Sura ya 1
Ufunuo—Upeo Wao Wenye Furaha!
1. Twajuaje Mungu ataka tuwe wenye furaha?
UFUNUO KWA YOHANA—kitabu hiki cha Biblia chenye kusisimua kinaleta maandishi ya kimungu kwenye upeo wenye furaha. Kwa nini tunasema “wenye furaha”? Basi, Mtungaji wa Biblia anaelezwa kuwa “Mungu mwenye furaha,” ambaye huaminisha “habari njema tukufu” kwa wale wanaompenda. Yeye anataka sisi pia tuwe wenye furaha. Hivyo, kwenye mwanzo Ufunuo unatuhakikishia hivi: “Mwenye furaha ni yeye ambaye husoma kwa sauti kubwa . . . maneno ya unabii huu.” Katika sura yao ya kumalizia tunaambiwa hivi: “Mwenye furaha ni yeyote anayeshika maneno ya unabii wa hati-kunjo hii.”—1 Timotheo 1:11; Ufunuo 1:3; 22:7, NW.
2. Ni lazima tufanye nini ili tupate furaha kupitia kitabu cha Ufunuo?
2 Sisi tunapataje furaha kupitia kitabu cha Ufunuo? Tunafanya hivyo kwa kupeleleza-peleleza maana ya ishara, au alama zacho zilizo wazi, na kutenda kupatana nazo. Historia yenye msukosuko ya aina ya binadamu karibuni itafikia upeo wayo wenye msiba mkuu, Mungu na Yesu Kristo wafikilizapo hukumu juu ya mfumo mbovu wa leo na kuweka mahali pao “mbingu mpya na dunia mpya,” ambamo hata ‘kifo hakitakuwa tena.’ (Ufunuo 21:1, 4, NW) Je! sisi sote hatutaki kuishi katika ulimwengu mpya kama huo, katika amani na usalama wa kweli? Tunaweza tukijenga imani yetu kupitia funzo la Neno la Mungu, kutia na unabii wa Ufunuo wenye kuchochea.
Apokalipsi—Ni Nini?
3. Watu wengi wanafikiri Apokalipsi na Har–Magedoni humaanisha nini?
3 Je! Ufunuo hauitwi pia Apokalipsi? Ndivyo, “ufunuo” ukiwa tafsiri ya Kiswahili ya a·po·kaʹly·psis katika hati ya Kigiriki. Watu wengi huweka Apokalipsi katika usawa na uharibifu wa ulimwengu kupitia vita ya nyukilia. Katika jiji moja la Teksasi, U.S.A., ambako hesabu kubwa za vichwa vyenye baruti za nyukilia vilikuwa vikifanyizwa, watu wenye maelekeo ya kidini walikuwa wakisema, “Sisi ndio tutakuwa wa kwanza kuangamia.” Viongozi wa kidini katika eneo hilo waliripotiwa kuwa “walisadikishwa kwamba Har–Magedoni si isiyoepukika tu bali pia imekaribia karibu, na kwamba ile vita ya mwisho kati ya kani za wema na ubaya, ya Mungu na Shetani, itatukia ikiwa maangamizi makubwa ya nyukilia.”a
4. Neno “apokalipsi” humaanisha nini hasa, na ni kwa sababu gani kitabu cha mwisho cha Biblia kwa kufaa kinaitwa “Ufunuo”?
4 Lakini apokalipsi ni nini hasa? Ingawa kamusi huifafanua kwa kutumia semi kama vile “msiba mkubwa wa ulimwengu wote mzima ulio karibu sana,” ile a·po·kaʹly·psis ya Kigiriki humaanisha kwa msingi “kuondoa shela” au “kugubua.” Hivyo, kile kitabu cha mwisho cha Biblia kinaitwa kwa kufaa “Ufunuo.” Hapa tunapata, si ujumbe wa vivi hivi wenye msiba utakaopata ulimwengu uliohukumiwa, bali kugubuliwa kwa kweli za kimungu zinazopasa kujenga katika mioyo yetu tumaini jangavu na imani isiyoondoleka.
5. (a) Ni nani wataharibiwa kwenye Har–Magedoni, na ni nani wataokoka? (b) Ni wakati ujao gani mtukufu unaongojea waokokaji wa Har–Magedoni?
5 Ni kweli, Har–Magedoni inaelezwa katika kitabu cha mwisho cha Biblia kuwa “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.” (Ufunuo 16:14, 16) Lakini itakuwa tofauti sana na maangamizi ya nyukilia! Maangamizi kama hayo inaelekea yangemaanisha utowesho wa uhai wote duniani. Tofauti na hilo, Neno la Mungu linatoa uhakikisho wenye furaha kwamba waovu tu wapingaji wa Mungu ndio wataharibiwa—na kani zilizo chini ya udhibiti wa Mungu. (Zaburi 37:9, 10; 145:20) Kundi kubwa la binadamu, kutoka mataifa yote, litaokoka upeo wa hukumu ya kimungu kwenye Har–Magedoni. Kisha Kristo Yesu atachunga na kuwaongoza kwenye uhai wa milele katika dunia paradiso. Je! wewe hutaki kuwa mmoja wao? Kwa furaha, Ufunuo unaonyesha kwamba huenda ukawa!—Ufunuo 7:9, 14, 17.
Kupeleleza-peleleza Siri za Kimungu
6. Kwa muda wa miaka iliyopita, ni vitabu gani ambavyo vimetangazwa na Mashahidi wa Yehova kutoa nuru juu ya Ufunuo?
6 Mapema kama 1917, Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi ilitangaza kitabu The Finished Mystery. Hiki kilikuwa maelezo ya mstari kwa mstari juu ya vitabu vya Biblia vya Ezekieli na Ufunuo. Kisha, kadiri matukio ya ulimwengu yalivyoendelea kufunuka katika utimizo wa unabii wa Biblia, kitabu chenye mabuku mawili kilichoitwa Light kilitayarishwa, kikatolewa katika 1930. Hicho, kilitoa funzo la uchunguzi wa kisasa wa Ufunuo. Nuru iliendelea ‘kumulikia waadilifu,’ hivi kwamba katika 1963 Mashahidi wa Yehova walitangaza kitabu chenye kurasa 704 “Babylon the Great Has Fallen!” God’s Kingdom Rules! Hicho kilitoa kwa urefu historia ya kuinuka na kuanguka kwa Babuloni Mkubwa, ile milki ya ulimwengu ya dini bandia, nacho kililetwa kwenye upeo kwa zungumzo la sura tisa za mwisho za Ufunuo. Kadiri ‘kile kijia cha waadilifu kilivyoendelea kuwa changavu zaidi,’ hasa kwa habari ya utendaji wa kundi, katika 1969 lilifuata buku lenye kurasa 384, “Then Is Finished the Mystery of God,” ambalo lilizungumzia sura 13 za kwanza za Ufunuo.—Zaburi 97:11; Mithali 4:18, NW.
7. (a) Kwa nini Mashahidi wa Yehova waliandaa kitabu hiki juu ya Ufunuo? (b) Ni misaada gani ya kufundisha imeandaliwa katika kitabu kwa manufaa ya wasomaji?
7 Kwa nini kitabu kingine juu ya Ufunuo kilitangazwa na kuchapwa upya wakati uliopo? Habari iliyo nyingi ambayo imetokea tayari ni yenye mambo mengi-mengi, na haikuwezekana kuitafsiri na kuitangaza ulimwenguni pote katika lugha nyingi. Kwa sababu hiyo, ilionekana inafaa kuandaa kitabu juu ya Ufunuo katika buku moja na kwa namna ambayo inaweza kutolewa kwa urahisi katika lugha kadhaa. Zaidi, fursa inachukuliwa katika buku hili kuandaa misaada ya kufundisha, kutia na vielezi, chati, na mihtasari, ambayo yapasa kusaidia wasomaji wafahamu waziwazi maana yenye kusisimua ya unabii huu mzuri ajabu.
8. Kuna sababu gani yenye nguvu hata zaidi kwa kutangazwa kwa kitabu hiki?
8 Sababu yenye nguvu zaidi ya kutangaza kitabu hiki ni ule uhitaji wa kwenda sambamba na ukweli wa sasa. Kwa kuendelea Yehova anaangaza nuru kubwa zaidi juu ya maana ya Neno lake, na sisi tunaweza kutazamia kwamba uelewevu wetu wa Ufunuo, pamoja na wa unabii mwingine, utaongezewa kadiri sisi tunavyokaribia zaidi ile dhiki kubwa. (Mathayo 24:21; Ufunuo 7:14) Ni jambo la maana sisi tupashwe habari. Kama alivyoandika mtume Petro kuhusu unabii wa kimungu: “Nyinyi mnafanya vizuri katika kulitolea uangalifu kama taa inayong’aa mahali penye giza, mpaka siku ipambazuke na nyota ya mchana izuke, ndani ya mioyo yenu.”—2 Petro 1: 19, NW.
9. (a) Pamoja na unabii mwingine, Ufunuo unaonyesha kwamba Mungu ataumba nini? (b) Ule ulimwengu mpya ni nini, na huenda wewe ukaokokaje hata kuuingia?
9 Ufunuo unaongeza ushuhuda wao kwenye unabii mwingine mwingi wa Biblia, kuonyesha kwamba Yehova Mungu anakusudia kuumba mbingu mpya na dunia mpya. (Isaya 65:17; 66:22; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:1-5) Kwanza kabisa, ujumbe wao unaelekezwa kwa Wakristo wapakwa-mafuta ambao Yesu amenunua kwa damu yake wakawe watawala wenzi pamoja naye katika mbingu. (Ufunuo 5:9, 10) Hata hivyo, habari njema hizi zitaimarisha pia imani ya yale mamilioni yanayotazamia uhai wa milele chini ya Ufalme wa Kristo. Je! wewe ni mmoja wa hawa? Basi Ufunuo utaimarisha tumaini lako la kuishi katika Paradiso, ukiwa sehemu ya ile dunia mpya, pamoja na mfurahio wa amani tele, afya yenye nishati nyingi, na mfuriko wa maandalizi ya Mungu ambayo hayatakoma kamwe. (Zaburi 37:11, 29, 34; 72:1, 7, 8, 16) Ikiwa wewe unataka kuokoka na kuingia ndani ya ulimwengu huo mpya, ni jambo la muhimu, ndiyo, la lazima, utoe uangalifu kwenye usimulizi dhahiri wa Ufunuo kuhusu upeo ulio karibu wenye kufanyiza kipindi maalumu cha historia.—Sefania 2:3; Yohana 13:17.
[Maelezo ya Chini]
a Süddeutsche Zeitung, Munich, Ujeremani, Januari 24, 1987.
[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 7]