Sura 12
Je! Una Kitambulisho cha Kuangamizwa au Kuokolewa?
1. Ni maulizo gani tunayotiwa moyo na somo hili tuyafikirie?
HALI ya kidini iliyopo leo inatutaka sisi tuonyeshe yaliyo hasa katika mioyo yetu. Je! twampenda Yehova na njia zake kweli kweli? Je! tuko kama Mwanaye, Yesu Kristo, aliyeambiwa hivi: “Wewe wapenda uadilifu na kuchukia uovu”? (Waebrania 1:9, Habari Njema kwa Watu Wote) Je! tuko tayari kuonyesha hivyo peupe ili wengine wajue msimamo wetu? Habari ya Biblia kuhusu Yehu na Yehonadabu mwana wa Rekabu inatusaidia tuchunguze upande wetu.
2. Yehu na Yehonadabu walikuwa nani?
2 Katika karne ya kumi K.W.K., Yehu alipakwa mafuta awe mfalme wa ufalme wa makabila kumi ya Israeli, ambao mji wake mkuu ulikuwa katika Samaria. Aliagizwa rasmi aangamize wote waliokuwa watu wa nyumba yenye uovu ya Mfalme Ahabu, pamoja na Malkia Yezebeli, aliyekuwa amekuza ibada ya Baali katika Israeli na akawa ameing’oa ibada ya Yehova. Yehonadabu, Mkeni (kwa sababu hiyo, si Mwisraeli), bila shaka alijua mpango wa Yehu wa kuangamiza alipotoka akamlaki Yehu. Lakini upendo wa Yehonadabu kwa Yehova ulikuwa na nguvu kadiri gani? Je! angejitambulisha waziwazi kuwa mtu aliyeamini kwa dhati kwamba ni Yehova, Mungu wa kweli tu, anayepaswa kuabudiwa?
“JE! MOYO WAKO NI MNYOFU PAMOJA NA MIMI?”
3. Yehonadabu alijulishaje peupe upande alikokuwa kuhusu ibada ya Yehova?
3 Wanaume hao wawili walipokwisha kusalimiana, Yehu akamwomba Yehonadabu aonyeshe wazi upande aliko. “Je! moyo wako ni mnyofu pamoja na mimi,” Yehu akauliza, “kama moyo wangu mwenyewe ulivyo pamoja na moyo wako?” Bila kusita Yehonadabu akaitika: “Ndio.” “Ikiwa ndio, nipe mkono wako,” Yehu akajibu. Basi akampandisha Yehonadabu katika gari lake, akasema: “Fuatana na mimi ukaone jinsi mimi sivumilii ushindani kuelekea Yehova.” Yehonadabu hakusita-sita kwa woga.—2 Wafalme 10:15, 16, New World Translation; ona Kumbukumbu la Torati 6:13-15.
4, 5. (a) Yehu aliwafanya waabudu wa Baali wajitambulishe kwa njia gani? (b) Ndipo Yehu alipochukua hatua gani, na Yehonadabu alikuwa wapi? (c) Wewe unaonaje juu ya kuangamizwa huko kwa waabudu wa Baali?
4 Walipofika Samaria, Yehu alichukua hatua ambazo zingetaka wote walioabudu Baali wajitambulishe wenyewe. Manabii, makuhani na waabudu wote wa Baali walialikwa kwenye dhabihu kuu katika nyumba ya Baali. Waliarifiwa kwamba watu wo wote ambao wangekosa kuhudhuria wangepoteza maisha zao. Yehu akaelekeza kwamba waabudu wote wa Baali wapewe mavazi ya kuvaa ili wapate kutambuliwa waziwazi. Pia wale waliojidai wanamwabudu Yehova walielekezwa kwa njia hiyo waonyeshe ni nani ambaye kwa kweli walitumikia. Ulionekana kuwa wakati wa sherehe nzuri ajabu kwa Baali na kwa Shetani Ibilisi, yule mungu wa uwongo ambaye Baali aliwakilisha.
5 Hapo hapakuwa mahali pa kuwapo waabudu wa kweli wa Yehova. Uchunguzi ulifanywa ili kuhakikisha kwamba ni waabudu wa Baali tu ndio wangekuwapo. Ndipo sherehe ikaanza. Wakati huo, nje, wanaume wa Yehu wakajitayarisha, na alipotoa ishara, wakatenda. “Waangamizeni! Msiache hata mmoja atoke,” akaamuru. Kila mwabudu wa Baali akaangamizwa. Nyumba ya Baali ikabomolewa mpaka chini. “Ndivyo Yehu alivyoangamiza Baali katika Israeli.” Yehonadabu alikuwa kando ya Yehu akishuhudia matukio hayo. (2 Wafalme 10:18-28, New World Translation) Wewe binafsi unakionaje kituko hicho? Ingawa hakuna wo wote kati yetu wanaofurahia kifo cha wengine, hata cha watu waovu, je! tunafahamu kwa nini kituko hicho kilihitajiwa na kwa nini kimeandikwa katika Biblia ili tusome leo?—Linganisha Ezekieli 33:11.
6. (a) Babeli Mkuu ataangamizwaje? (b) Alipokuwa hapa duniani, Yesu alionyeshaje kwamba hakuvumilia ushindani kuelekea Yehova?
6 Masimulizi hayo hayatupi ruhusa ya kuangamiza ama majengo ya vikundi vya kidini ama watu waliojitoa wafuate ibada ya uwongo. Yehova hakuweka mashahidi wake wa kisasa watekeleze hukumu zake za uadilifu. Bali amemweka Yesu Kristo aliyetukuzwa, akiwa Yehu Mkubwa Zaidi ndiye afanye hivyo. Kwa kuruhusu muungano wa serikali za kisiasa zionyeshe uchukivu wazo zenyewe kwa Babeli Mkuu, Mfalme huyo wa kimbingu atatokeza angamizo la milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo. (Ufunuo 6:2; 17:16; 19:1, 2) Alipokuwa hapa duniani, Yesu alikataa kufanya hata tendo moja la ibada ambalo lingemheshimu Ibilisi. Yeye alilaumu vikali kuwekwa kando kwa Neno la Yehova ili kufuata mapokeo ya kibinadamu, na pia kutumiwa kwa ibada ya Mungu ili kupata faida ya kibiashara. Yeye hakuvumilia ushindani kuelekea Yehova.—Luka 4:5-8; Mathayo 15:3-9; 21:12, 13.
7. (a) Ni nini baadhi ya mambo ya kisasa yanayoonyesha kuna ibada ya Baali? (b) Kwa nini Kristo akiwa Mfalme amevumilia mambo hayo?
7 Kwa nini, basi, Kristo, anayetawala sasa katikati ya adui zake, anaruhusu ibada ya Baali ya kisasa ifanikiwe, kama inavyoonekana kuwa. Kwa nini anaruhusu watu waendelee kuheshimu mungu wa huu mfumo wa mambo kwa kuyaweka kando matakwa ya Yehova, na kama inavyoonekana, wasiadhibiwe? Kwa nini anavumilia jinsi wanavyotenda kana kwamba Mungu hapingi uasherati wao, kutukuza kwao namna ya maisha ya kupenda mali, kujiingiza kwao katika mazoea ya kupashana habari na mashetani na huku wakijidai kuwa ni Wakristo, na kufundisha kwao mafundisho ya Kibabuloni kana kwamba hayo ni neno la Mungu? Ule mwigo wa kale unaonyesha kwamba imekuwa hivyo ili kuwajaribu watu, kuwaruhusu waonyeshe kwa nje ni nani wanayeabudu, na hivyo ijulikane kama wanastahili kuhifadhiwa au kuangamizwa.
8. Ni maulizo gani mazito tunayohitaji sisi kujiuliza wenyewe?
8 Wewe umechagua mwendo gani? Je! umeacha kabisa mazoea yote ambayo huenda yakakutambulisha kuwa mzoevu wa ibada ya Baali ya kisasa? Je! umejitenga na ulimwengu, ukachukua msimamo wa kuwa mwabudu wa kweli wa Yehova?—2 Wakorintho 6:17.
9. (a) Ikiwa kweli tuko kama Yehonadabu, tutakuwa tukifanya nini? (b) Maandiko yaliyotajwa yanakaziaje umaana wa mambo hayo?
9 Yehonadabu, akiwa mwabudu wa Yehova asiye Mwisraeli, alifananisha “kondoo wengine” ambao sasa wanakusanywa wakiwa na tumaini la uzima wa milele duniani. Je! wewe unaonyesha roho ya Yehonadabu? Je! uko tayari kujitambulisha peupe kuwa pamoja na Yehu Mkubwa Zaidi na pamoja na wafuasi wapakwa-mafuta walio duniani wanaoitangaza “siku [inayokuja] ya kisasi cha Mungu wetu”? Je! unashiriki pamoja nao kazi hiyo ya haraka? (Isaya 61:1, 2; Luka 9:26; Zekaria 8:23) Je! unampa Yehova ibada ya pekee, bila kuruhusu kitu kiingilie mahali anapopaswa kuwa katika moyo wako? (Mathayo 6:24; 1 Yohana 2:15-17) Je! maisha yako yanaonyesha kwamba uhusiano wako pamoja naye ni mali yako yenye bei kubwa zaidi sana, ya kwamba kila kitu kinginecho kinautegemea?—Zaburi 37:4; Mithali 3:1-6.
JE! UNAYO ALAMA ILE?
10. Biblia inaonyeshaje kwamba ni waabudu wa Yehova tu ndio watakaookolewa?
10 Kungekuwa ni kukosea sana kukata shauri kwamba mtu akijaribu kuishi maisha “mema” na akiacha dini zinazotenda mambo yanayolaumiwa waziwazi katika Neno la Mungu, hatakiwi tena kufanya zaidi. Wote wanaotumaini kuokoka waingie katika “dunia mpya” lazima pia watambuliwe bila kukosewa kuwa waabudu wa Yehova. (Ufunuo 14:6, 7; Zaburi 37:34; Yoeli 2:32) Ujumbe huo unatolewa na maono ambayo nabii Ezekieli alipewa kabla ya kuharibiwa kwa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K.
11. (a) Simulia maono yaliyoandikwa katika Ezekieli 9:1-11. (b) Ni nini kilichokuwa ufunguo wa kwenye wokovu?
11 Ezekieli alimsikia Yehova akiwaagiza wale waliowekwa waangamize Yerusalemu usio na imani pamoja na wakazi wao. Aliona wanaume sita wenye silaha za kuangamiza, na pia kulikuwa na mwanamume mmoja mwenye kuvaa kitani, akiwa na kidau cha wino cha mwandishi viunoni mwake. Kwanza Yehova akamwambia mwanamume huyo mwenye kuvaa vazi la kitani: “Pita kati ya mji, kati ya Yerusalemu, ukatie alama katika vipaji vya nyuso vya watu wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanyika kati yake.” Kisha akawaambia wale wengine sita: “Piteni kati ya mji nyuma yake, mkapige; jicho lenu lisiachilie, wala msione huruma; waueni kabisa, mzee, na kijana, na msichana, na watoto wachanga, na wanawake; lakini msimkaribie mtu ye yote mwenye hiyo alama; tena anzeni katika patakatifu pangu.” Ezekieli aliona katika maono uharibifu uliofuata—ukiwa mkubwa sana hata ikaonekana kana kwamba Waisraeli wote waliokuwa bado katika nchi hiyo walikuwa wakiangamizwa. (Ezekieli 9:1-11) Ufunguo wa kwenye wokovu ulikuwa nini? Ni alama ile katika kipaji cha uso wa mtu iliyowekwa na yule mwanamume mwenye kidau cha wino cha mwandishi.
12. (a) Yalikuwa mambo gani ya kuchukiza ambayo kwa sababu yayo wenye kutiwa alama walikuwa ‘wakiugua na kulia’? (b) Kwa nini Yehova alichukizwa sana na mambo hayo?
12 Watu “wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote” yaliyofanywa katika Yerusalemu ndio hao tu waliotiwa alama ya wokovu. “Machukizo” hayo yalikuwa nini? Matano yameorodheshwa: (1) “Sanamu ya wivu” katika mwingilio wa kwenda kwenye ua wa ndani wa hekalu la Yehova. Kama kitu hicho kilikuwa chenye umbo gani, kilikuwa kikipewa ibada ambayo Waisraeli walidaiwa wampe Yehova. (1 Wafalme 14:22-24) (2) Michoro ya ukutani ya watambazi na ya wanyama, ambayo mbele yayo uvumba ulikuwa ukifukiziwa mle mle ndani ya ua wa hekalu. (3) Wanawake wakiombolezea kifo cha mungu Tamuzi, ambalo ni jina jingine la Nimrodi yule mwasi Yehova. (Mwanzo 10:9) (4) Wanaume wakionyesha dharau kubwa kwa kugeuzia hekalu la Yehova visogo vyao na kulisujudia jua. (Kumbukumbu la Torati 4:15-19) (5) Likiwa dharau la mwisho, watu wakiijaza nchi jeuri na pia wakionyesha “tawi,” yaelekea ni mfano wa uume na uke, kwenye pua ya Yehova. Unafahamu kwa nini Yehova alichukizwa sana nao?—Ezekieli 8:5-17.
13. (a) Ukichukua moja kwanza, eleza juu ya mazoea ya kisasa yanayolinganika na hayo yaliyokuwa “machukizo.” (b) Unaonaje juu ya mazoea hayo?
13 Wewe binafsi unayaonaje mazoea ya kisasa ya Jumuiya ya Wakristo yanayolinganika na “machukizo hayo”? (1) Katika mengi ya makanisa yake kuna mifano ambayo mbele yayo watu wanainama katika kuabudu, ijapo Biblia inakataza kufanya hivyo. (1 Wakorintho 10:14; linganisha 2 Wafalme 17:40, 4l.) (2) Jumuiya ya Wakristo inafuata mtindo wa wazo la kwamba wanadamu waligeuka kutoka kwa wanyama badala ya kwamba waliumbwa na Mungu. Pia inashiriki katika kuonyesha ibada yenye bidii mbele ya mifano ya wanyama na ndege wanaotumiwa kufananisha taifa. (3) Jumuiya ya Wakristo inatumia msalaba katika ibada yake, ambao tangu zamani za kale ulikuwa mfano wa kidini wa Tamuzi, na inashiriki sherehe za kuombolezea wale ambao wamekufa katika vita vya umwagaji wa damu vinavyoonyesha roho ya Nimrodi. (Lakini ona Yohana 17:16, 17.) (4) Inageuzia kisogo yale ambayo Mungu anasema kupitia Neno lake na, badala yake, inachagua “nuru ya elimu” inayotolewa na sayansi ya kisasa na falsafa ya kibinadamu. (1 Timotheo 6:20, 21; linganisha Yeremia 2:13.) (5) Kana kwamba hilo halitoshi, Jumuiya ya Wakristo inaunga mkono mapinduzi mahali fulani fulani na inakuwa na maoni ya kufurahia uasherati, na huku ikijidai inasema katika jina la Mungu. (2 Petro 2:1, 2) Watu fulani wanaona mitindo hiyo kuwa yenye kukubalika. Huenda wasikubaliane nayo yote, lakini labda wanashiriki mingine au angalau kuiachilia iendelee. Wewe unaonaje juu ya mazoea hayo yenye kutomheshimu Mungu yanayoondoa watu mbali na Muumba wa wanadamu?
14. Kwa nini uhakika tu wa kwamba macho ya mtu yamefumbuka akaona udanganyifu wa makanisa haumaanishi kwa lazima kwamba atakuwa mwokokaji?
14 Macho ya watu wengi yamefumbuka wakaona udanganyifu wa makanisa, na hivyo hawaendi tena kanisani. Labda pia wanafadhaika kwa sababu ya jeuri na ukosefu mkubwa wa unyofu ulio katika ulimwengu. Lakini hilo halimaanishi kwa lazima kwamba wametiwa alama ya wokovu. Ni lazima watiwe alama na yule ‘mtu mwenye kidau cha wino cha mwandishi.’ Mambo ya hakika yanaonyesha kwamba leo jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” inafanya kazi hiyo ya kutia alama.—Mathayo 24:45-47.
15. (a) Alama ile ni nini? (b) Mtu anaipataje?
15 Wote wanaotaka kutiwa alama ya kuonyesha wana kibali ya Mungu lazima walikubali agizo ambalo Yehova anatoa kupitia jamii hiyo ya “mtumwa” wawe waabudu wa kweli wa Yehova. Ni lazima wasiwe watu wanaoheshimu Yehova kwa vinywa vyao lakini ambao kwa kweli wanazipenda njia za ulimwengu. (Isaya 29:13, 14; 1 Yohana 2:15) Ni lazima wampende Yehova, wapende viwango vyake na kuhisi kuwa wamehuzunishwa moyoni, ‘wakiugua na kulia,’ kwa sababu ya mafundisho na mazoea yasiyomheshimu. Hakuna mtu atakayetia alama halisi ya wino katika vipaji vya nyuso zao. Lakini watakapokuwa na alama ya mfano itaonekana wazi kwa wote kwamba, wao wakiwa Wakristo walio wakfu na kubatizwa, wameuvaa “utu mpya” unaoelezwa katika Waefeso 4:24. Wana imani iliyo hai. Peupe na faraghani wanajitahidi kutenda mambo yatakayomheshimu Yehova. Watu wote bila kujali asili yao, wanaotumaini kuokolewa waingie katika “dunia mpya” ni lazima wawe na alama hiyo. Si wale tu ambao wametoka katika Jumuiya ya Wakristo.
16. Kwa nini hayo ni yenye maana hasa kwa watoto na wazazi wao?
16 Hasa uhakika ulio wazi ni wa kwamba watekelezaji wa hukumu ya Yehova waliambiwa kwamba umri, jinsia, useja wala uhusiano wa ndoa haukuwa sababu ya kumwachilia mwenye kumkosea Yehova. Ni lazima mtu mmoja mmoja aliyeoa au aliyeolewa atiwe alama yake ili aje aokolewe. Ikiwa wazazi wanazuia watoto wao wasitiwe alama au wakishindwa kuwalea wawe watumishi wa Yehova, ni lazima walaumike kwa litakalopata watoto hao. Ijapokuwa watoto wenye kutii wazazi wanaomwogopa Mungu wanatazamwa na Yehova kuwa “watakatifu,” watoto waasi hawatazamwi hivyo. (1 Wakorintho 7:14; Zaburi 102:28; Mithali 20:11; 30:17) Ikiwa watoto ni wenye umri wa kutosha kuwa Wakristo waliobatizwa lakini hawataki kufuata matakwa hayo, kwamba wamebatizwa, hawakubatizwa, umri wao hautawafanya waokolewe. Basi, ni jambo la lazima kama nini, kwa mtu mmoja mmoja mwenye umri wa kujitegemea kutiwa alama waziwazi awe mtu aliyejiweka wakfu kwa Mungu na anayefanya mapenzi yake!
17. Tumejifunza nini hapa juu ya huruma za Yehova?
17 Yehova ameonyesha wanadamu huruma kubwa kwa kuwatuma mashahidi wake wakawaonye juu ya uharibifu unaokaribia sana na kuwaonyesha njia inayoelekeza kwenye usalama. Lakini anajua sana matendo ya dini ya uwongo na matunda mabovu ambayo imezaa. Wakati Babeli Mkuu itakapoangamizwa, hakuna huruma itakayoonyeshwa kwa wo wote wanaosisitizia kuing’ang’ania. Ili tuje tuokoke kutekelezwa kwa hukumu ya kimungu inayokuja, ni lazima tutembee katika hatua za Yesu Kristo tukiwa waabudu wa kweli wa Yehova, yule Muumba wa mbingu na dunia.
[Picha katika ukurasa wa 95]
Je! kweli wewe unayo alama unayohitaji ili uje uokolewe?