamini jinsi matukio hayo yalivyo na maana kwetu sisi binafsi. Kwa uhakika, namna wakati ujao wetu utakavyokuwa inaamuliwa na jinsi tunavyotenda kuelekea Yehova Mungu. Lile taraja la uzima wa milele litawezekana kwetu kwa sababu kwa hakika Mungu alitoa Mwana wake mzaliwa pekee awe dhabihu kwa dhambi zetu, kama inavyoonyeshwa na jaribio la Abrahamu kumtoa Isaka. (Yohana 3:16) Wo wote wanaoendelea ‘kuita ovu lishuke’ juu ya Yehova, wakimdharau au kupuuza makusudi yake yenye upendo, wanakuja chini ya laana ambayo maana yake itakuwa uharibifu wao wa milele. (Linganisha 1 Samweli 3:12-14; 2:12.) Lakini ikiwa sisi ni watu wenye kuthamini, ‘tutambariki’ yule Abrahamu Mkubwa Zaidi. Jinsi gani? Kwa kukiri bila kusita kwamba vitu vyema vyote, kutia na ile zawadi isiyostahilika ya uzima kupitia Mwanaye, vinatoka kwa Yehova. Pia, tutawaambia wengine juu ya wema wa Yehova na sifa bora sana za umaliki wake. (Yakobo 1:17; Zaburi 145:7-13) Kwa njia hiyo tunajiweka tayari kuja kupokea milele baraka zitokazo kwake.
ILE “MBEGU” YA ABRAHAMU ILIYOAHIDIWA
6. (a) Ni nani aliye “mbegu” kuu ya Abrahamu? (b) Tunaweza kupokeaje baraka zinazokuja kupitia yeye?
6 Ikiwa sehemu ya mpango wake wa kubarikia wanadamu Yehova alikusudia kuwe na serikali ya kimbingu yenye uadilifu. Yesu Kristo alizaliwa akiwa mzao wa Abrahamu, akiwa uzao, au “mbegu” yake yenye maana sana, na Yehova amempa huyo umaliki. (Wagalatia 3:16; Mathayo 1:1) Basi, kama inavyoonyeshwa na kiapo cha Yehova kwa Abrahamu, watu kutoka mataifa yote ya dunia watabarikiwa kupitia Yesu Kristo. Je! wewe unafanya linalotakwa ili uje ujipatie baraka hiyo? Kwa mfano, je! mwendo wako wa maisha unaonyesha kwamba wewe unathamini jinsi kutolewa kwa uhai wa Yesu kulivyo kwa maana kwako? Je! unatii kweli kweli mamlaka yake kuwa Mfalme?—Yohana 3:36; Matendo 4:12.
7. (a) Nani wengine wanaotiwa katika “mbegu ya Abrahamu”? (b) Twajuaje kwamba si wote wanaomtumikia Mungu kwa uaminifu wataenda mbinguni?
7 Mtume Yohana alipewa maono ya mbele yenye unabii ya matukio ya kimbingu ambayo katika hayo aliona wengine wameshirikiana na Yesu Kristo katika Mlima Sayuni. Hao, pia, ni sehemu ya “mbegu ya Abrahamu.” Kama inavyoelezwa katika Ufunuo 14:1-5, wao “wamenunuliwa katika wanadamu” na hesabu yao ni 144,000. (Wagalatia 3:26-29, New World Translation) Hao ni pamoja na nani? Biblia inaonyesha wazi kwamba halijapata kuwa kusudi la Mungu kamwe kupeleka mbinguni watu wote wenye maelekeo ya uadilifu. (Mathayo 11:11; Matendo 2:34; Zaburi 37:29) Pendeleo kuu la kushiriki pamoja na Kristo katika Ufalme wa mbingu ni la “kundi dogo” tu watakaokuwa wafalme na makuhani pamoja naye kwa miaka elfu.—Luka 12:32; Ufunuo 5:9, 10; 20:6.
8. Kuchaguliwa kwa “kundi dogo” kulianza wakati gani, na kunaendelea mpaka lini?
8 Kuchaguliwa kwa “kundi dogo” hilo kuliendeleaje? Mwaliko wenye neema wa kushiriki Ufalme wa kimbingu ulitolewa kwanza kwa Waisraeli wa asili. Lakini kwa sababu ya ukosefu wao wa imani, hawakutimiza hesabu yote ya 144,000. Hivyo Wasamaria na, baadaye, watu wa mataifa yote walialikwa. (Matendo 1:8) Wale wa kwanza wa warithi washirika pamoja na Kristo walipakwa mafuta kwa roho takatifu siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Kuchaguliwa kwa kikundi hicho kunaendelea mpaka 144,000 watakapotiwa muhuri na Mungu kuwa wamekubaliwa. Kisha fikira zinaelekezwa kwenye kukusanywa kwa watu watakaoishi duniani wakiwa raia wenye kuthamini wa serikali ya kimbingu.
9. (a) Ni semi gani zilizo katika Biblia zinazohusu jamii hiyo ya kimbingu? (b) Nani waliofananishwa na Israeli wa asili?
9 Wale walio warithi wa Ufalme pamoja na Kristo wanatajwa katika Maandiko kuwa “wachaguliwa,” “watakatifu,” watu ‘waliopakwa mafuta na Mungu.’ (2 Timotheo 2:10; 1 Wakorintho 6:1, 2; 2 Wakorintho 1:21, New World Translation) Pia wanasimuliwa kiujumla kuwa “bibi-arusi” wa Kristo. (Ufunuo 21:2, 9; Waefeso 5:22-32) Wakionwa kwa maoni mengine, wanaitwa “ndugu” za Kristo, “warithi washirika pamoja na Kristo” na “wana” wa Mungu. (Waebrania 2:10, 11; Warumi 8:15-17, New World Translation; Waefeso 1:5) Bila kujali taifa lao, kwa usemi wa kiroho, wao ni “Israeli wa Mungu.” (Wagalatia 6:16; Warumi 2:28, 29; 9:6-8) Yehova alipokomesha agano la Torati pamoja na Israeli wa mwili, aliingiza Israeli wa kiroho katika agano jipya pamoja naye mwenyewe. Lakini kushughulika kwake na Israeli wa mwili walipokuwa bado chini ya Torati kuliweka mfano wa mambo yatakayokuja. (Waebrania 10:1) Basi, ni nani aliyefananishwa na taifa la Israeli wa mwili, aliyechaguliwa na Mungu kuwa “mali ya pekee” yake? Mambo ya hakika yanaelekeza kwenye Israeli wa kiroho, wale ambao Mungu amechagua wakatawale pamoja na Kristo mbinguni. (Linganisha Kutoka 19:5, 6, New World Translation, pamoja na 1 Petro 1:3, 4 na 2:9.) Wakiwa pamoja na Kristo wanakuwa chombo ambacho kupitia hicho baraka zitatolewa kwa wengine watiifu miongoni mwa wanadamu. Kuthamini jambo hilo ni ufunguo wa kuifahamu Biblia.
WALE WANAOBARIKIWA KUPITIA ILE “MBEGU”
10. Nani wanaofananishwa na waabudu wa Yehova wasio Waisraeli?
10 Wakati ule Mungu alipokuwa akishughulika na taifa la Israeli kwa njia ya pekee, alifanya pia maandalizi ya upendo kwa ajili ya watu wasiokuwa wa taifa hilo lakini ambao mioyo yao iliongoza washiriki ibada ya kweli kwa kushirikiana na Waisraeli. Mtajo unaofaa kuangaliwa juu yao umo katika maandishi ya Biblia. Je! wao, pia, wana watu wa kisasa ambao wanawafananisha? Ndiyo, hasa. Kwa njia nyingi wanafananisha wale wasio Waisraeli wa kiroho lakini wanaofurahia taraja la ajabu la uzima wa milele wakiwa raia za kidunia za Ufalme wa Mungu. Hao ndio wale ambao Mungu alimwambia Abrahamu, akisema kwamba watu kutoka “mataifa yote ya dunia” wangejibariki wenyewe kupitia “mbegu” yake.—Mwanzo 22:18; Kumbukumbu la Torati 32:43.
11. (a) Ni mtajo gani uliofanywa juu ya kikundi hiki wakati wa kuwekwa wakfu kwa hekalu la Sulemani? (b) “Wageni” ‘wanaandamanaje na Yehova’ siku zetu, kama ilivyotabiriwa katika Isaya 56:6, 7?
11 Sikuzote limekuwa kusudi la Mungu wanadamu wote waunganishwe katika ibada ya kweli. Kwa kufaa, wakati wa kuwekwa wakfu kwa hekalu lililojengwa na Sulemani katika Yerusalemu, mfalme alisali kwamba Yehova angesikia sala ya wageni waliotaka kutoa ibada yenye kukubalika pamoja na Israeli. (2 Mambo ya Nyakati 6:32, 33) Na, katika Isaya 56:6, 7, Mungu aliahidi hivi: “Na wageni, walioandamana na [Yehova] ili wamhudumu, na kulipenda jina la [Yehova], kuwa watumishi wake; . . . Nitawaleta hao nao hata mlima wangu mtakatifu, na kuwafurahisha katika nyumba yangu ya sala; . . . kwa maana nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote.” Wakionyesha roho inayosemwa hapa, “wageni” wa kisasa wanajikusanya sasa kutoka mataifa yote, si wakiwa watazamaji wa vivi hivi, bali wakiwa watu ‘wanaoandamana na Yehova.’ Wanafanya hivyo kwa kuweka maisha zao wakfu kwake, wakionyesha mfano wa hilo kwa kuzamishwa katika maji kisha kutumikia kwa jinsi inayoonyesha wanalipenda “jina la [Yehova]” na yote ambayo linawakilisha.—Mathayo 28:19, 20.
12. Torati ya Musa inaonyeshaje kama wale wanaotumaini kuwa raia za kidunia za Ufalme wa Mungu ni lazima au si lazima wafuate viwango vya juu vinavyohusu Israeli wa kiroho?
12 Hata wao wanatakwa waonyeshe uaminifu kama Wakristo waliopakwa mafuta kwa roho. Chini ya Torati ya Musa, Yehova alimtaka “mgeni” aliyeikubali ibada ya kweli afuate sheria ile ile waliyofuata Waisraeli. (Hesabu 15:15, 16) Uhusiano uliokuwa kati yao haungekuwa ule wa kuvumilia tu bali wenye upendo wa kweli kweli. (Mambo ya Walawi 19:34) Hali kadhalika, wale waliofananishwa na wageni hao wanataka kuleta maisha zao katika upatano kamili na matakwa ya Yehova na kutumikia katika umoja wenye upendo pamoja na mabaki ya Israeli wa kiroho.—Isaya 61:5.
13. Ni mambo gani mbalimbali katika Isaya 2:1-4 tunayopaswa kuzingatia moyoni ikiwa twataka tuje tuokoke tuingie katika “dunia mpya”?
13 Kupitia Isaya, nabii wake, Yehova alisimulia habari ya umati wenye bidii wa watu kutoka “mataifa yote” ambao leo wanaenda makundi makundi kwenye nyumba ya Yehova ya ulimwengu mzima ya ibada. Alitabiri hivi: “Mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova], nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.” Matokeo ni kwamba ‘wamefua panga zao zikawa majembe’ na, hata wakiwa katikati ya ulimwengu huu wenye kujaa ugomvi, ‘hawajifunzi vita tena kamwe.’ (Isaya 2:1-4) Je! wewe unajiona ukiwa kati ya umati huo wenye furaha? Je! wewe unashiriki tamaa yao ya kujifunza matakwa ya Yehova, na kuyafuata hayo maishani mwako na kuacha kuzitegemea silaha za vita? Mungu ameahidi kwamba umati mkubwa wa wale wanaofuatia mwendo huo ‘utatoka katika dhiki ile iliyo kuu’ wakiwa waokokaji wa kuingia katika “dunia mpya” yake yenye amani.—Ufunuo 7:9, 10, 14; Zaburi 46:8, 9.