Kuangaza Nuru Katikati ya Giza la Dunia
“Tazama, giza litaifunika dunia, na giza kuu litazifunika kabila za watu; bali [Yehova] atakuzukia wewe, na utukufu wake utaonekana juu yako.”—ISAYA 60:2.
1. Ni jibu gani la uhakika linaloweza kutolewa kwa maswali yaliyotokezwa hapa?
KWELI hizi ni siku tukufu kuishi ndani yake! ‘Siku tukufu ati?’ huenda mtu akauliza. ‘Mnawezaje kusema hivyo, na huku ulimwengu wote unagaa-gaa katika ukosefu wa umoja wa kisiasa, kiuchumi, na kidini, katikati ya giza kubwa la kizazi cha nyukilia linaloyafunika mataifa?’ Lakini hizi ni siku tukufu—kwa sababu habari njema ambazo zinatangazwa sasa katika dunia yote, zinawapa nuru ya maarifa wanadamu wenye njaa ya ukweli kuhusu maana ya nyakati zetu na taraja la furaha la siku tukufu hata zaidi ambazo huenda wakaishi wazione!
2. (a) Ni maneno gani ya kutia moyo ambayo Yehova anatoa katika Isaya sura za 45 na 60? (b) “Mwanamke” wa Mungu ni nani?
2 Chanzo cha tumaini hilo zuri ajabu si mwingine ila Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, Muumba mkuu wa mbingu na dunia. (Isaya 45:12, 18) Yeye ndiye anayetoa amri iliyoandikwa katika Isaya sura ya 60, mstari wa 1: “Ondoka, [Ee mwanamke], uangaze; kwa kuwa nuru yako imekuja, na utukufu wa [Yehova] umekuzukia.” Ni nani “mwanamke” huyu? Yeye si mwanamke wa kimwili anayetetea uhuru wa wanawake. Badala yake, yeye ni tengenezo la kimbingu la Mungu lenye nguvu, lenye kusonga mbele. Yeye ni mwenzi aliyejitoa, na msaidizi wa Yehova Mungu, ambaye washiriki wake ni maelfu ya malaika washikamanifu na sasa wakiwa ni pamoja na “watakatifu” waliofufuliwa—wale ambao wamejithibitisha waaminifu mpaka kifo wakiwa Wakristo wapakwa mafuta hapa duniani.—Ufunuo 11:18; 2:10.
3. Mwanamke wa Mungu (a) ‘ameondokaje,’ na (b) ‘ameangazaje’?
3 ‘Ondoka, Ee mwanamke,’ anaamuru Yehova. Kwa kutii, tengenezo la kimbingu la Mungu limeondoka katika hali ya utasa, ya kutokuwa mtendaji kwa karne nyingi, likaja kwenye hali ya uzaaji wenye matunda. Mwaka wa 1914 mwanamke huyo alizaa Ufalme wa Kimasihi. (Ufunuo 12:1-5) Kuanzia mwaka wa 1919, ameingiza wanaye wapakwa mafuta walio duniani katika “nchi,” au hali ya ufanisi mtukufu wa kiroho. (Isaya 66:8) Zaidi ya hayo, tengenezo la kimbingu la Mungu ‘limeangaza’ nuru juu ya unabii mbalimbali wa Ufalme ulio mzuri sana. Wanaye wengi ‘wanafundishwa na Yehova.’—Isaya 54:1, 13.
Nuru Katikati ya Giza Kubwa
4. Yehova anasema juu ya tofauti gani kati ya watu wa Mungu na mataifa ya dunia?
4 “Nuru yako imekuja,” anatangaza Yehova. Kweli, ‘utukufu wa Yehova wenyewe umezuka’ juu ya tengenezo lake, nao umeonyeshwa kwa njia nzuri sana kwa watu wa Yehova waliorudishwa ambao wapo duniani. Lakini, kisha Yehova anaelekeza kwenye hali tofauti akisema: “Tazama, giza litaifunika dunia, na giza kuu litazifunika kabila za watu.” (Isaya 60:2) Je! hayo hayaelezi vizuri zilivyo hali za dunia yote tangu mwaka wa 1914?
5. Ni kwa sababu gani dini ya uwongo haiwezi kuona utatuzi wa matatizo ya kizazi cha nyukilia?
5 Jumuiya ya Wakristo hasa imeikataa ‘ishara ya kiunabii ya kuwapo kwa Yesu na ya umalizio wa mfumo wa mambo.’ Kwa hiyo, inajikwaa-kwaa katika giza la kiroho linalozidi kuwa zito. Dini za Jumuiya ya Wakristo zimejithibitisha kuwa zinashikamana kabisa na milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, Babuloni Mkuu—ambayo iko mbali-i-i na nuru ya ukweli. (Mathayo 24:3-14; Ufunuo 17:3-6) Dini ya kilimwengu haijatoa jibu lo lote kwa matatizo ya kizazi hiki cha nyukilia, wala haiwezi kufukuza giza kubwa, ukosefu wa tumaini wenye kutia wasiwasi sana, ambao umekalia watu. Kujiingiza kwa dini ya uwongo katika mambo ya mataifa ya kisiasa kutaiongoza hatimaye kwenye uharibifu.—Ufunuo 17:16, 17.
6, 7. (a) Utukufu wa Yehova ‘uliangazaje’ wakati wa miaka ya 1919-31? (b) Ulifikia upeo gani mwaka wa 1931?
6 Tofauti na hilo, Yehova anaendelea kusema juu ya tengenezo lake la kimbingu hivi: “[Yehova] atakuzukia wewe, na utukufu wake utaonekana juu yako.” (Isaya 60:2) Utukufu huo unamulikwa kwa Wakristo wapakwa mafuta hapa duniani, ili nao ‘waangaze nuru yao mbele ya watu.’ (Mathayo 5:16) Miaka 1919 mpaka 1931 ilikuwa miaka mitukufu ya kung’aa kwa nuru ya Ufalme, na hapo watu wa Yehova walitupa mbali kabisa zile pingu zilizobaki za mafundisho, mawazo na desturi za Kibabuloni. Wakati wa miaka hiyo, ndipo mabaki hayo madogo ya Wakristo wa kweli yalianza kutoa jibu la uhakika kwa swali “NI NANI ATAKAYEHESHIMU YEHOVA?”—hicho kikiwa ndicho kichwa cha makala ya funzo katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1926.
7 Halafu, katika mwaka wa 1931, utukufu wa Yehova ukaanza kuonekana kwa ukamili zaidi juu ya “mtumishi” wake, kwa maana walilikubali jina ambalo yeye mwenyewe amewapa—MASHAHIDI WA YEHOVA. (Isaya 43:10, 12) Wakati wa miaka 12 yenye mazao mengi na yenye kivumbi mpaka mwaka wa 1931, watangazaji wa Ufalme waliongezeka kutoka makumi machache tu wakafikia maelfu ya mashahidi wenye bidii.
‘Kuangaza’ Zaidi
8, 9. (a) Mwaka wa 1931, Mnara wa Mlinzi ulielekeza fikira kwenye kikundi gani kingine? (b) Kulingana na Maandiko, wao ‘wanatiwa alama’ jinsi gani?
8 Lakini, je, Yehova ‘angeangazia’ wapakwa mafuta wa “kundi dogo” peke yao? (Luka 12:32) Hapana, kwa maana miaka ya 1931 hadi 1938 ilithibitika kuwa kipindi kizuri sana cha uangazaji zaidi, kwa kuwa Mnara wa Mlinzi ulianza kuelekeza fikira waziwazi kwenye kikundi kingine. Makala ya funzo katika toleo lake la Septemba 1, 1931, ilikuwa na kichwa “MTU MWENYE KIDAU CHA WINO,” msingi wake ukiwa ni Ezekieli 9:1-11. Baada ya kutambulisha “mtu” huyo kuwa mabaki wapakwa mafuta, Mnara wa Mlinzi ulieleza hivi:
9 “Amri inatolewa ya ‘kutia alama juu ya vipaji vya nyuso za watu wanaougua na kulia kwa ajili ya machukizo yote yanayofanywa katikati’ ya Jumuiya ya Wakristo. . . . Bwana anaeleza juu ya jamii ya watu ambao ‘atawaokoa wakati wa taabu na kuwahifadhi hai na kuwabariki duniani.’ (Zab. 41:1, 2) Lazima hiyo iwe jamii ya watu ambao mara nyingi inaelezwa kuwa ‘mamilioni wanaoishi sasa ambao hawatakufa kamwe.’” Leo, inasisimua kuona kwa uhalisi mamilioni yao wakitiwa alama ya kuhifadhiwa, wanapovaa utU wa Ukristo wa kweli, wakiwa katika uhusiano wa kuwa wakfu kwa Yehova kupitia Kristo Yesu.—Mwanzo 22:15-18; Sefania 2:1-3; Waefeso 4:24.
10, 11. (a) Yehu alimfananishaje Yesu? (b) Mtambulishe “Yonadabu” wa kisasa.
10 Zinazopasa kuangaliwa hasa ni makala za funzo katika matoleo ya Mnara wa Mlinzi ya Julai 1 hadi Agosti 1, 1932. Zikisema juu ya Wafalme wa Pili sura za 9 na 10, makala hizo zilionyesha jinsi Mfalme Yehu alivyofananisha Mtekelezaji-Hukumu wa Yehova, Mfalme Yesu Kristo, anayewakilishwa duniani na mabaki wapakwa mafuta, ambao wanawaonya wengine juu ya utekelezaji wa hukumu ya Yehova inayokuja. Lakini ni nani aliyefananishwa na mwenzi wa Yehu, Yonadabu? Mnara wa Mlinzi ulijibu hivi:
11 “Yonadabu aliwakilisha au alifananisha jamii ile ya watu waliopo duniani sasa wakati ambao kazi ya Yehu inaendelea watu ambao . . . hawana upatano na tengenezo la Shetani, wanaochukua msimamo wao upande wa uadilifu, na ndio ambao Bwana atawahifadhi wakati wa Har–Magedoni, awapitishe taabu hiyo, na kuwapa uzima wa milele duniani.” Kisha Mnara wa Mlinzi ulionyesha hao kuwa ndio ‘wanaobarikiwa na Baba’ katika mfano wa Yesu wa ‘kondoo na mbuzi.’ (Mathayo 25:31-46) Ulisema hivi: “Hao ndio wanaofanyiza jamii ya ‘kondoo’ ambao wanapendelea watu wa Mungu waliopakwa mafuta, kwa sababu wanajua kwamba wapakwa mafuta wa Bwana wanafanya kazi ya Bwana.”
12. Ni ufunuo gani wenye kusisimua wa ukweli wa kimungu uliotolewa mwaka wa 1935?
12 Mimuliko hiyo ya nuru ya kiunabii iliwekea msingi hotuba ile inayojulikana sana juu ya “Ule Umati Mkubwa,” iliyotolewa Mei 31, 1935, na msimamizi wa Sosaiti Yetu, J. F. Rutherford, kwenye kusanyiko la Mashahidi wa Yehova la Washington, D.C. Lo, huo ulikuwa ufunuo wa ukweli wa kimungu ulio mzuri kama nini! Uthibitisho wenye kukata maneno ulitolewa wakati huo, ukatambulisha “mkutano mkubwa” wa Ufunuo 7:9 kuwa unahusiana na “kondoo wengine” wa Yohana 10:16, kuhusiana na jamii ya Yonadabu, na wale waliotiwa alama katika kipaji cha uso ili kuokoka, na mamilioni wanaoishi sasa ambao hawatakufa kamwe, na “kondoo” wanaotenganishwa na “mbuzi” ili warithi uzima wa milele katika makao ya Ufalme hapa duniani. Yote hayo yalizungumzwa katika Mnara wa Mlinzi, Agosti 1 na 15, 1935.
13. Ni dokezo gani jingine lililotolewa mwaka wa 1938?
13 Katika miaka iliyofuata, tengenezo la Mungu liliendelea kuelekeza fikira nyingi kwenye “mkutano mkubwa” na tumaini lao kuu la kuokoka waingie katika Paradiso itakayorudishwa duniani. Mashahidi wa Yehova walikutanika katika kusanyiko huko London, Uingereza, katika Septemba 9-11, 1938. Na huko hotuba mbili kuu zilipitishwa kwa kamba ya simu ya moja kwa moja mpaka kwenye makusanyiko mengine kuzunguka ulimwengu. Kwa kutegemea amri zilizotangulia ambazo wanadamu walipewa, moja ya hotuba hizo yenye kichwa “Jazeni Dunia,” ilidokeza kwamba “Wayonadabu” wenye kuokoka “dhiki kubwa” huenda, angalau, kwa wakati fulani, wakafunga ndoa na kuzaa watoto katika Utaratibu Mpya baada ya Har–Magedoni.—Mwanzo 1:28; 9:1, 7; ona Mnara wa Mlinzi, Oktoba 15 na Novemba 1, 1938.
14. Yehova aliwafanikishaje watu wake wakati wa miaka hiyo?
14 Wakati wa miaka hiyo, Bwana Yesu Kristo alikusanya na kupeleka wafanyi kazi zaidi. Kwa hiyo wahubiri shambani wakaongezeka kufikia karibu 50,000 mwaka wa 1938.—Mathayo 9:37, 38.
“Wafalme” na “Mataifa”
15, 16. “Wafalme” walishirikije katika utimizo wa Isaya 60:3-10 (a) katika nyakati za kale, na (b) katika nyakati za kisasa? (c) “Wageni” wanatumikaje sasa pamoja na “wafalme” hao?
15 Kazi hiyo ya kukusanya inaelezwa kwa njia ya kupendeza katika Isaya sura ya 60, mistari ya 3 hadi 10. Hapo Yehova anasema juu ya “wafalme” wanaoonekana kuhusiana na ‘kuangaza’ kwa Sayuni na wanaohudumia tengenezo hilo lililo mfano wa mke. Watu wa Mungu wa nyakati za kale waliporudi kutoka utumwa wa Babuloni, Mfalme Dario Mmedi na Mfalme Koreshi (Sairasi) wa Uajemi waliongoza katika kutoa uandalizi wa kurudisha ibada ya Yehova katika Yerusalemu. (Danieli 5:30, 31; 9:1; Ezra 1:1-3) Katika hilo, wanafananisha kwa kufaa Mfalme Mwenye Nguvu Zote, Yehova, na Mfalme mwenzi wake, Yesu, ambao wameongoza kurudishwa kwa ibada ya kweli kati ya watu wa Yehova wa kisasa. (Ufunuo 11:15, 17) Zaidi ya hayo, mabaki ya wapakwa mafuta wa waabudu wa kweli—wanaotarajia kuwa “wafalme,” ‘warithi pamoja na Kristo’—wamekuwa wakiongoza katika kazi ya kisasa ya kutoa ushahidi. Wanaotumikia pamoja nao ni “wageni”—wale ambao si wa Israeli wa kiroho, lakini ambao watakuwa raia wa kidunia wa Ufalme na ambao hata sasa wanashiriki katika utendaji wa kujenga wa kitheokrasi duniani pote.—Warumi 8:17; linganisha Isaya 61:5, 6.
16 Yehova mwenyewe anatualika hivi: “Inua macho yako, utazame pande zote!” Warithi wa Ufalme waliokusanywa sasa wanaungwa na ule “mkutano mkubwa . . . [wa] watu wa kila taifa”! (Ufunuo 7:9; Zekaria 8:23; Isaya 2:2, 3) ‘Wanatangaza sifa za Yehova,’ katika huduma ya bidii. Pia wanajitumikisha wenyewe katika shughuli kama za kujenga Majumba ya Ufalme kwa ajili ya ibada—mengine kati yayo yakiwa yanajengwa kwa siku mbili tu. ‘Wanatumikia’ (‘wanahudumu,’ NW) kwa kuunga mkono kwa moyo wote upanuzi wa duniani pote wa faida za Ufalme.—Isaya 60:4-7.
17, 18. (a) Kwa furaha, ni ‘urukaji’ gani wenye kusisimua unaoendelea sasa? (b) Tukio linalotokea majira fulani katika Palestina linaonyeshaje kwa kufaa ‘urukaji’ huo?
17 Kisha Yehova anauliza swali hili linalofaa: “Ni nani hawa warukao kama wingu, na kama njiwa waendao madirishani kwao [kama njiwa kwenye matundu ya nyumba ya ndege, NW]?” Wa kwanza kuja kwenye tengenezo la Mungu ni ‘wana wake kutoka mbali,’ wakijitenga kabisa na dini yote ya Kibabuloni. Wapakwa mafuta hao wanaleta vitu vya thamani, wakiweka wakfu vitu vyao vyote kwa ajili ya ‘jina la Yehova,’ Mungu wao. Akiwa “Mtakatifu wa Israeli,” ameweka jina lake juu yao na kuwapamba na pendeleo la kumtumikia wakiwa mashahidi wake. Wanaongoza katika kulitukuza jina la Bwana wao Mwenye Enzi Kuu, Yehova, kuwa ndilo kuu zaidi, lenye fahari zaidi, lenye utukufu zaidi katika ulimwengu wote.—Isaya 60:8, 9.
18 Kwa furaha, mabaki wapakwa mafuta hawajawa peke yao katika kufanya hivyo. Ingekuwa vigumu sana kama wangalikuwa peke yao! Kikundi hicho kinachozeeka kinaendelea kupungua zaidi, wakati wanapomaliza mmoja mmoja mwendo wao wa kidunia kwa ukamilifu. Wanabaki 9,000 hivi. Lakini wengine, wanaofikia hesabu ya mamilioni, wanamiminika kama njiwa kwenye “matundu ya nyumba ya ndege,” na kupata kimbilio katika tengenezo la Mungu. (NW) Wao ni kama makundi ya njiwa wanaoonekana katika Palestina wakati wa majira fulani—wakiruka kama wingu, wakiwa wengi mno mpaka wanatia anga giza kwa uhalisi.
‘Malango Yaliyo Wazi Kabisa’
19. Ni kwa nini “malango” ya tengenezo la Yehova yanabaki yakiwa wazi, na “wafalme” na “wageni” wanaitikiaje?
19 Kwa rehema, Yehova amefungua wazi kabisa malango ya tengenezo lake, ambalo sasa analiambia hivi: “Malango yako nayo yatakuwa wazi daima; hayatafungwa mchana wala usiku; ili watu wapate kukuletea utajiri wa mataifa.” Ndivyo ilivyo wakati huu “mkutano mkubwa” unapoendelea kuongezeka. Kwa furaha, “wageni” hao wanatoa wakati wao, nguvu na uwezo katika “utumishi mtakatifu mchana na usiku” (NW). Wanautumia “mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji” na kushiriki pamoja na wanaotarajia kuwa wafalme katika kuliletea jina la Yehova sifa yenye kulirembesha.—Isaya 60:10, 11; Ufunuo 7:4, 9, 15; 1 Wakorintho 16:9, NW.
20. (a) Ni nani ‘wataangamizwa’? (b) Tunaona utofautiano gani wa kufurahisha hapa?
20 Kisha, Yehova anasema na tengenezo lake, akisema: “Kila taifa na ufalme wa watu wasiotaka kukutumikia wataangamia; naam, mataifa hayo wataharibiwa kabisa.” Mataifa hayo ya kilimwengu yenye kiburi, na wapinzani wengine watanyenyekezwa kwenye Har–Magedoni. Tofauti na hivyo, Yehova anaremba patakatifu pake pa ibada. ‘Anapatukuza mahali penyewe pa miguu yake,’ zile nyua za kidunia za hekalu lake kuu la kiroho la ibada, na anafanya hivyo kwa kukusanya hesabu zinazoongezeka za mkutano mkubwa. Kupitia nabii mwingine, Yehova anatangaza hivi: “Nami nitatikisa mataifa yote, na vitu vinavyotamaniwa [vya] mataifa yote vitakuja; nami nitaijaza nyumba hii utukufu.” (Hagai 2:7) Lakini watesi, waasi-imani na wengine watakata tamaa kwa kulazimika kukubali kwamba kweli tengenezo la Mungu linawakilishwa kweli kweli na Mashahidi wa Yehova—‘mji wa Yehova, Sayuni wa Mtakatifu wa Israeli.’—Isaya 60:12-14.
21, 22. Yehova anarudia kutoa uhakikisho gani hapa? (b) Ni kwa njia gani, kama inavyofananishwa, watu wake ‘wananyonya maziwa ya mataifa’? (c) Ni funzo gani zaidi lenye kusisimua linalotungojea?
21 Yehova hatamwacha kamwe msaidizi wake aliye kama mke hata wapinzani wadhihaki kwa kadiri gani ‘wanaye na bintize’ hapa duniani. Badala yake, analiambia hivi tengenezo lake lenye ushikamanifu: “Nitakufanya kuwa fahari ya milele, furaha ya vizazi vingi. Utanyonya maziwa ya mataifa.” Kwa njia ya mfano wawakilishi wa kidunia wa tengenezo la Mungu wanatumia hivyo vitu vyote vinavyopatikana ili kuendeleza ibada ya kweli. Wanatumia kwa njia nzuri vifaa vya kisasa vya upashanaji wa habari, usafiri, na uchapaji ili kuzihubirisha habari njema. Ulinzi na uongozi wa Yehova vimekuwa na Mashahidi wa Yehova katika kazi hiyo. Wao, pia, wakitumikia kwa ajili ya tengenezo la Yehova la kimbingu, wanafurahia utimizo wa ahadi hii: “Nawe utajua ya kuwa mimi, [Yehova], ni mwokozi wako, na mkombozi wako, Mwenye enzi wa Yakobo.”—Isaya 60:15, 16.
22 Yehova anatupa kitia-moyo zaidi gani katika Isaya 60:17-22? Hayo ndiyo yatakayokuwa mazungumzo yenye kusisimua ya funzo letu lijalo.
Maswali ya Muhtasari
◻ Kuna utofautiano gani kati ya nuru na giza leo?
◻ Kulikuwako ‘nuru’ gani yenye kuendelea wakati wa miaka ya 1919-38?
◻ Andiko la Isaya 60:8 linatimizwaje katika nyakati za kisasa?
◻ “Wafalme” na “wageni” wanaingiaje katika ‘malango yaliyo wazi kabisa’?
[Sanduku katika ukurasa wa 9]
“Silaha za maangamizi yenye kutia hofu zinarundikwa kwa mwendo wenye kuongezeka. . . . Mashindano ya uundaji wa silaha leo yanafika mpaka kwenye bahari za ulimwengu na anga za juu. Kwa kweli inashangaza kwamba urundikaji wa silaha ni mojapo shughuli zenye kupanuka katika kipindi cha haribiko la uchumi na matazamio mabaya.”—Katibu Mkuu wa UM, Bwa. Javier Perez de Cuellar
“Pale, chini ya mlango nyumbani siku ile nyingine, ulikuwako ujumbe unaofahamika sana ukiwa ni kikaratasi cha kidini. ‘Je! tunakaribia Har–Magedoni?’ yalikuwa maneno yenye rangi nzito yaliyo juu ya anga lenye kushuka na umeme wa mvua wenye kupinda-pinda ukija kutupiga sisi. Kuna wakati ambao ujumbe wa namna hiyo ungetokeza tabasamu za kudhihaki. Kwa ghafula, halionekani kuwa jambo la kuchekesha tena.”—Haynes Johnson, The Washington Post