Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • gm sura 12 kur. 162-174
  • Chanzo cha Hali ya Juu Zaidi cha Hekima

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Chanzo cha Hali ya Juu Zaidi cha Hekima
  • Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Semi za Hekima
  • Kanuni za Hekima
  • Maneno Yenye Faida
  • Ndoa na Adili
  • Kanuni Zinazofanya Kazi Kweli Kweli
  • Neno la Mungu Ni Ukweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Je! Ndoa Yako Yaweza Kufanikiwa?
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
  • Jinsi ya Kufanikisha Ndoa
    Amkeni!—2011
  • Biblia Inavyoweza Kusaidia Ndoa Yako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?
gm sura 12 kur. 162-174

Sura 12

Chanzo cha Hali ya Juu Zaidi cha Hekima

“Ee BWANA [Yehova, NW], jinsi yalivyo mengi matendo yako! Kwa hekima umevifanya vyote pia. Dunia imejaa mali zako.” (Zaburi 104:24) Ndiyo, kuanzia fahari nyingi ya ulimwengu mzima wote ulio mkubwa mpaka uzuri mwororo wa ua, uumbaji washuhudia hekima isiyo na kifani ya Muumba wao. Teknolojia ya karne ya 20 si kitu ikilinganishwa na kazi za Mungu. Ikiwa Biblia ni Neno la Mungu, tungetazamia pia itoe uthibitisho wa hekima inayopita uwezo wa kibinadamu. Je! inafanya hivyo?

1. (Tia ndani utangulizi.) (a) Twaona wapi uthibitisho wa hekima ya Mungu isiyo na kifani? (b) Biblia yatoa shauri gani kuhusu hekima?

BIBLIA hukazia umaana wa hekima. Yasema: “Hekima ndicho kitu cha kwanza. Jipatie hekima; na pamoja na yote unayojipatia, jipatie uelewevu.” (Mithali 4:7, NW) Pia hukiri kwamba mara nyingi sisi wanadamu twakosa hekima, nayo hututia moyo: “Mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote kwa ukarimu.”—Yakobo 1:5.

2. Mtu aweza kuongezaje hekima yake?

2 Mungu ‘hupaje hekima kwa ukarimu’? Njia moja ni kwa kututia moyo tusome Biblia na kujifunza kutokana nayo. Kitabu cha Biblia cha Mithali chasihi: “Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; hata ukatega sikio lako kusikia hekima . . . ndipo utakapofahamu kumcha BWANA [hofu ya Yehova, NW], na kupata kumjua Mungu. Kwa kuwa BWANA [Yehova, NW] huwapa watu hekima.” (Mithali 2:1, 2, 5, 6) Tunapotumia shauri katika Biblia na kuona jinsi lilivyo na mafanikio, twatambua kwamba kweli kweli yawakilisha hekima ya kimungu.

Semi za Hekima

3, 4. (a) Biblia yasema nini juu ya ubatili wa kupenda fedha? (b) Biblia yaonyesha usawaziko gani mzuri katika kutushauri juu ya thamani ya fedha?

3 Ili kuthamini hilo vizuri zaidi, acheni tuangalie mistari michache ya Biblia. Fikiria usemi huu wa hekima: “Hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru . . . Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha.” (1 Timotheo 6:9, 10) Linganisha hilo na maoni ya ki-siku-hizi—angalau katika jamii ya watu wa nchi za Magharibi—inayotia moyo watu wafuatie fedha kuwa mradi wao wa kwanza. Kwa kusikitisha, wengi hupata utajiri wanaotafuta na bado huwa na hisia ya utupu na kutoridhika. Msaikolojia mmoja mwenye kuangalia mambo kihalisi alisema: “Kuwa namba 1 na tajiri hakukufanyi uhisi umetosheka, umeridhika, umeheshimiwa au kupendwa kikweli.”1

4 Si kwamba mtu anayefanya mambo ifaavyo aweza kuzipa fedha kisogo kabisa. Biblia yaonyesha hekima iliyosawazika vizuri inaposema: “Kwa maana hekima ni ulinzi, kama vile fedha ilivyo ulinzi; na ubora wa maarifa ni ya kwamba hekima humhifadhi yeye aliye nayo.” (Mhubiri 7:12) Hivyo, Biblia hutusaidia kuona kwamba fedha, zijapokuwa za maana, si za maana katika kila jambo. Ni za kutimiza lengo fulani tu, na zina thamani ndogo tusipokuwa na hekima ya kuzitumia inavyofaa.

5, 6. (a) Kwa nini shauri la Biblia la kuepuka mashirika mabaya ni lenye hekima? (b) Twafaidikaje na ‘kuenenda na wenye hekima’?

5 Taarifa hii ya Biblia ni ya kweli pia: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.” (Mithali 13:20) Je! umepata kuona jinsi washiriki wetu wanavyotuathiri sana? Mkazo wa marika umeingiza vijana katika ulevi, matumizi mabaya ya madawa ya kulevya, na mwenendo usio wa adili. Tukichangamana na wale wanaotumia lugha chafu, hatimaye twajikuta wenyewe tukitumia lugha chafu. Kuandamana na watu wasiofuatia haki huelekea kutufanya tuwe wasiofuatia haki. Ni kweli, kama isemavyo Biblia pia, “Mashirika mabaya yanaharibu mazoea yenye mafaa.”—1 Wakorintho 15:33, NW.

6 Kwa upande mwingine, mashirika mazuri yaweza kutufanya tuwe na maendeleo. Kwa ‘kuenenda pamoja na wenye hekima,’ sisi wenyewe tutakuwa wenye hekima zaidi. Tabia nzuri huambukia wengine, kama vile mbaya. Kwa mara nyingine, Biblia yaonyesha hekima katika kututia moyo tuchague washiriki wetu kwa uangalifu.

7. Ni nini kinachoifanya Biblia kuwa chanzo pekee sana cha ushauri?

7 Biblia ina maagizo mengi kama hayo ya kutusaidia tuongoze maisha zetu. Ikiwa chanzo cha ushauri, ni ya pekee sana. Sikuzote shauri layo ni lenye manufaa. Hiyo kamwe si ya kinadharia tu, nayo haitokezi madhara kwetu. Shauri la Biblia lenye kutia ndani mambo mengi halina kifani. Wale wanaoitumia maishani mwao, na kuona jinsi sikuzote inavyowafaidi, huja kuthamini Biblia kuwa chanzo cha pekee sana cha hekima.

Kanuni za Hekima

8. Biblia yaweza kutusaidiaje hata tunapokabili hali isiyotajwa waziwazi humo?

8 Lakini, vipi tukikabili hali ambayo haitajwi waziwazi katika Biblia? Mara nyingi, twakuta kanuni za kutuongoza zenye kutumika katika mambo mengi. Kwa kielelezo, wengi katika wakati fulani maishani mwao hukabili uamuzi unaohusu zoea la kuvuta tumbaku. Kwa kuwa tumbaku haikujulikana katika Mashariki ya Kati katika siku za Yesu, Biblia haiitaji. Hata hivyo, kuna kanuni za Biblia zinazofaa za kutusaidia tufanye uamuzi wa hekima katika jambo hili.

9-11. Kanuni za Biblia hutusaidia kwa njia gani tufikie uamuzi wenye hekima kuhusu kutumia tumbako, nasi twafaidikaje kwa kufuata kanuni hizo?

9 Ingawa yasemekana kuwa kuvuta tumbaku huleta raha, kwa halisi kwahusisha kuingiza ndani ya mapafu vichafuzi vikali sana. Mvutaji sigareti huchafua mwili wake, na pia mavazi yake na hewa inayomzunguka. Kuongezea hayo, kuvuta sigareti ni zoea lenye kutumikisha. Mara nyingi watu wanaotaka kuacha huona jambo hilo likiwa gumu sana. Tunapofikiria hilo, twaweza kuangalia Biblia itusaidie kufikia mkataa wa hekima juu ya kuvuta tumbaku.

10 Kwanza, fikiria tatizo la zoea lenye kutumikisha. Paulo, alipokuwa akinena juu ya vyakula, alisema: “Mimi sitajiruhusu niletwe na chochote chini ya mamlaka.” (1 Wakorintho 6:12, NW) Paulo alikuwa huru kula chakula cha aina yoyote, lakini alijua kwamba watu fulani nyuma huko walikuwa na dhamiri zenye kuchomwa rahisi. Kwa hiyo alisema hakuwa “mzoevu mwenye kutumikishwa” na vyakula fulani kwamba asiweze kuviacha ikiwa lazima kusudi asikwaze wengine. Ikiwa mtu hawezi kuacha kuvuta—au kutafuna—tumbaku, hakika yeye yuko ‘chini ya mamlaka yayo.’ Kwa hiyo taarifa ya Paulo juu ya habari ya chakula ni mwongozo mzuri kwa matumizi ya tumbaku. Hatupaswi kujiruhusu tuwe watumwa wa tabia fulani.

11 Pili, fikiria habari ya uchafuzi. Biblia yasema: “Tujitakase nafsi zetu na uchafu wote wa mwili na roho.” (2 Wakorintho 7:1) Bila shaka kuvuta sigareti ni uchafu, au uchafuzi, wa mwili. Uzito wa uchafuzi huo waonyeshwa na uhakika wa kwamba, kulingana na Shirika la Afya Ulimwenguni, hiyo husababisha watu zaidi ya milioni moja kufa mapema kila mwaka. Tukifuata kanuni ya Biblia juu ya kuendelea kujiweka safi na uchafu wa mwili, tutalindwa na hatari mbaya sana za kiafya za kuvuta sigareti, na pia madawa ya kulevya na uchafu mwingine mwingi.

Maneno Yenye Faida

12. Ni kwa nini sikuzote shauri la Biblia lakamatana na hali njema yetu ya kimwili na ya kihisia-moyo?

12 Hatupaswi kushangaa kwamba kufuata shauri la Biblia hutufaidi kimwili. Biblia imetoka kwa Mungu. Akiwa Muumba wetu, yeye ana maarifa ya kindani juu ya jinsi tulivyofanyizwa na tunachohitaji. (Zaburi 139:14-16) Sikuzote shauri lake lakamatana na hali njema yetu ya kimwili na kihisia-moyo.

13, 14. Kwa nini ni mwendo wa hekima kufuata shauri la Biblia juu ya kutosema uwongo?

13 Hilo laonyeshwa katika lile shauri la kutosema uwongo. Uwongo umewekwa miongoni mwa mambo saba anayochukia Yehova, na kitabu cha Ufunuo chatia wasemao uwongo miongoni mwa wale ambao hawatakuwa na mahali katika ulimwengu mpya wa Mungu. (Mithali 6:19; Ufunuo 21:8) Ingawa hivyo, kusema uwongo kumeenea sana. Gazeti moja la biashara lilisema: “U.S. inapatwa na pigo lililo baya zaidi la udanganyifu, ulaghai na mabaya yanayohusiana na hayo katika historia yayo.”2

14 Ingawa ni kwa kawaida sana, kusema uwongo ni kubaya kwa jamii na mtu mwenyewe. Clifford Longley anayechangia habari safu ya gazeti moja asema: “Uwongo huumiza mwenye kusema uwongo na anayeambiwa uwongo, katika kina cha ndani zaidi cha nafsi yao, kwa kukata ule uhusiano wa lazima kati ya akili na uhalisi.”3 The American Journal of Psychiatry lasema: “Umizo la akili kwa watu wanaoambiwa uwongo laweza kuwa haribifu sana. Maamuzi makubwa ya maisha yaweza kutegemezwa juu ya habari bandia iliyoaminiwa kuwa ni sahihi. Huenda pia uwongo ukawa na matokeo mabaya sana kwa wasemaji uwongo wenyewe.”4 Ni afadhali zaidi kama nini kusema kweli, kama ambavyo Biblia yashauri kwa hekima!

15, 16. Ni katika njia zipi inakuwa kwa faida yetu kufuata shauri la Biblia la kuonyesha wengine upendo?

15 Kwa kututia moyo, Biblia yatuambia kwamba twapaswa kuhangaikia wengine, kuwaonyesha upendo, na kuwasaidia. Maneno ya Yesu yajulikana sana: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.”—Mathayo 7:12.

16 Ulimwengu ungekuwa afadhali zaidi kama nini kama kila mtu angefuata kanuni hiyo! Na zaidi, kulingana na uchunguzi wa kisaikolojia uliofanywa katika United States, watu mmoja mmoja wangehisi vizuri zaidi. Wale watu 1,700 waliochunguzwa waliripoti kwamba kusaidia wengine kuliwapa hisi ya utulivu na faraja kutokana na kasoro zinazoletwa na wasiwasi kama vile kuumwa na kichwa na kupoteza sauti. Ripoti hiyo yafikia mkataa huu: “Basi, yaonekana kwamba kujali juu ya wengine ni sehemu ya asili ya mwanadamu kama vile kujijali wenyewe.”5 Hilo latukumbusha amri hii ya Biblia: “Mpende jirani yako kama nafsi yako.” (Mathayo 22:39; linganisha Yohana 13:34, 35.) Ni jambo la asili kujipenda wenyewe. Lakini ili kihisia-moyo tuwe na afya, Biblia yasema lazima tusawazishe upendo huo wa binafsi na upendo kwa wengine.

Ndoa na Adili

17. Kwa nini wakati mwingine shauri la Biblia huonekana kuwa la kikale?

17 Ingawa shauri la Biblia latoa uthibitisho wa hekima ya kina kirefu, sikuzote haisemi mambo ambayo watu wanataka kusikia. Mara nyingi, hushtakiwa kuwa ya kikale. Kwa nini? Kwa sababu ingawa shauri la Biblia ni la faida yetu ya muda mrefu, mara nyingi kulitumia hutaka nidhamu na kujinyima; na sifa hizi hazipendwi na wengi leo.

18, 19. Ni vipi vilivyo viwango vya Biblia juu ya ndoa na adili?

18 Chukua habari ya ndoa na adili. Viwango vya Biblia kuhusu mambo hayo ni imara kabisa. Hiyo hutaja waziwazi ndoa ya mke mmoja, mume mmoja kwa mke mmoja. Na ijapotaja visa vya kupita kiasi ambapo yawezekana kuwe talaka au kutengana, kwa ujumla yasema kwamba kifungo cha ndoa ni cha maisha. “Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke, akasema, Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja? Hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe.”—Mathayo 19:4-6; 1 Wakorintho 7:12-15.

19 Na zaidi, Biblia yasema kwamba mahali pekee pa ukaribiano wa kingono ni ndani ya kifungo cha ndoa. Yakataza ukaribiano huo nje ya ndoa. Twasoma: “Waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti.”—1 Wakorintho 6:9, 10.

20. Viwango vya Biblia juu ya adili vinapuuzwa kila mahali katika njia zipi?

20 Leo, viwango hivi vinapuuzwa kila mahali. Profesa wa sosholojia David Mace aandika: “Wakati wa karne hii utamaduni wetu umepatwa na mabadiliko makubwa, na mila na desturi nyingi za kale zimetikiswa. Ndoa haikuponyoka.”6 Mazoea yasiyofuata adili ni ya kawaida. Mahusiano ya ngono kati ya matineja wawili wenye kutafuta mapenzi mara nyingi huonwa kuwa kawaida. Kuishi pamoja kabla ya ndoa—‘ili kuhakikisha tu’—ni kawaida. Na watu wawili wakiisha kufunga ndoa, ngono haramu ni za kawaida.

21. Ni nini kimetokana na upuuzaji ulioenea sana wa viwango vya Biblia vya ndoa na adili?

21 Je! mazingira hayo yasiyofuatilia adili yameleta furaha? La, yameleta tu msukosuko—msukosuko wenye gharama—unaotokeza ukosefu wa furaha na nyumba zilizovunjika. Pia kuna tauni ya maradhi yanayoambukiwa kingono. Mweneo wa kisonono, kaswende, na maradhi ya macho (chlamydia), machache kati yayo, hauzuiliki. Katika miaka ya juzijuzi, mazoea ya umalaya na ngono za jinsia moja yameharakisha mweneo wa UKIMWI. Kuna mweneo wa wasichana wachanga waseja kupata watoto wakiwa wao wenyewe bado ni watoto. Ladies’ Home Journal kiliandika: “Mkazo juu ya ngono uliokuwa kawaida ya [miaka ya] sitini na sabini umeleta si furaha tele ya kibinadamu bali huzuni kubwa ya kibinadamu.”7

22. Kwa habari ya adili, ni nini huleta furaha iliyo kubwa zaidi?

22 Kwa hiyo, sasa twasikia maelezo kama yafuatayo yaliyotolewa na profesa wa sosholojia Carlfred B. Broderick: “Labda tumekua vya kutosha kufikiria kama isingetufaidi zaidi kuhimiza kuepuka ngono ya kabla ya ndoa kuwe sera inayofaa zaidi mahitaji ya raia zetu na haki yao ya uhuru: uhuru wa kutokuwa na maradhi, uhuru wa kutokuwa na mimba zisizotakwa.”8 Kwa kweli, kiwango cha Biblia cha adili kimethibitisha, baada ya muda, kuwa chenye kuleta furaha kubwa zaidi.

Kanuni Zinazofanya Kazi Kweli Kweli

23. (a) Ikiwa ndoa ni isiyo na furaha, je! talaka ndio utatuzi pekee uwezekanao? (b) Mbili kati ya funguo za ndoa imara ni zipi?

23 Kwa kuwa ndoa imekusudiwa idumu maisha, twahitaji kujua jinsi ya kuifanikisha. Wengine wamebisha kwamba ni afadhali kujiondoa katika ndoa isiyo na furaha kuliko kukaa nayo na kuhuzunika. Lakini kuna jambo jingine la kufanya: kujitahidi kutatua matatizo yanayosababisha ukosefu huo wa furaha. Hii ni sehemu nyingine ambayo Biblia husaidia. Tumekwisha kuona jinsi inavyotushauri tuwe waaminifu kwa mwenzi wetu wa ndoa, na huo ni ufunguo mmoja wa furaha, ndoa imara. Mwingine ni kutambua kwamba kwaweza tu kuwa kichwa kimoja katika ndoa, na Biblia yasema lazima iwe ni mume. Mke ashauriwa kuunga mkono mume wake na si kukaidi cheo chake. Kwa upande mwingine, mume, aambiwa atumie cheo chake kwa faida ya mke wake na asiwe na ubinafsi.—1 Wakorintho 11:3; 1 Timotheo 2:11-14.

24, 25. Biblia yatiaje moyo waume na wake watimize sehemu zao zifaazo katika ndoa?

24 Kwa mume, Biblia husema: “Vivyo hivyo imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote.” (Waefeso 5:28, 29) Mume anayependa hutumia mamlaka yake katika njia ya ufikirio. Yeye hukumbuka kwamba ingawa yeye ndiye kichwa, mke wake apaswa kufikiriwa na kuombwa maoni. Ndoa yamaanisha kushirikiana, si kutawala kwa mabavu.

25 Shauri la Biblia kwa wake latia ndani maneno haya: “Mke asikose kumstahi mumewe.” (Waefeso 5:33) Yeye hustahi mume wake kwa sababu ya cheo chake, na staha yake itaonyeshwa kwa yeye kumwunga mume mkono kama vile upendo wa mume wake utakavyothibitishwa kwa mume kumhangaikia mke. Kwa watu wengi mmoja mmoja wenye kufikiri ki-siku-hizi, ushauri kama huo haukubaliki. Lakini wenzi wanaotegemeza mahusiano yao juu ya upendo na staha—kama inavyoshauri Biblia—sikuzote wana furaha.

26. Je! viwango vya Kimaandiko vya ndoa vinafanya kazi kweli kweli? Toa kielezi.

26 Uhakika wa kwamba shauri la Biblia katika eneo hili lafanya kazi kweli kweli yaonyeshwa na jambo lililoonwa kutoka Bahari za Kusini. Watu wawili huko, baada ya miaka kumi wakiwa pamoja, walikuwa wamesadikishwa kwamba ndoa yao imeshindwa. Kwa hiyo wakaanza kupanga kutengana. Kisha mke akasema na mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Wakiwa pamoja, yeye na Shahidi huyo walijifunza ushauri wa Biblia kwa watu wawili waliooana. Mume aripoti hivi: “Mke wangu alipokuwa akijifunza kanuni za Biblia, alifanya jitihada za kuzitumia maishani mwake. Baada ya majuma machache, nilianza kuona mabadiliko fulani.” Akiwa amevutiwa na hali hiyo, mume huyo alikubali kujiunga katika funzo la Biblia la mke wake naye akajifunza shauri la Biblia kwa waume waliooa. Tokeo likawa nini? Mume asema: “Sasa tumepata msingi wa maisha ya familia yenye furaha kweli kweli.”

27. Ni utumizi wa kanuni zipi za Biblia unaoweza kusaidia Wakristo wavumilie umaskini wa kiuchumi?

27 Bado kukabiliana na umaskini ni eneo jingine ambalo shauri la Biblia limethibitika kuwa lenye kusaidia. Kwa kielelezo, kuvuta sigareti na ulevi, mambo mawili hayo yakiwa ni kinyume cha kanuni za Biblia, hufuja mali chache. (Mithali 23:19-21) Kuongezea hayo, Biblia hupendekeza bidii ya kazi, kwani mtu mwenye kufanya kazi kwa bidii mara nyingi aweza kupata njia ya kulisha familia yake kushinda mtu mvivu au mmoja anayepoteza tumaini. (Mithali 6:6-11; 10:26) Zaidi ya hayo, kufuata ushauri wa ‘kutohusudu wafanyao ubatili’ humzuia mtu asijiingize katika mambo kama vile uhalifu au kucheza kamari kuwa njia za kuepuka umaskini. (Zaburi 37:1) Mazoea kama hayo huenda yakaonekana yanatoa utatuzi wa upesi wa magumu ya kifedha, lakini mazao yayo ya muda mrefu ni machungu sana.

28-30. (a) Kutumia kanuni za Biblia kulisaidiaje mwanamke mmoja Mkristo akabiliane na umaskini wake? (b) Mambo yaliyoonwa ya maelfu ya Wakristo katika hali maskini za kiuchumi yashuhudia nini?

28 Je! shauri hilo linasaidia kikweli wale walio maskini sana, au je! ni nadharia ya kuwazia tu? Jibu ni, Ushauri huo hufanya kazi, kama inavyoonyeshwa na mambo mengi yaliyoonwa kuuzunguka ulimwengu. Katika kuchukua kielelezo kimoja tu, mwanamke mmoja Mkristo katika Asia alijikuta amekuwa mjane, bila ya pato lolote, na akiwa na mwana mmoja mchanga wa kutunza. Biblia ilimsaidiaje yeye na mwana wake?

29 Yeye alikuwa mwenye bidii ya kazi, kama inavyoshauri Biblia, akaanza kushona nguo na kuziuza. Kwa sababu alikuwa mfuatia haki na mwenye kutegemeka, sawa na ambavyo Biblia inashauri pia, baada ya muda mfupi akawa na wateja (wanunuzi) wa kawaida. (Wakolosai 3:23) Kisha, akageuza chumba kimoja kidogo katika nyumba yake kuwa mahali pa kulia akiwa anaamka karibu saa kumi kila asubuhi ili kutayarisha chakula cha kuuza, na hilo likaongezea pato lake. “Hata hivyo,” yeye asema, “twalazimika kuishi kisahili.” Lakini yeye akumbuka ushauri huu wa Biblia: “Tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo.”—1 Timotheo 6:8.

30 Yeye aongeza: “Ingawa naishi karibu na kiwango cha umaskini, mimi sioni chuki au uchungu. Kweli ya Biblia hunijaza mtazamo unaofaa.” Kuongezea, ameona kwamba ahadi inayostahili kuangaliwa aliyotoa Yesu imefanya kazi kweli kweli katika kisa chake. Yeye alisema: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na mambo yote hayo mengine [vitu vya lazima] mtaongezewa.” (Mathayo 6:33, NW) Ameona kwamba kwa kuweka utumishi wake kwa Mungu kwanza maishani mwake, sikuzote anapokea vitu vya lazima, kwa njia hii au hii. Aliyojionea mwanamke huyu Mkristo, pamoja na yale waliyojionea Wakristo wengi wasiohesabika walio maskini kiuchumi, yashuhudia kwamba shauri la Biblia lafanya kazi kweli kweli.

31. Hutukia nini tunapofuata shauri la Biblia, na hilo lashuhudia nini?

31 Katika sura hii, tumegusia tu utajiri mwingi wa shauri na ushauri ambao Biblia inao, nasi tumeona visa vichache tu ambapo shauri hili limefanya kazi. Mambo yaliyoonwa yaliyotajwa yaweza kuzidishwa mara elfu moja. Tena na tena, watu wanapofuata Biblia, wanafaidika. Wanapoipuuza, wanaumia. Hakuna mkusanyo mwingine wowote wa shauri, wa kale au wa ki-siku-hizi, ambao daima unafaidi na kutumika kwa watu wa rangi zote kuliko wa Biblia. Shauri la hekima kama hili haliwezi tu kuwa hekima ya watu. Uhakika wa kwamba Biblia ni akiba yenye utajiri wa hekima hiyo ni uthibitisho wenye nguvu kwamba hiyo ni Neno la Mungu.

[Blabu katika ukurasa wa 168]

Moyo wa kusaidia hufaidi kila mmoja

[Picha katika ukurasa wa 163]

Kuenenda na wenye hekima hutufanya tuwe wenye hekima, lakini kushirikiana na wapumbavu kutatuathiri vibaya

[Picha katika ukurasa wa 165]

Kuvuta tumbaku kwapasa kuepukwe kwa sababu ni kinyume cha kanuni za Biblia

[Picha katika ukurasa wa 171]

Wale wanaofuata shauri la Biblia katika ndoa wana msingi imara wa furaha

[Picha katika ukurasa wa 173]

Kufuata shauri la Biblia husaidia watu wakabiliane na matatizo makubwa ya umaskini

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki