“Zaidi Ya Mambo Yote, Iweni Na Upendo Mkubwa”
“Mwisho wa mambo yote umekaribia. . . . Zaidi ya mambo yote, iweni na upendo mkubwa ninyi kwa ninyi.”—1 PETRO 4:7, 8.
YESU alijua kwamba saa chache za mwisho pamoja na mitume wake zilikuwa muhimu. Alijua mambo ambayo wangekabili. Walikuwa na kazi nyingi ya kufanya, lakini wangechukiwa na kuteswa kama yeye. (Yohana 15:18-20) Alipokuwa nao usiku wa mwisho, aliwakumbusha tena na tena kwamba wanapaswa ‘kupendana.’—Yohana 13:34, 35; 15:12, 13, 17.
2 Mtume Petro ambaye alikuwapo usiku huo alielewa umuhimu wa kikumbusho cha Yesu. Miaka mingi baadaye, muda mfupi tu kabla ya Yerusalemu kuharibiwa, Petro aliandika na kukazia umuhimu wa upendo. Aliwashauri Wakristo hivi: “Mwisho wa mambo yote umekaribia. . . . Zaidi ya mambo yote, iweni na upendo mkubwa ninyi kwa ninyi.” (1 Petro 4:7, 8) Maneno ya Petro ni yenye maana sana kwa wale wanaoishi “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo. (2 Timotheo 3:1) “Upendo mkubwa” ni nini? Kwa nini ni muhimu tuwaonyeshe wengine upendo huo? Na tunawezaje kuonyesha upendo huo?
“Upendo Mkubwa” Ni Nini?
3 Watu wengi hufikiri upendo ni hisia inayojitokeza yenyewe. Lakini Petro hakuwa akizungumzia upendo wa aina yoyote tu; alikuwa akizungumzia upendo wa hali ya juu sana. Neno “upendo” kwenye 1 Petro 4:8 ni tafsiri ya neno la Kigiriki a·gaʹpe. Neno hilo linamaanisha upendo usio na ubinafsi ambao unaongozwa na kanuni. Kitabu kimoja kinasema: “Mtu anaweza kuamriwa kuonyesha upendo wa agape kwa sababu upendo huo si hisia tu bali ni azimio linalomwongoza kutenda.” Kwa kuwa tumerithi mwelekeo wa kuwa na ubinafsi, tunahitaji kukumbushwa mara kwa mara tupendane kulingana na kanuni za Mungu.—Mwanzo 8:21; Waroma 5:12.
4 Lakini hiyo haimaanishi kwamba tupendane kwa sababu tu tumeamriwa kufanya hivyo. A·gaʹpe si upendo usio na hisia. Petro alisema ni lazima tuwe na ‘upendo mkubwa [kihalisi, “unaopanuka”] sisi kwa sisi.’a (Kingdom Interlinear) Hata hivyo, upendo huo unahitaji jitihada. Msomi mmoja alisema hivi kuhusu neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mkubwa”: “Linatoa wazo la mwanariadha anayekaza misuli yake na kujikakamua kwa nguvu zake zote kumaliza mbio.”
5 Basi hatupaswi kuonyesha upendo wetu kwa watu wachache tu au inapokuwa rahisi kufanya hivyo. Tunahitaji ‘kuupanua’ moyo wetu na kuonyesha upendo wa Kikristo hata katika hali ngumu. (2 Wakorintho 6:11-13) Ni wazi kwamba tunahitaji kusitawisha upendo huo na kujitahidi kuukuza kama vile mwanariadha anavyohitaji kufanya mazoezi na kujitahidi kuboresha stadi zake. Ni muhimu kuwa na upendo huo sisi kwa sisi. Kwa nini? Angalau kwa sababu tatu.
Kwa Nini Tunapaswa Kupendana?
6 Kwanza, “kwa sababu upendo unatoka kwa Mungu.” (1 Yohana 4:7) Yehova, ambaye ndiye Chanzo cha sifa hii yenye kuvutia, alitupenda sisi kwanza. Mtume Yohana anasema hivi: “Kwa hili upendo wa Mungu ulifunuliwa kwa habari yetu, kwa sababu Mungu alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee kuja ulimwenguni ili tupate uzima kupitia yeye.” (1 Yohana 4:9) Mwana wa Mungu ‘alitumwa’ awe mwanadamu, atimize huduma yake, na kufa kwenye mti wa mateso—yote hayo yalifanywa ili “tupate uzima.” Tunapaswa kuitikiaje upendo huo mkubwa sana tulioonyeshwa na Mungu? Yohana anasema: “Ikiwa Mungu alitupenda hivi, basi sisi wenyewe tuko chini ya wajibu wa kupendana.” (1 Yohana 4:11) Ona kwamba Yohana anaandika, “Ikiwa Mungu alitupenda hivi”—si alikupenda wewe tu, bali alitupenda sisi. Basi funzo ni wazi: Ikiwa Mungu anawapenda waabudu wenzetu, sisi pia tunapaswa kuwapenda.
7 Pili, ni muhimu sana tupendane zaidi wakati huu ili tuweze kuwasaidia ndugu zetu wenye uhitaji kwa sababu “mwisho wa mambo yote umekaribia.” (1 Petro 4:7) Tunaishi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Hali za ulimwengu, misiba ya asili, na upinzani hutuletea magumu. Tunahitaji kuwa na uhusiano wa karibu hata zaidi na wenzetu hali zinapokuwa ngumu. Upendo mkubwa utatuunganisha kabisa na kutuchochea ‘tutunzane.’—1 Wakorintho 12:25, 26.
8 Tatu, tunahitaji kupendana kwa sababu hatutaki ‘kumpa Ibilisi nafasi’ ya kututumia vibaya. (Waefeso 4:27) Shetani yuko macho kutumia kutokamilika kwa waamini wenzetu, iwe ni udhaifu wao, kasoro zao, na makosa yao ili kutukwaza. Je, tutaacha kutaniko kwa sababu mwamini mwenzetu alisema bila kufikiri au alitutendea vibaya? (Methali 12:18) Hatutafanya hivyo ikiwa tuna upendo mkubwa sisi kwa sisi! Upendo huo hutusaidia kudumisha amani na kumtumikia Mungu kwa umoja na “bega kwa bega.”—Sefania 3:9.
Jinsi ya Kuonyesha Kwamba Unawapenda Wengine
9 Ni lazima upendo uanze nyumbani. Yesu alisema kwamba wafuasi wake wa kweli wangetambuliwa kwa upendo kati yao wenyewe. (Yohana 13:34, 35) Ni lazima upendo uonyeshwe kutanikoni na pia katika familia—kati ya wenzi wa ndoa na kati ya wazazi na watoto. Haitoshi tu kuwapenda washiriki wa familia; tunahitaji kuwaonyesha upendo kwa njia zinazofaa.
10 Wenzi wa ndoa wanawezaje kuonyeshana upendo? Mume anayempenda mke wake kikweli humwonyesha kwa maneno na matendo kwamba anamthamini, hadharani na hata faraghani. Yeye humheshimu na kuzingatia mawazo, maoni, na hisia zake. (1 Petro 3:7) Anatanguliza masilahi yake na kufanya yote awezayo kumtunza kimwili, kiroho, na kihisia. (Waefeso 5:25, 28) Mke anayempenda mume wake kikweli “humheshimu sana,” hata ingawa nyakati nyingine mume wake anapungukiwa. (Waefeso 5:22, 33) Yeye humuunga mkono mume wake na kujitiisha kwake, naye si mwenye kudai mno, bali anashirikiana na mumewe kutanguliza mambo ya kiroho.—Mwanzo 2:18; Mathayo 6:33.
11 Wazazi, mnawezaje kuwaonyesha watoto wenu upendo? Mnaonyesha kwamba mnawapenda mnapojitahidi kuwaandalia mahitaji ya kimwili. (1 Timotheo 5:8) Lakini watoto hawahitaji tu chakula, mavazi, na makao. Wanahitaji mazoezi ya kiroho ili wampende na kumtumikia Mungu wa kweli maishani. (Methali 22:6) Kwa hiyo ni lazima familia itenge wakati wa kujifunza Biblia, kuhubiri, na kuhudhuria mikutano ya Kikristo pamoja. (Kumbukumbu la Torati 6:4-7) Ili kufanya mambo hayo kwa ukawaida, unahitaji kujidhabihu sana, hasa katika nyakati hizi za hatari. Unapowajali na kujitahidi kuwatunza watoto wako kiroho, unaonyesha kwamba unawapenda na unafikiria masilahi yao ya milele.—Yohana 17:3.
12 Ni muhimu pia wazazi waonyeshe kwamba wanawapenda watoto wao kwa kushughulikia mahitaji yao ya kihisia. Watoto ni dhaifu; mioyo yao michanga inahitaji kuhakikishiwa kwamba unawapenda. Waambie kwamba unawapenda, waonyeshe kabisa unawapenda, ukifanya hivyo unawahakikishia kwamba wanapendwa na kuthaminiwa. Wapongeze kwa uchangamfu na kutoka moyoni, unapofanya hivyo, wanatambua kwamba unaona na kuthamini jitihada zao. Watie nidhamu kwa upendo, unapofanya hivyo unawaonyesha kwamba unajali sifa ambazo wanakuza. (Waefeso 6:4) Wonyesho huo wote wa upendo husaidia kujenga familia yenye furaha na umoja ambayo inaweza kupinga mikazo ya siku hizi za mwisho.
13 Upendo hutusukuma kutokazia fikira kasoro za wengine. Kumbuka kwamba Petro alipowashauri wasomaji wake ‘wawe na upendo mkubwa wao kwa wao,’ alisema ni muhimu sana kufanya hivyo, “kwa sababu upendo hufunika dhambi nyingi.” (1 Petro 4:8) ‘Kufunika’ dhambi hakumaanishi kuficha dhambi nzito. Wale walio na madaraka kutanikoni wanapaswa kujulishwa dhambi hizo ili wazishughulikie. (Mambo ya Walawi 5:1; Methali 29:24) Si jambo la upendo hata kidogo na ni kinyume cha Maandiko kuwaruhusu wale wanaotenda dhambi nzito waendelee kuwaumiza au kuwadhulumu watu wasio na hatia.—1 Wakorintho 5:9-13.
14 Mara nyingi, makosa na kasoro za waamini wenzetu huwa ndogo sana. Nyakati nyingine sote hujikwaa kwa maneno au matendo na kuwavunja moyo au hata kuwaumiza wenzetu. (Yakobo 3:2) Je, tunapaswa kutangaza kasoro za wengine? Kufanya hivyo kutasababisha tu migogoro kutanikoni. (Waefeso 4:1-3) Ikiwa tunaongozwa na upendo, ‘hatutafichua kosa’ la mwabudu mwenzetu. (Zaburi 50:20) Kama vile simiti na rangi zinavyofunika mianya iliyo ukutani, ndivyo upendo unavyofunika kasoro za wengine.—Methali 17:9.
15 Upendo utatufanya tuwasaidie wale walio na uhitaji mkubwa. Hali zinapozidi kuzorota katika siku hizi za mwisho, huenda nyakati nyingine waamini wenzetu wakahitaji msaada wa kimwili. (1 Yohana 3:17, 18) Kwa mfano, je, kuna mshiriki wa kutaniko letu ambaye amepatwa na matatizo ya kiuchumi au amepoteza kazi? Basi pengine tunaweza kumsaidia kimwili hali zetu zikiruhusu. (Methali 3:27, 28; Yakobo 2:14-17) Je, nyumba ya mjane mzee inahitaji kurekebishwa? Basi pengine tunaweza kujitolea kusaidia kuirekebisha.—Yakobo 1:27.
16 Hatupaswi kuwapenda tu wale wanaoishi karibu nasi. Nyakati nyingine, huenda tukapata habari za watumishi wa Mungu katika nchi nyingine ambao wamekumbwa na dhoruba kali, matetemeko ya nchi, au vita. Huenda wakahitaji sana chakula, mavazi, na vitu vingine. Haidhuru wao ni wa taifa au kabila gani. ‘Tunaupenda ushirika mzima wa akina ndugu.’ (1 Petro 2:17) Kwa hiyo, kama makutaniko ya karne ya kwanza, tuko tayari kuunga mkono mipango ya kutoa misaada. (Matendo 11:27-30; Waroma 15:26) Tunapoonyesha upendo katika njia hizo zote, tunaimarisha vifungo vinavyotuunganisha katika siku hizi za mwisho.—Wakolosai 3:14.
17 Upendo hutusukuma kuwahubiria wengine habari njema za Ufalme wa Mungu. Fikiria mfano wa Yesu. Kwa nini alihubiri na kufundisha? ‘Aliwasikitikia’ umati kwa sababu ya hali yao mbaya ya kiroho. (Marko 6:34) Walipuuzwa na kudanganywa na wachungaji wa dini za uwongo, ambao walipaswa kuwafundisha kweli za kiroho na kuwapa tumaini. Kwa hiyo, akichochewa na upendo na huruma nyingi ya kutoka moyoni, Yesu aliwafariji watu kwa “habari njema ya ufalme wa Mungu.”—Luka 4:16-21, 43.
18 Leo pia, watu wengi wamepuuzwa kiroho na kudanganywa na hawana tumaini. Ikiwa, kama Yesu, sisi tunajali mahitaji ya kiroho ya wale wasiomjua Mungu wa kweli, basi upendo na huruma zitatusukuma kuwahubiria habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mathayo 6:9, 10; 24:14) Kwa sababu muda unaobaki ni mfupi, huu ndio wakati wa kuhubiri himahima ujumbe huu unaookoa uhai.—1 Timotheo 4:16.
“Mwisho wa Mambo Yote Umekaribia”
19 Kumbuka, Petro alipotushauri tuwe na upendo sisi kwa sisi, alianza shauri lake kwa maneno haya: “Mwisho wa mambo yote umekaribia.” (1 Petro 4:7) Hivi karibuni ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu utachukua mahali pa ulimwengu huu mwovu. (2 Petro 3:13) Sasa si wakati wa kuwa na mtazamo wa kutojali. Yesu alituonya hivi: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mtego.”—Luka 21:34, 35.
20 Basi na tujitahidi kabisa ‘kuendelea kukesha,’ tukitambua umuhimu wa nyakati tunamoishi. (Mathayo 24:42) Na tuwe macho kuepuka majaribu yoyote ya Shetani ambayo yanaweza kutukengeusha. Tusiruhusu kamwe ulimwengu huu usio na upendo utuzuie kuwaonyesha wengine upendo. Zaidi ya yote, na tuzidi kumkaribia Yehova, Mungu wa kweli ambaye hivi karibuni Ufalme wake wa Kimasihi utatimiza kusudi lake tukufu kwa dunia.—Ufunuo 21:4, 5.
[Maelezo ya Chini]
a Kwenye 1 Petro 4:8, tafsiri nyingine za Biblia husema ni lazima tupendane “kutoka moyoni,” “kindani,” au “kwa bidii.”
MASWALI YA FUNZO
• Yesu aliwapa wanafunzi wake shauri gani la mwisho, na tunajuaje kwamba Petro alielewa umuhimu wa shauri hilo? (Fu. 1-2)
• “Upendo mkubwa” ni nini? (Fu. 3-5)
• Kwa nini tunapaswa kupendana? (Fu. 6-8)
• Unawezaje kuonyesha kwamba unawapenda wengine? (Fu. 9-18)
• Kwa nini huu si wakati wa kuwa na mtazamo wa kutojali, na tunapaswa kuazimia kufanya nini? (Fu. 19-20)
[Picha katika ukurasa wa 29]
Familia yenye umoja inaweza kuvumilia kwa njia bora zaidi mikazo ya siku hizi za mwisho
[Picha katika ukurasa wa 30]
Upendo hutusukuma kuwasaidia wale walio na uhitaji mkubwa
[Picha katika ukurasa wa 31]
Tunawaonyesha wengine upendo kwa kuwahubiria habari njema za Ufalme wa Mungu