Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • si kur. 19-25
  • Kitabu Cha Biblia Namba 2—Kutoka

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kitabu Cha Biblia Namba 2—Kutoka
  • “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YALIYOMO KATIKA KUTOKA
  • KWA NINI NI CHENYE MAFAA
  • Kuzijua Njia za Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Kutoka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Kutoka—Kutoka Utawala wa Mabavu Mpaka Kwenye Utaratibu wa Kitheokrasi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Yesu Kristo Alikuwaje Nabii Kama Musa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
Pata Habari Zaidi
“Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
si kur. 19-25

Kitabu Cha Biblia Namba 2—Kutoka

Mwandikaji: Musa

Mahali Kilipoandikiwa: Jangwani

Uandikaji Ulikamilishwa: 1512 K.W.K.

Wakati Uliohusishwa: 1657-1512 K.W.K.

1. (a) Ni nini mambo makuu ya Kutoka? (b) Ni majina gani yamepewa Kutoka, nacho ni mwendelezo wa simulizi gani?

MASIMULIZI yenye kugusa moyo ya ishara na miujiza yenye maana kubwa alizofanya Yehova katika kukomboa watu wa jina lake kutoka kwenye mateso ya Misri, kupanga Israeli kitengenezo wakiwa mali yake ya pekee kama “ufalme wa makuhani, na taifa takatifu,” na mwanzo wa historia ya Israeli likiwa taifa la kitheokrasi—hayo ndiyo mambo makuu ya kitabu cha Biblia cha Kutoka. (Kut. 19:6) Katika Kiebrania kinaitwa We’elʹleh shemohthʹ, maana yake “Sasa haya ndiyo majina,” au kwa usahili Shemohthʹ, “Majina,” kulingana na maneno yacho ya kwanza. Jina la ki-siku-hizi (la Kiingereza) linatoka kwa Septuagint ya Kigiriki, ambamo huitwa Eʹxo·dos, ambalo limetoholewa Kilatini kuwa Exodus, maana yake “Kutoka” au “Mwondoko.” Kwamba Kutoka ni mwendelezo wa simulizi katika Mwanzo huonyeshwa na neno la ufunguzi, “Basi” (kwa uhalisi, “Na”), na kwa kuorodhesha tena majina ya wana wa Yakobo, kama ilivyotwaliwa kutoka kwa maandishi kamili zaidi ya Mwanzo 46:8-27.

2. Kutoka chafunua nini kuhusu jina YEHOVA?

2 Kitabu cha Kutoka hufunua jina bora sana la Mungu, YEHOVA, likiwa na utukufu na utakato walo wote. Akiendelea kuonyesha kwa uwazi sana kina cha maana ya jina lake, Mungu alimwambia Musa, “MIMI NITATHIBITIKA KUWA KILE AMBACHO MIMI NITATHIBITIKA KUWA,” na akaongeza kwamba yeye apaswa kuambia Israeli, “MIMI NITATHIBITIKA KUWA [Kiebrania: יהוה, ’Eh·yehʹ, kutoka kitenzi cha Kiebrania ha·yahʹ] amenituma kwenu nyinyi.” Jina YEHOVA (יהוה, YHWH) hutoka kwa kitenzi cha Kiebrania cha aina moja ha·wahʹ, “kuwa,” na kwa hakika humaanisha “Yeye Husababisha Iwe.” Hakika uwezo na vitendo vya kutia hofu vya Yehova ambavyo sasa alitokeza kwa ajili ya watu wake, Israeli, vilitukuza na kuvisha jina hilo utukufu mkubwa, kulifanya ukumbusho “kizazi baada ya kizazi,” jina la kupewa kicho kwa umilele. Kati ya mambo yote kuna mafaa zaidi kwamba sisi tujue historia nzuri ajabu inayolizunguka jina hilo na kwamba sisi tuabudu Mungu pekee wa kweli, Yeye ambaye anajulisha rasmi hivi, “Mimi ni Yehova.”a—Kut. 3:14, 15; 6:6, NW.

3. (a) Twajuaje kwamba Musa alikuwa mwandikaji wa Kutoka? (b) Kutoka kiliandikwa lini, nacho chahusu kipindi gani?

3 Musa ndiye mwandikaji wa Kutoka, hilo likionyeshwa kwa kuwa ndicho buku la pili la Pentateuki. Kitabu chenyewe kinasajili (kinaandika) visa vitatu vya Musa kufanya maandishi yaliyoandikwa kwa kuelekezwa na Yehova. (17:14; 24:4; 34:27) Kulingana na wasomi wa Biblia Westcott na Hort, Yesu na waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo wananukuu au kurejezea Kutoka mara zaidi ya 100, kama wakati Yesu aliposema: “Je! Musa hakuwapa torati?” Kutoka kiliandikwa katika jangwa la Sinai, katika mwaka 1512 K.W.K., mwaka mmoja baada ya wana wa Israeli kutoka Misri. Kinachukua kipindi cha miaka 145, tangu kifo cha Yusufu katika 1657 K.W.K. hadi kusimamishwa kwa tabenakulo (hema) ya ibada ya Yehova katika 1512 K.W.K.—Yn. 7:19; Kut. 1:6; 40:17.

4, 5. Ni ushuhuda gani wa kiakiolojia ambao waunga mkono simulizi la Kutoka?

4 Kwa kufikiria kwamba matukio ya Kutoka yalitukia miaka kama 3,500 iliyopita, kuna kiasi kikubwa cha kushangaza cha ushuhuda wa kiakiolojia (kuchimbuliwa kwa vitu vya kale) na mwingineo wa nje unaothibitisha usahihi wa maandishi hayo. Majina ya Kimisri yanatumiwa kwa usahihi katika Kutoka, na vichwa vya habari vilivyotumiwa vyalingana na vya maandishi ya Kimisri. Akiolojia huonyesha kwamba ilikuwa desturi ya Wamisri kuruhusu wageni kuishi Misri lakini kuendelea kujitenga nao. Maji ya Naili yalitumiwa kuogea, jambo linalokumbusha kwamba binti ya Farao alioga humo. Matufali yaliyotengenezwa kwa nyasi au bila hizo yamepatikana. Pia, wakati wa fanaka ya Misri wafanya mizungu walikuwa mashuhuri.—Kut. 8:22; 2:5; 5:6, 7, 18; 7:11.

5 Majumba ya vitu vya ukumbusho huonyesha kwamba Mafarao waliongoza kibinafsi wapanda-magari ya farasi wa vita kwenda kwenye pigano, na Kutoka hudokeza kwamba Farao wa siku za Musa alifuata desturi hiyo. Jinsi alivyoshushiwa staha! Lakini ikoje kwamba maandishi ya kale ya Kimisri hayatoi mrejezo wowote juu ya safari ya Waisraeli katika bara lao wala msiba uliopata Misri? Akiolojia imeonyesha kwamba ilikuwa desturi kwa nasaba mpya ya watawala Wamisri kufuta chochote kisicholeta sifa katika maandishi yaliyotangulia. Wao hawakuandika kamwe ushinde wenye kushusha hadhi. Yale mapigo juu ya miungu ya Misri—kama vile mungu wa Naili, mungu-vyura, na mungu-jua—yaliyovunjia heshima miungu hiyo bandia na kuonyesha Yehova kuwa mkuu zaidi, hayangefaa vitabu vya taifa lenye kiburi.—14:7-10; 15:4.b

6. Kupiga kambi kwa mapema kwa Waisraeli hutambulishwa kwa ujumla na sehemu zipi?

6 Utumishi wa miaka 40 wa Musa akiwa mchungaji chini ya Yethro ulimfahamisha hali za maisha na sehemu zenye maji na chakula katika eneo hilo, kwa njia hiyo kumstahilisha vizuri aongoze kule Kutoka. Njia yenyewe ya kule Kutoka haiwezi kufuatishwa kwa uhakika leo, kwa kuwa sehemu mbalimbali zinazotajwa katika simulizi hilo haziwezi kujulikana kikamili. Hata hivyo, Mara, mojawapo kambi za mapema katika Peninsula ya Sinai, kwa kawaida hutambulishwa kuwa ‛Ein Hawwara, kilometa 80 Kusini ya Kusini-Mashariki mwa Suez ya kisasa. Elimu, mahali pa kambi ya pili, tangu zamani hutambulishwa kuwa Wadi Gharandel, karibu kilometa 88 Kusini ya Kusini-Mashariki mwa Suez. Linalovutia ni kwamba, sehemu hiyo ya kisasa yajulikana kuwa mahali pa chemchemi penye majani mabichi na mitende, ikikumbusha Elimu ya Kibiblia, iliyokuwa na “chemchemi kumi na mbili, na mitende sabini.”c Hata hivyo, uasilia wa simulizi la Musa hautegemei Waakiolojia kuthibitisha kambi mbalimbali kwenye njia iliyopitwa.—15:23, 27.

7. Ni ushuhuda gani mwingine, kutia ndani ujenzi wa tabenakulo, uthibitishao kwamba Kutoka kimepuliziwa na Mungu?

7 Simulizi la ujenzi wa tabenakulo kwenye nyanda kabla ya Sinai hufaana na hali za mahali hapo. Msomi mmoja alieleza hivi: “Katika namna, mwundo, na vitu vilivyotumiwa, tabenakulo yafaa jangwa kabisa. Mbao zilizotumiwa katika jengo zapatikana huko kwa wingi.”d Iwe ni kuhusu majina, desturi, dini, mahali, jiografia, au vitu vilivyotumiwa, ushuhuda mwingi wa nje huthibitisha simulizi lililopuliziwa na Mungu la Kutoka, ambalo sasa lina miaka kama 3,500.

8. Kutoka huonyeshwaje kuwa kinafungamana na Maandiko yale mengine kikiwa kimepuliziwa na Mungu na chenye mafaa?

8 Waandikaji wengine wa Biblia walirejezea Kutoka daima, kuonyesha umaana na thamani yacho ya kiunabii. Miaka zaidi ya 900 baadaye, Yeremia aliandika “Mungu wa kweli, Yule aliye mkuu, Aliye mweza yote, Yehova wa majeshi likiwa jina lake,” alichukua hatua ya kuwatoa watu wake, Israeli, kutoka Misri “kwa ishara na kwa miujiza na kwa mkono imara na kwa mkono ulionyooshwa na kwa uhofisho mkuu.” (Yer. 32:18-21, NW) Miaka zaidi ya 1,500 baadaye, mwingi wa ushuhuda wa Stefano uliomwongoza kufia imani aliutegemeza juu ya habari iliyo katika Kutoka. (Mdo. 7:17-44) Maisha ya Musa yanatajwa kwetu kuwa kielelezo cha imani kwenye Waebrania 11:23-29, na Paulo hurejezea sana Kutoka katika kututolea sisi leo vielelezo na maonyo. (Mdo. 13:17; 1 Kor. 10:1-4, 11, 12; 2 Kor. 3:7-16) Yote hayo yanatusaidia tuthamini jinsi sehemu za Biblia zinavyofungamana vizuri, kila kisehemu kikishiriki katika ufunuo wa kusudi la Yehova katika njia yenye mafaa.

YALIYOMO KATIKA KUTOKA

9. Musa azaliwa na kulelewa chini ya hali gani?

9 Yehova ampa Musa utume, akikazia Jina la Ukumbusho Lake (1:1–4:31). Baada ya kutaja wana wa Israeli ambao wameingia Misri, ndipo Kutoka kinaandika juu ya kifo cha Yusufu. Baada ya muda mfalme mpya atokea kutawala Misri. Aonapo kwamba Waisraeli wanaendelea “kuzidika na kukua wakiwa wenye uweza zaidi kwa kadiri kubwa sana isivyo kawaida,” atumia hatua za kukandamiza, kutia ndani kufanyishwa kazi ngumu ya lazima (shokoa), na ajaribu kupunguza idadi ya wanaume wa Israeli kwa kuagiza uangamizo wa watoto wote wa kiume waliotoka kuzaliwa. (1:7, NW) Ni chini ya hali hizo kwamba mwana azaliwa kwa Mwisraeli wa nyumba ya Lawi. Mtoto huyo ni wa tatu katika familia. Awapo na miezi mitatu, mama yake amficha ndani ya kisafina cha matete kati ya matete kando ya Mto Naili. Apatikana na binti ya Farao, ambaye ampenda mvulana huyo na kumlea. Mama yake mwenyewe awa mlezi wa kumnyonyesha, na kama tokeo, akua katika makao ya Kiisraeli. Baadaye aletwa kwenye baraza la Farao. Aitwa Musa, maana yake “Aliyechotwa [yaani, kuokolewa kutoka majini].”—Kut. 2:10; Mdo. 7:17-22.

10. Ni matukio gani yaongozayo kwenye Musa kupewa utume maalumu wa utumishi?

10 Musa huyo anapendezwa na hali njema ya Waisraeli wenzake. Aua Mmisri kwa ajili ya kutenda vibaya Mwisraeli. Kama tokeo, alazimika kutoroka, na kwa hiyo aja katika bara la Midiani. Huko aoa Sipora binti ya Yethro, kuhani wa Midiani. Baada ya muda Musa awa baba ya wana wawili, Gershomu na Eliazari. Kisha, akiwa na miaka 80, baada ya kutumia miaka 40 katika jangwa, Musa apewa na Yehova utume wa utumishi maalumu katika utakaso wa jina la Yehova. Siku moja akichunga mifugo ya Yethro karibu na Horebu, “mlima wa Mungu [wa kweli, NW],” Musa aona kichaka cha miiba kikiwaka moto lakini kisiteketee. Aendapo kuchunguza, malaika wa Yehova asema naye, akimwambia juu ya kusudi la Mungu la kutoa watu Wake “wana wa Israeli, katika Misri.” (Kut. 3:1, 10) Musa atatumiwa kuwa chombo cha Yehova katika kuweka huru Israeli kutoka utumwa wa Kimisri.—Mdo. 7:23-35.

11. Sasa Yehova ajulisha jina lake katika maana gani maalumu?

11 Kisha Musa auliza jinsi yeye atamtambulisha Mungu kwa wana wa Israeli. Ni hapa, kwa mara ya kwanza, kwamba Yehova ajulisha maana halisi ya jina lake, akilishirikisha na kusudi lake mahususi na kuliimarisha kuwa ukumbusho. “Hivi ndivyo wewe utasema kwa wana wa Israeli, ‘MIMI NITATHIBITIKA KUWA amenituma mimi kwa nyinyi . . . Yehova Mungu wa mababu wenu, Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo, amenituma mimi kwa nyinyi.’” Jina lake, Yehova, humtambulisha kuwa yeye ambaye atasababisha litimie kusudi lake kwa kukamatana na watu wa jina lake. Kwa watu wake, wazao wa Abrahamu, atawapa bara waliloahidiwa mababu wao, “bara linalotiririka maziwa na asali.”—Kut. 3:14, 15, 17, NW.

12. Yehova aeleza Musa nini kuhusiana na kuweka Waisraeli huru, nao watu waitikiaje ishara hizo?

12 Yehova amweleza Musa kwamba mfalme wa Misri hataruhusu Waisraeli waende huru bali kwamba Yeye kwanza atalazimika kupiga Misri kwa vitendo Vyake vyote vya ajabu. Musa apewa ndugu yake, Haruni, kuwa mneni, nao wapokea ishara tatu za kufanya ili kusadikisha Waisraeli kwamba wao waja katika jina la Yehova. Wakiwa njiani kwenda Misri, mwana wa Musa alazimika kutahiriwa ili kuzuia kifo katika familia, ikikumbusha Musa juu ya matakwa ya Mungu. (Mwa. 17:14) Musa na Haruni wakusanya wanaume wazee wa wana wa Israeli na kuwapasha habari juu ya kusudi la Yehova la kuwatoa Misri na kuwapeleka kwenye Bara Lililoahidiwa. Wafanya ishara hizo, na watu waamini.

13. Ni nini tokeo la kabiliano la kwanza baina ya Musa na Farao?

13 Mapigo juu ya Misri (5:1–10:29). Musa na Haruni sasa waenda kwa Farao na kutangaza kwamba Yehova, Mungu wa Israeli, amesema: “Wape watu wangu ruhusa waende.” Kwa sauti ya madharau, Farao mwenye kiburi ajibu: “BWANA [Yehova, NW] ni nani, hata niisikilize sauti yake, na kuwapa Israeli ruhusa waende zao? Mimi simjui BWANA [Yehova, NW], wala sitawapa Israeli ruhusa waende zao.” (5:1, 2) Badala ya kuwaweka Waisraeli huru, awalazimisha kufanya kazi ngumu zaidi. Hata hivyo, Yehova arudia tena ahadi zake za ukombozi, kwa mara nyingine akikamatanisha hilo na utakaso wa jina lake: “Mimi ni YEHOVA . . . nitakuwa [nitathibitika kuwa, NW] Mungu kwenu . . . Mimi ni YEHOVA.—6:6-8.

14. Wamisri walazimishwaje watambue “chanda cha Mungu”?

14 Ishara ambayo Musa afanya mbele ya Farao, kwa kumwagiza Haruni atupe chini fimbo yake iwe nyoka, yaigwa na makuhani wa Misri wenye kuzoea mizungu. Ijapokuwa nyoka zao zamezwa na nyoka mkubwa wa Haruni, bado moyo wa Farao wawa mgumu. Sasa Yehova achukua hatua ya kuleta mfululizo wa mapigo mazito kumi juu ya Misri. Kwanza, mto wao Naili na maji yote ya Misri yageuka kuwa damu. Kisha pigo la vyura laja juu yao. Mapigo hayo mawili yaigwa na makuhani wenye kuzoea mizungu, lakini sivyo kwa lile pigo la tatu, lile la nzi-waumaji juu ya binadamu na mnyama. Makuhani wa Misri walazimika kutambua kwamba hicho ni “chanda cha Mungu.” Hata hivyo, Farao akataa kuwaacha Israeli waende.—8:19.

15. Ni mapigo gani yapatayo Wamisri peke yao, na ni kwa sababu gani pekee Yehova aruhusu Farao aendelee?

15 Mapigo matatu ya kwanza yawapata Wamisri na Waisraeli pia, lakini kuanzia la nne na kuendelea, ni Wamisri peke yao wapigwao, Israeli wakisimama tofauti chini ya ulinzi wa Yehova. Pigo la nne ni mabumba ya mainzi. Kisha yafuata tauni juu ya mifugo wote wa Misri, kisha majipu yenye vidonda juu ya binadamu na mnyama, hata kwamba makuhani wenye kuzoea mizungu washindwa kusimama mbele ya Musa. Kwa mara nyingine Yehova aruhusu moyo wa Farao uwe mgumu, akimjulisha rasmi hivi kupitia Musa: “Lakini, nilikusimamisha wewe kwa sababu ii hii, ili nikuonyeshe uweza wangu, tena kwamba jina langu litangazwe katika dunia yote.” (9:16) Kisha Musa atangazia Farao pigo lifuatalo, “mvua ya mawe nzito sana,” na hapa Biblia yasajili (yaandika) kwa mara ya kwanza kwamba baadhi ya watu miongoni mwa watumishi wa Farao wahofu neno la Yehova na kutenda kupatana nalo. Mapigo ya nane na tisa—vamio la nzige na giza lenye kuleta huzuni—yafuatana upesi mfululizo, na Farao mwenye moyo mgumu, mwenye ghadhabu atisha Musa atakufa akijaribu kuona uso wake tena.—9:18.

16. Yehova aamuru nini kuhusu Kupitwa na Mwadhimisho wa Mikate Isiyotiwa Chachu?

16 Kupitwa na kupigwa dharuba kwa mzaliwa wa kwanza (11:1–13:16). Sasa Yehova atangaza, “Liko pigo moja bado, nitakaloleta juu ya Farao na juu ya Misri”—kifo cha mzaliwa wa kwanza. (11:1) Yeye aagiza kwamba mwezi wa Abibu uwe wa kwanza wa miezi kwa Israeli. Katika siku ya 10, wao wapaswa kutwaa kondoo au mbuzi—wa kiume, mwenye mwaka mmoja, asiye na waa—na katika siku ya 14, wapaswa kumwua. Katika jioni hiyo ni lazima watwae damu ya mnyama huyo na kuinyunyiza kwenye miimo miwili ya mlango na kizingiti cha juu cha mlango, halafu lazima wakae ndani ya nyumba na kula mnyama huyo aliyechomwa, ambaye hakuna mfupa wake hata mmoja wapasa kuvunjwa. Hakupasi kuwe chachu yoyote katika nyumba, na lazima wale haraka-haraka, wamevaa na tayari kupiga hatua za kuondoka. Kupitwa itatumika kuwa ukumbusho, msherehekeo kwa Yehova katika vizazi vyao vyote. Itafuatwa na Mwadhimisho wa Mikate Isiyotiwa Chachu ya siku saba. (Baadaye, Yehova atoa maagizo zaidi kuhusu miadhimisho hiyo, naye aamuru kwamba wazaliwa wa kwanza wa kiume wote wa Israeli, wa wanadamu na wanyama, lazima watakaswe kwake.)

17. Ni matukio gani yatiayo alama usiku huo kuwa wa kukumbukwa?

17 Israeli wafanya sawa na alivyoamuru Yehova. Kisha msiba wapiga! Usiku-kati Yehova aua wazaliwa wa kwanza wote wa Misri, akipita na kukomboa mzaliwa wa kwanza wa Israeli. “Ondokeni, tokeni katika watu wangu,” Farao apiga kelele. “Wamisri nao wakawahimiza watu” waondoke upesi. (12:31, 33) Waisraeli hawaondoki mikono mitupu, kwa maana wao waomba na kupokea kutoka kwa Wamisri vitu vya fedha na vya dhahabu na mavazi. Wapiga hatua kutoka Misri katika mpango wa pigano, kufikia hesabu ya watu wenye uwezo 600,000, pamoja na familia zao na andamano kubwa lililochangamana la wasio Waisraeli, na pia mifugo mikubwa ya wanyama. Hilo linatilia alama ya mwisho wa miaka 430 tangu kuvuka Frati kwa Abrahamu ili aingie bara la Kanaani. Hakika huo ni usiku wa kufanyiwa ukumbusho.—Kut. 12:40, NW, kielezi-chini cha pili; Gal. 3:17.

18. Ni utakaso gani wa jina la Yehova wa kutia tamati watukia kwenye Bahari ya Shamu?

18 Jina la Yehova latakaswa kwenye Bahari ya Shamu (Nyekundu) (13:17–15:21). Akiwaongoza mchana kwa nguzo ya wingu na usiku kwa nguzo ya moto, Yehova aongoza Israeli kupitia njia ya Sukothi. Kwa mara nyingine Farao awa na moyo mgumu, akiwakimbiza na magari-farasi ya vita yaliyochaguliwa ili awanase, ndivyo anavyofikiri, kwenye Bahari ya Shamu (Nyekundu). Musa awatuliza watu, akisema: “Msiogope, simameni tu, mkauone wokovu wa BWANA [Yehova, NW] atakaowafanyia leo.” (14:13) Kisha Yehova afanya bahari irudi nyuma, ikifanyiza kipitio cha kutorokea ambamo Musa aongoza Waisraeli kwenye usalama ng’ambo ya mashariki. Majeshi yenye nguvu ya Farao yapiga mbio kuwafuatia, ndipo tu wananaswa na kufa maji katika maji yenye kurejea. Jinsi ulivyo utakaso wa tamati wa jina la Yehova! Jinsi kilivyo kisababishi kitukufu cha kumwonea shangwe! Shangwe hiyo kisha yaonyeshwa katika wimbo mkuu wa ushindi wa kwanza katika Biblia: “Nitamwimbia BWANA [Yehova, NW], kwa maana ametukuka sana; farasi na mpanda farasi amewatupa baharini. BWANA [Yehova, NW] ni nguvu zangu, . . . Naye amekuwa wokovu wangu. . . . BWANA [Yehova, NW] atatawala milele na milele.”—15:1, 2, 18.

19. Ni matukio gani yatiayo alama safari ya kuelekea Sinai?

19 Yehova afanya agano la Sheria kwenye Sinai (15:22–34:35). Katika hatua zenye kufuatana, kama walivyoongozwa na Yehova, Israeli wasafiri kuelekea Sinai, mlima wa Mungu wa kweli. Watu wanung’unikapo juu ya maji machungu kule Mara, Yehova awafanyia yawe matamu. Kwa mara nyingine, wanung’unikapo juu ya ukosefu wa nyama na mkate, yeye awapa kware jioni na mana yenye usukari, kama umande juu ya ardhi, asubuhi. Mana hii yatumika kuwa mkate kwa Waisraeli kwa miaka 40 inayofuata. Pia, kwa mara ya kwanza katika historia, Yehova aagiza kuadhimishwa kwa siku ya pumziko, au sabato, akiagiza Waisraeli waokote kiwango maradufu cha mana katika siku ya sita na hatoi siku ya saba. Pia awafanyia maji kule Refidimu na kupigana na Amaleki kwa ajili yao, na kumwagiza Musa aandike hukumu Yake kwamba Amaleki wataangamizwa kabisa.

20. Tengenezo bora zaidi lafanywaje?

20 Kisha baba-mkwe wa Musa, Yethro, amletea yeye mke wake na wana wawili wake. Sasa umefika wakati wa tengenezo bora zaidi katika Israeli, na Yethro achangia shauri zuri lenye kutumika. Yeye ashauri Musa asijichukulie mzigo wote bali aweke wanaume wenye uwezo, wanaomhofu Mungu ili kuhukumu watu wakiwa wakuu wa maelfu, mamia, mahamsini, na makumi. Musa afanya hivyo, hivi kwamba sasa ni kesi ngumu tu zinazomfikia.

21. Kisha Yehova afanya ahadi gani, lakini kwa kutegemea masharti gani?

21 Katika muda wa miezi mitatu baada ya kule Kutoka, Israeli wapiga kambi katika jangwa la Sinai. Hapa Yehova aahidi hivi: “Sasa basi ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko makabila yote ya watu; maana dunia yote pia ni mali yangu, nanyi mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani, na taifa takatifu.” Watu watoa nadhiri hivi: “Hayo yote aliyoyasema BWANA [Yehova, NW] tutayatenda.” (19:5, 6, 8) Kufuatia kipindi cha utakaso wa Israeli, Yehova ashuka mlimani kwenye siku ya tatu, akisababisha utoe moshi na kutetema.

22. (a) Ni amri zipi zilizo katika yale Maneno Kumi? (b) Ni maamuzi gani mengine ya kihukumu yawekwayo mbele ya Israeli, na taifa hilo laingizwaje katika agano la Sheria?

22 Kisha Yehova achukua hatua ya kutoa Maneno Kumi, au Amri Kumi. Zakazia ujitoaji kamili kwa Yehova, huku zikikataza kuwa na miungu mingine, ibada ya mifano, na kulitumia jina la Yehova kwa njia ya upuuzi. Waisraeli waamriwa watumikie siku sita na kisha kutunza sabato kwa Yehova, na kuheshimu baba na mama. Sheria juu ya uuaji wa kukusudia, uzinzi, kuiba, kutoa ushuhuda wa bandia, na kutamani zakamilisha yale Maneno Kumi. Kisha Yehova aendelea kuwawekea maamuzi ya kihukumu, maagizo kwa ajili ya taifa jipya hilo, yakihusu utumwa, kunajisi, majeraha, ridhaa, wizi, madhara ya moto, ibada bandia, utongozi, kuwatenda vibaya wajane na mayatima, mikopo, na mambo mengine mengi. Sheria za Sabato zatolewa, na misherehekeo mitatu ya kila mwaka yapangwa kwa ajili ya ibada ya Yehova. Kisha Musa aandika maneno ya Yehova, dhabihu zatolewa, na nusu ya damu yanyunyizwa juu ya madhabahu. Kitabu cha agano chasomewa watu, na baada ya wao kuthibitisha nia yao ya kutii, ile nusu nyingine ya damu yanyunyizwa juu ya kitabu na juu ya watu wote. Kwa hiyo Yehova afanya agano la Sheria pamoja na Israeli kupitia mpatanishi, Musa.—Ebr. 9:19, 20.

23. Ni maagizo gani ambayo Yehova ampa Musa mlimani?

23 Kisha Musa aenda kwa Yehova mlimani akapokee Sheria. Kwa siku 40 mchana na usiku, apewa maagizo mengi kuhusu vitu vya kutumiwa kujenga tabenakulo, maelezo mengi ya vyombo vyayo, maelezo kamili madogo-madogo ya tabenakulo yenyewe, na mshono wa mavazi ya kikuhani, kutia ndani bamba la dhahabu safi, lenye nakshi “Utakatifu ni wa Yehova,” (NW) juu ya kilemba cha Haruni. Maelezo mengi juu ya kuwekwa cheoni na kutumika kwa ukuhani yatolewa, na Musa akumbushwa kwamba Sabato itakuwa ishara kati ya Yehova na wana wa Israeli “milele.” Kisha Musa apewa mabamba mawili ya Ushuhuda yaliyoandikwa kwa “chanda cha Mungu.”—Kut. 28:36; 31:17, 18.

24. (a) Watu wafanya dhambi gani, na tokeo lawa nini? (b) Kisha Yehova afunuaje jina na utukufu wake kwa Musa?

24 Upande ule mwingine watu wafadhaika na kuuliza Haruni awafanyie mungu wa kuwatangulia. Haruni afanya hivyo, akifanyiza ndama wa dhahabu, ambaye watu waabudu katika kile aitacho “sikukuu kwa BWANA [Yehova].” (32:5) Yehova anena juu ya kumaliza Israeli, lakini Musa awaombea, ingawa avunja yale mabamba yeye mwenyewe akiwa na kasirani yenye kuwaka. Wana wa Lawi sasa wasimama upande wa ibada safi, na kuchinja 3,000 za washerehekeaji wenye fujo. Pia Yehova awapiga kwa tauni. Baada ya Musa kumsihi Mungu aendelee kuongoza watu wake, aambiwa aweza kutupia jicho utukufu wa Mungu na aagizwa achonge mabamba mawili ya ziada ambayo juu yayo Yehova ataandika tena yale Maneno Kumi. Musa aendapo juu mlimani safari ya pili, Yehova achukua hatua ya kumtangazia rasmi jina la Yehova wakati Yeye apitapo: “Yehova, Yehova, Mungu mwenye rehema na neema, wa polepole kukasirika na mwingi katika fadhili za upendo na kweli, mwenye kuhifadhi fadhili za upendo kwa ajili ya maelfu.” (34:6, 7, NW) Kisha aeleza matakwa ya agano lake, na Musa aliandika kama lilivyo leo katika Kutoka. Musa ashukapo kutoka Mlima Sinai, ngozi ya uso wake inatoa miale kwa sababu ya utukufu wa Yehova uliofunuliwa. Kama tokeo, alazimika kuvaa shela juu ya uso wake.—2 Kor. 3:7-11.

25. Maandishi yasimulia nini kuhusu tabenakulo na wonyesho wa uwazi zaidi wa utukufu wa Yehova?

25 Ujenzi wa tabenakulo (35:1–40:38). Kisha Musa aita Israeli pamoja na kuwapokeza maneno ya Yehova, akiwaambia kwamba wenye moyo wenye nia wana pendeleo la kuchangia tabenakulo na wenye moyo wa hekima pendeleo la kuifanyia kazi. Upesi yaripotiwa kwa Musa: “Watu waleta vitu vingi sana zaidi ya hivyo vitoshavyo kwa ajili ya utumishi wa hiyo kazi, ambayo BWANA [Yehova, NW] aliagiza ifanywe.” (36:5) Chini ya mwelekezo wa Musa wafanya kazi waliojazwa roho ya Yehova waanza kujenga tabenakulo na vyombo vyayo na kutengeneza mavazi yote kwa ajili ya makuhani. Mwaka mmoja baada ya Kutoka, tabenakulo yakamilishwa na kusimamishwa juu ya uwanda mbele ya Mlima Sinai. Yehova aonyesha kibali chake kwa kufunika hema hilo la mkutano kwa wingu lake na kwa kujaza tabenakulo utukufu wake, hata kwamba Musa ashindwa kuingia hemani. Uongozi wa Yehova kwa Israeli wakati wa safari zao zote waonyeshwa alama na wingu ilo hilo wakati wa mchana na moto wakati wa usiku. Sasa ni mwaka 1512 K.W.K., na hapo maandishi ya Kutoka yaisha, jina la Yehova likiwa limetakaswa kwa utukufu kupitia matendo yake ya ajabu yaliyofanywa kwa ajili ya Israeli.

KWA NINI NI CHENYE MAFAA

26. (a) Kutoka chaimarishaje imani katika Yehova? (b) Marejezo kwenye Kutoka katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yaongezaje imani yetu?

26 Zaidi ya yote, Kutoka hufunua Yehova kuwa Mkomboaji na Mtengenezaji mkuu na Mtimizaji wa makusudi yake mazuri sana, nacho chaimarisha imani yetu katika yeye. Imani hiyo yaongezeka tuchunguzapo marejezo mengi kwenye Kutoka katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, kuonyesha utimizo wa sehemu nyingi za agano la Sheria, uhakikisho wa ufufuo, tendo la Yehova la kutegemeza watu wake, vitangulizi vya kazi ya Kikristo ya kutoa msaada, shauri juu ya kufikiria wazazi, matakwa ya kupata uzima, na jinsi ya kuona haki ya kulipa kisasi. Hatimaye Sheria ilijumlishwa katika amri mbili kuhusu kuonyesha upendo kwa Mungu na binadamu mwenzi.—Mt. 22:32—Kut. 4:5; Yn. 6:31-35 na 2 Kor. 8:15—Kut. 16:4, 18; Mt. 15:4 na Efe. 6:2—Kut. 20:12; Mt. 5:26, 38, 39—Kut. 21:24; Mt. 22:37-40.

27. Maandishi ya kihistoria ya Kutoka ni yenye faida gani kwa Mkristo?

27 Kwenye Waebrania 11:23-29 twasoma juu ya imani ya Musa na ya wazazi wake. Kwa imani alitoka Misri, kwa imani alisherehekea Kupitwa, na kwa imani aliongoza Israeli kupitia Bahari ya Shamu. Waisraeli walibatizwa katika Musa na kula chakula cha kiroho na kunywa kinywaji cha kiroho. Walitazamia tungamo-mwamba, au Kristo, lakini bado hawakuwa na kibali cha Mungu, kwa maana walimtia Mungu katika mtihani na kuwa waabudu sanamu, waasherati, na wanung’unikaji. Paulo aeleza kwamba hilo latumika kwa Wakristo leo: “Basi mambo hayo yaliwapata wao kwa jinsi ya mifano, yakaandikwa ili kutuonya sisi, tuliofikiliwa na miisho ya zamani. Kwa hiyo anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.”—1 Kor. 10:1-12; Ebr. 3:7-13.

28. Vivuli vya Sheria na mwana-kondoo wa Kupitwa vimetimizwaje?

28 Mwingi wa umaana wenye kina kirefu cha kiroho wa Kutoka, pamoja na matumizi yake ya kiunabii, yametolewa katika maandishi ya Paulo, hasa katika Waebrania sura 9 na 10. “Basi torati, kwa kuwa ni kivuli cha mema yatakayokuwa, wala si sura yenyewe ya mambo hayo, kwa dhabihu zile zile wanazozitoa kila mwaka daima, haiwezi wakati wo wote kuwakamilisha wakaribiao.” (Ebr. 10:1) Kwa hiyo, sisi twapendezwa kukijua kivuli na kuielewa sura. Kristo ‘alitoa dhabihu moja idumuyo hata milele.’ Yeye aelezwa kuwa “Mwana-kondoo wa Mungu.” Hata mfupa mmoja wa huyu “Mwana-Kondoo” haukuvunjwa, sawa na ilivyokuwa katika kifananishi. Mtume Paulo aeleza hivi: “Kwa maana Pasaka [Kupitwa, NW] wetu amekwisha kutolewa kuwa sadaka, yaani, Kristo; basi na tuifanye karamu, si kwa chachu ya kale, wala kwa chachu ya uovu na ubaya, bali kwa yasiyochachika, ndio weupe wa moyo na kweli.”—Ebr. 10:12; Yn. 1:29 na 19:36—Kut. 12:46; 1 Kor. 5:7, 8—Kut. 23:15.

29. (a) Tofautisha agano la Sheria na agano jipya. (b) Ni dhabihu gani ambazo Waisraeli wa kiroho wamtolea Mungu sasa?

29 Yesu alikuwa Mpatanishi wa agano jipya, sawa na Musa alivyokuwa mpatanishi wa agano la Sheria. Tofauti baina ya maagano hayo inaelezwa waziwazi pia na mtume Paulo, anenaye juu ya ‘hati iliyoandikwa [kwa mkono ya amri, NW] ikiisha kuondolewa na kifo cha Yesu juu ya mti wa mateso. Yesu aliyefufuliwa akiwa Kuhani Mkuu ni “mhudumu wa patakatifu, na wa ile hema ya kweli, ambayo Bwana [Yehova, NW] aliiweka wala si mwanadamu.” Makuhani chini ya Sheria walitoa “[utumishi mtakatifu katika, NW] mfano na kivuli cha mambo ya mbinguni” kulingana na kigezo cha kifananishi kilichotolewa na Musa. “Lakini sasa [Yesu, NW] amepata huduma iliyo bora zaidi, kwa kadiri alivyo mjumbe wa agano lililo bora, lililoamriwa juu ya ahadi zilizo bora.” Lile agano la kale lilitanguliwa na kufutiliwa mbali kuwa orodha ya amri zenye kuleta kifo. Wayahudi hao wasioelewa hilo wanaelezwa kuwa fahamu zao zilikuwa zimechakaa, lakini waamini wale wathaminio kwamba Israeli wa kiroho wamekuja chini ya agano jipya waweza “kwa nyuso zilizoondolewa shela kurudisha kama vioo utukufu wa Yehova” (NW), wakiwa wamestahilishwa vya kutosha kuwa wahudumu. Kwa dhamiri zilizosafishwa waweza kutoa “dhabihu [yao wenyewe] ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake.”—Kol. 2:14; Ebr. 8:1-6, 13; 2 Kor. 3:6-18; Ebr. 13:15; Kut. 34:27-35.

30. Kukombolewa kwa Israeli na kuadhimishwa kwa jina la Yehova katika Misri kulitangulia kuwa kivuli cha nini?

30 Kutoka huadhimisha jina na enzi kuu ya Yehova, kikielekeza mbele kwenye ukombozi mtukufu wa taifa la Kikristo la Israeli wa kiroho, ambalo kwalo yasemwa hivi: “Basi ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu; ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa la Mungu.” Nguvu za Yehova kama vile zaonyeshwa wazi sana na kukusanya Israeli wake wa kiroho kutoka kwenye ulimwengu ili kuadhimisha jina lake ni mwujiza sawa na zile nguvu alizoonyesha kwa ajili ya watu wake katika Misri ya kale. Kwa kumhifadhi Farao ili amwonyeshe nguvu Zake na ili kwamba jina Lake lipate kujulishwa rasmi, Yehova alitangulia kuonyesha ushuhuda mkubwa zaidi ambao ungetimizwa kupitia Mashahidi Wakristo wake.—1 Pet. 2:9, 10; Rum. 9:17; Ufu. 12:17.

31. Kutoka chatangulia kuwa kivuli cha nini kuhusiana na ufalme fulani na kuwapo kwa Yehova?

31 Kwa hiyo, twaweza kusema kutoka kwa Maandiko kwamba taifa lililoundwa chini ya Musa lilielekeza kwenye taifa jipya chini ya Kristo na kwenye ufalme ambao hautatikiswa kamwe. Kwa sababu ya hilo, tunatiwa moyo ‘tutolee Mungu utumishi mtakatifu kwa hofu ya kimungu na kicho.’ (NW) Sawa na ambavyo kuwapo kwa Mungu kulifunika tabenakulo jangwani, ndivyo aahidivyo kuwapo kwa umilele pamoja na wale ambao wamhofu: “Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. . . . Andika ya kwamba maneno hayo ni amini na kweli.” Hakika Kutoka ni sehemu muhimu na yenye mafaa ya maandishi ya Biblia.—Kut. 19:16-19—Ebr. 12:18-29; Kut. 40:34—Ufu. 21:3, 5.

[Maelezo ya Chini]

a Kutoka 3:14, NW, kielezi-chini; Insight on the Scriptures, Buku 2, ukurasa 12.

b Insight on the Scriptures, Buku 1, kurasa 532,535; Archaeology and Bible History, 1964, J. P. Free, ukurasa 98.

c Insight on the Scriptures, Buku 1, kurasa 540-1.

d Exodus, 1874, F. C. Cook, ukurasa 247.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki