Kutoka—Kutoka Utawala wa Mabavu Mpaka Kwenye Utaratibu wa Kitheokrasi
YEHOVA alisikia vilio vyao wakiwa “watumwa chini ya utawala wa mabavu.” Wakati wa kuchukua hatua ulikuwa umefika, na yeye alifanya hivyo akiwa Mwokozi wao Mwenye Nguvu Zote. Muda mfupi baada ya hapo, Mungu aliwaimarisha watu wake waliochaguliwa wakiwa mpango mzuri wa kitheokrasi.
Kwa kweli, hayo ndiyo masimulizi yenye kusisimua utakayoona katika kitabu cha Biblia cha Kutoka. Kitabu hicho kilichoandikwa na nabii Mwebrania, Musa, kinasimulia mambo yaliyowapata Waisraeli kuanzia 1657 mpaka 1512 K.W.K. Kati ya mambo yenye kuvuta fikira ya kitabu hicho ni miujiza yenye kustaajabisha na sheria bora sana.
Lakini je, kitabu cha Kutoka kina maana halisi katika karne ya 20? Hasa-a, kama itakavyoonyeshwa na mazungumzo mafupi yetu.
Muhtasari wa Kutoka
Wakiwa wakaaji katika Misri, wazao wa Yakobo wanaongezeka haraka sana hata amri ya kifalme inatolewa wateseke wakiwa “watumwa chini ya utawala wa mabavu.” (NW) Hata Farao anatoa amri ya watoto wote wa kiume wa Kiisraeli wauawe. Mtoto mmoja anaokoka baada ya mama yake kumweka juu ya Mto Naili aelee akiwa ndani ya kisafina cha mafunjo. Binti-Farao amwona mtoto huyo na kumlea, na ampa jina Musa, linalomaanisha “aliyeokolewa katika maji.” Ingawa analelewa katika nyumba ya kifalme, anapofika umri wa miaka 40 Musa anawaunga mkono watu wake mwenyewe wenye kuonewa, na anamwua Mmisri mmoja. Anapolazimika kukimbia, anaenda Midiani, ambako anaoa na kuishi akiwa mchungaji. Kisha Farao anakufa, lakini Farao mwingine anawatawala Waisraeli kwa mabavu. Ndipo Mungu anaposikia kilio chao cha kutaka msaada.—Kutoka 1:1–2:25.
Siku moja Musa anaona kichaka kinachowaka moto lakini, kwa mwujiza, hakichomeki. Kupitia malaika hapo Yehova anampa mgawo wa kurudi Misri na kuwaongoza Waisraeli watoke katika utumwa wa ukatili. Mungu anamweka rasmi Haruni nduguye awe msemaji wake.—Kutoka 3:1–4:31.
Musa na Haruni wanakuja mbele za Farao, na kuuliza kwamba Waisraeli waruhusiwe washerehekee sikukuu ya Yehova jangwani. Kwa ukaidi mtawala huyo wa Kimisri anakataa, lakini ndipo Yehova anapochukua hatua ili ajifanyie jina mwenyewe. Farao mwenye kupita cheo na waganga wake hakika hawalinganiki na Musa, ambaye Yehova anatumia kuleta mapigo yenye kishindo. Hata baada ya mapigo tisa, mtawala wa mabavu huyo Mmisri ni mwenye kichwa kikubwa!—Kutoka 5:1–10:29.
Katika kutazamia pigo la kumi, Yehova anawaamuru Waisraeli washerehekee “kupitwa.” Katika Nisani 10, wanachukua mwana-kondoo au mwana-mbuzi kwa ajili ya kila jamaa. Mnyama huyo anauawa katika Nisani 14 na damu yake inanyunyizwa juu ya miimo ya mlango na juu ya vizingiti vya mlango wa nyumba zao. Wanamchoma juu ya moto na kumla baada ya jua kushuka, pamoja na mboga chungu na mkate usiotiwa chachu. Jamaa hizo zote zikiwa zingali ndani ya nyumba, karibu usiku wa manane malaika wa Yehova aizunguka nchi hiyo lakini apita kila nyumba ya Kiisraeli. Pigo la kumi lapiga. Kifo chapata kila mzao wa kwanza wa Misri, kutia mtoto wa kwanza wa Farao. Baada ya hilo awaruhusu Waisraeli waende zao.—Kutoka 11:1–12:36.
Hata hivyo, upesi mwonezi huyo Mmisri na majeshi yake wanawafuatia mbio-mbio. Lakini Yehova atoa wokovu kwa kufungua njia ya kutorokea kuvuka Bahari Nyekundu (Bahari ya Shamu). Halafu, Waisraeli wakiwa salama kwenye ufuo ule mwingine, Mungu aifanya bahari hiyo imfunike Farao na jeshi lake lenye kuwafukuza, wote wanakunywa maji na kufa. Hiyo ilikuwa njia yenye kishindo kama nini ya kumjua Yehova na uwezo wake wenye kutisha!—Kutoka 12:37–15:21.
Kutoka hapo kwenda Mlima Sinai katika Uarabu Waisraeli wanajifunza zaidi juu ya Yehova pindi baada ya pindi, kwa kuwa anafanya maji machungu yawe matamu, anawapa kware wengi na kuwaandalia chakula kitamu wanachokiita mana. Katika mwezi wao wa tatu baada ya kukombolewa kutoka utawala wa mabavu wa Kimisri, wanapiga kambi kwenye nyanda za Mlima Sinai. Hapo wanapokea sheria za Mungu, kutia zile “Amri Kumi” (Maneno Kumi), na wanaingia katika agano pamoja na Yehova, Mwokozi wao Mwenye Nguvu Zote.—Kutoka 15:22–24:18; Kumbukumbu la Torati 4:13.
Musa atumia siku 40 katika mlima huo na kupokea maagizo kuhusu ibada ya kweli na ujenzi wa hema la ibada la Yehova, hekalu linaloweza kubebwa. Wakati uo huo, Waisraeli wanatengeneza na kuabudu ndama wa dhahabu. Anaposhuka kutoka kwenye mlima, Musa anaona hilo na anakasirika sana hata anavunja-vunja yale mawe mawili ambayo juu yake zile Amri Kumi zimeandikwa kwa njia ya mwujiza. Baada ya adhabu wanayostahili kutolewa juu ya waabudu-sanamu hao wenye kukosa, kwa mara nyingine aukwea mlima na huko apokea mawe mawili mengine. Musa anaona utukufu wa Mungu na kusikia Yehova akitangaza kwamba Yeye ni mwenye rehema lakini hakosi kutoa adhabu inayostahili.—Kutoka 25:1- 34:7.
Musa akiisha kurudi kutoka kwenye mlima mara hii ya pili, ujenzi wa hema la ibada unaanza, kwa kufuatisha kiolezo kilichotolewa na Yehova. Kufikia mwishoni mwa mwaka wa kwanza tangu Israeli awekwe huru, hema hili la ajabu na vyombo vyalo vyote linakamilika. Hema hilo la ibada linasimamishwa na kuwekwa tayari kabisa kisha Yehova analijaza utukufu wake.—Kutoka 34:8–40:38.
Inaelekea, umeguswa moyo sana na kurudiwa kwa matukio hayo yenye kusisimua. Lakini wewe binafsi unaposoma Kutoka huenda ukawa na maulizo fulani, ambayo mengine yayo huenda yakajibiwa sasa tunapozungumza sehemu tatu kuu za kitabu hicho kwa njia ya maswali na majibu.
“Watumwa Chini ya Utawala wa Mabavu”
• 3:1—Yethro, baba-mkwe wa Musa, alikuwa kuhani wa aina gani?
Kwa wazi Yethro alikuwa mzee wa ukoo aliyekuwa kichwa cha kabila la Wamidiani na alikuwa na daraka la kufundisha na kuwaongoza katika mambo ya maisha na ya kidini. Kwa kuwa Wamidiani walikuwa wazao wa Abrahamu kupitia Ketura, walikumbuka ibada ya kweli ambayo Abrahamu sikuzote alipasisha nyumba yake. Hatuwezi kuwa na hakika dini ya kabila hilo ilikuwa safi kadiri gani katika siku za Musa. Lakini Yethro alionyesha kumthamini sana Yehova ingawa yeye hakuwa amewekwa rasmi na Mungu.—Kutoka 18:1-24.
• 4:11—Je! Yehova ndiye mwenye lawama ya kasoro kama kuwa kipofu?
Hapana, Yehova siye mwenye daraka la kila kisa cha kasoro za kimwili kama kuwa kipofu na kiziwi. Mambo hayo yametokea hasa kwa sababu Mungu ameruhusu jamii yenye dhambi ya kibinadamu iwepo, wakosaji Adamu na Hawa wakiwa ndio walipoteza ukamilifu wao wenyewe na kwa hiyo, wakapoteza uweza wao wa kuzaa watoto wakamilifu. (Ayubu 14:4; Warumi 5:12) Wazao wao walipozaa watoto, kutokamilika zaidi na zaidi, kutia ndani kasoro za kimwili, zimetokea. Kwa kuruhusu hali hiyo isitawi, Mungu angeweza kusema juu yake mwenyewe kuwa ‘anafanya’ bubu, kiziwi na kipofu. Ni kwa makusudi fulani, lakini ni katika pindi chache tu, Yehova amesababisha upofu na ububu wa kimwili. (Mwanzo 19:11; Luka 1:20-22, 62-64; Matendo 13:8-11) Watu wakichagua kuwa bubu na vipofu kiroho, yeye anawaruhusu waendelee katika kutosadiki kwao na kukataa ujumbe wake, kwa njia hiyo ‘anawafanya’ bubu na vipofu katika maana ya kiroho. (Isaya 6:9, 10) Lakini Yehova amewawezesha kusikia na kuona kiroho wale wanaotafuta kumpendeza. Zaidi ya hayo, kupitia Ufalme wake mikononi mwa Yesu Kristo, Mungu mwenye upendo, Yehova atawakomboa wanadamu katika upofu wa kimwili na kasoro nyinginezo zote.—Isaya 61:1, 2; 1 Yohana 4:8; Ufunuo 21:1-4.
• 4:24-26—Ni uhai wa nani uliokuwa hatarini, na ni jambo gani lililotokea?
Kwa sababu kifungu hicho hakiko wazi, twadokeza hivi: Mwana wa Musa alielekewa na tisho la kifo kwa kutojipatanisha na agano la mapema zaidi la tohara. (Mwanzo 17:9-14) Baada ya kuondoa govi la mtoto huyo, Sipora alifanya ushuhuda huo wa kukubaliana na agano hilo uguse miguu ya malaika aliyekuwa amechukua umbo la binadamu, hivyo akaonyesha hakukuwa sababu tena ya kumfanya mwanaye afe. Kama alikuwa akimsemesha Yehova kupitia malaika huyo kuwa ni “bwana arusi wa damu,” ilikuwa ni kama kwamba alikuwa amekubali cheo cha mke katika agano la tohara, Mungu akiwa ndiye mume.
• 6:3—Kwa kuwa Abrahamu, Isaka na Yakobo walilitumia jina Yehova, ni kwa maana gani Mungu hakuwa amewajulisha jina hilo?
Kwa halisi jina Yehova linamaanisha “Yeye Anafanya Iwe,” yaani, kulingana na kusudi la Mungu. Abrahamu, Isaka na Yakobo walitumia jina hilo la kimungu na walipokea ahadi kutoka kwa Yehova. Hata hivyo hawakujua wala kujionea Yehova kuwa Ndiye anayefanya ahadi hizo zitimizwe kabisa. (Mwanzo 12:1, 2; 15:7, 13-16; 26:24; 28:10-15) Hata hivyo, upesi jina la Yehova lingekuwa na maana kubwa zaidi kwa wazao wao, Waisraeli. Wangepata kujua maana halisi ya jina hilo wakati Yehova angetimiza kusudi lake kuelekea Israeli kwa kuwakomboa katika utawala wa mabavu kisha awape Nchi ya Ahadi katika kutimiza agano lake na babu zao.
• 7:22—Makuhani Wamisri walipata wapi maji ambayo yalikuwa bado kugeuzwa yawe damu?
Wangaliweza kutumia maji fulani ambayo yalikuwa yametekwa katika Mto Naili kabla ya pigo hilo. Hata hivyo, inaelekea maji ambayo yalikuwa bado kugeuzwa yawe damu yangeweza kukusanywa kwa kuchimba visima katika udongo wenye maji-maji kuizunguka Naili. (Kutoka 7:24) Pengine makuhani walitumia maji hayo ili watende udanganyifu wao.
• 12:29—Je! watu wa kiume na wa kike wote walionwa kuwa wazaliwa wa kwanza?
Wazaliwa wa kwanza walikuwa wa kiume tu. Hilo linaonyeshwa na uhakika wa kwamba baadaye, wakati kubadilishana kulipofanywa kwa kumpa Yehova Walawi, ni watu wa kiume peke yao waliohesabiwa. (Hesabu 3:40-51) Farao mwenyewe alikuwa mzaliwa wa kwanza, lakini yeye hakuuawa kwa sababu yeye alikuwa na nyumba yake mwenyewe na si kichwa cha nyumba aliyeuawa bali mzaliwa wa kwanza wa nyumba ndiye aliyeuawa katika usiku huo wa Kupitwa.—Kutoka 12:12.
Wakombolewa na Yehova
• 15:8—Kwa kuwa maji ya Bahari Nyekundu ‘yaligandamana,’ je, yalikuwa barafu?
Neno la Kiebrania lililotafsiriwa hapa kuwa ‘kugandamana’ lina maana ya kurudi au kuwa nzito. Katika Ayubu 10:10 neno hilo linatumiwa kuhusu kufanyiza jibini. Kwa hiyo kwa lazima haimaanishi kwamba kuta za maji zilikuwa barafu. Kwa kuwa hakuna kitu chenye kuonekana kilichokuwa kikiyazuilia maji hayo, yangekuwa yenye kuonekana yamegandamana au yakawa magumu au mazito ili yaendelee kusimama. Ikiwa upepo uliotangulia kutajwa ulikuwa wenye baridi ya kuweza kufanya maji hayo yawe barafu, bila shaka mtajo fulani wa baridi hiyo nyingi ungetajwa.—Kutoka 14:21.
Wapangwa Kuwa Theokrasi
• 20:5—Je! hiyo ina maana kwamba waaminifu wangepewa adhabu?
Hapana, kwa sababu kila mtu, akiisha kufikia umri ambao anabeba daraka lake mwenyewe, anahukumiwa kwa msingi wa mwenendo na mwelekeo wake mwenyewe. (Linganisha Ezekieli 18:20.) Hata hivyo, wakati taifa la Israeli baadaye liligeukia ibada ya sanamu, lilipatwa na matokeo maovu ya jambo hilo kwa vizazi vingi baadaye. Waaminifu hawakuadhibiwa binafsi kwa ajili ya dhambi ya taifa hilo, ingawa walihisi matokeo fulani ya hilo. Ilikuwa vigumu kwa washika-ukamilifu hao kupinga uasi mkubwa wa kidini wa taifa hilo, lakini kwa kufanya hivyo walifurahia fadhili za upendo za Yehova.
• 23:20-23—Malaika anayetajwa hapa alikuwa nani, na jina la Yehova lilikuwa “limo ndani yake” jinsi gani?
Malaika wengine kando ya Yesu Kristo kabla ya kuja kwake duniani walitumiwa kupokeza Musa Sheria ya Mungu. (Yohana 1:1-3, 14; Waebrania 2:2, 3) Lakini ni jambo la akili kukata kauli kwamba malaika ambaye Yehova alisema “jina langu limo ndani yake” alikuwa Yesu kabla ya kuja kwake duniani. Yeye alitumiwa kuwaongoza Waisraeli walipokuwa njiani kwenda kwenye Nchi ya Ahadi. (1 Wakorintho 10:1-4) Yesu, ambaye jina lake linamaanisha “Wokovu wa Yehova,” ndiye aliye mkuu katika kutegemeza na kuondolea lawama jina la Babaye.
• 32:25—Kwa sababu gani Haruni hakupewa adhabu kwa ajili ya kufanyiza yule ndama wa dhahabu?
Haruni alifanya hivyo kwa kuamriwa na watu, si kwa sababu moyo wake ulikubaliana na ibada ya sanamu. Baadaye, kwa wazi alijiunga na Walawi wenzake katika kuchukua msimamo upande wa Yehova kupinga wale waliojiinua juu ya Musa katika pindi hiyo. Karibu watu 3,000 (inaelekea wachocheaji) walichinjwa, lakini wengine zaidi walikuwa na hatia kwa sababu baada ya wale 3,000 kuuawa Musa aliwakumbusha watu kwamba walikuwa wametenda dhambi kubwa. Kwa hiyo watu wengi zaidi ya Haruni tu walionyeshwa rehema ya Yehova wakati huo.—Kutoka 32:1-6, 26-35.
• 34:26—Amri ya kutomtokosa (kutochemsha) mwana-mbuzi katika maziwa ya mamaye ilikuwa yenye kutoa maana gani?
Kuchemsha au kutokosa mwana-mbuzi katika maziwa ya mamaye, yaripotiwa kulikuwa sherehe ya kipagani ya kutokeza mvua Kwa hiyo huenda Waisraeli wakawa walipewa sheria hiyo wajiepushe na mazoea hayo Hata hivyo, amri hiyo, pamoja na nyingine inaelekea inatilia mkazo uhakika wa kwamba kuna utaratibu unaofaa na unaopasa mambo yote. Yehova aliandaa maziwa ya mama yalishe mtoto wake. Lakini kuchemsha mtoto wake katika maziwa hayo kungetokeza umizo na kifo, kinyume kabisa cha kusudi la maziwa hayo. Inaonekana pia sheria hiyo iliwapa watu wa agano la Mungu somo la kwamba hawapaswi kutenda kwa njia isiyo ya huruma, bali wangepaswa kuwa wenye kuhurumia.
Kutoka Kina Maana Halisi kwa Waaminifu
Kutoka ni masimulizi yenye kugusa moyo ya utumwa katika utawala wa mabavu, ukombozi wa kimungu na kufanywa kwa jamii ya kitheokrasi. Lakini mashahidi wa Yehova wa karne ya 20 wanaweza kujifunza nini katika kitabu hicho?
Yehova anawategemeza watu wake. Alifanya hivyo kwa kuwategemeza na kuwabariki Waisraeli walipokuwa “watumwa chini ya utawala wa mabavu.” (Kutoka 1:7, 14, NW) Vivyo hivyo, Yehova anawategemeza mashahidi wake wa kisasa, hata wanapokabili mateso makali.
Yehova ni Mkombozi asiyeweza kulinganishwa na mwingine. Jambo hilo lilikuwa wazi kama nini kwenye Bahari Nyekundu! Vivyo hivyo, mashahidi wake wa kisasa wanaweza kuwa na uhakika kwamba wao, wakiwa kikundi, wataokoka ‘dhiki kuu’ inayokuja chini ya mkono wenye nguvu zote wa Mkombozi Mkubwa huyu.—Mathayo 24:20-22; Ufunuo 7:9, 14.
Yehova ndiye Mungu wa tengenezo la kitheokrasi. Sheria zake, zilipotiiwa, ziliwasaidia Waisraeli wamwabudu yeye katika njia ya utaratibu, ya usalama, ya furaha ambayo iliheshimu jina lake. Kwa kufananishwa na hayo, Yehova amewafanya tengenezo mashahidi wake wa leo kuwa udugu wenye utaratibu, wenye usalama na wenye furaha. Kwa ajili ya usalama na furaha yetu wenyewe, basi, ni lazima tumtumikie Mungu kwa uaminifu tukiwa sehemu ya jamii hiyo ya kitheokrasi inayotukuza jina lake.—Zaburi 100:1-5; 1 Petro 2:17.
Hizo ni kati ya faida nyingi zinazopatikana katika kitabu cha Kutoka. Imani yetu na itiwe nguvu tunapofikiria masimulizi hayo yenye kusisimua ya ukombozi wa kimungu kutoka utawala wa mabavu mpaka kwenye utaratibu wa kitheokrasi.
[Picha katika ukurasa wa 20]
Kwenye Mlima Sinai Yehova aliwafanya Waisraeli kuwa tengenezo la kitheokrasi