Ni Nani Atakayeiokoka “Siku ya Yehova”?
“Mwapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu, mkingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova!”—2 PETRO 3:11, 12.
1. Ni nani ambao wametenda wakiwa na roho na nguvu ya Eliya?
YEHOVA MUNGU ameteua kutoka miongoni mwa wanadamu watu mmoja-mmoja watakaokuwa warithi-washirika pamoja na Mwana wake, Yesu Kristo, katika Ufalme wa kimbingu. (Waroma 8:16, 17) Wakiwa wangali duniani, Wakristo watiwa-mafuta wamefanya kazi kwa roho na nguvu ya Eliya. (Luka 1:17) Katika makala iliyotangulia, tuliona ufanani fulani-fulani kati ya utendaji wao mbalimbali na ule wa nabii Eliya. Lakini vipi juu ya kazi ya mwandamizi wa Eliya, nabii Elisha?—1 Wafalme 19:15, 16.
2. (a) Muujiza wa mwisho wa Eliya ulikuwa nini, nao wa kwanza wa Elisha ulikuwa nini? (b) Kuna ithibati gani ya kwamba Eliya hakuenda mbinguni?
2 Muujiza wa mwisho uliofanywa na Eliya ulikuwa ule wa kugawanya maji ya Mto Yordani kwa kuyapiga kwa vazi lake rasmi. Hilo liliwawezesha Eliya na Elisha wavuke kupitia ardhi kavu. Walipokuwa wakitembea upande wa mashariki wa huo mto, dhoruba ya upepo ilimchukulia mbali Eliya hadi mahali pengine duniani. (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 15 lenye kichwa “Eliya Alipaa Kuingia Mbingu Zipi?”) Vazi rasmi la Eliya liliachwa. Elisha alipolitumia kuupiga Yordani, maji yake yaligawanyika tena, yakimwezesha kurudi kupitia ardhi kavu. Muujiza huo ulionyesha wazi kwamba Elisha alikuwa mwandamizi wa Eliya katika kuendeleza ibada ya kweli katika Israeli.—2 Wafalme 2:6-15.
Sifa za Kimungu Ni Muhimu
3. Paulo na Petro walisema nini juu ya kuwapo kwa Yesu na “siku ya Yehova”?
3 Karne kadhaa baada ya siku za Eliya na Elisha, mtume Paulo na mtume Petro walihusianisha “siku [fulani] ya Yehova” inayokuja pamoja na kuwapo kwa Yesu Kristo na zile ambazo wakati huo zilikuwa “mbingu mpya na dunia mpya” za wakati ujao. (2 Wathesalonike 2:1, 2; 2 Petro 3:10-13) Ili kuokoka siku kuu ya Yehova—Mungu aangamizapo maadui wake na kuokoa watu wake—lazima tumtafute Yehova na kuonyesha usikivu na uadilifu. (Sefania 2:1-3) Lakini sifa nyingine za ziada zaonekana tufikiriapo kwa uangalifu matukio yanayomhusisha nabii Elisha.
4. Bidii ina fungu gani katika utumishi wa Yehova?
4 Bidii kwa ajili ya utumishi wa Mungu ni muhimu ikiwa tutaokoka “siku ya Yehova.” Eliya na Elisha walikuwa wenye bidii katika utumishi wa Yehova. Wakiwa na bidii hiyohiyo, leo baki la Wakristo watiwa-mafuta humtolea Yehova utumishi mtakatifu na huongoza katika kuhubiri habari njema.a Tangu katikati ya miaka ya 1930, wamewatia moyo wote wanaokubali ujumbe wa Ufalme na kutumainia kuishi milele duniani wajiweke wakfu kwa Yehova na kubatizwa. (Marko 8:34; 1 Petro 3:21) Mamilioni ya watu wameitikia kwa mwelekeo mzuri kitia-moyo hicho. Wakati mmoja walikuwa katika giza la kiroho na wafu katika dhambi, lakini sasa wamejifunza kweli ya Mungu, wamekubali lile tumaini la uhai wa milele kwenye paradiso ya kidunia, nao wamekuwa wana bidii katika utumishi wa Yehova. (Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3-5) Kwa bidii, kushirikiana, ukaribishaji-wageni, na matendo yao mengine yaliyo mema, wao huburudisha sana ndugu wa Kiroho wa Kristo walio duniani bado.—Mathayo 25:31-46.
5. Kwa nini ni jambo la maana sana kufanyia “ndugu” za Yesu mambo mema, nasi tuna kielelezo gani cha siku ya Elisha?
5 Wawafanyiao “ndugu” za Yesu mambo mema kwa sababu hao watiwa-mafuta ni wafuasi wake, wana tumaini la kuokoka “siku ya Yehova.” Mume na mke katika kijiji cha Shunemu walibarikiwa sana kwa kuwa wenye fadhili kwa Elisha na hadimu wake na kwa kuwakaribisha. Mume na mke hao hawakuwa na mwana, naye mume alikuwa mzee. Lakini Elisha alimwahidi huyo mwanamke Mshunami kwamba angezaa mwana, na hilo kwa hakika lilitukia. Mwana huyo wa pekee alipokufa miaka kadhaa baadaye, Elisha alienda Shunemu na kumfufua. (2 Wafalme 4:8-17, 32-37) Ni thawabu nyingi kama nini kwa kumkaribisha Elisha!
6, 7. Naamani aliweka kielelezo gani, na hilo laathirije kuokoka “siku ya Yehova”?
6 Unyenyekevu unahitajiwa ili kukubali mwelekezo wenye kutegemea Biblia kutoka kwa “ndugu” za Kristo kukiwa na tumaini la kuokoka siku ya Yehova. Naamani, mkuu wa jeshi Msiria, alilazimika kuonyesha unyenyekevu ili kufuata dokezo la msichana Mwisraeli aliyetekwa na kutafuta ponyo kwa kwenda Israeli kumtafuta Elisha. Badala ya kutoka nyumbani kwake ili amlaki Naamani, Elisha alimtumia ujumbe huu: “Enenda ukaoge katika Yordani mara saba, na nyama ya mwili wako itakurudia, nawe utakuwa safi.” (2 Wafalme 5:10) Kujionea fahari kwa Naamani kulikosewa, naye akakasirika, lakini baada ya kwenda kwa unyenyekevu na kujichovya Yordani mara saba, “nyama ya mwili wake ikarudi ikawa kama nyama ya mwili wa mtoto mchanga, akawa safi.” (2 Wafalme 5:14) Kabla ya kurudi nyumbani, Naamani alifunga safari ndefu kurudi Samaria ili kumshukuru nabii wa Yehova. Akiwa ameazimia kutofaidika kimwili kutokana na nguvu zenye kupewa na Mungu, Elisha alitoka ili amlaki Naamani, lakini hakukubali zawadi zozote. Naamani alimwambia Elisha hivi kwa unyenyekevu: “Mtumwa wako hatatoa tena sadaka ya kuteketezwa wala dhabihu kwa miungu mingine, ila kwa BWANA [“Yehova,” NW].”—2 Wafalme 5:17.
7 Kwa kufuata kwa unyenyekevu shauri la Kimaandiko la watiwa-mafuta, mamilioni ya watu wanabarikiwa sana leo. Isitoshe, kwa kudhihirisha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu, watu hao wenye moyo wa haki wamesafishwa kiroho. Sasa wanaonea shangwe pendeleo la kuwa marafiki wa Yehova Mungu na Yesu Kristo. (Zaburi 15:1, 2; Luka 16:9) Na ujitoaji wao kwa Mungu na kwa utumishi wake utathawabishwa kwa kuhifadhiwa kwao wasipatwe na uharibifu wa milele ukaribiao kuwapata wakosaji wenye kiburi, wasiotubu, katika “siku ya Yehova” inayokaribia kwa kasi.—Luka 13:24; 1 Yohana 1:7.
“Aliye Upande Wangu Ni Nani?”
8. (a) Watakaookoka “siku ya Yehova” wana mtazamo gani kuelekea kufanya mapenzi ya kimungu? (b) Yehu alipewa utume gani? (c) Yezebeli alipasa kupatwa na nini?
8 Wanaotumainia kuokoka “siku ya Yehova” lazima pia waamue kufanya mapenzi ya kimungu. Eliya alitabiri kwa ujasiri kuharibiwa kwa familia ya Mfalme Ahabu yenye kuua kimakusudi na kuabudu Baali. (1 Wafalme 21:17-26) Hata hivyo, kabla ya ufishaji huo kufanywa, ilikuwa lazima Elisha, mwandamizi wa Eliya, akamilishe kazi fulani ambayo haikuwa imemalizika. (1 Wafalme 19:15-17) Wakati wa Yehova ulipowadia, Elisha alimwagiza hadimu aende na kumtia mafuta Yehu, mkuu wa jeshi, awe mfalme mpya wa Israeli. Baada ya kuyamimina mafuta juu ya kichwa cha Yehu, huyo hadimu alimwambia hivi: “BWANA, Mungu wa Israeli, asema hivi, Nimekutia mafuta uwe mfalme juu ya watu wa BWANA, yaani, juu ya Israeli. Nawe utawapiga nyumba ya Ahabu, bwana wako, ili nijilipize kisasi cha damu ya watumishi wangu manabii, na damu ya watumishi wote wa BWANA, mkononi mwa Yezebeli. Kwa maana nyumba yote ya Ahabu wataangamia.” Malkia Yezebeli mwovu angetupwa kwa mbwa na asipate kuzikwa kwa heshima.—2 Wafalme 9:1-10.
9, 10. Neno la Eliya lilitimizwaje katika kisa cha Yezebeli?
9 Wanaume wa Yehu walitambua uhalali wa kutiwa mafuta kwake, wakapiga mbiu juu ya kuwa kwake mfalme mpya wa Israeli. Akitenda kwa kukata maneno, Yehu alipiga mbio kuelekea Yezreeli ili kuanza kazi yake ya kufisha viongozi waasi-imani wa ibada ya Baali. Aliyekuwa wa kwanza kupatwa na mshale wa ufishaji wa Yehu alikuwa mwana wa Ahabu, Mfalme Yehoramu. Alipanda farasi kutoka jijini akaulize ikiwa Yehu alikuwa amekuja kwa utume wa amani. “Amani gani, maadamu uzinzi wa mama yako Yezebeli na uchawi wake ni mwingi?” Yehu akajibu. Kisha, mshale wa Yehu ukadunga moyo wa Yehoramu.—2 Wafalme 9:22-24.
10 Wanawake wa kimungu huepuka kuwa kama Yezebeli au wanawake wowote wa aina yake. (Ufunuo 2:18-23) Kufikia wakati ambapo Yehu alifika Yezreeli, Yezebeli alikuwa amejaribu kujifanya avutie. Akitazama chini kutoka dirishani, alimsalimu Yehu kwa tisho ambalo halikuwa wazi. Yehu akawauliza mahadimu wake: “Aliye upande wangu ni nani?” Mara moja, maofisa wawili watatu wakatazama chini. Je, walikuwa upande wa Yehu? “Mtupeni chini,” Yehu akahimiza. Ndipo, wakatenda kwa kukata maneno, wakimtupa Yezebeli mwovu nje ya dirisha. Yadhaniwa kuwa alikanyagwa-kanyagwa chini ya kwato za farasi. Watu walipokuja kumzika, “hawakuona kitu ila kifuvu cha kichwa chake, na miguu yake, na vitanga vya mikono yake.” Ni utimizo wenye kutazamisha ulioje wa neno hili la Eliya: “Mbwa wataila nyama ya Yezebeli”!—2 Wafalme 9:30-37.
Kutegemeza Ibada ya Kweli kwa Dhati
11. Yehonadabu alikuwa nani, naye alionyeshaje kutegemeza kwake ibada ya kweli?
11 Wanaotumaini kuokoka “siku ya Yehova” na kuishi milele duniani lazima wategemeze ibada ya kweli kwa moyo wote. Lazima wawe kama Yehonadabu, au Yonadabu, mwabudu wa Yehova asiye Mwisraeli. Yehu alipoendelea kutimiza utume wake kwa bidii, Yehonadabu alitaka kuonyesha kukubali kwake na kutegemeza kwake. Kwa hiyo akaondoka ili kumlaki mfalme mpya wa Israeli, aliyekuwa akielekea Samaria ili kufisha waliosalia wa nyumba ya Ahabu. Alipomwona Yehonadabu, Yehu aliuliza hivi: “Je! moyo wako umenyoka, kama moyo wangu ulivyo pamoja na moyo wako?” Kukubali kwa Yehonadabu kulimsukuma Yehu anyooshe mkono wake na kumwalika Yehonadabu aingie gari lake la vita, akisema hivi: “Fuatana nami, ukaone wivu wangu kwa BWANA.” Bila kukawia, Yehonadabu alikubali pendeleo la kumwonyesha mfishaji mtiwa-mafuta wa Yehova kumtegemeza kwake.—2 Wafalme 10:15-17.
12. Kwa nini Yehova hudai kwa kufaa ujitoaji usiohusisha wengine?
12 Kutegemeza ibada ya kweli kwa dhati kwa hakika kwafaa, kwa kuwa Yehova ndiye Muumba na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima, ambaye hudai na hustahili kwa kufaa ujitoaji wetu usiohusisha wengine. Aliwaamuru Waisraeli hivi: “Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia. Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi, BWANA, Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu.” (Kutoka 20:4, 5) Wale watumainio kuokoka “siku ya Yehova” lazima wamwabudu yeye peke yake, wakifanya hivyo “kwa roho na kweli.” (Yohana 4:23, 24) Lazima wawe thabiti kwa ajili ya ibada ya kweli, kama Eliya, Elisha, na Yehonadabu.
13. Kama vile moyo wa Yehonadabu ulivyokuwa pamoja na Yehu, ni nani ambao humkiri Mfalme wa Kimesiya, nao huonyeshaje hilo?
13 Baada ya kufishwa kwa nyumba ya Ahabu, Mfalme Yehu alichukua hatua nyingine za kutambulisha waabudu wa Baali na kuondolea mbali dini hiyo isiyo ya kweli katika Israeli. (2 Wafalme 10:18-28) Leo, Mfalme wa kimbingu Yesu Kristo amewekwa rasmi afishe maadui wa Yehova na kutetea enzi kuu Yake. Kama vile moyo wa Yehonadabu ulivyokuwa pamoja na Yehu, leo “umati mkubwa” wa “kondoo wengine” wa Yesu humkubali Kristo kwa moyo wote kuwa Mfalme wa Kimesiya nao hushirikiana na ndugu zake wa kiroho walio duniani. (Ufunuo 7:9, 10; Yohana 10:16) Wanatoa uthibitisho wa hilo kwa kuzoea dini ya kweli na kushiriki kwa bidii katika huduma ya Kikristo, kuonya maadui wa Mungu juu ya “siku ya Yehova” inayokaribia kasi.—Mathayo 10:32, 33; Waroma 10:9, 10.
Matukio Yenye Kutazamisha Yako Mbele!
14. Ni jambo gani liko mbele ya dini isiyo ya kweli?
14 Yehu alichukua hatua ya kukomesha ibada ya Baali katika Israeli. Siku yetu, kupitia kwa Yehu Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo, Mungu ataharibu Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli. Karibuni tutaona utimizo wa maneno haya ya malaika aliyomwambia mtume Yohana hivi: “Nazo pembe kumi ulizoziona, na hayawani-mwitu, hawa watamchukia kahaba [Babiloni Mkubwa] na watamfanya ukiwa na kuwa uchi, na watakula kabisa sehemu zake zenye nyama na watamchoma kabisa kwa moto. Kwa maana Mungu alitia hilo ndani ya mioyo yao ili kutekeleza fikira yake, hata kutekeleza fikira yao moja kwa kumpa hayawani-mwitu ufalme wao, mpaka maneno ya Mungu yawe yamekwisha kutimizwa.” (Ufunuo 17:16, 17; 18:2-5) “Pembe kumi” zawakilisha mamlaka za kisiasa za kijeshi zinazotawala duniani. Ingawa kwa sasa zina uhusiano wenye uzinzi kiroho na Babiloni Mkubwa, muda wake ni mfupi. Sehemu ya kisiasa ya ulimwengu huu itaharibu dini isiyo ya kweli, naye “hayawani-mwitu”—Umoja wa Mataifa—atakuwa na fungu kuu pamoja na zile “pembe kumi” katika kumwangamiza kabisa Babiloni Mkubwa.b Ni pindi iliyoje ya kumsifu Yehova.—Ufunuo 19:1-6.
15. Ni jambo gani litakalotukia jaribu lifanywapo la kuharibu tengenezo la kidunia la Mungu?
15 Baada ya Mfalme Yehu kushambulia vikali ibada ya Baali, nyumba yake ya kifalme iligeuzia uangalifu maadui wa kisiasa wa Israeli. Mfalme Yesu Kristo atachukua hatua kama hiyo. Nguvu za kisiasa zitabaki baada ya kuharibiwa kwa dini isiyo ya kweli iliyo ya Kibaali. Chini ya uvutano wa Shetani Ibilisi, maadui hao wa enzi kuu ya Yehova watafanya shambulio la kufa na kupona wakijaribu kuharibu tengenezo la kidunia la Mungu. (Ezekieli 38:14-16) Lakini Yehova atamfanya Mfalme Yesu Kristo awaangushe kwa kuwaharibu kwenye Har–Magedoni, “vita ya siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote,” kwa kumalizia utetezi wa enzi kuu ya Yehova!—Ufunuo 16:14, 16; 19:11-21; Ezekieli 38:18-23.
Kutumikia kwa Bidii ya Elisha
16, 17. (a) Twajuaje kwamba Elisha alikuwa mwenye bidii hadi mwisho wa uhai wake? (b) Twapaswa kufanya nini na mishale ya kweli?
16 Mpaka “siku ya Yehova” ikomeshapo mfumo wote mwovu wa mambo wa Shetani, watumishi wa Mungu watakuwa na ujasiri na wenye bidii kama Elisha. Mbali na kazi yake akiwa hadimu wa Eliya, Elisha alitumikia peke yake akiwa nabii wa Yehova kwa miaka zaidi ya 50! Naye Elisha alikuwa mwenye bidii hadi mwisho wa maisha yake marefu. Kabla tu ya kifo chake, alitembelewa na mjukuu wa Yehu, Mfalme Yehoashi. Elisha alimwambia apige mshale nje ya dirisha. Huo mshale ukaenda mbio hadi kwenye shabaha yake, naye Elisha akasema kwa mkazo hivi: “Mshale wa BWANA wa kushinda, naam, mshale wa kushinda Shamu, kwa maana utawapiga Washami katika Afeki hata utakapowaangamiza.” Kisha Elisha alipomwomba, Yehoashi alipiga ardhi kwa mishale yake. Lakini alifanya hilo bila bidii, akipiga mara tatu tu. Ndipo Elisha akasema kwamba, kwa sababu hiyo, Yehoashi angepewa ushindi mara tatu tu dhidi ya Shamu, na ndivyo ilivyotokea. (2 Wafalme 13:14-19, 25) Mfalme Yehoashi hakuwaangusha Washami kikamili, ‘hata kuwaangamiza.’
17 Ingawa hivyo, wakiwa na bidii kama ya Elisha, baki la watiwa-mafuta huendeleza pigano dhidi ya ibada isiyo ya kweli. Waandamani wao wenye matumaini ya kidunia wanafanya vivyo hivyo. Isitoshe, wote wanaotumaini kuokoka “siku ya Yehova” hufanya vema kukumbuka maneno ya Elisha mwenye bidii juu ya kuipiga ardhi. Acheni tuchukue mishale ya kweli na kuipiga kwa bidii—tena na tena—ndiyo, hadi Yehova asemapo kazi tufanyayo na mishale hiyo imekamilika.
18. Twapaswa kuitikiaje maneno ya 2 Petro 3:11, 12?
18 Karibuni “siku ya Yehova” itakomesha mfumo mwovu wa mambo uliopo. Kwa hiyo acheni tujiruhusu kuchochewa na maneno ya mtume Petro yenye kutia moyo. “Kwa kuwa vitu vyote hivi vitafumuliwa hivyo,” Petro akasema kwa mkazo, “nyinyi mwapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu, mkingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova!” (2 Petro 3:11, 12) Kila sehemu ya mfumo huu ifumuliwapo na moto wa hasira ya Mungu ionyeshwayo kupitia Yesu Kristo, ni wale tu walio na rekodi ya mwenendo mnyoofu na ya ujitoaji-kimungu ndio watakaoponyoka. Usafi wa kiadili na wa kiroho ni muhimu. Ndivyo na kuwapenda wanadamu wenzi, kuonyeshwako kwa kuitikia mahitaji yao, hasa katika njia ya kiroho kupitia huduma yetu ya Kikristo.
19. Twapaswa kufanya nini ili kuokoka “siku ya Yehova”?
19 Je, maneno na matendo yako hukutambulisha kuwa mtumishi mwaminifu na mwenye bidii wa Mungu? Ikiwa ndiyo, waweza kuwa na tumaini la kuokoka “siku ya Yehova” kuingia ulimwengu mpya ulioahidiwa wa Mungu. Ndiyo, waweza kuokoka ikiwa utawafanyia mema ndugu wa kiroho wa Kristo kwa sababu ni wafuasi wake, kama vile mume na mke Washunami walivyomkaribisha Elisha. Ili kuokoka lazima uwe kama Naamani, aliyekubali kwa unyenyekevu agizo la kimungu, akawa mwabudu wa Yehova. Ikiwa watamani sana kuishi milele katika paradiso ya kidunia, lazima uonyeshe kutegemeza kwa dhati ibada ya kweli, kama alivyofanya Yehonadabu. Kisha waweza kuwa miongoni mwa watumishi waaminifu wa Yehova, ambao karibuni watajionea utimizo wa maneno haya ya Yesu: “Njoni, nyinyi ambao mmebarikiwa na Baba yangu, rithini ufalme uliotayarishwa kwa ajili yenu tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu.”—Mathayo 25:34.
[Maelezo ya Chini]
a Ona sura ya 18 na ya 19 ya kitabu “Let Your Name Be Sanctified,” kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Ona ukurasa wa 254-256 katika kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
Ungejibuje?
◻ Ni zipi baadhi ya sifa zinazohitajiwa ili kuokoka “siku ya Yehova”?
◻ Mume na mke Washunami waliweka kielelezo gani siku ya Elisha?
◻ Ni somo gani lipatikanalo kutokana na Naamani?
◻ Twaweza kufuataje kielelezo cha Yehonadabu?
◻ Andiko la 2 Petro 3:11, 12 lapaswa lituathirije?