Sura 20
‘Mdogo Awa Taifa Hodari’
1. (a) Kwa habari ya ukubwa wa ongezeko la waabudu wa kweli, Yehova alitabiri nini? (b) Ni nani hasa anayetokeza hilo, na namna gani?
KWA MUDA mrefu wale walio waabudu wa Yehova wamekuwa wachache kwa hesabu, wakilinganishwa na idadi ya wanadamu wote. Lakini wakati wetu huu hesabu yao inaongezeka kwa kadiri yenye kusisimua wenye kupenda uadilifu. Kwa habari ya ukubwa wa ongezeko, Yehova mwenyewe alitabiri hivi: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; mimi, [Yehova], nitayahimiza hayo wakati wake.” (Isaya 60:22) Kama andiko hilo linavyoeleza, Yehova mwenyewe anatimiza hilo. Namna gani? Kwa kutokeza kati ya watumishi wake hali inayowatofautisha kabisa na vikundi vya mataifa yanayowazunguka na inayovutia sana wenye mioyo minyofu.
2. (a) Unabii wa Isaya 60:1, 2 unaelekezwa kwa nani? (b) Ni kwa njia gani “utukufu wa [Yehova]” ulifanywa umwangazie mwanamke huyo? (c) Mabaki ‘wameangazaje‘?
2 Hilo lilitabiriwa katika Isaya 60:1, 2, ambapo Yehova anasema na “mwanamke” wake, tengenezo lake la viumbe wa kiroho walio washikamanifu na pia wana waliozaliwa kwa roho walio hapa duniani, akimwambia: “Ondoka, uangaze; kwa kuwa nuru yako imekuja, na utukufu wa [Yehova] umekuzukia. Maana, tazama, giza litaifunika dunia, na giza kuu litazifunika kabila za watu; bali [Yehova] atakuzukia wewe, na utukufu wake utaonekana juu yako.” Msingi wa tofauti hiyo ni kuzaliwa kwa Ufalme wa Kimasihi mikononi mwa Yesu Kristo mwaka wa 1914. Ndipo “utukufu wa [Yehova]” ulipoangazia tengenezo la kimbingu, lililouzaa Ufalme huo. Kulikuwa na sababu ya shangwe kati yao. (Ufunuo 12:1, 2, 5, 10-12) Na hapa duniani mabaki ya warithi wa Ufalme walishiriki furaha hiyo. Kuanzia mwaka wa 1919, ‘waliangaza’ wakati walipoanza kazi ya kutangaza ulimwenguni pote Ufalme wa Mungu kuwa ndio tumaini halisi na la pekee la wanadamu.—1 Petro 2:9; Mathayo 5:14-16.
3. (a) Kwa nini, hasa tangu mwaka wa 1914, ‘giza limeifunika dunia’? (b) Ondoleo pekee la matatizo ni nini?
3 Tofauti na hilo, mwaka wa 1914 vikundi vya mataifa ya ulimwengu, vikiwa vinapigana ili kudumisha enzi yavyo vyenyewe, viliingia katika muhula wa jeuri na wenye ukosefu wa usalama ambao havijapata kutoka katika huo kamwe. Ukosefu wa uthabiti tangu wakati huo umefanya wengi wafahamu kwamba, ijapokuwa “maendeleo ya kisayansi,” hawana wakati ujao ulio salama wa kutegemea. Kweli kweli, ‘giza linaifunika dunia.’ Kwa nini hawawezi kuona njia ya kutokea? Kwa sababu mataifa yamemkataa Yehova kuwa Mwenye Enzi Kuu. Ni watawala wachache wanaotoa utumishi wa mdomo kwa “Mungu” ambaye jina lake hawalitumii kamwe. Wamekaza nia waongoze mambo wenyewe, lakini matatizo wanayopata yanazidi uwezo wa mwanadamu kuyatatua. (Yeremia 8:9; Zaburi 146:3-6) Ulimwengu wa sasa, pamoja na pupa na ufisadi wake, umeingia katika “siku za mwisho” wake. Hakuna njia ambayo kwa hiyo ulimwengu huu unaweza kuepuka uharibifu unaouotea. Ni watu wanaouamini kabisa Ufalme wa Mungu tu ndio wanaoweza kutazamia wakati ujao wakiwa na hakika. Kwa hesabu yenye kuongezeka, wenye mioyo minyofu sasa wanalifahamu hilo. Wanashirikiana kwa bidii pamoja na Mashahidi wa Yehova, wanaozungumza juu ya Ufalme na pia wanajitahidi kwa bidii kufuata yale wanayohubiri.
‘MDOGO AWA ELFU’
4. Kwa utimizo wa Isaya 60:4, ni kazi gani ya kukusanya iliyokaziwa fikira?
4 Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilipoisha, kukusanywa kwa warithi wa Ufalme kulikuwa bado kukamilishwa. Bado walikuwako “wana” na “binti” wa Yerusalemu wa kimbingu waliohitajiwa ili kujazia hesabu iliyotabiriwa ya 144,000 ya watu ambao wangetawala pamoja na Kristo mbinguni. Ingawa hivyo, Yehova alitabiri kufungwa kwa kazi hiyo, akisema: “Inua macho yako, utazame pande zote; wote wanakusanyana; wanakujia wewe; wana wako watakuja kutoka mbali, na binti zako watabebwa nyongani.” (Isaya 60:4) Yakiwa ni matokeo ya kutangazwa kwa Ufalme kulikofanywa tangu mwaka wa 1919 na baada ya hapo, maelfu zaidi walijiweka wakfu kwa Yehova, wakabatizwa na kupakwa mafuta kwa roho takatifu. Ingawa hivyo, wote pamoja, kikundi kizima cha warithi wa Ufalme kilisemwa na Yesu kuwa “kundi dogo” tu. (Luka 12:32) Ili kutimiza yaliyotabiriwa katika Isaya 60:22, bila shaka wangekuwako zaidi ambao wangekusanywa kwenye ibada ya kweli. Imekuwa hivyo hasa!
5. Chanzo cha ongezeko zaidi kimesimuliwaje katika Isaya 55:5?
5 Hao wanasemwa katika Isaya 55:5 hivi: “Tazama, utaita taifa usilolijua, na taifa lisilokujua wewe litakukimbilia, kwa sababu ya [Yehova], Mungu wako, na kwa ajili yake Mtakatifu wa Israeli; maana [amekurembesha].” Hao ni watu kutoka nje ya Israeli wa kiroho. Wanakuja kutoka mataifa mengi lakini wanakuwa watu wenye umoja, wote wakiunga mkono kwa ushikamanifu Ufalme wa Mungu. Wao ni “taifa” ambalo mabaki ya Israeli wa kiroho ‘hawakujua’ wakati huo kulingana na ufahamu wao wa Maandiko, wala watu hao hawakuwa wamewatambua zamani watumishi wa Mungu inavyopasa. Lakini yakiwa ni matokeo ya kuhubiriwa kwa habari njema, wanavutiwa kwa sababu wanafahamu kwamba Waisraeli hao wa kiroho wanaabudu Mungu wa kweli na kwa sababu wanaona ndani yao urembo wa kiroho unaoweza kutokana na baraka ya Mungu tu.
6. Ujumbe wa Ufalme unafikishwa kwenye umbali gani, na kwa matokeo gani yenye kusisimua?
6 Ijapokuwa yote ambayo Shetani amefanya ili azuie kuhubiriwa kwa ujumbe wa Ufalme na kugeuza fikira za watu kwenye shughuli nyingine, nuru ya ukweli inaendelea kuenea hata kwenye sehemu za mbali sana za dunia. Matokeo yamekuwa kama Mungu alivyomwambia zamani “mwanamke” wake kupitia unabii huu: “Ndipo utakapoona na kutiwa nuru, na moyo wako utatetemeka na kukunjuka; kwa kuwa wingi wa bahari utageuzwa kukujia, utajiri wa mataifa utakuwasilia. . . . Na kuzitangaza sifa za [Yehova].” (Isaya 60:5, 6) Ndiyo, “mkutano mkubwa” wa watu ambao wakati mmoja walikuwa sehemu ya “bahari” ya wanadamu waliojitenga na Mungu, watu ambao maisha zao zilitiwa giza na “giza kuu” linalofunika mataifa, wamejiunga pamoja na Israeli wa kiroho. Machoni pa Mungu, hao ndio wenye bei kweli kweli kutoka mataifa yote.
7. Kwa jinsi ongezeko lilivyotabiriwa, Yehova anaonyeshaje kitu kilicho cha bei kweli kweli machoni pake?
7 Wakati wa kujengwa upya kwa hekalu la Yehova katika Yerusalemu, yeye aliongoza nabii wake Hagai atangaze hivi: “Nitatikisa mataifa yote, na vitu vinavyotamaniwa na mataifa yote vitakuja; nami nitaijaza nyumba hii utukufu, asema [Yehova] wa majeshi.” (Hagai 2:7) Mwishowe kusukwasukwa na kutikiswa huko kwa mataifa kutaongoza kwenye kuangamizwa kwao, lakini kabla hilo halijatukia ni lazima “vitu vinavyotamaniwa na mataifa yote” vikusanywe kutoka kati yao na kuingizwa katika hekalu kuu la kiroho la Yehova, nyumba yake ya ibada ya ulimwenguni pote. Wakiwa humo watapata usalama wakati ulimwengu utakapoanguka katika maangamizi. Waabudu hao walio hai ndio wenye bei kwa Yehova. Yeye hataki utajiri wao wa kimwili. (Mika 6:6-8) Kitu chenye bei kubwa zaidi sana wanachoweza kumpa Yehova ni ibada yao ya nafsi yote. Wanakuja wakiwa na matoleo ya kujitoa kwa moyo na utumishi wa bidii, wote ‘wakizitangaza sifa za Yehova.’ Kutokea kwao kumeleta furaha kwa watumishi washikamanifu wa Yehova mbinguni na duniani kama nini!
8. Ni vionyesho gani ambavyo Biblia inatoa juu ya kadiri ya kukusanywa kwa wanaotazamiwa kuwa warithi wa kidunia wa Ufalme?
8 Waabudu hao wa Yehova wanaolipokea tumaini la uzima katika dunia ya Paradiso, watakuwa wangapi? Biblia haiweki hesabu kamili. Imeachwa wazi ili watu wengi kutoka mataifa yote, wanaotaka, wafaidike na maandalizi ya upendo ya Yehova. Ingawa hivyo, kionyesho cha jambo la kutazamia kinapatikana katika Isaya 60:8, andiko linaloeleza kuwa wao ni mfano wa njiwa “warukao kama wingu”—wingu ambalo kidogo linaitia giza dunia chini. Hilo linaelekeza kwenye mmiminiko wa hesabu kubwa ya watu katika muda mfupi. Kwa sababu ya kuja kwa wingi hivyo kwa waabudu wa Yehova, ilitabiriwa kwamba, “mdogo” wa Israeli wa kiroho ‘angekuwa elfu, na mnyonge angekuwa taifa hodari,’ na Yehova akasema kwamba yeye ‘angeyahimiza hayo wakati wake.’ (Isaya 60:22) Je! hiyo inalingana na yale ambayo yametukia hakika?
9. Ongezeko hilo limetukia kwa kadiri gani tangu mwaka wa 1935?
9 Baada ya vita ya ulimwengu ya kwanza kulikuwako elfu wachache tu waliokuwa wakishiriki kwa bidii kutoa ushuhuda wa peupe juu ya Ufalme. Kufikia mwaka wa 1935 wakajumlika kidogo zaidi ya 60,000 ulimwenguni pote. Mwaka wa 1941 hesabu ya watangazaji wa Ufalme ilipita hesabu ya 100,000. Kufikia mwaka wa 1953, kukawa na zaidi ya 500,000. Miaka kumi iliyofuata wakafikia hesabu ya milioni moja. Kufikia mwisho wa 1984, wakawa 2,842,531. Kwa wastani, wanatumia kila siku kuzidi saa milioni moja ili waonyeshe wengine sababu gani Ufalme wa Mungu unatoa tumaini halisi kwa ajili ya wakati ujao. Kwa kulinganisha na hesabu ya wale ambao, wakiwa Mashahidi wa Yehova, wanatoa ushahidi wa kwamba wao ni raia za Ufalme wa Kimasihi wa Yehova, ni jambo linalofaa kuangaliwa kwamba mataifa fulani ya ulimwengu leo ni madogo katika hesabu kuliko “taifa” hilo linalozidi kukua. Ingawa hivyo, “taifa” hilo la pekee halishiriki siasa za ulimwengu lakini limejitoa tu kwa utumishi wa Mungu wa kweli.
10. (a) Ni hali gani zinazofanya ukuzi huo uwe wa ajabu machoni petu? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba ongezeko zaidi bado litakuja?
10 Je! unabii huo utatimizwa kwa kadiri hiyo? Yale ambayo tayari yametukia ni mengi kutosha kufaa simulio hilo la Biblia. Na pia, ni jambo la ajabu tunapozifikiria hali ambazo chini yazo kazi hiyo imefanywa—vizuizi vilivyoondolewa, ushahidi wa mwelekezo wa kimungu wa kuifanikisha, kujitoa ambako kumeonyeshwa na wale wanaoishiriki. Yaliyo ya ajabu, pia, ni mabadiliko ambayo imefanyiza katika maisha za watu. Lakini ongezeko la watu wanaojipanga waziwazi upande wa Yehova halisimami, wala halipungui. Wakati wa miaka ya majuzi wamekuwako, kwa wastani, zaidi ya watu 10,000 wenye kujitoa kila mwezi ili wazamishwe katika maji, na jumla imekuwa ikipanda juu kila mwaka. Wote hao, kwa kutimiza yanayofananishwa na ubatizo wao, huenda wakawa na tazamio lenye kutumainisha la kuokoka kuingia katika “dunia mpya.”
11. (a) Biblia inaonyeshaje kwamba mamilioni hao wanakuwa sehemu ya tengenezo? (b) Kusudi kuu la tengenezo hilo ni nini?
11 Mamilioni hayo ya watu si wanafunzi wa Biblia wenye kujitegemea wenyewe, kila mmoja akimtumikia Mungu kwa njia yake mwenyewe. Ni watu ambao kwa utii wanakuwa sehemu ya tengenezo lionekanalo la Yehova. Kama tulivyokwisha kuona, kwanza warithi wa Ufalme ‘walikusanywa’ pamoja. Sasa wengine kutoka mataifa, wakiwa na tumaini la uzima wa kidunia ‘wanawajia.’ (Isaya 60:4, 5) Wameungana katika “kundi moja” chini ya “mchungaji mmoja,” Yesu Kristo. (Yohana 10:16) Mtume Petro alisimulia Wakristo wa kweli kuwa ‘ushirika wa ndugu’ ulimwenguni pote, na Paulo akawaomba sana wasijitenge wawe peke yao bali ‘wakusanyike pamoja,’ na kuzidi kufanya hivyo kwa kadiri siku ile ya kutekelezwa kwa hukumu ya kimungu inavyokaribia. (1 Petro 5:9, New World Translation; Waebrania 10:23-25) Kwa njia hiyo wanatiwa nguvu na kutayarishwa washiriki kusudi kuu la kuwapo kwa tengenezo hilo. Ni kusudi gani? Ni kutukuza jina la Yehova.—1 Petro 2:9; Isaya 12:4, 5.
KAZI INAYOPASA KUFANYWA
12. (a) Yesu alionyeshaje kazi ambayo sote tumepaswa tuwe tukiishiriki? (b) Ni ya maana kadiri gani, na kwa nini?
12 Wote wanaokuja kushirikiana na tengenezo la Yehova wanafahamu upesi kwamba wale waliomo ni wafanya kazi. Kwa kufuata mfano wa Yesu Kristo wote ni wahubiri wenye bidii wa Ufalme wa Mungu, ambao ndio njia ambayo kwa hiyo jina la Yehova litaondolewa malawama. Yesu mwenyewe alisema: “Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu . . . maana kwa sababu hiyo nalitumwa.” (Luka 4:43) Yeye alisema kwa bidii juu ya uhitaji wa wengine kutegemeza maisha zao juu ya kufanya mapenzi ya Mungu. Alifundisha wafuasi wake wafanye kazi ile ile aliyokuwa akifanya. Alitabiri kwamba wakati huu tunamoishi, ‘habari njema ya ufalme ingehubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote.’ (Mathayo 24:14) Hiyo ndiyo kazi iliyo ya maana zaidi sana ambayo ye yote kati yetu anaweza kufanya. Kwa nini hivyo? Kwa sababu kupitia hiyo tunategemeza enzi halisi ya Yehova Mungu, ambayo juu yake hali njema ya uumbaji wote inategemea. Kwa kushiriki utendaji huo kwa moyo wote, tunaonyesha tunathamini fadhili zisizostahilika za Yehova zilizo nyingi. Pia tunasaidia wanadamu wenzetu wajifaidi wenyewe na njia moja tu ambayo kwa hiyo inawezekana kwao kuja kuokoka dhiki kubwa inayokaribia sana.—Linganisha 1 Timotheo 4:15, 16.
13. (a) Katika Isaya 60:17, ni hali gani iliyotabiriwa kwa tengenezo la Yehova? (b) Ili tuione kwa ukamili, ni lazima tufanye nini? (c) Wanaofanya hivyo wana tazamio gani mbele yao?
13 Hali wanazopata katika tengenezo la Yehova zinachangamsha mioyo yao. Ni kama Yehova alivyotabiri kupitia Isaya: “Nitaweka amani iwe waangalizi wako na uadilifu uwe wagawaji-kazi wako.” (Isaya 60:17, New World Translation) Amani iliyomo si ya kuwaziwa tu bali ni uhakika, tunda la roho takatifu ya Mungu. Hiyo haimaanishi kwamba mtu anaona amani hiyo kwa ukamili kwa sababu tu anashirikiana na tengenezo. Ni lazima yeye binafsi ajifunze ‘kufuata mambo ya amani na mambo yafaayo kwa kujengana.’ (Warumi 14:19) Anahitaji kujifunza kuonyesha hekima ya kimungu kwa kushughulika na makosa ya wengine, atoe ushahidi wa ustahimilivu na kujiweza, kusamehe wengine hata kama yeye anavyotaka Mungu amsamehe. Ndiyo, ni lazima pia ‘afanye amani.’ (Yakobo 3:17, 18; Wagalatia 5:22, 23; Wakolosai 3:12-14) Wale wanaofanya hivyo wanaona furaha kubwa ya kuwa sehemu ya “taifa hodari” linalotokea sasa na lenye kujitoa kwa utumishi wa Yehova, “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11, New World Translation) Ni washiriki wa “taifa” hilo watakaohifadhiwa wakati Yehova atakapotekeleza hukumu juu ya ulimwengu mzima unaomtii Shetani kuwa mtawala.