Sura 1
Amani na Usalama wa Kweli Ni Karibu!
1. Ni hali gani zinazofanya amani na usalama wa kweli utamanike sana?
KAMA vile watu walio wengi leo wanavyotamani sana, bila shaka wewe watamani sana amani na usalama. Kila mahali watu wamechoka na uhalifu, jeuri, vita na tisho la nyukilia. Pia, wengi hawana kazi nzuri, nyumba inayofaa, au chakula cha kutosha. Ingekuwa furaha iliyoje ikiwa matatizo kama hayo yangeweza kutatuliwa na dunia hii iwe makao ya kupendeza, yenye usalama kwa wakaaji wayo!
2, 3. (a) Ikiwa amani na usalama wa kweli ni karibu kweli kweli, ni maswali gani ambayo yanahitaji kuulizwa? (b) Tendo lililochukuliwa na Umoja wa Mataifa linaonekanaje kuwa linapatana na tamaa ya amani na usalama?
2 Kwa kushangaza, kuna sababu nzuri kuamini kwamba kitulizo kinachotamaniwa sana ki karibu, kwamba amani na usalama ulimwenguni pote wakaribia kuwa hakika! Lakini ni nani atakayetimiza hilo? Je! mataifa ya ulimwengu huu yataweka kando tofauti zao ili yaweze kutimiza hilo?
3 Unabii wa Biblia wenye kupendeza ulieleza kwamba wakati ungefika ambapo viongozi wa ulimwengu wangetangaza “amani na usalama!”a Kwa kweli, wakati Umoja wa Mataifa ulipotangaza 1986 kuwa “Mwaka wa Kimataifa wa Amani” uliuliza matengenezo kila mahali yafanye jitihada ya pekee kuanzia mwaka huo na kuendelea yaendeleze mradi wa “amani, usalama wa kimataifa na ushirikiano.”1
4. Ili mpango wo wote wa amani na usalama ukunufaishe wewe, ni matatizo gani ambayo lazima utatue?
4 Lakini je! hiyo ingekuwa “amani na usalama” wa kweli? Je! ungefika ndani ya ujirani wako na ndani ya nyumba yako na kuondoa matatizo yanayokupata wewe binafsi? Je! ungetatua tatizo la kuongezeka kwa uhalifu na uzoelevu wa dawa za kulevya, gharama zenye kupanda za chakula, kutozwa sana kodi, uchafuzi unaoenea, na kudhoofika daima kwa vifungo vya jamaa? Maadamu zo zote za hali hizi zinaendelea, zinaelekea kuharibu amani na usalama wako binafsi.
5, 6. Kwa msingi wa mambo ambayo umejionea mwenyewe maishani, je! wewe unaamini kwamba wanadamu watayatatua matatizo hayo?
5 Kweli, wanadamu wanatumaini kwamba wao wanaweza kuyaondoa magumu hayo. Wanasema kwamba, wakiwa huru na gharama zinazowalemea za vita, wanaweza kutumia mali ile yote, uchunguzi, na wafanyi kazi kuyatatua matatizo haya.
6 Je! kweli wewe waamini hayo? Je! kuna ushuhuda wo wote ulio hakika unaoonyesha kwamba wanadamu wanaweza kuleta matatuzi yenye kudumu? Historia inaonyesha nini? Kwa kweli, mambo ambayo wewe umejionea mwenyewe maishani yanakuambia nini?
7, 8. (a) Tungetazamia kupata utatuzi wapi penginepo? (b) Biblia ni kitabu chenye kujulikana kadiri gani?
7 ‘Lakini ikiwa wanadamu hawana matatuzi, kunabaki nini?’ labda utauliza. Basi, uhakika usioweza kupingwa unaonyesha kwamba dunia na vitu vilivyo hai ndani yayo vinatoa ushuhuda wa ubuni wenye akili. (Waebrania 3:4) Je! inawezekana kwamba Yeye aliyeanzisha ubuni huu yumo katika shauri hili? Je! atajitia katika mambo ya wanadamu? Ni Biblia pekee inayotoa majibu kwa maulizo hayo.
8 Basi, kwa sababu ya mambo yanayohusika, je! halingekuwa jambo linalofaa kufikiria yale ambayo Biblia husema juu ya shauri hili? Pengine unafahamu kwamba ndicho kitabu ambacho kimetafsiriwa na kuenezwa zaidi duniani. Ikiwa nzima au sehemu, mabilioni ya nakala zimeenezwa katika lugha zaidi ya 1,800.2 Lakini je! wewe ulifahamu kwamba kitabu hiki cha kale kinatoa matatuzi ya mambo yenyewe ambayo tunahangaikia sana katika karne hii ya 20?
9, 10. (a) Biblia inasema nini juu ya wakati ujao, na juu ya serikali za kibinadamu? (b) Ufalme wa Mungu ni nini, na ni wakati gani utakapochukua utawala kutoka serikali zote za kisasa?
9 Watu wengi wanajua kwamba Biblia inatabiri ‘mwisho wa dunia.’ Lakini ni wachache wanaojua inayosema juu ya wakati mwisho huo utakapokuja, au juu ya jinsi maisha yatakavyokuwa hapa duniani baadaye. (Mathayo 24:21, 22; 2 Petro 3:11-13) Huenda hata wakasali Sala ya Bwana, ambamo wanauliza ‘ufalme wa Mungu uje.’ (Mathayo 6:9, 10) Lakini ni wachache wanaofahamu kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali halisi itakayochukua mahali pa mifumo yote ya sasa ya kisiasa. Kama alivyoeleza nabii Danieli: “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, . . . utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.
10 Kwa kupendeza, unabii wa Biblia kuhusu “amani na usalama” uliotangulia kuzungumzwa unatia ndani sehemu hizi: “Wakati wo wote wanaposema: ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa juu yao papo kwa hapo.” (1 Wathesalonike 5:3, NW) Kwa hiyo ni wazi kwamba amani yo yote wanayotangaza viongozi wa kibinadamu itakuwa ya muda mfupi sana. Kwa kuwa unabii unaonyesha kwamba mara tu baadaye tawala zote za kibinadamu zitavunjwa-vunjwa na kuondolewa zisiwepo, na mahali pazo patachukuliwa na serikali moja duniani pote—Ufalme wa Mungu.
11, 12. Ni baadhi ya tofauti gani zilizopo kati ya yale ambayo Biblia inasema Ufalme wa Mungu utafanya na yale ambayo viongozi wa kibinadamu wanajaribu kufanya?
11 Tena, Biblia inafunua wazi tofauti mbalimbali kati ya amani na usalama ambao Ufalme wa Mungu utaleta na amani na usalama ambao viongozi wa kibinadamu wanaahidi. Leo wanadamu wanasema juu ya kupunguza silaha kwa njia ya mapatano ya amani. Lakini, Biblia inasema kwamba karibuni Mungu atakomesha kabisa uundaji wote wa silaha na kuondoa vyanzo vile vya msingi vinavyoleta vita. (Zaburi 46:9; Isaya 2:2-4) Na usalama ambao Mungu anaahidi si wa kutokuwa na vita kati ya mataifa tu. Ni wa kutokuwa na adui wa namna yo yote, hata mtu ye yote asiogope tena—mchana au usiku. (Mika 4:3, 4) Pia, sasa wanadamu wanashughulika ili wazuie uhalifu, lakini kusudi la Mungu lililotangazwa ni kuondoa kabisa hata mielekeo na hali zinazoongoza kwenye uhalifu.—Zaburi 37:8-11; Wagalatia 5:19-21.
12 Pia mataifa yanajivunia maendeleo katika uchunguzi wa kitiba na njia bora za kuwatunzia wagonjwa na wazee. Lakini Biblia inaeleza namna serikali ya Mungu itakavyoleta afya kamili na yenye kuendelea, hata kuondoa kuzeeka na kifo! (Ufunuo 21:3, 4) Kwa kuongezea, chini ya Ufalme wa Mungu kazi ya mtu itakuwa yenye maana kweli kweli, ikileta uradhi wa kweli. Kwa maana unawezaje kuwa mwenye furaha ikiwa kazi yako inakuvuruga fikira na huoni unalotimiza katika maisha?—Isaya 65:21-23; Warumi 8:19-21.
13. Ni maswali gani ambayo yangefaa tuchunguze?
13 Wewe unaamini ni jambo gani linalotoa aina ya amani na usalama utakaofanyia maendeleo kila sehemu ya maisha yako—ahadi za wanadamu, au ahadi za Mungu kama zinavyotekelezwa na serikali ya Ufalme wake? Kwa kufuata yale yanayotolewa na ulimwengu wote kwa ujumla, je! kweli umepata unachotaka katika maisha? Namna gani ukijiacha uvutwe na yanayoelekea kuwa ni yenye kupendwa na watu wengi sasa, lakini utambue kwamba umedanganywa na ahadi zinazopotosha, zikikuacha bila amani na usalama halisi? Kwa upande mwingine, je! unaweza kuwa na uhakika kwamba yale ambayo Biblia inaahidi ni yenye kuaminika, yenye mafaa, na yanayoweza kutukia kikweli? Kwa hakika, majibu kwa maulizo haya yanahitaji uchunguzi wa makini.
[Maelezo ya Chini]
a 1 Wathesalonike 5:3, NW.
[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 4]
[Picha katika ukurasa wa 9]
Hakuna mtu atakayeogopa tena—mchana au usiku