Iweni na Juhudi Nyingi Katika Kupendana
“Iweni na juhudi nyingi katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi.”—1 Pet. 4:8.
1, 2. Mwandikaji wa Biblia Yohana anahakikishaje ubora kuonyesha upendo wa agápē katika maisha zetu?
KATIKA barua yake ya kwanza kwa Wakristo wenzake mtume Yohana anataja upendo wa Mungu wa kutuma Mwanawe akakomboe wanadamu na kuonyesha kwamba lazima Wakristo waige wonyesho huo wa upendo. Hilo si jambo la hiari ya mtu bali ni wajibu wa kupendana. Anasema hivi: “Wapenzi, ikiwa Mungu alitupenda sisi hivi, basi sisi wenyewe tuko chini ya wajibu wa kupendana.” (1 Yohana 4:11, NW) Kwa hiyo hapa Yohana anakazia ubora wa amri “mpya” ya Yesu. (Yohana 13:34, 35) Imewapasa Wakristo wawe mifano myema katika kuonyeshana upendo. Yehova mwenyewe ameweka mfano katika kuonyesha upendo wenye kuongozwa na kanuni (agápē) kwa watoto wake wa kidunia. Kwa hiyo, tukiwa watoto watiifu wa Mungu, na watumishi wake, imetupasa tufuate mfano huo na kuonyesha upendo, si kwa Yehova Mungu tu, bali pia sisi kwa sisi.
2 Yohana anahakikisha tena wajibu huo na kuonyesha uzito wa jambo lenyewe, katika 1 Yohana 4:20 na 21, ambapo anaandika hivi: “Mtu akisema, Nampenda Mungu, naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona. Na amri hii tumepewa na yeye, ya kwamba yeye ampendaye Mungu, ampende na ndugu yake.” Kwa hiyo jambo hili la kuonyesha upendo wa agápē, upendo wa kujitoa, kwa ajili ya ndugu au dada wa Kikristo wa mtu ni jambo zito sana, kwa sababu kwa njia hiyo tunaonyesha tunampenda Yehova Mungu mwenyewe.
3. Ndugu yetu anayeonekana tunayepaswa kupenda ni nani?
3 Ndugu yetu anayeonekana tunayepaswa kupenda ni nani? Hatuwezi kusema ni mtu wa mbari yetu tu, wa rangi yetu tu wala wa taifa letu tu, sivyo? Bali, ndugu yetu ni mtumishi mwenzetu wa Yehova katika kundi la kwetu la Kikristo, au katika kundi jingine lo lote la mashahidi wa Yehova wa Kikristo katika dunia yote. Yeye ni ndugu yetu katika imani. (Gal. 3:26-28) Kwa hiyo tunalazimishwa na upendo wa Yehova kuwa na juhudi nyingi sana katika kupenda ndugu zetu wa Kikristo, kwa njia hiyo tukihakikisha tu Wakristo wa kweli.
4. Paulo anapendekeza nini katika 2 Wakorintho 13:5, na kwa hiyo imewapasa wote wafikirie maulizo gani hapa?
4 Kama tengenezo leo, mashahidi wa Kikristo wanaonyeshana upendo huo. Hawapigani kati ya vikundi vikundi vya mataifa mbalimbali; hakuna upendeleo wa kikabila wala chuki. Na ndivyo imepaswa kuwa. Bila shaka alama ya Ukristo wa kweli imo katika tengenezo hilo. Lakini ulizo ndilo hili: Sisi kama watu mmoja mmoja tunaendeleaje katika jambo hili la kuonyesha ndugu zetu wa Kikristo upendo? Je! mmoja mmoja tunaonyeshana upendo wa kweli wa agápē? Katika habari hii ni vema kila mmoja ajichunguze kulingana na kanuni iliyowekwa katika Neno la Yehova. Naam, ni kama alivyosema Paulo: “Endeleeni kuchunguza kama mmo katika imani, endeleeni kujihakikisha mlivyo.”—2 Kor. 13:5, NW.
5. (a) Je! upendo kama sifa ya Wakristo ni Jambo la hiari ya mtu? (b) Upendo wa Mkristo umepaswa ufike wapi?
5 Tumejifunza kutokana na maneno ya Yesu na kutokana na Yohana pia kwamba upendo kwa ndugu zetu ni sifa ya lazima ya Kikristo. Si jambo tunaloweza kusema ni la hiari ya mtu; upendo si jambo tunaloweza kuzoea wakati inapofaa tu. Bali, kwa kweli amri ya Yesu kwa wanafunzi wake ya kupendana ni sheria ya kifalme, inayopaswa kuongoza matendo yetu yote. Wala hatuwezi kupenda washiriki wachache tu kundini, bali upendo wetu umepaswa ukunjuke utie ndani ushirika mzima wa ndugu katika sehemu zote za dunia. Ni kama alivyoandika Petro: “Iweni na upendo kwa ushirika mzima wa ndugu.” (1 Pet. 2:17, NW) Basi, ni jambo la maana kama nini tusiweke mpaka wa upendo wetu bali tukunjuke kutia ndani ushirika mzima wa ndugu.
UPENDO WA KIKRISTO KWA NDUGU UNAPATIKANAJE?
6. Mkristo anawezaje kuanza kupata uwezo wa kuonyesha upendo wa agápē?
6 Kwa kuwa upendo ni wa maana sana katika maisha ya Mkristo, ni kwa njia gani basi Mkristo anavyoupata upendo huo? Leo wako wengi katika kundi la Kikristo walio wapya sana katika ibada ya Yehova, na inafaa sana watake kutimiza sheria ya kifalme, “amri mpya” ambayo Yesu aliwekea wafuasi wake. Kwanza tunafahamu kwamba upendo wa agápē kweli ni tunda la roho ya Mungu, kama Paulo anavyoonyesha katika Wagalatia 5:22. Kwa hiyo lazima Mkristo atafute na kufuata uongozi wa roho takatifu akiwa na umoja na tengenezo ambalo Yehova anatumia duniani leo.
7. Kwa sababu gani maarifa juu ya Neno la Mungu ni ya maana kwa mtu anayesitawisha sifa ya upendo?
7 Tena, kumjua Yehova Mungu na sifa zake za ajabu ni kwa maana zaidi kuliko jambo jingine lo lote. Katika habari hii, lazima Mkristo ajifunze upendo ni nini hasa na unavyotendea ndugu yake au mwanadamu mwenzake. Bila shaka, maarifa hayo yanatokana na kujifunza Neno la Mungu, kwa faragha na kwa kushirikiana na watu wa Mungu walio duniani leo. Kwa hiyo lazima Mkristo asitawishe ufahamu mwingi sana wa kweli zote zilizomo katika Neno la Mungu na kuwa mwanafunzi mwenye bidii wa Biblia. Kama alivyosema Petro, imetupasa tusitawishe tamaa ya “maziwa . . . yasiyoghoshiwa” ya neno.—1 Pet. 2:2.
8. Je! moyo unahusika, na kwa sababu gani?
8 Halafu tena moyo wa mtu unahusika, kwa sababu upendo kwa msingi ni sifa ya moyo. Ndiyo sababu Petro aliandika hivi: “Jitahidini kupendana kwa moyo.” (1 Pet. 1:22) Mtu akiwa anajua vizuri upendo wa agape ni nini na namna unavyotenda, moyo wake unaweza kuongozwa kuelekea njia inayofaa katika kuonyesha upendo, kwanza kwa Yehova, Mungu wa upendo, kisha kwa ndugu zake na mwanadamu mwenzake. Mkristo akiisha kusitawisha upendo huo katika moyo wake hiyo inamwezesha kujiweka wakf kwa Yehova mwishowe, Mungu wa upendo, kisha kuendeleza wakf wake kwa kutimiza sheria za Yehova na kuongoza maisha yake kila siku kupatana na kanuni za Mungu zilizomo katika Neno lake.—1 Yohana 5:3.
9. (a) Ni jambo gani lililo gumu zaidi kuliko kupata maarifa juu ya Biblia au kuliko kuhubiri? (b) Upendo wa agápē ni maana kadiri gani kwa Mkristo kwa habari ya uhusiano wake na ndugu zake?
9 Huenda Wakristo wengine wakaona si vigumu sana kujaza akili zao na maarifa juu ya Yehova na sheria na matakwa yake, na huenda wakawa wanafurahia kwenda nje kuzihubiri habari njema za ufalme wa Mungu kwa wengine. Walakini, nyakati nyingine kuishi kupatana na kweli na kujifunza ‘kujitahidi kupendana kwa moyo’ kunakuwa kugumu zaidi kwa watu ao hao kuliko kulivyo kugumu kupata maarifa juu ya amri, sheria na kanuni, au kuhubiri hadharani. Hapa ndipo ambapo ni lazima Mkristo ajifunze kufuata kanuni kuhusu nia zake, mwenendo wake, uhusiano wake na kila mtu kundini, na humo ndimo upendo huo wa agápē ulimo wa maana sana sana. Hiyo inamaanisha kwamba lazima Mkristo ajifunze kuishi kupatana na kweli zote kwa moyo.
10. Yohana anatoa onyo gani juu ya upendo, na kwa hiyo imempasa Mkristo aongoze upendo kwa kufaa namna gani?
10 Ikiwa tunapenda ndugu zetu, basi lazima tuondoe cho chote ambacho kingeelekea kututenganisha na ye yote kati yao. Lazima tujihadhari tusianze kupenda mambo yasiyofaa. Yohana alionya ndugu zake wa Kikristo wasiupende ulimwengu, kwa sababu aliwapenda. Alisema hivi: “Msiwe mkipenda wala ulimwengu wala vitu vilivyomo katika ulimwengu. Mtu ye yote akipenda ulimwengu, upendo wa Baba haumo katika yeye; kwa sababu kila kitu kilichomo katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na kujionyesha kwa mtu mali yake—hakitokani na Baba, bali chatokana na ulimwengu.” (1 Yohana 2:15, 16, NW) Kwa hiyo kama mtu angeanza kuupenda ulimwengu au vitu vilivyomo ulimwenguni, upendo wake ungepotolewa. Angekuwa akijitenganisha na ndugu zake wasiopenda ulimwengu wala vitu vya kilimwengu. Karibuni asingeonekana akiwa pamoja na ndugu zake katika mikutano ya kundi wala katika utumishi wa shambani wa Kikristo, bali angekuwa akitafuta washirika wa kilimwengu au mapendezi ya kilimwengu badala ya ndugu zake wa Kikristo. Lo! lazima tuwe waangalifu namna gani basi tuendelee kuelekeza upendo wetu upande unaofaa na kutafuta sikuzote kushirikiana na wale wanaomwabudu Yehova kama sisi!
11. (a) Kuwa na upendo wa kweli wa agápē kwa wengine kumepaswa kutuzuie tusifikiri kwa njia gani? (b) Ni nini kinachoharibika tusipoonyesha upendo wa kweli kwa ndugu zetu?
11 Upendo wenye kuongozwa na kanuni kabisa umepaswa utufanye tufikirie wengine, si sisi wenyewe tu na mapendezi yetu wenyewe, tukisisitiza kwamba tuna haki ya kufanya mambo hata yawe na matokeo gani juu ya wengine. Kwa hiyo imetupasa tuwe tukifikiria sura yetu wenyewe na mapendezi yetu wenyewe, ili kwa mambo hayo tusije tukaudhi mtu kundini wala kumkwaza. (2 Kor. 6:3, 6) Imetupasa tuangalie mwenendo wetu, usemi wetu na mashirika yetu, tukikumbuka mapendezi ya ndugu zetu wala si yetu wenyewe tu, tukifikiria matokeo yanavyoweza kuwa juu yao kwa sababu ya tunayofanya au kusema. (Flp. 2:4) Ni vizuri kukumbuka kwamba upendo wa agápē usipokuwa unasitawi vizuri ndani yetu, kwa kweli uhusiano wetu na Yehova unaharibika. Kumbuka maneno ya Yohana: “Kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona.”—1 Yohana 4:20
KWA KUIGA UPENDO WA YEHOVA
12. Yehova anatuwekea mfano gani katika habari hii ya upendo, na kwa hiyo Petro anatushauri tufanye nini?
12 Ni vizuri pia kufikiri kwamba Yehova anatupenda sote, na sote tu wasiokamilika. Kwa hiyo Yehova hapendi wachache tu kundini, bali kupitia kwa mpango wake wenye upendo ana nia ya kutusamehe makosa yetu na kukubali utumishi wetu wa upendo. Kwa hiyo kweli na kuthamini kwa kweli ustahili wa ndugu zetu machoni pa Yehova ndio msingi wa upendo mwingi sana wa moyoni tunaoonyesha ndugu zetu. Petro alishauri hivi: “Zaidi ya yote iweni na juhudi nyingi katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi. Mkaribishane ninyi kwa ninyi, pasipo kunung’unika; kila mmoja kwa kadiri alivyoipokea karama, itumieni kwa kuhudumiana; kama mawakili wema wa neema mbalimbali za Mungu.” (1 Pet. 4:8-10) Kwa hiyo Yehova anampa kila mmoja karama ya kutumia katika utumishi wa kimungu naye anakubali utumishi wetu kujapokuwapo kutokamilika kwetu, udhaifu wetu mbalimbali na makosa. Tukipenda ndugu zetu kama Yehova anavyotupenda, imetupasa tuweze kuepuka kutazama makosa yao tu na kujifunza kufanya kazi kwa umoja na WOTE kundini, tukifunika makosa ya wengine kwa upendo.
13. Wazee wanawezaje kuonyesha upendo kwa wazee wenzao kundini?
13 Ndivyo inavyopaswa kuwa hasa kwa wazee rasmi katika makundi ya Kikristo. Wazee wengine hawapaswi kujiona ni wakuu kuliko wazee wengine ati kwa sababu wamekuwa katika tengenezo la Mungu muda mrefu zaidi wala kwa sababu wamekuwa wazee waliowekwa kwa muda mrefu zaidi. Bali, imewapasa wawathamini wazee wenzao na ubora wao na heshima yao ya kibinadamu machoni pa Mungu, wakiheshimu maoni na mawazo yao, yakiwa yana msingi wa Neno la Mungu. Yehova haweki tofauti yo yote kwa sababu mtu amekuwa akitumikia kwa muda mrefu zaidi wala kwa sababu ya muda ambao amekuwa mzee. Kwa hiyo imewapasa wale ambao wamekuwa katika utumishi wa Yehova muda mrefu zaidi wasijaribu kulazimisha wazee wengine wakubaliane na mawazo au maoni yao bali imewapasa wajifunze kufanya kazi pamoja nao kwa upendo, wakiwaheshimu inavyostahili kwa sababu ya “karama” yao ya huduma na matumizi yao ya karama hiyo wakiwa, wazee waliowekwa.
14. Paulo anatoa shauri gani juu ya kushirikiana ni wazee, nalo linawezaje kutumiwa na wote kundini.
14 Jambo ilo hilo linahusu wote katika kundi la Mungu kwa habari ya kufanya kazi pamoja na wazee. Hakuna hata mmoja wa wazee aliye mkamilifu, kwa hiyo lazima tujiangalie tusikuze makosa au kutokamilika kwa kibinadamu kwa mzee na kuelekea kudharau mashauri yake au maagizo yenye msingi wa Neno la Mungu. Hatuwezi kudharau mashauri ati kwa sababu hatupendi tabia fulani za kipekee za mzee fulani. Sivyo, bali lazima tuachilie makosa madogo na kutokamilika, kisha tutazame upendo wa mzee kwa Yehova na juhudi yake kwa utumishi Wake, tukijifunza kuheshimu wazee wote na kushirikiana na wote kundini. Paulo anakazia jambo hilo katika Waebrania 13:17, anaposema hivi: “Watiini wenye kuwaongoza, na kuwanyenyekea; maana hao wanakesha kwa ajili ya [nafsi] zenu, kama watu watakaotoa hesabu, ili kwamba wafanye hivyo kwa furaha wala si kwa kuugua; maana isingewafaa ninyi.” Ni vizuri kama nini kwa akina ndugu kufanya kazi kwa umoja na wazee na kuonyesha wanawapenda wao kwa moyo na kazi njema wanayofanya!
15. Ungetumiaje 1 Timotheo 1:5 kwa habari hii ya kupendana sana sana kwa moyo?
15 Naam, imetupasa tupende ndugu zetu wote kwa moyo safi, na kwa moyo wote. Kumbuka vile Paulo alivyomwambia Timotheo: “Mwisho wa agizo hilo ni upendo utokao katika moyo safi na dhamiri njema, na imani isiyo na unafiki.” (1 Tim. 1:5) Hiyo inamaanisha kwamba moyo wetu unasafishwa na kweli, nasi tukijiona tuna upungufu fulani katika kupenda ndugu zetu, imetupasa tuache kweli itakase maisha zetu kwa kulitumia Neno la Mungu mara nyingi zaidi. Moyo safi umepaswa utuchochee tuwe na uhusiano wenye afya, wa uaminifu na wenye mafaa na ndugu wote kundini. Ndipo dhamiri yetu itakapokuwa dhamiri njema kwa sababu itakuwa imetulia. Tutakuwa na hakika kwamba tunafanya yaliyo haki. Kwa vyepesi wengine wataweza kuona upendo wetu, kwa sababu hautakuwa wonyesho wa kinafiki. Upendo wa kweli ni sifa ya kimungu, sifa safi ya ndani iliyo halisi na inayotokana na moyo mwema, ulio safi.
16. Ni kwa njia gani imewapasa wazee watoe mashauri ikiwa wana upendo wa kweli kwa ndugu zao?
16 Wale ambao ni wazee kundini wanaweza kuonyesha upendo huo wa moyoni kwa ndugu zao kwa kuwa wenye huruma wanaposema nao. Katika habari hii unyenyekevu bila shaka ni wa maana. Mzee asijawe na kiburi, akidhani yu bora kuliko wengine kundini. Kila mmoja kundini ni mali yenye thamani, ni mmoja wa “kondoo” za Yehova. (Yohana 10:16) Kwa hiyo wakati wazee wanaposema na wengine na kuwapa mashauri, lazima wafikirie matokeo ya maneno au matendo yao juu ya wengine. Mashauri yao yatolewe kwa unyenyekevu na upole. Wagalatia sura ya sita, mstari wa kwanza, inaonyesha kwamba “roho ya upole” ni ya maana wakati mtu anapojaribu kusaidia ndugu kiroho. Basi, hiyo ndiyo njia ya upendo; mtu ajaribu kwa unyofu kusaidia mwingine wala si kujiweka kama mkubwa zaidi kuliko wengine au kama wa maana zaidi kwa sababu yao cheo.
UPENDO MWINGI SANA WA “AGAPE” WAONYESHWA NA WOTE
17, 18. Tunawezaje kufuata mashauri ya Paulo (a) ‘kuonya wasiokaa kwa utaratibu,’ na (b) ‘kutia moyo walio dhaifu’?
17 Katika 1 Wathesalonike 5:14, mtume Paulo alitoa mashauri mema juu ya vile SOTE katika kila kundi tunavyoweza kukunjuka tutimize mahitaji ya ndugu zetu, kwa njia hiyo tukikunjuka katika kupendana: “Ndugu, twawasihi, waonyeni wale wasiokaa kwa utaratibu.” Hapa hakuwa akisema na wazee tu kundini, bali na WOTE kundini. Huenda wakati fulani tukaona mtu fulani kundini akielekea kuingia katika mwenendo mbaya, na huo ungekuwa wakati wa kufaa kufuata shauri la Paulo ‘kuonya wasiokaa kwa utaratibu.’ Hiyo haimaanishi kwamba tungekaripia ndugu kwa ukali au pengine kuanza kupiga domo juu ya jambo analofanya. Sivyo, bali imetupasa tujaribu kumsaidia ndugu yetu kwa busara na kwa kipekee na kumwelekeza upande unaofaa, tukimtia moyo afuate matendo yafaayo na kuacha yasiyofaa. Bila shaka, tukiona kwamba jambo ni zito sana, ingekuwa vizuri kulizungumza na mmoja wa wazee anayeweza kumpa mashauri anayohitaji yeye asiyekaa kwa utaratibu.
18 Paulo aliandika pia kwamba imetupasa ‘tutie moyo walio dhaifu.’ (1 The. 5:14) Katika makundi mengi wako wazee wa umri, pengine wenye udhaifu wa mwili, ambao huenda wana huzuni kwa sababu hawawezi kuendesha utumishi wa shambani kama walivyokuwa wakifanya wakati mmoja. Huenda wakajiona hoi kidogo na kupungukiwa na uwezo wao. Tunaweza kuwasaidia kiroho inapohitajiwa na kuwaonyesha vile wote kundini wanavyothamini mfano wao mwema wa kuhudhuria mikutano na kushiriki katika utumishi, ingawa wanafanya hivyo kidogo, na kuwatia moyo kwa njia yo yote tuwezayo.
19. Kwa sababu gani huenda ndugu akawa dhaifu katika mambo fulani, nasi tunawezaje ‘kutia nguvu wanyonge’?
19 Katika andiko ilo hilo Paulo alishauri pia ‘tutie nguvu wanyonge.’ Pengine wewe umeona wengine walio wanyonge katika kazi ya kuhubiri au katika kuhudhuria mikutano. Unaweza kuzungumza na ndugu hao kwa upendo, na kujaribu kuwatia moyo, na nyakati nyingine, kufanya mipango inayofaa uwasaidie. Au huenda tukaona mtu fulani anayedhoofika katika imani, pengine kwa sababu ya kufikiri-fikiri juu ya matukio ya wakati ujao. Wako wengine wanaouliza sikuzote maulizo yasiyo na majibu ya Maandiko, nao wazee au wengine kundini wasipoweza kujibu maulizo yao, wanaanza kutilia mashaka utimizo wa unabii mbalimbali au hata kutia mashaka kwamba Yehova hatumii tengenezo lake leo. Tunawezaje kusaidia hao walio dhaifu? Bila shaka tunaweza kuwatia moyo wautambue ubora wa kundi, sivyo? Angalia vile Yehova anavyotumia tengenezo lake leo kufanya habari njema zihubiriwe! Hiyo ndiyo kazi aliyosema Yesu lazima ifanywe, nalo ni tengenezo gani jingine linaloifanya? (Mt. 24:14; 28:19, 20) Yesu alisema pia kwamba kungekuwa na jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ambayo ingetoa chakula cha kiroho kwa watu wa Mungu, na leo watu wa Yehova peke yao ndio wanaolishwa vizuri kiroho, kwa sababu ya kushirikiana na “mtumwa” huyo. (Mt. 24:45, 46) Kupitia kwalo tumeingia katika ushirika wa karibu na Yehova, Mwanawe na watu wake duniani. Tungeweza kwenda wapi tukiliacha tengenezo la Mungu leo? Hakuna kwingine ko kote kwa kwenda! (Yohana 6:66-69) Hili ndilo tengenezo moja peke yake analotumia, na ikiwa sisi wenyewe tunasadiki hilo, imetupasa tuweze kusaidia wengine walio dhaifu katika imani.
20. Paulo alimaanisha nini aliposema ‘tuvumilie na watu wote’?
20 Paulo aliandika pia, “Vumilieni na watu wote.” (1 The. 5:14) Kwa hiyo fadhili zetu na upendo wa kidugu umepaswa utie ndani kila mtu kundini. Imetupasa tuwe na nia ya kuachilia udhaifu na kutokamilika kwa kila mtu na kuvumilia watu wote, si kuvumilia wengine tu tunapoona ni vyepesi kufanya hivyo. Lazima tujifunze kuwa wenye saburi wala si kulaumu-laumu wengine wala kuwa wenye kudai. Kupatana na 1 Wathesalonike 5:15, tunataka ‘kuangalia mtu awaye yote asimlipe mwenziwe mabaya kwa mabaya; bali sikuzote tulifuate lililo jema, sisi kwa sisi na kwa watu wote.’ Katika mstari wa 13 wa sura iyo hiyo, Paulo alisema: “Iweni na amani ninyi kwa ninyi.” Kwa hiyo imetupasa sikuzote tujaribu kuwa na amani na ndugu zetu.
21. Upendo wetu umepaswa kuonyeshwaje katika mikutano ya Kikristo?
21 Imetupasa tuwe na upendo wenye kuonekana kwa ndugu zetu, si uliokufa. Umepaswa utie ndani kuhurumia ndugu zetu. Kwa mfano, tunapohudhuria mikutano yetu ya kundi, si vizuri kusema na wale tunaojua sana peke yao, bali imetupasa pia tutafute wapya na wenye haya au wanaokaa peke yao na kuwasalimu na kuzungumza nao. Kwa njia hiyo tunawatia moyo na kuwasaidia wajione kutulia na kufurahia ushirika wa ndugu. Wala tusingetaka kusahau watoto. Upendo wetu umepaswa utuongoze tuzungumze nao pia, na kuwasifu kwa jitihada zao nzuri katika kumtumikia Yehova Mungu. Imetupasa tuwajulishe namna tunavyofurahia mfano mwema wanaoweka katika kazi ya shambani na mwenendo wao mwema shuleni na nyumbani. Kwa njia hiyo tunawatia moyo kwa upendo waendelee kufuata njia inayofaa ya kumtumikia Yehova Mungu.
KUONYESHA UPENDO KWA VITU VYA KIMWIU
22. (a) Nyakati nyingine huenda ikawa lazima tuonyeshe upendo wetu kwa njia gani, naye Yesu aliwekaje mfano unaofaa? (b) Ni nyingine gani za njia kwazo tunaweza kuonyesha upendo kwa njia ya kimwili
22 Tunapozidi kuingia katika “wakati wa mwisho” wa taratibu hii ya kale tunajua kwamba kuna uhitaji wa kukaribiana zaidi nyakati zote katika kifungo cha upendo, tukiwa na juhudi nyingi katika kupendana. Huenda nyakati zikatokea tunapoona kwamba ndugu zetu wanahitaji msaada, nalo ni jambo zuri kama nini kwamba tunawajua sana na kuwapenda! Nyakati nyingine huenda isitoshe kutoa msaada wa kiroho tu, kwa maana huenda kukawa na uhitaji wa msaada wa kimwili. Yohana aliandika habari za uhitaji huu katika 1 Yohana 3:17 na 18: “Lakini mtu akiwa na riziki ya dunia, kisha akamwona ndugu yake ni mhitaji, akamzuilia huruma zake, je! upendo wa Mungu wakaaje ndani yake huyo? Watoto wadogo, tusipende kwa neno, wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.” Tukionyesha upendo kwa ndugu zetu kimwili, kwa kufanya hivyo tunakuwa pia tukiiga mfano mwema aliouweka Yesu. Tunakumbuka kwamba, nyakati nyingine alilisha umati wa watu chakula cha kimwili na cha kiroho pia hata wakaweza kurudi makwao bila kuzimia njiani. (Mt. 14:14-21; 15:32-38) Kwa hiyo huenda nyakati nyingine tukaweza kuonyesha upendo kwa njia ya kimwili pia. Huenda ndugu au dada zetu wa kiroho wakawa wagonjwa. Wakati huo tunaweza kuonyesha upendo mwingi sana kwa kuwafanyia mambo kama vile kuwaletea chakula, kuwasaidia kusafisha nyumba zao au kwenda dukani kuwanunulia vitu. Huenda wakawako wengine wanaohitaji msaada wafike mikutanoni na huenda tukawa na gari. Tunaweza kuonyesha upendo kwa njia yenye kufaa kwa kwenda mikutanoni pamoja nao. Naam, ziko njia nyingi sana ambazo kwazo upendo unaofaa unaweza kuonyeshwa sasa na wakati ujao, kwa kutoa msaada unaohitajiwa kwa njia ya kimwili.
23. Huenda tukatakiwa kufanya nini siku moja ikiwa tunao upendo mwingi sana kwa ndugu zetu?
23 Magumu yanawakabili watumishi wote wa Mungu leo, na kuna dalili zenye kuonyesha kwamba magumu hayo yataongezeka. Kwa hiyo ni jambo la hekima kufahamiana vizuri na ndugu zetu, sikuzote tukionyeshana upendo mwingi sana. Tunajua tunaishi katika “siku za mwisho” naye Shetani anajua hivyo pia. Akijua kwamba wakati wake ni mfupi, anayaletea mataifa ya dunia magumu mengi. Huenda sote tukapaswa kukabili hali zenye kuhatirisha uhai wetu wenyewe. Kisha huenda tukatakiwa kuonyesha namna ya upendo alioonyesha Yesu, kufikia hatua ya kutoa uhai wetu kwa ajili ya ndugu zetu. 1974 Yearbook (au Annuaire) of Jehovah’s Witnesses kinatoa mifano myema juu ya namna ndugu zetu katika Nazi ya Ujeremani walivyosaidiana kwa upendo wakikabiliwa na mateso makali sana. Kwa kweli walikuwa wanapendana sana nao wonyesho wa upendo huo ulikuwa wa kiroho na kimwili pia, wakisaidiana waendelee kuwa waaminifu katika utumishi wa Yehova na kulindana katika hali yo yote. Je! wewe utafanya hivyo? Je! wewe utalinda ndugu zako kwa upendo, usiwasaliti kamwe kamwe? Wakati ujao ulio karibu, huenda maisha zetu zenyewe zikategemea kupendana kwa njia hiyo.
24. Kwa sababu gani Mkristo hahitaji sheria zenye maelezo mengi juu ya kila hali kwa habari ya kuonyesha ndugu zake upendo?
24 Sasa hivi sote tunaweza kujengana tukiwa na roho ya upendo wa agápē. Hatuna haja ya kupewa sheria wala amri za kutuambia tunapopaswa kupendana. Kumbuka kwamba amri ya Yesu ya kupenda ilionyesha haitupasi kusita bali imetupasa tuchukue hatua ya kwanza kuonyesha ndugu zetu upendo nyakati zote. Tukiwa na upendo mwingi sana kwa ndugu zetu, mioyo yetu itatuchochea kutoa msaada wote tuwezao na po pote unapohitajiwa. Hivyo, kama Wakristo wa kweli, tutatokeza kwa kuonyeshana upendo, nao ulimwengu utaiona alama yenye kutambulisha ya upendo.
25, 26. (a) Upendo wa kweli unatendaje, kulingana na 1 Wakorintho 13:4-7? (b) Kwa sababu gani ni jambo la maana sana kupendana sana sana kwa moyo?
25 Katika 1 Wakorintho 13:4 mpaka 7, Paulo anatoa masimulizi mazuri sana ya namna upendo wa kweli wa Kikristo unavyopaswa kutenda. Anasema hivi: “Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabari; haujivuni; haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya; haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli; huvumilia yote; huamini yote; hutumaini yote; hustahimili yote.” Na katika mstari wa 8 mtume anaendelea kusema hivi: “Upendo haupungui neno wakati wo wote [“haushindwi kamwe,” NW].” Upendo huo unatakiwa, si kwa wazee na watumishi wa huduma peke yao, bali kwa Wakristo wote wanaoitwa mashahidi wa Yehova leo.
26 Naam, kama alivyosema Paulo, “upendo haushindwi.” Haimpasi Mkristo kuacha kupenda kamwe wala hakuna mpaka wa kupenda wala sheria inayoweza kupunguza upendo. Upendo wa kweli unaweza kuzoewa wakati wo wote na mahali po pote. Katika Warumi 13:8, Paulo alisema kwamba upendo ndiyo deni ya pekee ambayo Wakristo wamepaswa kuwa nayo wao kwa wao. Leo mwisho wa taratibu hii unakaribia mbio mbio. Kwa hiyo, kati ya nyakati zote, HUU ndio wakati wa kuwa na “juhudi nyingi katika kupendana.” (1 Pet. 4:8) Je! si kweli kwamba, kama watumishi wa Mungu, tunatumaini kuishi pamoja milele sisi kwa sisi? Hiyo inamaanisha imetupasa tutake pia kupendana milele. Kwa hiyo huu ndio wakati wa kuimarisha vifungo vyetu kama Wakristo na kusitawisha uwezo wa kupendana sana sana kwa moyo, kwa njia hiyo tukimwiga Mungu wetu mwenye upendo, Yehova.
—Kutoka The Watchtower, Sept. 1, 1975.