Sura 22
Kuitambua Dini ya Kweli
1. Ni nani waliokuwa wakizoea dini ya kweli katika karne ya kwanza?
HAKUWEZI kuwa na shaka juu ya wale waliokuwa wakizoea dini ya kweli katika karne ya kwanza. Walikuwa ni wafuasi wa Yesu Kristo. Hao wote walikuwa wa tengenezo lile moja tu la Kikristo. Namna gani leo? Wale wanaozoea dini ya kweli wanaweza kutambuliwaje?
2. Wale wanaozoea dini ya kweli wanaweza kutambuliwaje?
2 Akieleza namna tunavyoweza kuwatambua, Yesu alisema: “Mtawatambua kwa matunda yao. . . . Kila mti mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya. . . . Ndiposa kwa matunda yao mtawatambua.” (Mathayo 7:16-20) Ni matunda gani mazuri ambayo ungetazamia wanaoabudu Mungu kwa njia ya kweli wazae? Wamepaswa wawe wakisema nini na kutenda nini sasa?
KUTAKASA JINA LA MUNGU
3, 4. (a) Ni jambo gani lililoombwa kwanza katika Sala ya Kielelezo ya Yesu? (b) Yesu alitakasaje jina la Mungu?
3 Wanaoabudu Mungu kwa njia ya kweli wangetenda kupatana na ile Sala ya Kielelezo ambayo Yesu aliwapa wafuasi wake. Jambo la kwanza ambalo Yesu alitaja ni hili: “Baba yetu uliye katika mbingu, acha jina lako litakaswe.” (NW) Tafsiri nyingine ya Biblia inayasema maneno hayo hivi: “Jina lako na lionwe kuwa takatifu.” (Mathayo 6:9, Jerusalem Bible) Maana yake nini kutakasa au kuliona jina la Mungu kuwa takatifu? Yesu alifanyaje hivyo?
4 Yesu alionyesha alivyofanya alipomwambia hivi Baba yake katika sala: “Jina lako nimewadhihirishia watu wale ulionipa katika ulimwengu.” (Yohana 17:6) Ndiyo, Yesu alijulisha wengine jina la Mungu, yaani, Yehova. Yeye hakushindwa kutumia jina hilo. Yesu alijua kwamba lilikuwa kusudi la Baba yake jina Lake litukuzwe katika dunia yote. Hivyo aliuweka mfano wa kulitangaza jina hilo na kuliona kuwa takatifu.—Yohana 12:28; Isaya 12:4, 5.
5. (a) Kundi la Kikristo linahusianaje na jina la Mungu? (b) Ili tupate wokovu ni lazima tufanye nini?
5 Biblia inaonyesha kwamba kuwapo kwenyewe kwa kundi la Kikristo kunahusiana na jina la Mungu. Mtume Petro alieleza kwamba Mungu ‘aligeuza fikira zake kuelekea mataifa ili achukue kati yao watu kwa ajili ya jina lake.’ (Matendo 15:14, NW) Hivyo ni lazima watu wa kweli wa Mungu walione jina lake kuwa takatifu na kulijulisha katika dunia yote. Kwa kweli, kujua jina hilo ni kwa lazima ili kupata wokovu, kama Biblia inavyosema: “Kwa maana ‘kila mtu anayeita juu ya lile jina la Yehova ataokolewa.’”—Warumi 10:13, 14, NW.
6. (a) Je! makanisa kwa ujumla yanaliona jina la Mungu kuwa takatifu? (b) Je! kuna wo wote wanaolishuhudia jina la Mungu?
6 Basi, ni nani leo wanaoliona jina la Mungu kuwa takatifu na kulijulisha katika dunia yote? Makanisa kwa ujumla yanaepuka kulitumia jina hilo Yehova. Mengine hata yameliondoa katika tafsiri zao za Biblia. Lakini, kama ungezungumza na majirani wako na mara nyingi utaje Yehova, ukitumia jina lake, unadhani wangesema wewe ni wa tengenezo gani? Kuna jamii moja tu ya watu inayoufuata kweli kweli mfano wa Yesu katika jambo hilo. Kusudi lao kubwa maishani ni kumtumikia Mungu na kushuhudia jina lake, kama Yesu alivyofanya. Hivyo wamechukua jina la Kimaandiko “Mashahidi wa Yehova.”—Isaya 43:10-12.
KUTANGAZA UFALME WA MUNGU
7. Yesu alionyeshaje umaana wa ufalme wa Mungu?
7 Katika Sala ya Kielelezo ambayo Yesu alitoa, alionyesha vilevile umaana wa ufalme wa Mungu. Alifundisha watu kusali hivi: “Ufalme wako uje.” (Mathayo 6:10) Yesu aliukazia mara nyingi Ufalme huo kuwa ndiyo njia pekee ya kuondoa taabu za wanadamu. Yeye na mitume wake walifanya hivyo kwa kuwahubiri watu juu ya ufalme huo “kijiji kwa kijiji” na “nyumba kwa nyumba.” (Luka 8:1, NW; Matendo 5:42; 20:20) Ufalme wa Mungu ulikuwa ndicho kichwa cha mahubiri na mafundisho yao.
8. Yesu alionyeshaje jambo ambalo lingekuwa ndio ujumbe mkuu wa wafuasi wake wa kweli katika hizi “siku za mwisho”?
8 Namna gani siku zetu? Ni nini mafundisho yaliyo makuu ya tengenezo la Kikristo la kweli, la Mungu? Katika kutabiri juu ya hizi “siku za mwisho,” Yesu alisema: “Na habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14, NW) Basi inawapasa watu wa Mungu leo waufanye Ufalme uwe ndio ujumbe wao ulio mkuu.
9. Ni watu gani leo wanaouhubiri ujumbe wa Ufalme?
9 Jiulize hivi: Mtu akija mlangoni pako na kuzungumza juu ya ufalme wa Mungu kuwa ndilo tumaini la kweli la wanadamu, utadhani mtu huyo ni wa tengenezo gani? Je! kuna watu wa dini nyingine ambao si Mashahidi wa Yehova waliopata kuzungumza nawe juu ya ufalme wa Mungu? Wapi! Kwanza wengi sana kati yao hata hawajui ufalme wenyewe ni kitu gani! Wao hawasemi juu ya serikali ya Mungu. Hata hivyo serikali hiyo ni habari zinazoutetemesha ulimwengu. Nabii Danieli alitabiri kwamba ufalme huo ‘ungezivunja vipande vipande na kuziharibu serikali nyingine zote kisha huo pekee uitawale dunia.’—Danieli 2:44.
KUHESHIMU NENO LA MUNGU
10. Yesu aliheshimuje Neno la Mungu?
10 Njia nyingine ambavyo wale wanaozoea dini ya kweli wanaweza kutambuliwa ni kwa maoni yao kuelekea Biblia. Nyakati zote Yesu aliheshimu Neno la Mungu. Mara nyingi alilitumia liwe ndiyo mamlaka ya mwisho ya kuamulia mambo. (Mathayo 4:4, 7, 10; 19:4-6) Vilevile Yesu aliheshimu Biblia kwa kuishi kulingana na mafundisho yake. Hakuidharau kamwe Biblia. Badala yake, yeye aliwalaumu wale walioshindwa kufundisha mambo yanayopatana na Biblia na waliotaka kupunguza nguvu ya mafundisho ya Biblia kwa kutokeza mawazo yao wenyewe.—Marko 7:9-13.
11. Ni maoni gani juu ya Neno la Mungu ambayo mara nyingi makanisa yanaonyesha?
11 Makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yanafuata mfano wa Kristo katika jambo hilo? Je! yanaiheshimu sana Biblia? Makasisi wengi leo hawaamini masimulizi ya Biblia juu ya dhambi ya Adamu, gharika ya siku za Noa, juu ya Yona na yule samaki mkubwa, na masimulizi mengine. Vilevile wanasema kwamba mwanadamu alitokea hapa duniani kwa njia ya mageuzi, si kwa kuumbwa moja kwa moja na Mungu. Je! kwa njia hiyo wanatia watu moyo waheshimu Neno la Mungu? Vilevile, viongozi fulani wa makanisa wanatoa hoja ya kwamba kufanya ngono na mtu asiye mwenzi wako wa ndoa si vibaya, au kwamba matendo ya kulalana wanaume kwa wanaume na wanawake kwa wanawake au kuoa wanawake wengi yanaweza kufaa. Je! ungesema kwamba wanatia watu moyo waitumie Biblia iwe uongozi wao? Bila shaka hawaufuati mfano wa Mwana wa Mungu na mitume wake.—Mathayo 15:18, 19; Warumi 1:24-27.
12. (a) Ni kwa sababu gani ibada ya wengi ambao hata wanayo Biblia haimpendezi Mungu? (b) Iwapo watu wanaotenda mabaya kwa makusudi wanaruhusiwa waendelee kuwa kanisani, lazima tukate shauri gani?
12 Kuna washiriki wa kanisa walio na Biblia na hata wanaoisoma, lakini mwenendo wa maisha yao unaonyesha kwamba hawaifuati. Juu ya watu kama hao, Biblia inasema: “Wanakiri ya kwamba wanamjua Mungu, bali kwa matendo yao wanamkana.” (Tito 1:16; 2 Timotheo 3:5) Ikiwa washiriki wa kanisa wanaocheza kamari, wanaolewa au wanaofanya makosa mengine wanaruhusiwa waendelee kuwa katika kanisa lao, hiyo inaonyesha nini? Ni ushuhuda wa kwamba tengenezo lao la kidini halikubaliwi na Mungu.—1 Wakorintho 5:11-13.
13. Ni uamuzi gani mzito ambao lazima mtu afanye ikiwa ameona kwamba mafundisho ya kanisa lake hayapatani na Biblia?
13 Ikiwa umefikiria zile kurasa zilizotangulia za kitabu hiki, ukiyasoma Maandiko yaliyomo, umepata kujua mafundisho ya msingi ya Neno la Mungu. Lakini namna gani iwapo mafundisho ya tengenezo la kidini unaloshirikiana nalo hayapatani na yale ya Neno la Mungu? Hapo una tatizo kubwa. Ni tatizo la kuamua kama utakubali ukweli wa Biblia ama utaukataa kwa kupende-lea mafundisho ambayo Biblia haiyaungi mkono. Bila shaka, ni juu yako kuamua. Walakini, inakupasa uamue kwa uangalifu. Hiyo ni kwa sababu uamuzi unaofanya utahusu msimamo wako pamoja na Mungu na mataraja (matumaini) yako ya kuishi milele katika paradiso duniani.
KUJITENGA NA ULIMWENGU
14. (a) Ni alama gani nyingine ya kutambulisha dini ya kweli? (b) Ni kwa sababu gani ni jambo la maana sana waabudu wa kweli watimize takwa hilo?
14 Hata hivyo alama nyingine inayotambulisha wale wanaozoea kufuata dini ya kweli ni ya kwamba “wao si sehemu ya ulimwengu,” kama Yesu alivyosema. (Yohana 17:14, NW) Maana yake ni kwamba waabudu wa kweli wanaendelea kujitenga na ulimwengu mchafu na mambo yake. Yesu Kristo alikataa kuwa mtawala wa ulimwengu. (Yohana 6:15) Unaweza kufahamu ni kwa sababu gani kuendelea kujitenga na ulimwengu ni kwa maana sana unapokumbuka kwamba Biblia inasema Shetani Ibilisi ndiye mtawala wa ulimwengu. (Yohana 12:31; 2 Wakorintho 4:4) Uzito wa jambo hilo unaonwa zaidi kutokana na maneno haya ya Biblia: “Kwa hiyo, ye yote anayetaka kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya mwenyewe kuwa adui ya Mungu.”—Yakobo 4:4, NW.
15. (a) Je! kweli makanisa unayoyajua “si sehemu ya ulimwengu”? (b) Je! unajua dini yo yote inayotimiza takwa hilo?
15 Je! mambo ya hakika yanaonyesha kwamba makanisa yaliyo katika mtaa wako yanazingatia shauri hilo? Je! kweli makasisi na vilevile washiriki wa makanisa “si sehemu ya ulimwengu”? Au wanajiingiza sana katika utukuzo wa taifa, siasa na mapambano ya kitabaka (ya watu wa vyeo mbalimbali) ya ulimwengu? Maulizo hayo si magumu kujibiwa, kwa kuwa shughuli za makanisa hayo zinajulikana mahali pote. Kwa upande mwingine, ni rahisi vilevile kuzichunguza shughuli za Mashahidi wa Yehova. Kwa kufanya hivyo, utaona kwamba wao kweli wanaufuata mfano wa Kristo na wafuasi wake wa kwanza kwa kuendelea kujitenga na ulimwengu, mambo yake ya kisiasa na njia zake za kichoyo, za uchafu wa kukosa adili na zenye jeuri.—1 Yohana 2:15-17.
UPENDO KATI YAO WENYEWE
16. Ni njia gani ya maana ambayo kwa hiyo wanafunzi wa kweli wa Kristo wanaweza kutambuliwa?
16 Njia ya maana zaidi ambayo katika hiyo wanafunzi wa kweli wa Kristo wanaweza kutambuliwa ni kwa kupendana wao kwa wao. Yesu alisema: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:35) Je! matengenezo ya kidini unayoyajua sana yana upendo huo? Kwa mfano, yanafanya nini wakati zile nchi wanamoishi zinapopigana?
17. Matengenezo ya kidini pamoja na wanaoshirikiana nayo yako namna gani katika kutimiza takwa hilo la kuonyesha upendo kati yao wenyewe?
17 Unajua inavyokuwa. Kwa kufuata amri ya watu wa ulimwengu, washiriki wa matengenezo mbalimbali ya kidini wanaenda kwenye uwanja wa vita na kuwachinja waamini wenzao wa nchi nyingine. Hivyo Mkatoliki anaua Mkatoliki mwenzake, Mprotestanti anaua Mprotestanti mwenzake na Mwislamu anaua Mwislamu mwenzake. Je! unadhani mwendo huo unapatana na Neno la Mungu na kwa kweli unaonyesha ile roho ya Mungu?—1 Yohana 3:10-12.
18. Mashahidi wa Yehova wako namna gani katika shauri hilo la kuonyeshana upendo?
18 Mashahidi wa Yehova wako namna gani katika shauri hilo la Yesu la kuonyeshana upendo? Wao hawafuati mwenendo wa dini za ulimwengu. Hawawachinji waamini wenzao katika uwanja za vita. Wao wamekuwa bila hatia ya kusema uongo hivi, “Nampenda Mungu,” na huku wakichukia ndugu yao wa taifa jingine, kabila au jamii nyingine. (1 Yohana 4:20, 21) Lakini wao wanaonyesha upendo katika njia nyingine vilevile. Njia gani? Kwa namna wanavyoshughulika na majirani wao na kwa jitihada zao za upendo za kutaka kusaidia wengine wajifunze habari za Mungu.—Wagalatia 6:10.
DINI MOJA YA KWELI
19. Kwa sababu gani ni jambo la akili na la Kimaandiko vilevile kusema kwamba kuna dini moja tu ya kweli?
19 Mawazo mazuri yanaonyesha kwamba kungekuwako dini moja tu ya kweli. Hiyo inapatana na uhakika wa kwamba yule Mungu wa kweli “si Mungu wa machafuko, bali wa amani.” (1 Wakorintho 14:33) Biblia inasema kwamba hakika kuna “imani moja” tu. (Waefeso 4:5) Basi, ni nani walio kikundi cha waabudu wa kweli leo?
20. (a) Kulingana na ushuhuda huo, ni nani ambao kitabu hiki kinawaonyesha kuwa ndio waabudu wa kweli leo? (b) Je! ndivyo wewe unavyoamini? (c) Ni njia gani inayofaa ya kujuana na Mashahidi wa Yehova?
20 Tunasema wazi bila kusita kwamba ni Mashahidi wa Yehova. Ili upate kusadiki hilo tunakukaribisha ujuane nao zaidi. Njia inayofaa kufanya hivyo ni kuhudhuria mikutano yao kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Kwa kuwa Biblia inaonyesha kwamba kuzoea dini ya kweli kunaleta uradhi mkubwa sasa na kufungua njia ya kufurahia uzima katika paradiso duniani, bila shaka itakufaa ufanye uchunguzi huo. (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Tunakukaribisha kwa uchangamfu ufanye hivyo. Sababu gani usichunguze sasa hivi?
[Picha katika ukurasa wa 185]
Kama ungezungumza na mtu juu ya Yehova na ufalme wake, watu wangesema wewe ni wa dini gani?
[Picha katika ukurasa wa 186]
Je! mtu anaheshimu Neno la Mungu ikiwa anatenda tofauti nalo?
[Picha katika ukurasa wa 188, 189]
Yesu alikataa kuwa mtawala wa kisiasa
[Picha katika ukurasa wa 190]
Unakaribishwa kwa uchanga uhudhurie mikutano ya Mashahidi wa Yehova