Vipindi vya Wakati
Maana: Tarehe (miezi, miaka) hutia alama wakati ambapo matukio yanatendeka. Biblia huonyesha wakati kwa kuuhusianisha na muda wa maisha ya watu mbalimbali, kipindi ambacho watawala fulani walitawala, au matukio mengine yanayojulikana. Ina orodha kamili ya wakati ambapo matukio yalitendeka tangu kuumbwa kwa Adamu. Pia, orodha hiyo ya Biblia ilionyesha mapema wakati ambapo matukio fulani muhimu yangetukia katika utimizo wa kusudi la Mungu. Kalenda ya Gregory, inayotumiwa sasa na watu wengi ulimwenguni, ilianza kutumiwa mwaka wa 1582. Marejeo mbalimbali hayakubaliani juu ya wakati ambapo inasemekana kuwa matukio fulani katika historia ya kale yalitendeka. Hata hivyo, miaka fulani muhimu, kama vile 539 K.W.K., wakati wa kuanguka kwa Babiloni, na 537 K.W.K., wakati wa kurudi kwa Wayahudi kutoka utekwani, imethibitishwa kabisa. (Ezra 1:1-3) Kwa kutegemea miaka hiyo, inawezekana kutumia kalenda za kisasa kuonyesha wakati ambapo matukio ya kale ya Biblia yalitendeka.
Je, wanasayansi wamethibitisha kwamba wanadamu wamekuwa duniani kwa mamilioni ya miaka, wala si kwa maelfu kadhaa ya miaka kama vile Biblia inavyoonyesha?
Njia zinazotumiwa na wanasayansi za kuhesabu wakati hutegemea makisio yanayoweza kusaidia lakini ambayo mara nyingi huleta matokeo yanayopingana kabisa. Kwa hiyo, vipindi vya wakati wanavyotoa husahihishwa kila mara.
Ripoti moja katika New Scientist la Machi 18, 1982, inasema hivi: “‘Siamini kwamba nilisema maneno niliyosema mwaka mmoja hivi uliopita.’ Ndivyo Richard Leakey alivyowaambia wasikilizaji mashuhuri kwenye mazungumzo ya jioni Ijumaa iliyopita katika Royal Institution. Alikuwa amekuja kufunua kwamba maoni ya watu wengi, ambayo hivi karibuni alikuwa ameyaunga mkono katika mfululizo wa vipindi vyake katika televisheni ya BBC The Making of Mankind, ‘huenda sehemu zake muhimu zilikuwa na makosa.’ Sasa anaona mzazi wa kale zaidi wa mwanadamu kuwa ni mchanga sana kuliko ile miaka milioni 15-20 ambayo alikuwa ameunga mkono kwa uthabiti sana katika televisheni.”—Uku. 695.
Mara kwa mara, njia mpya za kukadiria wakati hutokezwa. Njia hizo zinategemeka kadiri gani? The New Encyclopædia Britannica (1976, Macropædia, Buku la 5, uku. 509) inasema hivi kuhusu njia moja inayoitwa thermoluminescence: “Kwa sasa hivi, kupima wakati kwa kutumia thermoluminescence hutegemea sana tumaini badala ya mambo ya hakika.” Pia, gazeti Science (Agosti 28, 1981, uku. 1003) linasema kwamba mifupa ambayo kwa kipimo cha amino asidi ilionekana kuwa ina umri wa miaka 70,000, kwa kipimo cha harakati-redio ilionekana kuwa ina miaka 8,300 au 9,000 tu.
Popular Science (Novemba 1979, uku. 81) linasema kwamba mwanafizikia Robert Gentry “anaamini kwamba huenda vipimo vyote vya wakati ambavyo vilipimwa kwa kutumia harakati-redio vimekosa kulenga shabaha—si kwa miaka michache tu, bali kwa miaka mingi sana.” Makala hiyo inasema kwamba uchunguzi wake unaweza kufanya watu wakate kauli kwamba “huenda ikawa mwanadamu amekuwapo kwa maelfu machache tu ya miaka badala ya miaka milioni 3.6.”
Hata hivyo, kumbuka wanasayansi wanaamini kwamba umri wa dunia yenyewe ni mkubwa zaidi kuliko umri wa mwanadamu. Biblia haipingi jambo hilo.
Je, umri wa watu walioishi kabla ya Gharika, kama ilivyotajwa katika Biblia, ulipimwa kulingana na miaka ileile tunayotumia sisi?
Ikiwa mtu atafikiri kwamba “miaka” hiyo ni lazima ilingane na miezi yetu, basi Enoshi alikuwa na umri wa miaka saba alipopata wana, na Kenani alikuwa na umri wa miaka mitano tu alipomzaa mwana. (Mwa. 5:9, 12) Bila shaka, jambo hilo haliwezekani.
Orodha ya wakati iliyotolewa kuhusiana na Gharika huonyesha urefu wa miezi na miaka iliyotumiwa wakati huo. Kulinganisha Mwanzo 7:11, 24 na 8:3, 4 huonyesha kwamba miezi mitano (kutoka tarehe 17 ya mwezi wa 2 mpaka tarehe 17 ya mwezi wa 7) ililingana na siku 150, au miezi mitano yenye siku 30 kila mwezi. “Mwezi wa kumi” pamoja na vipindi vingine baada ya mwezi huo kabla ya kufika mwaka unaofuata, unatajwa moja kwa moja. (Mwa. 8:5, 6, 8, 10, 12-14) Inaonekana kwamba miaka yao ilikuwa ya miezi kumi na miwili yenye siku 30 kila mwezi. Tangu zamani za kale, kalenda ya mwezi ilirekebishwa mara kwa mara ili kulingana na urefu wa mwaka wa jua, kama inavyoonyeshwa na Waisraeli wanaposhika sherehe za kukusanya za majira katika nyakati hususa. Kwa hiyo sherehe hizo ziliendelea kutukia wakati wa majira yanayofaa.—Law. 23:39.
Kumbuka kwamba Mungu aliwaumba wanadamu waishi milele. Dhambi ya Adamu ndiyo iliyoleta kifo. (Mwa. 2:17; 3:17-19; Rom. 5:12) Wale walioishi kabla ya Gharika walikuwa karibu zaidi na ukamilifu kuliko sisi leo, kwa hiyo waliishi muda mrefu zaidi. Lakini kila mmoja wao alikufa kabla ya kufikia miaka elfu moja.
Kwa nini Mashahidi wa Yehova husema kwamba Ufalme wa Mungu ulianzishwa mwaka wa 1914?
Mambo mawili yanayothibitisha yanaelekeza kwenye mwaka huo: (1) Orodha ya wakati ya Biblia na (2) matukio ya tangu mwaka wa 1914 yanayotimiza unabii. Hapa tutachunguza orodha ya wakati. Kuhusu utimizo wa unabii, ona kichwa “Siku za Mwisho.”
Soma Danieli 4:1-17. Mstari wa 20-37 huonyesha kwamba unabii huo ulitimia kumhusu Nebukadneza. Lakini pia una utimizo mkubwa zaidi. Tunajuaje hivyo? Mstari wa 3 na 17 huonyesha kwamba ndoto ambayo Mungu alimpa Mfalme Nebukadneza hushughulika na Ufalme wa Mungu na ahadi ya Mungu ya kumpa Ufalme huo “yeyote yule amtakaye . . . [hata] mwanadamu aliye wa hali ya chini zaidi.” Biblia nzima huonyesha kwamba Yehova alikusudia Mwana wake mwenyewe, Yesu Kristo, awatawale wanadamu akiwa mwakilishi Wake. (Zab. 2:1-8; Dan. 7:13, 14; 1 Kor. 15:23-25; Ufu. 11:15; 12:10) Maelezo ya Biblia kumhusu Yesu yanaonyesha kwamba kwa kweli ndiye aliyekuwa “mwanadamu aliye wa hali ya chini zaidi.” (Flp. 2:7, 8; Mt. 11:28-30) Basi, ile ndoto ya kinabii inaelekeza kwenye wakati ambapo Yehova angempa Mwana wake mwenyewe mamlaka ya kuwatawala wanadamu.
Ni jambo gani ambalo lingetokea kabla ya wakati huo? Utawala juu ya wanadamu, kama unavyowakilishwa na mti na kisiki chake, ungekuwa na “moyo wa mnyama.” (Dan. 4:16) Katika historia ya wanadamu kungekuwa na serikali ambazo zingekuwa na tabia za wanyama-mwitu. Katika nyakati za kisasa, tai anatumiwa kuwakilisha Marekani; simba, Uingereza; joka, China. Pia Biblia inatumia wanyama-mwitu kuwakilisha serikali za ulimwengu na mfumo wa ulimwenguni pote wa utawala wa kibinadamu chini ya uvutano wa Shetani. (Dan. 7:2-8, 17, 23; 8:20-22; Ufu. 13:1, 2) Kama Yesu alivyoonyesha katika unabii wake unaoelekeza kwenye umalizio wa mfumo wa mambo, Yerusalemu “lingekanyagwa-kanyagwa na mataifa, mpaka nyakati zilizowekwa za mataifa zitimie.” (Luka 21:24) “Yerusalemu” liliwakilisha Ufalme wa Mungu kwa sababu ilisemekana kwamba wafalme wake walikaa kwenye “kiti cha ufalme wa Yehova.” (1 Nya. 28:4, 5; Mt. 5:34, 35) Basi, serikali za Mataifa, zinazowakilishwa na wanyama-mwitu, ‘zingeikanyaga-kanyaga’ haki ya Ufalme wa Mungu ya kuelekeza mambo ya wanadamu nazo zingetawala chini ya uongozi wa Shetani.—Linganisha na Luka 4:5, 6.
Serikali hizo zingeruhusiwa zitawale kwa muda gani kabla Yehova hajampa Yesu Kristo Ufalme huo? Andiko la Danieli 4:16 linasema “nyakati saba” (“miaka saba,” BHN, na pia kielezi-chini katika VB kwenye mstari wa 13). Biblia huonyesha kwamba katika kuhesabu wakati wa kinabii, siku moja huhesabiwa kuwa mwaka mmoja. (Eze. 4:6; Hes. 14:34) Basi, ni “siku” ngapi zinazohusika? Andiko la Ufunuo 11:2, 3 hueleza waziwazi kwamba miezi 42 (miaka 3 1/2) katika unabii huo huhesabiwa kuwa siku 1,260. Miaka 7 itakuwa mara mbili ya siku hizo, au siku 2,520. Kutumia kanuni ya “siku moja kwa mwaka mmoja” kutatokeza miaka 2,520.
“Nyakati saba” zilianza wakati gani? Baada ya Sedekia, mfalme wa mwisho katika utawala uliowakilisha Ufalme wa Mungu, kuondolewa na Wababiloni kutoka kiti cha ufalme katika Yerusalemu. (Eze. 21:25-27) Mwishowe, mapema mwezi wa Oktoba 607 K.W.K., sehemu ya mwisho ya enzi ya Kiyahudi ikatoweka. Kufikia wakati huo gavana Myahudi, Gedalia, ambaye Wababiloni walikuwa wamemwacha atawale, alikuwa ameuawa, na Wayahudi waliobaki walikuwa wamekimbilia Misri. (Yeremia, sura ya 40-43) Orodha ya wakati ya Biblia inayotegemeka inaonyesha kwamba hilo lilitukia miaka 70 kabla ya mwaka wa 537 K.W.K., mwaka ambao Wayahudi walirudi kutoka utekwani; yaani, ilitukia kufikia mapema mwezi wa Oktoba 607 K.W.K. (Yer. 29:10; Dan. 9:2; kwa habari zaidi, ona kitabu “Ufalme Wako Uje,” uku. 186-189.)
KUHESABU ZILE “NYAKATI SABA”
“Nyakati saba” = 7 x 360 = miaka 2,520
“Wakati” wa Kibiblia, au mwaka = 12 x siku 30 = 360. (Ufu. 11:2, 3; 12:6, 14)
Katika utimizo wa “nyakati saba” kila siku hulingana na mwaka mmoja. (Eze. 4:6; Hes. 14:34)
Mapema Oktoba, 607 K.W.K., hadi Desemba 31, 607 K.W.K. = mwaka 1⁄4
Januari 1, 606 K.W.K., hadi Desemba 31, 1 K.W.K. = miaka 606
Januari 1, 1 W.K., hadi Desemba 31, 1913 = miaka 1,913
Januari 1, 1914, hadi mapema Oktoba, 1914 = mwaka 3/4
Jumla: miaka 2,520
Basi, wakati huo unahesabiwaje mpaka mwaka wa 1914? Kuhesabu miaka 2,520 kutoka mapema mwezi wa Oktoba 607 K.W.K., hutufikisha mapema mwezi wa Oktoba 1914 W.K., kama ilivyoonyeshwa katika chati.
Ni nini lililotukia wakati huo? Yehova alimkabidhi Mwana wake, Yesu Kristo, aliyetukuzwa mbinguni, mamlaka ya kuwatawala wanadamu.—Dan. 7:13, 14.
Basi kwa nini bado kuna uovu mwingi duniani? Baada ya Kristo kutawazwa, Shetani na roho wake waovu walitupwa kutoka mbinguni mpaka duniani. (Ufu. 12:12) Kristo akiwa Mfalme hakuchukua hatua ya kuwaangamiza mara moja wote waliokataa kuikubali enzi kuu ya Yehova na kumkubali yeye mwenyewe akiwa Masihi. Badala yake, kama alivyotabiri, kazi ya kuhubiri duniani pote ilipasa kufanywa. (Mt. 24:14) Hiyo itasababisha kugawanywa kwa watu wa mataifa yote; wale walio waadilifu watapewa tazamio la uzima wa milele, na waovu watakatiliwa mbali milele katika kifo. (Mt. 25:31-46) Kabla ya wakati huo, hali ngumu sana zilizotabiriwa kutukia “siku za mwisho” zingeenea. Kama ilivyoonyeshwa chini ya kichwa “Siku za Mwisho,” matukio hayo yamekuwa yakionekana waziwazi tangu mwaka wa 1914. Mambo yote ambayo Yesu alitabiri yatatukia, kutia ndani “dhiki kuu” ambapo ulimwengu mbovu wa sasa utakoma.—Mt. 24:21, 22.
Mwisho wa ulimwengu huu mbovu utakuja wakati gani?
Yesu alijibu hivi: “Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.” Hata hivyo, alisema hivi pia: “Kwa kweli ninawaambia ninyi kwamba kizazi hiki hakitapitilia mbali kamwe mpaka mambo yote hayo yatukie.”—Mt. 24:36, 34.
Pia, baada ya kusimulia matukio ambayo yangefuata kuanzishwa kwa Ufalme mikononi mwa Yesu Kristo katika mwaka wa 1914, andiko la Ufunuo 12:12, huongeza hivi: “Furahini, enyi mbingu nanyi mnaokaa ndani yake! Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”