Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • pe sura 27 kur. 225-230
  • Namna ya Kupata Msaada kwa Sala

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Namna ya Kupata Msaada kwa Sala
  • Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SALA AMBAZO MUNGU ANASIKIA
  • SALA ZA KUSAIDIA WENGINE
  • Mkaribie Mungu Katika Sala
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Zawadi ya Sala
    Biblia Inatufundisha Nini?
  • Jinsi ya Kusali na Kusikiwa na Mungu
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Mkaribie Mungu Kupitia Sala
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
Pata Habari Zaidi
Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
pe sura 27 kur. 225-230

Sura 27

Namna ya Kupata Msaada kwa Sala

1. Ni msaada gani tunaohitaji kutoka kwa Mungu, na tunaupokeaje?

ILI KUACHANA na uvutano mwovu wa ulimwengu, Wakristo hasa wanahitaji msaada unaopokewa kupitia sala. Yesu alisema: “Yule Baba mbinguni atawapa roho takatifu wale wanaomwomba.” (Luka 11:13, NW) Tunahitaji roho takatifu ya Mungu au kani yake ya utendaji, sawa na vile tunavyohitaji kujifunza Neno lake na kushirikiana na tengenezo lake. Lakini ili tupokee roho takatifu, ni lazima tusali ili tupewe hiyo.

2. (a) Sala ni nini? (b) Ni namna gani mbalimbali za sala? (c) Kwa sababu gani sala ni ya maana?

2 Sala ni usemi wenye heshima unaotolewa kwa Mungu. Inaweza kuwa kwa namna ya ombi, kama vile tunapomwomba Mungu atupatie vitu fulani. Lakini sala inaweza vilevile kuwa wonyesho wa shukrani au sifa kwa Mungu. (1 Mambo ya Nyakati 29:10-13) Ili tuwe na uhusiano mwema na Baba yetu wa kimbingu, ni lazima tuzungumze naye kwa ukawaida katika sala. (Warumi 12:12; Waefeso 6:18) Kani yake ya utendaji, inayopokewa kwa kuomba, inaweza kututia nguvu tufanye mapenzi yake tujapoletewa taabu zo zote au vishawishi na Shetani au ulimwengu wake.—1 Wakorintho 10:13; Waefeso 3:20.

3. (a) Ni nguvu gani tunayoweza kupokea kutoka kwa Mungu? (b) Ni kwa njia gani pekee tunaweza kudumisha uhusiano mwema na Mungu?

3 Labda unapigana kikweli ili ujiondolee tabia au zoea fulani lisilompendeza Mungu. Ikiwa ni hivyo, tafuta msaada wa Yehova. Mwendee katika sala. Mtume Paulo alifanya hivyo, naye aliandika: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.” (Wafilipi 4:13; Zaburi 55:22; 121:1, 2) Mwanamke aliyeacha mwendo wa uasherati alisema: “Yeye ndiye mtu aliye na ule uwezo wa kukusaidia utoke katika hali hiyo. Ni lazima uwe na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova, na njia pekee ya kuudumisha uhusiano huo wa kibinafsi ni kusali.”

4. Mwanamume mmoja alipataje nguvu ya kuacha mazoea ya kuvuta tumbako?

4 Hata hivyo huenda mtu akasema: ‘Mimi nimemwomba Mungu msaada mara nyingi, lakini bado nashindwa kuacha mabaya.’ Watu wanaovuta tumbako wamesema hivyo. Mtu aliye kama huyo alipoulizwa hivi: “Unasali wakati gani?” alijibu: “Jioni kabla ya kwenda kulala, asubuhi ninapoamka, halafu nikiisha kuwa dhaifu na kuvuta tumbako kidogo ninamwambia Yehova kwamba ninasikitika kwa yale ambayo nimefanya.” Rafikiye alisema: “Wakati ambao unahitaji msaada wa Mungu kweli kweli ni wakati ule unapotaka kunyosha mkono uishike tumbako, au sivyo? Huo ndio wakati ambao imekupasa umpelekee Yehova sala ili akutie nguvu.” Mwanamume huyo alipofanya hivyo, alipokea msaada wa kuacha kuvuta tumbako.

5. (a) Ni nini kinachotakwa ili kumtumikia Mungu vya kufaa? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba mara nyingi kuteseka kunahusika katika kuacha utendaji wenye dhambi?

5 Hiyo si kusema kwamba kumpelekea Mungu sala, pamoja na kujifunza Neno lake na kushirikiana na tengenezo lake linaloonekana, kutakufanyia iwe rahisi kutenda mema. Bado utatakwa ufanye jitihada; ndiyo, vita vikali, ambavyo huenda hata vikatokeza kuteseka. (1 Wakorintho 9:27) Mazoea mabaya yanaweza kutokeza tamaa nyingi za kutaka kufanya mabaya. Hivyo kwa kawaida kuteseka kunatokea wakati mtu anapoacha utendaji wenye dhambi. Je! wewe una nia ya kuteseka ili ufanye yaliyo mema?—1 Petro 2:20, 21.

SALA AMBAZO MUNGU ANASIKIA

6. (a) Ni kwa sababu gani wengi wanaona ni vigumu kusali? (b) Tunahitaji nini ili sala zetu zisikiwe?

6 Watu wengi wanaona ni vigumu kusali. “Mimi nina taabu ya kumpelekea sala mtu nisiyeweza kuona,” ndivyo alivyokiri mwanamke mmoja kijana. Kwa kuwa hakuna binadamu ambaye amemwona Mungu, tunahitaji imani ili tusali na kusikiwa na Mungu. Tunahitaji kuamini kwamba kweli Yehova yuko na anaweza kutimiza tunayoomba. (Waebrania 11:6) Tukiwa na imani ya aina hiyo, na tukimkaribia Mungu kwa unyofu wa moyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba atatusaidia. (Marko 9:23) Hivyo, ijapokuwa Kornelio yule afisa Mrumi wa jeshi hakuwa sehemu ya tengenezo la Mungu wakati huo, aliposali kwa unyofu wa moyo ili apate mwongozo, Mungu alijibu sala yake.—Matendo 10:30-33.

7. (a) Ni sala za aina gani zinazompendeza Mungu? (b) Ni sala za aina gani ambazo Mungu hatasikiliza?

7 Watu fulani wanatatizwa sana kueleza mambo yaliyo katika mioyo yao. Walakini, hilo lisiwazuie kusema na Mungu katika sala. Tunaweza kuwa na hakika kwamba yeye anajua mahitaji yetu na atafahamu tunayotaka kusema. (Mathayo 6:8) Ebu fikiri: Ni usemi gani ambao unathamini sana kutoka kwa mtoto—shukrani zake anazotoa kwa maneno rahisi, kwa unyofu wa moyo, au maneno maalumu (ya pekee) ambayo mtu fulani amemwambia aseme? Vivyo hivyo Baba yetu aliye mbinguni anathamini semi rahisi, za unyofu wa moyo, kutoka kwetu. (Yakobo 4:6; Luka 18:9-14) Hahitaji maneno maalumu au usemi fulani wa kidini. Yeye hata hatawasikiliza wale wanaosali kwa kutumia usemi usio wa kawaida au wenye maneno makubwa-makubwa ya kujivuna ili wajipendekeze kwa watu, au wanaosema mambo yale yale kwa kuyarudia-rudia bila unyofu wa moyo.—Mathayo 6:5, 7.

8. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Mungu anaweza kusikia sala zinazotolewa kwa ukimya? (b) Je! Biblia inaonyesha kwamba ni lazima tusali tukiwa katika hali fulani yo yote au mahali po pote?

8 Hata unaposali kwa ukimya, Mungu anaweza kusikia. Nehernia alipofanya hivyo, Mungu aliitikia ombi lake la moyo mnyofu, na vivyo hivyo la Hana. (Nehemia 2:4-8; 1 Samweli 1:11-13, 19, 20) Wala jambo lililo la maana si kikao cha mwili wa mtu anaposali. Unaweza kusali ukiwa katika hali yo yote, wakati wo wote na mahali po pote. Walakini, Biblia inaonyesha kwamba hali ya unyenyekevu, kama vile kuinamisha kichwa au kupiga magoti, inafaa. (1 Wafalme 8:54; Nehemia 8:6; Danieli 6:10; Marko 11:25; Yohana 11:41) Naye Yesu alionyesha kwamba ni vizuri ikiwa sala za kibinafsi zinaweza kutolewa faraghani, mahali pasipoonwa na watu.—Mathayo 6:6.

9. (a) Imetupasa tuelekeze sala zetu zote kwa nani, na kwa sababu gani? (b) Ili sala zetu zikubalike kwa Mungu, zimepasa zitolewe kwa jina la nani?

9 Sala ni sehemu ya ibada yetu. Kwa sababu hiyo Muumba wetu pekee, Yehova Mungu, ndiye amepaswa apelekewe sala zetu, wala si mtu mwingine ye yote. (Mathayo 4:10) Nayo Biblia inaonyesha kwamba inawapasa Wakristo wamfikie Mungu kupitia Yesu, aliyetoa uhai wake ili aondoe dhambi zetu. Maana yake ni kwamba imetupasa tupeleke sala zetu kwa jina la Yesu.—Yohana 14:6, 14; 16:23; Waefeso 5:20; 1 Yohana 2:1, 2.

10. (a) Ni sala za nani zisizompendeza Mungu? (b) Ni takwa gani la kwanza ambalo ni lazima tulitimize ikiwa sala zetu zitasikiwa na Mungu?

10 Walakini, je! ni sala zote zinazompendeza Yehova? Biblia inasema hivi: “Yeye aligeuzaye sikio lake asiisikie sheria, hata sala yake ni chukizo.” (Mithali 28:9; 15:29; Isaya 1:15) Kwa hiyo tukitaka Mungu asikie sala zetu, takwa la kwanza ni kwamba tufanye mapenzi yake, tuzitii sheria zake. Bila hivyo Mungu hatatusikiliza, kama vile mtu mnyofu hangesikiliza kipindi cha redio ambacho anaona si chenye adili njema. Biblia inasema: “Lo lote tuombalo, twalipokea kwake, kwa kuwa twazishika amri zake, na kuyatenda yapendezayo machoni pake.”—1 Yohana 3:22.

11. Maana yake nini kujitahidi kutimiza yale tunayoomba?

11 Maana ya hiyo ni kwamba lazima tujitahidi kutimiza yale tunayoomba. Kwa mfano, lingekuwa kosa mtu kumwomba Mungu msaada ili aache kuvuta tumbako au bangi kisha aende akanunue vitu hivyo. Wala hangeweza kumwomba Yehova msaada ili aepuke uasherati kisha asome vitabu na kutazama sinema na vipindi vya televisheni vinavyoonyesha uasherati. Au ikiwa kucheza kamari ndio udhaifu wa mtu, hangeweza kumwomba Mungu msaada aache kucheza kamari kisha aende kwenye mashindano ya farasi au mahali penginepo ambapo michezo ya kamari inaendeshwa. Ili sala zetu zisikiwe na Mungu, tunahitaji kumwonyesha kwa vitendo vyetu kwamba tunapomwambia mambo fulani hatuyasemi kwa mchezo tu.

12. (a) Ni mambo gani tunayoweza kutia katika sala zetu? (b) Ili sala zetu ziwe zenye kupendeza kwa Mungu, lazima tujifunze nini?

12 Basi, ni mambo gani ya kibinafsi tunayoweza kutia katika sala tunazomtolea Yehova? Kwa hakika, lo lote linalohusu uhusiano wetu pamoja na Mungu linafaa kuzungumzwa katika sala, kutia ndani afya yetu ya kimwili, vilevile kulea watoto. (2 Wafalme 20:1-3; Waamuzi 13:8) Mtume Yohana aliandika hivi: “Hata kiwe ni kitu gani tunachoomba kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia sisi.” (1 Yohana 5:14, NW) Hivyo jambo la maana ni kwamba maombi yetu yapatane na mapenzi ya Mungu. Maana ya hiyo ni kwamba kwanza tunahitaji tujifunze yaliyo mapenzi yake. (Mithali 3:5, 6) Ndipo tukiyafikiria mapenzi na makusudi ya Mungu tunaposali, badala ya kuhangaikia faida zetu wenyewe tu, sala zetu zitakubalika kwa Yehova. Inafaa kumshukuru Yehova kila siku kwa mema anayotupatia.—Yohana 6:11, 23; Matendo 14:16, 17.

13. (a) Yesu alionyeshaje mambo yanayopasa kuwa ndiyo ya kwanza kufikiriwa katika sala zetu? (b) Ni mambo gani yaliyo ya pili kwa ubora tunayopaswa kuomba?

13 Yesu aliwapa wafuasi wake sala ya kielelezo iwaongoze kujua aina ya sala ambayo Mungu anakubali. (Mathayo 6:9-13) Sala hiyo inaonyesha kwamba jina la Mungu, ufalme wake na kufanya mapenzi yake duniani ndiyo mambo ya kwanza. La pili, tunaweza kuomba mahitaji yetu binafsi, kama vile chakula chetu cha kila siku, msamaha wa dhambi, na kukombolewa katika kishawishi na kutokana na yule mwovu, Shetani Ibilisi.

SALA ZA KUSAIDIA WENGINE

14. Biblia inaonyeshaje umaana wa kusali kwa ajili ya wengine?

14 Yesu alionyesha kwa mfano wake umaana wa kusali kwa ajili ya wengine. (Luka 22:32; 23:34; Yohana 17:20) Mtume Paulo alijua ubora wa sala za namna hiyo na mara nyingi aliwaomba wengine wasali kwa ajili yake. (1 Wathesalonike 5:25; 2 Wathesalonike 3:1; Warumi 15:30) Alipokuwa gerezani aliandika hivi: “Ninatumaini kwamba kupitia sala za ninyi watu nitawekwa huru.” (Filemoni 22, NW; Waefeso 6:18-20) Ya kwamba upesi baada ya hapo Paulo alifunguliwa kutoka gerezani inaonyesha faida ya sala zilizotolewa kwa ajili yake.

15. Ni maombi ya aina gani tunayoweza kutoa kwa habari ya watu tunaopenda?

15 Vilevile Paulo alitoa sala zenye msaada kwa ajili ya wengine. “Sikuzote tunasali kwa ajili yenu, kwamba Mungu wetu apate kuwahesabu ninyi kuwa mnastahili mwito wake,” akaandika. (2 Wathesalonike 1:11, NW) Na kwa kundi jingine alieleza: “Sisi tunasali kwa Mungu ili msipate kutenda jambo lo tote baya . . . bali kwamba mwe mkifanya yaliyo mema.” (2 Wakorintho 13:7, NW) Bila shaka ni vema kufuata mfano wa Paulo na kutoa maombi kwa ajili ya watu tunaopenda kwa kuwataja wazi-wazi. Kweli kweli, “kuomba [au, kusihi kwa unyofu wa moyo kwa] mwenye haki kwafaa sana, akiomba kwa bidii.”—Yakobo 5:13-16.

16. (a) Ili tupate msaada unaohitajiwa, imetupasa tusali wakati gani? (b) Ni kwa sababu gani sala ni pendeleo kubwa sana?

16 Anapoongoza funzo la Biblia, mara nyingi mhudumu mmoja anauliza hivi: “Je! wewe unasali nyakati nyingine, si wakati ule tu wa funzo lako la Biblia la kila juma?” Ili tupate msaada tunaohitaji, lazima tuseme na Mungu mara nyingi katika sala. (1 Wathesalonike 5:17; Luka 18:1-8) Jifunze kuzungumza naye kwa unyenyekevu kama vile ungezungumza na rafiki unayependa na kutumainia. Kweli kweli, ni pendeleo zuri ajabu kuweza kumpelekea sala yule Mtawala mtukufu wa ulimwengu mzima, yule Msikiaji wa sala, na kujua kwamba yeye anakusikia!—Zaburi 65:2.

[Picture on page 227]

Imempasa mtu afanye nini anaposhawishwa kuvuta tumbako—asali ili apate msaada au ashindwe na kishawishi?

[Picture on page 229]

Je! wewe unasali upate msaada kisha unajiingiza katika utendaji unaoweza kukuongoza utende mabaya?

[Picture on page 230]

Je! wewe unasali kwa faragha au ni wakati tu unapokuwa pamoja na wengine?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki