Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • su sura 22 kur. 167-174
  • Usitamani Kilichoachwa Nyuma!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Usitamani Kilichoachwa Nyuma!
  • Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “YAAKAANDIKWA ILI KUTUONYA SISI”
  • ‘KUTAMANI NCHI ILIYO BORA’
  • Wingu Kubwa Sana la Mashahidi!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Mambo Makuu Kutoka Kitabu cha Mwanzo—II
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Je, Una Imani Kama ya Abrahamu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Kujitahidi Kuufikia Ufalme
    “Ufalme Wako Uje”
Pata Habari Zaidi
Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
su sura 22 kur. 167-174

Sura 22

Usitamani Kilichoachwa Nyuma!

1. (a) Watumishi wa Mungu wana baraka gani mbele karibuni sana? (b) Hata hivyo, watu fulani wamefanya nini?

UTIMIZO wa unabii wa Biblia pasipo kukosea unaonyesha kwamba sisi leo tupo penye lango lenyewe la kuingia katika mfumo mpya wa mambo yenye utukufu. Karibuni ulimwengu mbovu utakuwa umeenda zake, pamoja na masikitiko ya moyo, vipingamizi na huzuni ambazo umesababisha. Dunia itageuzwa iwe Paradiso ambamo waabudu wa Mungu wa kweli wataweza kufurahia milele uzima mkamilifu wa kibinadamu. Kwa habari ya uhakika wa ahadi zake juu ya mambo hayo, Yehova alimwambia mtume Yohana hivi: “Andika ya kwamba maneno hayo ni amini na kweli.” (Ufunuo 21:1-5) Hata hivyo, ingawa huenda likaonekana kuwa jambo geni, watu fulani wanaozijua kweli hizo wanageuka na kwenda kwenye namna ya maisha ya ulimwengu ambao Mungu anasema atauangamiza. Sikitiko wee! Kwa nini wanafanya hivyo?

2. (a) Ili mtu aepuke matokeo hayo, imempasa afanye nini baada ya kujifunza ukweli mara ya kwanza? (b) Akishindwa kufanya hivyo, huenda kufikiri kwake kukaongozwa na nini, na matokeo yawe nini?

2 Waliposikia mara ya kwanza habari njema juu ya Ufalme wa Mungu na utakayofanya, walizipokea kwa moyo wa furaha. Lakini ni jambo la maana pia mtu kusonga mbele kufikia kukomaa kwa Kikristo, kuongeza kina cha ufahamu wa Neno la Mungu na kutafuta njia za kulifuata kikamili katika maisha yake. (Waebrania 6:1, 11, 12) Ikiwa ukosefu wa kuthamini unamfanya mtu ye yote apuuze hilo, hataendelea kuyaona mapendeleo ya kumtumikia Mungu kuwa yenye bei sana. Huenda mtu kama huyo akakosa saburi ya baraka halisi ambazo Mungu ameahidi, huku akishindwa kuthamini uhitaji wake wa ukuzi wa kiroho na umaana wa kushiriki sana kadiri iwezekanavyo kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi ambayo Mungu ametupa tuifanye sasa. Huenda kutosheleza tamaa ya mali za kimwili na kinachoonekana kuwa raha kukaanza kuchukua wakati wake zaidi na zaidi. Kisha anaweka mapendezi ya kiroho mahali pa pili. Yote hayo hayatukii mara moja, bali kidogo kidogo, huyo anarudi nyuma kuingia katika ulimwengu.—1 Timotheo 6:9, 10.

3. (a) Kwa nini ni hatari kuchagua watu wasiomwabudu Yehova wawe rafiki? (b) Ni wakati gani ambao huenda mtu akajikuta kwa urahisi yu katika ushirika uliolegezwa pamoja na watu hao?

3 Huenda mtu akasema kwamba anataka kuja kuokoka kuingia katika “dunia mpya,” ili aishi katika ulimwengu ambamo uadilifu unakaa. Lakini uchaguzi wake wa watu wa kushirikiana nao unathibitisha anayosema? Bila shaka, hatuwezi kukosa kukutana kila siku na watu wasiomtumikia Yehova—kazini, shuleni, tunaponunua vitu dukani, hata nyumbani. Lakini wakati wa saa za kupumzika kazini, kabla na baada ya kwenda shuleni, wakati wa kupiga simu au kutembelea rafiki, katika nyakati za tafrija, ni ushirika gani ambao yeye anachagua? Je! inafanya tofauti kweli kweli? Biblia inaonya hivi: “Msipotezwe. Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.” (1 Wakorintho 15:33, New World Translation) Lakini “mashirika mabaya” ni nini? Je! inafanya tofauti yo yote kama watu fulani hawamwabudu Yehova, wanafanya tu yanayoonekana yanafaa machoni pao wenyewe? Kwa kutegemea yale tuliyokwisha kujifunza, sisi twajua kwamba watu wa namna hiyo hawataokoka waingie katika “dunia mpya.” Watu wo wote wanaopunguza umaana wa viwango vya Yehova wanapochagua rafiki upesi watajikuta wamerudi katika ulimwengu ambao wakati mmoja walifikiri walikuwa wakiuacha nyuma. Lakini mifano yenye kuonya iliyoandikwa katika Maandiko inaweza kutulinda tusifuate mwendo huo ikiwa tunaizingatia moyoni.—1 Wakorintho 10:11.

“YAAKAANDIKWA ILI KUTUONYA SISI”

4. (a) Waisraeli walikuwa na maisha ya aina gani katika Misri baada ya kufa kwa Yosefu? (b) Kwa nini “kundi kubwa lililochangamana” lilijiunga na Israeli walipokombolewa katika Misri? (c) Mwigo huo umetimizwaje wakati wetu?

4 Yehova alipokomboa Waisraeli katika utumwa wa Misri, hiyo ilikuwa faraja kwao kama nini! Haikosi kuwa. Ule uonevu wenye ukatili waliokuwa wamepata baada ya kufa kwa Yosefu ulifanya Misri iwe kama tanuri yenye moto walimokuwa wametupiwa. (Kutoka 1:13, 14; Kumbukumbu la Torati 4:20) Lakini ndipo Yehova akaleta mapigo kumi juu ya Misri. Tofauti kati ya Mungu wa kweli na ile miungu ya Misri ikawa wazi. Basi, Waisraeli walipoiacha nchi hiyo, “kundi kubwa la watu waliochangamana” la wasio Waisraeli likaenda pamoja nao, kama vile leo “mkutano mkubwa” unavyojitenga na ulimwengu na unashirikiana na mabaki ya Israeli wa kiroho. (Kutoka 12:38) Lakini ikawaje kambini mara walipotoka Misri?

5. (a) Muda mfupi baada ya kukombolewa kwao, ‘walirudije Misri’? (b) Kwa nini ikawa hivyo?

5 Stefano, mwanafunzi Mkristo anaeleza hivi: “Kwa mioyo yao wakarejea Misri.” Hilo lilitukia miezi michache tu baada ya kukombolewa kwao. (Matendo 7:39, 40) Ni nini kilichotoa ushahidi wa hilo? Walifanya ndama wa dhahabu—kitu walichokuwa wamezoea katika Misri—kisha wakatangaza ati walikuwa wakiwa na “sikukuu kwa [Yehova].” Kumbe walikuwa wakifuata mfano wa Wamisri. (Kutoka 32:1-6) Yehova aliwakasirikia vikali. Mwenendo wao ulipingana moja kwa moja na ile Sheria iliyotolewa kwenye Mlima Sinai. Maelfu wakapoteza uhai wao. Kwa nini jambo hilo lilitukia? Ijapokuwa walijua amri za Yehova, kwa wazi hawakuwa wameimarisha moyoni hali ya kuzithamini amri hizo na pia kuthamini uhakika wa kwamba Mungu wa kweli ndiye alikuwa akiwaongoza.

6. (a) Yehova aliwafanyia maandalizi gani jangwani? (1 Wakorintho 10:3, 4) (b) Kwa nini baadhi yao walianza kutamani mambo waliyokuwa wakipata huko Misri?

6 Walipoondoka Misri, Waisraeli na pia ‘kundi lenye kuchangamana’ lililoenda pamoja nao walijua lililokuwa jambo jema la kufanya. Lakini baada ya mwaka mmoja kupita, bado hawakuwa katika Nchi ya Ahadi; bado hawakuwa na nyumba katika “nchi yenye wingi wa maziwa na asali.” Wote walikuwa na chakula cha kimwili cha kutosha, na hasa kulikuwako chakula cha kiroho kwa wingi. Ile nguzo ya wingu na ya moto iliwapa ushahidi wa kila siku kwamba Yehova alikuwa akiwaongoza. Kwenye Bahari Nyekundu na kwenye Mlima Sinai walikuwa wameona ushahidi wenye kutia woga wa kimungu juu ya uwezo wa Yehova. Lile agano la Torati liliwapa chakula na kiburudisho cha kiroho. Liliwapa pia mengi ya kufanya kibinafsi, likiwaonyesha mahali walipohitaji kurekebisha mwenendo wao, kufikiri kwao, nia zao, ili hayo yawe yenye kumpendeza Yehova. Lakini badala ya kuthamini yote ambayo Yehova alikuwa akiwafanyia, walianza kutamani vitu vya kimwili walivyokuwa navyo Misri. Tamaa yenye choyo ikaongoza wengi kwenye uangamivu.—Hesabu 11:4-6, 31-34.

7. (a) Wapelelezi waliporudisha ripoti zao, kwa nini watu walisema juu ya kurudi Misri? (b) Matokeo yakawa nini? (Waebrania 3:17, 19)

7 Muda mfupi baada ya hayo, Musa akawatuma wanaume wakapeleleze Nchi ya Ahadi. Waliporudi wote wakakubali kwamba ilikuwa “yenye wingi wa maziwa na asali” kweli kweli. Lakini kumi kati ya wapelelezi hao waliogopa watu wa huko, wakaogopeshwa na miji yao yenye maboma. Hawakumtegemea Yehova kwa moyo wao wote, wakafanya mioyo ya wengine iteteme kwa woga. Tena mawazo yao yakarudi Misri, wakasema juu ya mipango ya kurudi huko. Kwa sababu ya ukosefu wao wa imani, kizazi kizima cha wenye umri wa miaka 20 na zaidi mwishowe kikafa jangwani, kisiingie kamwe Nchi ya Ahadi.—Hesabu 13:27-33; 14:1-4, 29.

8. (a) Ili Loti na jamaa yake waokolewe wakati Sodoma ulipoangamizwa, iliwapasa kufanya nini? (b) Kwa nini mke wa Loti aligeuzwa akawa nguzo ya chumvi? (c) Hilo lina ujumbe gani wenye kutuonya sisi?

8 Muda wa zaidi ya miaka 400 iliyotangulia, somo ilo hilo lilikaziwa katika hali tofauti. Loti, mpwa wa Abrahamu alikuwa ameenda kuishi katika Sodoma, mji wenye adili mbaya lakini wenye ufanisi wa mali. Ukosefu wa adili ulikuwa mbaya sana katika Sodoma na wilaya zake hata Yehova akaazimu kuuangamiza, usipate kujengwa tena hata! Malaika walitumwa wakamwokoe Loti na nyumba yake. Loti alipoonya wale waliotazamiwa kuoa binti zake, machoni pao “akawa kama achezaye.” Lakini hakuwa akicheza. Kulipopambazuka malaika wakamtoa Loti na jamaa yake haraka nje ya mji na kuwaambia wakimbie bila kutazama nyuma. Maisha zao zilitegemea utii. Loti na binti zake wawili wakafanya waliyoambiwa, wakaokoka. Lakini kwa wazi mke wa Loti hakutaka kuachana na vitu vya kimwili walivyokuwa wakiviacha nyuma. Alipogeuka atazame nyuma, akapoteza uhai wake, akawa nguzo ya chumvi. Je! sisi binafsi tumezingatia moyoni kinachomaanishwa na hilo? Ili tusikose maana yake, Yesu alilitia katika onyo lenye kuhusu haraka ya kukimbia kutoka katika huu mfumo wa kale katika wakati wetu. Ni wakati alikuwa akionya juu ya kutosumbukia mno mali za kimwili aliposema kifupi hivi: “Kumbukeni muke wa Loti.” (Mwanzo 19:12-26, Union Version; Luka 17:31, 32, Zaïre Swahili Bible) Ni nini kinachoweza kutulinda tusitumbukie ndani ya mitego iliyonasa Waisraeli na mke wa Loti?

‘KUTAMANI NCHI ILIYO BORA’

9. Imani ni nini, na tunaweza kuisitawishaje?

9 Ili tuepuke kuvutwa tutazame nyuma, tunahitaji kusitawisha imani yenye kuongezeka katika yale yaliyoko mbele. Waebrania 11:1, New World Translation, hufasili imani kuwa “taraja lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, wonyesho dhahiri wa mambo ya hakika ijapokuwa hayajaonwa.” Ni uhakikisho, kama hati ya uwenyeji, ya kwamba tutapata kile ambacho Mungu ameahidi. Imani inategemea ushahidi wenye nguvu, na kwa hiyo tuna sababu zenye nguvu za kuamini yale yasiyoweza kuonwa kwa jicho la kimwili. Si kukubali jambo upesi-pesi, au wepesi wa kusadiki kwa sababu jambo fulani linasikika kuwa zuri. Ili tuwe na imani ya kweli, ni lazima tujali sana ili sisi binafsi tupate kuujua sana ushahidi ulio msingi wake. Pia tunahitaji kufikiria kwa uangalifu jinsi yale tunayojifunza yanavyohusu maisha zetu wenyewe na kusitawisha hali ya kuyathamini kutoka moyoni.

10. (a) Abrahamu alitoaje ushahidi wa imani yake, na kwa muda gani? (b) Twajuaje kwamba alilofanya lilikuwa sahihi?

10 Abrahamu alikuwa na imani kama hiyo. Kwa sababu hiyo, Abrahamu alipoelekezwa na Yehova aliacha nyuma mji wenye ufanisi wa Uru katika Kaldea (Ukaldayo), akahamia mbali Kanaani, nchi ambayo hakuwa ametangulia kuiona hata kidogo. Ili kujisalimisha, akaishi huko akiwa mkazi wa kigeni, bila kujishikamanisha mwenyewe na wo wote wa miji yenye ufalme. “Alikuwa akiutazamia mji wenye misingi [Ufalme wa Kimasihi wa Yehova], ambao mwenye kuubuni na kuujenga ni Mungu.” Kama angaliendelea kuyatamani maisha katika Kaldea, bila shaka angalirudi. Badala ya kufanya hivyo, yeye alikuwa ‘akiitamani nchi iliyo bora, yaani, ya mbinguni.’ (Waebrania 11:8-16) Abrahamu hakutamani hiyo “nchi iliyo bora” kwa miaka michache tu, wala hata kwa miaka kumi wala ishirini. Yeye aliendelea kufanya hivyo mpaka kufa kwake, miaka 100 au zaidi baada ya kuondoka Uru. Yeye hakusema tu alikuwa na imani; aliionyesha kwa kazi zake. Kwa sababu hiyo amehakikishiwa kuja kupata thawabu. Tazamio la kufufuliwa kwake ni la hakika sana, kama Yesu alivyosema, ‘kwa Mungu, Abrahamu anaishi.’—Luka 20:37, 38; Yakobo 2:18.

11. Isaka na Yakobo walionyeshaje kwamba wao, pia, walikuwa na imani?

11 Lakini namna gani Isaka mwana wa Abrahamu, na Yakobo mwana wa Isaka? Hao hawakuwa wamepata kuonja namna ya maisha ya Kaldea. Lakini hawakuona hilo kuwa sababu ya kutaka wakajionee wenyewe yalikuwa maisha ya namna gani. Walipojifunza kwa wazazi wao juu ya ahadi za Yehova, walizizingatia hizo moyoni. Walisitawisha imani kama ile ya Abrahamu. Wao, pia, walikuwa ‘wakiitamani nchi iliyo bora.’ Mungu hakuwaonea haya.—Waebrania 11:9, 16, 20, 21; Mwanzo 26:24, 25; 28:20-22.

12. Ni nini kilichoongoza Esau na Dina katika matatizo makubwa?

12 Kwa upande mwingine, Esau, ndugu ya Yakobo hakuthamini mambo ya kiroho. Alioa wanawake wasiokuwa waabudu wa Yehova. Badala ya kuweka mambo matakatifu kama hazina, akauza haki yake ya mzaliwa wa kwanza apate mlo mmoja tu. (Mwanzo 25:29-34; 26:34, 35; Waebrania 12:14-17) Yeye alikuwa mtu aliyetaka raha ya kimwili sasa. Dina, binti Yakobo, pia aliingia katika tatizo kubwa. Kwa nini? Kwa sababu alipenda kushirikiana na “binti za nchi” wapagani.—Mwanzo 34:1, 2.

13. (a) Hasa maisha yako namna gani kwa watu walio sehemu ya ulimwengu leo? (b) Ni nini kitakachotulinda sisi tusivutwe kurudi nyuma katika huo?

13 Ikiwa wewe, kama Abrahamu, Isaka na Yakobo ‘unaitamani nchi iliyo bora,’ kuishi chini ya Ufalme wa Kimasihi wa Yehova, usijiruhusu uvutwe kurudi katika ulimwengu. Kumbuka, ulimwengu hautoi wakati ujao wenye kudumu. “Bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.” Na hayo yatakuwa maisha yenye kuridhisha sana kama nini!—1 Yohana 2:17.

[Picha katika ukurasa wa 172]

Mkumbuke mke wa Loti!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki