Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • tp sura 8 kur. 86-93
  • Ni Nani Wataokoka?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni Nani Wataokoka?
  • Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mifano ya Zamani ya Kuokoka
  • Analotafuta Yehova Katika Mioyo ya Kibinadamu
  • Unaloweza Kufanya Sasa
  • Mfano wa Unabii Uliofananisha Wokovu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Kwanza Uharibifu wa Ulimwengu—Ndipo Amani ya Ulimwengu
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Waokolewa Wakiwa Hai Kupitia Dhiki Kubwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Je, Uko Tayari Kwa Ajili ya Wokovu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
Pata Habari Zaidi
Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
tp sura 8 kur. 86-93

Sura 8

Ni Nani Wataokoka?

1. (a) Kuokoka kwa mtu kuingia katika Mfumo Mpya wa Mungu wenye amani kutategemea nini? (b) Ufunuo sura ya 7 unaelezaje wale ambao wataokoka ili waishi duniani katika Paradiso?

KUOKOKA uharibifu wa ulimwengu unaokuja hakutakuwa jambo la nasibu, kama inavyotukia mara nyingi katika vita vya kibinadamu. Hakutaamuliwa na mahali anapoishi mtu. Wala hakutatokana na mtu kufanya haraka kukimbilia mahali fulani pa kujikinga na makombora au kimbilio jingine asikiapo mlio wa king’ora cha kuonya hatari. Kuokoka kutategemea rehema ya Mungu pamoja na uchaguzi wa mtu kabla ya kuanza “dhiki kubwa.” Wewe unaweza kufanyaje uchaguzi utakaokuweka miongoni mwa wale watakaookoka na kuishi duniani katika Mfumo Mpya wa Mungu wenye amani, wa kiparadiso?—Ufunuo 7:9, 10, 14, 15.

2. Ni nani awekaye masharti ya kuokokea, nayo yanapatikana wapi?

2 Biblia haitabiri tu kwamba kutakuwa na waokokaji wa uharibifu wa ulimwengu unaokuja. Inaandaa pia kielelezo cha kutusaidia tujue hao watakuwa watu wa namna gani. Kwa kuwa ni Mungu anayefanya iwezekane kuokoka, kwa kufaa yeye ndiye anayeyaweka masharti.

3. Ili kuweko amani na usalama, ni kwa sababu gani inahitajiwa kabisa watenda maovu wakatiliwe mbali?

3 Kwa hekima na kwa haki Mungu atahakikisha kwamba watakaookoka ni watu ambao watakuwa rasilimali katika Mfumo Mpya wake, si wale ambao wangeuletea madhara. Kama angeacha watu wasio waadilifu waokoke, kusingekuwa na amani na usalama kwa waadilifu. Makao na usalama wao wa kibinafsi bado yangehatarishwa. Lakini Biblia inaahidi hivi: “Watenda mabaya wataharibiwa, bali wamngojao [Yehova, NW] ndio watakaoirithi nchi.” Mungu akitumia kwa ukamilifu tu kiwango hicho, kama kilivyoonyeshwa wazi kwenye Zaburi 37:9-11, hapo ndipo waokokaji watakapoweza ‘kujifurahisha kwa wingi wa amani.’ Namna Mungu atakavyofanya hilo inaonwa katika pindi zilizopita wakati uovu wa wanadamu ulipomtia Mungu katika wajibu wa kuleta uharibifu.

Mifano ya Zamani ya Kuokoka

4-6. (a) Ni nini linaloshuhudia kwamba uharibifu wa Yerusalemu katika 70 W.K. ni uhakika wa kihistoria? (b) Kwa sababu gani uharibifu huo ulikuja? (c) Ni jambo gani lililowezesha wanafunzi wa Yesu waponyoke?

4 Katika mji wa Roma leo lingali linasimama tao la tangu karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida, lile Tao la Tito. Katika tao hilo pana picha inayoonyesha vitu vikichukuliwa kutoka hekaluni Yerusalemu baada ya ule uharibifu wa 70 W.K. Kwa sababu hiyo uharibifu huo ni uhakika wa kihistoria. Jambo lililo uhakika wa kihistoria pia ni kwamba makumi ya miaka kabla ya uharibifu huo Yesu Kristo alikuwa ametabiri kwamba ungekuja na namna watu wangeweza kuuokoka.

5 Watu wa Kiyahudi walikuwa wamegeuka wakamwacha Mungu ili wafuate wanadamu na mapokeo ya kidini yaliyofanywa na mwanadamu. (Mathayo 15:3-9) Waliweka tumaini lao hakika katika watawala wa kisiasa wa kibinadamu badala ya katika Ufalme wa Mungu ulioahidiwa. (Yohana 19:15) Walifikia hatua ya kuukataa na kuupinga ukweli uliotangazwa na Mwana wa Mungu na mitume wake. Yesu alionya juu ya matokeo ambayo mwendo huo ungeyaleta.—Mathayo 23:37, 38; 24:1, 2.

6 Matokeo yalikuwa sawasawa kama yalivyotabiriwa. Katika mwaka 66 W.K. Wayahudi waliasi Roma. Baada ya Waroma kufanya shambulio la kwanza juu ya Yerusalemu walianza safari isiyotazamiwa ya kurudi kwao. Jambo hilo lilikuwa ndilo kile kiishara na nafasi kwa waliomwamini Yesu wafanye alilokuwa amesema: Kimbieni—tokeni katika mji uliohukumiwa maangamizi na katika mkoa wote wa Uyahudi, hata kama ni kitu gani kingekuwa lazima kiachwe nyuma. Wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo walifanya jambo lilo hilo. Ndipo, katika mwaka 70 W.K., Warumi wakarudi, na wakiisha kuuzingira, wakauharibu Yerusalemu na wale waliokosa kusikiliza. Mwanahistoria Myahudi Yosefu, shahidi aliyeona mwenyewe, anasema kwamba watu 1,100,000 katika Yerusalemu walikufa kwa njaa kuu, magonjwa, magombano ya wenyewe kwa wenyewe, au kwa upanga wa Waroma. Lakini Wakristo wale waliochukua hatua ya uhakika waliponyoka.—Luka 19:28, 41-44; 21:20-24; Mathayo 24:15-18.

7. Iliwahitaji watu wafanye nini ili waokoke wakati Babuloni ilipoharibu taifa la Kiisraeli?

7 Hali inayofanana na hiyo ilikuwa imekuwako karibu karne saba mapema wakati Yehova Mungu aliruhusu majeshi ya Kibabuloni chini ya Mfalme Nebukadreza (wa Pili) yaliharibu taifa la Kiisraeli. Uharibifu huo, pia, ni historia yenye maandishi ya kuithibitisha. Kwa muda wa miaka mingi kabla ya hapo, Mungu kupitia kwa manabii wake alikuwa amewaonya watu hao waasi-imani kwamba mwendo wao ulikuwa ukiongoza kwenye afa. Mwito wa Mungu kwao ulikuwa, “Geukeni, geukeni kutoka njia zenu mbaya, kwa maana mbona iwapase ninyi kufa?” (Ezekieli 33:11, NW) Walio wengi hawakuamini onyo hilo. Na hata wakati majeshi ya Babuloni yalipozingira Yerusalemu, Waisraeli hao bado waliendelea kutumaini kwamba uharibifu usingekuja. Lakini ulitukia kama ulivyotabiriwa. Hata hivyo Mungu alihakikisha kwamba wale walioonyesha imani yao kwa kutii walihifadhiwa.—Yeremia 39:15-18; Sefania 2:2, 3.

8-10. (a) Kwa sababu gani Yehova alileta uharibifu wa ulimwengu katika siku za Noa? (b) Kwa sababu gani Noa na jamaa yake waliachiliwa?

8 Nyuma zaidi katika historia ya kibinadamu tunapata wonyesho wa kwanza kabisa wa kielelezo cha kimungu cha kuokokea! Hakikuhusu, uharibifu wa taifa moja tu bali wa ulimwengu. Na huo pia ni uhakika wa kihistoria, unaohusu Gharika ya duniani pote wakati wa miaka 2370/2369 K.W.K., katika siku za Noa. Biblia inasema hivi juu ya hali zilizokuwako kabla ya uharibifu huo wa ulimwengu: “Kwa hiyo Yehova akaona kwamba ubaya wa mwanadamu ulikuwa tele katika dunia na kila elekeo la fikira za moyo wake lilikuwa baya tu wakati wote. Na dunia ikaja kuharibika machoni pa Mungu wa kweli na dunia ikawa yenye kujazwa jeuri.”—Mwanzo 6:5, 11, NW.

9 Uovu na jeuri hiyo ulimtia Mungu katika wajibu wa kuchukua hatua. Noa na jamaa yake peke yao ndio walioonyesha imani na utii. Kwa sababu ya kuwaonea rehema, na ili ahifadhi haki na uadilifu duniani, Yehova Mungu “hakukosa kuadhibu ulimwengu wa kale . . . wa watu wasiomwogopa Mungu.” Tokeo lilikuwa kwamba ‘ulimwengu ule wa wakati huo ulipatwa na uharibifu ulipogharikishwa kwa maji.’—2 Petro 2:5; 3:5-7, NW.

10 Hata hivyo Noa na jamaa yake waliokoka. Kwa sababu gani? Kwanza, wao hawakufuatana na huo “ulimwengu wa watu wasiomwogopa Mungu” katika ukosefu wao wa uadilifu. Hawakujiacha wajitie sana katika mambo ya kawaida ya maisha, kula, kunywa, kufunga ndoa, hata wawe wasiojali mapenzi ya Mungu au wasiosikia onyo lake. Noa ‘alitembea na Mungu’ katika uadilifu. Hilo halikumaanisha kwamba yeye na jamaa yake walijizuia tu kufanya madhara. Bali, walichukua hatua ya uhakika kufanya mambo yaliyofaa. Waliamini kikweli yale ambayo Mungu alisema, na walionyesha hivyo kwa kujenga safina kubwa sana yenye ghorofa tatu iliyokuwa na urefu wa futi zaidi ya 400. Noa alichukua hatua hakika pia kwa kuwa “mhubiri wa uadilifu,” akiambia wengine juu ya makusudi ya Mungu, akiitetea njia ya uadilifu.—Mwanzo 6:9, 13-16; Mathayo 24:37-39; Waebrania 11:7, NW.

11. Kama inavyoonyeshwa na mifano hiyo yenye kuonya, ni lazima sisi tufanye nini ikiwa tutaokoka uharibifu wa ulimwengu unaokuja?

11 Watu hao wanane waliokoka kwa sababu ya imani na kazi zao zenye kutokana na imani. Yesu na mitume wake walirejeza kwenye uharibifu huo wa ulimwengu kuwa wenye maana ya kiunabii ya jambo linalowaelekea watu katika huu “wakati wa mwisho.” Kwa hiyo ni wazi kwamba lazima sisi pia tujiondoe katika ushirika wa ulimwengu unaoelekea kwenye uharibifu, sawa na walivyofanya Noa na jamaa yake. Sisi pia lazima tuishi kupatana na mapenzi ya Mungu. Hatuwezi kuongozwa na kanuni zetu wenyewe tu na kutazamia kuokoka. Neno la Mungu linasema: “Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu; lakini mwisho wake ni njia za mauti.” (Mithali 16:25) Wala kuwa na sura yo yote ya kujionyesha kijuujuu tu kuwa na uadilifu hakutaokoa mtu. Kwa maana Yehova anaona yaliyo katika moyo.—Mithali 24:12; Luka 16:15.

Analotafuta Yehova Katika Mioyo ya Kibinadamu

12, 13. (a) Ni hali gani zinazofanya watu wengi watake badiliko? (b) Kwa sababu gani jambo hilo halitoshi kuwahakikishia kuokoka kwao kuingia katika Mfumo Mpya wa Mungu? (c) Ili tuwe miongoni mwa waokokaji, ni jambo gani ambalo lazima litusukume kuona kihoro juu ya hali mbaya za sasa?

12 Watu wengi hawafurahii hali za sasa, na wanaonyesha hivyo kwa malalamiko, maandamano ya kupinga, na katika nchi fulani-fulani kwa uasi wenye jeuri. Wengi wanachukizwa sana na kodi ya juu na gharama ya maisha inayopanda sana. Wanaonyesha masikitiko makubwa kwa sababu ya hatari ya uhalifu. Woga unawafanya watake badiliko. Lakini, je! hilo linatosha kuwahakikishia wataokoka waingie katika Mfumo Mpya wa Mungu? Hapana, halitoshi. Kwa sababu gani?

13 Kwa sababu mtu angeweza kutofurahia hali hizo lakini awe mwenye ubinafsi. Huenda hata akakubali namna fulani za ukosefu wa unyofu na wa adili—mradi yeye mwenyewe hataabiki. Hata hivyo, watu wenye mioyo inayofaa wanaona mambo kwa njia tofauti. Wanapojifunza Biblia wanaona kwamba hali mbaya ni dalili za nje tu za ugonjwa wenyewe hasa wa ulimwengu. Wanafahamu kwamba dalili hizo zinaonyesha kutokujali kuyajua na kuyafanya mapenzi ya Mungu na kutokujali kuishi kulingana na viwango vyake vya uadilifu. Kwa hiyo, wao hawaingiwi na kihoro kwa sababu hasa ya madhalimu ya kijamii, uhalifu, uchafuzi, au tisho la vita. Bali, watu hao wenye mioyo inayofaa wanaingiwa na kihoro hasa kwa kuona jina la Mungu likiharibiwa sifa na mwendo wa ufisadi wa wanadamu. Na wanaingiwa na kihoro kwamba wengine, si wao wenyewe tu, wanataabika sana kutokana na mambo hayo.

14. Ni akina nani ‘waliotiwa alama’ ya kuokokea wakati wa Yerusalemu kuharibiwa na Wababuloni?

14 Ili tuokoke uharibifu wa ulimwengu unaokuja, ni lazima tuwe kama wale ambao waliachiliwa wakati Babuloni ilipoharibu Yerusalemu katika 607 K.W.K., watu ambao maelezo yanawasema kuwa “wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote” yenye kufanywa katika mji huo. (Ezekieli 9:4) Hali zilikuwa ‘za kuchukiza’ kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, maskini walikuwa wakigandamizwa, wengine hata wakishikiliwa na wananchi wenzao isivyo halali katika utumwa. (Yeremia 34:13-16) Hali ya kiadili ya ufalme wa Yuda ilikuwa imekuwa mbaya hata zaidi ya ile ya ufalme wa Israeli, iliyoelezwa mapema zaidi na nabii Hosea kuwa hivi: “Kuna kutamka malaana na kuzoea udanganyifu na kuua na kuiba . . . na vitendo vya umwagaji damu vimegusa vitendo vingine vya umwagaji damu.” (Hosea 4:2; Ezekieli 16:2, 51, NW) Wale peke yao walioingiwa na kihoro moyoni kwa sababu ya ukosefu huo wa uadilifu na wa heshima kwa Mungu ndio ‘waliotiwa alama’ ya kuokokea.—Ezekieli 9:3-6.

15. Ni nini kinachozuia watu fulani wasifanye mabadiliko yanayohitajiwa ili kuokoka uharibifu wa ulimwengu unaokuja?

15 Ingawa wengi leo wangependa wafurahie milele uzima duniani katika amani, ufanisi, na faraja, wao hawataki kufanya mabadiliko ambayo kujifunza na kufuata kielelezo cha Biblia kwa mambo yanayofaa kungeleta katika njia yao ya maisha. Katika marefu ya kina cha moyo wao, kwa kweli hawapendi uadilifu wala hawajali wanadamu wenzao kwa moyo mweupe. Kwa kuwa Mfumo Mpya wa Mungu utatokeza jamii mpya ya kidunia ambamo “uadilifu utakaa,” habari njema zinazouhusu zinawavutia wale tu wanaopenda uadilifu. Wengine wanahisi wakilaumiwa nazo.—2 Petro 3:13; 2 Wakorintho 2:14-17, NW.

Unaloweza Kufanya Sasa

16-18. (a) Mtu anakujaje kuwa ‘aliyetiwa alama’ ya kuokokea? (b) Ni hatua gani anayopaswa achukue, juu ya ibada ya uwongo, halafu juu ya ibada ya kweli? (c) Lazima aoneje mashirika ya kisiasa kama vile UM?

16 Yehova atahifadhi wale tu wanaotaka kwa moyo mweupe kuishi chini ya utawala wake wenye uadilifu. Yeye hatalazimisha watu wo wote waishi wakati huo chini ya hali ambazo wao wenyewe hawazitaki. Basi, wale watakaohifadhiwa ni wale watakaoonyesha ukubali wao wa kweli wa utawala wake wa kimungu sasa. Wanakuwa ‘waliotiwa alama’ ya kuokokea kwa kuuvaa “utu mpya” wa Kikristo, wakipatanisha maisha zao na njia za Mungu na kutoa ushahidi wa kwamba kweli wao ni wanafunzi wa Mwana wa Mungu. Kwa njia hiyo ‘wanachagua uzima’ na baraka, si kifo. (Wakolosai 3:5-10; Kumbukumbu 30:15, 16, 19) Wewe utachagua nini?

17 Uchaguzi wako unahusu kujiweka chini ya Mungu katika ibada. Yesu alisema: “Saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu.” (Yohana 4:23) Basi kuokoka uharibifu wa ulimwengu unaokuja kunataka mtu aache ibada yote ya uwongo na ashiriki katika ibada ya kweli. Pia, waokokaji hawatapatikana miongoni mwa wale wanaoweka tumaini lao katika Umoja wa Mataifa au mashirika mengine ya kisiasa, kwa kuwa hayo ni sehemu ya ulimwengu utakaoharibiwa.—Ufunuo 17:11; 18:17-21.

18 Baraka zisizo na mwisho zinawangoja wale wanaochukua mwendo unaoongoza kwenye kuokolewa. Fikiria sasa mengine kati ya mambo makubwa ambayo Mungu anawaahidia wale wanaoliamini Neno lake na kuthibitisha imani hiyo kwa kuchukua hatua ya uhakika.

[Picha katika ukurasa wa 87]

“Mkutano mkubwa” utaokoka uharibifu wa ulimwengu ili waishi duniani katika Mfumo Mpya wa Mungu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki