Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 1/1 kur. 6-11
  • Je, Una Imani Kama ya Abrahamu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Una Imani Kama ya Abrahamu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kutii Mwelekezo wa Mungu
  • Imani Iliyo Kama ya Abrahamu Leo
  • Wenye Imani Licha ya Majaribu
  • Uvumilivu Leo
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Abrahamu Alikuwa Nani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Ibrahimu—Rafiki ya Mungu
    Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia
  • Abrahamu na Sara Walimtii Mungu
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 1/1 kur. 6-11

Je, Una Imani Kama ya Abrahamu?

“Mwana wa binadamu awasilipo, je, kwa kweli ataipata hiyo imani duniani?”—LUKA 18:8.

1. Kwa nini ni vigumu kwa mtu kudumisha imani yenye nguvu leo?

SIKU hizi, si rahisi mtu kudumisha imani yenye nguvu. Ulimwengu huwasonga Wakristo sana ili kuwakengeusha wasifikirie mambo ya kiroho. (Luka 21:34; 1 Yohana 2:15, 16) Wengi hulazimika kujitahidi sana kuendelea kuishi huku wakikabili vita, misiba, maradhi, au njaa. (Luka 21:10, 11) Katika mataifa kadhaa, kuna utamaduni wenye nguvu usio wa kidini, na wowote wanaoishi kulingana na imani yao huonwa kuwa watu wasiotumia akili, hata washupavu. Isitoshe, Wakristo wengi hunyanyaswa kwa sababu ya imani yao. (Mathayo 24:9) Swali ambalo Yesu aliuliza yapata miaka 2,000 iliyopita, bila shaka lafaa: “Mwana wa binadamu awasilipo, je, kwa kweli ataipata hiyo imani duniani?”—Luka 18:8.

2. (a) Kwa nini imani yenye nguvu ni muhimu kwa Mkristo? (b) Lingekuwa jambo lenye manufaa kuiga kielelezo cha nani cha imani?

2 Ingawa hivyo, ukweli ni kwamba, hiyo imani yenye nguvu ni muhimu ikiwa tutafanikisha maisha yetu sasa na wakati ujao kupokea uhai udumuo milele ulioahidiwa. Akinukuu maneno ya Yehova kwa Habakuki, mtume Paulo aliandika: “‘Lakini mwadilifu wangu ataishi kwa sababu ya imani,’ na, ‘ikiwa yeye ajikunyata, nafsi yangu haina upendezi katika yeye.’ . . . Bila imani haiwezekani kumpendeza [Mungu] vema.” (Waebrania 10:38–11:6; Habakuki 2:4) Paulo alimwambia Timotheo: “Pigana pigano bora la imani, pata mshiko imara juu ya uhai udumuo milele ambao uliitiwa.” (1 Timotheo 6:12) Basi, inawezekanaje kuwa na imani isiyovunjika? Tunapofikiria swali hilo, lingekuwa jambo lenye manufaa kuchunguza mwanamume aliyeishi miaka ipatayo 4,000 iliyopita, na bado imani yake yastahiwa sana katika dini tatu kubwa—Uislamu, Dini ya Kiyahudi, na Ukristo. Mwanamume huyo ni Abrahamu. Kwa nini imani yake ilikuwa yenye kutokeza hivyo? Je, leo twaweza kumwiga?

Kutii Mwelekezo wa Mungu

3, 4. Kwa nini Tera alihamisha familia yake kutoka Uru kwenda Harani?

3 Abrahamu (ambaye mwanzoni aliitwa Abramu) atajwa kwa mara ya kwanza, mapema sana katika Biblia. Katika Mwanzo 11:26, twasoma: “Tera . . . akamzaa Abramu, na Nahori na Harani.” Tera na familia yake waliishi Uru wa Wakaldayo, jiji lenye usitawi kusini mwa Mesopotamia. Hata hivyo, hawakukaa huko. “Tera alimtwaa Abramu mwanawe, na Lutu [Loti] mwana wa Harani, mwana wa mwanawe, na Sarai [Sara] mkwewe, mke wa Abramu mwanawe, wakatoka wote katika Uru wa Wakaldayo, waende nchi ya Kanaani, wakafika mpaka Harani wakakaa huko.” (Mwanzo 11:31) Nahori, ndugu yake Abrahamu, pia alihamisha familia yake kwenda Harani. (Mwanzo 24:10, 15; 28:1, 2; 29:4) Ingawa hivyo, kwa nini Tera alihama kutoka Uru, jiji lenye usitawi kwenda Harani, jiji lililokuwa mbali?

4 Miaka ipatayo 2,000 baada ya wakati wa Abrahamu, mwanamume mwaminifu Stefano alieleza kuhusu kuhama huko kwa familia ya Tera kusiko kwa kawaida, alipokuwa akizungumza mbele ya Sanhedrini ya Kiyahudi. Yeye alisema: “Mungu wa utukufu alimtokea baba yetu wa zamani Abrahamu alipokuwa katika Mesopotamia, kabla ya yeye kuanza kukaa katika Harani, naye akamwambia, ‘Nenda utoke katika nchi yako na kutoka katika jamaa zako na uje hadi kuingia katika nchi ambayo nitakuonyesha wewe.’ Ndipo akaenda kutoka nchi ya Wakaldayo na kuanza kukaa katika Harani.” (Matendo 7:2-4) Tera alitii yale ambayo Yehova alimtaka Abrahamu afanye kwa kuwahamisha watu wa karibu wa nyumbani mwake kwenda Harani.

5. Abrahamu alikwenda wapi baada ya baba yake kufa? Kwa nini?

5 Familia ya Tera iliishi katika jiji lao jipya. Miaka kadhaa baadaye, Abrahamu aliposema juu ya “nchi yangu,” alimaanisha eneo la Harani, wala si Uru. (Mwanzo 24:4) Hata hivyo, Harani halingekuwa makao ya kudumu ya Abrahamu. Kulingana na Stefano, “baada ya baba [ya Abrahamu] kufa, Mungu akamsababisha abadili makao yake hadi kwenye nchi hii ambamo nyinyi sasa mwakaa.” (Matendo 7:4) Kwa kutii mwongozo wa Yehova, Abrahamu, alivuka Eufrati na kuingia nchi ya Kanaani, akiandamana na Loti.a

6. Yehova alimtolea Abrahamu ahadi gani?

6 Kwa nini Yehova alimfanya Abrahamu ahamie Kanaani? Sababu ilihusu makusudi ya Mungu kwa mwanamume huyo mwaminifu. Yehova alikuwa amemwambia Abrahamu: “Toka wewe katika nchi yako, na jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka nchi nitakayokuonyesha; nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, na kukubariki, na kulikuza jina lako; nawe uwe baraka; nami nitawabariki wakubarikio, naye akulaaniye nitamlaani; na katika wewe jamaa zote za dunia watabarikiwa.” (Mwanzo 12:1-3) Abrahamu angekuwa baba ya taifa kubwa ambalo lingefurahia ulinzi wa Yehova na kumiliki nchi ya Kanaani. Ahadi ya ajabu sana! Lakini Abrahamu angelazimika kufanya mabadiliko makubwa maishani mwake ili kurithi nchi hiyo.

7. Ilimpasa Abrahamu awe tayari kufanya mabadiliko gani ili awe tayari kurithi ahadi ya Yehova?

7 Alipoondoka Uru, Abrahamu aliacha jiji lenye usitawi na yaelekea pia aliacha jamaa ya baba yake—vyanzo muhimu vya usalama nyakati hizo za wazee wa ukoo. Alipoondoka Harani, alijitenga na watu wa nyumba ya baba yake, kutia na familia ya Nahori ndugu yake, akahamia nchi isiyojulikana. Huko Kanaani, yeye hakutafuta usalama kwa kuishi ndani ya jiji lenye kuta. Kwa nini? Punde baada ya Abrahamu kuingia katika nchi hiyo, Yehova alimwambia: “Ondoka, ukatembee katika nchi hii katika mapana yake, na marefu yake, maana nitakupa wewe nchi hiyo.” (Mwanzo 13:17) Abrahamu mwenye umri wa miaka 75 na Sara mke wake mwenye umri wa miaka 65, walifuata maagizo hayo. “Kwa imani yeye alikaa kama mgeni asiye mzalia katika nchi ya ahadi kama katika nchi ya ugenini, na kukaa katika mahema.”—Waebrania 11:9; Mwanzo 12:4.

Imani Iliyo Kama ya Abrahamu Leo

8. Kwa kufikiria kielelezo cha Abrahamu na mashahidi wengine wa kale, yatupasa kusitawisha nini?

8 Abrahamu na familia yake wametajwa miongoni mwa ‘wingu kubwa la mashahidi wa kabla ya Ukristo’ wanaotajwa katika Waebrania sura ya 11. Kwa kuzingatia imani ya watumishi hao wa zamani wa Mungu, Paulo awatia Wakristo moyo “[wa]ondoe kila uzito na dhambi [ukosefu wa imani] ambayo hututatanisha kwa urahisi.” (Waebrania 12:1) Naam, ukosefu wa imani waweza ‘kututatanisha kwa urahisi.’ Lakini katika siku ya Paulo na yetu pia, Wakristo wa kweli wameweza kusitawisha imani yenye nguvu inayoweza kulinganishwa na ile ya Abrahamu na wengineo wa nyakati za kale. Akizungumza juu yake mwenyewe na pia Wakristo wenzake, Paulo asema: “Sisi si namna irudiyo nyuma kwenye uangamivu, bali namna iliyo na imani kuelekea kuhifadhi hai nafsi.”—Waebrania 10:39.

9, 10. Kuna uthibitisho gani kwamba wengi leo wana imani kama ile ya Abrahamu?

9 Ni kweli, ulimwengu umebadilika tangu wakati wa Abrahamu. Hata hivyo, tungali twamtumikia “Mungu [yuleyule] wa Abrahamu,” naye habadiliki. (Matendo 3:13; Malaki 3:6) Yehova anastahili kuabudiwa leo kama alivyoabudiwa wakati wa Abrahamu. (Ufunuo 4:11) Wengi hujiweka wakfu kabisa kwa Yehova na kama Abrahamu, wao hufanya mabadiliko yoyote yale yahitajiwayo maishani mwao ili kufanya mapenzi ya Mungu. Mwaka uliopita, watu 316,092 walithibitisha hadharani wakfu wao kwa kukubali ubatizo wa maji “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.”—Mathayo 28:19.

10 Haikuwa lazima kwa wengi wa Wakristo hao wapya kusafiri kwenda katika nchi za kigeni ili kutimiza wakfu wao. Ingawa hivyo, katika maana ya kiroho, wengi wao walisafiri mbali sana. Kwa kielelezo, huko Mauritius, Elsie alikuwa mlozi wa kike. Kila mtu alimwogopa. Painia mmoja wa pekee alipanga kujifunza Biblia pamoja na binti ya Elsie, na hilo likatokeza fursa kwa Elsie ‘kugeuka kutoka kwenye giza hadi kwenye nuru.’ (Matendo 26:18) Kwa kuzingatia kupendezwa kwa binti yake, Elsie alikubali kujifunza Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. Funzo lake liliongozwa mara tatu kwa juma kwa sababu alihitaji kutiwa moyo daima. Mazoea yake ya mizungu hayakumletea furaha yoyote, na alikuwa na matatizo mengi ya kibinafsi. Ingawa hivyo, hatimaye aliweza kufanya badiliko kubwa la kuacha ibada ya roho waovu na kuanza ibada ya kweli. Watu walipokuja kutafuta huduma zake, alikuwa akiwaeleza kwamba Yehova pekee ndiye awezaye kuwalinda na uovu. Sasa Elsie ni Shahidi aliyebatizwa, na watu 14 miongoni mwa familia yake na marafiki wake wameikubali kweli.

11. Ni mabadiliko gani ambayo wale wanaojiweka wakfu kwa Yehova wako tayari kufanya?

11 Wengi kati ya wale waliojiweka wakfu kumtumikia Mungu mwaka uliopita hawakulazimika kufanya mabadiliko makubwa kama hayo. Lakini wote walibadilika wakaacha kuwa wafu kiroho, wakawa hai kiroho. (Waefeso 2:1) Ingawa wamo ulimwenguni kimwili, wao si sehemu yake tena. (Yohana 17:15, 16) Sawa na Wakristo watiwa-mafuta, ambao “uraia wao uko katika mbingu,” wao ni kama “wakazi wa muda.” (Wafilipi 3:20; 1 Petro 2:11) Waliishi kupatana na viwango vya Mungu, wakichochewa zaidi na kumpenda Mungu na jirani. (Mathayo 22:37-39) Wao hawafuatii miradi ya kimwili yenye ubinafsi, au kuona uhitaji wa kutimiza jambo fulani katika ulimwengu huu. Badala yake, wao hukaza macho yao kwenye ‘mbingu mpya na dunia mpya ambazo katika hizo uadilifu utakaa.’—2 Petro 3:13; 2 Wakorintho 4:18.

12. Ni utendaji gani ulioripotiwa mwaka uliopita ambao watoa uthibitisho kwamba, wakati wa kuwapo kwake, Yesu ameipata “hiyo imani duniani”?

12 Abrahamu alipohamia Kanaani, yeye na familia yake walikuwa peke yao huko, wakitegemezwa na kulindwa na Yehova tu. Hata hivyo, bila shaka Wakristo hawa 316,092 waliobatizwa karibuni hawako peke yao. Ni kweli kwamba Yehova huwategemeza na kuwalinda kupitia roho yake, kama alivyomfanyia Abrahamu. (Mithali 18:10) Isitoshe, yeye huwategemeza kupitia “taifa” lenye kutenda la kimataifa lenye watu wengi zaidi kushinda baadhi ya mataifa ya ulimwengu leo. (Isaya 66:8) Mwaka uliopita, kilele cha raia 5,888,650 wa taifa hilo walithibitisha imani yao yenye kutenda kwa kuzungumza na majirani wao juu ya ahadi za Mungu. (Marko 13:10) Walitumia muda wenye kutokeza wa saa 1,186,666,708 katika kazi hiyo, wakitafuta kupata watu wenye kupendezwa. Tokeo lilikuwa kwamba mafunzo ya Biblia 4,302,852 yaliongozwa pamoja na wengine wanaotaka kusitawisha imani yao. Ukiwa wonyesho zaidi wa bidii yao, watu 698,781 katika “taifa” hilo walishiriki katika utumishi wa painia, ama kwa wakati wote ama kwa mwezi mmoja ama zaidi. (Habari zote kuhusu utendaji wa Mashahidi wa Yehova mwaka uliopita zapatikana kwenye ukurasa wa 12 hadi 15.) Rekodi hiyo yenye kutokeza ni jibu lifaalo na halisi kwa swali la Yesu, “Mwana wa binadamu awasilipo, je, kwa kweli ataipata hiyo imani duniani?”

Wenye Imani Licha ya Majaribu

13, 14. Fafanua baadhi ya magumu ambayo Abrahamu na familia yake walikabili huko Kanaani.

13 Mara nyingi, hali zilikuwa ngumu kwa Abrahamu na watu wa nyumba yake huko Kanaani. Kwenye pindi moja hivi, kulikuwako njaa kali sana ambayo ilimfanya ahame Kanaani kwenda Misri. Isitoshe, watawala wa Misri na wa Gerari (karibu na Gaza) walijaribu kumtwaa Sara, mke wa Abrahamu, kwa ajili yao wenyewe. (Mwanzo 12:10-20; 20:1-18) Kulikuwako pia mapambano baina ya wachungaji wa mifugo ya Abrahamu na wale wa mifugo ya Loti, nayo yaliwatenganisha watu wa nyumba hizo mbili. Bila ubinafsi, Abrahamu aliacha Loti achague nchi kwanza, naye akachagua kuishi katika Wilaya ya Yordani, iliyoonekana kama Edeni kwa rutuba na uzuri wake.—Mwanzo 13:5-13.

14 Ndipo Loti akahusika katika vita baina ya mfalme wa Elamu ya mbali na washirika wake, na wafalme wa majiji matano kwenye Bonde la Sidimu. Hao wafalme wa kutoka ugenini waliwashinda kabisa wafalme wa hayo majiji matano na kutwaa mateka kwa wingi, kutia ndani Loti na mali zake. Abrahamu aliposikia yaliyokuwa yametokea, aliwafuatia wafalme hao wa kigeni bila kuogopa, akaweza kumwokoa Loti na watu wa nyumbani mwake. (Mwanzo 14:1-16) Hata hivyo, Loti alipatwa na jambo baya zaidi ya hilo huko Kanaani. Kwa sababu fulani, yeye alianza kukaa Sodoma licha ya sifa ya ukosefu wa adili wa jiji hilo.b (2 Petro 2:6-8) Alipoonywa na malaika wawili kwamba jiji hilo lingeharibiwa, Loti alikimbia pamoja na mkewe na binti zake. Hata hivyo, mke wa Loti alipuuza maagizo hususa ya malaika nalo tokeo likawa kwamba, alifunikwa kwa chumvi. Hali ya Loti ilishuka kufikia kiwango cha kuishi kwa muda fulani katika pango huko Zoa, akiwa na binti zake wawili. (Mwanzo 19:1-30) Lazima matukio hayo yalimsumbua Abrahamu sana, hasa kwa kuwa Loti alikuwa amekuja Kanaani akiwa sehemu ya watu wa nyumbani mwa Abrahamu.

15. Licha ya matatizo ambayo Abrahamu alikabili alipokuwa akiishi mahemani katika nchi ya kigeni, ni kufikiri kupi kusikofaa ambako kwa wazi yeye aliepuka?

15 Je, Abrahamu alikuwa na shaka wakati wowote kama iliwapasa yeye na Loti kukaa Uru pamoja na jamaa ya baba yake au kukaa Harani pamoja na ndugu yake Nahori? Je, alitamani wakati wowote kuweza kukaa katika jiji lenye kuta, mahali penye usalama badala ya kukaa katika mahema? Je, labda alikuwa na shaka juu ya hekima ya kujidhabihu kwa kuwa mzururaji katika nchi ya kigeni? Akizungumza juu ya Abrahamu na familia yake, mtume Paulo aliandika hivi: “Kama kwa kweli wangalifuliza kukumbuka mahali hapo walipokuwa wametoka, wangalikuwa na fursa ya kurudi.” (Waebrania 11:15) Hata hivyo, hawakurudi. Bila kuvunjwa moyo na magumu hayo, walikaa mahali Yehova alipotaka wakae.

Uvumilivu Leo

16, 17. (a) Wakristo wengi hukabili matatizo gani leo? (b) Wakristo wana mtazamo gani ufaao? Kwa nini?

16 Uvumilivu kama huo waonekana katika Wakristo leo. Ingawa kumtumikia Mungu huwaletea shangwe kubwa, maisha si rahisi kwa Wakristo wa kweli katika siku hizi za mwisho. Ingawa wanaishi katika paradiso ya kiroho, wao hupatwa na misongo ileile ya kiuchumi iwapatayo majirani wao. (Isaya 11:6-9) Wengi wamekuwa wahasiriwa wasio na hatia wa vita vya mataifa, na wengine wamekuwa na hali yenye umaskini sana kwa kosa lisilo lao. Isitoshe, wao huvumilia matatizo ya kuwa kikundi kidogo kisichopendwa wa wengi. Katika nchi nyingi wao huhubiri habari njema wajapokabili ubaridi mwingi. Katika nchi nyingine wao hushambuliwa kwa mambo ya udanganyifu na wale ‘watungao madhara kwa njia ya sheria’ na “kuihukumu damu isiyo na hatia.” (Zaburi 94:20, 21) Hata katika nchi ambako Wakristo hawashambuliwi, na ambako wanasifiwa na wengine kwa sababu ya viwango vyao vya juu, wanatambua kuwa wao ni tofauti na wanashule wenzao na wafanyakazi wenzao—kama vile Abrahamu, aliyeishi mahemani huku majirani wake wakiishi majijini. Naam, si rahisi kuishi katika ulimwengu na bado ‘usiwe sehemu’ yake.—Yohana 17:14.

17 Basi je, sisi hujutia kujiweka kwetu wakfu kwa Mungu? Je, sisi twatamani kwamba tungeendelea kuwa sehemu ya ulimwengu huu, tukiwa kama watu wengineo? Je, sisi husikitika kwa sababu ya vitu ambavyo tumedhabihu katika utumishi wa Yehova? La, Hasha! Badala ya kutazama nyuma kwa kutamani, tunatambua kwamba kitu chochote tuwezacho kuwa tumedhabihu hakikuwa na thamani yoyote halisi kikilinganishwa na baraka tunazofurahia sasa na tutakazofurahia wakati ujao. (Luka 9:62; Wafilipi 3:8) Isitoshe, je, watu katika ulimwengu ni wenye furaha? Ukweli ni kwamba, wengi wao wanatafuta majibu ambayo sisi tunayo tayari. Wao huteseka kwa sababu ya kutofuata mwongozo ambao sisi hufuata kutoka kwa Mungu kupitia kurasa za Biblia. (Zaburi 119:105) Na wengi wao hutamani aina ya uandamani wa Kikristo na ushirika wenye kupendeza sana ambao sisi hufurahia pamoja na waamini wenzetu.—Zaburi 133:1; Wakolosai 3:14.

18. Matokeo huwa nini hatimaye Wakristo waonyeshapo ujasiri kama ule wa Abrahamu?

18 Ni kweli, nyakati nyingine inatupasa kuwa wajasiri kama Abrahamu alipowafuatia watekaji wa Loti. Lakini tunapokuwa wajasiri, Yehova hubariki matokeo. Kwa kielelezo, katika Ireland ya Kaskazini chuki imeimarika sana kwa sababu ya jeuri za kidini, na inahitaji ujasiri ili kutopendelea upande wowote. Hata hivyo, Wakristo waaminifu wamefuata maneno ambayo Yehova alimwambia Yoshua: “Uwe hodari na moyo wa kishujaa; usiogope wala usifadhaike; kwa kuwa BWANA, Mungu wako, yu pamoja nawe kila uendako.” (Yoshua 1:9; Zaburi 27:14) Kwa miaka mingi msimamo wao wa kutoogopa umefanya waheshimiwe, na leo wanaweza kuhubiri kwa uhuru katika jumuiya zote za nchi hiyo.

19. Wakristo hufurahia kuwa wapi, nao hutarajia matokeo gani kwa uhakika wanapofuata mwongozo wa Yehova?

19 Hatuhitaji kuwa na shaka kwamba, hata tukabili hali gani, tukifuata mwelekezo wa Yehova, hatimaye matokeo yatamletea utukufu nasi tutapata manufaa za kudumu. Licha ya magumu na dhabihu mbalimbali, hakuna mahali pengine ambapo pangekuwa afadhali zaidi kwetu kuwa, kuliko kuwa katika utumishi wa Yehova, tukifurahia ushirika pamoja na ndugu zetu Wakristo huku tukitarajia kwa uhakika wakati ujao wa milele ambao Mungu ameahidi.

[Maelezo ya Chini]

a Yaelekea Abrahamu alimwasilisha Loti, mpwa wake wa kiume, wakati baba yake Loti, ndugu yake Abrahamu, alipokufa.—Mwanzo 11:27, 28; 12:5.

b Watu fulani wamedokeza kwamba Loti alianza kukaa katika jiji ili apate usalama zaidi baada ya kutekwa na wale wafalme wanne.

Je, Wakumbuka?

◻ Kwa nini imani yenye nguvu ni muhimu?

◻ Abrahamu alionyeshaje kwamba alikuwa na imani yenye nguvu?

◻ Kujiweka wakfu huambatanaje na mabadiliko maishani mwa mtu?

◻ Kwa nini tunafurahia kumtumikia Mungu licha ya matatizo yoyote ambayo huenda tukakabili?

[Picha katika ukurasa wa 7]

Abrahamu alikuwa tayari kufanya mabadiliko makubwa maishani mwake ili kurithi ahadi

[Picha katika ukurasa wa 9]

Uthibitisho waonyesha kwamba Yesu ameipata “hiyo imani duniani” wakati wa kuwapo kwake

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki