Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • rs uku. 74-uku. 77
  • Falsafa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Falsafa
  • Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Habari Zinazolingana
  • Kutumia kwa Yehova “Upumbavu” ili Kuwaokoa Wanaoamini
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Hekima ya Kweli Inapaza Sauti Kubwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • ‘Lo! Kina cha Hekima ya Mungu!’
    Mkaribie Yehova
  • “Heri Mtu Yule Aonaye Hekima”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
rs uku. 74-uku. 77

Falsafa

Maana: Neno falsafa linatokana na maneno ya Kigiriki yanayomaanisha “kupenda hekima.” Falsafa inayozungumziwa hapa haitokani na imani katika Mungu, bali inajaribu kuwapa watu wote maoni yanayopatana kuhusu ulimwengu na inajaribu kuwafanya wawe wachambuzi. Inatumia sana njia za kukisia-kisia badala ya kufanya uchunguzi ili kutafuta kweli.

Tunaweza kupataje ujuzi na hekima ya kweli?

Met. 1:7; Zab. 111:10: “Kumwogopa Yehova ndio mwanzo wa ujuzi . . . [na ] wa hekima.” (Ikiwa ulimwengu haukuumbwa na Muumba mwenye akili bali ulitokana na nguvu fulani tu zisizo na akili, basi je, kweli inawezekana kuwa na maoni yanayopatana kuhusu ulimwengu? Je, hekima inaweza kupatikana kwa kuchunguza kitu kisichopatana na akili? Wale wanaojaribu kuufahamu ulimwengu au uhai wenyewe, huku wakimkataa Mungu na kusudi lake, huambulia patupu. Wanaelewa kimakosa yale wanayojifunza na kutumia vibaya mambo wanayopata. Kutomwamini Mungu huharibu ufunguo unaoongoza kwenye ujuzi sahihi na hufanya isiwezekane kwa watu wote kuwa na maoni yanayopatana.)

Met. 2:4-7: “Ikiwa utaendelea kuutafuta kama fedha, na kuendelea kuutafuta kama hazina zilizofichika, ndipo utakapoelewa kumwogopa Yehova, nawe utapata kumjua Mungu. Kwa maana Yehova mwenyewe anatoa hekima; kinywani mwake hutoka ujuzi na utambuzi. Naye atawawekea wanyoofu hazina ya hekima inayotumika.” (Yehova hutoa msaada unaohitajika kupitia Neno lake lililoandikwa na tengenezo lake linaloonekana. Ni lazima pia mtu awe na hamu na bidii na kutumia akili kwa njia inayofaa.)

Je, inawezekana kupata kweli kamili kutoka Chanzo hiki?

2 Tim. 3:16; Yoh. 17:17: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu.” “[Yesu alimwambia Baba yake wa mbinguni:] Neno lako ni kweli.” (Je, si jambo linalopatana na akili kwamba Muumba wa ulimwengu anauelewa kikamili? Katika Biblia yeye hajatuambia mambo yote kuhusu ulimwengu, lakini yale ambayo ameandika humo si makisio; hayo ni ya kweli. Yeye pia ameonyesha katika Biblia kusudi lake kwa dunia na kwa wanadamu na jinsi atakavyolitimiza. Nguvu zake zisizo na mwisho, hekima yake kuu zaidi, haki yake isiyo na kasoro, na upendo wake mkuu vinatoa uhakikisho kwamba kusudi hilo litatimizwa kikamili, na kwa njia bora zaidi. Kwa hiyo sifa zake zinatuhakikishia kwamba kusudi lake lililoandikwa hutegemeka kabisa; hilo ni kweli.)

Falsafa za wanadamu zilitoka wapi?

Zinatokana na watu walio na upungufu: Biblia inatuambia hivi: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yer. 10:23) Historia inathibitisha kwamba kujaribu kupuuza upungufu huo hakujatokeza mambo mema. Wakati mmoja, “Yehova a[li]anza kumjibu Ayubu kutoka katika dhoruba ya upepo, akasema: ‘Ni nani huyu anayefunika shauri kwa maneno yasiyo na ujuzi? Tafadhali jifunge viuno vyako, kama mwanamume, na acha mimi nikuulize maswali, nawe unijulishe. Ulikuwa wapi nilipoweka msingi wa dunia? Niambie, ikiwa unaelewa.’” (Ayu. 38:1-4) (Kwa kawaida wanadamu wana upungufu. Isitoshe, maisha yao ni mafupi na kwa kawaida wanaishi katika utamaduni mmoja au mazingira ya aina moja tu. Kwa hiyo, ujuzi wao ni mchache, na mambo yote yanahusiana hivi kwamba sikuzote wanagundua mambo ambayo hawajapata kuyafikiria vya kutosha. Falsafa yoyote wanayoanzisha itakuwa na upungufu huo.)

Zinatokana na wanadamu ambao si wakamilifu: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Rom. 3:23) “Kuna njia ambayo imenyooka mbele ya mwanadamu, lakini njia za kifo ndizo mwisho wake baadaye.” (Met. 14:12) (Kwa sababu ya kutokamilika huko, mara nyingi falsafa za wanadamu huonyesha ubinafsi ambao labda huleta raha ya muda lakini pia kukata tamaa na huzuni nyingi.)

Zinachochewa na roho waovu: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yoh. 5:19) “Yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa.” (Ufu. 12:9) “Wakati fulani mlitembea ndani yake kulingana na mfumo wa mambo wa ulimwengu huu, kulingana na mtawala wa mamlaka ya hewa, roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii.” (Efe. 2:2) (Falsafa zinazowatia watu moyo wasitii matakwa mazuri na manyoofu ya Mungu zinaonyesha uvutano huo. Si ajabu kwamba, kama historia inavyothibitisha, mara nyingi falsafa na mipango ya wanadamu imewaletea watu wengi huzuni.)

Kwa nini ni jambo la busara kujifunza mafundisho ya Yesu Kristo badala ya falsafa za wanadamu?

Kol. 1:15-17: “Yeye [Yesu Kristo] ndiye mfano wa Mungu asiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote; kwa sababu kwa njia yake vitu vingine vyote viliumbwa mbinguni na duniani . . . Vitu vingine vyote vimeumbwa kupitia yeye na kwa ajili yake. Pia, yeye ni wa kabla ya vitu vingine vyote na kwa njia yake vitu vingine vyote vilifanywa kuwapo.” (Uhusiano wake wa karibu sana na Mungu unamwezesha atusaidie tujifunze kweli kumhusu Mungu. Zaidi ya hayo, akiwa yule ambaye vitu vingine vyote viliumbwa kupitia kwake, Yesu ana ujuzi kamili wa ulimwengu mzima ulioumbwa. Hakuna mwanafalsafa yeyote anayeweza kutupa msaada huo.)

Kol. 1:19, 20: “Mungu aliona ni vema ujazo wote ukae katika yeye [Yesu Kristo], na kupitia yeye apatanishe tena kwake mwenyewe vitu vingine vyote kwa kufanya amani kupitia damu aliyomwaga juu ya mti wa mateso.” (Kwa hiyo, Yesu Kristo ndiye yule ambaye kupitia kwake Mungu amekusudia kuupatanisha pamoja Naye tena uumbaji wote. Mungu pia amemkabidhi Yesu utawala juu ya dunia yote, kama inavyoonyeshwa katika Danieli 7:13, 14. Kwa hiyo, matazamio yetu ya kupata uzima wakati ujao yanategemea kumjua yeye na kukubali mafundisho yake.)

Kol. 2:8: “Mjihadhari: labda kuna mtu ambaye atawachukua ninyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyifu mtupu kulingana na pokeo la wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.” (Lingekuwa kosa baya kama nini kuchagua falsafa hiyo yenye udanganyifu ya wanadamu badala ya kujipatia hekima ya kweli tukiwa wanafunzi wa Yesu Kristo, ambaye ndiye mtu wa pili kwa ukuu ulimwenguni, wa pili kutoka kwa Mungu mwenyewe!)

Mungu anaionaje “hekima” inayotokana na falsafa ya wanadamu?

1 Kor. 1:19-25: “Imeandikwa: ‘Nitaiangamiza hekima ya watu wenye hekima, na akili ya watu wenye akili nitaitupa kando.’ Yuko wapi mtu mwenye hekima? Yuko wapi mwandishi? Yuko wapi mwenye kubishania maneno wa mfumo huu wa mambo? Je, Mungu hakuifanya hekima ya ulimwengu iwe upumbavu? Maana, kwa kuwa katika hekima ya Mungu, ulimwengu kupitia hekima yake haukuja kumjua Mungu, Mungu aliona vema kupitia upumbavu wa linalohubiriwa awaokoe wale wanaoamini. . . . Kwa sababu kitu kipumbavu [machoni pa watu wa ulimwengu] cha Mungu ni chenye hekima zaidi kuliko wanadamu, na kitu dhaifu [machoni pa watu wa ulimwengu] cha Mungu ni chenye nguvu zaidi kuliko wanadamu.” (Maoni hayo ya Mungu hakika si ya kuonea wala hayakosi kupatana na akili. Yeye ameandaa katika Biblia, ambayo ni kitabu kinachoenezwa zaidi ulimwenguni, taarifa iliyo wazi kuhusu kusudi lake. Amewatuma mashahidi wake wawatangazie wote wanaotaka kusikiliza. Ni upumbavu kama nini kwa kiumbe chochote kufikiri kwamba kina hekima nyingi kuliko Mungu!)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki