Sura 15
Kwa Sababu Gani Kujali Yale Yanayowapata Watu Wengine?
1. (a) Ni nini kimewafanya watu wengi wajifikirie wenyewe tu na wasiwajali sana watu wengine? (b) Matokeo yamekuwa nini?
KUJALI hali ya wengine bila ubinafsi hakuonekani sana leo. Ijapokuwa kila mtu anazaliwa akiwa na uwezo wa kupenda, wakati wengine wanapotumia hali ili wajifaidi wenyewe isivyo haki, au wakati jitihada za mtu mwenyewe za kuonyesha upendo zinapoeleweka vibaya, huenda akaamua kwamba njia bora ni kujifikiria yeye mwenyewe tu. Watu wengine, wanapoona kwamba mara nyingi wale wanaotumia wanadamu wenzao kujifaidi wenyewe wanafanikiwa kwa vitu vya kimwili, huenda wakafikiri hii ndiyo njia ya kufanikiwa. Matokeo ni kwamba watu wengi wana roho fulani ya kutotumainiana na wana marafiki wachache wa kweli, iwapo wanao wo wote. Ni nini kinachosababisha hali hii isiyo na furaha?
2. (a) Biblia inatambulishaje mzizi wa tatizo hilo? (b) Maana yake nini kumjua Mungu?
2 Kinachokosekana ni upendo, aina ya upendo unaojionyesha wazi kwa kujali masilahi ya daima ya wengine. Na kwa sababu gani unakosekana? Ikilitaja shina la tatizo lenyewe, Biblia inasema hivi: “Yeye asiyependa, hakumjua Mungu, kwa maana Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Ni kweli kwamba watu mmoja mmoja wenye kutafuta faida yao wenyewe wanajidai kumwamini Mungu hata kuhudhuria kanisani. Lakini ukweli ni kwamba wao hawamjui Mungu kweli kweli. Kumjua Mungu kunamaanisha kuujua sana utu wake, kuikubali mamlaka yake, kisha kutenda kupatana na yale tunayojua juu yake. (Yeremia 22:16; Tito 1:16) Kwa hiyo, basi, ili tupate mfurahio wa kweli wa maisha unaokuja wakati tu mtu anapoonyesha wengine upendo na kuupokea kutoka kwao pia, lazima tupate kumjua Mungu vema na kuyatumia tunayojifunza.
3. Mungu ameonyeshaje upendo wake mkuu kwa wanadamu?
3 “Katika hili pendo la Mungu lilionekana kwetu, kwamba Mungu amemtuma Mwanawe pekee ulimwenguni, ili tupate uzima kwa yeye,” akaandika mtume Yohana. “Hili ndilo pendo, si kwamba sisi tulimpenda Mungu [kwanza], bali kwamba yeye alitupenda sisi, akamtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu. Wapenzi, ikiwa Mungu alitupenda sisi hivi, imetupasa na sisi kupendana.” (1 Yohana 4:9-11) Mungu hakuuacha mwendo wa wanadamu usio wa upendo uuzime upendo wake mwenyewe. Kama inavyoelezwa kwenye Warumi 5:8, NW: “Mungu anapendekeza upendo wake mwenyewe kwetu sisi kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.”
4. Hiyo inakufanya wewe binafsi uhisi namna gani juu ya Mungu?
4 Ni watu wangapi uwapendao sana ambao ungetoa uhai wako kwa ajili yao—watu ambao hawajapata kukufanyia wewe lo lote? Ikiwa wewe u mzazi, ungetaka mtoto wako afie nani? Hiyo ndiyo aina ya upendo ambao Mungu alionyesha kwa ajili yetu. (Yohana 3:16) Kujua hilo kunakufanya uhisi namna gani juu ya Mungu? Ikiwa tunathamini kweli kweli jambo ambalo amefanya, tutaona kwamba si mzigo kutii amri zake.—1 Yohana 5:3.
5. (a) Ni nini “amri mpya” ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake? (b) Kujitolea Mungu kwetu akiwa mtawala kunahusikaje katika amri hiyo? (c) Basi, utii kwa hiyo “amri mpya” unataka nini?
5 Usiku uliotangulia kifo chake, Yesu aliwapa wanafunzi wake mojapo amri hizo. Ingewatambulisha kama walio tofauti na sehemu nyingine yote ya ulimwengu. Alisema hivi: “Amri mpya nawapa, Mpendane.” Amri ya Yesu ilikuwa “mpya” kwa sababu alikuwa akisema wapende wengine, si kama vile walivyojipenda wenyewe tu, bali “kama vile nilivyowapenda ninyi”—kuwa na nia ya kutoa uhai wao kwa ajili ya mtu na mwenzake. (Yohana 13:34, 35; 1 Yohana 3:16) Upendo wa aina hiyo unaonyesha sisi tumejitolea Mungu kwa kulithibitisha kuwa la uwongo dai la Ibilisi kwamba hakuna mwanadamu atakayetii Mungu kwa kuhatarisha uhai wake mwenyewe. (Ayubu 2:1-10) Kwa wazi, kutii “amri mpya” hiyo kunataka kujaliana kwa kina kirefu.—Yakobo 1:27; 2:15, 16; 1 Wathesalonike 2:8.
6. Upendo unapasa uonyeshwe kuelekea nani wengine, na kwa sababu gani?
6 Lakini Kristo aliufia ulimwengu wa wanadamu, si wanafunzi wake tu. Hivyo Maandiko yanahimiza hivi: “Kadiri tupatavyo nafasi na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.” (Wagalatia 6:10) Nafasi za ‘kuwatendea watu wote mema’ zinazuka kila siku. Upendo wetu usipokuwa mnyimivu, lakini mkunjufu na mkarimu, tunamwiga Mungu, “kwa kuwa yeye anafanya jua lake liinuke juu ya watu waovu na wema na kufanya inyeshe juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.”—Mathayo 5:43-48, NW.
Kuheshimu Miili na Mali za Wengine
7. Ni jambo gani ambalo huenda likaongoza namna tunavyotendea miili na mali za watu wengine?
7 Tunaishi katikati ya ulimwengu usio na upendo. Pengine wewe unaona kwamba si sikuzote umekuwa mwenye kufikiria wengine kama ambavyo ungaliweza kufanya. Lakini ikiwa mtu anataka amtumikie Mungu, anahitaji kudhamiria ajitahidi ‘kubadili akili yake.’ (Warumi 12:1, 2, NW) Anahitaji kubadili mwelekeo wake juu ya miili na mali za wengine.
8. (a) Ni nini kinachoonyesha kutojali mali za wengine mahali pote? (b) Ni shauri gani katika Biblia, ikiwa linafuatwa, lingeweza kuzuia mtu asifanye mambo hayo?
8 Katika maeneo fulani kuna kutojali sana mali za watu wengine. Vijana wanaharibu mali za wenyewe na za serikali ili waone raha tu. Au wanaharibu kwa makusudi uzuri wa vitu ambavyo wengine wamefanyia kazi kwa bidii wavipate. Watu wengine, huenda wakafadhaishwa na uharibifu huo wa mali za wengine, hata hivyo wao washiriki kuuleta kwa kutupa-tupa takataka katika bustani za starehe, barabarani, au katika majengo ya serikali. Je! matendo hayo yanapatana na onyo la upole la Yesu: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo”? (Mathayo 7:12) Mwenendo huo usio wa upendo unaonyesha kwamba mtu hapatani kwa ukamili na kusudi la Mungu kwa dunia hii kuwa paradiso.
9. (a) Wivi unakuwa na matokeo gani juu ya maisha za watu wote? (b) Kwa sababu gani wivi ni mbaya machoni pa Mungu?
9 Kujali uhai wa mtu na mali yake kunafanya iwe kawaida mahali pengi kufunga milango kwa kufuli, kufunga madirisha kwa makomeo, kuwa na mbwa-walinzi. Maduka yanapandisha bei yalipie vitu vilivyoibwa. Lakini wivi hautakuwa na nafasi katika Mfumo Mpya wa Mungu. Kwa sababu hiyo, watu wo wote wanaotumaini kuwa humo lazima wajifunze kuishi sasa kwa njia ambayo itashiriki kuwaletea usalama wanadamu wenzao. Biblia inaonyesha kwamba “zawadi ya Mungu” ni kwamba mwanadamu ‘aone mema kwa ajili ya kazi yake yote ya bidii.’ Kwa hiyo ni kosa kujaribu kumnyima matokeo ya kazi yake. (Mhubiri 3:13, 5:18, NW) Watu wengi waliokuwa wakosefu wa unyofu wakati uliopita wamebadilika. Hawajiepushi tu na wivi; bali wamejifunza pia furaha ya kuwapa wengine. (Matendo 20:35) Wakiwa na tamaa ya kumpendeza Mungu, wameyathamini moyoni yaliyoandikwa kwenye Waefeso 4:28: “Mwibaji asiibe tena; bali afadhali afanye juhudi, akitenda kazi iliyo nzuri kwa mikono yake mwenyewe, apate kuwa na kitu cha kumgawia mhitaji.”
10. (a) Tunaweza kuonyeshaje tunawafikiria wengine kwa namna tunavyosema nao? (b) Ni nini kitamsaidia mtu ajifunze kuonyesha upendo kwa njia hiyo?
10 Mara nyingi, hasa wakati mambo yanapoharibika, wanachohitaji wengine si kitu cha kimwili, bali wanahitaji fadhili. Hata hivyo, wakati makosa ya mtu yanapoonekana, ni nini kinachotukia mara nyingi? Huenda kukawa na mifoko mikali ya hasira, usemi wa matusi, au maneno yenye kuchoma. Hata wengine wanaokubali kwamba hilo ni kosa wanashindwa kuzuia ulimi wao. Mtu anaweza kushindaje tabia hiyo? Hasa kinachokosekana ni upendo, na hiyo yaonyesha uhitaji wa kupata kumjua Mungu. Wakati mtu anapothamini kadiri ambavyo Mungu amemtendea yeye rehema, hataona ni vigumu sana kusamehe wengine. Huenda hata akaanza kuona njia za kumsaidia mkosaji, akimtolea msaada wa fadhili ili afanye maendeleo.—Mathayo 18:21-35; Waefeso 4:31–5:2.
11. Kwa sababu gani tusiwe wenye matusi katika usemi wetu, hata wakati wengine wanapokuwa hawatutendei fadhili?
11 Ni kweli kwamba huenda watu wengine wasitumie shauri hilo jema kutoka Neno la Mungu katika shughuli zao pamoja nasi. Yajapokuwa makusudio yetu ya moyo mweupe, huenda nyakati fulani tukajikuta kwamba sisi ndio wenye kutendwa vibaya nao. Tutafanyaje wakati huo? Biblia inashauri hivi: “Usijiache mwenyewe ushindwe na lililo ovu, bali endelea kushinda lililo ovu kwa lililo jema.” (Warumi 12:17-21; 1 Petro 2:21-23, NW) Fadhili zenye kuendelea upande wetu huenda baada ya muda zikaulainisha mwelekeo wao na kutokeza sifa zao bora. Vyo vyote watakavyoitikia, wakati sisi tunapoendelea kutokeza wazi fadhili, tunaonyesha kwamba tunaitegemeza njia ya Mungu ya kutawala, ambayo msingi wake ni upendo.
Kushinda Ubaguzi wa Kikabila, Kitaifa na Kijamii
12, 13. Biblia inasaidiaje mtu aondoe hisia zo zote za ubaguzi usio na msingi mzuri, wa kikabila, kitaifa au kijamii?
12 Mtu aliye na upendo wa kweli hauonyeshi kwa kuvutwa na kabila la watu, rangi ya ngozi, utaifa wao wala cheo walicho nacho katika hali ya kijamii. Kwa sababu gani sivyo? Kwa sababu anauthamini ukweli wa Biblia kwamba “[Mungu] alifanya kila taifa la wanadamu kutoka katika mmoja.” (Matendo 17:26) Basi wanadamu wote wana ukoo mmoja. Hakuna kabila wala taifa lililo bora kuliko jingine katika asili ya urithi.
13 Hakuna mtu aliye na sababu yo yote ya kujisifu kwa sababu ya ubabu wa jamaa yao, kabila, rangi, utaifa au cheo katika maisha. “Wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Warumi 3:23, NW) Basi kila mtu ana tegemeo juu ya dhabihu ya ukombozi ya Kristo. Na Biblia inaonyesha kwamba wale watakaoachiliwa waipite “dhiki kubwa” inayokuja wanatoka katika “kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.”—Ufunuo 7:9, 14-17.
14. Kwa sababu gani jambo baya lililokupata mwenyewe si msingi unaofaa wa kuonyesha ubaguzi dhidi ya watu wa kabila au taifa fulani?
14 Akijaribu kutetea ubaguzi wake usio na msingi mzuri, huenda mtu akakumbuka jambo fulani baya alilotendwa na mtu fulani wa kabila au taifa fulani. Lakini je! kila mtu wa kabila au taifa hilo alihusika katika kosa hilo? Na je! si watu wa kabila au taifa la mtu mwenyewe wamekuwa wenye hatia ya mambo ayo hayo? Ikiwa tunatumaini kuishi katika Mfumo Mpya wa Mungu wenye amani, tunahitaji kusafisha mioyo yetu iondokwe na kiburi cho chote kinachoelekea kutenganisha urafiki wetu na watu wengine.
15. Kama maelezo ya mtu juu ya kabila au utaifa yangekwaza mwamini mwenzake, jambo hilo lingekuwa na matokeo gani juu ya msimamo wake mwenyewe mbele za Mungu na Kristo?
15 Yaliyomo mioyoni mwetu yanakuja kutokeza siku moja katika vinywa vyetu. Kama vile Kristo Yesu alivyosema: “Mtu, kinywa chake hunena yale yaujazayo moyo wake.” (Luka 6:45) Namna gani kama maneno yenye kuonyesha ubaguzi usio na msingi mzuri yangekwaza mtu aliyekuwa akionyesha kupendezwa na tengenezo la Yehova? Jambo hilo ni zito sana hivi kwamba Yesu alionya hivi: “Ye yote atakayemkosesha mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, afadhali afungiwe jiwe la kusagia shingoni mwake, na kutupwa baharini.”—Marko 9:42.
16. Yesu alionyeshaje kutopendelea ambako imetupasa tuonyeshe watu wengine?
16 Wakristo wana wajibu wa kuonyesha kupendezwa na wengine bila kujali kabila, utaifa au cheo katika maisha. (Yakobo 2:1-9) Ni kama Yesu alivyohimiza: “Ufanyapo karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa [mwenye furaha, NW], kwa kuwa hao hawana cha kukulipa.” (Luka 14:13, 14) Kwa kuwa na upendezi huo wa kuwajali wengine, tunazionyesha sifa zenye upendo za Baba yetu wa kimbingu.
Kupendezwa kwa Upendo na Masilahi ya Milele ya Wengine
17. (a) Ni kitu gani chenye thamani zaidi ya vyote tunachoweza kukishiriki na wengine? (b) Kwa sababu gani tuhisi tukisukumwa na moyo kufanya hivyo?
17 Kuwajali kwetu wengine hakupasi kuwe juu ya mahitaji yao ya kimwili tu. Wala upendo wetu usingekuwa kamili kwa sababu tu sisi ni wenye fadhili kwa watu wa namna zote. Ili maisha yawe na maana kweli kweli, watu wanahitaji kujua Yehova na makusudi yake. Katika sala kwa Baba yake, Yesu alisema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” (Yohana 17:3) Ikiwa umekisoma kitabu hiki tangu mwanzo, unajua namna ya kuipata zawadi hiyo. Umejionea mwenyewe yale ambayo Maandiko yanatabiri juu ya “dhiki kubwa,” na mashuhuda yaonekanayo yanayohakikisha kukaribia kwayo. Unajua kwamba Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee kwa wanadamu. Lakini je! upendo kwa Yehova na kwa mwanadamu mwenzako unakusukuma utake kuyashiriki maarifa hayo muhimu pamoja na wengine?
18. (a) Kwenye Mathayo 24:14, ni kazi gani aliyotabiri Yesu kwa siku zetu? (b) Yatupasa tuoneje juu ya kushiriki katika kazi hiyo?
18 Alipokuwa akisema juu ya “umalizio wa mfumo wa mambo” Yesu alitabiri hivi: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia nzima yote inayokaliwa kwa ajili ya ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakuja.” (Mathayo 24:3, 14, NW) Lo! ni pendeleo kama nini kumwakilisha Mtawala Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima, Yehova mwenyewe, wakati mtu anaposhiriki katika “ushuhuda” huo! Nafasi ya kushiriki katika kazi hii ya pekee ingali wazi, lakini si kwa muda mrefu zaidi.
19. Kwa sababu gani tusiruhusu hisia yo yote ya kukosa uwezo wa kibinafsi ituzuie tusishiriki katika kazi hiyo?
19 Unapolifikiria taraja la kushiriki katika kazi hii ya “ushuhuda kwa mataifa yote,” ni vema kujua kwamba si uwezo wa mtu wa kibinafsi, bali ni Mungu anayesababisha ujumbe huo uzae matokeo. (Matendo 16:14; 1 Wakorintho 3:6) Ikiwa wewe unasukumwa na moyo wenye nia ya kupenda, Yehova anaweza kukutumia utimize mapenzi yake. Kama alivyosema mtume Paulo: “Na tumaini hilo tunalo mbele za Mungu kwa njia ya Kristo. Si kwamba twatosha sisi wenyewe kufikiri neno lo lote kwamba ni letu wenyewe, bali utoshelevu wetu watoka kwa Mungu.”—2 Wakorintho 3:4-6.
20. (a) Je! kila mtu ataziitikia habari njema kwa kupendezwa? (b) Ni faida gani inayotimizwa kwa kuwahubiri watu walio baridi au hata wapinzani?
20 Bila shaka, tusitazamie kwamba kila mtu ataitikia kwa kupendezwa. Wengi watakuwa baridi. Wengine watapinga. Hata hivyo wanaweza kubadilika. Sauli wa Tarso, ambaye wakati mmoja alikuwa mtesi wa Wakristo, alikuja kuwa mtume wa Yesu mwenye bidii. (1 Timotheo 1:12, 13) Kama wengine wanaujua au hawaujui, wanauhitaji ujumbe wa Ufalme. Kwa hiyo tunapaswa kuwajali, tukiwa na nia ya kujitoa tuongezee masilahi yao ya daima. (1 Wathesalonike 2:7, 8) Hata wasipoutaka ujumbe wa Ufalme, bado mema fulani yanatimizwa. Ushuhuda unatolewa, jina lake Yehova linatukuzwa, ‘kubaguliwa’ kwa watu kunafanywa, nasi tunaonyesha ushikamanifu wetu wenyewe kwa Yehova.—Mathayo 25:31-33.
Kujali Yanayoipata Jamaa Yako Mwenyewe
21. Ni daraka gani alilo nalo kichwa cha jamaa kwa habari ya masilahi ya kiroho ya jamaa yake?
21 Jitihada zako za kusaidia wengine wapate manufaa kutokana na maandalizi yenye upendo ya Yehova zinapasa zielekezwe kwa jamaa yako pia. Kwa mfano, kichwa cha jamaa ana daraka kwa ukuzi wa kiroho wa jamaa. Hiyo inaongozwa moja kwa moja na ukawaida wa mipango yake kwa mazungumzo ya jamaa ya Neno la Mungu. Na wakati sala za baba kwa ajili ya jamaa zinapoonyesha kina kirefu cha kujitoa na kuwa na shukrani, hiyo inaweza kuufinyanga mwelekeo wa jamaa nzima.
22. Kwa sababu gani ni jambo la maana baba awatie nidhamu watoto wake, na ni nini kinachopasa kumsukuma afanye hivyo?
22 Daraka lake linatia na kutoa nidhamu pia. Matatizo yanapotokea, huenda ikaelekea kuwa rahisi zaidi kuyapuuza. Lakini ikiwa nidhamu inatolewa wakati tu baba anapoudhika, au ikiwa matatizo yanatatuliwa wakati yanapokuwa mazito tu, pana jambo linalokosekana. Inasema hivi Mithali 13:24: ‘Baba ampendaye mwanawe humrudi mapema.’ Kwa sababu hiyo baba mwenye upendo anatoa nidhamu bila ugeugeu. Yeye anawaeleza watoto wake mambo kwa subira na kufikiria udhaifu wa kiakili, wa kimoyoni na wa kimwili wa watoto wake. (Waefeso 6:4; Wakolosai 3:21) Ikiwa wewe ni baba, je! wewe una upendo wa aina hiyo kwa watoto wako? Je! una nia ya kuchukua daraka hili, ukiwa unafikiria si wakati huu tu bali pia masilahi ya wakati ujao wa jamaa yako?—Mithali 23:13, 14; 29:17.
23. Mama anaweza kushirikije kuongezea masilahi ya kiroho ya jamaa yake?
23 Mke, pia, anaweza kushiriki sana kuleta hali njema ya jamaa. Ushirikiano wake na mumeye na kuutumia wakati wake kwa manufaa afinyange maisha za watoto kwa njia ya kimungu, kwa kawaida inaonekana katika mwenendo na mwelekeo wa watoto. (Mithali 29:15) Hata wakati ambapo nyumba haina baba, fundisho la uangalifu kutoka katika Biblia pamoja na mfano mwema linazaa matokeo mema.
24. (a) Mwamini akielekewa na upinzani kutoka kwa mwenzi wake wa ndoa, ni suala gani ambalo mwamini huyo anapaswa aendelee kulikazia fikira? (b) Chini ya hali hizo, mwenzi asiyeamini angeonyeshwaje upendo?
24 Lakini namna gani ikiwa baba aliye nyumbani halikubali Neno la Mungu, au hata anamtesa mkeye? Inampasa mke afanyeje? Ikiwa anampenda Yehova, hatamgeuzia Yeye kisogo. Shetani ndiye aliyedai kwamba wanadamu wangemwacha Mungu wakiwekwa chini ya magumu. Hakika mke hataki ajikute akifanya aliyoyasema Shetani. (Ayubu 2:1-5; Mithali 27:11) Wakati ule ule Biblia inamhimiza atafute masilahi ya mumeye ya daima. Kuacha ule anaoujua kuwa ndio ukweli kungemaanisha kupoteza uzima wa milele kwa wote wawili. Lakini akiendelea kuwa imara katika imani yake, huenda akamsaidia mumeye apate wokovu. (1 Wakorintho 7:10-16; 1 Petro 3:1, 2) Zaidi ya hilo, kwa kuendelea kuziheshimu nadhiri zake za ndoa, hata akiwa katika ugumu, mke anaonyesha heshima yake yenye kina kirefu kwa Mwanzishi wa ndoa, Yehova Mungu.
25. Uamuzi wa mzazi unayahusuje mataraja ya uzima ya watoto?
25 Sababu nyingine yenye nguvu kwa mzazi anayeamini kuwa na ushikamanifu kwa Mungu ajapoelekewa na upinzani ni watoto. Mungu anatoa uhakikisho wa kwamba watoto wadogo wa watumishi wake waliojitoa watahifadhiwa waipite “dhiki kubwa” inayokuja. Hata ikiwa mzazi mmoja tu ndiye mtumishi wa Yehova, Yeye anawahesabu watoto hao wadogo kuwa “watakatifu.” (1 Wakorintho 7:14) Lakini ikiwa mzazi ‘angeepa’ asifanye mapenzi ya Mungu, hapo ingekuwaje? Mzazi huyo angejipotezea mwenyewe na pia watoto wake wadogo msimamo wenye kibali mbele za Mungu. (Waebrania 12:25, NW) Lo! hiyo ingekuwa hasara yenye msiba kama nini!
26. Ili tutende kwa kujiletea manufaa sisi wenyewe na wengine, tunahitaji kufanya nini?
26 Basi, hata tuangalie upande gani wa maisha, ni wazi kwamba kuna uhitaji wa kutokujifikiria sisi wenyewe tu, bali kuwafikiria wengine pia. Sisi wenyewe tutapokea upendo tukiyafanya mazoea ya kuwaonyesha wengine pia upendo. (Luka 6:38) Lakini ili tuonyeshe upendo wa kweli na tusipotoshwe na kuwaza kwa upumbavu kwa kibinadamu, ni lazima tumjue Yehova na kufurahia uhusiano mwema naye. Hata hivyo, kufanya kwetu hivyo kunatia ndani uchaguzi ambao lazima tuufanye sisi binafsi.
[Picha katika ukurasa wa 171]
Aina ya upendo ambao lazima watumishi wa Yehova wawe nao inawapa wajibu wa kupendezwa na wengine kweli kweli hata kama ni wa kabila, utaifa au cheo gani maishani