Mashahidi wa Yehova Wanaamini Nini?
“Tunataka kusikia kwako uonavyo wewe; kwa maana katika habari za madhehebu hiyo imejulikana kwetu kwamba inanenwa vibaya kila mahali.” (Matendo 28:22) Viongozi hao wa jumuiya katika Roma ya karne ya kwanza waliweka mfano mzuri sana. Wao walitaka kusikia kutokana na chanzo chenyewe badala ya kutokana na wachambuzi wa nje tu.
Vivyo hivyo, mambo yanasemwa dhidi ya Mashahidi wa Yehova leo mara nyingi, na lingekuwa kosa kutazamia kuujua ukweli juu yao kutokana na vyanzo vyenye kutangulia kuwa na maoni mabaya dhidi yao bila kujua ukweli. Kwa hiyo sisi tunafurahi kukueleza baadhi ya imani zetu kubwa-kubwa.
Biblia, Yesu Kristo, na Mungu
Sisi tunaamini kwamba “kila andiko limepewa kwa maongozi ya Mungu, na linafaa.” (2 Timotheo 3:16, Zaire Swahili Bible) Na ingawa watu fulani wanadai kwamba sisi si Wakristo kwa uhakika, wanalosema si kweli hata kidogo. Sisi tunaunga mkono kabisa ushuhuda wa mtume Petro kwa habari ya Yesu Kristo: “Hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.”—Matendo 4:12.
Hata hivyo, kwa kuwa Yesu alisema kwamba yeye ni “Mwana wa Mungu” na kwamba ‘Baba alinituma mimi,’ Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba Mungu ni mkuu kuliko Yesu. (Yohana 10:36; 6:57) Yesu mwenyewe alikiri hivi: “Baba ni mkuu kuliko mimi.” (Yohana 14:28; 8:28) Hivyo sisi hatuamini kwamba Yesu yuko sawa na Baba, kama vile fundisho la Utatu linavyosema. Bali, tunaamini kwamba yeye aliumbwa na Mungu na kwamba yeye ni mdogo kwa cheo kuliko Mungu.—Wakolosai 1:15; 1 Wakorintho 11:3.
Katika lugha ya Kiswahili, jina la Mungu ni Yehova. Biblia husema: “Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.” (Zaburi 83:18) Kupatana na tangazo hilo, Yesu aliweka mkazo mkuu juu ya jina la Mungu, akifundisha wafuasi wake kusali hivi: “Baba yetu katika mbingu, acha jina lako litakaswe.” Na yeye mwenyewe alipelekea Mungu sala hivi: “Mimi nimefanya jina lako lidhihirike kwa watu ulionipa mimi.”—Mathayo 6:9; Yohana 17:6, NW.
Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba inawapasa wao wawe kama Yesu katika kufanya jina na makusudi ya Mungu yadhihirike kwa wengine. Kwa sababu hiyo sisi tumelichukua jina Mashahidi wa Yehova kwa sababu tunaiga Yesu, ‘Shahidi aliye Mwaminifu.’ (Ufunuo 1:5; 3:14) Kwa kufaa, andiko la Isaya 43:10 linaambia watu wenye kuwakilisha Mungu hivi: “Ninyi ni mashahidi wangu, asema [Yehova, NW], na mtumishi niliyemchagua.”
Ufalme wa Mungu
Yesu alifundisha wafuasi wake kusali, “Ufalme wako uje,” na akafanya Ufalme huo uwe ndicho kichwa kikuu cha fundisho lake. (Mathayo 6:10; Luka 4:43) Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba Ufalme ni serikali halisi kutoka mbinguni, kwamba huo utatawala juu ya dunia, na kwamba Yesu Kristo ndiye Mfalme wao aliyewekwa rasmi asiyeonekana. “Serikali ile itakuwa juu ya bega lake,” Biblia inasema. “Kwa habari ya ongezeko la serikali yake na amani hakutakuwa na mwisho.”—Isaya 9:6, 7, tafsiri ya King James Version.
Hata hivyo, si Yesu Kristo peke yake atakayekuwa mfalme wa serikali ya Mungu. Yeye atakuwa na watawala-wenzi wengi pamoja naye mbinguni. “Ikiwa sisi tutaendelea kuvumilia,” mtume Paulo aliandika, “sisi tutatawala pia pamoja tukiwa wafalme.” (2 Timotheo 2:12, NW) Biblia inaonyesha kwamba hesabu ya wanadamu wale watakaofufuliwa watawale pamoja na Kristo mbinguni ni ndogo tu, nayo ni “mia na arobaini na nne elfu, walionunuliwa katika nchi.”—Ufunuo 14:1, 3.
Bila shaka, ni lazima serikali yo yote iwe na raia, na Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba mabilioni ya watu wengine zaidi ya watawala hao wa kimbingu watapokea uzima wa milele. Hatimaye dunia, ambayo itakuwa imegeuzwa kuwa paradiso yenye sura nzuri, itajawa na raia hao wastahilifu wa Ufalme wa Mungu, wote wakijiweka chini ya utawala wa Kristo na watawala-wenzi wake. Hivyo Mashahidi wa Yehova wanasadiki kwa imara kwamba dunia haitaharibiwa kamwe na kwamba ahadi hii ya Biblia itatimizwa: “Waadilifu wenyewe watamiliki dunia, nao watakaa milele juu yayo.”—Zaburi 37:29; 104:5, NW.
Lakini Ufalme wa Mungu utakujaje? Je! utakuja kwa njia ya mataifa yote kujitolea yajiweke chini ya serikali ya Mungu? Kinyume cha hivyo, Biblia inaonyesha kwa kufaa kwamba kuja kwa Ufalme huo kutataka Mungu ajiingize moja kwa moja katika mambo ya dunia: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele . . . bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.
Ufalme wa Mungu utakuja wakati gani? Kwa kutegemea msingi wa mambo ya unabii wa Biblia ambayo yanatimizwa sasa, Mashahidi wa Yehova wanaamini utakuja karibuni sana. Sisi tunakualika wewe ufikirie mambo fulani ya unabii yanayotabiri matukio yenye kuonyesha “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo ulio mbovu. Matukio hayo yameandikwa kwenye Mathayo 24:3-14; Luka 21:7-13, 25-31, NW; na 2 Timotheo 3:1-5.
Kwa sababu sisi ‘tunapenda Yehova Mungu wetu kwa moyo wetu wote, nafsi yote, akili zote, na nguvu zote, na jirani yetu kama sisi wenyewe,’ sisi hatuna migawanyiko ya kitaifa, kikabila, na kijamii. (Marko 12:30, 31, NW) Sisi tunajulikana kote kote kwa ajili ya upendo unaodhihirishwa miongoni mwa ndugu zetu Wakristo wanaopatikana katika mataifa yote. (Yohana 13:35; 1 Yohana 3:10-12) Hivyo sisi tunadumisha msimamo wa kutokuwamo kuelekea mambo ya kisiasa ya mataifa hayo. Sisi tunajaribu kuwa kama wanafunzi wa kwanza-kwanza wa Yesu, ambao yeye alisema hivi juu yao: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:16, NW) Sisi tunaamini kwamba kuendelea kujitenga na ulimwengu kunamaanisha kuepuka mwenendo wa ukosefu wa adili unaopatikana sana leo, kutia na kusema uwongo, kuiba, kufanya uasherati, uzinzi, ngono za watu wa jinsia moja, matumizi mabaya ya damu, ibada ya sanamu, na mambo mengine kama hayo yanayolaumiwa vikali katika Biblia.—1 Wakorintho 6:9-11; Waefeso 5:3-5; Matendo 15:28, 29.
Tumaini kwa Wakati Ujao
Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba maisha yetu ya sasa katika ulimwengu huu siyo tu yaliyopo. Sisi tunaamini kwamba Yehova alituma Kristo duniani amwage damu ya uhai wake iwe ukombozi ili wanadamu waweze kupata msimamo wenye uadilifu pamoja na Mungu na kupokea uzima wa milele katika mfumo mpya wa mambo. Kama vile mtume mmoja wa Yesu alivyosema: “Sasa sisi tumetangazwa rasmi kuwa waadilifu kwa damu yake.” (Warumi 5:9; Mathayo 20:28, NW) Mashahidi wa Yehova wana shukrani nyingi sana sana kwa Mungu na Mwanaye kwa ajili ya uandalizi huo wa ukombozi unaofanya maisha ya wakati ujao yawezekane.
Mashahidi wa Yehova wana hakika kamili katika maisha ya wakati ujao, yenye kutegemea ufufuo kutoka kwa wafu chini ya Ufalme wa Mungu. Sisi tunaamini, kama vile Biblia inavyofundisha, kwamba wakati mtu anapokufa anaacha kabisa kuwako, kwamba “siku hiyo mawazo yake yapotea.” (Zaburi 146:3, 4; Ezekieli 18:4; Mhubiri 9:5) Ndiyo, maisha ya wakati ujao kwa wafu yanategemea kukumbukwa kwao na Mungu katika ufufuo.—Yohana 5:28, 29.
Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wanasadiki kwamba watu wengi wanaoishi sasa wataokoka waendelee kuishi wakati Ufalme wa Mungu utakapoleta mwisho kwa serikali zote zilizopo na, kama vile Noa na jamaa yake walivyoiokoka Gharika, wao wataendelea kuishi wafurahie uzima milele katika dunia iliyosafishwa. (Mathayo 24:36-39; 2 Petro 3:5-7, 13) Lakini sisi tunaamini kwamba kuokoka huku kunategemea kutimiza matakwa ya Yehova, kama vile Biblia inavyosema: “Ulimwengu unapitilia mbali . . . , bali yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anabaki milele.”—1 Yohana 2:17, NW; Zaburi 37:11; Ufunuo 7:9, 13-15; 21:1-5.
Kwa wazi, haiwezekani hapa kumaliza kueleza imani zote za Mashahidi wa Yehova, lakini sisi tunakualika wewe upate habari zaidi.
Isipokuwa imeonyeshwa vingine, mitajo yote ya Biblia imetolewa katika Biblia ya Union Version na New World Translation of the Holy Scriptures (NW) ya Kiingereza.
[Blabu katika ukurasa wa 4]
Sisi tumelichukua jina Mashahidi wa Yehova kwa sababu sisi tunaiga Yesu