Ubatizo
Maana: Neno “batiza” linatokana na neno la Kigiriki ba·ptiʹzein, linalomaanisha “kuchovya, kutumbukiza.” (A Greek-English Lexicon, iliyoandikwa na Liddell na Scott) Ubatizo wa Kikristo wa maji ni wonyesho wa kwamba mtu anayebatizwa amejiweka wakfu kikamili, kabisa, na bila masharti kupitia Yesu Kristo ili afanye mapenzi ya Yehova Mungu. Maandiko hurejezea pia ubatizo wa Yohana, ubatizo kwa roho takatifu, ubatizo kwa moto, na mwingine mbalimbali.
Je, watu ambao kwa kweli wanaliamini Neno la Mungu hujizuia wasibatizwe?
Mt. 28:19, 20: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”
Mdo. 2:41: “Wale waliokubali neno lake kwa ukunjufu wa moyo wakabatizwa.”
Mdo. 8:12: “Walipomwamini Filipo, aliyekuwa akitangaza habari njema ya ufalme wa Mungu na juu ya jina la Yesu Kristo, wakabatizwa, wanaume na pia wanawake.”
Mdo. 8:36-38: “Sasa walipokuwa wakienda juu ya ile barabara, wakafika mahali penye maji, na towashi [Mwethiopia] akasema: ‘Tazama! Maji; ni nini kinachonizuia nisibatizwe?’ Ndipo akaamuru gari lisimame . . . naye [Filipo] akambatiza.”
Je, ubatizo wa maji wa Kikristo ni wa kunyunyizia maji au kuzamisha kabisa?
Marko 1:9, 10: “Yesu akaja . . . , Yohana akambatiza katika [Mto] Yordani. Mara moja alipopanda kutoka majini akaona mbingu zikifunguka.”
Mdo. 8:38: “Nao wote wawili wakashuka na kuingia ndani ya maji, Filipo na pia towashi; naye akambatiza.”
Je, Wakristo wa karne ya kwanza waliwabatiza watoto wachanga?
Mt. 28:19: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi . . . mkiwabatiza.”
Mdo. 8:12: “Walipomwamini Filipo . . . wakabatizwa, wanaume na pia wanawake.”
Hata hivyo, baadaye, Origen (185-254 W.K.) aliandika: “Ni desturi ya kanisa kwamba hata watoto wachanga wabatizwe.” (Selections From the Commentaries and Homilies of Origen, Madras, India; 1929, uku. 211) Ubatizo huo ulithibitishwa na Baraza la Carthage (karibu mwaka wa 252 W.K.).
Augustus Neander, mwanahistoria wa kidini, aliandika hivi: “Sikuzote kulikuwa na uhusiano kati ya imani na ubatizo; na kwa hiyo inaelekea sana . . . kwamba desturi hiyo ya kuwabatiza watoto wachanga haikujulikana katika kipindi hicho [katika karne ya kwanza]. . . . Kutambuliwa kwa desturi hiyo kuwa mapokeo ya mitume katika karne ya tatu, ni uthibitisho wa kupinga badala ya kuunga mkono kwamba ilitokana na mitume.”—History of the Planting and Training of the Christian Church by the Apostles (New York, 1864), uku. 162.
Je, ubatizo wa maji wa Kikristo unatokeza msamaha wa dhambi?
1 Yoh. 1:7: “Ikiwa tunatembea katika nuru kama yeye mwenyewe alivyo katika nuru, . . . damu ya Yesu Mwana wake hutusafisha kutoka katika dhambi yote.” (Kwa hiyo, damu ya Yesu ndiyo inayosafisha dhambi zetu wala si maji ya ubatizo.)
Mt. 3:11: “Mimi [Yohana Mbatizaji] ninawabatiza ninyi kwa maji kwa sababu ya toba yenu; lakini yule anayekuja nyuma yangu [Yesu Kristo] ana nguvu kuliko mimi, ambaye viatu vyake mimi sistahili kuvivua.” (Mstari wa 5 na 6, pia Matendo 13:24, huonyesha kwamba alilofanya Yohana lilielekezwa, si kwa watu wote, bali kwa Wayahudi. Kwa nini? Kwa sababu ya dhambi za Wayahudi dhidi ya agano la Sheria na kuwatayarisha kwa ajili ya Kristo.)
Mdo. 2:38: “Tubuni, na acheni kila mmoja wenu abatizwe katika jina la Yesu Kristo kwa msamaha wa dhambi zenu.” (Je, ubatizo wenyewe uliwaletea msamaha? Hebu fikiria: Wayahudi walioshiriki kumuua Kristo ndio walioambiwa maneno hayo. [Ona mstari wa 22 na 23.] Ubatizo wao ungethibitisha jambo fulani. Jambo gani? Kwamba sasa wanamwamini Yesu kuwa Masihi, yule Kristo. Kwa kufanya hivyo tu ndipo wangeweza kusamehewa dhambi zao. [Matendo 4:12; 5:30, 31])
Mdo. 22:16: “Simama, ubatizwe na uoshe dhambi zako kwa kuliitia jina lake.” (Pia Matendo 10:43)
Ni nani wanaobatizwa kwa roho takatifu?
1 Kor. 1:2; 12:13, 27: “Kwenu ninyi ambao mmetakaswa katika muungano na Kristo Yesu, mlioitwa kuwa watakatifu . . . Kwa kweli kwa roho moja sote tulibatizwa katika mwili mmoja, kama ni Wayahudi au ni Wagiriki, kama ni watumwa au ni walio huru, nasi sote tulinyweshwa roho moja. Basi ninyi ni mwili wa Kristo.” (Kama andiko la Danieli 7:13, 14, 27 linavyoonyesha, “watakatifu” hao hutawala pamoja na Mwana wa binadamu, Yesu Kristo, katika Ufalme.)
Yoh. 3:5: “Mtu asipozaliwa kwa maji na roho, hawezi kuingia katika ufalme wa Mungu.” (Mtu ‘anazaliwa kwa roho’ wakati anapobatizwa kwa roho hiyo. Andiko la Luka 12:32 linaonyesha kwamba “kundi dogo” tu ndilo lililo na pendeleo hilo. Ona pia Ufunuo 14:1-3.)
Je, wote wanaobatizwa kwa roho takatifu husema kwa lugha au wana zawadi za maponyo?
1 Kor. 12:13, 29, 30: “Kwa kweli kwa roho moja sote tulibatizwa katika mwili mmoja . . . Je, wote ni mitume? . . . Je, wote hufanya matendo yenye nguvu? Je, wote wana zawadi za maponyo? Je, wote husema kwa lugha?”
Ona pia “Uponyaji” na “Kusema kwa Lugha.”
‘Ubatizo kwa ajili ya wafu’—unamaanisha nini?
1 Kor. 15:29, UV: “Au je! Wenye kubatizwa kwa ajili ya wafu watafanyaje? Kama wafu hawafufuliwi kamwe, kwa nini kubatizwa kwa ajili yao?”
Neno la Kigiriki hy·perʹ, linalotafsiriwa hapa “kwa ajili ya,” pia humaanisha “juu ya,” “kwa niaba ya,” “badala ya,” “kwa kusudi la,” n.k. (A Greek-English Lexicon, iliyoandikwa na Liddell na Scott) Neno hilo linamaanisha nini katika andiko hilo? Je, Paulo alikuwa akipendekeza watu walio hai wabatizwe kwa ajili ya wale waliokuwa wamekufa bila kubatizwa?
Yale maandiko mengine yanayotaja kifo kuhusiana na ubatizo moja kwa moja hurejelea ubatizo ambao mtu mwenyewe hubatizwa, wala si ubatizo kwa ajili ya mtu mwingine, aliyekufa
Rom. 6:3: “Hamjui kwamba sisi sote tuliobatizwa katika Kristo Yesu tulibatizwa katika kifo chake?” (Pia Marko 10:38, 39)
Kol. 2:12: “Kwa maana [ninyi washiriki walio hai wa kutaniko la Kolosai] mlizikwa pamoja naye katika ubatizo wake, na kwa uhusiano pamoja naye mlifufuliwa pia pamoja kupitia imani yenu katika utendaji wa Mungu, aliyemfufua huyo kutoka kwa wafu.”
Fasiri iliyo katika “Tafsiri ya Ulimwengu Mpya” ni sahihi kisarufi na inapatana na maandiko haya mengine ya Biblia
1 Kor. 15:29: “Kama sivyo, watafanya nini wale wanaobatizwa kwa kusudi la kuwa wafu? Ikiwa wafu hawatafufuliwa kamwe, kwa nini pia wanabatizwa kwa kusudi la kuwa hivyo?” (Kwa hiyo, wanabatizwa, au wanazamishwa, katika mwendo wa maisha utakaoongoza kwenye kifo cha kushika utimilifu kama kile cha Kristo na kisha wafufuliwe kwenye uzima wa kiroho kama yeye.)
Ni nini linalotokana na ubatizo wa moto?
Luka 3:16, 17: “Yeye [Yesu Kristo] atawabatiza ninyi kwa . . . moto. Sepetu yake ya kupepetea imo mkononi mwake ili kuusafisha kabisa uwanja wake wa kupuria . . . Makapi atayateketeza kwa moto usioweza kuzimwa.” (Uharibifu wa makapi hayo utakuwa wa milele.)
Mt. 13:49, 50: “Hivyo ndivyo itakavyokuwa katika umalizio wa mfumo wa mambo: malaika watatoka kwenda na kuwatenga waovu kutoka katikati ya waadilifu nao watawatupa ndani ya tanuru ya moto.”
Luka 17:29, 30: “Siku ambayo Loti alitoka Sodoma kulinyesha moto na kiberiti kutoka mbinguni na kuwaangamiza wote. Itakuwa vivyo hivyo siku ile ambayo Mwana wa binadamu atafunuliwa.”
Si sawa na ubatizo kwa roho takatifu, uliokuwa wa wanafunzi
Mdo. 1:5: “Yohana, kwa kweli, alibatiza kwa maji, lakini ninyi [mitume waaminifu wa Yesu] mtabatizwa kwa roho takatifu siku chache baadaye.”
Mdo. 2:2-4: “Ghafula kukatokea kutoka mbinguni kelele kama ile ya upepo wenye nguvu unaovuma, nao ukaijaza nyumba yote ambamo walikuwa wameketi. Nao wakaona ndimi kama za moto, nazo zikagawanyika huku na huku, na mmoja ukaketi juu ya [lakini haukumfunika au kumzamisha] kila mmoja wao, nao wote wakajazwa roho takatifu wakaanza kusema katika lugha tofauti, kama vile roho ilivyokuwa ikiwawezesha kusema.”