Sura ya 10
Kukirihi “Vitu Vyenye Kina Kirefu vya Shetani”
THIATIRA
1. Thiatira lilikuwa mahali gani kuhusiana na makundi mengine, na lilikuwa na mazingira ya kidini ya namna gani?
KILOMETA zapata 68 kusini-mashariki mwa Bargama (Pargamamu) kuna Akhisari, mji wa Kituruki wenye kusitawi. Yapata miaka 1,900 iliyopita, mji huu ndipo mahali lilipokuwa Thiatira. Mwangalizi asafiriye angeweza kwa urahisi kufikia Thiatira kwa barabara ya barani kutoka Pargamamu na kisha azunguke kwenye makundi yanayobaki ya Ufunuo sura ya 3—Sardisi, Filadelfia, na Laodikia. Tofauti na Pargamamu, Thiatira halionekani kuwa lilikuwa kitovu chenye maana cha ibada ya maliki, lakini lilikuwa na vihekalu na mahekalu yaliyowekwa wakfu kwa tumungu twa kipagani. Thiatira lilikuwa na sifa ya kuwa kitovu cha biashara ya kiuchumi.
2, 3. (a) Ni nini lililokuwa limeandikwa mapema zaidi juu ya Mthiatira mmoja aliyepata kuwa Mkristo? (b) Kuna umaana gani kwa Wakristo katika Thiatira kwamba Yesu ni “Mwana wa Mungu” na kwamba yeye ana “macho kama mwali wenye moto”?
2 Paulo alipokuwa akihubiri Makedonia, alikutana na mwanamke wa Thiatira aliyeitwa Lidia, muuza zambarau. Lidia pamoja na watu wote wa nyumba yake walikubali kwa mteremo ujumbe aliokuwa akihubiri Paulo na akaonyesha ukaribishaji-wageni usio wa kawaida. (Matendo 16:14, 15) Akawa Mthiatira wa kwanza kutiwa kwenye maandishi aliyekubali Ukristo. Baada ya muda fulani, jiji lenyewe likaja kuwa na kundi la Wakristo. Yesu anaelekeza huko ujumbe wake ulio mrefu kupita zote: “Na kwa malaika wa kundi katika Thiatira andika: Hivi ndivyo vitu ambavyo Mwana wa Mungu asema, yeye ambaye ana macho yake kama mwali wa moto, na nyayo zake kama shaba safi.”—Ufunuo 2:18, NW.
3 Huu ndio wakati pekee ambapo usemi “Mwana wa Mungu” unaonekana katika Ufunuo, ingawa mahali kwingine Yesu humtaja Yehova kuwa “Baba yangu.” (Ufunuo 2:27; 3:5, 21) Tumizi la jina hilo la cheo hapa inaelekea linakumbusha Wakristo wa Thiatira juu ya uhusiano wa karibu alio nao Yesu pamoja na Yehova. Mwana huyu “ana macho yake kama mwali wa moto”—onyo kwa Wakristo katika Thiatira kwamba hukumu yake itawaka dhidi ya chochote anachoona kuwa kinachafua kundini. Kwa kurejeza mara ya pili kwenye nyayo zake zenye kuwaka, zilizo kama shaba, yeye anakazia kielelezo chake mwenyewe cha uaminifu wenye kung’aa alipokuwa akiitembea dunia hii. Wale Wakristo katika Thiatira bila shaka walitii shauri hili, na ndivyo nasi lazima tutii leo!—1 Petro 2:21.
4, 5. (a) Ni kwa nini Yesu angeweza kusifu Wakristo katika Thiatira? (b) Kundi katika Thiatira ni kifananishi jinsi gani leo cha makundi ya Mashahidi wa Yehova?
4 Kwa furaha, Yesu anaweza kusifu hao waliomo Thiatira. Yeye anasema: “Mimi najua matendo yako, na upendo wako na imani na huduma na uvumilivu, na kwamba matendo yako ya baadaye yanazidi yale ya hapo kwanza.” (Ufunuo 2:19, NW) Tofauti na Waefeso, Wakristo wapakwa-mafuta huko hawakupoteza ule upendo wao wa kwanza kwa ajili ya Yehova. Imani yao ni thabiti. Zaidi ya hilo, matendo yao yanazidi yale ya hapo kwanza, na kama vile yale makundi matatu yaliyotangulia, Wakristo katika Thiatira wanavumilia. Ni kifananishi kama nini cha yale makundi karibu 100,000 ya Mashahidi wa Yehova kotekote duniani leo! Upendo kwa ajili ya Yehova unang’aa kwa kupenya, kwa kuwa roho ya bidii katika huduma inaenea pote katika tengenezo, ikichochea wachanga na wazee. Nambari inayozidi kuongezeka wanajitumikisha wenyewe wakiwa mapainia, hivyo wakitumia kwa hekima ule wakati ambao ungali unabaki kutangaza tumaini tukufu la Ufalme wa Yehova unaokuja!—Mathayo 24:14; Marko 13:10.
5 Kwa miongo fulani, waaminifu wengi, wa mabaki ya wapakwa-mafuta na ule umati mkubwa pia, wamekuwa wakionyesha kielelezo kizuri cha uvumilivu katika utumishi wa Mungu, huku ulimwengu unaowazunguka ukiwa umekuwa ukizidi kutumbukia ndani ya giza zito lisilo na tumaini. Lakini acheni sisi tuwe na ushujaa! Ufunuo unathibitisha ule ushahidi wa manabii wa Mungu wakati wa mapema zaidi. “Hiyo siku ya Bwana [Yehova, NW] iliyo kuu i karibu; i karibu, nayo inafanya haraka sana.”—Sefania 1:14; Joeli 2:1; Habakuki 2:3; Ufunuo 7:9; 22:12, 13.
“Huyo Mwanamke Yezebeli”
6. (a) Yajapokuwa mambo yenye kusifika, ni tatizo gani analoona Yesu katika kundi la Thiatira linalohitaji uangalifu wa mara moja? (b) Yezebeli alikuwa nani, na je! yeye alikuwa na dai halali la kuwa nabii wa kike?
6 Macho yenye moto ya Yesu yamepenya zaidi. Yeye anaona jambo linalohitaji uangalifu wa mara moja. “Hata hivyo,” yeye anawaambia Wakristo katika Thiatira, “mimi nina hili dhidi yako, kwamba wewe wavumilia huyo mwanamke Yezebeli, ambaye hujiita mwenyewe nabii wa kike, naye huwafundisha na kuongoza vibaya watumwa wangu wafanye uasherati na kula vitu vilivyodhabihiwa kwa sanamu.” (Ufunuo 2:20, NW) Katika karne ya kumi K.W.K., Malkia Yezebeli, mke mwabudu Baali wa Mfalme Ahabu wa Israeli, alikuwa amekuwa mwenye sifa mbaya sana kwa sababu ya njia zake za kuua kimakusudi, kufanya uzinzi na za kutawala. Yehu, akiwa mpakwa-mafuta wa Yehova, aliagiza auawe. (1 Wafalme 16:31; 18:4; 21:1-16; 2 Wafalme 9:1-7, 22, 30, 33) Yezebeli mwabudu-sanamu hakuwa na dai la kuwa nabii wa kike. Yeye hakuwa kama Miriamu na Debora, waliotumikia wakiwa manabii wa kike waaminifu katika Israeli. (Kutoka 15:20, 21; Waamuzi 4:4; 5:1-31) Na roho ya Yehova haikumsukuma atoe unabii kama ilivyosukuma Ana mwenye umri wa uzee na wale mabinti wanne wa Filipo mweneza-evanjeli.—Luka 2:36-38; Matendo 21:9.
7. (a) Kwa kutaja “huyo mwanamke Yezebeli,” kwa wazi Yesu anarejezea uvutano gani? (b) Huenda wanawake washiriki fulani wakawa waliteteaje mwendo wao wa kujitakia yao?
7 Kwa wazi, basi, “huyo mwanamke Yezebeli” anayedai kuwa nabii wa kike katika Thiatira ni bandia. Yeye hana utegemezo wa roho ya Mungu. Yeye ni nani? Inaelekea, yeye ni mwanamke au kikundi cha wanawake wanaotenda wakiwa uvutano wenye kufisidi na usio na haya katika kundi lile. Wanawake washiriki fulani huenda wakawa walikuwa wakiwahusisha washiriki katika ukosefu wa adili, huku wakitetea kwa ukavu wa macho mwendo wao wa kujitakia yao kwa kutumia maandiko kimakosa. Kutoa unabii kibandia kweli kweli! Wangevuta wengine waangukie njia zao wenyewe za “uasherati, ukosefu wa usafi, hamu ya ngono, tamaa yenye kudhuru, na uchoyo, ambao ni ibada ya sanamu.” (Wakolosai 3:5, NW) Wangetaka wale waliomo kundini washiriki katika mtindo wa maisha wenye ukosefu wa adili, kujitafutia yao wenyewe kwa namna ile ambayo sasa inakubaliwa, au kuachiliwa, katika dini zilizo nyingi za Jumuiya ya Wakristo.
8. (a) Ni nini tamko la hukumu la Yesu juu ya yule “Yezebeli” katika Thiatira? (b) Uvutano wa kike usiofaa umehisiwaje katika nyakati za ki-siku-hizi?
8 Yesu anaendelea kuwaambia wazee katika Thiatira hivi: “Na mimi nilimpa wakati wa kutubu, lakini yeye hataki kutubu uasherati wake. Tazama! Mimi niko karibu kutupa yeye katika kitanda cha ugonjwa, na wale wanaofanya uasherati pamoja na yeye katika dhiki kubwa, wasipotubu matendo yake.” (Ufunuo 2:21, 22, NW) Kama vile yule Yezebeli wa kwanza kabisa kwa wazi alivyomtawala Ahabu na kisha akamkaidi Yehu, mfishaji wa Mungu, ndivyo uvutano huu wa kike huenda ukawa unajaribu kutumia hila juu ya waume na wazee. Inaonekana kwamba wazee katika Thiatira wanavumilia uvutano huu usio na kiasi wa Yezebeli. Hapa Yesu anatoa onyo kali kwao, pamoja na kwa kundi lililo kwenye tufe lote la watu wa Yehova leo. Katika nyakati za ki-siku-hizi, baadhi ya wanawake kama hao wenye nia ngumu wameshawishi waume zao wawe waasi-imani na hata wamechukua hatua ya kimahakama dhidi ya watumishi waaminifu wa Yehova.—Linga Yuda 5-8.
9. (a) Ni kwa nini maneno ya Yesu juu ya Yezebeli hayaonyeshi sifa mbaya juu ya wanawake wote katika kundi? (b) Ni wakati gani tu uvutano wa Kiyezebeli unapozuka?
9 Hili kwa vyovyote halionyeshi sifa mbaya juu ya wanawake waaminifu katika kundi la Kikristo. Siku hizi, sehemu kubwa ya kazi ya kutoa ushuhuda inatimizwa na akina dada waaminifu; kupitia mafunzo ya Biblia ya nyumbani wanayoongoza, wanaleta ndani ya kundi misongamano ya watu wapya. Mungu mwenyewe anabariki mpango huu, kama inavyoonyeshwa na Zaburi 68:11, NW: “Yehova mwenyewe hutoa usemi; wanawake wanaosimulia habari njema ni jeshi kubwa.” Huenda waume wakavutwa kwa mema na mwenendo wa upole, wenye staha wa wake zao, ambao “ni wenye thamani kubwa katika macho ya Mungu.” (1 Petro 3:1-4, NW) Mke hodari, mwenye bidii ya kufanya kazi anasifiwa na Mfalme Lemueli. (Mithali 31:10-31, NW) Ni wakati tu wanawake wanaporuka mpaka kwa kutongoza wanaume au kwa kukaidi au kupuuza ukichwa ndipo uvutano wa Kiyezebeli unapozuka.—Waefeso 5:22, 23; 1 Wakorintho 11:3.
10. (a) Ni kwa nini Yezebeli na watoto wake walipokea hukumu? (b) Wale wanaokuwa watoto wa Yezebeli wako katika hali gani ya hatari, na watu kama hao imewapasa wafanye nini?
10 Akirejezea “huyo mwanamke Yezebeli,” Yesu anaendelea: “Na watoto wake mimi nitaua kwa tauni yenye kufisha, ili makundi yote yajue kwamba mimi ndiye ambaye huchunguza figo na mioyo, na mimi nitatoa kwa nyinyi mmoja mmoja kulingana na matendo yenu.” (Ufunuo 2:23, NW) Yesu ameruhusu Yezebeli na watoto wake wakati wa kutubu, lakini wao wanaendelea katika njia zao za ukosefu wa adili na kwa sababu hiyo lazima wapokee hukumu. Hapa pana ujumbe wenye nguvu nyingi kwa Wakristo leo. Wale wanaoiga Yezebeli, wawe ni wanaume au wanawake, na hivyo wamekuwa watoto wake kwa kuhalifu kanuni za Biblia juu ya ukichwa na maadili au kwa kuwa wenye kichwa kigumu hivi kwamba wanapuuza utaratibu wa kitheokrasi, kwa njia ya kiroho wamo katika hali yenye hatari sana ya ugonjwa. Ni kweli, ikiwa mmoja kama huyo anawaita wazee katika kundi wakamwombee, hiyo “sala ya imani itafanya huyo asiye na maelekeo mazuri ahisi vema, na Yehova atainua yeye”—maadamu yeye anatenda kwa unyenyekevu kupatana na sala hizo. Lakini yeyote asifikiri kwamba yeye anaweza kudanganya Mungu au Kristo kwa kujaribu kuficha matendo ya ukosefu wa adili au kwa kujivika wonyesho wa nje-nje wa utumishi wenye bidii.—Yakobo 5:14, 15, NW.
11. Makundi leo yanasaidiwa jinsi gani yakae macho ili yaone upenyezi wa uvutano wa kike usio halali?
11 Kwa furaha, yaliyo mengi ya makundi ya Mashahidi wa Yehova leo yako macho kuona hatari hii. Wazee wanalinda waone miendo ya mielekeo isiyo ya kitheokrasi na utendaji makosa. Wanajaribu kusaidia wanaume na wanawake walio katika njia ya hatari ili hao wajenge hali ya kiroho na kurekebishwa kabla haijawa kuchelewa mno. (Wagalatia 5:16; 6:1) Kwa upendo na kwa uthabiti, waangalizi hawa Wakristo wanazuia jitihada yoyote ya kike ya kufanyiza vikundi vikundi vya kuendeleza miendo kama ile ya ukombozi wa wanawake. Zaidi ya hilo, pindi kwa pindi shauri la wakati wenye kufaa linatolewa katika vichapo vya Mashahidi wa Yehova.a
12. Ni kwa njia gani jamii ya Yohana leo inaonyesha bidii kama ile ya Yehu?
12 Hata hivyo, kunapokuwa na ukosefu wa adili mbaya sana, na hasa hilo linapokuwa ni zoea, watenda dhambi wasiotubu lazima watengwe na ushirika. Sisi tunakumbuka bidii ya Yehu katika kuondolea mbali dalili zote za uvutano wa Kiyezebeli katika Israeli. Hali moja na hiyo, ile jamii ya Yohana leo inachukua tendo thabiti, ikiwawekea kielelezo waandamani wenzao wa jamii ya “Yonadabu” na kujionyesha wenyewe kuwa tofauti kwa mbali sana na wahudumu wenye kuendekeza wa Jumuiya ya Wakristo.—2 Wafalme 9:22, 30-37; 10:12-17.
13. Ni nini litakalowapata wale wanaoshindwa na uvutano wenye makosa wa kike?
13 Akiwa Mjumbe na Hakimu wa Yehova, Mwana wa Mungu anatenda kwa usahihi katika kutambulisha Yezebeli wa ki-siku-hizi na kumtupa ndani ya kitanda cha ugonjwa, kwa kuwa ugonjwa wake wa kiroho ni wenye kusendeka kweli kweli. (Malaki 3:1, 5) Wale ambao wameshindwa na uvutano huu wenye makosa wa kike pia watapatwa na dhiki kubwa—ile huzuni ya kutengwa na ushirika, kukatiliwa mbali na kundi la Kikristo kama kwamba ni wafu. Isipokuwa hawa wanatubu, wanageuka, na wanakubaliwa tena ndani ya kundi, wanakabili pia kifo cha kimwili kwa “tauni yenye kufisha”—mwishowe kabisa, katika ile dhiki kubwa. Kwa wakati huu, kurudishwa kunawezekana ikiwa wanatubia kabisa matendo yao yenye kosa.—Mathayo 24:21, 22; 2 Wakorintho 7:10.
14. (a) Yesu anatumiaje wazee katika kushughulikia matatizo fulani, kama vile uvutano wowote wa Kiyezebeli? (b) Imelipasa kundi liungeje mkono wazee wanaoshughulikia matatizo kama hayo?
14 “Makundi yote” lazima yaje kujua kwamba Yesu anachunguza “figo,” zile hisia zenye kina kirefu zaidi sana, na ‘moyo,’ yule mtu wa ndani-ndani zaidi, kutia na makusudio yaliyo chinichini. Kutimiza hilo, yeye anatumia nyota, au wazee wenye kuitibarika, katika kushughulikia matatizo fulani fulani, kama vile uvutano wowote wa Kiyezebeli unaotokea. (Ufunuo 1:20, NW) Baada ya hawa wazee kuchunguza kikamili jambo fulani la aina hii na hukumu imekwisha pitishwa, si juu ya watu mmoja mmoja kuchungua-chungua ni kwa sababu gani na kwa nini hatua ilichukuliwa vile. Wote wamepaswa kukubali kwa unyenyekevu kumalizwa kwa mambo na wazee na kuendelea kuunga mkono nyota hizi za kundi. Ushikamanifu kwa Yehova na kwa mipango yake ya kitengenezo utathawabishwa. (Zaburi 37:27-29; Waebrania 13:7, 17) Kwa upande wako mwenyewe, fungu lako na liwe baraka wakati Yesu anampa kila mtu mmoja mmoja kulingana na matendo yake.—Wagalatia 5:19-24; 6:7-9.
‘Shikilia kwa Imara Ulicho Nacho’
15. (a) Yesu alikuwa na vitu gani vya kusema kwa wale ambao hawakufisidiwa na Yezebeli? (b) Ni jambo gani linaloonyesha kwamba si wote waliodai kuwa Wakristo huko nyuma katika 1918 walikuwa wamefisidiwa na Jumuiya ya Wakristo yenye kuasi imani?
15 Maneno yanayofuata ya Yesu yanaleta faraja: “Hata hivyo, mimi nasema kwa nyinyi wengine mliomo Thiatira, wale wote ambao hawana fundisho hili, wale hasa ambao hawakupata kujua ‘vitu vyenye kina kirefu vya Shetani,’ kama wasemavyo: Mimi siweki juu yenu nyinyi mzigo mwingine wowote. Hata hivyo, shikilieni kwa imara kile mlicho nacho mpaka mimi nije.” (Ufunuo 2:24, 25, NW) Kuna nafsi zenye uaminifu katika Thiatira ambazo hazikuvutwa na Yezebeli. Hali moja na hiyo, kwa miaka 40 kabla ya 1918 na tangu hapo, si Wakristo wote waliovumilia njia za ukosefu wa adili, zenye ufisadi ambazo zimeenea sana katika Jumuiya ya Wakristo. Kile kikosi kidogo cha Wanafunzi wa Biblia, kinachojulikana sasa kuwa Mashahidi wa Yehova, kilichojaribu kusaidia washiriki wa kanisa waone asili isiyo ya Kikristo ya mengi ya mafundisho ya Jumuiya ya Wakristo, kimechukua hatua ya kujiondolea itikadi zote za Kibabuloni na mazoea yaliyopokewa kupitia Jumuiya ya Wakristo yenye kuasi imani. Hii inatia ndani fundisho lenye kuendekeza la “huyo mwanamke Yezebeli.”
16. Ingawa Yesu na baraza lenye kuongoza la Kikristo la karne ya kwanza hakuongeza mzigo zaidi, ni vitu gani ambavyo lazima viepukwe?
16 Ile jamii ya Yohana leo imetia moyo pia waandamani wao, ule umati mkubwa, kujihadhari na mavutano ya ukosefu wa adili, kama yale yaliyomo katika ulimwengu wa matumbuizo wenye kushusha tabia. Hakuna haja ya kuona au kujaribu ufisadi kwa sababu ya udadisi au ili kujifunza cha kuepuka. Ni mwendo wa hekima kukaa mbali sana na “vitu vyenye kina kirefu vya Shetani.” Kama asemavyo Yesu: “Mimi siweki juu yenu nyinyi mzigo mwingine wowote.” Hili linatukumbusha ile amri ya baraza lenye kuongoza la Kikristo la karne ya kwanza. “Roho takatifu na sisi wenyewe tumependelea tusiongeze mzigo zaidi kwenu nyinyi, isipokuwa vitu hivi vya lazima, kuendelea kushika mwiko wa vitu vilivyotolewa dhabihu kwa sanamu na wa damu na wa vitu vilivyonyongwa na wa uasherati. Ikiwa kwa uangalifu mnajiepusha nyinyi wenyewe na vitu hivyo, mtafanikiwa.” (Matendo 15:28, 29, NW) Kwa ajili ya ufanisi wa kiroho, epuka dini bandia, tumizi baya la damu (kama vile kutiwa damu mishipani) na ukosefu wa adili! Na yaelekea afya yako ya kimwili itapewa himaya vilevile.
17. (a) Shetani ameshawishije watu leo kwa “vitu vyenye kina kirefu”? (b) Mwelekeo wetu umepaswa kuwa nini juu ya “vitu vyenye kina kirefu” vya ulimwengu wa Shetani wenye kutatanisha?
17 Shetani ana “vitu vyenye kina kirefu” vingine leo, kama vile makisio-makisio magumu na falsafa ambazo husifu-sifu mno ule uwezo wa akili. Kuongezea masababio ya ukosefu wa adili na yenye kuendekeza, hivi hutia ndani kuwasiliana na roho na ile nadharia ya mageuzi. Muumba mwenye hekima yote anaonaje hivi “vitu vyenye kina kirefu”? Mtume Paulo anamnakili kuwa akisema: “Mimi nitaharibu hekima ya wenye hekima.” Tofauti na hayo, “vitu vyenye kina kirefu vya Mungu” ni sahili, ni vyenye kueleweka, na vyenye kuchangamsha moyo. Wakristo wenye hekima huepuka “vitu vyenye kina kirefu” vya ulimwengu wa Shetani wenye kutatanisha. Kumbuka, “ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hubaki milele.”—1 Wakorintho 1:19, Kingdom Interlinear; 2:10; 1 Yohana 2:17, NW.
18. Ni baraka gani ambazo Yesu aliwaahidi Wakristo wapakwa-mafuta wanaobaki kuwa waaminifu kuteremka mpaka mwisho, na ni pendeleo gani ambalo hawa wafufuliwa watakuwa nalo kwenye Har–Magedoni?
18 Kwa Wakristo hao katika Thiatira, sasa Yesu anasema maneno yenye kuchangamsha moyo. Hayo yanawatia moyo pia Wakristo wapakwa-mafuta leo: “Na yeye ambaye hushinda na kushika matendo yangu kuteremka mpaka mwisho mimi nitampa mamlaka juu ya mataifa, na yeye atachunga watu kwa ufito wa chuma hivi kwamba watavunjwa vipande vipande kama vyombo vya udongo wa mfinyanzi, sawasawa na ambavyo mimi nimepokea kutoka kwa Baba yangu.” (Ufunuo 2:26, 27, NW) Ni pendeleo zuri ajabu kweli kweli. Mamlaka hii ambayo washindi wapakwa-mafuta wanapokea kwenye ufufuo wao ni ushiriki pamoja na Yesu katika kupunga “ufito wa chuma” wa uharibifu dhidi ya mataifa yenye kuasi kwenye Har–Magedoni. Zikifanikiwa zaidi sana, zile nguvu-moto za nyukilia za mataifa zitalialia kama fataki zilizolowa maji wakati Kristo atavunja vipande vipande adui zake kama vile angefanyia vyombo vya udongo wa mfinyanzi.—Zaburi 2:8, 9; Ufunuo 16:14, 16; 19:11-13, 15.
19. (a) Ni nani aliye “ile nyota ya asubuhi,” naye atapewaje kwa wale ambao hushinda? (b) Ni kitia-moyo gani unachotolewa ule umati mkubwa?
19 Yesu anaongeza hivi: “Na mimi nitampa ile nyota ya asubuhi.” (Ufunuo 2:28, NW) Yesu mwenyewe anaeleza baadaye hiyo “nyota” ni nini, akisema: “Mimi ndiye ule mzizi na mzao wa Daudi, na ile nyota nyangavu ya asubuhi.” (Ufunuo 22:16, NW) Ndiyo, Yesu ndiye anayetimiza ule unabii ambao Yehova alilazimisha utoke katika midomo isiyo na nia ya Balaamu: “Nyota itatokea katika Yakobo; na fimbo ya enzi itainuka katika Israeli.” (Hesabu 24:17) Yesu atawapaje “nyota ya asubuhi” wale ambao hushinda? Kwa wazi, ni kwa kujipa mwenyewe kwao, kwa kuwachukua ndani ya uhusiano ulio wa karibu zaidi sana, ulio wa usiri zaidi sana naye. (Yohana 14:2, 3) Hakika ni kichocheo chenye nguvu nyingi cha kuvumilia! Vilevile, ni jambo lenye kuchochea kwa ule umati mkubwa kujua kwamba “ile nyota nyangavu ya asubuhi” karibuni itatumia mamlaka yayo ya Ufalme ili kurudisha Paradiso hapa duniani!
Dumisha Ukamilifu
20. Ni matukio gani katika Jumuiya ya Wakristo yanayotukumbusha baadhi ya udhaifu katika kundi la Thiatira?
20 Ujumbe huu lazima uwe ulitia moyo sana Wakristo katika Thiatira. Ebu wazia—yule Mwana wa Mungu aliyetukuzwa katika mbingu alikuwa amesema ana kwa ana kwa Wakristo katika Thiatira juu ya baadhi ya matatizo yao! Hakika, angalau baadhi yao katika kundi lile waliitikia uchungaji kama huo wa upendo. Ujumbe huu ulio mrefu kupita zote za jumbe saba unatusaidia pia kulitambua kundi la kweli la Kikristo leo. Katika 1918 wakati Yesu alipokuja hekaluni kuhukumu, yaliyo mengi zaidi ya matengenezo yaliyodai kuwa ya Kikristo yalikuwa yamechafuliwa na ibada ya sanamu na ukosefu wa adili kiroho. (Yakobo 4:4) Baadhi yayo yaliweka msingi wa itikadi zao juu ya mafundisho ya wanawake wenye akili ngumu wa karne ya 19, kama vile Ellen White wa Waadventisti wa Siku ya Sabato na Mary Baker Eddy wa Wanasayansi wa Kikristo, na hivi majuzi zaidi wanawake wamekuwa wakihubiri kutoka mimbara. (Tofautisha 1 Timotheo 2:11, 12.) Miongoni mwa namna tofautitofauti za Ukatoliki, mara nyingi, Maria ndiye wa mbele kuheshimiwa kuliko Mungu na Kristo. Yesu hakumheshimu hivyo. (Yohana 2:4; 19:26) Je! matengenezo yanayoruhusu uvutano wa kike usio halali kama huo yangeweza kweli kukubaliwa kuwa ya Kikristo?
21. Kuna masomo gani kwa watu mmoja mmoja katika ujumbe wa Yesu aliopelekea Thiatira?
21 Wakristo mmoja mmoja, wawe wale wa jamii ya Yohana au wa kondoo wengine, watafanya vema kufikiria ujumbe huo. (Yohana 10:16) Huenda wengine wakaliona kuwa jambo lenye kushawishi kufuata mwendo rahisi, kama walivyofanya wale wanafunzi wa Yezebeli wa Thiatira. Pia kuna kishawishi cha kuacha msimamo unaofaa. Leo, kunakuwa na lazima ya kukabili masuala kama vile kula vitu vilivyofanyizwa kwa damu au kukubali kutiwa damu mishipani. Huenda wengine wakahisi kwamba bidii katika utumishi wa shambani au kutoa hotuba kunawapa haki ya kutokuwa waangalifu sana katika maeneo mengine, kama vile kutazama sinema na kanda za vidio zenye kuonyesha jeuri na ukosefu wa adili, au kujifurahisha mno kileo. Onyo la Yesu kwa Wakristo katika Thiatira linatuambia sisi ni lazima tusifanye mambo kama hayo yasiyofaa. Yehova anatutaka sisi tuwe safi, wenye nafsi kamili, si waliogawanyika, kama walivyokuwa Wakristo wengi katika Thiatira.
22. Yesu anakaziaje umaana wa kuwa na sikio lenye kusikia?
22 Kwa kumalizia, Yesu anatangaza hivi: “Acheni yeye ambaye ana sikio asikie ambacho roho husema kwa makundi.” (Ufunuo 2:29, NW) Kwa mara ya nne, Yesu anarudia hapa kibwagizo hiki chenye kuamsha, nacho kitamalizia jumbe zote tatu ambazo zingali zinakuja. Je! wewe una sikio lenye kuitikia? Basi endelea kusikiliza kwa makini kadiri Mungu, kwa roho yake aendeleavyo kuandaa shauri kupitia mfereji wake.
[Maelezo ya Chini]
a Ona, mathalani, ile makala “Wanawake Wakristo Waaminifu Ni Waabudu wa Mungu Wenye Thamani” katika Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 2003.
[Picha katika ukurasa wa 51]
Leo, sehemu iliyo kubwa zaidi ya kazi ya kutoa ushuhuda inatimizwa na akina dada waaminifu wanapounga mkono mamlaka ya kitheokrasi kwa kutumia kiasi