Wanateswa kwa Ajili ya Uadilifu
Labda umesikia kwa rafiki na watu wako wa ukoo kwamba Mashahidi wa Yehova wanakorofiana na sheria, kwamba wanapigwa marufuku na serikali fulani, au kwamba pengine ni watu wabaya. Kwa sababu gani wanasemewa kinyume?
Si kwa sababu Mashahidi hawaheshimu sheria bali ni kwa sababu wanafuata hatua za Yesu. Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba watu wangewashutumu, wangewatesa, na wangesema kwa uwongo kila namna ya jambo baya juu yao. Hiyo ni kwa sababu mpinzani mkuu wa Mungu, Shetani, ndiye mungu wa ulimwengu huu, naye angependa kuondoa watu wasimtumikie Mungu. —Mathayo 5:10-12; 10:16-22, 34-39; 24:9, 10; Yohana 15:17–16:3; 2 Timotheo 3:12; 1 Petro 5:8; Ufunuo 12:17.
Mitume walipokamatwa wakapelekwa mahakamani, haikuwa kwa sababu walikuwa wahalifu, watu wenye jeuri, au wafitini wa serikali. Ilikuwa kwa sababu walikuwa wakizihubiri habari njema. Mtume Paulo alipoomba rufani ya kesi yake kwenye mahakama za juu zaidi, ilikuwa kwa kutetea na kuthibitisha kisheria haki ya Wakristo ya kuzihubiri habari njema. —Matendo 4:18-20; 5:28-32; Wafilipi 1:7.
Leo, Mashahidi wa Yehova ni Wakristo wenye kutii sheria wanaolipa kodi zao na kuonyesha heshima kwa wale walio katika mamlaka. Wanamlipa Kaisari mambo ya Kaisari na mambo ya Mungu wanamlipa Mungu. Ikiwa wanapingana na mamlaka yo yote ya kiserikali, ni kwa sababu serikali inakataa kutambua kazi yao ya kuhubiri, au kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo katika mambo baina ya mataifa. Lakini katika hilo ni lazima Mashahidi wa Yehova wachukue msimamo ule ule waliochukua mitume, waliosema: “Ni lazima kumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” —Matendo 5:29, NW; Marko 12:17; Yohana 18:36; Tito 3:1, 2.
Mashahidi wa Yehova hawatafuti kuteswa bali wangependelea kuishi maisha matulivu na ya kimya. Hata hivyo, ikiwa kwa sababu ya kufuata kwao sheria ya Mungu na mfano wa Yesu Kristo wanateswa, wanafurahi kuvumilia jambo hilo. —Mathayo 5:10-12; Matendo 5:40, 41; 1 Wakorintho 4:12; 1 Timotheo 2:2; 1 Petro 3:14, 15; 4:12-16.
• Ni kwa sababu gani watumishi wa Yehova wanashutumiwa na kuteswa?
• Ni kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova mara nyingine wanapingana na mamlaka za kiserikali, kama mitume wale Wakristo?
• Watumishi wa Yehova wanaonaje mateso?
[Picha katika ukurasa wa 29]
Yesu alipelekwa mbele ya Pilato na mtume Paulo alifungwa gerezani kwa sababu ya kuhubiri Ufalme wa Mungu