Sitawisha Upendano Mwingi
“Jitahidini kupendana kwa moyo.”—1 Pet. 1:22.
1, 2. (a) Upendo ni wa maana kadiri gani? (b) Sababu gani hata wanasayansi wasiosadiki kuwako kwa Mungu wanakubali upendo kuwa wa lazima?
UPENDO ni wa lazima ili kufurahia amani, furaha na uradhi. Kweli, bila upendo haifai kuishi—uhakika ambao hata wanasayansi wenye kusadiki vitu vinavyoonekana tu wanakubali. “Nataka kuhakikisha ubora usio na mfano wa upendo . . . Upendo ni wa lazima,” akaandika Sir Julian Huxley, mwanasayansi anayejulikana sana.
2 Sababu gani hata wale wanaokataa kukubali kuwako kwa Muumba wanakazia ubora wa upendo? Kwa sababu moja, uchunguzi wa kisayansi umethibitisha uhitaji wetu wa upendo. Uchunguzi huu waonyesha kwamba, kama vile ilivyo lazima kutosheleza njaa ili mtu aishi, ndivyo wanadamu wanavyohitaji pia upendo na kupendwa. Ashley Montagu mwanasayansi aliandika hivi: “Kutokana na uchunguzi wa waganga na wachunguzi fulani twajua sasa kwamba upendo ni sehemu ya lazima ya chakula cha kila mtoto mchanga na kwamba asipopendwa hatakua awe mtu mwenye afya . . . Hata ijapo alishwe chakula cha kimwili vizuri, huenda akakonda akafa.”
SABABU WANADAMU WANAO UPENDO
3. (a) Sababu gani kwa kawaida watoto wanapokea upendo wanaohitaji? (b) Wanadamu walipokea wapi uwezo huu wa kupenda?
3 Walakini, kwa furaha hakuna hatari kubwa kwamba mtoto atakosa kupokea utunzaji wenye huruma, usio na choyo ambayo anahitaji. Hii ni kwa sababu kwa asili, kama Biblia isemavyo, ‘mama mlezi anawatunza watoto wake mwenyewe.’ (1 The. 2:7) Akina mama watoto walipata wapi upendo huu wanaoonyesha kwa watoto wao? Haukujitokeza wenyewe. Je! si wazi kwamba ulitiwa ndani yao na Muumba mwenye upendo? Sisi sote tunao uwezo wa kupenda na, kwa kusitawisha, sifa hii yaweza kuonyeshwa katika njia nzuri, zenye kuchangamsha moyo zaidi.
4. (a) Sababu gani twajua kwamba Adamu alipewa sifa ya upendo wakati wa kuumbwa? (b) Kuna ushuhuda gani kwamba Adamu alimpenda Hawa, na kwamba uwezo huu wa kupendana wanaume na wanawake ulipelekwa kwa watoto wake?
4 Yehova Mungu alitoa zawadi hii ya upendo wakati wa kuumbwa kwa wanadamu wawili wa kwanza. Twajua hivi kwa sababu Adamu aliumbwa “kwa mfano wa Mungu.” Na kwa kuwa “Mungu ni upendo”—upendo ukiwa sifa yake kuu—kiumbe kilichoumbwa kwa mfano wake kingekuwa pia na upendo huo. (Mwa. 1:26, 27; 1 Yohana 4:8) Kwamba Adamu mtu wa kwanza alipewa upendo amwonyeshe mke wake mpya mzuri inaonyeshwa na alivyofurahia kumwona: “Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu.” (Mwa. 2:23) Hata ijapokuwa Adamu alifanya dhambi akapoteza kukamilika, alipelekea watoto wake uwezo wa kupenda, kutia na uwezo ambao wanadamu wanao wa kuona furaha inayovutia wanaume na wanawake. Ndiyo, mtu wa hekima wa kale alisema kwamba mojawapo la mambo manne ambayo ni ya ajabu mno kwake kufahamu lilikuwa “mwendo wa mtu pamoja na msichana.”—Mit. 30:19; Mwa. 24:67; 26:8.
UPENDO NI WENYE KUPANUKA
5. Zaidi ya upendo wa mahaba kati ya wanaume na wanawake, kuna ushuhuda gani wa upendo kati ya watu wa ukoo?
5 Lakini zaidi ya upendo huu wa mahaba unaoweza kuwako kati ya wanaume na wanawake, kwa kawaida wanadamu wanayo maono ya asili, makubwa ya kupenda watu wao wa ukoo. Hivyo wakati Yusufu, baada ya miaka mingi ya kutengana, alipomwona Benyamini, “moyo wake ulimwonea shauku nduguye.” Baadaye, “akaanguka shingoni mwa ndugu yake Benyamini, akalia; Benyamini naye akalia shingoni mwake.” (Mwa. 43:30; 45:14) Upendo huu wa kijamaa ulimvuta pia Andrea, alipokuwa amemwona Masihi, amtafute ndugu yake Petro ampashe habari hizi za maana sana.—Yohana 1:40-42.
6. Ni mifano gani ya Biblia inayoonyesha kwamba upendo wa mtu waweza kutia ndani wengine zaidi ya watu wa ukoo?
6 Hata hivyo sifa hii ya upendo yaweza kupanuka itie ndani na watu wengine zaidi ya watu wa ukoo wa mtu. Yonathani, Mbenyamini mwana wa Sauli Mfalme wa Israeli, alivutwa sana na sifa nzuri za Daudi, mzao wa Yuda, hata “nafsi yenyewe ikafungamana na nafsi ya Daudi, naye Yonathani akaanza kumpenda kama nafsi yake mwenyewe.” Baadaye, Yonathani alipouawa, Daudi alivutwa hata akamwita “ndugu,” na kusema: “Ndugu yangu Yonathani, ulikuwa mwenye kupendeza sana kwangu. Upendo wako kwangu ulikuwa wa ajabu zaidi kuliko upendo kutoka kwa wanawake.” Upendo wa Ruthu Mmoabu kwa mkwewe Naomi ni mfano mwingi wa namna upendo unavyoweza kutia ndani watu wengine kuliko watu wa ukoo.—1 Sam. 18:1; 2 Sam. 1:26, NW; Ruthu 1:16, 17.
7. Upendo wa Kikristo wapaswa utie ndani nani?
7 Wale wanaokuwa Wakristo wa kweli yawapasa pia wawe na upendano mchangamfu wa kidugu, bila kujali kabila, taifa, cheo au hali ya uchumi ya ndugu na dada zao wa Kikristo. Yesu alionyesha hili, kwa kusema: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:35) Hata hivyo, upendo wa kweli wa Kikristo hauwezi kuonyeshwa kwa watumishi wenzetu wa Mungu peke yao. Lazima upanuke utie ndani na wengine. Hasa, Yesu aliamuru hivi: “Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi; ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni.”—Mt. 5:44, 45.
UPENDO TUNAOHITAJI KUSITAWISHA
8. Eleza namna upendo unavyoweza kuonyeshwa katika kadiri na maana mbalimbali.
8 Kwa wazi, sifa hii ya upendo ambayo Mungu aliwapa wanadamu yaweza kuonyeshwa katika kadiri na maana mbalimbali. Namna gani hivyo? Kwa sababu kwa wazi upendo alio nao Mkristo kwa adui anayemtesa si huruma ile ile ambayo mama mlezi anayo kwa mtoto wake mchanga, ambayo Yusufu alikuwa nayo kwa Benyamini, ambayo Yonathani alimwonea Daudi, au ambayo Mkristo anamwonea mwamini mwenzake. Mungu hatutazamii tumfurahie adui, au hata kwa lazima kumtaka. Hata hivyo inatulazimu tumpende. Je! hili ni lenye kupingana?
9, 10. (a) Kujua maana ya agápē na namna Yehova anavyoutumia, kunatusaidiaje tufahamu kwamba watu wanaweza kupendwa lakini wasitakiwe? (b) Twawezaje kuonyesha upendo kwa watu waovu, wenye ufisadi?
9 Hapana, sivyo, tukiisha fahamu maana ya neno kuu la Kigiriki linalotafsiriwa “upendo” katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, au yaitwayo Agano Jipya. Kijina cha neno hilo ni agape. Kwa habari ya agápē, ya Mungu kwa wanadamu, An Expository Dictionary of New Testament Words ya W. E. Vine yasema hivi: “Huu si upendo usiojali, au shauku, yaani haukuvutwa na ubora wo wote katika vitu vyake.” Nao ni uhakika: Wanadamu wote si wenye kupendeka sana. Lakini kwa kweli hili si kosa lao.—Efe. 4:17-19; Tito 3:3.
10 Kwa sababu ya kurithi kutoka kwa Adamu, wanadamu wote walichukuliwa mimba katika dhambi wakazaliwa na maelekeo ya kutenda mabaya. (Zab. 51:5) Mungu ajua haya. Hivyo anavutwa awapende wanadamu, si kwa sababu ya kustahili au ubora wo wote upande wao, bali hasa kwa sababu yeye anajua kwamba, baadaye, wanadamu wengi wataitikia upendo wake wapatanishe maisha zao na mapenzi yake. (Rum. 5:8-11) Kwa hiyo, agápē humaanisha upendo unaotofautishwa kwa kuheshimu kanuni. Hivyo, basi, tukiiga mfano wa Baba yetu wa kimbinguni tutawapenda hata wale wasioonyesha kustahili upendo wetu. Huenda wakawa wenye kuchukia na kudharau sana wanadamu, wachoyo na hata wafisadi au wahalifu. Twachukia wanayofanya na kusema, hata hivyo, wakati uo huo, tutapendezwa na hali njema yao wenyewe. Tutafanya kadiri tuwezavyo tuwatie moyo waitikie upendo wa Mungu. Je! wewe wasitawisha upendo huo kwa wanadamu wote, ule unaoongozwa na kanuni?
11, 12. (a) Je! upendo wa Mkristo kwa ndugu zake uongozwe na kanuni tu? (b) Upendo wa kati ya mume na mke na upendo wa Yehova kwa Mwana wake waonyeshaje kwamba agápē unatia ndani zaidi ya upendo unaoongozwa na kanuni?
11 Lakini si upendo unaoongozwa na kanuni tu, usio na shauku na huruma, ambao mtume Petro alikuwa akifikiria alipowaandikia Wakristo wenzake: “Jitahidini kupendana kwa moyo.” (1 Pet. 1:22) Ijapokuwa sehemu kubwa ya agápē, ni kuheshimu kanuni, upendo huu waweza pia kutia ndani shauku na kutaka sana. Hivyo twasoma: “Imewapasa waume nao kuwapenda [kiarifa agapáo] wake zao.” (Efe. 5:28) Kwa wazi hii haimaanishi kwamba imewapasa waume za Kikristo kuwapenda wake zao kama wanavyowapenda adui zao! Sivyo; bali, badala yake, shauri hili “kuwapenda wake zao” lamaanisha kwamba imewapasa pia waume wawe na maono ya huruma na shauku kwa wake zao, kama Muumba alivyokusudia.
12 Kwamba neno hilo la Kigiriki agápē laweza kutia ndani maono mengi sana ya shauku na kutaka sana yaonyeshwa pia katika mifano mingine ya Biblia. Kwa mfano, tunaambiwa hivi: “Baba ampenda Mwana.” (Yohana 3:35) Upendo wa Mungu kwa Mwana wake, Yesu Kristo, hauongozwi tu na kuheshimu kanuni. Yehova anamhurumia Yesu, kama Biblia isemavyo: “Baba yuna shauku na Mwana na humwonyesha mambo yote anayofanya mwenyewe.” Yehova Mungu akasema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.”—Yohana 5:20, NW; 2 Pet. 1:17.
13. (a) Imewapasa Wakristo wawe na upendano wa kadiri gani? (b). Maana asili ya neno la Kigiriki kwa “sana” yaonyeshaje kadiri inayofaa ya upendo wetu?
13 Hivyo, basi, hii ndiyo kadiri ya upendo ambao lazima Wakristo wasitawishe kwa mmoja na mwenzake. Si upendo baridi, au upendo unaoonyeshwa kwa watu ambao huenda hata wasiwatake kwa sababu ni wajibu tu. Bali ni mchangamfu, wenye kuhurumia wengine, kama upendo ule wa huruma ambao mtu anamwonyesha jamaa yake ambaye anapenda sana, na ambao Yehova anamwonyesha Mwana wake mpendwa sana. Mtume Petro alitia mkazo kwamba upendano wetu umepaswa uwe wa namna au kadiri hii alipotia moyo hivi: “Mpendane sana” au kama tafsiri nyingine zinavyosema, “kwa shauku ya nguvu” “kwa nguvu zenu zote.” (1 Pet. 1:22, New World Translation; New American Standard Bible; The New English Bible) Neno la kwanza la Kigiriki linalotafsiriwa “sana” lamaanisha, kwa halisi, “kwa kukunjuka.” (Kingdom Interlinear Translation) Kwa hiyo, upendo wetu lazima ujitahidi kwa nguvu sana. Je! wewe wasitawisha upendo wa namna hii?
14. (a) Sababu gani ni lazima tujitahidi kusitawisha upendo? (b) Twawezaje kujifunza kupendana?
14 Ni lazima sote tujitahidi kufanya hivyo. Hii ni kwa sababu kutokutii kwa Adamu kwa muda wa miaka 6,000 iliyopita kumeingiza sana jamaa ya kibinadamu katika dhambi na kutokamilika, kukiharibu uwezo wetu wa kuonyesha sifa kuu ya Yehova ya upendo. Hata maono ya asili ya upendo ambayo kwa kawaida watu wa ukoo mmoja wanaonyeshana yanapotolewa mara nyingi, kama vile mifano ya kale ya Kaini, Esau na ndugu mzazi mmoja za Yusufu. Biblia ilitabiri kwamba hii pia ingekuwa wazi “siku za mwisho” wakati watu wangekuwa “wasiowapenda wa kwao.” (2 Tim. 3:1-3) Kwa hiyo, ni lazima kama nini tusitawishe upendo ili tuufanye uwe hai katika mioyo yetu! Lakini sisi tunaoishi katika kipindi hiki chenye hatari cha “siku za mwisho” twawezaje kujifunza kupendana? Mtume Paulo anaeleza hivi: “Katika upendano [wa udugu], hamna haja niwaandikie; maana ninyi wenyewe mmefundishwa na Mungu kupendana.” (1 The. 4:9) Mungu anatufundishaje huu?
NAMNA TUMEFUNDISHWA NA MUNGU KUPENDA
15. (a) Ni katika njia gani yaweza kusemwa kwamba Yehova anatufundisha kupendana? (b) Wakristo wana wajibu wa kupendana kwa kadiri gani?
15 Anafanya hivyo katika njia nyingi. Twaweza kusema kwamba kwa kumwumba mtu katika mfano wake, akiwapa wanadamu uwezo wa kupenda, kweli ijapokuwa sasa tu wenye dhambi, Mungu ametuelekeza tuwe wenye kupenda. Halafu, pia, Mungu ametufundisha tupendane kwa kufanya mara nyingi kujizoeza upendo kuwa amri. Kulingana na Yesu Kristo, mojawapo ya amri kubwa mbili za sheria ya Mungu kwa Israeli ilikuwa: “Mpende jirani yako kama nafsi yako.” Mwanafunzi Yakobo aliiita hii “sheria ya kifalme.” (Mt. 22:39; Law. 19:18; Yak. 2:8) Walakini, akisema kama mjumbe wa Mungu, Yesu alifunua kwamba inawapasa Wakristo wawe na upendo ulio mkubwa hata zaidi, wakipendana kama yeye alivyokuwa amewapenda wanafunzi wake. (Yohana 13:34; 1 Yohana 3:16) Lakini Yehova amewafundisha wanadamu kupendana katika njia nyingine yenye kuvuta sana.
16. (a) Hasa ni katika njia gani nzuri Yehova anatufundisha kupendana? (b) Ni wonyesho gani mkubwa kuliko wote wa upendo wa Mungu?
16 Hii ni kwa mfano. Mtume Paulo alisema na makutano katika jimbo la kale la Kirumi la Galatia, Asia Ndogo, akisema juu ya Mungu hivi: “Alitenda mema, akiwapeni mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akiwashibisha mioyo yenu chakula na furaha.” (Matendo 14:17) Hivyo Mungu hatuamuru tupendane tu, bali anaonyesha kwa mfano namna ya kupendana. (Mt. 5:44, 45) Mfano wake bora zaidi wa kuonyesha upendo ni mpango wa kutoa mali yake yenye thamani zaidi kwa faida yetu. Biblia yaeleza hivi: “Mungu amemtuma Mwanawe pekee ulimwenguni, ili tupate uzima kwa yeye. . . . Wapenzi, ikiwa Mungu alitupenda sisi hivi, imetupasa na sisi kupendana.”—1 Yohana 4:9-11.
17. Matokeo ya kujifunza kwetu kweli juu ya Yehova na mipango yake ya ajabu kwetu yamepaswa yawe nini?
17 Hivyo, tunapoyafikiria mambo ya ajabu ambayo Yehova amefanya—kutupatia baraka tele za vitu vya kimwili, lakini hasa zawadi ya Mwana wake inayowezesha uzima wa milele katika taratibu mpya yenye haki—tunajifunza juu ya namna Mungu na Muumba Yehova alivyo mwema. Matokeo ya kuikubali kwetu kweli hii yenye maana sana juu ya mipango ya Yehova kisha kuishi kupatana nayo yamepaswa yawe nini? Mtume Petro alisema juu ya “upendano wa ndugu usio na unafiki,” ndiyo, uhusiano mzuri wa ujamaa wa udugu na upendo! Na hivyo katika kushukuru kwetu, ni nini la maana sana tunalofanya? Petro aliongeza hivi: “Pendaneni sana kutokana na moyo.”—1 Pet. 1:22, NW.
SABABU UPENDO MWINGI SANA WA LAZIMA SANA WAKATI HUO
18. Petro aliandika barua yake ya kwanza wakati gani, na wakati huo ni nini kilichokaribia?
18 Ili tufahamu sababu gani upendo mwingi ulikuwa wa lazima katika siku za Petro, ni lazima tuzichunguze hali zilizokuwako wakati huo. Petro aeleza hivi: “Mwisho wa mambo yote umekaribia; basi, iweni na akili, mkeshe katika sala. Zaidi yote iweni na [upendano mwingi sana].” (1 Pet. 4:7, 8) Ni kweli, wakati huo mwisho ulikuwa umekaribia. Petro aliandika barua wakati fulani kati ya mwaka wa 62 kufika 64 C.E., na ilikuwa punde baada ya hapo kwamba, katika mwaka wa 70, mwisho ukaja kwa taratibu ya mambo ya Kiyahudi. Majeshi ya Kirumi yaliharibu eneo lote la Uyahudi, na hasa Yerusalemu. Na unabii wa Yesu watusaidia tufahamu sababu gani ilikuwa lazima kwa Wakristo wakati huo wawe na “[upendano mwingi sana].”
19. (a) Ni ishara gani ambayo Yesu alitoa ili Wakristo wajue kwamba mwisho ulikaribia, na ishara hii ilitimizwaje? (b) Wakristo waliwezaje kutii amri ya Yesu kukimbia, na je! lilikuwa jambo la hekima kutii?
19 Yesu alitabiri hivi: “Hapo mtakapoona mji wa Yerusalemu umezungukwa na majeshi, ndipo jueni ya kwamba uharibifu wake umekaribia.” (Luka 21:20; Mt. 24:15) Ilikuwa Novemba mwaka wa 66 C.E. majeshi ya Kirumi chini ya Sesho Gallo yalipouzunguka Yerusalemu. Yaliingia mpaka mjini, mahali palipofikiriwa kuwa ‘patakatifu’ kwa Wayahudi, wakaushambulia ukuta wa hekalu, wakifukua chini yake. Warumi wangaliweza kwa vyepesi kuuteka mji mzima, lakini kwa ghafula, bila sababu yo yote ya wazi kwa kufanya hivyo, Jemadari Gallo akaondoka akarudi. Hii iliwapa Wakristo nafasi ya kutii onyo lifuatalo: “Ndipo walio katika Uyahudi na wakimbilie milimani.” (Luka 21:21-24) Mwisho majeshi ya Kirumi chini ya Jemadari Tito yalirudi yakaiharibu nchi, ikitokeza kifo cha watu walioripotiwa 1,100,000 katika Yerusalemu peke yake, “dhiki kubwa” kweli kweli!
20. Kuna ushuhuda gani kwamba Wakristo walitii amri ya Yesu?
20 Lakini namna gani Wakristo? Eusebio Pamfilo mwanahistoria wa karne ya tatu anasema hivi: “Lakini, jamii nzima ya kanisa katika Yerusalemu, wakiisha kuamriwa kwa ufunuo wa kimungu, waliopewa watu huko wenye utawa unaokubaliwa kabla ya vita, iliondoka katika mji huo, ikakaa katika mji fulani mdogo ng’ambo ya Yordani, uitwao Pela.”a Ndiyo, kwa wazi Wakristo walitii maagizo ya Kristo na, wakati Sesho Gallo na majeshi yake walipokwisha kuondoka, Wakristo walikimbilia milimani karibu na Pela, kwa njia hiyo wakaokoa maisha zao. Lakini haikuwa vyepesi kwao.
21. (a) Sababu gani Yesu alikazia haraka ya kukimbia mara hiyo? (b) Yaelekea Wakristo wenye kukimbia walipatwa na hali gani?
21 Akijua kwamba matukio juu ya kurudi kwa askari za Kirumi—chini ya Jemadari Tito—yangefanya upesi karibu isiwezekane kutoka katika mji wenye uharibifu, Yesu alikuwa ametangulia kusihi hivi: “Aliye juu ya dari asishuke kuvichukua vitu vilivyomo nyumbani mwake; wala aliye shambani asirudi nyuma kuichukua nguo yake.” (Mt. 24:17, 18) Kama matokeo, mamia, na labda maelfu, ya Wakristo watiifu waliondoka kwa haraka mara Gallo na majeshi yake walipoondoka, wakichukua pamoja nao mali chache. Ilikuwa vyema kwa vile hawakulemewa, kwa maana safari ilikuwa ndefu, nchi ilikuwa yenye mawe mawe na bila shaka hali za hewa zilikuwa mbaya wakati huo wa mwaka. Katika hali hizo, mabishano na taabu nyingine kati ya wakimbizi yangaliweza kutukia kwa vyepesi. Halafu, pia, kulikuwako tatizo la mahali ambako wangeishi wote.
22. (a) Ni hali gani zilizokuwako wakati huo katika eneo lote? (b) Sababu gani ilikuwa lazima wakati huo Wakristo watumie shauri la Petro?
22 Labda mwishowe walijenga vibanda vya muda karibu na Pela, yaelekea wakijenga huko kambi ya wakimbizi milimani. Hatujui. Lakini kwa vyo vyote, ilikuwa vigumu kwao. Ulikuwa wakati wa upungufu wa vitu na wenye shida katika eneo lote. Mwisho wa taratibu nzima hiyo ya Kiyahudi ulikaribia! Kwa hiyo, kutia moyo kwa Petro kulikoongozwa na Mungu kulifaa sana kwa wasomaji wa barua yake, waliokuwa katika “hali ya ugeni”: “Mwisho wa mambo yote umekaribia; . . . Zaidi ya yote iweni na juhudi nyingi katika kupendana.” (1 Pet. 1:1; 4:7, 8) Wakiwa na upendo huo, Wakristo hawangeoneana choyo na kukasirikiana, bali wangeshirikiana na kujengana na kutiana nguvu wavumilie hali zenye kujaribu walizokabili.
SABABU UPENDO MWINGI SANA SASA
23. Je! maonyo ya Biblia juu ya kukaribia kwa mwisho yana maana kwetu leo?
23 Walakini, hatutaki tuufikirie wakati huo wa zamani tu. Kwa maana unabii wa Yesu juu ya “mwisho wa taratibu ya mambo” wahusu wakati wa leo; hasa, sasa ndio wakati utimizo wake mkuu unapotumika. Vile vile onyo linalofanana na hilo la Petro kwamba “mwisho wa mambo yote umekaribia.” Kusudi la Mungu ni kuiharibu taratibu nzima hii mbovu na kuleta “mbingu mpya na nchi mpya” katika wakati ujao ulio karibu! (Mt. 24:3-22; 2 Pet. 3:13) Hivyo twaishi katika wakati ambao uharibifu wenye kuogofya wa Yerusalemu na mazingira yake hautalingana na ile “dhiki kubwa” iliyo karibu sana sasa! Majaribu ambayo itawapasa Wakristo wengi wakabili wakati wa “dhiki kubwa” iliyo mbele huenda yakawa kama yale yaliyovumiliwa pindi mbili za majuzi.
24, 25. (a) Ni mambo gani ambayo Mashahidi wa Malawi walivumilia, na sababu gani kutii shauri la Petro kulikuwa kwa maana kwao? (b) Ni kujichunguza gani kungekuwa kwa hekima kwetu kufanya?
24 Ya kwanza ya hizi ilitia ndani mashahidi wa Yehova katika Malawi. Chini ya habari “Mashahidi wa Yehova—Wakimbilia Maisha Zao,” gazeti New York Times la Oktoba 22, 1972, lilitoa taarifa hivi: “Juma iliyokwisha kulitokea habari kutoka nchi ndogo ya Afrika Mashariki ya Malawi juu ya kuteswa . . . kunajisiwa kwa washiriki wanawake wa kikundi, kuchomwa moto kwa nyumba za Mashahidi na kufukuzwa kwa lazima kwa jamia kubwa ya wafuasi 23,000 katika nchi.” Kwa sababu ya uaminifu wao kwa sheria ya Mungu, Mashahidi wa Malawi walifukuzwa mpaka wakavuka mpaka na kulazimishwa kuingia katika kambi kubwa ya wakimbizi ambako, kwanza, kulikuwako upungufu mkubwa wa mahitaji ya maisha. Kwa sababu ya shida wengi wakafa. Ni jambo la maana kama nini kutii shauri lililoongozwa na Mungu, “zaidi ya yote iweni na juhudi nyingi katika kupendana,” chini ya hali hizo zenye taabu.
25 Wingi wa Mashahidi wa Malawi walishinda jaribu lao wakiwa waaminifu kwa Mungu na nguvu kiroho, na bila shaka lililowasaidia kulikuwa kutii kwao shauri hilo la Biblia lililotangulia. Lakini namna gani sisi wenyewe? Je! tunajitayarishia majaribu yaliyoko mbele? Je! tunasitawisha maono mengi ya kuhurumiana, kama Yusufu alivyomwonea ndugu yake, kama Yonathani alivyomwonea Daudi, na kama Yehova Mungu anavyomwonea Mwana wake Yesu Kristo? Kujizoeza upendo huo ni kwa lazima kweli kweli katika hizi “siku za mwisho.”
26, 27. (a) Ni nini lililotukia Desemba mwaka wa 1972 katika Managua, Nicaragua, na lingeweza kuwa tazamio dogo la nini? (b) Mashahidi wa Yehova walionyeshaje upendano wakati wa msiba huo katika Managua?
26 Labda matatizo yaliyoko mbele yalitazamiwa na msiba ulioripotiwa katika Awake! la Machi 8, 1973, lililosema hivi: “Ile ishara ingali ipo. Yatangaza hivi kwa ushuhuda wa kimya: MANAGUA, WAKAZI 404,700. Na katikati ya mji mlinzi mwingine wa kimya ashuhudia. Saa iliyo katika mlango mkuu wa Makao ya Serikali yaonyesha saa 6:35. Wakati wa giza, mji mkuu wa Nicaragua ulianguka katika tetemeko la dunia lenye kuogofya wakati wa saa hiyo ya asubuhi mapema, Jumamosi, Desemba 23, 1972.” Ndiyo, ule mji ukakoma—kazi ya mabomba haikufaulu, nguvu za umeme (stimu) zilikoma, karibu kila kitu kilikoma. Karibuni jambo hili litatukia, si kwa mji mmoja, bali kila mji utaanguka—taratibu nzima ya mambo itakoma! Ni jambo gani la lazima kwetu kujizoeza wakati wa hali hizo?
27 Mamia mengi ya mashahidi wa Yehova katika Nicaragua na katika nchi za ujirani walionyesha upendo wao mwingi sana, kama Awake! lilivyoripoti: “Mara hiyo jitihada zilianza kufanywa ili kuwaangalia Mashahidi hawa [waliopatwa na tetemeko la dunia] na jamaa zao. Bila shaka upendo wa kweli ulio katikati ya watu wa Mungu ulijionyesha wenyewe. Mnamo alasiri ya Jumamosi Shahidi akawasili akiwa na gari na galeni 300 za maji kutoka kundi la umbali wa maili kumi na sita. . . . Ndipo saa 4 za usiku magari mawili ya kwanza yenye vifaa yalipowasili kutoka mashahidi wa Yehova katika Liberia, Costa Rica. Punde kidogo, magari mengine mawili yakawasili kutoka Mashahidi katika Tegucigalpa, Honduras. Hivyo, kwa muda wa kama saa 24 baada ya msiba huo, chakula, mavazi, dawa, maji na mafuta ya motokaa yalipatikana!”
28. (a) Twaweza kujifunza nini kutokana na yaliyotukia Managua? (b) Ni katika njia gani nyingine mashahidi wa Yehova wamekuwa wakipokea mazoezi katika kuonyesha upendano?
28 Twaweza kujifunza kutokana na tukio hilo. Wakati taabu kubwa na misiba mikubwa inapotukia kila mahali, jambo tunalohitaji zaidi ya yote, ni upendano mwingi sana. Na tunapofikiri juu yake, je! sisi kama mashahidi wa Yehova hatukuwa tukipokea mazoezi ili tuzikabili hali hizo? Tunakutana pamoja kwa kawaida katika makusanyiko, makubwa na madogo, ambapo tunapokea agizo na kutiana moyo kuzuri ili tupendane. Pia, tumekuwa na kafeteria za kulishana, na kwa ukaribishaji-wageni tumewapatia Wakristo wenzetu mahali pa kulala katika nyumba zetu. Lo! mazoezi bora ya kupendana na kutunzana namna gani! Lakini yatupasa tuendelee kuonyesha sifa hii bora ya upendo ambayo Mungu aliwapa wanadamu, lakini ambayo imepotolewa na kutumiwa vibaya kwa miaka 6,000 ya dhambi na kutokamilika. Ni lazima tuendelee kusitawisha upendano mwingi sana sasa, kwa sababu mwisho wa mambo yote umekaribia sana.
[Maelezo ya Chini]
a The Ecclesiastical History Pamphilus, kilichotafsiriwa kutoka Kigiriki, na C. F. Crusé (1894), ukurasa wa 75.
[Picha katika ukurasa wa 535]
Upendo wa kweli kwa Daudi ulimwongoza Yonathani ampe zawadi fulani kama ishara ya shauku yake