Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 6/15 kur. 10-16
  • “Amani na Usalama!”—Halafu “Uharibifu wa Ghafula”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Amani na Usalama!”—Halafu “Uharibifu wa Ghafula”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “SIKU YA KISASI” CHA YEHOVA
  • “UHARIBIFU WA GHAFULA”
  • WAKISEMA “AMANI NA USALAMA!”
  • NI KIDANGANYA-MACHO TU
  • Maoni Ya Biblia Juu Ya Amani Na Usalama
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Amani Kutoka kwa Mungu Wakati Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Kutazama Mbele ya “Amani na Usalama” Wenye Kufanyizwa na Binadamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Amani na Usalama wa Kweli Ni Karibu!
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 6/15 kur. 10-16

“Amani na Usalama!”—Halafu “Uharibifu wa Ghafula”

“Wakati wo wote wanaposema: ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa juu yao papo kwa hapo.”—1 Wathesalonike 5:3, NW.

1. Wachunguzi wengi wa hali za ulimwengu wanasema nini sasa?

WACHUNGUZI wengi wa mambo ya kibinadamu wanakubali kwamba hali za ulimwengu zimezidi kuharibika sana miaka ya majuzi. Katika Kanada, kwenye Mashauriano ya Ulimwengu Mzima juu ya Wakati Ujao, msimamizi mkuu wa Klabu cha Roma,a Aurelio Peccei, alitamka hivi: “Ulimwengu umo katika hali mbaya zaidi sasa kuliko vile ulivyokuwa miaka kumi iliyopita—tena unazidi sana kuwa mbaya. Siku hizi ulimwengu unaanza kufanana zaidi na zaidi na risasi yenye kuruka-ruka huku na huku wakati unapowaya-waya kwa kupatwa na msiba mmoja baada ya mwingine.” André Fontaine, mhariri wa gazeti la kila siku Le Monde la Paris, alisema hivi: “Hakuna mtu katika nchi za Magharibi anayeelekea kushindana na matatizo makubwa sana kama vile infuleshoni na ukosefu wa kazi ya kuajiriwa. Pengo lililo kati ya nchi za Kaskazini na Kusini linazidi kupanuka. Kuna vita nyingi zaidi na zaidi, na mashindano ya kuunda silaha yanaogopesha sana. Basi mimi sioni sababu yo yote ya kutazamia mambo mazuri wakati ujao.  . . . Mimi sioni Serikali yo yote ulimwenguni leo inayoelekea kuwa na uwezo wa kushindana na yale matatizo makubwa-makubwa ya kiuchumi yaliyopo wakati wetu.” Na gazeti fulani la Afrika Kusini lilisema hivi: “Inaonekana wanadamu wameshuka sana katika tabia wakawa na ushenzi wa kinyama, wakaingia katika uasherati, kutokujali madaraka yao, kuwa na uchoyo na pupa.”

2. Hali zilizo katika jamii ya kibinadamu zinafananaje na zile zilizokuwako muda mfupi tu kabla ya gharika ya siku ya Noa?

2 Hali zilizo katika jamii ya kibinadamu leo zinalingana na mambo yaliyotukia duniani muda mfupi tu kabla Mungu hajaharibu ulimwengu wa kale kwa kutumia gharika ya dunia nzima, huku akiachilia Noa mwenye haki na jamaa yake peke yao. Kuhusu siku hizo, Biblia inasema: “[Yehova] akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani . . . Dunia ikaharibika mbele za Mungu, dunia ikajaa dhuluma.” (Mwanzo 6:5, 11) Yesu Kristo alitabiri kwamba “sawasawa na zile siku za Noa zilivyokuwa” ndivyo wakati wetu ungekuwa. (Mathayo 24:37, NW) Kwa mara nyingine tena dunia nzima ‘imejaa dhuluma’ kwa sababu “maovu ya mwanadamu” ni tele. Hali hizo zilizokuwako kabla ya Gharika zilionyesha mwisho wa taratibu hiyo ya mambo ya kale ilikaribia sana mwisho wayo. Kwa hiyo leo ushuhuda wa hali za ulimwengu zinazotimiza unabii wa Biblia unaonyesha wazi kwamba taratibu hii ya mambo imo katika “wakati wa mwisho” wake, “siku za mwisho” zayo. Ndivyo mambo yamekuwa tangu mwaka wa 1914 W.K.—Danieli 12:4; Mathayo 24:3-14; 2 Timotheo 3:1-5.

3. (a) Tunajuaje kwamba tumekwisha kuingia sana “siku za mwisho”? (b) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kamili kwamba unabii wa Biblia utatimia?

3 Yesu alitabiri kwamba wengine wa wale waliokuwa hai wakati zilipoanza “siku za mwisho” wangeendelea kuwa hai wauone mwisho wa taratibu hii. Tayari miaka 68 imepita tangu “kizazi” cha mwaka wa 1914 kilipouona mwanzo wa taabu hizi. (Mathayo 24:34) Basi wakati wa hiki “kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka” ni kama umekwisha. (Wafilipi 2: 15) Punde si punde huenda tukajionea wenyewe utimizo wa unabii mwingi wa Biblia unaohusiana na ‘kupita kwa ulimwengu.’ (1 Yohana 2: 17) Tena tunaweza kuwa na uhakika kamili kwamba unabii huo utatimizwa kwa mapana na marefu. Yehova, ‘yeye atangazaye mwisho tangu mwanzo,’ yeye aliyeuvuvia unabii huo kwa roho yake, “ameapa, akisema, Hakika yangu kama vile nilivyoazimia, ndivyo itakavyokuwa.”—Isaya 14:24; 46:10; 2 Petro 1:20, 21.

“SIKU YA KISASI” CHA YEHOVA

4. Mmoja wa unabii mbalimbali unaohusiana na mwisho wa taratibu hii ni unabii gani, nao unatokeza maswali gani?

4 Kati ya unabii mwingi wa Biblia unaohusu mwisho wa taratibu hii ya mambo unapatikana ule ulioandikwa kwenye 1 Wathesalonike sura ya 5, mistari 2 na 3, NW. Huo unasema hivi: “Kwa kuwa ninyi wenyewe mwajua sana kwamba siku ya Yehova inakuja sawasawa kama mwivi usiku. Wakati wo wote wanaposema: ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa juu yao papo kwa hapo sawasawa na utungu juu ya mwanamke mwenye mimba; nao hawataokoka kwa vyo vyote.” Huo usemi wa “Amani na usalama” ni usemi gani? Ni nani anayeusema? Na ni uharibifu gani unaokuja mara tu baada ya usemi huo?

5. Unabii ulio kwenye 1 Wathesalonike 5:2, 3 unahusu tukio gani?

5 Mistari hiyo ya Biblia inasema habari ya “siku ya Yehova,” ambayo itatokeza “uharibifu wa ghafula.” Kwa hiyo inafahamika wazi kwamba unabii huu unahusu ile “siku” au kipindi kile cha wakati ambapo Yehova atafikiliza hukumu zake juu ya taratibu hii mbovu ya mambo inayoongozwa na Shetani yule Ibilisi. (2 Wakorintho 4:4; Ufunuo 12:9) Hiyo ndiyo itakayokuwa “siku ya kisasi” cha Yehova. (Isaya 61:2) Yesu alikitaja kipindi hicho kwa kusema: “Wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.” (Mathayo 24:21) Mtume Paulo aliandika kwamba ufikilizaji wa hukumu unaokuja ungekuwa na maana ya “kufunuliwa kwake Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika na uweza wake; katika mwali wa moto; huku akiwalipiza kisasi wao wasiomjua Mungu, na wao wasioitii Injili ya Bwana wetu Yesu.” Kisha akaongezea hivi: “Watakaoadhibiwa kwa maangamizi ya milele, kutengwa na uso wa Bwana na utukufu wa nguvu zake.”—2 Wathesalonike 1:7-9.

6. “Dhiki kubwa” itaanzaje na itamalizikaje?

6 “Dhiki kubwa” inayokuja, “siku ya kisasi” cha Yehova, itaipata taratibu nzima ya mambo ya sasa—dini zayo za uongo na vilevile mipango yayo ya kiuchumi, kijamii na kisiasa. Mfuatano wa matukio ya hiyo “dhiki kubwa” umeonyeshwa na unabii mbalimbali uliotolewa katika kitabu cha Biblia cha Ufunuo. Unabii huo unafunua kwamba “siku ya kisasi” cha Yehova itaanza na uharibifu wa dini yote ya uongo. Itamalizika wakati sehemu za kisiasa na nyinginezo za ulimwengu wa Ibilisi, pamoja na wafuasi wazo, wadogo kwa wakubwa,” zitakapoharibiwa hatimaye.—Ufunuo sura ya 17 mpaka ya 19.

“UHARIBIFU WA GHAFULA”

7. Usemi wa “Amani na usalama!” unakuja muda mfupi tu kabla ya jambo gani?

7 Usemi wa “Amani na usalama!” basi unatamkwa muda mfupi tu kabla ya kutokea kwa “uharibifu wa ghafula” wa milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, milki inayoitwa ‘Babeli Mkuu’ katika unabii wa Biblia. (Ufunuo 17:5) Milki-mwanamke huyo inatajwa kuwa “yule kahaba mkuu . . . ambaye wafalme wa nchi wamezini naye.” (Ufunuo 17:1, 2) Lakini mambo yatakuwa mengine, kwa sababu wengi wa hawa “wafalme wa nchi” waliokuwa “wapenzi” wa kahaba huyo watamgeuka, kwa maana tunaambiwa hivi: “Hao watamchukia yule kahaba, nao watamfanya; kuwa mkiwa na uchi, watamla nyama yake, watamteketeza kabisa kwa moto.’—Ufunuo 17:16.

8. Kwa nini Yehova atahukumu dini ya kilimwengu kwa ukali mwingi hivyo?

8 Kwa nini taratibu hiyo ya ulimwengu ya kidini ihukumiwe vikali hivyo? Neno la Mungu linajibu: “Kwa maana dhambi zake zimefika hata mbinguni.” (Ufunuo 18:5) Moja kati ya dhambi hizo ni hii: “Ndani yake ilionekana damu ya manabii, na ya watakatifu, na ya wale wote waliouawa juu ya nchi.” (Ufunuo 18:24) Dini ya kilimwengu imehusika katika vita ambavyo vimechinja mamia ya mamilioni ya watu muda wa karne zote, huku ikikosa kufundisha wafuasi wayo kweli inayohusu Mungu na sheria zake. Pia, dini ya uongo ndiyo imekuwa mwongozi wa kutesa watumishi wa kweli wa Mungu. (Luka 11:47-51; Ufunuo 17:6) Kwa hiyo, kwa njia ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja, Yehova anamwona ‘Babeli Mkuu’ kuwa mwenye lawama la damu iliyomwagwa ya “wale wote waliouawa juu ya nchi” kwa sababu ya mambo aliyotenda au aliyoshindwa kutenda.

9, 10. (a) Watu wengine wamesema nini juu ya lawama la dini ya uongo la kuwa na hatia ya damu mpaka leo yetu hii? (b) Kwa kweli, ‘Babeli Mkuu’ amekuwa akitumikia nani?

9 Dini ya uongo inaendelea kujilundika hatia ya damu mpaka leo hii. Kwa mfano, gazeti Post la New York la Mei 18, 1981, lilitoa habari hizi: “Rais wa hapo nyuma kidogo, Carter, alisema jana kwamba chuki na jeuri ni mambo yanayofanya ionekane kwamba ‘ulimwengu umekwenda wazimu.’ “Alisema pia kwamba “imani nyingi sana ya kidini inayopasa kuunganisha watu katika upendo inaonekana mara nyingi kuwa imo katika wazimu huo na mauaji yanayofanywa.” Vivyo hivyo, siku mbili kabla ya hapo ukurasa wa mhariri Mike Royko ulisema katika gazeti ilo hilo kwamba Wakatoliki, Waprotestanti, Waislamu na Wayahudi “wanamtolea [Mungu] ibada yao kwa kuuana.” Alisema hivi: “Mimi nadhani wao wanawaza kwamba ikiwa upande mmoja unaweza kufagilia mbali upande ule mwingine, jambo hilo litahakikisha kwamba njia ya kuabudu ya upande wenye kushinda ndiyo sahihi.” Alisema pia kwamba ingawa papa wa Kanisa Katoliki la Roma anasemwa kuwa mtu mwenye amani, wafuasi wake wana sifa ya kwamba wamekuwa wakimwaga mamilioni kadha ya galani za damu wakati hasira zao zilipopanda.”

10 Hivyo, ile “dhiki kubwa” ina haki ya kuanza uharibifu wayo kwenye milki ya ulimwengu yenye makufuru na unafiki ya dini ya uongo. Hiyo ni hukumu yenye haki kwa sababu dini ya kilimwengu, ‘Babeli Mkuu,’ imedai kuwa inatumikia Mungu, kumbe imekuwa ikitumikia yule Ibilisi. Kwa hiyo imetumia “uchawi” wayo kufanya mamia ya mamilioni ya watu yawe yakidanganyika kutumikia mapendezi ya Ibilisi.—Ufunuo 17:3-6; 18:23.

11. Ni nini linaloonyesha kwamba uharibifu wa dini ya uongo unakuja kwa mfyatuko wenye kugutusha watu?

11 Anguko la ‘Babeli Mkuu’ laja kwa ghafula sana, bila kutazamiwa hata kidogo na ulimwengu. Uharibifu wake utakuja kwa ghafula sana hata watawala wa kisiasa waliomwunga mkono wagutuke sana, kwa maana tunasoma hivi: “Na hao wafalme wa nchi, waliozini naye na kufanya anasa pamoja naye, watalia na kumwombolezea; wauonapo moshi wa kuungua kwake wakisimama mbali kwa hofu ya maumivu yake, wakisema, Ole, ole, mji ule ulio mkuu, Babeli, mji ule ulio na nguvu! kwa kuwa katika saa moja hukumu yako imekuja.” Wengine—wale “wafanya biashara” wenye kusafiri waliomwunga mkono—watapiga yowe ilo hilo: “Ole, ole . . . kwa kuwa katika saa moja utajiri mwingi namna hii umekuwa ukiwa.”—Ufunuo 18: 9-19.

12. Ni kwa njia gani uharibifu unakuja bila kutazamiwa na kwa maumivu mengi?

12 Maneno haya yanafanana na maelezo yaliyo katika 1 Wathesalonike 5:2 na 3, NW, yanayoonyesha kwamba uharibifu huo unakuja kwa ghafula sana na bila kutazamiwa, kwa maana “siku ya Yehova” itapasa kuja “sawasawa kama mwivi usiku.” Ni kwa njia gani inakuja “kama mwivi usiku”? Katika maana ya kwamba watu walio wengi wamekuwa hawaendelei kukesha wauone ufunuo wa hatua kwa hatua wa mapenzi ya Mungu. Wao wamelala kiroho. Wako kama mtu anayekuwa amelala usiku wakati mwivi ajapo bila kutazamiwa. Watu wa namna hiyo wamejiruhusu wapumbae akili mpaka wakaiunga mkono taratibu hii ya mambo iliyohukumiwa maangamizi. Kwa hiyo uharibifu wa Babeli Mkuu unawajia bila kutazamiwa. Naam, “siku ya Yehova” ya kuharibu sehemu zote za taratibu ya Shetani itakuja “sawasawa kama mwivi usiku.” Uharibifu utawajilia adui za Mungu kwa ghafula na kwa njia yenye maumivu, “sawasawa na utungu juu ya mwanamke mwenye mimba; nao hawataokoka kamwe.”—Angalia pia 2 Petro 3:10.

WAKISEMA “AMANI NA USALAMA!”

13, 14. (a) Kwa muda mrefu mataifa yamezungumzaje habari za amani na usalama? (b) Kwa nini hakuna yo yote ya jitihada hizo za kuleta amani imetimiza 1 Wathesalonike 5:2, 3?

13 Matukio yenye kuutikisa ulimwengu yataonekana wakati wa “uharibifu wa ghafula” juu ya dini ya uongo na ulimwengu wote wa Shetani. Lakini uharibifu huo unatanguliwa muda mfupi sana na usemi wa “Amani na usalama!” Basi inafaa sana tujue tangazo hilo la “Amani na usalama!” lingeweza kuwa na maana gani. Kwanza, haionekani kwamba litakuwa zile jitihada za kikawaida tu ambazo mataifa hufanya nyakati zote yakitaka amani. Wao wamezungumza habari hizo muda mrefu. Kwa mfano, baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza mataifa yalitia sahihi mkataba wa amani huko Versailles. Baadaye, nchi zilizo nyingi ziliitia sahihi hati ya mapatano ya kukaa kwa amani yaliyofanywa kati ya Kellogg na Briand mwaka wa 1928. Vita ya Ulimwengu ya Pili ilipomalizika mikataba (maafikiano) ya kukaa kwa amani ilifanywa. Katika miaka ya majuzi Urusi na United States (Amerika) zimezungumza habari za amani na kutia sahihi mapatano fulani ya kuzuia utengenezaji wa silaha za vita. Mataifa mbalimbali ya Mashariki ya Kati yamefanya-fanya mara nyingi mapatano ya amani.

14 Lakini hakuna hata moja ya jitihada hizo inayotimiza maelezo yaliyo kwenye Wathesalonike 5:2, 3, NW. Kwa sababu gani? Kwa sababu ile “dhiki kubwa,” “siku ya kisasi” cha Yehova, haijaanza. Kumbuka kwamba Paulo alisema uharibifu ungekuja kwa ghafula, “papo kwa hapo,” baada ya tangazo la “Amani na usalama!” Zaidi ya hilo, utimizo wa jambo hilo lazima ufyatuke kwa njia inayotosha kuonyesha ukweli wa habari zilizoandikwa juu yao ili uonekane kuwa unabii ulioongozwa na Yehova hasa. Lazima tangazo la “Amani na usalama!” liwe tukio lisilo na kifani, liwe tofauti na jitihada zile nyingi za kuleta amani ambazo zimekuwa zikifanywa kufikia wakati huo.

15. Kulingana na namna mambo yalivyo, ni nani atakayekuwa akisema “Amani na usalama”?

15 Pia, hao ‘wanaosema’ maneno ya “Amani na usalama!” muda mfupi tu kabla ya mwisho kuja ni kina nani? Haielekei kuwa kwamba sehemu yo yote ya ulimwengu huu ingeweza kutangaza jambo kama hilo bila kuungwa mkono au kuongozwa na zile mamlaka kubwa-kubwa za kisiasa. Kwa hiyo, inaonekana kwamba watawala wa mataifa watahusika sana katika utimizo wa unabii huo. Tengenezo la Umoja wa Mataifa, linalosemekana kuwa limejitokeza kuleta amani, huenda pia likahusika. Namna gani wanadini? Kwa sababu wao wamejifanya sana sehemu ya ulimwengu, ‘wakizini na wafalme wa dunia,’ inaelekea kuwa kwamba wataziunga mkono au washiriki wenyewe katika jitihada ambazo mamlaka za kisiasa zitafanya kuelekea upande huo. Kwa kufanya hivyo watakuwa wakiiga manabii wa uongo wa Yuda ya zamani waliotamka hivi kiuongo: “[Yehova] amesema, Mtakuwa na amani.” Badala ya kuwa na amani hiyo, baada ya muda mfupi Mungu angewaletea msiba mbaya, kama Yeremia nabii wake wa kweli alivyokuwa ametabiri.—Yeremia 23:16-22.

16, 17. (a) Je! inaelekea kuwa mataifa yanasonga mbele sasa yakalete “amani na usalama” wa namna yo yote? (b) Hata hivyo, kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba yatatangaza amani na usalama?

16 Lakini je! hivi majuzi mataifa yamekuwa yakisonga mbele kuelekea namna yo yote ya “amani na usalama”? Kutokana na habari za majuzi, huenda ikaonekana kwamba yamekuwa hayafanyi hivyo. Geoge Kennan, aliyekuwa balozi wa Amerkia kule Urusi, alisema hivi: “Kwa muda wa miaka 30 iliyopita msukosuko wa mambo ya kisiasa haujapata kuwa mwingi sana na hatari sana kama ulivyo leo. Muda wote huo hakujapata kuwako hali za kutokuelewana, za kuoneana mashaka, za kuvuruga akili na za hofu tupu ya mambo ya kijeshi” kama zilivyo leo. Ukurasa wa mhariri katika gazeti Star la Toronto uliongezea hivi: “Haikuwa hofu juu ya wakati ujao, bali ni jambo lenye kuonyesha dalili mbaya zaidi: Hofu juu ya wakati wa sasa.”

17 Katika miezi ya majuzi mamlaka (serikali) zile kubwa-kubwa zimelaumiana na kutishana. Fujo za raia, mapinduzi na vita ni mambo ambayo yametokea katika sehemu nyingi za dunia. Uchumi wa ulimwengu umefanyiwa mabadiliko mengi mpaka ukawa hauwezi kusimama mahali pamoja. Uhalifu na jeuri vimezidi kuongezeka mpaka vikaenea katika sehemu nyingi sana. Kwa uhakika, linaonekana kuwa jambo gumu kutazamia “watu” waseme “Amani na usalama!” kwa sababu ya mambo kwenda hivyo. Lakini Neno la Yehova halishindwi kamwe kutimia. (Isaya 55:11; 1 Wathesalonike 5:3, Today’s English Version; The Jerusalem Bible) Linapotuambia kwamba tukio hilo litafika kabla tu ya kufyatuka kwa “uharibifu wa ghafula,” basi ni hakika kwamba ndivyo itakavyokuwa, hata kama jambo hilo linaonekana kwa sasa kuwa gumu sana kutendeka.

18. Ni kwa njia gani unabii mbalimbali uliotolewa kuipinga Babeli ya kale unaweza kutusaidia tuamini unabii wa kisasa utatimizwa?

18 Ukumbuke unabii mwingi ambao Mungu aliongoza watumishi wake wautangaze kuipinga Babeli ya kale, mamlaka hodari ya ulimwengu iliyokuwako karne nyingi kabla ya Wakati wa Kawaida. Mwandikaji mmoja alikadiria kwamba ingekuwa vigumu sana unabii mkubwa-mkubwa wa kuipinga Babeli ya kale kutimia, akisema uwezekano ulikuwa wa nafasi moja kati ya nafasi 5,000,000,000! Bila shaka wengi wa watu wa Mungu katika nyakati za kale walishangaa unabii huo ungewezaje kutimizwa juu ya mamlaka ya ulimwengu ya Babeli, iliyo hodari na thabiti. Lakini ulitimizwa, ukatendeka kwa mapana na marefu. Kwa hiyo leo, huenda ikaonekana kama kwamba hakuwezi kutokea usemi wa “Amani na usalama!” halafu uharibifu wa taratibu ya ulimwengu. Lakini Neno la Mungu la unabii linatamka kwamba ndivyo itakavyokuwa!

NI KIDANGANYA-MACHO TU

19. Usemi wa “Amani na usalama” hautamaanisha nini?

19 Tunaweza kuwa na uhakika juu ya jambo hili: Ile kelele ya kutangaza “Amani na usalama!”—hata iwe itakuwa ya namna gani—haimaanishi kwamba hali inayoonyesha namna ulimwengu ulivyo kwa kweli itakuwa imebadilishwa. Wala haimaanishi kwamba mataifa yatatupa silaha zao au yaachilie mbali nia zao za ukatili. “Hapana amani kwa wabaya; asema Mungu wangu.” (Isaya 57:21) Maana yake ni kwamba, kwa muda huo tu viongozi wa ulimwengu wataupiga ukelele wa “Amani na usalama!” kwa njia ya wazi zaidi kuliko namna imepata kuwa hapo kwanza. Watafanya hivyo kwa sababu matatizo yatakuwa yamekwisha kuwalemea sana wakashindwa na la kufanya au kwa sababu wataona watafaidi nafsi zao kwa kuanzisha kanuni mpya za kuendesha mambo.

20. (a) Tunawezaje kuwa na uhakika sana kwamba hali za ulimwengu zitazidi kuharibika? (b) Tunaweza kutazamia watu walio wengi wafanye nini kwa habari ya ibada ya Mungu?

20 Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika mwingi hivyo kwamba ulimwengu huu utazidi kuharibika? Ni kwa sababu 2 Timotheo 3:1, 13 inatabiri kwamba katika hizi “siku za mwisho . . . watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu.” Kwa hiyo, usemi wa “Amani na usalama!” utakuwa kidanganya-macho tu. Hali ya kweli ya wanadamu haitabadilishwa na usemi huo. Ulimwengu huu unaoongozwa na Shetani hauna la kufanya ili kukomesha ongezeko kubwa sana la uhalifu na jeuri, wala hauna la kufanya ukomeshe kuvunjika-vunjika kwa jamaa, wala kubadili mambo ili uasherati uache kuenea kama unavyofanya, wala kuzuia mamilioni ya matendo ya kuua vitoto vingali tumboni mwa uzazi, wala kutatua lo lote la matatizo yale makubwa-makubwa ya wanadamu. (Yeremia 10:23) Wala watu walio wengi hawatageuka kwa ghafula wafuate ibada ya kweli ya Mungu. Unabii wa Biblia ulitaja kwa usahihi kwamba katika wakati wetu watu ‘wangependa anasa kuliko kumpenda Mungu. Kwa nje wangeonekana kama watu wenye kumcha Mungu, lakini wangeikana nguvu yake.’—2 Timotheo 3:4, 5, HNWW; angalia pia Mathayo 7:13, 14.

21. Watumishi wa Yehova watayafahamu matangazo yanayokuja ya “Amani na usalama!” kuwa yenye maana gani?

21 Hivyo, ingawa ulimwengu utadanganywa na matumaini ya bure tu wakati wa tangazo linalokuja la “Amani na usalama!” watumishi wa Yehova hawatadanganywa. Bali, wao watajua jambo lifuatalo juu ya utimizo unaokuja wa unabii huo: Watajua kwamba ni ishara ya mwisho yenye kuonyesha “dhiki kubwa” imekaribia kuanza! Wanajua, pia, kwamba “siku ya kisasi” cha Mungu itakapomalizika, watumishi wake waaminifu wataingia ndani ya taratibu mpya ya mambo yenye haki waanze maisha yasiyokoma wakiwa katika dunia iliyosafishwa itakayogeuzwa iwe paradiso. (2 Petro 3:13; Ufunuo 7:9-17) Wakati huu matukio hayo yenye kusisimua yanapozidi kutukaribia mbio-mbio, nia yetu inapasa kuwa nini?

[Maelezo ya Chini]

a Hiki ni kikundi cha watu wanaoheshimiwa kuwa wenye akili nyingi wanaochanganua hali za ulimwengu.

[Blurb katika ukurasa wa 15]

Watumishi wa Mungu hawatadanganywa na kelele inayokuja ya kutangaza “Amani na usalama!”

[Picha katika ukurasa wa 10]

Hali zilizopo duniani zinafanana na zile zilizokuwako kabla ya Gharika, wakati ambao dunia ‘ilijaa dhuluma’

[Picha katika ukurasa wa 12]

Hukumu ya Mungu juu ya dini ya uongo ni kali sana kwa sababu “dhambi zake zimefika hata mbinguni’’

[Picha katika ukurasa wa 13]

Hakuna jitihada zo zote za wakati uliopita katika kizazi chetu zimetimiza 1 Wathesalonike 5:2, 3 kwa sababu “uharibifu wa ghafula” haujaja bado

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki